Uwe Chonjo Kuanza Mafunzo ya Biblia
1 Kuanza na kuongoza mafunzo ya Biblia ya nyumbani ni sehemu ya utume wetu tukiwa Mashahidi wa Yehova. (Mt. 28:19, 20) Kwa hiyo, je! wewe utakuwa mmoja wa wafanyakazi wenzi wa Mungu katika kufanya hivyo? (1 Kor. 3:9) Ni pendeleo kama nini kusaidia wengine waje kumjua Mtu aliye mkuu zaidi katika ulimwengu wote mzima!
2 Kukiwa na matatizo mengi sana yanayofungamanishwa na matukio ya ulimwengu yenye kubadilika kasi, watu mmoja mmoja wenye mioyo ya ufuatiaji haki wanatafuta majibu wajue kwa nini mambo haya yanatukia. Muda mrefu uliopita Yehova aliandaa majibu ya maswali hayo. Watu wenye mioyo myeupe wanapopewa maagizo katika Neno la Mungu, wanafarijiwa. Kwa sababu hiyo, tunahitaji kuwa chonjo kuona fursa za kuanza mafunzo ya Biblia.—Mit. 3:27.
UWE CHONJO KUONA FURSA
3 Je! wewe umefikiria kuanza funzo la Biblia na mshiriki wa jamaa ya karibu au mtu unayejuana naye ambaye hayumo katika ukweli? Kuwajua kutakupatia busara katika kutumia utambuzi kwa habari ya wakati unaofaa kuzungumza jambo hilo pamoja nao. Kumbuka kwamba swali lililochaguliwa vizuri au neno katika wakati unaofaa huenda likaamsha kupendezwa kwao katika ukweli. Udadisi wa mtu unapoamshwa, mazungumzo yenye mazao hufuata mara nyingi, na huenda funzo la Biblia likaanzishwa.
4 Katika visa vingi mwenendo mwema wa mwenzi Mkristo umetumika kufungulia njia asiye mwamini aje katika ukweli. (1 Pet. 3:1, 2) Kwa kawaida wenzi wasioamini pamoja na washiriki wengine wasioamini wa familia wanathamini wanapotambuliwa na kustahiwa na washiriki wa kundi. Kuwaonyesha upendezi wa kibinafsi kunaweza kusaidia sana kujenga mahusiano ya kirafiki. Kwa kufanya kazi pamoja na mwenzi au mshiriki wa familia aliyemo katika ukweli, huenda ukaweza kuanzisha funzo la Biblia.
5 Tunaposhiriki kazi ya nyumba kwa nyumba, twaweza kujaribu kuanza funzo la Biblia katika ziara ya kwanza. Hilo laweza kufanywaje? Baadhi ya wahubiri wamefanikiwa kufanya hilo wakati mwenye-nyumba anapouliza maswali yanayoweza kujibiwa moja kwa moja kutoka kichapo fulani. Mtu huyo akikubali kusoma fasihi au akitualika ndani, twaweza kutumia fursa hiyo kuendeleza mazungumzo na pengine kumwonyesha jinsi funzo linavyoongozwa. Amua utakaa muda mrefu kadiri gani katika ziara ya kwanza. Huenda ikanufaisha kurudi saa au tarehe ya baadaye kuendeleza mazungumzo. Katika ziara za wakati ujao, huenda ukataka kuendelea kuzungumzia ile habari uliyotanguliza katika ziara ya kwanza. Au huenda ukazungumza juu ya swali lililozushwa kwenye umalizio wa ziara iliyotangulia.
PINDI ZA USHAHIDI WA VIVI HIVI
6 Ushahidi wa vivi hivi waweza kuwa njia nyingine yenye kuzaa matunda katika jitihada zetu za kuanza mafunzo ya Biblia ya nyumbani. Katika utendaji wetu wa siku baada ya siku, tunakuta watu wengi mmoja mmoja ambao huenda wakataka kujifunza. Ili kutusaidia tuwe wenye mafanikio, twaweza kutumia baadhi ya matangulizi yaliyotahiniwa kutoka kitabu Kutoa Sababu kuanzisha mazungumzo. Nawe usijizuie kumtolea funzo la Biblia hapo mwanzoni kwa sababu ya kwamba mtu huyo aishi mahali penginepo na huenda tusiweze kuwa na fursa ya kuongoza funzo hilo sisi wenyewe.
7 Uwe chonjo kuona pindi za kutoa ushahidi vivi hivi, na uwe umejitayarisha kwa kubeba ugavi wa kutosha wa trakti na magazeti ambavyo vitakuza upendezi wa msikilizaji katika ukweli. (Mhu. 11:1) Ikiwa mtu aonyesha kupendezwa na ukweli naye haishi katika eneo la kundi lenu, pata anwani yake na habari nyingine inayohitajika na kuipitisha kwa kundi anakoishi ili mtu fulani aweze kumtunza ifaavyo.
8 Kazi ya kufanya wanafunzi si ya wachache tu. Ni ya wote kundini. Kukumbuka kwamba ni utume wa Kikristo tuwe wafanya wanafunzi kutatutia moyo tuwe chonjo kuona fursa za kuanza mafunzo ya Biblia.