Muono-Ndani Juu ya Habari
Kuzuia Jeuri
Ikifikiria ongezeko thabiti la jeuri miongoni mwa vijana-matineja, jarida American Health laripoti kwamba “mapigano pamoja na marafiki, wanadarasa na majirani ndicho kiuaji Na. 1 cha wabalehe wa mjini na ndicho kiuaji Na. 2 cha wabalehe wote katika Amerika.”
Katika jitihada ya kuzuia maelekeo yenye jeuri, kitovu cha kutoa mashauri katika Boston hutoa mtaala ambao huwezesha wanafunzi wacho waigize michezo ya vituko vifupi-vifupi kuhusu jeuri. Kwa njia hii, wao “huanza kutambua vigezo vyenye kuhusiana na jeuri” na waweza “kuona vigezo hivyo vya kasirani vikiwa ndani yao wenyewe,” aeleza mkurugenzi wa programu hiyo.
Wanafunzi hao hujifunza kuhusu jinsi mwili hutenda mambo uwapo na kasirani, kuhusu mtiririko wenye kuongezeka wa umajimaji adrinalini ambao huzishinda nguvu za kujiweza kwa mtu, na kuhusu thamani ya kufanya mawasiliano ya kupoesha kasirani “kabla mwili haujaitikia kwa kutokeza kemikali zenye kuuchochea ufanye kitendo fulani.” Wao hujifunza kwamba kwa kuuliza maswali na kuongea kwa utulivu na polepole, mkabiliano wenye kasirani kali waweza kuepukwa.
Kwa muda mrefu wanafunzi wa Biblia wametambua kwamba jeuri huzaa jeuri na kwamba, “jawabu la upole hugeuza hasira.” (Mithali 15:1) Biblia hutushauri tukimbie, pale pale mwanzoni, wakati tukabiliwapo na mkabiliano ambao waweza kulipusha kasirani. Mfalme Sulemani mwenye hekima aliandika hivi: “Mwanzo wa ugomvi ni kama kutoboa penye maji; basi acheni ugomvi kabla haujafurika.”—Mithali 17:14.
Ulimwengu Wote Mzima Uliundwa
Mwishoni mwa Mei wanafizikia kama 200, kutia na washindi kadhaa wa zawadi ya Nobeli, walikutanika Blois, Ufaransa. Mkutano wao wenye urefu wa juma moja ulikuwa wa kuadhimisha mwaka wa 25 wa kugunduliwa kwa “uvunjaji wa sheria ya CP,” ambao waonekana ni kuvunja sheria zenye kufikiriwa kuwa huleta uwiano wenye upatano mkamilifu kati ya vitu vyenye viasili vya kimata na vyenye viasili vipinga-mata.
Lakini nadharia hii hutokeza pia matatizo mengi mbali na kuyatatua. Ikinukuu maneno ya Profesa Mrusi Andrei Linde, International Herald Tribune iliripoti hivi: “Jambo lenye kuleta tokeo la kinyumenyume,” yeye akasema, “ni kwamba uwiano huu wenye upatano ndio uliotokeza ulimwengu wote mzima wenye utaratibu.” Alipouiizwa kama “uvunjaji wa sheria ya CP” ulionyesha kwamba kuna kusudi la kuwako kwa ulimwengu wote mzima, Jean Audouze mtaalamu Mfaransa ashughulikaye na uchunguzi wa umbo la ulimwengu alitaarifu hivi: “Siku fulani-fulani mimi hufikiri kunalo, na siku fulani-fulani mimi hufikiri hakuna. Ulimwengu wote mzima haufanani katika mambo yote. Na ulimwengu wote mzima umeundwa. Na mambo mawili haya yanastaajabisha. Ulimwengu wote mzima si kitu kilichotokea bila mpango.”
Ulimwengu wote mzima haukutokea kwa aksidenti wala bila mpango. Mwanzo 1:1 wasema: “Hapo mwanzo Mungu aliziumba mbingu na nchi.” Ulimwengu wote mzima una utaratibu kwa sababu Yehova, aliye Muumba, “ni Mungu, si mwenye kukosa utaratibu,” bali Mmoja ambaye kazi zake ni “kamilifu.”— 1 Wakorintho 14:33, NW; Kumbukumbu 32:4; linganisha Isaya 40:26; 42:5.
Ugoni-Jinsia-Moja na Wakatoliki
Papa ametaarifu kwa kurudia-rudia kwamba msimamo rasmi wa Kanisa Katoliki kuhusu mwenendo wa ugoni-jinsia-moja ni kwamba ni wenye kosa. Kama aelezavyo, “kwa uhakika jamii ya Ukristo wa mapema haikuwa yenye uendekevu.” Si maaskofu na mapadri wote Wakatoliki hukubali jambo hilo.
Mapema katika 1989, askofu Mfaransa Jacques Gaillot alidai kwamba yeye alikuwa akirudia tu kuyatamka maneno ya Yesu alipoandika kwamba “wagoni-jinsia-moja watutangulia sisi kuingia katika ufalme wa Mungu.”
Hata hivyo, jambo ambalo Askofu Gaillot hakutaja ni kwamba Yesu alikuwa anamaanisha makahaba wenye kutubu—wala si malaya wazoelevu—kwamba ndio wangeingia katika Ufalme wa Mungu wakiwa wamewatangulia viongozi wa Kiyahudi wa siku yake.—Mathayo 21:28-32.
Vivyo hivyo, padri Mhispania Jose Ramon Carrasco aliandika majuzi katika karatasi-habari ya Madrid el Pais kwamba “Yesu Kristo hakuwalaani vikali kamwe wagoni-jinsia-moja. . . . Aliponena juu ya upendo, alinena juu ya kupenda jirani na hakutaja wazi kamwe kama jirani huyo alipaswa kuwa mwanamume au mwanamke, au angepaswa kumpenda akiwa katika kikao gani, umbo gani au jinsi gani.”
Hata hivyo, usimulizi wa Kibiblia waonyesha kwamba Yesu hakuwa akimaanisha mahusiano ya ugoni-jinsia-moja. Katika mfano wa maneno kuhusu Msamaria Mwema, yeye alieleza upendo wa jirani wamaanisha nini hasa, yaani, kuonyesha upendezi usio na ubinafsi katika hali njema ya wengine.—Luka 10:29-37.
Biblia yataarifu hivi kuhusu wenye kuzoea ugoni-jinsia-moja: “Msidanganywe; wala walio wakosa-maadili, wala waabudu-sanamu, wala wazinzi, wala wagoni-jinsia-moja . . . hawatarithi ufalme wa Mungu.”—1 Wakorintho 6:9-11, Revised Standard Version, chapa ya Kikatoliki.