Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Utafutaji wa Mwenye Kuasilishwa Nataka kuwashukuru kwa ono “Mshangao Wenye Kusisimua.” (Februari 22, 1997) Ilichochea kwelikweli kusoma juu ya vile mwana huyu alivyompata mama yake mzazi na kutambua kwamba alikuwa dada yake wa kiroho pia!
M. G. D., Italia
Nilisoma simulizi la maisha ya Dana Folz kwa machozi. Nina ndugu aliyeasilishwa ambaye alipata kukutana na mama yake alipokuwa mtu mzima. Haukuwa muungano wenye kufurahisha. Hata leo, lazima ashughulike na hisia zisizofaa kuelekea familia yetu. Makala hiyo ilinisaidia kuona umaana wa kumwonyesha subira na upendo.
M. D. L., Argentina
Nilipata gazeti lenu ndani ya msala wa sehemu ya biashara ya hapa kwetu. Lilitia ndani mojawapo ya masimulizi yenye kusisimua zaidi ambayo nimewahi kusoma! Mara nyingi nimeulizwa: “Namna gani ikiwa mtoto alichukuliwa mimba wakati wa kubakwa? Hampendelei kutoa mimba chini ya hali kama hizi?” Hakuna ombi zaidi lenye kushawishi kwa ajili ya uhai wa wasiozaliwa lingaliweza kutolewa kuliko simulizi la maisha halisi lenye kusisimua la Dana Folz.
M. P., Marekani
Uhalifu Uliopangwa Mimi ni mshauri wa usalama na mshiriki wa Halmashauri ya Uhusiano Kati ya Polisi na Jumuiya. Nilipata madokezo yenu juu ya namna uwezavyo kulinda familia yako kutokana na uhalifu yakiwa yenye kutumika na yenye mafaa. (“Uhalifu Uliopangwa—Jinsi Unavyokuathiri,” katika toleo la Machi 8, 1997) Tayari nimezungusha gazeti hilo kwa washiriki wengine wa halmashauri. Inaburudisha kufahamu kwamba siku moja ulimwengu usio na uhalifu utapatikana.
C. E. J. A., Nigeria
Makala hizo zilikuwa zenye msaada hasa kwa sababu nimekuwa nikijifunza Biblia na mtu ambaye amehusika na uhalifu uliopangwa kwa miaka 11 iliyopita. Magumu ya kukata kabisa vifungo pamoja na uhalifu uliopangwa yalielezwa kwa usahihi. Kwa msaada wa Yehova, yeye pia aweza kujitoa akiamua kufanya hivyo.
A. M., Marekani
Maua Nina umri wa miaka kumi, na ninataka kuwashukuru kwa ajili ya makala “Maua Huonyesha Kwamba Mtu Fulani Anajali.” (Machi 8, 1997) Ilinifunza namna ya kutunza maua ili yadumu muda mrefu zaidi.
L. C., Italia
Kwa miaka mingi nimekuwa nikitaka kujua namna ya kutunza vizuri maua, kwa maana nayapenda mno. Hata hivyo, sikuzote yangenyauka upesi sana. Madokezo katika Amkeni! kwa kweli yamenisaidia. Nashukuru sana kwa kazi mnayofanya.
J. P., Mexico
Kuzaliwa kwa Nyota Ile makala “Kuzaliwa kwa Nyota Katika ‘Kiota’ cha Tai” (Machi 8, 1997) ilinifanya nitue na kufikiri kwa uzito kwa muda mfupi juu ya uumbaji mzuri na usioharibiwa wa Yehova Mungu. Nilichochewa sana.
J. A., Australia
Uasilishaji Kwa kweli naweza kujihusianisha na ile makala “Ombi Kutoka Moyoni.” (Machi 8, 1997) Nilikuwa mama asiyeolewa nilipokuwa na umri wa miaka 19. Mama yangu alikuwa mwenye hasira na mkali, akinijulisha kabisa kwamba hakumtaka mtoto huyo. Nilihisi kwamba ingekuwa masilahi bora ya mtoto wangu kuacha mtu mwingine amwasilishe. Baada ya kuwa Mkristo, nilisali kwa miaka 15 kwamba ningalikutana naye. Hatimaye sala yangu ilijibiwa muda fulani uliopita, na niliweza kukutana naye na kushiriki habari njema pamoja naye. Alikuwa mwenye kuelewa hali zilizonisukuma nimtoe aasilishwe. Shauri langu kwa akina mama walio katika hali hii ni kwamba waendelee kusali kwa Yehova. Huenda ikatukia kwamba utaweza kuungana tena na mtoto wako. Ikiwa sivyo, Mungu aweza kukupatia amani ya akili na moyo iwapo unamwitibari kabisa.
G. S., Marekani