Je, Una ‘Moyo Mtiifu’?
SOLOMONI alipopata kuwa mfalme wa Israeli la kale, alihisi kupungukiwa. Kwa hiyo alimwomba Mungu ampe hekima na ujuzi. (2 Mambo ya Nyakati 1:10) Solomoni alisali hivi pia: “Nipe mimi mtumwa wako moyo wa adili [“mtiifu,” NW] niwahukumu watu wako.” (1 Wafalme 3:9) Ikiwa Solomoni angalikuwa na ‘moyo mtiifu,’ angalifuata sheria na kanuni za Mungu naye angepata baraka za Yehova.
Moyo mtiifu si mzigo wenye kulemea bali hutokeza shangwe. Mtume Yohana aliandika hivi: “Hivi ndivyo kumpenda Mungu humaanisha, kwamba tushike amri zake; na bado amri zake si zenye kulemea.” (1 Yohana 5:3) Bila shaka, twapaswa kumtii Mungu. Kwa vyovyote, Yehova ndiye Muumba wetu Mkuu. Dunia na vyote vilivyomo ni vyake, hata almasi na dhahabu zote. Kwa hiyo, kwa kweli hatuwezi kumpa Mungu chochote kimwili, ingawa yeye huturuhusu tutumie fedha zetu kuonyesha kwamba twampenda. (1 Mambo ya Nyakati 29:14) Yehova hututarajia tumpende na kutembea kwa unyenyekevu pamoja naye, tukifanya mapenzi yake.—Mika 6:8.
Yesu Kristo alipoulizwa ni ipi iliyo amri kuu katika Sheria, alisema hivi: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote. Hii ndiyo amri kubwa zaidi sana na ya kwanza.” (Mathayo 22:36-38) Njia moja ya kuonyesha upendo huo ni kumtii Mungu. Kwa hiyo, kila mmoja wetu apaswa kumwomba Yehova ampe moyo mtiifu.
Walikuwa na Moyo Mtiifu
Biblia ina vielelezo vingi vya watu waliokuwa na moyo mtiifu. Kwa mfano, Yehova alimwambia Noa ajenge safina kubwa ili kuhifadhi uhai. Hiyo ilikuwa kazi kubwa iliyochukua miaka 40 au 50 hivi. Hata kukiwa na vyombo vyote vya kisasa vyenye kutumia umeme na vifaa vingine vipatikanavyo leo, ingekuwa kazi kubwa kujenga chombo hicho kikubwa ambacho kingeweza kuelea juu ya maji. Isitoshe, Noa alipaswa kuwaonya watu ambao bila shaka walimdhihaki na kumfanyia mzaha. Lakini alitii kila kitu. Biblia husema: “Hivyo ndivyo alivyofanya.” (Mwanzo 6:9, 22; 2 Petro 2:5) Noa alionyesha upendo wake kwa Yehova kwa kumtii kwa uaminifu kwa miaka mingi. Ni kielelezo bora kama nini kwetu sote!
Pia, mfikirie mzee wa ukoo, Abrahamu. Mungu alimwambia ahame kutoka Uru wa Wakaldayo na kwenda katika nchi asiyoijua. Abrahamu alitii bila shaka yoyote. (Waebrania 11:8) Kwa maisha yake yaliyosalia yeye na familia yake waliishi mahemani. Baada ya miaka mingi akiwa mgeni katika nchi hiyo, Yehova alimbariki yeye na mke wake mtiifu, Sara, kwa mtoto aliyeitwa Isaka. Lazima Abrahamu mwenye umri wa miaka 100 awe alimpenda kama nini mwana wake wa uzeeni! Miaka kadhaa baadaye, Yehova alimwagiza Abrahamu amdhabihu Isaka akiwa toleo la kuteketezwa. (Mwanzo 22:1, 2) Kufikiria tu kufanya hivyo lazima kuwe kulimwumiza Abrahamu. Hata hivyo, aliendelea kutii kwa sababu alimpenda Yehova naye aliamini kwamba mbegu iliyoahidiwa ingekuja kupitia Isaka, hata ikiwa Mungu angemfufua kutoka kwa wafu. (Waebrania 11:17-19) Hata hivyo, Abrahamu alipokuwa karibu kumwua mwana wake, Yehova alimzuia na kusema: “Sasa ninajua ya kuwa unamcha Mungu, iwapo hukunizuilia mwanao, mwanao wa pekee.” (Mwanzo 22:12) Kwa kuwa alitii, Abrahamu mcha-Mungu alikuja kuitwa “rafiki ya Yehova.”—Yakobo 2:23.
Yesu Kristo ndiye kielelezo chetu bora kabisa cha utii. Kabla hajawa mwanadamu, alipendezwa na utumishi mtiifu kwa Baba yake mbinguni. (Mithali 8:22-31) Akiwa mwanadamu, Yesu alimtii Yehova katika kila jambo, sikuzote akipendezwa na kufanya mapenzi yake. (Zaburi 40:8; Waebrania 10:9) Hivyo, Yesu angeweza kusema hivi kikweli: “Sifanyi jambo lolote kwa uanzisho wangu mwenyewe; bali kama vile Baba alivyonifundisha nasema mambo haya. Na yeye aliyenituma yuko pamoja nami; yeye hakuniacha peke yangu mwenyewe, kwa sababu sikuzote mimi hufanya mambo yale yanayompendeza.” (Yohana 8:28, 29) Hatimaye, ili kutetea enzi kuu ya Yehova na kukomboa wanadamu watiifu, Yesu alitoa uhai wake kwa hiari, akifa kifo chenye maumivu makali zaidi na chenye kutweza zaidi. Kwa kweli, “alipojipata mwenyewe katika sura ya kuwa binadamu alijinyenyekeza mwenyewe akawa mtiifu hadi kifo, ndiyo, kifo juu ya mti wa mateso.” (Wafilipi 2:8) Ni kielelezo kizuri kama nini katika kudhihirisha moyo mtiifu!
Utii Nusu-Nusu Hautoshi
Si watu wote ambao wamedai kumtii Mungu ambao kwa kweli wamefanya hivyo. Mfikirie Mfalme Sauli wa Israeli la kale. Mungu alimwagiza awafutilie mbali Waamaleki waovu. (1 Samweli 15:1-3) Ingawa Sauli aliwaharibu wakiwa taifa, alimwacha hai mfalme wao na kuhifadhi baadhi ya kondoo na ng’ombe wao. Samweli aliuliza hivi: “Mbona, basi, hukuitii sauti ya BWANA?” Sauli alijibu kwa kusema hivi: “Hakika mimi nimeitii sauti ya BWANA . . . watu [wa Israeli] waliteka nyara, kondoo na ng’ombe walio wazuri . . . kusudi wavitoe dhabihu kwa BWANA.” Akikazia uhitaji wa utii kamili, Samweli alijibu hivi: “Je! BWANA huzipenda sadaka za kuteketezwa na dhabihu sawasawa na kuitii sauti ya BWANA? Angalia, kutii ni bora kuliko dhabihu, na kusikia kuliko mafuta ya beberu. Kwani kuasi ni kama dhambi ya uchawi, na ukaidi ni kama ukafiri na vinyago; kwa kuwa umelikataa neno la BWANA, yeye naye amekukatia wewe usiwe mfalme.” (1 Samweli 15:17-23) Sauli alipoteza mambo mengi kama nini kwa sababu hakuwa na moyo mtiifu!
Hata Mfalme Solomoni mwenye hekima, aliyeomba apewe moyo mtiifu, hakuendelea kumtii Yehova. Kinyume cha mapenzi ya Mungu, alioa wanawake wa kigeni waliomfanya atende dhambi dhidi ya Mungu. (Nehemia 13:23, 26) Solomoni alipoteza kibali cha Mungu kwa sababu hakuendelea kuwa na moyo mtiifu. Ni onyo lililoje kwetu!
Hilo halimaanishi kwamba Yehova hutaka watumishi wake wa kibinadamu wawe wakamilifu. Yeye ‘hukumbuka ya kuwa sisi tu mavumbi.’ (Zaburi 103:14) Bila shaka sisi sote hukosea nyakati fulani, lakini Mungu aweza kuona ikiwa kwa kweli tunatamani moyoni kumpendeza. (2 Mambo ya Nyakati 16:9) Tukikosea kwa sababu ya kutokamilika kwa kibinadamu lakini tutubu, twaweza kuomba msamaha kwa msingi wa dhabihu ya fidia ya Kristo, tukiwa na hakika kwamba Yehova ‘atatusamehe kabisa.’ (Isaya 55:7; 1 Yohana 2:1, 2) Huenda tukahitaji msaada wa wazee Wakristo wenye upendo ili tuweze kupata nafuu kiroho na kuwa na imani yenye nguvu na moyo mtiifu.—Tito 2:2; Yakobo 5:13-15.
Utii Wako Ni Kamili Kadiri Gani?
Tukiwa watumishi wa Yehova, bila shaka wengi wetu huhisi kwamba tuna moyo mtiifu. Huenda tukafikiri, Je, si mimi hushiriki katika kazi ya kuhubiri Ufalme? Je, si nina msimamo imara, masuala makubwa-makubwa kama suala la kutokuwamo yazukapo? Na je, si mimi huhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida, kama vile mtume Paulo alivyohimiza? (Mathayo 24:14; 28:19, 20; Yohana 17:16; Waebrania 10:24, 25) Ni kweli kwamba watu wa Yehova kwa ujumla huonyesha utii wa kutoka moyoni katika mambo ya maana kama hayo.
Lakini namna gani mwenendo wetu katika mambo ya kila siku, pengine katika mambo yanayoonekana kuwa madogo? Yesu alitaarifu hivi: “Mtu aliye mwaminifu katika lililo dogo zaidi sana ni mwaminifu katika lililo kubwa pia, na mtu asiye mwaminifu katika lililo dogo zaidi sana ni asiye mwaminifu katika lililo kubwa pia.” (Luka 16:10) Kwa hiyo ingefaa kila mmoja wetu ajiulize mwenyewe, Je, nina moyo mtiifu kuhusu mambo madogo-madogo ambayo hata wengine hawajui?
Mtunga-zaburi alionyesha kwamba hata nyumbani mwake, ambamo wengine hawakumwona, yeye ‘alikwenda kwa unyofu wa moyo.’ (Zaburi 101:2) Uketipo nyumbani mwako, huenda ukawasha televisheni na kuanza kutazama sinema fulani. Papo hapo, utii wako waweza kutahiniwa. Huenda hiyo sinema ikawa na mambo yasiyo ya adili. Je, utaendelea kuitazama, ukisababu kwamba hiyo ndiyo aina ya sinema ambazo huonyeshwa siku hizi? Au moyo wako mtiifu utakuchochea kutenda kulingana na amri hii ya Kimaandiko, ‘msiache uasherati na ukosefu wa usafi hata utajwe miongoni mwenu’? (Waefeso 5:3-5) Je, utazima televisheni, hata ikiwa hadithi ni yenye kusisimua? Au je, utabadili idhaa ikiwa programu fulani inakuwa yenye jeuri? “Yehova mwenyewe humchunguza mwadilifu na pia mwovu,” akaimba mtunga-zaburi, “na yeyote apendaye jeuri nafsi Yake kwa hakika humchukia.”—Zaburi 11:5, NW.
Moyo Mtiifu Huleta Baraka
Bila shaka, kuna maeneo mengi maishani ambamo kwa faida twaweza kujichunguza kuona ikiwa kwa kweli twamtii Mungu kutoka moyoni. Kumpenda kwetu Yehova kwapaswa kutusukume tumpendeze na kufanya mambo atuambiayo katika Neno lake, Biblia. Moyo mtiifu utatusaidia kudumisha uhusiano mzuri pamoja na Yehova. Kwa kweli, ikiwa sisi ni watiifu kikamili, ‘maneno ya vinywa vyetu, na mawazo ya mioyo yetu yatapata kibali mbele za BWANA.’—Zaburi 19:14.
Kwa sababu Yehova atupenda, yeye hutufundisha utii kwa faida yetu wenyewe. Nasi hujinufaisha sana kwa kuzingatia kwa moyo wote mafundisho ya Mungu. (Isaya 48:17, 18) Kwa hiyo, acheni tukubali kwa furaha msaada ambao Baba yetu wa kimbingu huandaa kupitia Neno lake, roho yake, na tengenezo lake. Twafundishwa vema sana hivi kwamba ni kana kwamba twasikia sauti nyuma yetu ikituambia: “Njia ni hii, ifuateni.” (Isaya 30:21) Yehova atufundishapo kupitia Biblia, vichapo vya Kikristo, na mikutano ya kutaniko, na tukaze fikira, tutumie tunayojifunza, na kuwa “watiifu katika mambo yote.”—2 Wakorintho 2:9.
Moyo mtiifu utatokeza shangwe nyingi na baraka nyingi. Utatuletea amani ya akili, kwa kuwa tutajua kwamba tunampendeza vema Yehova Mungu nasi tunafanya moyo wake ushangilie. (Mithali 27:11) Moyo mtiifu utatulinda tunapojaribiwa tufanye makosa. Basi, kwa hakika twapaswa kumtii Baba yetu wa kimbingu na kumwomba hivi: “Nipe mimi mtumwa wako moyo wa adili [“mtiifu,” NW].”
[Picha katika ukurasa wa 29]
Kutoka kwa Self-Pronouncing Edition of the Holy Bible, iliyo na tafsiri ya King James na ile ya Revised