Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g93 3/22 kur. 3-4
  • Kwa Nini Kuna Maonyo Mengi Bandia?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kwa Nini Kuna Maonyo Mengi Bandia?
  • Amkeni!—1993
  • Habari Zinazolingana
  • Kiumbe Mwepaji—Mchukiwa Tena Mpendwa
    Amkeni!—1994
  • Matabiri ya Mwisho wa Ulimwengu
    Amkeni!—1995
  • Jitihada ya Kutafuta Matabiri Yenye Kutegemeka
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1993
g93 3/22 kur. 3-4

Kwa Nini Kuna Maonyo Mengi Bandia?

Mwisho wa Ulimwengu—Ni Karibu Kadiri Gani?

HADITHI husimuliwa juu ya mvulana aliyetunza kondoo za wanakijiji. Ili kuleta msisimuko fulani, siku moja alipaza sauti, “Mbwa mwitu! Mbwa mwitu!” na hakukuwa na mbwa mwitu. Wanakijiji walikimbia nje wakiwa na marungu ya kufukuzia mbwa mwitu huyo, ila tu kupata hakukuwa yeyote. Hilo lilimfurahisha sana yule mvulana hivi kwamba alirudia kilio kile. Tena wanakijiji wakakimbia nje na marungu yao, ila tu kugundua kwamba lilikuwa onyo jingine bandia. Baada ya hayo mbwa mwitu alikuja, na mvulana akapiga kilio cha kuonya, “Mbwa mwitu! Mbwa mwitu!” lakini wanakijiji walipuuza kilio chake wakifikiri ni kionyo kingine bandia. Walikuwa wamedanganywa mara nyingi sana.

Ndivyo imekuwa kwa wale wanaopiga mbiu juu ya mwisho wa ulimwengu. Kwa muda wa karne nyingi tangu siku za Yesu, utabiri mwingi usiotimizwa umefanywa hivi kwamba wengi hawauchukui kwa uzito.

Gregory 1, papa kuanzia 590 hadi 604 W.K., katika barua kwa mfalme wa Ulaya, alisema: “Pia tunataka Ewe Mtukufu ujue, kama vile tumejifunza kwa maneno ya Mungu Mwenye Enzi katika Maandiko Matakatifu, kwamba mwisho wa ulimwengu wa sasa tayari ni karibu na kwamba Ufalme usio na kikomo wa Watakatifu unakaribia.”

Katika karne ya 16, Martin Luther, mwanzilishi wa Kanisa la Lutheri, alitabiri kwamba mwisho ulikuwa karibu sana. Kulingana na chanzo kimoja, yeye alisema: “Kwa sehemu yangu, nina hakika kwamba siku ya hukumu i karibu sana.”

Kuhusu kimojawapo vikundi vya kwanza vya Baptisti, inaripotiwa: “Wanabaptisti wa mapema Karne ya Kumi na Sita waliamini kwamba Mileani ingetukia mwaka 1533.”

“Edwin Sandys (1519-1588), Askofu Mkuu wa York na wa Uingereza . . . asema, . . . ‘Acheni tuwe na hakika kwamba kuja huku kwa Bwana ni karibu.’”

William Miller, ambaye kwa ujumla husifiwa kwa kuanzisha Kanisa la Adventisti, ananukuliwa akisema: “Nina uhakika kabisa kwamba wakati fulani kati ya Machi 21, 1843, na Machi 21, 1844, kulingana na njia ya Kiyahudi ya kuhesabu wakati, Kristo atakuja.”

Je! kushindwa kutimia kwa utabiri huo mbalimbali kunamaanisha kwamba wale walioufanya ni manabii bandia, kupatana na maana ya Kumbukumbu la Torati 18:20-22? Andiko hilo husema: “Lakini nabii atakayenena neno kwa kujikinai kwa jina langu, ambalo sikumwagiza kulinena, au atakayenena katika jina la miungu mingine, nabii yule atakufa. Nawe ukisema moyoni mwako, Tutajuaje neno asilolinena BWANA [Yehova, New World Translation]? Atakaponena nabii kwa jina la BWANA [Yehova, NW], lisifuate jambo lile wala kutimia, hilo ndilo neno asilolinena BWANA [Yehova, NW].”

Kuna wale wanaotabiri mambo ya kuvutia juu ya mwisho wa ulimwengu ili kuvuta fikira za watu na kufuatwa nao, lakini wengine wamesadikishwa kwa unyofu kwamba mbiu zao ni za kweli. Wanasema juu ya matazamio yanayotegemea fasili yao yenyewe ya andiko fulani au tukio la asili. Wao hawadai kwamba utabiri wao mbalimbali ni ufunuo mbalimbali kutoka kwa Yehova na kwamba katika maana hiyo wanatabiri katika jina la Yehova. Hivyo, katika hali hizo, maneno yao yanapokosa kutimia, hawapaswi kuonwa kuwa manabii bandia kama wale tunaotahadharishwa kwenye Kumbukumbu la Torati 18:20-22. Katika udhaifu wao wa kibinadamu, wao hufasili mambo kimakosa.a

Bila kukatizwa tamaa na ushinde wa hapo mbeleni, inaonekana wengine wamechochewa na kukaribia kwa mwaka 2000 na wamefanya utabiri mwingineo juu ya mwisho wa ulimwengu. The Wall Street Journal la Desemba 5, 1989, lilichapisha makala yenye kichwa “Harara ya Mileani: Manabii Waongezeka, Mwisho ni Karibu.” Mwaka 2000 ukiwa unakaribia, waevanjelisti mbalimbali wanatabiri kwamba Yesu anakuja na kwamba miaka ya 1990 itakuwa “wakati wa matatizo yasiyopata kuonwa tena.” Makala hii ilipokuwa ikiandikwa, tukio la karibuni lilikuwa katika Jamhuri ya Korea, ambako Misheni ya Siku Zijazo ilitabiri kwamba mnamo Oktoba 28, 1992, katika usiku wa manane, Kristo angekuja na kuwachukua waamini hadi mbinguni. Vikundi kadhaa vinginevyo vya kutangaza mwisho vilifanya matabiri ayo hayo. Wingi wa maonyo bandia unasikitisha. Hayo ni kama vile vilio vya mvulana mchungaji kusema mbwa mwitu, mbwa mwitu—upesi watu huyapuuza, na onyo la kweli lijapo, hilo pia hupuuzwa.

Lakini kwa nini kumekuwa na mwelekeo huo wa kutoa maonyo bandia katika muda wa karne nyingi hadi kufikia siku yetu, kama vile Yesu alivyosema yangetolewa? (Mathayo 24:23-26) Baada ya kuwaambia wafuasi wake kuhusu matukio mbalimbali ambayo yangetia alama kurudi kwake, Yesu aliwaambia hivi, kama tusomavyo kwenye Mathayo 24:36-42: “Habari ya siku ile na saa ile hakuna aijuaye, hata malaika walio mbinguni, wala Mwana, ila Baba peke yake. Kwa maana kama vile ilivyokuwa siku za Nuhu, ndivyo kutakavyokuwa kuja kwake Mwana wa Adamu. . . . Kesheni basi; kwa maana hamjui ni siku ipi atakayokuja Bwana wenu.”

Waliambiwa si kwamba tu walinde na kujitayarisha bali pia walinde kwa hamu. Warumi 8:19 (Habari Njema kwa Watu Wote) husema: “Viumbe vyote vinatazamia kwa hamu Mungu awadhihirishe watoto wake.” Asili ya binadamu ni kwamba tunapotumaini sana na kutamani jambo fulani na kulingoja kwa hamu, tunapata kishawishi chenye nguvu kuweza kuliona likitimia upesi hata wakati ithibati haitoshi. Katika hamu yetu maonyo bandia yaweza kutolewa.

Ni nini basi kitakachotofautisha onyo la kweli na yale ya bandia? Ili kupata jibu, tafadhali ona makala ifuatayo.

[Maelezo ya Chini]

a Wakiwa na hamu ya kuja kwa pili kwa Yesu, Mashahidi wa Yehova wamedokeza tarehe zilizogeuka kuwa zenye kosa. Kwa sababu hiyo, wengine wamewaita manabii bandia. Hata hivyo, katika pindi hizo, hawakudhubutu kutoa utabiri mbalimbali ‘katika jina la Yehova.’ Hawakusema kamwe, ‘Haya ni maneno ya Yehova.’ Mnara wa Mlinzi, jarida rasmi la Mashahidi wa Yehova, limesema: “Sisi hatuna kipawa cha kutoa unabii.” (Januari 1883, ukurasa 425 Kiingereza) “Wala maandishi yetu hayapaswi kuabudiwa wala kuonwa kuwa yasiyokosea.” (Desemba 15, 1896, ukurasa 306) Mnara wa Mlinzi limesema pia kwamba uhakika wa kwamba wengine wana roho ya Yehova “haumaanishi wale wanaotumikia wakiwa Mashahidi wa Yehova wamepuliziwa. Haumaanishi kwamba maandishi katika gazeti hili Mnara wa Mlinzi yamepuliziwa na hayawezi kukosea na hayana makosa.” (Mei 15, 1947, ukurasa 157) “Mnara wa Mlinzi halidai kuwa limepuliziwa kwa yale linayosema, wala si lisiloweza kupingwa.” (Agosti 15, 1950, ukurasa 263) “Akina ndugu wanaotayarisha vichapo hivyo wanakosea. Maandishi yao hayajapuliziwa kama yale ya Paulo na waandikaji wengine wa Biblia. (2 Tim. 3:16) Na hivyo, nyakati nyingine imekuwa lazima kusahihisha maoni, kadiri uelewevu ulivyoongezeka. (Mit. 4:18)”—Februari 15, 1981, ukurasa 19.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki