Sanduku La Swali
◼ Wakaribishaji wanaweza kuwasaidiaje wazazi ili nao wawasaidie watoto wao kudumisha utaratibu ufaao mikutanoni?
Kwa asili watoto huwa na nguvu, na hawajazoea kuketi kwa muda mrefu. Baada ya mkutano, watoto huwa na nguvu inayowachochea kukimbia-kimbia na kuwafukuza watoto wengine ndani ya Jumba la Ufalme au kwenye sehemu nyingine za kufanyia mikutano, kwenye maegesho ya magari, au kwenye kijia. Hata hivyo, ni ya kweli mithali isemayo, ‘mwana aliyeachiliwa humwaibisha mzazi wake.’—Mit. 29:15.
Kwa kusikitisha, akina ndugu na dada zetu wenye umri mkubwa zaidi wamejeruhiwa vibaya kwa sababu ya kugongwa na kuangushwa na watoto. Hilo limesababisha kuteseka kusikofaa, na gharama zisizohitajika kwa wazazi na kutaniko. Kwa ajili ya usalama wao na wa wengine, watoto hawapaswi kuruhusiwa kukimbia na kucheza ndani au nje ya Jumba la Ufalme.
Wazazi wana daraka la Kimaandiko la kuwazoeza watoto wao kustahi ifaavyo mahali petu pa ibada. (Mhu. 5:1a) Kwenye mikutano, makusanyiko, na mikusanyiko yetu ya Kikristo, wakaribishaji hupewa mgawo wa kuhakikisha kwamba ‘mambo yote yanatukia kwa mpango’ na kwamba kuna “utaratibu mzuri.” (1 Kor. 14:40; Kol. 2:5) Wapaswa kuwa chonjo kabla, wakati, na baada ya programu, ndani na nje vilevile. Ikiwa mtoto anakimbia au amekuwa mtukutu, mkaribishaji aweza kumsimamisha kwa upole na kumweleza mtoto kwa nini hapaswi kujiendesha jinsi hiyo. Pia mzazi wa mtoto apaswa kuelezwa tatizo hilo kwa njia ya fadhili na kuonyeshwa uhitaji wa kumwangalia mtoto wake. Mzazi apaswa kuitikia ifaavyo.
Inaeleweka kwamba nyakati fulani vitoto vichanga na watoto wadogo waweza kulia au kuvuruga mikutano inapoendelea. Wakaribishaji, ambao hufika angalau dakika 20 kabla ya programu kuanza, wanaweza kuhifadhi viti vichache vya nyuma kwenye jumba kwa ajili ya wazazi ambao wangependa kuketi hapo pamoja na watoto wao wachanga. Sisi wengine twapaswa kuonyesha ushirikiano kwa kuwaachia viti hivyo.
Ikiwa mtoto anavuruga, mzazi apaswa kuchukua hatua fulani. Mzazi asipofanya hivyo na mvurugo huo ukengeushe fikira, mkaribishaji apaswa kumwomba mzazi kwa njia ya fadhili ikiwa angependa kumpeleka mtoto huyo nje ya jumba. Tunapokaribisha wapya walio na watoto wachanga kwenye mikutano, twapaswa kuketi pamoja nao na kuwasaidia ikiwa watoto wanalia au kusababisha mvurugo katika njia fulani-fulani.
Tunapata shangwe tuonapo watoto wa kila umri kwenye Jumba la Ufalme na kutazama mwenendo wao mzuri ndani ya nyumba ya Mungu. (1 Tim. 3:15) Kwa kuheshimu mpango wa Yehova wa ibada, wanampa heshima nao huthaminiwa na wote kutanikoni.