Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • km 5/10 kur. 3-5
  • “Wewe Ungekuwa Painia Mzuri!”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Wewe Ungekuwa Painia Mzuri!”
  • Huduma Yetu ya Ufalme—2010
  • Habari Zinazolingana
  • Mapainia Hutoa na Kupokea Baraka
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Utumishi wa Painia—Je, Wakufaa Wewe?
    Huduma Yetu ya Ufalme—1998
  • Baraka za Huduma ya Painia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Sasa Ndio Wakati wa Kuhubiri!
    Huduma ya Ufalme—2005
Pata Habari Zaidi
Huduma Yetu ya Ufalme—2010
km 5/10 kur. 3-5

“Wewe Ungekuwa Painia Mzuri!”

1. Dada mmoja alionaje huduma yake ya painia?

1 “Hakuna kazi nyingine yoyote ambayo ingeniletea uradhi au thawabu nyingi hivi za kiroho.” Hayo ni maneno ya Kathe B. Palm. Yeye alikuwa painia ambaye kwa miaka mingi alijitoa kabisa kufanya kazi ya kuhubiri kotekote nchini Chile, huko Amerika Kusini. Labda mtu anayekutakia maisha yenye kuridhisha ya watumishi wa wakati wote, amekuambia hivi: “Wewe ungekuwa painia mzuri!”

2. Eleza kwa nini tunapata uradhi mwingi kwa kushiriki katika utendaji wa kiroho.

2 Maisha Yanayoridhisha: Yesu, ambaye ni Kielelezo chetu, aliburudika kikweli alipofanya mapenzi ya Baba yake. (Yoh. 4:34) Kwa hiyo, Yesu aliwafundisha wafuasi wake kwa moyo mweupe kwamba uradhi wa kweli unatokana na utendaji unaohusiana na ibada ya Yehova. Tunaridhika tunapofanya sikuzote kazi ambazo Yehova anakubali. Zaidi ya hayo, furaha yetu inaongezeka tunapotumia wakati, nguvu, na mali zetu, kuwasaidia wengine.—Mdo. 20:31, 35.

3. Huenda tukapata shangwe gani kwa kutumia muda mrefu zaidi katika huduma?

3 Kadiri tunavyotumia wakati katika huduma, ndivyo tunavyopata fursa za kujionea shangwe ya kuanzisha na kuongoza mafunzo ya Biblia. Tunapoendelea kupata uzoefu na ustadi katika huduma, huenda tukatambua kwamba bado kuna watu wanaopendezwa katika eneo letu, ijapokuwa wenye nyumba wengi wanakataa ujumbe wetu. Baada ya kuwa mapainia kwa mwaka mmoja, mapainia wa kawaida wanaweza kuhudhuria Shule ya Utumishi wa Painia, na kupata mazoezi ambayo wanaweza kutumia katika huduma. (2 Tim. 2:15) Tunapoendelea na utumishi wa wakati wote bila kuacha, huenda tukawa tunapanda mbegu za kweli zitakazotoa mazao baadaye.—Mhu. 11:6.

4. Vijana wanaoelekea kumaliza shule wanapaswa kufikiria nini?

4 Vijana: Je, umefikiria kwa makini mambo utakayofanya baada ya kumaliza masomo ya msingi? Mpaka leo hii, umepanga mambo mengi maishani mwako kupatana na ratiba yako ya shule. Baada ya kumaliza shule utafanya nini? Badala ya kuanza kazi ya wakati wote, je, umefikiria na kusali kuhusu lengo la kuwa painia wa kawaida? Mambo ambayo utajifunza—kuwahubiria watu wa malezi mbalimbali, kushinda vizuizi vya binafsi, na kusitawisha sifa ya kujizuia na ustadi wa kufundisha—yatakunufaisha katika maisha yako yote.

5. Wazazi na ndugu na dada kutanikoni wanawezaje kuwatia vijana moyo wawe mapainia?

5 Wazazi, je, mnafanya yote mwezayo kuwasaidia watoto wenu waamue kuwa watumishi wa wakati wote? Maneno yenu na mfano wenu mzuri unaweza kuwasaidia sana kutanguliza mambo ya Ufalme. (Mt. 6:33) Ray, aliyeanza utumishi wa painia baada ya kumaliza shule ya upili, anasema hivi: “Mama yangu alikuwa na maoni kwamba utumishi wa painia unafanya maisha yawe yenye kuridhisha sana.” Kwa maneno na matendo, wote kutanikoni wanaweza kuwatia wengine moyo wawe mapainia. Jose, anayeishi Hispania, anasema hivi: “Ndugu na dada katika kutaniko letu waliuona utumishi wa painia kuwa kazi bora kwa vijana. Msaada wao, maelezo yao, na uthamini wao kwa utumishi wa painia ulinisaidia niamue kuwa painia.”

6. Iwapo sasa tunakosa tamaa ya kuwa painia, tunaweza kufanya nini?

6 Kushinda Vizuizi: Lakini vipi ikiwa hutamani kuwa painia? Iwapo unahisi hivyo sasa, sali kwa Yehova na umweleze hisia zako. Unaweza kumwambia hivi: “Sijui kama ninaweza kuwa painia, lakini ninataka kufanya yale yanayokupendeza.” (Zab. 62:8; Met. 23:26) Kisha, tafuta mwongozo wake kupitia Neno na tengenezo lake. Mapainia wengi wa kawaida “walionja” utumishi wa painia walipokuwa mapainia wasaidizi, na wakapata shangwe nyingi hivi kwamba wakaamua kuwa watumishi wa wakati wote.—Zab. 34:8.

7. Tunaweza kufanya nini tukiogopa kwamba hatutaweza kutimiza takwa la saa 70?

7 Namna gani ukiogopa kwamba hutaweza kutimiza takwa la kuhubiri kwa muda wa saa 70 kila mwezi? Ongea na mapainia ambao hali zao za maisha zinafanana na zako. (Met. 15:22) Halafu, andika ratiba kadhaa zinazoweza kukufaa. Huenda ukaona kwamba si vigumu sana kununua wakati ambao umekuwa ukiutumia katika shughuli zisizo za lazima ili uutumie katika huduma.—Efe. 5:15, 16.

8. Kwa nini inafaa tuchunguze upya hali zetu mara kwa mara?

8 Chunguza Upya Hali Zako: Mara nyingi hali za maisha zinabadilika. Kwa hiyo, inafaa uchunguze hali zako mara kwa mara. Kwa mfano, huenda ikawa unakaribia kustaafu kazi yako ya kuajiriwa. Randy, aliyestaafu mapema, anasema hivi: “Uamuzi wangu wa kustaafu mapema umeniwezesha kujiunga na mke wangu katika utumishi wa painia wa kawaida, na tumepata fursa ya kuhamia eneo lenye uhitaji mkubwa zaidi. Nimepata baraka nyingi kwa sababu ya uamuzi wangu, lakini baraka kubwa kuliko zote ni dhamiri safi.”

9. Waume na wake wanapaswa kufikiria nini?

9 Baada ya kuchunguza hali zao kwa uangalifu, baadhi ya waume na wake, wameona kwamba si lazima wote wawili wafanye kazi ya wakati wote. Huenda jambo hili likamaanisha kwamba watahitaji kuridhika na vitu vichache maishani, lakini wanaweza kupata baraka nyingi kwa kujinyima kwa njia hiyo. John, ambaye mke wake aliacha kazi yake hivi majuzi ili apanue huduma yake, anasema: “Ninafurahi sana ninapojua kwamba mke wangu anajishughulisha na utumishi wa Yehova siku nzima.”

10. Ni nini kinachowasukuma Wakristo waamue kuwa mapainia?

10 Njia ya Kuonyesha Upendo na Imani: Yehova amesema kwamba kazi ya kuhubiri ni muhimu kuliko kazi nyingine yoyote. Ulimwengu huu utaharibiwa hivi karibuni, na ni wale tu wanaoliitia jina la Yehova watakaookoka. (Rom. 10:13) Moyo ulio na uthamini na upendo mwingi kwa Yehova kwa ajili ya yote ambayo ametufanyia, utatusukuma tutii amri ya Mwana wake ya kuhubiri kwa bidii. (Mt. 28:19, 20; 1 Yoh. 5:3) Zaidi ya hayo, tukiamini kikweli kwamba tunaishi katika siku za mwisho, hatutatumia ulimwengu kikamili, bali tutasukumwa kufanya yote tuwezayo katika huduma maadamu tungali na wakati.—1 Kor. 7:29-31.

11. Mtu akikuambia kwamba ungekuwa painia mzuri, unapaswa kuyaonaje maneno yake?

11 Mtu hawi painia wa kawaida kwa sababu tu anaitikia mwito wa kuhubiri kwa muda wa saa fulani kila mwezi, bali anafanya hivyo kwa sababu anampenda Mungu. Basi, iwapo mtu atakuambia kwamba ungekuwa painia mzuri, ona jambo hilo kuwa pongezi. Fikiria kwa uzito na usali kuhusu lengo la kujiunga na wale ambao tayari wanashiriki katika utumishi huu wenye kuridhisha.

[Blabu katika ukurasa wa 4]

Wazazi, je, mnafanya yote mwezayo kuwasaidia watoto wenu waamue kuwa watumishi wa wakati wote?

[Blabu katika ukurasa wa 5]

Yehova amesema kwamba kazi ya kuhubiri ni muhimu kuliko kazi nyingine yoyote.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki