“Imani Hufuata Jambo Lililosikiwa”
1 Tunapopata mtu aliye na “mwelekeo ufaao kwa ajili ya uhai udumuo milele,” ni lazima kuimarisha imani ya mtu huyo kuhusu yale ambayo amesikia. (Mdo. 13:48, NW; Rum. 10:17) Ili kutimiza hayo, twapaswa kufuatia maandikisho na maangusho ya magazeti kwa kurudi ili kupeleka matoleo ya karibuni na kuzungumza zaidi. Hata hivyo, kumbuka mradi wa kuanzisha funzo katika kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele. Hapa pana madokezo yanayoweza kusaidia:
2 Unapofanya ziara ya kurudia, mliyozungumza juu ya makala “Msifuni Mfalme wa Umilele!,” unaweza kuanza kwa njia hii:
◼ “Tulipoongea wakati uliopita, tulipitia baadhi ya uthibitisho mkubwa unaohakikisha kwamba kuna Mungu aliye mweza yote. Hata hivyo, kujua tu juu ya kuwapo kwake hakutoshi. Twahitaji kujua jina lake. Je, wewe humwita Mungu kwa jina gani? [Ruhusu itikio.] Mamilioni ya watu humwita ‘Bwana’ au ‘Mungu’ tu, ambayo ni majina ya vyeo yasiyorejezea mtu binafsi. Kwa kuongezea, yeye hutaka tumjue kwa jina lake. [Soma Zaburi 83:18.] Biblia hutuambia mengi kuhusu Yehova Mungu, kama inavyoelezwa katika kitabu hiki.” Onyesha picha iliyo kwenye ukurasa wa 29 wa kitabu Ujuzi, na usome maelezo yayo. Baada ya kuzungumzia mafungu ya kwanza matatu katika sura ya 3, utakuwa umeanzisha funzo!
3 Kwa wale mliochunguza makala “Sababu Kwa Nini Dini ya Kilimwengu Itaisha,” huenda ukataka kufuatia kupendezwa kwa kusema:
◼ “Baada ya kusoma makala hiyo, huenda ulipendezwa na ukweli wa kwamba hatuwezi kuona dini zote kuwa sawa. Dini ya kweli na dini isiyo ya kweli zipo. Hili hutokeza swali la kiakili, Ni ibada ya nani ambayo Mungu anakubali? Jibu lilitolewa na Yesu, nalo lakaziwa katika kitabu hiki.” Fungua kwenye sura ya 5 ya kitabu Ujuzi, na usome fungu la 4, kutia ndani Yohana 4:23, 24. Kisha uulize, “Je, uko tayari kukubali funzo la Biblia nyumbani bila malipo?” Ikiwa itikio lafaa, fungua sura ya 1 na uanzishe funzo.
4 Ikiwa kupendezwa kulionyeshwa katika “Amkeni!” la Aprili 22, unaporudi unaweza kujaribu mfikio huu kuanzisha funzo katika kitabu “Ujuzi”:
◼ “Unaweza kukumbuka kuwa tulikuwa na mazungumzo juu ya matazamio ya kuona ulimwengu bila vita hatimaye. Ni vigumu kuwazia huo ungekuwa namna gani. Hili ni wazo la mchoraji mmoja kuuhusu. [Onyesha picha iliyo kwenye kurasa 188-189 katika kitabu Ujuzi.] Je, haitapendeza kufurahia mazingira haya? [Fungua kurasa 4-5, onyesha picha, na usome sanduku hilo.] Kichwa cha kitabu hiki chafanana na maneno ya Yesu yapatikanayo kwenye Yohana 17:3. [Soma.] Ukiniruhusu, ningependa kukuonyesha jinsi kitabu hiki chaweza kutumiwa pamoja na Biblia yako kupata ujuzi wenye kuokoa uhai.” Mwenye nyumba akikubali, anzisha funzo katika sura ya kwanza.
5 Ikiwa ulimfikia mtu aliyekuwa na shughuli ulipoenda mara ya kwanza, unaporudi unaweza kusema hivi:
◼ “Nilikutembelea majuzi nikakuachia nakala za magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Majarida haya huleta staha kwa Biblia na mwongozo wayo wa adili. Kwa sababu nahisi likiwa jambo muhimu kwa kila mtu kuelewa Neno la Mungu, nimerudi ili kukuonyesha jambo litakalokusaidia kufanya hivyo.” Onyesha kitabu Ujuzi, na uelekeze kwenye yaliyomo katika ukurasa wa 3. Uliza ni sura ipi inayompendeza zaidi, ifungue, na uanzishe funzo.
6 Shangwe yetu itakuwa kubwa ikiwa tutaweza ‘kuwafungulia wengine mlango wa imani’ uongozao kwenye uhai udumuo milele.—Mdo. 14:27; Yn. 17:3.