Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Hangaiko la Habari Nilisoma mfululizo wa makala “Hangaiko la Habari—Lakuathirije?” (Januari 8, 1998) Mnasema kwamba kwa sehemu takataka za habari zaweza kuwa zikichangiwa na ongezeko la habari na magazeti. Nahisi kwamba gazeti lenu laweza kuwa likichangia takataka hizi. Je, huu si uchambuzi usio haki, kwa kuwa gazeti lenu lina hatia ileile ya takataka za habari?
J. K., Marekani
Mfululizo wetu wa makala ulifunua takataka za habari “zisizofaa.” Kwa hakika “Amkeni!” halijachangia katika jambo hili, kwa kuwa kusudi lake kama lilivyotaarifiwa ni ‘kuchunguza sana matukio ya sasa na kutoa maana ya kweli ya matukio hayo.’ Habari ya namna hiyo haiwezi kamwe kuwa isiyofaa.—Mhariri.
Maria na Kristo Aliyefufuliwa Nawaandikia ili kulalamika kuhusu makala katika “Kuutazama Ulimwengu,” yaani, “Je, Maria Alikuwa Mtu wa Kwanza Kumwona Kristo Aliyefufuliwa?” (Januari 8, 1998) Mnadhihirisha kwamba hamjui Maandiko, jambo ambalo pia ladokeza kwamba hampendezwi na kweli. Kuna mambo mengi yaliyotukia na yaliyosemwa ambayo hayatiwi ndani ya Biblia. Someni Yohana 21:25.
J. G., Marekani
Makala yetu ilikuwa ikiripoti tu yaliyosemwa katika gazeti rasmi la habari la Vatikani “L’Osservatore Romano.” Papa John Paul wa Pili alinukuliwa hapo akidai kwamba Maria “huenda ikawa alikuwa ndiye mtu wa kwanza kutokewa na Yesu aliyefufuliwa.” Ingawa tunaheshimu itikadi ambazo wasomaji wetu huenda wakawa nazo, kwa wazi hakuna uthibitisho wowote wa Kibiblia kwa dai hilo.—Mhariri.
Wale Watunga-Mashairi wa Zamani Ile makala “Wale Watunga-Mashairi wa Zamani—Si Waimbaji Tu wa Nyimbo za Mapenzi” (Februari 8, 1998) ilikuwa mchanganuo stadi wa fungu lililotimizwa na hawa waimbaji-watunga-mashairi katika jamii ya enzi za kati. Nikiwa mwalimu wa fasihi, nimejifunza juu ya watunga-mashairi Wareno, na makala yenu ilinisaidia kuelewa kikamili harakati hii. Makala zilizo bora namna hii hulipa gazeti lenu ustahifu.
R. N. A., Brazili
Nakiri kwamba ilihitaji jitihada kuanza kusoma makala hii, lakini mara nilipoianza, ilivutia upendezi wangu mara moja. Hasa, nilifurahi kujua ni nani ambaye labda alianzisha ile desturi ya “kutanguliza wanawake.” Japani haina ile desturi ya “kutanguliza wanawake,” lakini mume wangu, aliyelelewa akiwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova tangu wakati alipokuwa mchanga, amefuata desturi hiyo bila kuacha tangu tulipochumbiana. (Sasa tumeoana kwa muda wa miaka mitano.) Ninafurahi sana.
Y. N., Japani
Upatanisho wa Mama na Mtoto Niliguswa moyo sana na makala “Upatanisho wa Kipekee.” (Februari 22, 1998) Kujua uzao wangu kuliniathiri sana kihisia-moyo. Mama yangu na baba yangu hawakufunga ndoa kamwe. Mara nyingi ningeulizia kuhusu baba yangu, lakini nilijibiwa kwa ufupi sana. Majuzi nilimwuliza mama yangu jina kamili la baba yangu. Kwa kutumia kitabu kinachoorodhesha nambari za simu, niliweza kumpata dada yake, na nilishangaa kufahamu kwamba huyo dada yake ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova! Alinieleza kwamba baba yangu alikufa mwaka wa 1980, bila kufunga ndoa kamwe. Ijapokuwa hivyo, mama yangu na shangazi yangu, wamekuwa kitia-moyo kwelikweli katika wakati wa uhitaji. Pia makala zenu zimenisaidia sana kupona.
L. D., Marekani