Je, Unaweza Kushiriki Kutoa Ushahidi Jioni?
1. Kulingana na msomi mmoja, mtume Paulo alihubiri nyumba kwa nyumba wakati gani?
1 Kulingana na kitabu Daily Life in Bible Times, ilikuwa kawaida kwa Paulo kuhubiri nyumba kwa nyumba “kuanzia saa 10 jioni na kuendelea hadi usiku.” Hatujui ikiwa hiyo ndiyo iliyokuwa ratiba ya Paulo, lakini tunajua kwamba alikuwa tayari ‘kufanya mambo yote kwa ajili ya habari njema.’ (1 Kor. 9:19-23) Hilo lingehusisha kupanga mambo ili ahubiri nyumba kwa nyumba wakati ambapo angeweza kuzungumza na watu wengi zaidi.
2. Kwa nini jioni ni wakati mzuri wa kushiriki katika huduma?
2 Wahubiri katika maeneo mengi wamekuwa na desturi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba asubuhi, katikati ya juma. Je, katika eneo lenu, wakati huo bado unafaa? Painia mmoja anaeleza hivi kuhusu eneo lake: “Si rahisi kuwapata watu nyumbani mchana. Lakini watu wengi huwa nyumbani jioni.” Kutoa ushahidi jioni huandaa fursa bora, hasa ya kuwahubiria wanaume habari njema. Mara nyingi, wenye nyumba hawana shughuli nyingi sana na wako tayari kwa mazungumzo. Ikiwa kuna manufaa ya kufanya hivyo, wazee wanapaswa kupanga mikutano ya utumishi jioni.
3. Tunawezaje kuonyesha utambuzi tunaposhiriki kutoa ushahidi jioni?
3 Tumia Utambuzi: Ni muhimu kuwa wenye busara tunaposhiriki kutoa ushahidi jioni. Kwa mfano, ukimtembelea mtu wakati usiofaa, kama vile wakati anapokula chakula cha jioni, ni vizuri kumwambia utamtembelea baadaye. Ikiwa giza limeingia, simama mahali ambapo mwenye nyumba atakuona, na bila kukawia jitambulishe na ueleze kusudi la kumtembelea. Pia, ni jambo la busara kuhubiri wawili wawili au kwa vikundi na kubaki katika barabara zenye mwangaza wa kutosha ambazo zina watu. Usiwatembelee watu usiku sana ili usiwasumbue wanapojiandaa kulala. (2 Kor. 6:3) Ikiwa eneo si salama baada ya giza kuingia, hubiri eneo hilo kabla ya jua kuzama.—Met. 22:3.
4. Ni baraka gani zinazotokana na kushiriki kutoa ushahidi jioni?
4 Baraka: Utumishi unafurahisha zaidi tunapowapata watu na kuwatolea ushahidi. Kadiri tutakavyotoa ushahidi, ndivyo tutakavyopata fursa zaidi za kuwasaidia wengine “waokolewe na kupata ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Tim. 2:3, 4) Je, unaweza kurekebisha ratiba yako ili ushiriki kutoa ushahidi jioni?