Programu Mpya ya Kusanyiko la Mzunguko
1 Bwana wetu alitabiri kwamba wanafunzi wake wangepata dhiki. (Mt. 24:9) Tuyaoneje majaribu? Ni nini kitakachotuwezesha kuvumilia dhiki? Programu ya kusanyiko la mzunguko la mwaka wa utumishi wa 2004 itajibu maswali hayo. Kichwa chake ni “Shangilieni Katika Tumaini. Vumilieni Chini ya Dhiki.”—Rom. 12:12.
2 Mifululizo Miwili ya Hotuba: Mfululizo wa kwanza wenye kichwa “Zaa Matunda kwa Uvumilivu,” utazungumzia jinsi tunavyozaa matunda. Wahubiri kadhaa watahojiwa kuhusu jinsi wanavyohubiri na kufundisha wakitambua umuhimu wa kazi hiyo. Wazazi hasa wanapaswa kusikiliza kwa makini sehemu yenye kichwa “Unapotiwa Nidhamu na Yehova,” ambayo itazungumzia jinsi wazazi wanavyoweza kuwasadikisha watoto. Msemaji wa mwisho katika mfululizo huo atakazia mambo tunayopaswa kufanya ili ulimwengu usituathiri na kutufanya tukose kuzaa matunda.—Marko 4:19.
3 Kichwa cha mfululizo wa pili ni “Kimbia kwa Uvumilivu Shindano la Mbio.” Hotuba hiyo itaonyesha jinsi maisha yetu yalivyo kama shindano la mbio. Kwa nini twahitaji kukimbia kulingana na kanuni? Twawezaje kuondoa kila uzito na kutochoka kabisa katika mbio za uhai? Shauri la Kimaandiko la wakati unaofaa litatusaidia tuendelee kukimbia kwa uvumilivu.
4 Uvumilivu Hutokeza Kibali cha Mungu: Hotuba zitakazotolewa na waangalizi wasafirio zitaimarisha imani ya wale wanaozisikiliza na kutumia shauri hilo. Mojawapo ya hotuba za mwangalizi wa wilaya ina kichwa “Uvumilivu Hutokeza Hali Yenye Kukubaliwa.” Hotuba ya watu wote itajibu maswali haya: Mataifa yanapaswa kutumaini jina la nani, na ni mambo gani yanayohusika? Hotuba ya kumalizia yenye kichwa, “Kwa Kuvumilia Mtajipatia Nafsi Zenu,” itazungumzia jinsi Yesu alivyovumilia ukosefu wa haki bila kuwa na uchungu.
5 Usisahau kubeba kitabu chako cha Shule ya Huduma na Mnara wa Mlinzi wa juma hilo. Andika mambo yatakayokusaidia kukaza fikira na ambayo utayatumia wakati ujao. Mambo makuu ya programu hiyo yatazungumziwa baadaye katika kutaniko.
6 Yehova mwenyewe ametayarisha karamu hii ya chakula cha kiroho. Njoo ule! Tutashangilia ikiwa tutahudhuria ili kufaidika na programu yote.—Isa. 65:14.