Kupainia—Wonyesho wa Upendo
1 Upendo kwa Yehova na kwa wanadamu wenzetu ndio hutusukuma kushiriki kikamili zaidi katika kazi ya kuhubiri. Upendo kwa Yehova na kwa wanadamu ukuapo, sisi huchochewa kupangia kuwa na ushiriki mwingi hata zaidi hudumani. Upendo wetu hupanuka kadiri tukuavyo katika “maarifa sahihi” ya Neno la Mungu. (Flp. 1:9, 10, NW) Kadiri tunavyojifunza zaidi kuhusu mapenzi ya Yehova, ndivyo tunavyotambua uharaka wa nyakati tunamoishi. Hilo linaongeza kuhangaikia kwetu wengine. Wengi wanaonyesha hangaikio lao la upendo kwa kufanya utumishi wa upainia.
2 Je! wewe unaweza kufanya marekebisho yanayohitajiwa ili uwe painia msaidizi au wa kawaida? Ni kweli, si kila mmoja wetu anaweza kupainia. Lakini kila mmoja wetu apaswa achanganue hali zake kwa sala.
3 Ni Wakristo wachache wanaopata kwamba wana wakati mwingi wa ziada wa kupainia; kwa hiyo, inakuwa lazima ‘kununua wakati’ unaotumiwa sasa katika yale mambo mengine yasiyo ya lazima. (Efe. 5:15-17, NW) Upendo wetu kwa Mungu na kwa wanadamu wapasa utufanye tutake kudhabihu baadhi ya mapendezi yetu ya kibinafsi na starehe ili kuonyesha upendo wetu kwa ukamili zaidi. (Mk. 12:33) Mali nyingi tulizo nazo, na labda tunahisi kuwa ni za kawaida, zaweza kuonwa kuwa anasa katika sehemu nyinginezo za ulimwengu.
4 Wazazi wanaweza kufanya nini ili kuwasaidia watoto wao wafikiri kwa njia hiyo ya kimungu? Wazazi wapaswa kuwawekea watoto wao miradi ya kitheokrasi kuanzia umri mchanga. Wanapokaribia kumaliza shule, je! wanafikiria miradi ya kilimwengu au ya kiroho? Tunataka tusaidie vijana wetu waone faida za kudumu zinazotokana na kuingia katika utumishi wa upainia wakati wa umri mchanga. Hiyo ni kuweka hazina mbinguni. (Mt. 6:19-21) Hilo humpendeza Mungu na hutoa ithibati ya uaminifu-mshikamanifu na ujitoaji wetu kwake. Na huokoa uhai wa wengine.
5 Ni mapenzi ya Mungu kwamba “watu wote waokolewe.” (1 Tim. 2:4) Je! tunaweza kuonyesha kwamba hayo ndiyo mapenzi yetu pia? Tunaweza kufanya hivyo ikiwa tunataka kuweka faida za Ufalme kwanza. Tunaweza pia kufanya hivyo kwa kuwa na uhakika kwamba Yehova ataandaa mambo ya lazima ya maisha. (Mt. 6:31-33) Huenda hali za kiuchumi zikawa mbaya hata zaidi, lakini ahadi ya Yehova ya kututunza haibadiliki kamwe.—Zab. 37:25.
6 Kujitahidi wenyewe ili kushiriki katika huduma ya shambani kwa kadiri hali zetu ziruhusuvyo ni wonyesho wa upendo. Kwa wengine hilo litamaanisha kuwa painia wa kawaida. Kwa nini usifanye yote uwezayo ili uanze kufikia Septemba 1, 1992?