Ripoti ya Watangazaji Ufalme
Katika New Zealand—Siku ya Kukumbukwa
“TUNAFURAHI kabisa kuwa pamoja nanyi. Hatutalisahau kamwe!”
“Katika mashirika yangu yote ya kitheokrasi, mimi sijapata kamwe kuona jambo kama hili.”
“Ilionekana kana kwamba tulikuwa tukifurahia siku katika mfumo mpya wa mambo.”
Haya yalikuwa baadhi ya maelezo ya wajumbe kwenye programu ya mzinduo wa makao makuu ya tawi la Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi katika New Zealand, Novemba 29, 1986. Ni kwa sababu gani watu hawa walivutwa sana hivyo? Ni kwa sababu ilikuwa siku yenye kukumbukwa kweli kweli. Acheni tushiriki pamoja nanyi baadhi ya sababu kwa nini ilikuwa hivyo.
Kwanza, vile vifaa vizuri sana vilivyokuwa vikiwekwa wakfu vilifanya siku hiyo iwe yenye kukumbukwa. John E. Barr, wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, alilieleza lile Jumba la Ufalme jipya lililokuwa limejengwa pamoja na vifaa vya tawi kuwa “-zuri, -dhanifu, -enye kuvutia . . . Kazi iliyomalizika huonyesha uangalifu wa makini sana kwa mambo madogo-madogo, kwa uzuri. Mambo yote yanaonekana kufaana.”
Udugu wa Kikristo
Halafu, lilikuwa jambo la kukumbukwa kuona pamoja wengi sana wa wakale, Mashahidi ambao wamekuwa wakitumikia Yehova kwa uaminifu kwa miaka mingi sana. Kwa kweli, wao ndio waliokuwa wengi zaidi miongoni mwa wageni 658 walioalikwa. Walipokutana na rafiki wa zamani, wengi wao wakiwa hawakuwa wamewaona kwa miongo mingi ya miaka, walihisi kama Paulo, wakati, baada ya safari ndefu, alikutana na akina ndugu kutoka Roma: “Paulo alipowaona [ndugu zake] alimshukuru Mungu, akachangamka.” (Matendo 28:15) Kujionea kwa macho mifano kama hiyo ya ushikamanifu wenye kuendelea—baadhi yao wakiwepo ijapokuwa afya mbaya—kilikuwa chanzo cha kutia-moyo na shukrani.
Siku hiyo ilikuwa yenye kukumbukwa, pia, kwa sababu ya udugu mchangamfu wa kimataifa waliojionea. Mashahidi wa Yehova ni udugu wa duniani pote, na hilo lilishuhudiwa na wageni waliokuja kutoka sehemu zilizo mbali kama vile Australia, United States, Kanada, Uingereza, Taiwan na pia kutoka Papua New Guinea, Samoa, na visiwa vingine vya Pasifiki Kusini. Simu za kuandikwa zilikuja kutoka kwa wengi ambao hawakuweza kuwapo kibinafsi, kutia salamu kutoka Baraza Linaloongoza, washiriki wa jamaa ya Betheli ya Brooklyn, na darasa la 82 la shule ya Gileadi ya umisionari. Kweli kweli, lilikuwa jambo lenye kutia imani nguvu kufahamu kupendezwa kwa ndugu wengi sana katika nchi nyingi sana kulikoonyeshwa katika mzinduo wa vifaa vya tawi la New Zealand.
Misingi Iliyowekwa na Mashahidi Washikamanifu
Kukumbushwa juu ya historia ndefu ya kazi ya kuhubiri katika New Zealand iliyoongoza kwenye kujengwa kwa vifaa hivi vya tawi vya karibuni zaidi lilikuwa jambo lenye kusisimua na pia likafanya siku hiyo iwe yenye kukumbukwa. (Linganisha Waebrania 10:32.) Kama msemaji mmoja alivyosema: “Ingawa misingi halisi ya Betheli hii nzuri mpya yenye sehemu nyingi ni ya maana, iliyo ya maana zaidi ni misingi ya mfano iliyowekwa na akina ndugu na dada washikamanifu, wenye kujidhabihu kurudi nyuma mpaka mwanzo wa karne hii.”
Hiyo ilifuatwa na mahoji ya wanaume na wanawake waaminifu 11 ambao walikuwa na jumla ya miaka 680 ya utumishi ulio wakfu. Miongoni mwao, walieleza juu ya mmoja wa mikusanyiko iliyo ya kwanza kabisa katika New Zealand, katika 1913. Walikumbuka hali ngumu za kupainia katika Kisiwa cha Kusini katika miaka ya muda wa tangu 1930, hali zenye shida za miaka ya Vita ya Ulimwengu ya Pili tengenezo lilipopigwa marufuku, kuundwa kwa tawi la New Zealand katika 1947, kufika kwa misionari wa Gileadi wa kwanza, na kujengwa kwa Jumba la UfaIme la kwanza nchini katika 1950. Hisia ya ujumla ya wale waliohojiwa ilikuwa: “Tunashukuru kama nini kuwa hapa na kuona ushuhuda wa ongezeko ambalo, katika siku za mapema zaidi, hatungeweza kamwe kuota kwamba linawezekana!”
Baraka ya Yehova
Pengine jambo lililo kubwa lililofanya siku hiyo iwe isiyoweza kusahauliwa lilikuwa ule ufahamu wa kwamba baraka ya Yehova ilikuwa imeongoza kazi ya ujenzi na kuileta katika hali ya kuzaa matunda. Kwa kufaa, sehemu moja ya programu ya siku hiyo ilikuwa na kichwa: “Mkono Mwema wa Mungu [Wetu] Ulikuwa Juu [Yetu].”—Nehemia 2:8.
Mkono mwema wa Yehova ulionekana katika usaidizi na ushirikiano na wanabiashara na wenye mamlaka wa huko, pamoja na katika sifa za Kikristo zilizodhihirishwa na wafanya kazi wenyewe penye mahali pa ujenzi. Mwanabiashara mmoja, aliyezuru mahali pa ujenzi, alisema: “Mimi sijapata kamwe kuona po pote penginepo ile hisia ya amani na utulivu niliyo nayo nikiwa hapa.”
Baraka ya Yehova ilionekana katika ukarimu wa Mashahidi wa kawaida kuzunguka nchi waliotegemeza mradi huo kifedhi llionekana pia katika moyo wa kupenda wa wale waliojitolea wenyewe kufanya kazi yenyewe. Wote pamoja, 1,237 walijaza fomu za maombi ya kutoa utumishi wao, baadhi yao wakisafiri penye mahali pa ujenzi kutoka nchi za mbali na kwa gharama zao wenyewe wakatumie majuma machache au meizi wakisaidia katika kazi ya ujenzi Akasema ndugu mmoja: “Kusaidia katika mahali pa [ujenzi] ulikuwa upeo katika maisha yangu.”
Kama alivyotaja Ndugu Barr katika hotuba ya mzinduo, vifaa hivyo vipya vya tawi vyapaswa kuonwa kuwa “ushuhuda wa nje, ulio dhahiri wa Ufalme wa Mungu wa Kimasihi uliosimamishwa sasa.” Ndiyo, ilikuwa kweli kweli siku ya kukumbukwa kwa New Zealand. Mwishoni, kulikuwako itikio la kutoka moyoni kwa upande wa wote waliohudhuria kwa azimio lililoahidi “utegemezo kamili kwa tengenezo la Yehova kama linavyowakilishwa na tawi letu.”