Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w91 1/1 kur. 4-7
  • Shangwe ya Duniani Pote

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Shangwe ya Duniani Pote
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “Shangwe Ambayo Hakuna Mtu Anayeweza Kuiondoa”
  • “Kwenye Sehemu ya Mbali Zaidi Sana ya Dunia”
  • ‘Mwe na Upendo Ninyi kwa Ninyi’
  • Watu Wenye Amani
  • “Umeyaona Mateso Yangu”
  • Tumikia Yehova kwa Shangwe ya Moyo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Mtumikie Yehova kwa Moyo Wenye Kujaa Furaha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Watu Wenye Furaha—Kwa Sababu Gani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • Wafanya Kazi Wenzi Katika Mavuno
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
w91 1/1 kur. 4-7

Shangwe ya Duniani Pote

“TAZAMA, watumishi wangu wataimba kwa furaha [shangwe, NW] ya moyo.” (Isaya 65:14) Ndivyo alivyosema Yehova kupitia nabii wake Isaya, na lo! maneno yake yanapata utimizo mzuri kama nini miongoni mwa Mashahidi wa Yehova! Inatoka wapi shangwe ya moyo wao? Kutokana na ibada yao yenye umoja ya Yehova Mungu. Yeye ndiye “Mungu mwenye furaha,” na wale wanaomwabudu ‘wana shangwe katika Yehova.’ (1 Timotheo 1:11; Zekaria 10:7, NW) Ujitoaji huu wenye shangwe unawa-leta katika umoja wa kuwa taifa moja huku wote pamoja wakihubiri habari njema za Ufalme na kupaaza sauti ya duniani pote ya sifa kwa Mungu wao.—Ufunuo 7:9, 10.

“Shangwe Ambayo Hakuna Mtu Anayeweza Kuiondoa”

Kwa kweli, kutangaza jina na Ufalme wa Mungu ni chanzo cha shangwe ya daima kwa Mashahidi wa Yehova. (Marko 13:10) Wao wanaitikia maneno ya mtunga zaburi: “Jisifuni kwa jina lake takatifu, na ufurahi moyo wao wamtafutao BWANA [Yehova, NW].”—Zaburi 105:3.

Mara nyingi, wao wanashinda vipingamizi ili kufanya hilo. Katika Hispania, Isidro alijiweka wakfu kwa Yehova, naye alitaka kuongea na wengine juu Yake. Lakini yeye ni mwendeshaji wa gari kubwa mwenye wakati mchache wa kuwa huru, mwenye kufunga safari ndefu wakati wa usiku na kulala wakati wa mchana. Isidro alitaka kutoa ushahidi kwa waendeshaji wengine wa magari makubwa, lakini angewezaje kufanya hivi?

Aliunga katika gari lake kubwa redio aina ya CB (“citizens band”) ambayo angeweza kutumia kuongea na waendeshaji wengine wa magari. Upesi akagundua kipitio kimoja cha kupashana habari kisichotumiwa sana, cha 13, akaamua kukitumia kwa faida. Bila shaka, mara ya kwanza alipoomba waendeshaji wengine wa magari makubwa kuongea nao juu ya Biblia katika redio CB, jibu halikuwa zuri. Lakini wengine wao walisikiliza. Habari ikaenea, na wengi zaidi na zaidi wa hao waendeshaji Wahispania wa magari makubwa wakafungulia kipitio cha kupashana habari cha 13. Hivi majuzi, Isidro alipata habari kwamba ingawa mtu mmoja anachukua hatua za kuendeleza funzo lake la Biblia.

Katika Italia mwanamume mmoja alipata habari juu ya Mashahidi wa Yehova kupitia maongezi aliyokuwa nayo ndani ya bus. Mke wake alikutana nao kupitia rafiki. Wote wawili walijifunza Biblia wakawa na hamu ya kushiriki na wengine mambo waliyojifunza. Walikuwa na hamu sana hivi kwamba mwanamume huyo alikataa kupandishwa cheo katika kazini naye mke akaacha kazi yenye mshahara mnono ili waweze kutumia wakati mwingi zaidi kueleza wengine habari njema za Ufalme. Je! ilistahili? Ndiyo. Mwanamume huyo anasema hivi: “Tangu sisi tulipopata kujua ukweli, mke wangu na mimi tumekuwa na shangwe ya kusaidia watu 20 waje kwenye maarifa sahihi juu ya kusudi la Mungu. Jioni inapofika, na mimi ninaporudi nyumbani baada ya mchana wa kuwa katika utumishi wa Yehova, ni kweli ninajisikia nimechoka. Lakini nina furaha, nami namshukuru Yehova kwa kuwa amenipa shangwe ambayo hakuna mtu anayeweza kuiondoa.”

“Kwenye Sehemu ya Mbali Zaidi Sana ya Dunia”

Wale walio katika taifa la Mungu lenye shangwe wanaonyesha bidii kama hiyo popote walipo, hata katika “sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia.” (Matendo 1:8, NW) Ni mahali pachache palipo mbali kuliko Greenland ya kaskazini. Na bado, hata huko, kilometa  320 kaskazini ya Duara ya Aktiki, kuna lile kundi dogo la Ilulissat, lenye watu 19. Wao wanahubiri habari njema zile zile kama wale mume na mke Waitalia, nao walisisimuka mwaka uliopita kuona watu saba wa Greenland wakibatizwa kwa ufananisho wa wakfu wao kwa Yehova.

Maelfu mengi ya kilometa kutoka Greenland, katika kisiwa cha kitropiki cha Mauritius katika Bahari ya Hindi, Anjinee ana shangwe iyo hiyo. Hapo kwanza mambo yalikuwa magumu kwa Anjinee. Katika Mauritius kuhudhuria mikutano ya Kikristo na kuhubiri peupe juu ya Mungu ni mambo yasiyoonwa kuwa utendaji unaomfaa binti mseja wa asili ya Uhindu wa India. Lakini Anjinee alivumilia. Sasa, miaka tisa baada ya yeye kuanza mwendo wake wa Kikristo, wengine wa watu wa ukoo wake wanajifunza Biblia pia.

Kuhusiana na Anjinee inapasa kutaja Emilio, upande ule mwingine wa ulimwengu, katika Honduras. Emilio alisikia wafanya kazi wenzake wakizungumzia Biblia kazini naye akaomba ashiriki mazungumzo. Hakujua kusoma lakini alisikiliza kwa furaha maandiko ya Biblia yaliposomwa. Ukweli wa Kikristo ulipopenya moyo wake, Emilio aliacha mtindo-maisha wake wa kukosa adili na akaacha kunywa kupita kiasi. Mashahidi wa Yehova walimfundisha kusoma na kuandika, na sasa yeye ni mhudumu katika taifa la Mungu lenye shangwe.

Maelfu ya kilometa kaskazini-magharibi ya Honduras, mama mmoja Mweskimo katika Alaska alijifunza ukweli ule ule wa Kikristo. Bibi huyu aliishi katika kijiji kilichojitenga sana, na njia yake pekee ya kupashana habari na Mashahidi wa Yehova ilikuwa kupitia barua. Hivyo basi alijifunza kupitia barua, akauliza maswali yake kwa barua, na sasa anashiriki kwa bidii kujulisha jirani zake mambo anayoyajua. Mifano kama hii ingeweza kuzidishwa kwa karibu mara zisizojulikana. Kotekote duniani, watu wenye mioyo ya usikivu wanakuja ‘kutumikia Yehova kwa mshangilio.’—Zaburi 100:2, NW.

‘Mwe na Upendo Ninyi kwa Ninyi’

Jambo moja linalovutia watu wote hawa ni ule upendo ulio katika taifa la Mungu lenye shangwe. Yesu alisema hivi: “Mkipendana, watu wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu.” (Yohana 13:35, HNWW) Upendo wa Kikristo unaonekana katika maisha za kila siku za Wakristo hawa wa kweli, na hasa katika nyakati za taabu.

Katika nchi moja ya Kiafrika ambako, kwa kusikitisha, utendaji wa Mashahidi wa Yehova umepigwa marufuku, kulikuwa na ukavu mbaya sana. Watu kumi elfu walikufa, na makundi mazima ya ng’ombe yakaangamia. Mashahidi waliendeleaje kuwa hai? Kwa kula mizizi ya mimea na kokwa zilizopikwa za maparachichi (avokado)! Lakini shida yao ilipunguzwa sana wakati ambapo, kwa msaada wa Mungu, bila kutazamia Mashahidi katika nchi nyinginezo walipata ruhusa kupeleka humo tani 25 za misaada. Kwa kweli, kujapokuwa na marufuku, misaada hii ilisindikizwa na maaskari-jeshi kuhakikisha imetolewa kwa usalama!

Kwa kweli, Mashahidi hao Waafrika walipata shangwe nyingi mno kupokea uhakikisho huu wa upendo wa ndugu zao kwa ajili yao huku wakijionea utimizo wa maneno ya Isaya: “Tazama, mkono wa BWANA [Yehova, NW] haukupunguka, hata usiweze kuokoa; wala sikio lake si zito, hata lisiweze kusikia.”—Isaya 59:1.

Watu Wenye Amani

Watu wenye mioyo ya usikivu wanavutiwa pia kwenye taifa la Mungu lenye shangwe kwa sababu washiriki walo wameacha njia za kivita za ulimwengu huu na ‘wakafua panga zao ziwe majembe.’ (Isaya 2:4) Katika El Salvador, nyumba ya mwanamume mmoja aliyekuwa askari-jeshi hapo kwanza ilijaa kumbukumbu za kazi-maisha yake ya kijeshi. Lakini alipoanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, alisitawisha mapendezi ya amani. Mwishowe, aliondolea nyumba yake kila kitu kilichohusiana na vita na akaanza kazi ya kuhubiri kwa bidii.

Majeshi yenye kupinga serikali yalipokamata kijiji chake, alichukuliwa kuwa mfungwa—kwa wazi mtu fulani alionyesha kwamba hapo kwanza yeye alikuwa askari-jeshi. Hata hivyo, yeye akaeleza kwamba hakuwa tena askari bali mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Wataka mapinduzi walimshtaki juu ya kuwa na silaha katika nyumba yake, lakini utafutaji ukafunua kwamba hakuwa na yoyote. Msimamizi wa wataka mapinduzi ndipo akauliza majirani juu yake. Mfano mmoja wa maelezo yaliyotolewa ni huu: “Yeye anatembea huku na huku tu barabarani akihubiri juu ya Biblia siku baada ya siku.” Mwanamume huyo aliachiliwa. Bila shaka, bidii yake ilitumika kuokoa maisha yake.

Ripoti kutoka nchi moja ya Kiafrika inaeleza juu ya askari wawili waliojifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Mmoja alitumikia katika jeshi la serikali, yule mwingine alipigana upande wa waasi. Mwishowe, wote wawili wakaamua ‘kufua panga zao ziwe majembe’ nao wakajiondoa katika kazi ya askari-jeshi. Walipohudhuria mikutano ya Kikristo kwa mara ya kwanza, yule askari mpinga serikali aliuliza yule mwingine hivi: “Unataka nini hapa?” Yeye akajibu: “Na wewe je, unataka nini hapa?” “Halafu,” ripoti inamalizia, “kwa kukumbatiana, walitoa machozi ya shangwe kwa sababu wangeweza kuwa pamoja katika amani.” Wanaume wote hawa wawili waliokuwa wanajeshi hapo kwanza bila shaka walisali kwa Mungu hivi: “Ee MUNGU [Yehova, NW], Mungu wa wokovu wangu, uniponye na damu za watu, na ulimi wangu utaiimba haki yako.”—Zaburi 51:14.

“Umeyaona Mateso Yangu”

“Na nishangilie, nizifurahie fadhili zako, kwa kuwa umeyaona mateso yangu. Umeijua nafsi yangu taabuni.” (Zaburi 31:7) Ndivyo alivyosali mtunga zaburi, na wengi leo wanashangilia kwa sababu Neno la Mungu linawasaidia kuelekeana na mateso yao. Katika Ufaransa mmoja wa Mashahidi wa Yehova anaongoza funzo pamoja na mwanamke anayesumbuliwa na skizofrenia (ugonjwa wa akili). Mwanamke huyu alikuwa amekuwa chini ya matibabu ya akili kwa muda fulani, lakini yakawa hayakusaidia. Juma lile la baada ya yeye kuanza funzo lake, daktari wa akili alimwuliza hivi: “Je! kweli wewe unaelewa jambo ambalo mwanamke huyo anakueleza kutokana na Biblia?” Hivyo basi juma lililofuata, yule Shahidi akaenda kwenye ofisi yake na kujifunza Biblia pamoja na bibi huyo daktari akiwapo.

Baada ya funzo, huyo daktari wa akili alimwambia Shahidi hivi: “Muda wa miaka iliyopita nimekuwa na upendezi katika dini za wagonjwa wangu, lakini niliona kwamba hakuna tegemezo halisi lililotolewa na dini yoyote. Ingawa hivyo, katika kisa chako mambo ni tofauti. Bi. P — anakuja mara mbili kwa juma kupata ushauri, naye ananilipa kwa jambo hilo. Na bado, kwa fundisho lako la Biblia na ushauri mwema, wewe unafanya kazi nzuri zaidi bila malipo. Anafanya maendeleo mazuri. Endelea na wema huu, nami nakuhakikishia ushirikiano wangu kamili wakati wowote utakapouhitaji.”

Biblia inasema hivi: “Heri watu wanaojua sauti ya furaha; wanakwenda, Ee BWANA [Yehova, NW], kwa nuru ya uso wako. Kwa jina lako wanafurahi muchana kutwa.” (Zaburi 89:15, 16, ZSB) Kila mmoja wa Mashahidi wa Yehova anajua kwamba zaburi hii ni ya kweli. Kutoka kwenye vinywa vyao mpaazo wa sauti ya shangwe duniani pote unapanda juu kwa sifa ya Yehova. Wengi zaidi na zaidi wanamiminika kutoka mataifa kumsifu Mungu pamoja nao. Kwa nini usishirikiane nao ujionee shangwe hiyo wewe mwenyewe?

[Picha katika ukurasa wa 7]

Mashahidi wa Yehova wanapatikana katika mataifa yote na wanasema mamia ya lugha tofauti. Lakini wote wanasema lugha ile ile ya ukweli na wote ni wa taifa lenye shangwe lile lile moja

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki