Siku Tatu za Kuburudishwa Kiroho
1. Tunatazamia kufaidikaje na kusanyiko la wilaya la mwaka huu?
1 Katika ulimwengu huu wa Shetani ambao ni kama nchi iliyokauka kiroho, Yehova anaendelea kuwaburudisha watumishi wake. (Isa. 58:11) Njia moja ambayo Yehova anatumia ili kutuandalia burudisho, ni makusanyiko ya wilaya ya kila mwaka. Kusanyiko la mwaka huu likaribiapo, tunaweza kujitayarishaje kuburudishwa na kuwapa wengine burudisho?—Met. 21:5.
2. Tunapaswa kukamilisha matayarisho gani?
2 Ikiwa bado hujafanya hivyo, anza sasa kupanga mambo yako ya binafsi na shughuli zako kazini ili uweze kuhudhuria siku zote tatu. Je, umekadiria muda wa kusafiri hadi kusanyikoni kila siku ili uweze kufika kwa wakati na kutafuta kiti kabla ya programu kuanza? Hatungependa kukosa sehemu yoyote ya chakula cha kiroho ambacho Yehova ametuandalia! (Isa. 65:13, 14) Je, umekamilisha mipango ya usafiri na mahali pa kulala?
3. Ni mapendekezo gani yatakayotusaidia sisi na familia yetu kufaidika kikamili na programu?
3 Ni nini kitakachokusaidia kuwa makini wakati wa programu? Ikiwezekana, pumzika vya kutosha kila usiku. Mtazame msemaji. Fungua Biblia yako na ufuatane na msemaji anaposoma kila andiko. Andika mambo makuu. Itafaa familia kuketi pamoja ili wazazi waweze kuwasaidia watoto wao kuwa makini. (Met. 29:15) Labda mnaweza kuzungumzia mambo makuu ya programu kila jioni mkiwa familia. Ili familia yenu iendelee kunufaika hata baada ya kusanyiko, tengeni kipindi fulani cha jioni ya Ibada ya Familia ili mzungumzie mambo hususa katika programu ambayo familia yenu inaweza kutumia.
4. Tunaweza kuwasaidiaje wengine katika kutaniko letu wapate burudisho la kiroho?
4 Wasaidie Wengine Wapate Burudisho: Tunataka wengine wapate burudisho la kiroho pia. Je, kuna wahubiri wenye umri mkubwa au wahubiri wengine kutanikoni wanaohitaji msaada wa kuhudhuria kusanyiko? Je, una uwezo wa kuwasaidia? (1 Yoh. 3:17, 18) Wazee, na hasa waangalizi wa vikundi, wanapaswa kuhakikisha kwamba wahubiri kama hao wanapata msaada wanaohitaji.
5. Tutasambazaje mialiko ya kusanyiko? (Ona pia sanduku kwenye ukurasa huu.)
5 Kama kawaida, majuma matatu kabla ya kusanyiko tutakuwa na kampeni ya kuwaalika watu kwenye kusanyiko. Makutaniko yanapaswa kuazimia kusambaza mialiko yote na katika sehemu kubwa iwezekanavyo ya eneo la kutaniko. Hata hivyo, ikiwa mwishoni mwa kampeni familia yenu itakuwa haijasambaza mialiko yote, tafadhali ileteni mnapokuja kusanyikoni. Itatumiwa kuwaalika watu ambao tutawahubiria isivyo rasmi katika mji wa kusanyiko. Mialiko ambayo hamtazamii kutumia mkiwa katika mji wa kusanyiko inapaswa kupewa mkaribishaji mnapoingia katika jengo la kusanyiko siku ya Ijumaa. Habari kuhusu jinsi ya kutumia mialiko hiyo itatolewa kusanyikoni.
6. Tunaweza kuwafurahisha wengine jinsi gani kwa kuwa na tabia nzuri?
6 Tabia Nzuri Hufurahisha: Katika nyakati hizi ambapo watu wengi ‘wanajipenda wenyewe’ na hawajali hisia za wengine, inafurahisha kama nini kuwa pamoja na Wakristo wenzetu wanaojitahidi kuwa na tabia nzuri! (2 Tim. 3:2) Tunaonyesha tabia nzuri kwa kuingia kwa utulivu na utaratibu, malango ya jengo la kusanyiko yanapofunguliwa saa 2:00 asubuhi. Ni tabia nzuri pia kuhifadhi viti kwa ajili ya wale tu tunaoishi nao, tunaosafiri nao katika gari letu au lao, au watu tunaojifunza Biblia pamoja nao. Tunafuata mwelekezo wa mwenyekiti wa kusanyiko anapotuomba tuketi na kusikiliza muziki unaotangulia kila sehemu ya programu. Ni adabu nzuri kuzima peja na simu za mkononi au kupunguza sauti kabisa ili tusiwakengeushe wengine wakati wa programu. Pia, si tabia nzuri kuzungumza bila sababu, kuandika ujumbe mfupi, au kuzurura-zurura kwenye vijia vya jengo la kusanyiko.
7. Tunaweza kuburudishwa na kuwaburudisha ndugu zetu kwa njia zipi tunaposhirikiana nao?
7 Ushirika Wenye Kufurahisha: Makusanyiko hutuandalia fursa nzuri sana za kufurahia umoja na udugu wa Kikristo unaoburudisha. (Zab. 133:1-3) Jitahidi ‘kupanuka’ kwa kujitambulisha kwa ndugu na dada wa makutaniko mengine. (2 Kor. 6:13) Unaweza kuwa na lengo la kujua angalau mtu mmoja au familia moja kila siku. Kipindi cha pumziko kinatupa fursa nzuri ya kufanya hivyo. Kwa hiyo, beba chakula chepesi ili ufurahie ushirika wa akina ndugu wakati unapokula badala ya kuondoka na kwenda kula katika mikahawa iliyo karibu. Jambo hilo linaweza kukusaidia kuanzisha urafiki wa kudumu.
8. Kwa nini tunapaswa kujitolea kufanya kazi kusanyikoni, na tunaweza kufanya hivyo jinsi gani?
8 Inaburudisha kama nini kufanya kazi pamoja na Wakristo wenzetu katika utumishi mtakatifu! Je, unaweza kujitolea kusaidia katika idara fulani au kulisaidia kutaniko lako linapoombwa kufanya usafi wa sehemu fulani? (Zab. 110:3) Ikiwa huna mgawo wowote kwa sasa, fikiria kama unaweza kuwaendea ndugu katika Idara ya Utumishi wa Kujitolea utakapokuwa kusanyikoni. Kazi ikifanywa na watu wengi huwa rahisi na huleta shangwe.
9. Kwa nini tunapaswa kuzingatia sana mwenendo, mavazi, na mapambo yetu wakati wa kusanyiko?
9 Mwenendo Wetu Huwavutia Wanaotutazama: Tunapaswa kuwa na mwenendo mzuri muda wote wa kusanyiko, kutia ndani kabla na baada ya programu. Watu wanaotutazama tunapokuwa katika mji wa kusanyiko wanapaswa kuona tofauti yenye kuburudisha kati yetu na watu wasio Mashahidi. (1 Pet. 2:12) Mavazi na mapambo yetu kusanyikoni, mahali tunapolala, na katika mikahawa yanapaswa kuonyesha kwamba tunamheshimu Yehova. (1 Tim. 2:9, 10) Kuvaa beji zetu kutatutambulisha kwa wanaotutazama na huenda kukatokeza fursa ya kuwaambia kuhusu kusanyiko letu na kutoa ushahidi.
10. Tunaweza kuhakikishaje kwamba wafanyakazi wa hoteli na mikahawa wana maoni mazuri kuelekea kusanyiko letu?
10 Tunaweza kuwa wenye kuburudisha kwa wafanyakazi wa hoteli na mikahawa jinsi gani? Hatupaswi kuhifadhi vyumba zaidi ya tutakavyotumia, kwa kuwa hilo litawazuia wahudhuriaji wengine kupata vyumba wanavyohitaji na huenda mwenye hoteli akapata hasara. Ikiwa kuna wateja wengi tunapowasili au tunapoondoka hotelini, tunapaswa kuwa na subira na wenye neema. (Kol. 4:6) Inafaa kuwapa bakshishi watu wanaotuhudumia mikahawani, wanaotubebea mizigo hotelini, wanaotusafishia chumba, na wanaotuhudumia kwa njia nyinginezo.
11. Taja mambo yaliyoonwa yanayoonyesha kwamba mwenendo wa Kikristo hutoa ushahidi mzuri.
11 Mwenendo wetu wakati wa kusanyiko unawafanya watu wawe na maoni gani? Kulingana na gazeti moja la habari, meneja wa jengo moja lililotumiwa kwa ajili ya makusanyiko alisema hivi: “Watu hawa ni wenye heshima sana. Sisi hufurahi sana wanapotumia jengo letu kila mwaka.” Mwaka uliopita, mtu fulani asiye Shahidi alipoteza kifuko chake cha pesa katika hoteli ambayo baadhi ya wahudhuriaji wa kusanyiko walilala. Kifuko hicho kilipopatikana na kupelekwa kwa meneja wa hoteli kikiwa na vitu vyote, meneja huyo alimwambia aliyepoteza kifuko hicho hivi: “Ni vizuri kwamba idadi kubwa ya wateja tulio nao sasa ni Mashahidi kwa kuwa wanahudhuria kusanyiko lao karibu na hapa. La sivyo, labda kifuko chako hakingerudishwa.”
12. Kusanyiko likaribiapo, tunapaswa kuazimia nini, na kwa nini?
12 Makusanyiko ya mwaka huu yanakaribia sana. Wakati mwingi umetumiwa na jitihada nyingi zimefanywa kutayarisha programu na kufanya hali za kusanyiko ziwe zenye kuburudisha. Uwe na lengo la kuhudhuria siku zote tatu, na uwe tayari kufurahia mambo ambayo yameandaliwa na Yehova na tengenezo lake. Azimia kuwaburudisha wengine kupitia tabia nzuri, ushirika wenye kufurahisha, na mwenendo mzuri. Hivyo, wewe na wengine mnaweza kuwa na hisia kama za mhudhuriaji mmoja wa kusanyiko la mwaka uliopita aliyeandika, “Sijapata kuona kipindi kingine chenye kuridhisha kama hiki!”
[Blabu katika ukurasa wa 4]
Kama kawaida, majuma matatu kabla ya kusanyiko tutakuwa na kampeni ya kuwaalika watu kwenye kusanyiko
[Blabu katika ukurasa wa 6]
Mavazi na mapambo yetu kusanyikoni, mahali tunapolala, na katika mikahawa yanapaswa kuonyesha kwamba tunamheshimu Yehova
[Blabu katika ukurasa wa 7]
Azimia kuwaburudisha wengine kupitia tabia nzuri, ushirika wenye kufurahisha, na mwenendo mzuri
[Sanduku katika ukurasa wa 4-7]
Vikumbusho vya Kusanyiko la Wilaya—2011
◼ Saa za Programu: Siku zote tatu, programu itaanza saa 3:20 asubuhi. Milango itafunguliwa saa 2:00 asubuhi. Muziki unaotangulia kila sehemu ya programu unapotangazwa, sote tunapaswa kuketi ili programu ianze kwa utaratibu na heshima. Programu itaisha saa 10:55 jioni siku ya Ijumaa na Jumamosi, na saa 9:40 jioni siku ya Jumapili.
◼ Maegesho: Katika sehemu zote za makusanyiko ambapo tumeruhusiwa kuegesha magari, sehemu za kuegesha zitapatikana bila malipo. Wale watakaofika kwanza, ndio watakaopata mahali pa kuegesha kwanza. Watu walio walemavu wanaweza kuonyeshwa ufikirio wa pekee.
◼ Viti: Unaweza kuhifadhi viti kwa ajili ya wale tu tunaoishi nao, tunaosafiri nao katika gari letu au lao, au watu tunaojifunza Biblia pamoja nao.—1 Kor. 13:5.
◼ Chakula cha Mchana: Tafadhali beba chakula cha mchana badala ya kuondoka mahali pa kusanyiko wakati wa mapumziko ili kwenda kutafuta chakula. Mfuko au sanduku dogo la kubebea chakula ambalo linaweza kutoshea chini ya kiti linaweza kutumiwa. Mifuko au masanduku makubwa ya kubebea chakula na pia vyombo vya glasi haviruhusiwi kusanyikoni.
◼ Michango: Tunaweza kuonyesha kwamba tunathamini mipango ya kusanyiko kwa kutoa michango ya hiari kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote kwenye Jumba letu la Ufalme au kusanyikoni. Cheki au hundi zozote zinazotolewa kusanyikoni zinapaswa kuandikwa “International Bible Students Association,” au jina la shirika la kisheria linalotumiwa nchini kwenu.
◼ Aksidenti na Hali za Dharura: Hali ya dharura ya kimatibabu ikitokea kusanyikoni, tafadhali wasiliana na mkaribishaji aliye karibu, ambaye ataijulisha mara moja Idara ya Huduma ya Kwanza ili mtu anayestahili kutoa huduma ya kwanza achunguze hali hiyo na kutoa msaada unaohitajika. Ikihitajika, ndugu katika idara hii wataitisha gari la kubebea wagonjwa. Jambo hili litapunguza idadi ya simu zinazopokewa na kitengo cha huduma za dharura.
◼ Dawa: Ikiwa unatumia dawa ulizoagizwa na daktari, tafadhali hakikisha umebeba za kutosha kwa kuwa hazitapatikana kusanyikoni.
◼ Viatu: Kila mwaka watu kadhaa hujeruhiwa kwa sababu ya viatu. Kwa hiyo, ni vizuri kuvaa viatu vya kawaida, vinavyokutoshea vizuri na vinavyokuwezesha kutembea kwenye ngazi, viunzi vya chuma, na maeneo mengine, bila kujikwaa.
◼ Marashi: Makusanyiko mengi hufanywa ndani ya majumba. Basi, litakuwa jambo la fadhili kuepuka kutumia marashi yenye harufu kali ambayo huenda yakawaathiri wale walio na matatizo ya kupumua au matatizo mengine kama hayo.—1 Kor. 10:24.
◼ Fomu za Tafadhali Fuatia Upendezi (S-43): Ukikutana na mtu yeyote anayependezwa unapohubiri wakati wa kusanyiko, unapaswa kutumia fomu ya Tafadhali Fuatia Upendezi kutoa habari kumhusu mtu huyo. Wahubiri wanapaswa kubeba fomu moja au mbili kusanyikoni. Unaweza kuwaachia ndugu kwenye Idara ya Vitabu fomu ulizojaza ili zishughulikiwe, au umpe mwandishi wa kutaniko lenu unaporudi nyumbani.—Ona Huduma Yetu ya Ufalme ya Novemba 2009, uku. 4.
◼ Mikahawa: Fanya jina la Yehova liheshimiwe kupitia mwenendo wako mzuri kwenye mikahawa. Toa bakshishi ikiwa ni jambo la kawaida katika eneo la kwenu.
◼ Hoteli:
(1) Tafadhali usihifadhi vyumba vingi kuliko utakavyohitaji, wala chumba kisikaliwe na watu wanaozidi idadi inayoruhusiwa.
(2) Usifute hifadhi ya chumba isipokuwa kwa sababu ya hali ya dharura. Julisha wasimamizi wa hoteli mara moja unapogundua kwamba hutatumia chumba kilichokuwa kimehifadhiwa.—Mt. 5:37.
(3) Chukua kigari cha kubebea mizigo wakati tu unapokuwa tayari kukitumia, na ukirudishe mara moja ili wengine waweze kukitumia.
(4) Pika tu katika vyumba ambavyo upishi umeruhusiwa.
(5) Wape bakshishi wafanyakazi wa hoteli ambao wanakusaidia kubeba mizigo, na pia yule anayekusafishia chumba.
(6) Fuata vizuri utaratibu uliowekwa hotelini kuhusu kiamsha-kinywa, kahawa, au barafu ambazo huandaliwa kwa ajili ya wageni.
(7) Nyakati zote, onyesha tunda la roho unaposhughulika na wafanyakazi wa hoteli. Wanawahudumia watu wengi sana na wanathamini tunapokuwa wenye fadhili, subira, na kiasi.
(8) Bei ya chumba iliyoonyeshwa katika Orodha ya Mahali pa Kulala Palipopendekezwa ni ya siku moja bila kutia ndani kodi. Ukiambiwa bei ya juu kuliko bei iliyoorodheshwa, au ulipishwe vitu ambavyo hukuviagiza wala kuvitumia, kataa gharama hizo na uwajulishe ndugu katika Idara ya Mahali pa Kulala kusanyikoni upesi iwezekanavyo.
(9) Kukiwa na shida kuhusiana na chumba chako hotelini, julisha Idara ya Mahali pa Kulala ukiwa ungali kusanyikoni ili ndugu waweze kukusaidia.
◼ Kazi ya Kujitolea: Tutafurahia kusanyiko hata zaidi iwapo tutajitolea kusaidia kufanya kazi inayohusika. (Mdo. 20:35) Yeyote ambaye angependa kujitolea anapaswa kwenda kwenye Idara ya Utumishi wa Kujitolea kusanyikoni. Watoto walio chini ya umri wa miaka 16 wanaweza kujitolea kufanya kazi, lakini wafanye hivyo chini ya usimamizi wa mzazi au mtunzaji wao. Pia, wanaweza kufanya kazi chini ya usimamizi wa mtu mzima ambaye amekabidhiwa daraka hilo na mzazi au mtunzaji wao.
[Sanduku katika ukurasa wa 5]
Tutaisambazaje Mialiko?
Ili tuweze kusambaza mialiko katika eneo lote, itatubidi kusema kifupi. Labda tunaweza kusema hivi: “Jambo. Tunashiriki katika kampeni ya ulimwenguni pote ya kusambaza mwaliko huu. Hii ni nakala yako. Habari zaidi zinapatikana katika mwaliko.” Upande wa mbele wa mwaliko unaamsha upendezi, kwa hiyo, unapompa mwenye nyumba mwaliko, hakikisha kwamba anauona vizuri upande huo wa mbele. Uwe mchangamfu. Ikifaa, tunaweza kuambatanisha magazeti yetu na mialiko hiyo tunapoisambaza katika siku za Jumamosi na Jumapili.