Krismasi—Je! Ndiyo Njia ya Kumkaribisha Yesu?
KUZALIWA kwa Mkombozi, Mesiya aliyengojewa kwa muda mrefu, kulikuwa wakati wa kushangilia kweli kweli. “Msiogope!” malaika akawatangazia wachungaji katika ujirani wa Bethlehemu, “Nimewaleteeni habari njema ya furaha kuu kwa watu wote. Kwa maana leo hii katika mji wa Daudi amezaliwa Mwokozi kwa ajili yenu, ndiye Kristo Bwana.” Malaika wengi wakajiunga, wakimsifu Mungu hivi: “Utukufu kwa Mungu juu mbinguni, na amani duniani kwa watu aliopendezwa nao.” (Luka 2:10-14, Habari Njema kwa Watu Wote) Wengine huenda wakakata maneno kwamba Wakristo wanapaswa kuwaiga malaika hao katika kuonyesha shangwe juu ya kuja kwa Kristo duniani wakati huo wa nyuma.
Hiyo haikuwa rekodi ya kwanza katika Biblia ya malaika wakipaza sauti katika nyimbo za sifa. Msingi wa dunia ulipowekwa, ‘nyota za asubuhi ziliimba pamoja, na wana wote wa Mungu wakapiga kelele kwa furaha.’ (Ayubu 38:4-7) Tarehe barabara ya tukio hilo haikurekodiwa katika Biblia. (Mwanzo 1:1, 14-18) Iwe kipindi hicho kilikuwa chenye shangwe jinsi gani, Wakristo hawajatoa hoja kwamba kwa sababu malaika walipiga makofi, wao wanapaswa kusherehekea kila mwaka uumbaji wa dunia na labda kutumia sikukuu ya kipagani ili kuadhimisha kipindi hicho.
Na bado hivyo ndivyo watu waadhimishao Krismasi wanavyofanya kuhusu kuzaliwa kwa Yesu Kristo. Uchunguzi katika karibu ensaiklopedia yoyote yenye kutegemeka chini ya kichwa “Krismasi” huthibitisha kwamba tarehe ya kuzaliwa kwa Kristo haijulikani. Biblia haisemi lolote kuhusu tarehe hiyo.
“Baragumu Ikitoa Sauti Isiyojulikana”
“Mungu si Mungu wa machafuko, bali wa amani,” akaandika mtume Paulo, kwa kusahihisha kukosa utaratibu kwa kundi katika Korintho ya kale. Katika muktadha uo huo, aliuliza hivi: “Baragumu ikitoa sauti isiyojulikana, ni nani atakayejifanya tayari kwa vita?” (1 Wakorintho 14:8, 33) Sasa, ikiwa Mungu wa utaratibu alikusudia Wakristo waadhimishe kuzaliwa kwa Mwana wake duniani, je, Yeye angewaacha wanadamu wasiokamilika wachague kwa maoni yao wenyewe tarehe kutokana na sikukuu za kipagani na kukubali mazoea yasiyo ya kimungu?
Kuchunguza mifano michache ya Kibiblia kunaelewesha wazi kwamba Yehova Mungu hashughuliki na watu wake katika njia hiyo. Wakati alipotaka Waisraeli wafanye miadhimisho ya kila mwaka chini ya Sheria ya Musa, Mungu alichagua tarehe mahususi na kuwaambia jinsi ya kuadhimisha vipindi hivyo vya sikukuu. (Kutoka 23:14-17; Mambo ya Walawi 23:34-43) Ingawa Yesu Kristo hakuagiza kamwe kuzaliwa kwake kuadhimishwe, aliwaagiza wafuasi wake waadhimishe tarehe moja mahususi. “Usiku ule aliotolewa,” Nisani 14, 33 W.K., Yesu alianzisha mwadhimisho wa Chakula cha Jioni cha Bwana, kwa kutumia mkate usiotiwa chachu na divai. Aliagiza hivi: “Fanyeni hivi kwa ukumbusho wangu.” (1 Wakorintho 11:23, 24) Sauti ya baragumu kuhusu ni wakati gani na jinsi gani Chakula cha Jioni cha Bwana kingeadhimishwa iko wazi na dhahiri. Basi vipi kuhusu Krismasi? Hatupati mahali popote katika Biblia agizo lolote la kuadhimisha kuzaliwa kwa Kristo, wala haituambii ni wakati gani au jinsi gani ya kufanya hivyo.
‘Kuwapata Watu’
“Ee, bila shaka ninajua Krismasi ina mwanzo wa kipagani,” akasema kasisi mmoja kwenye Kanisa la Sayuni la Tokyo, “lakini maadam watu wa kawaida wanapendezwa na Ukristo wakati wa Desemba 25 na wanapata kujifunza mafundisho ya Yesu Mheshimiwa, Krismasi ina mahali payo katika Ukristo.” Wengi hukubaliana na kusababu kwake. Je! unaamini kwamba kuridhiana kwa jinsi hiyo kunafaa?
Wengine hutoa hoja kwamba hata Paulo aliridhiana ili kupata waamini. “Mimi hujifanya mtumwa wa kila mtu,” yeye akaandika, “ili nivute watu wengi kadiri iwezekanavyo . . . Ninapofanya kazi pamoja na Wasio Wayahudi, mimi huishi kama Asiye Myahudi, nje ya Sheria ya Kiyahudi, ili ni wavute Wasio Wayahudi. . . . Yote haya mimi hufunya kwa ajili ya gospeli, ili kushiriki katika baraka zayo.” (1 Wakorintho 9:19-23, Today’s English Version) Je! maneno hayo yanaonyesha kwamba ni jambo la haki kutumia sikukuu ya kipagani ili kuwavutia Wasio Wayahudi kwenye Ukristo?
Fikiria kwa uangalifu muktadha wa taarifa ya Paulo. Katika mstari wa 21, alisema hivi: “Hii haimaanishi kwamba mimi sitii sheria ya Mungu; kwa kweli niko chini ya sheria ya Kristo.” (TEV) Kwa hiyo yeye hakuridhiana katika mambo yaliyokiuka sheria ya Kristo, bali ‘aliishi kama Asiye Myahudi’ kwa kustahi desturi na mazoea ya kwao maadam hazikupingana na amri za Kikristo.a
Ukiwa na hilo akilini, fikiria jinsi kukubali sikukuu za kipagani katika “Ukristo” kwa kuziita Krismasi kungeonekana kwa kuonwa kulingana na amri ya Biblia inayofuata: “Msifungiwe nira pamoja na wasioamini, kwa jinsi isivyo sawasawa; kwa maana pana urafiki gani kati ya haki na uasi? . . . Au yeye aaminiye ana sehemu gani pamoja na yeye asiyeamini? . . . Kwa hiyo, tokeni kati yao, mkatengwe nao, asema Bwana [Yehova, NW], msiguse kitu kilicho kichafu, nami nitawakaribisha.” (2 Wakorintho 6:14-17) Haidhuru ni udhuru upi mbalimbali unaotolewa, kughoshi Ukristo na sikukuu za kipagani siyo njia ya kumkaribisha Yesu akiwa Mwokozi. Lingalikuwa jambo lisilofaa katika karne ya kwanza wakati Yesu alipokuja katika mnofu, na vivyo hivyo haifai leo wala katika wakati ujao, wakati Kristo atakapokuja akiwa Mfalme kutekeleza hukumu za Mungu. (Ufunuo 19:11-16) Kwa hakika, wale wanaopendelea kuadhimisha sikukuu za kipagani kwa kisingizio cha kwamba ni “za Kikristo” huenda sana wakawa wanamkana Yesu Kristo.
“Wakristo Waliojificha” Hawakurudishwa
Jifunze kutokana na kile kilichowapata Wakatoliki katika Japani wakati wa enzi ya shogun (gavana wa kijeshi). Ukatoliki ulipoanza kukandamizwa katika 1614, Wakatoliki Wajapani 300,000 hivi walikuwa na mambo matatu ya kuchagua: kuwa wafia-imani, kuacha imani yao, au kuendelea kisiri. Wale walioendelea kisiri waliitwa Wakristo waliojificha. Ili kuendesha imani yao kisirisiri, walifuata desturi mbalimbali za Kibuddha na Kishinto. Katika kawaida yao ya ibada, walitumia Maria Kannon, ambaye alikuwa Maria aliyegeuzwa kuwa bodhisattva wa Kibuddha katika umbo la mama anayebeba mtoto. Sikukuu zao zilichanganya dini ya Kibuddha, ya Kikatoliki, na desturi za Kishinto. Hata hivyo, walipolazimishwa kuhudhuria maziko ya Kibuddha, waliimba sala za Kikristo na kufanya modoshi, sherehe ya kubatilisha mahubiri ya Kibuddha. Ni jambo gani limewapata “Wakristo” hao?
“Kwa maoni ya Kirishitans [Wakristo] walio wengi,” chaeleza kitabu The Hidden Christians, “ushikamano wa kidini ulikua ndani yao ukifanya iwe vigumu kuacha ibada ya miungu ya Kishinto na Kibuddha.” Marufuku yalipoondolewa na wamisionari Wakatoliki kurudi Japani, walio wengi wa wale “Wakristo waliojificha” walishikilia aina yao ya dini ya mchanganyiko.
Hata hivyo, je, Kanisa la Katoliki lingeweza kwa kufaa kuwachambua wale “Wakristo waliojificha” waliokataa kurudishwa kwa Ukatoliki wa Kiroma? Kanisa la Katoliki limekubali hivyo hivyo mafundisho na sikukuu nyingine za kipagani, kutia ndani Krismasi. Ikiwa Wakatoliki na Waprotestanti, huku wakidai kuwa Wakristo, wamefanya “Ukristo” wao uwe wa kipagani kwa sikukuu za kipagani, je, wasingekuwa pia wakimkataa Yesu Kristo?
Warudishwa Kwenye Ukristo wa Kweli
Setsuko, Mkatoliki mchaji kwa miaka 36, alipata kutambua jambo hilo hatimaye. Baada ya Vita ya Ulimwengu 2, alijaribu kujaza hali yake ya uwazi wa kiroho kwa kushirikiana na kanisa la Katoliki. ‘Inaridhisha kama nini!’ alifikiri alipohudhuria Misa ya Krismasi na kuona miti mizuri sana ya Krismasi ndani na nje ya kanisa lake. “Nilionea fahari mapambo yetu mazuri, yaliyoshinda yale ya makanisa ya karibu,” akasema. Hata hivyo, Setsuko kwa kweli hakuwa na uelewevu wowote wa mafundisho ya Kikatoliki, ingawa alikuwa hata akifundisha shule ya Jumapili kwa muda fulani. Kwa hiyo alipotaka kushughulika zaidi katika kazi ya kanisa, alimwuliza padri wake maswali machache. Badala ya kujibu maswali yake, padri alimfanya aonekane mdogo. Kwa kutamauka, aliamua kujifunza Biblia yeye mwenyewe. Majuma mawili baadaye, Mashahidi wa Yehova wakamtembelea, naye akakubali funzo la Biblia nyumbani.
Yeye aeleza hivi: “Ilinitia uchungu kukabili kweli za Biblia zilizokanusha mambo niliyoamini mbeleni. Hata nikapatwa na alopecia neurotica, ugonjwa wa kupoteza nywele kwa ajili ya kufadhaika. Hata hivyo, polepole nuru ya kweli ikaangaza moyoni mwangu. Nilishangaa sana kujifunza kwamba Yesu asingaliweza kuzaliwa katika Desemba yenye baridi na mvua, wakati wachungaji wasingaliweza kuchunga kondoo zao wakiwa nje usiku. (Luka 2:8-12) Hilo liliondolea mbali maoni yangu ya siku ya kuzaliwa kwa Yesu, kwani tulikuwa tumetumia pamba kuwa kama theluji kupamba mandhari za kondoo na wachungaji.”
Baada ya kujisadikishia mwenyewe kuhusu mambo ambayo Biblia hufundisha kweli kweli, Setsuko akaamua kuacha kusherehekea Krismasi. Yeye hana tena “ile roho ya Krismasi” mara moja kwa mwaka bali yeye hudhihirisha kila siku ile roho ya kutoa kwa uchangamfu wa Kikristo.
Ikiwa wewe unamwamini Kristo kwa moyo mweupe, usikasirike unapoona wapagani wakinajisi Krismasi. Wanarudia tu kile ilichokuwa mwanzoni—sikukuu ya kipagani. Krismasi haimwongozi mtu yeyote kumkaribisha Yesu Kristo, ambaye amerudi kwa hali ya kutoweza kuonekana akiwa Mfalme wa kimbingu. (Mathayo, sura 24 na 25; Marko, sura 13; Luka, sura 21) Badala ya hiyo, Wakristo wa kweli huonyesha roho ya kufanana na Kristo mwaka mzima, na wao hutangaza rasmi habari njema za Ufalme, ambao Yesu amekuwa Mfalme. Hivyo ndivyo Mungu ataka tumkaribishe Yesu Kristo akiwa Mwokozi wetu na Mfalme wa Ufalme.—Zaburi 2:6-12.
[Maelezo ya Chini]
a Linganisha njia mbili ambazo kwazo Paulo aliitikia juu ya swala la tohara. Ingawa alijua kwamba “kutahiriwa si kitu,” yeye alimtahiri Timotheo mwandamani wake wa kusafiri, aliyekuwa Myahudi kwa upande wa mama yake. (1 Wakorintho 7:19; Matendo 16:3) Katika kisa cha Tito, mtume Paulo aliepuka kumtahiri likiwa jambo la kikanuni katika shindano pamoja na Watetezi wa Dini ya Kiyahudi. (Wagalatia 2:3) Tito alikuwa Mgiriki na kwa hiyo, tofauti na Timotheo, yeye hakuwa na sababu yoyote halali ya kutahiriwa. Ikiwa yeye, mtu Asiye Myahudi, angetakiwa atahiriwe, ‘Kristo hangemfaidia neno.’—Wagalatia 5:2-4.
[Picha katika ukurasa wa 7]
Wakristo wa kweli humheshimu Yesu mwaka mzima