“Hekima Huonyeshwa Kuwa Yenye Uadilifu kwa Matendo Yake”
1. Watu fulani huionaje kazi yetu ya kuhubiri?
1 Wakati mwingine, wenye nyumba hukataa kutusikiliza kwa sababu wanatuelewa vibaya au wamepata habari zisizo za kweli kuhusu Mashahidi wa Yehova. Labda maoni yao yameathiriwa na ripoti mbaya katika vyombo vya habari. Katika maeneo mengine, hata tunaitwa “madhehebu hatari.” Tunapaswa kufanya nini tunapokabili hali kama hizo?
2. Ni nini kitakachotusaidia kuepuka kuvunjika moyo tunaposhutumiwa na watu?
2 Dumisha Mtazamo Unaofaa: Katika karne ya kwanza, mara nyingi Yesu na watumishi wengine wa Yehova walieleweka kimakosa na hata kusemwa vibaya. (Mdo. 28:22) Hata hivyo, hawakuruhusu shutuma hizo ziwafanye waionee aibu kazi yao ya kuhubiri. Yesu alisema: “Hekima huonyeshwa kuwa yenye uadilifu kwa matendo yake.” (Mt. 11:18, 19) Aliendelea kufanya mapenzi ya Baba yake kwa bidii, akiwa na uhakika kwamba wale ambao walitaka kujua ukweli wangeona thamani ya habari njema. Tunaweza kuepuka kuvunjika moyo kwa kukumbuka kwamba hata Mwana wa Mungu alitendewa vivyo hivyo.
3. Kwa nini hatushangazwi na ripoti mbaya na upinzani tunaopata leo?
3 Yesu alionyesha kwamba ulimwengu ungewachukia wafuasi wake kama tu walivyomchukia. (Yoh. 15:18-20) Hivyo, hatushangazwi na ripoti mbaya na upinzani tunaopata leo. Kwa kweli, tunatazamia mambo kama hayo yawe mengi zaidi, kadiri tunavyosonga ndani zaidi ya siku za mwisho na hasira ya Shetani kuzidi kuongezeka. (Ufu. 12:12) Tunaweza kufurahi kwa kuwa mambo haya yanaonyesha kwamba ulimwengu wa Shetani utaharibiwa hivi karibuni.
4. Watu wanapokataa habari njema, tunapaswa kufanyaje?
4 Toa Jibu la Upole: Watu wanapokataa kutusikiliza, tunapaswa kuwajibu kwa neema na upole kila wakati. (Met. 15:1; Kol. 4:5, 6) Hali zikiruhusu, tunaweza kumweleza mwenye nyumba mnyoofu kuwa kuna habari nyingi zisizo za kweli kuhusu Mashahidi wa Yehova au tumuulize ni nini kinachofanya awe na maoni aliyo nayo. Kwa kuwa tumemjibu kwa upole, huenda akashuku mambo aliyoyasikia kuhusu Mashahidi wa Yehova, na awe tayari kuwasikiliza Mashahidi wengine watakaomtembelea. Hata hivyo, ikiwa mwenye nyumba amekasirika sana, huenda ikawa vyema kuondoka kwa upole. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova anathamini huduma yetu licha ya maoni mabaya ya watu.—Isa. 52:7.