Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w92 7/1 kur. 21-23
  • Mimi Niliitikia Wakati wa Mavuno

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mimi Niliitikia Wakati wa Mavuno
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ndoa na Mambo ya Kusisimua
  • Kukubali Kweli
  • Kuvuna Katika Rasi ya Palmas
  • Kwenda Buchanan ya Chini
  • Mapendeleo na Baraka za Ziada
  • Niliacha Kupiga Watu Barabarani Nikawa Mhudumu Mkristo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Kumkaribia Mungu Kulinisaidia Niwezane na Hali
    Amkeni!—1993
  • Shangwe na Matatizo ya Kuwalea Watoto Wanane Ili Wafuate Njia za Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Kitabu-mwaka cha Mashahidi wa Yehova 1990
    1990 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
w92 7/1 kur. 21-23

Mimi Niliitikia Wakati wa Mavuno

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA WINIFRED REMMIE

“MAVUNO ni mengi, lakini watenda kazi ni wachache.” Maneno hayo ya Bwana Yesu yalichochewa na huruma nyingi kwa ajili ya watu waliokuwa hoi na kutawanyika kama kondoo wasio na mchungaji. Nimekuwa na hisia hiyo hiyo, na kwa miaka 40 iliyopita, nimejaribu sikuzote kuitikia ifaavyo mwito wa Bwana Mkubwa wa kufanya kazi wakati wa mavuno—Mathayo 9:36, 37, HNWW.

Nilizaliwa Afrika Magharibi katika familia yenye watoto saba, wote wasichana. Wazazi wetu walikuwa wororo, walakini wenye kushurutisha utii; walikuwa pia wenye kufuatia dini sana. Kuhudhuria kanisa na shule ya Jumapili kila juma kusingeweza kuepukwa. Kwangu hilo halikuwa tatizo kwa sababu nilipenda mambo ya kiroho. Kwa kweli, nikiwa na umri wa miaka 12, niliwekwa rasmi kuongoza masomo ya shule ya Jumapili.

Ndoa na Mambo ya Kusisimua

Katika 1941, nikiwa na umri wa miaka 23, niliolewa na Lichfield Remmie, karani wa hesabu kwenye ofisi ya serikali. Tulikuwa wenye ufanisi kifedha, lakini upendo wa mambo ya kusisimua na tamaa ya kupata utajiri wa kimwili ilitupeleka Liberia katika 1944. Badiliko katika maisha ya mume wangu, na hatimaye katika maisha yangu, lilikuja katika 1950 alipokutana na Hoyle Ervin, mishonari wa Mashahidi wa Yehova. Baada ya majuma matatu tu ya kujifunza, mume wangu alianza kushiriki katika kazi ya kuhubiri.

Niliudhika wakati mume wangu alipoacha kuhudhuria kanisa. Kwa vyovyote vile, alikuwa Mprotestanti mwaminifu ambaye hata alifunga kula wakati wa majira ya Lenteni. Wakati wa kwanza nilipomwona akienda kuhubiri, akiwa na mkoba mkononi, nilikasirika sana. “Ni jambo gani limekupata?” nikataka kujua. “Mtu mashuhuri kama wewe kwenda kuhubiri pamoja na watu hao wapumbavu!” Alikuwa mpole na mtulivu wakati wa karipio hilo.

Siku iliyofuata, Ndugu Ervin alitembelea nyumba yetu ili kujifunza na Lichfield. Kama kawaida, nilinyamaza wakati wa funzo hilo. Labda ni kwa sababu hiyo kwamba Ndugu Ervin aliniuliza kama sikujua kusoma. Nini? Mimi, nisijue kusoma? Hayo ni matukano yaliyoje! Ningemwonyesha jinsi nilivyoelimika! Ningefunua dini hiyo bandia!

Kukubali Kweli

Muda mfupi baada ya hayo, niliona kitabu Let God Be True (Acheni Mungu Apatikane Kuwa wa Kweli) kwenye meza ya sebule. ‘Hicho ni kichwa cha upuzi kama nini,’ nikawaza. ‘Mungu amekuwa wa kweli sikuzote, ama sivyo?’ Nilipopitia kitabu hicho, upesi nilipata sababu nyingine ya kulalamika. Kilisema kwamba mwanadamu hana nafsi, yeye ni nafsi! Hata mbwa na paka ni nafsi! Hilo lilinikasirisha kweli kweli. ‘Hilo ni fundisho la upumbavu kama nini!’ nikawaza.

Mume wangu aliporudi, nilimkabili kwa hasira. “Wadanganyi hawa husema kwamba mwanadamu hana nafsi. Hawa ni manabii wawongo!” Mume wangu hakugombana; badala ya hiyo, alijibu kwa utulivu: “Winnie, kila kitu kimo katika Biblia.” Baadaye, wakati Ndugu Ervin aliponionyesha kwa saburi kutoka kwa Biblia yangu mwenyewe kwamba sisi ni nafsi na kwamba nafsi yetu inaweza kufa, nilishangaa. (Ezekieli 18:4) Lile lililonivutia hasa ni lile andiko kwenye Mwanzo 2:7, linalotaarifu hivi: “Mtu [Adamu] akawa nafsi hai.”

Nilikuwa nimekosea kama nini! Nilihisi nimedanganywa na makasisi na sikuhudhuria kanisa tena kamwe. Badala ya hiyo, nilianza kuhudhuria mikutano ya Kikristo ya Mashahidi wa Yehova. Ilivutia kama nini kuona upendo uliokuwa miongoni mwao! Hiyo bila shaka ilikuwa ndiyo dini ya kweli.

Kuvuna Katika Rasi ya Palmas

Karibu miezi mitatu baadaye, mume wangu alikuwa na nafasi ya kuiba kiasi kikubwa cha pesa kutoka kwa kampuni alikofanyia kazi—lakini hakufanya hivyo. Wafanyakazi wenzake walimdhihaki: “Remmie, utakufa ukiwa maskini.”

Hata hivyo, kwa sababu ya unyoofu wake, alipandishwa cheo na kutumwa kwenye Rasi ya Palmas ili afungue ofisi mpya huko. Tulihubiri kwa bidii na baada ya miezi miwili tu, tulikuwa na kikundi kidogo kilichopendezwa sana na ujumbe wa Biblia. Baadaye, wakati Lichfield aliposafiri kwenda mji mkuu, Monrovia, ili kupata vifaa vya ofisi mpya, alibatizwa. Pia aliomba msaada kutoka kwa Sosaiti ili kutunza wale katika Rasi ya Palmas waliokuwa wakionyesha kupendezwa na kweli.

Sosaiti iliitikia kwa kutuma Ndugu na Dada Faust kwenye Rasi ya Palmas. Dada Faust alinisaidia sana, na katika Desemba 1951, nilionyesha wakfu wangu kwa Yehova kwa kubatizwa. Sasa kushinda wakati mwingine wowote, nilipiga moyo konde “kukusanya matunda kwa uzima wa milele.” (Yohana 4:35, 36) Katika Aprili 1952, nilianza huduma ya wakati wote nikiwa painia.

Jitihada zangu zilibarikiwa na Yehova mara moja; katika mwaka mmoja, nilisaidia watu watano hadi wakfu na ubatizo. Mmoja wao, Louissa Makintosh, alikuwa binamu wa aliyekuwa rais wa Liberia wakati huo, W. V. S. Tubman. Alibatizwa na kuingia huduma ya wakati wote naye aliendelea akiwa mwaminifu kwa Mungu hadi kifo chake katika 1984. Pindi nyingi alitolea rais huyo ushahidi.

Kwenda Buchanan ya Chini

Katika 1957, wakati wa ziara ya mwangalizi wa wilaya, mume wangu na mimi tulialikwa kuwa mapainia wa pekee. Baada ya mazungumzo ya pamoja na sala, tulikubali mgawo huo. Lichfield alihitaji miezi kadhaa ili kumaliza kazi yake ya kimwili katika Rasi ya Palmas, kwa hiyo nilitangulia kwenda Buchanan ya Chini, eneo lisilohubiriwa, ili kuanza kazi ya kuhubiri huko.

Baada ya kufika huko, nilikaa pamoja na familia ya akina Maklean. Siku iliyofuata, kama ilivyokuwa desturi, nilipelekwa kwa mdogo wa chifu wa kabila la Pele. Chifu huyo na familia yake walinikaribisha kwa uchangamfu nami nilitolea ushahidi kikundi kidogo cha watu nyumbani mwake. Watu wasiopungua sita wa wale niliosema nao siku hiyo, kutia na huyo mdogo wa chifu pamoja na mke wake, walikuwa Mashahidi hatimaye.

Upesi nilijipata nikiongoza funzo la Mnara wa Mlinzi kukiwa na hudhurio la watu zaidi ya 20. Nilihitaji kumtegemea Yehova sana, naye alinipa imara na uwezo uliohitajiwa ili kutunza kondoo zake. Nilipojihisi nimechoka au nimekosa utoshelevu, ningekumbuka waaminifu wa zamani, hasa wanawake kama vile Debora na Hulda, waliotekeleza tume za Yehova bila woga.—Waamuzi 4:4-7, 14-16; 2 Wafalme 22:14-20.

Katika Machi 1958, baada ya miezi mitatu tu katika Buchanan ya Chini, nilipokea barua iliyoniarifu juu ya ziara ya mwangalizi wa mzunguko, John Sharuk. Nilikodi chumba cha chini ya nyumba fulani kilichoweza kutosha umati mkubwa. Kisha nikasafiri hadi Buchanan ya Juu kukutana na Ndugu Sharuk, lakini hakuja. Baada ya kungojea hadi giza la jioni, nilirudi Buchanan ya Chini nikiwa nimechoka.

Katika usiku wa manane, nilisikia mlango ukibishwa. Nilipoufungua, nilimwona si mwangalizi wa mzunguko peke yake bali pia na mume wangu, ambaye kuwasili kwake kwa ghafula kulilingana vizuri sana na kuwasili kwa Ndugu Sharuk. Walinipataje? Walikuwa wamekutana na mwindaji na kumwuliza ikiwa alimjua mwanamke aliyehubiria watu juu ya Yehova. “Ndiyo,” akajibu, na kisha akawaelekeza hadi nyumbani kwangu. Nilifurahi jinsi gani kwamba kwa muda wa miezi mitatu tu katika Buchanan ya Chini, nuru yangu ilikuwa inang’aa kwa uangavu sana!—Mathayo 5:14-16.

Tulifurahia kilele cha hudhurio cha watu 40 wakati wa ziara ya Ndugu Sharuk. Baadaye kundi lenye kusitawi lilianzishwa, na tuliweza kujenga Jumba la Ufalme lenye kupendeza. Hata hivyo, maisha hayakuwa bila matatizo sikuzote. Kwa mfano, katika 1963 mnyanyaso wa kidini ulitokea katika Kolahun, na mume wangu alikamatwa na kufungwa gerezani. Alipigwa vibaya sana hivi kwamba akalazimika kulazwa hospitali.

Muda mfupi baada ya kuondoka kwake hospitali, mwaka huo huo, tulikuwa na mkusanyiko katika Banga. Katika siku ya mwisho, askari-jeshi walikusanya wote waliohudhuria wakatuamuru tuisalimu bendera. Tulipokataa, askari-jeshi hao walitulazimisha tuweke mikono yetu juu na kulitazama jua moja kwa moja. Pia walipiga wengine wetu kwa sehemu ya nyuma ya bunduki zao. Ili kunisaidia nidumishe uaminifu wangu wa kimaadili kwa Mungu, niliimba kimoyomoyo wimbo wa Ufalme “Msiwaogope!” Baadaye askari-jeshi hao walitutupa sisi ndani ya gereza chafu. Siku tatu baadaye ndugu kutoka nchi za kigeni waliachiliwa, na Lichfield na mimi tukafukuzwa nchini kwenda Sierra Leone. Mashahidi wa hapo waliachiliwa siku iliyofuata.

Mapendeleo na Baraka za Ziada

Tulipewa mgawo wa kufanya kazi pamoja na Kundi la Bo, kusini mwa Sierra Leone. Tulitumikia huko kwa muda wa miaka minane kabla ya kuhamishwa Njala. Tulipokuwa Njala mume wangu aliwekwa rasmi kutumikia akiwa mwangalizi wa mzunguko wa badala, na mimi nikawa na pendeleo la kuandamana naye aliposhiriki katika utumishi huo. Halafu, katika miaka ya katikati ya 1970, tulipewa mgawo mwingine wa kutumikia katika Kundi la Freetown Mashariki.

Nimepata thawabu ya kuona wengi wa wale niliojifunza Biblia nao wakikubali ibada ya kweli. Nina watoto na wajukuu wa kiroho zaidi ya 60 wakiwa “barua zenye sifa.” (2 Wakorintho 3:1) Baadhi yao wamehitaji kufanya mabadiliko makubwa, kama vile Victoria Dyke, aliyekuwa nabii wa kike wa farakano la Aladura. Baada ya kuzungumzia 1 Yohana 5:21, alitupilia mbali hirizi nyingi na vifaa vingi vya uchaji. Alionyesha wakfu wake kwa ubatizo na hatimaye akawa painia wa pekee, akiwasaidia watu wengi wa ukoo wakubali kweli.

Katika Aprili 1985, mume wangu alikufa, miezi michache tu kabla ya ukumbusho wetu wa ndoa wa kila mwaka wa 44. Lakini sikuachwa peke yangu. Nimeendelea kumtumikia Msaidizi wangu, Yehova, nikiwa mhudumu wa wakati wote. Na ninahisi kifungo cha pekee na wale ambao nimewasaidia kupata kumjua. Wao ni familia yangu katika maana ya pekee. Ninawapenda nao wanipenda. Ninapokuwa mgonjwa, wao huja kwa haraka kunitunza, na bila shaka, mimi huwasaidia pia.

Pasipo shaka, ikiwa ningalipaswa nirudie maisha yangu tena, ningalichukua mundu wangu kwa furaha na kujiunga katika mavuno nikiwa mfanyakazi mwenzi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Winifred Remmie leo

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki