Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Uahirishaji Ile makala “Uahirishaji—Mwizi wa Wakati” (Aprili 8, 1995) iliandikwa katika njia ya kihalisi na yenye ucheshi. Nilipokuwa nikiisoma, nilijipata nikijicheka, kwa kuwa nimekuwa na zoea baya sana la kuahirisha.
F. B. H., Brazili
Nimekuwa mwahirishaji mbaya sana katika sehemu kubwa ya maisha yangu, kwa hiyo hii ilikuwa habari ya wakati ufaao kwangu. Iliandikwa vizuri, na napanga kutumia hiyo habari kunisaidia kupanga wakati wangu vyema zaidi. Mara nyingi nimekuwa nikitaka kuandika barua ya shukrani kwa makala tofauti-tofauti na sijapata wakati wa kufanya hivyo kamwe. Sasa hatimaye nimetimiza hilo!
M. H., Marekani
Nilikuwa nikipitia-pitia hilo gazeti nilipoona hiyo makala. Nilisoma utangulizi, nikifikiri kwamba ningesoma sehemu iliyobaki ya hiyo makala baadaye. Lakini maneno ya kufungua yalisema: “Ngoja kwanza! Usiache kusoma makala hii!” Natambua sasa kwamba nimejiruhusu kunyang’anywa wakati kwa sababu ya uahirishaji.
A. E., Italia
Mimi ni fundi wa nguo, na uahirishaji ulikuwa umekuwa njia ya maisha kwangu. Nilipuuza kuandika mambo ya kufanywa, kupangia wakati ufaao, na kupanga kwa ajili ya kukatizwa kwa shughuli. Lakini sasa nimejifunza kutumia madokezo yenu, na nafurahia thawabu.
S. N., Nigeria
Siku za Mwisho Nikiwa mweneza-evanjeli wa wakati wote, ningependa kuwashukuru kwa majarida yetu. Nilipokuwa nikisoma mfululizo wa makala kuu katika toleo la Aprili 22, 1995, “Je, Hizi Ndizo Siku za Mwisho?,” niliwaza, ‘Makala hizi ziko wazi, moja kwa moja, na zimewekwa picha kwa njia bora kama nini!’ Utaratibu wazo, picha nzuri mno, na maelezo ya picha kwa kweli yaliweka wazi mambo makuu na kufanya hizo makala kuwa rahisi kusoma na kufahamu. Ilikuwa furaha kutolea majirani wetu magazeti hayo!
J. B., Marekani
Malengelenge Nilisoma makala yenu “Malengelenge—Kukabiliana na Maumivu.” (Aprili 22, 1995) Siku tatu baadaye nilipatwa na vipele vya ngozi ambavyo vilifanana sana na ufafanuzi wa malengelenge katika makala yenu. Nilienda kwa daktari na kumwambia kwamba nilifikiri huenda nilikuwa na malengelenge. Na kwa hakika, yeye aliniambia kwamba nilikuwa mwenye ujuzi sana—uchunguzi wangu wa dalili za ugonjwa ulikuwa sahihi! Kwa kuwa huo ugonjwa uligunduliwa katika hatua ya mapema, yeye alisema kwamba singepatwa na maumivu mengi sana ambayo wagonjwa wengi wa malengelenge hupata. Asanteni kwa makala yenu!
K. B., Marekani
Matreshka Asanteni kwa makala “Matreshka—Ni Mwanasesere Alioje!” (Aprili 22, 1995) Nilipokuwa nikiisoma, nilifurahishwa na jinsi ilivyoandikwa. Picha ni zenye kuvutia! Nimekuwa nikivutiwa na mwanasesere huyu tangu nilipokuwa mdogo, lakini sikujua chochote kuhusu chanzo chake. Sasa nitalazimika kumsihi mtu aninunulie mmoja!
M. T., Italia
Utoaji-Mimba Makala “Vijana Huuliza . . . Je, Utoaji-Mimba—Ndio Suluhisho?” ilinasa uangalifu wangu. (Machi 8, 1995) Miaka 24 iliyopita, wakati nilishika mimba nilipokuwa na umri wa miaka 15, nilipatwa na hisia nyingi zilezile walizopata wasichana waliotajwa katika hiyo makala. Baba ya kitoto alinitia moyo nitoe mimba, lakini nikaamua kukizaa kitoto changu. Kasisi wangu alitaka nipeane mtoto wangu atunzwe na mtu mwingine. Sikukanyaga Kanisa Katoliki tena! Ingawa hivyo, wazazi wangu walikuwa wenye kutegemeza. Nilianza kufikiri kuhusu kumpa mtoto wangu ulezi imara wa kiroho. Mashahidi wa Yehova walipokuja nyumbani kwetu, nilikubali funzo la Biblia na baada ya muda mfupi nikabatizwa. Leo niko katika ndoa yenye furaha. Na mwana wangu? Anatumikia kwenye makao makuu ya Mashahidi wa Yehova. Nashikwa na hofu nifikiriapo kuhusu shauri la kwanza—utoaji-mimba. Huo si suluhisho!
G. J., Marekani