Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • km 9/03 kur. 3-4
  • Iweni na Bidii Katika “Kutoa Ushahidi Kamili”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Iweni na Bidii Katika “Kutoa Ushahidi Kamili”
  • Huduma Yetu ya Ufalme—2003
  • Habari Zinazolingana
  • Ongea Juu ya Utukufu wa Umaliki wa Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • Je, Uko Tayari Kuhubiri Isivyo Rasmi?
    Huduma ya Ufalme—2009
  • Unaweza Kuhubiri Isivyo Rasmi!
    Huduma Yetu ya Ufalme—2010
  • Usisahau Kamwe Wewe Ni Shahidi!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
Pata Habari Zaidi
Huduma Yetu ya Ufalme—2003
km 9/03 kur. 3-4

Iweni na Bidii Katika “Kutoa Ushahidi Kamili”

1 Kama Yesu na watumishi wengine wengi waaminifu wa kale, mtume Paulo alikuwa mhubiri mwenye bidii wa habari njema, ‘akitoa ushahidi kamili’ katika hali mbalimbali. Hata alipokuwa katika kifungo cha nyumbani, “akawa akiwapokea kwa fadhili wote wale walioingia ndani kwake, akiwahubiri ufalme wa Mungu na kufundisha mambo yahusuyo Bwana Yesu Kristo kwa uhuru wa usemi ulio mkubwa zaidi sana.”—Mdo. 28:16-31.

2 Nasi pia tunaweza kuwa na bidii katika “kutoa ushahidi kamili” nyakati zote. Hiyo inatia ndani kuwahubiria watu tunaokutana nao tunaposafiri kuelekea au kutoka kwenye makusanyiko na katika mji au jiji la kusanyiko.—Mdo. 28:23; Zab. 145:10-13.

3 Ni Mahubiri ya Vivi Hivi au Yasiyo Rasmi? Je, kuna tofauti yoyote? Ndiyo. Jambo linalofanywa vivi hivi hutukia tu bila kutarajiwa au kukusudiwa, halina mpango au si muhimu sana. Bila shaka, huduma yetu haifanywi vivi hivi. Sawa na Paulo, tunaona ni muhimu kumtukuza Mungu kwa kuwahubiria wengine, na tunapaswa kujitahidi kutoa ushahidi tunapokuwa safarini mwaka huu. Hata hivyo, twaweza kusema ifaavyo kwamba tunawafikia wengine isivyo rasmi, yaani tukiwa tumestarehe, kwa mazungumzo ya kirafiki, na ya kawaida. Njia hiyo inaweza kuleta matokeo.

4 Jitayarishe Kutoa Ushahidi: Paulo alihitaji kutafuta nafasi za kutoa ushahidi alipokuwa katika kifungo cha nyumbani huko Roma. Akiwa huko, aliwaalika viongozi wa dini Wayahudi wa eneo hilo nyumbani mwake. (Mdo. 28:17) Ingawa kulikuwa na kutaniko la Kikristo huko Roma, Paulo aligundua kwamba Wayahudi wa jiji hilo hawakujua mengi kuhusu imani ya Kikristo. (Mdo. 28:22; Rom. 1:7) Hakuogopa “kutoa ushahidi kamili” kuhusu Yesu Kristo na kuhusu Ufalme wa Mungu.

5 Wafikirie wale wote ambao huenda ukakutana nao unaposafiri ambao hawajui mengi kuhusu Mashahidi wa Yehova. Labda hata hawajui kwamba tunawafundisha wengine Biblia bila malipo. Uwe makini ili upate fursa za kuwahubiria wale unaokutana nao unaposafiri, unapopumzika njiani, unapokuwa kwenye kituo cha petroli, madukani, unapolala hotelini, unapokula mikahawani, unaposafiri kwa magari ya umma, na kadhalika. Panga mapema jinsi utakavyoanzisha mazungumzo na kutoa ushahidi mfupi. Siku zijazo unaweza kufanya mazoezi ya kuwahubiria isivyo rasmi majirani zako, watu wa ukoo, wafanyakazi, na marafiki.

6 Utahitaji vichapo unapohubiri isivyo rasmi. Vichapo gani? Unaweza kutumia trakti Je, Ungependa Kujua Mengi Zaidi Kuhusu Biblia? Kazia mafungu matano ya kwanza ambayo yanaeleza sababu mbalimbali za kusoma Biblia. Onyesha sehemu ya kuomba funzo la Biblia bila malipo iliyo nyuma ya trakti hiyo. Ukimpata mtu anayependezwa, mpe broshua Anataka. Beba kijitabu Good News for All Nations ili uwaonyeshe watu wanaozungumza lugha nyingine. Ukurasa wa 2 unaonyesha jinsi unavyoweza kukitumia kutoa ushahidi. Ikiwa unasafiri kwa gari, huenda ukabeba vichapo vingine vichache vya msingi kwa ajili ya wale wanaopendezwa na ujumbe wa Ufalme.

7 Zingatia Sura na Mwenendo Wako: Twapaswa kuhakikisha kwamba mwenendo, mavazi, na mapambo yetu hayatawafanya wengine wawe na maoni mabaya au ‘waseme vibaya’ kuhusu tengenezo la Yehova. (Mdo. 28:22) Hatupaswi kufanya hivyo tunapohudhuria kusanyiko tu bali pia tunaposafiri na wakati wa mapumziko. Gazeti la Mnara wa Mlinzi la Agosti 1, 2002, ukurasa wa 18, fungu la 14, lilionya hivi: “Hatupaswi kuvalia mavazi ya kujionyesha, ya kiajabu-ajabu, yanayochochea nyege, yanayofunua uchi, au ya mitindo inayopita kiasi. Kwa kuongezea, tunapaswa kuvalia kwa njia ya ‘kumstahi Mungu.’ Hilo ni jambo linalotufanya tutafakari, sivyo? Hatupaswi kuvalia tu kwa njia inayofaa wakati tunapohudhuria mikutano na kuvalia ovyoovyo nyakati nyingine. Sikuzote mavazi yetu yanapaswa kuonyesha staha na heshima kwa kuwa sisi ni Wakristo na wahudumu wakati wote.”—1 Tim. 2:9, 10.

8 Tunapaswa kuvalia kwa kiasi na kwa heshima. Iwapo sikuzote mavazi na mwenendo wetu unaonyesha kwamba tunamwamini Mungu, hatutaogopa kuhubiri isivyo rasmi kwa sababu tumevalia kiholela.—1 Pet. 3:15.

9 Kuhubiri Isivyo Rasmi Kuna Matokeo: Paulo alipata matokeo mazuri sana kutokana na jitihada zake za kuhubiri alipokuwa katika kifungo cha nyumbani kwa miaka miwili huko Roma. Luka aliripoti kwamba ‘wengine walianza kuamini mambo yaliyosemwa.’ (Mdo. 28:24) Paulo alieleza matokeo aliyopata kwa “kutoa ushahidi kamili” alipoandika hivi: “Mambo yangu yamegeuka kuwa kwa ajili ya kusonga mbele kwa habari njema badala ya kuwa vingine, hivi kwamba vifungo vyangu vimejulikana kwa watu wote kwa kushirikiana na Kristo miongoni mwa Walindaji wa Praetori wote na wale wengine wote; na walio wengi zaidi kati ya akina ndugu katika Bwana, wakihisi uhakika kwa sababu ya vifungo vyangu vya gereza, wanaonyesha moyo mkuu hata zaidi kulisema neno la Mungu bila hofu.”—Flp. 1:12-14.

10 Baada ya kuhudhuria siku moja ya kusanyiko la wilaya mwaka jana, wenzi fulani wa ndoa walipata matokeo mazuri walipomhubiria mwanamke aliyehudumu mkahawani, alipowauliza kuhusu beji zao za kusanyiko. Walimweleza kuhusu kusanyiko na kuhusu tumaini la wanadamu la wakati ujao linalopatikana katika Biblia. Walimpa trakti Je, Ungependa Kujua Mengi Zaidi Kuhusu Biblia? na wakamweleza kuhusu mpango wa kujifunza Biblia bila malipo. Mwanamke huyo alisema kwamba alitaka mtu fulani amtembelee, hivyo aliandika jina na anwani yake nyuma ya trakti hiyo, na akawaomba wenzi hao wafanye mpango huo. Ni nani ajuaye matokeo utakayopata mwaka huu kwa “kutoa ushahidi kamili” kwa bidii?

11 Eneza Habari Njema kwa Bidii: Hebu wazia jinsi mtume Paulo alivyofurahi aliposikia kwamba Wakristo wenzake walikuwa wakiiga bidii yake! Na tufanye yote tuwezayo kueneza habari njema isivyo rasmi kuhusu mafundisho yetu ya Biblia tunapohudhuria makusanyiko.

[Maswali ya Funzo]

1, 2. Kwa nini unavutiwa na maoni ya Paulo kuhusu kuhubiri habari njema, nasi tunawezaje kumwiga katika “kutoa ushahidi kamili”?

3. Tunawezaje kuepuka mahubiri yasiyo rasmi kuwa mahubiri ya vivi hivi?

4. Ni nini kilichomwezesha Paulo kutoa ushahidi alipokuwa nyumbani?

5, 6. Tuna fursa zipi za kutoa ushahidi kwa njia isiyo rasmi, na tunaweza kufanya matayarisho gani ili kufanya hivyo kikamili?

7, 8. Tunapaswa kutii shauri gani kuhusu sura na mwenendo wetu tunaposafiri na wakati wa mapumziko?

9. Paulo alipata matokeo gani alipohubiri huko Roma?

10. Wenzi fulani wa ndoa walipata matokeo gani walipotoa ushahidi mwaka jana?

11. Tunapaswa kusitawisha sifa gani ili kueneza habari njema kwa “kutoa ushahidi kamili” wakati wa makusanyiko?

[Sanduku katika ukurasa wa 3]

Vichapo Vinavyohitajiwa Katika Mahubiri Yasiyo Rasmi

■ Je, Ungependa Kujua Mengi Zaidi Kuhusu Biblia? (trakti)

■ Mungu Anataka Tufanye Nini? (broshua)

■ Good News for All Nations (kijitabu)

■ Vichapo vingine vya msingi

[Sanduku katika ukurasa wa 4]

Usiwasahau!

Nani? Wote wanaopendezwa ambao walihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo au hotuba ya pekee. Je, tumewaalika kusanyikoni? Yamkini wengi wao watahudhuria wakitiwa moyo kwa fadhili. Wanapofurahia ushirika wenye kujenga na programu ya kiroho yenye kutia moyo kwenye kusanyiko, watavutwa karibu na Yehova na tengenezo lake. Kwa nini usiwaalike uone kama watakuja? Waeleze habari zote, kama vile tarehe, mahali pa kusanyiko na wakati vipindi vinapoanza na kumalizika.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki