“Wajueni Sana Watu Kama Hao”
MAMBO hayakuwa shwari katika kutaniko la Korintho. Kulikuwa kumekuwa na kisa chenye kushtua cha ukosefu wa adili, na mafarakano yalikuwapo kati ya ndugu. Wengine walikabili matatizo mazito ya kibinafsi au walikuwa na maswali yaliyohitaji kujibiwa. Ndugu fulani walikuwa wakipelekana mahakamani; wengine hata walikuwa wakikana ufufuo.
Maswali mazito yalitokea pia. Je, wale walio katika nyumba zilizogawanyika kidini waishi na wenzi wao wasioamini, au watengane? Fungu la dada kutanikoni lilikuwa jipi? Je, ilifaa kula nyama zilizotolewa dhabihu kwa sanamu? Mikutano—kutia ndani Mlo wa Jioni wa Bwana—iongozweje?—1 Wakorintho 1:12; 5:1; 6:1; 7:1-3, 12, 13; 8:1; 11:18, 23-26; 14:26-35.
Yaelekea sana Akaiko, Fortunato na Stefana, wakihangaikia hali njema ya ndugu zao katika mazingira ya kiroho yenye taabu, walifunga safari ya kumtembelea mtume Paulo katika Efeso. Pamoja na habari hizo zenye kusumbua, yawezekana kwamba walikuwa wanampelekea Paulo barua kutoka hilo kutaniko yenye maswali juu ya masuala hayo. (1 Wakorintho 7:1; 16:17) Ni wazi kwamba, si ndugu hao watatu tu waliohangaikia hali hiyo. Kwa hakika, Paulo tayari alikuwa amepata habari kutoka kwa “wale walio wa nyumbani mwa Kloe” kwamba fitina ilikuwako miongoni mwa washiriki wa kutaniko. (1 Wakorintho 1:11) Hakuna shaka kwamba, ripoti ya hao wajumbe ilimsaidia Paulo kupata uelewevu wa wazi zaidi wa hiyo hali, kuamua shauri atakalotoa, na jinsi ya kujibu maswali yaliyozushwa. Ingeonekana kwamba barua ambayo sasa twaijua kuwa Wakorintho wa Kwanza ni jibu la Paulo, lililoongozwa na roho takatifu ya Mungu. Huenda Akaiko, Fortunato, na Stefana ndio waliopeleka hiyo barua.
Akaiko, Fortunato, na Stefana walikuwa nani? Twaweza kujifunza nini kwa kusoma yale ambayo Maandiko husema juu yao?
Watu wa Nyumbani mwa Stefana
Watu wa nyumbani mwa Stefana walikuwa “malimbuko” ya huduma ya Paulo katika Akaya, mkoa wa Roma, Kusini mwa Ugiriki, karibu mwaka wa 50 W.K., nao walibatizwa na Paulo mwenyewe. Yaonekana kwamba, Paulo aliona wale wa nyumbani mwa Stefana kuwa kielelezo chema, walio na uvutano mkomavu wenye kusawazisha kwa Wakorintho. Aliwasifu kwa uchangamfu kwa sababu ya utendaji wao kwa niaba ya kutaniko: “Tena ndugu, nawasihi; (mnawajua watu wa nyumbani mwa Stefana kwamba ni malimbuko ya Akaya, nao wamejitia katika kazi ya kuwahudumu watakatifu); watiini watu kama hawa, na kila mtu afanyaye kazi pamoja nao, na kujitaabisha.” (1 Wakorintho 1:16; 16:15, 16) Haielezwi ni nani hasa waliokuwa wa “nyumbani” mwa Stefana. Huo usemi waweza tu kumaanisha washiriki wa familia lakini ungeweza pia kutia ndani watumwa na waajiriwa. Kwa kuwa katika Kilatini Akaiko lilikuwa jina la kawaida la mtumwa, na Fortunato lilikuwa jina la kawaida la mtu aliyewekwa huru, wafafanuzi wengine wa Biblia wanadhania kwamba hao wawili wangaliweza kuwa washiriki wa nyumba iyo hiyo.
Kwa vyovyote, Paulo aliwaona watu wa nyumba ya Stefana kuwa vielelezo vyema. Washiriki wayo walikuwa “wamejitia katika kazi ya kuwahudumu watakatifu.” Familia ya Stefana lazima iwe ilitambua kwamba kulikuwa na kazi ya kufanywa kwa faida ya kutaniko na wakakubali kwa hiari utumishi huo kuwa daraka la kibinafsi. Tamaa yao ya kutoa utumishi huo kwa watakatifu bila shaka ilistahili kuungwa mkono na kutambuliwa.
“Wameniburudisha Roho Yangu, na Roho Zenu Pia”
Ingawa Paulo alihangaikia hali katika Korintho, kufika kwa wale wajumbe watatu kulimchangamsha. Paulo anasema: “Nami nafurahi kwa sababu ya kuja kwao Stefana na Fortunato na Akaiko; maana hawa wamenikirimia kwa wingi yale niliyopungukiwa kwenu. Maana wameniburudisha roho yangu, na roho zenu pia.” (1 Wakorintho 16:17, 18) Kwa kufikiria hali katika Korintho, kutenganishwa kimwili kutoka kwa Wakorintho huenda kulikuwa chanzo cha masumbufu ya Paulo, lakini sasa kuwapo kwa wajumbe wao kulilipia kutokuwapo kwa kutaniko zima. Yaelekea ripoti yao ilimpa Paulo habari kamili ya hali na angalau kumwondolea kiasi fulani cha hofu zake. Hata hivyo huenda mambo hayakuwa mabaya kama alivyokuwa amewazia.
Kulingana na Paulo, utume wa watatu hao haukuburudisha roho yake tu bali pia ulichangamsha roho ya kutaniko la Wakorintho. Hakuna shaka kwamba kilikuwa kitulizo kwao kujua kwamba wajumbe wao walikuwa wamemweleza Paulo kwa wazi kila upande wa hiyo hali na kwamba wangerudi wakiwa na shauri lake.
Kwa hiyo Stefana na waandamani wake wawili walipendekezwa kwa shauku kwa sababu ya kujitaabisha kwao kwa niaba ya Wakorintho. Paulo aliwathamini sana wanaume hao hivi kwamba waliporudi walipaswa kutoa uongozi katika kutaniko la Wakorintho lililogawanyika. Mtume awasihi ndugu: “Watiini watu kama hawa, na kila mtu afanyaye kazi pamoja nao na kujitaabisha. . . . Wajueni sana watu kama hao.” (1 Wakorintho 16:16, 18) Mapendekezo yenye nguvu kama hayo yaonyesha kwa wazi uaminifu-mshikamanifu kamili wa wanaume hao licha ya mikazo katika kutaniko. Watu kama hao wapaswa kuheshimiwa.—Wafilipi 2:29.
Ushirikiano Wenye Uaminifu Hutokeza Matokeo Mema
Hakuna shaka juu ya hilo, ushirikiano wa karibu pamoja na tengenezo la Yehova na wawakilishi walo hutokeza matokeo mema. Paulo alipoandika ile barua ijulikanayo sasa kuwa Wakorintho wa Pili, muda mfupi baada ya barua ya kwanza, tayari mambo yalikuwa yakiboreka kutanikoni. Utendaji wenye subira wa kuendelea wa ndugu kama Akaiko, Fortunato, na Stefana, pamoja na ziara ya Tito, ulikuwa umetokeza matokeo mazuri.—2 Wakorintho 7:8-15; linganisha Matendo 16:4, 5.
Washiriki wa makutaniko ya siku ya kisasa ya watu wa Yehova waweza kunufaika kwa kutafakari juu ya kutajwa kifupi katika Maandiko kwa wanaume hao waaminifu. Kwa kielelezo, tuseme hali yenye kuendelea katika kutaniko la kwenu haiwezi kusuluhishwa upesi kwa sababu fulani nayo yawahangaisha ndugu. Ni nini kipaswacho kufanywa? Igeni Stefana, Fortunato, na Akaiko, ambao hawakuacha daraka lao la kumweleza Paulo juu ya hiyo hali kisha kwa uhakika acheni mambo mikononi mwa Yehova. Bidii kwa ajili ya uadilifu haikuwafanya kamwe wachukue hatua kwa kujitegemea au ‘kununa juu ya BWANA.’—Mithali 19:3.
Makutaniko ni ya Yesu Kristo, na kwa wakati wake ufaao, sawa na katika Korintho, atatenda ili kusuluhisha magumu yoyote ambayo huenda yakatokeza tisho kwa hali yao njema ya kiroho na amani yayo. (Waefeso 1:22; Ufunuo 1:12, 13, 20; 2:1-4) Kwa sasa, tukifuata kielelezo chema kilichowekwa na Stefana, Fortunato, na Akaiko na kuendelea kujitaabisha katika kuwahudumu ndugu zetu, sisi pia tutakuwa tukitegemeza mpango wa kutaniko kwa uaminifu-mshikamanifu, kuwajenga ndugu zetu, na ‘kuwahimiza katika upendo na kazi nzuri.’—Waebrania 10:24, 25.