Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • wi kur. 3-11
  • Biblia—Je! Imepuliziwa na Mungu?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Biblia—Je! Imepuliziwa na Mungu?
  • Je! Ulimwengu Usio na Vita Utakuwako Wakati Wowote?
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Je! Kuna Uthibitisho wa Kupuliziwa?
  • Je! Biblia Imejaa Mambo Yenye Kupingana?
  • Ieleweke na Wasomi Tu?
  • Je! Kuna Msingi Wowote wa Kibiblia kwa Torati ya Mdomo?
  • Sheria ya Mdomo—Kwa Nini Iliandikwa?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Dini ya Kiyahudi—Jitihada ya Kutafuta Mungu Kupitia Andiko na Pokeo
    Jitihada ya Ainabinadamu ya Kutafuta Mungu
  • Unabii Mwingi Uliotimizwa
    Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu?
  • Torati Ni Nini?
    Maswali ya Biblia Yajibiwa
Pata Habari Zaidi
Je! Ulimwengu Usio na Vita Utakuwako Wakati Wowote?
wi kur. 3-11

Biblia—Je! Imepuliziwa na Mungu?

1, 2. Kwa nini wengi huistahi Biblia, na waandikaji wayo hutoa dai gani?

THE New Encyclopædia Britannica huita Biblia “labda [ndiyo] mkusanyo wa vitabu wenye uvutano zaidi katika historia ya kibinadamu.” Biblia inaheshimiwa sana na wengi kwa sababu ya kuwa ya kale sana—sehemu zayo zikiwa ziliandikwa miaka 3,500 iliyopita. Hata hivyo, shauri layo lenye kutumika, lenye kupatana na hali za kisasa ni sababu moja kwamba zaidi ya nakala bilioni tatu zimegawanywa na kwamba imetafsiriwa, ikiwa kamili au kwa sehemu, katika karibu lugha elfu mbili, hiyo ikiifanya kuwa kitabu chenye kuuzwa zaidi ulimwenguni kwa wakati wote.

2 Kando na mambo hayo ya hakika, yote ambayo hufanya Biblia istahiwe, bado kuna jambo jingine ambalo limeifanya kuwa yenye uvutano na yenye kuvutia muda wote wa enzi zilizopita—dai layo la kuwa ufunuo uliopuliziwa na Mungu Mweza Yote. Musa, aliyekusanya pamoja ile Torati (vile vitabu vitano vya kwanza vya Biblia) ‘aliandika’ yote ambayo Mungu alimwambia aandike, yaliyotia ndani masimulizi ya uumbaji, maandishi ya Furiko la siku ya Noa, na historia ya Abrahamu na shughuli za Musa mwenyewe pamoja na Mungu. (Kutoka 24:3, 4) Mfalme Daudi alisema: “Roho ya BWANA imenena kupitia mimi, ujumbe wake u juu ya ulimi wangu.” (2 Samweli 23:2) Waandikaji wengine wa Biblia walitoa dai ilo hilo la kuwa na mwongozo wa kimungu. Maandishi hayo yote pamoja hufanyiza maelezo ya Mungu mwenyewe ya historia—maana yayo ya kweli, ufasiri wayo, na tokeo layo la mwisho. Wale waandikaji wengi mbalimbali wa Maandiko—wafalme, vibarua wa kuajiriwa, makuhani, na wengine—wote walikuwa wakitenda wakiwa waandishi katika kuandika mawazo ya Mungu, yule Mtungaji wa Biblia na Mhakikishaji wa ahadi zayo.

3. Ni jambo gani huonyesha kwamba imani katika Mungu na imani katika sayansi hupatana?

3 Kwa kuwa Biblia hudai kuwa na mtungaji wa kimungu, labda swali la kwanza kabisa kwa wengi huhusiana na kuwako kwenyewe kwa Mtungaji wayo. Wengi hukataa kabisa kuwako kwa Mungu. Wengine, wakidhani kuwa watu wote wenye akili wamekataa wazo la kuwako kwa Mungu na imani katika Biblia, huuliza: “Kwa nini wanasayansi hawaamini katika Mungu?” Je! kweli wazo hilo ni la kweli? Makala moja katika gazeti New Scientist ilisema kwamba “maoni ambayo kwa kawaida hutarajia wanasayansi kuwa si waamini . . . ni maoni yenye kosa kabisa.”2 Makala iyo hiyo iliripoti kwamba chunguzi za vivi hivi katika vyuo vikuu, taasisi za utafiti, na maabara za viwanda huonyesha kwamba “wengi kama wanane kwa kila wanasayansi 10 hufuata imani ya kidini au hukubali kanuni ‘zisizo za kisayansi.’” Hivyo si sahihi kusema kwamba imani haipatani na sayansi au wanasayansi. (Mageuzi—Je! ni Uhakika?”))

MAGEUZI​—JE! NI UHAKIKA?

SIMULIZI la Mwanzo la uumbaji hutaarifu kwamba vitu vyote vilivyo hai viliumbwa ‘kwa aina zake,’ au vikundi vya msingi. (Mwanzo 1:12, 24, 25) Katika kuendeleza nadharia yao, wanamageuzi wengi wamedhihaki simulizi la Biblia. Lakini je, kuna uthibitisho wowote kwamba aina mpya ya kiumbe imetokea wakati wowote kwa sababu ya kuzalishana kati ya viumbe tofauti au migeuko papale?e Tokea yale maandishi ya mapema zaidi hadi leo, mbwa wangali mbwa, na paka huendelea kuwa paka. Hata mende, ambao huonekana miongoni mwa masalio ya mapema zaidi ya wadudu, kwa kweli wafanana kabisa na wale wa kisasa.

Kweli kweli, ni uthibitisho gani ambao umetokezwa na jumuiya ya wanasayansi kwa muda upitao miaka mia moja ya uchunguzi wa bidii nyingi tangu kitabu cha Darwin Origin of Species?f Baadhi ya wastadi wamefikia mikataa gani?

REKODI YA VISUKUKU: Ushuhuda wa visukuku huitwa na baadhi ya watu ‘mahakama ya mwisho ya rufani’ kwa sababu ndiyo historia ya kweli pekee ya uhai ipatikanayo kwa sayansi. Hiyo huonyesha nini?

Profesa wa sayansi kiasili John Moore aliripoti juu ya matokeo ya uchunguzi mwingi uliofanywa na Geological Society of London na Palaeontological Association of England. “Wanasayansi wapatao 120, wote wakiwa wataalamu, walitayarisha sura 30 katika kitabu chenye kutokeza cha kurasa zaidi ya 800 ili kutoa rekodi ya visukuku ya mimea na wanyama . . . Kila namna au aina kubwa ya mmea na mnyama huonyeshwa kuwa na historia iliyojitenga na iliyo tofauti na namna au aina zile nyingine zote! Vikundi vya mimea na wanyama pia hutokea ghafula katika rekodi ya visukuku. . . . Hakuna dalili ya mzazi mmoja wa kale, sembuse uhusiano na mtambaazi yeyote, yule adhaniwaye kuwa mzazi.”—Should Evolution Be Taught?, 1970, kurasa 9, 14.

JE! MIGEUKO PAPALE INGEWEZA KUWA ILISABABISHA MAGEUZI? Kwa sababu ya hali yenye kudhuru ya migeuko papale, The Encyclopedia Americana hukubali hivi: “Uhakika wa kwamba migeuko papale iliyo mingi ni yenye kudhuru kiumbe unaoonekana kuwa haupatani na yale maoni ya kwamba migeuko papale ndiyo chanzo cha mali ghafi ya mageuzi. Ndiyo, mutanti zinazoonyeshwa kwa vielezi katika vitabu vya mafundisho ya biolojia ni mkusanyo wa vitu visivyo vya kawaida na vidubwana na mgeuko papale waonekana kuwa wenye kuleta uharibifu badala ya kuwa njia yenye ujenzi.”—1977, Buku la 10, ukurasa 742.

NAMNA GANI NYANI-WATU? Science Digest ilitaarifu hivi: “Uhakika wenye kutokeza ni kwamba uthibitisho wote tulio nao wenye kuonekana wa mageuzi ya kibinadamu bado waweza kutiwa katika jeneza moja, na nafasi ibaki! . . . Mathalani, yaonekana kuwa nyani wa kisasa walitokea bila kujulikana walikotoka. Hawana wakati uliopita, hawana rekodi ya visukuku. Na asili ya kweli ya wanadamu wa kisasa—watu walio wima, walio uchi, wenye kuunda zana, wenye ubongo mkubwa—ikiwa tutajiambia kweli, ni jambo la kifumbo jinsi iyo hiyo.”—Mei 1982, ukurasa 44.

NADHARIA ILIYO KATIKA HATARI: Angalia maelezo yafuatayo ya Michael Denton, mwanabiolojia wa molekyuli, kama yalivyonukuliwa kutoka kitabu chake Evolution: A Theory in Crisis:

“Hapawezi kuwa na shaka kwamba Darwin hakuwa na kitu kama uthibitisho wa kutosha wa kuanzisha nadharia yake ya mageuzi. . . . Nadharia yake ya ujumla, kwamba uhai wote duniani ulikuwa umeanza na ukawa umegeuka-geuka kwa mrundamano wenye kufuatana wa hatua kwa hatua wa migeuko papale yenye kutukia kinasibu, ingali, kama ilivyokuwa katika wakati wa Darwin, nadhariatete yenye kukisiwa sana bila utegemezo hakika kabisa wa moja kwa moja na iliyo mbali sana na ukweli wenye kujidhihirisha ambao baadhi ya wateteaji wayo wenye nguvu zaidi wangetaka tuamini. . . . Mtu angetarajia kwamba nadharia ya umaana mkubwa sana hivyo, nadharia ambayo kihalisi ilibadili ulimwengu, ingalikuwa jambo lililo la halisi kabisa, jambo lililo zaidi ya ngano.”—Chapa ya 1986, kurasa 69, 77, 358.

e Tofauti yapasa kufanywa kati ya kile ambacho kimeitwa “mageuzi madogo,” au usitawi wenye kuendelea, kujipatanisha na hali, na mabadiliko ndani ya aina, na “mageuzi makubwa,” ambayo hufundisha kwamba aina moja hugeuka kuwa nyingine. Wale wafundishao mageuzi kwa kawaida hurejezea wazo hilo la pili.

f Kwa mazungumzo marefu, ona Maswali Matano Muhimu Kuhusu Chanzo cha Uhai.

Je! Kuna Uthibitisho wa Kupuliziwa?

4. Ni kweli zipi za kisayansi zilizotajwa maelfu ya miaka iliyopita katika Biblia?

4 Mtu afikiapo mkataa kwamba kuna uthibitisho wenye kusadikisha wa kuwako kwa Muumba, bado swali labaki kama amewapulizia watu waandike mawazo na makusudi yake katika Biblia. Kuna sababu nyingi kwa nini sisi twaweza kuwa na hakika kwamba ndivyo ilivyo, mojawapo ikiwa usahihi wayo wa kisayansi. (Ona kisanduku, “‘Katika Mwanzo Mungu Aliumba’ . . .” ukurasa 6.) Kwa mfano, zaidi ya miaka 3,000 iliyopita, Ayubu alisema kwamba Mungu “huining’iniza dunia pasipo kitu.” (Ayubu 26:7, JP) Miaka 2,700 hivi iliyopita, nabii Isaya alitaarifu kwamba Mungu “hukaa juu ya duara ya dunia.” (Isaya 40:22, JP) Sasa, Ayubu au Isaya wangeweza kujuaje kweli hizo za msingi za kisayansi kwamba dunia imeangikwa katika anga na ni duara? Zaweza kuwa zinajulikana vema leo, lakini taarifa hizo zilitolewa wakati ambapo mawazo kama hayo yalikuwa hayajasikika. Je! ufunuo wa kimungu silo elezo lenye kupatana na akili zaidi?

“KATIKA MWANZO MUNGU ALIUMBA” . . .

. . . “MBINGU NA DUNIA.” (Mwanzo 1:1, JP)—Wanasayansi walio wengi leo huafikiana kwamba ulimwengu wote mzima ulikuwa na mwanzo. Mwastronomia Robert Jastrow aliandika hivi: “Sasa tunaona jinsi uthibitisho wa elimu ya anga na nyota unavyoongoza kwenye maoni ya kibiblia juu ya mwanzo wa ulimwengu. Mambo madogomadogo yanatofautiana, lakini mambo ya maana katika masimulizi ya elimu ya anga na nyota na ya Biblia ya Mwanzo ni mamoja: mfululizo wa matukio wenye kuongoza kwa binadamu ulianza ghafula na mara moja katika pindi mahususi ya wakati, katika mmeremeto wa nuru na nishati.”—God and the Astronomers, 1978, ukurasa 14.

. . . “VIUMBE HAI.” (Mwanzo 1:20)—Mwanafizikia H. S. Lipson, akijua haielekei kuwa uhai ulijitokeza wenyewe, alisema hivi: “Elezo pekee linalokubalika ni uumbaji. Mimi najua kwamba jambo hili ni chukizo kabisa kwa wanafizikia, kama lilivyo kwangu mimi, lakini haitupasi kamwe kukataa nadharia tusiyopenda ikiwa uthibitisho wa majaribio unaiunga mkono.”—Physics Bulletin, Buku la 31, 1980, ukurasa 138.

Hata kama haielekei hivyo, je, uhai wa kujitokeza wenyewe haungaliweza kutukia hata hivyo? Mwanafizikia aliye pia Mwastronomia Fred Hoyle, asema hivi: “Hakuna uthibitisho hakika hata kidogo kuunga mkono nadhariatete ya kwamba uhai ulianza katika mchuzi wa mchanganyiko wa kaboni hapa juu ya Dunia.” Pia ataarifu hivi: “Kadiri wanabiokemia wagunduavyo mambo mengi zaidi na zaidi juu ya utata mwingi mno wa uhai, inakuwa wazi kwamba uwezekano wao kuanza kwa aksidenti ni mdogo mno hivi kwamba wazo hilo halistahili kufikiriwa. Uhai usingaliweza kutokea kwa bahati.” Hoyle aongeza: “Wanabiolojia hupendelea mawazio yasiyothibitishwa ili wakatae lililo dhahiri sana, kwamba ule utendaji mfululizo wa amino asidi 200,000, uliotokeza uhai, haukutokea kwa bahati.” Kwa kweli, yeye huuliza, ‘Kuunganishwa kwa kemikali kiaksidenti pekee katika tope la mchanganyiko wa kaboni kungewezaje hasa kutokeza vimeng’enya 2,000 vilivyo muhimu kwa uhai?’ Yeye asema uwezekano ni moja katika 1040,000, au “kama ule uwezekano wa kurusha mfululizo usiokatizwa wa sita mara 50,000 kwa dadu zilizo sawasawa!” (The Intelligent Universe, F. Hoyle, 1983, kurasa 11-12, 17, 23) Aongeza, “Ikiwa mtu haathiriwi ama na imani za kijamii ama na mazoezi ya kisayansi asadiki kwamba uhai ulijitokeza [wenyewe] juu ya Dunia, hesabu hiyo rahisi hufanya wazo hilo lisistahili kufikiriwa hata kidogo.”—Evolution From Space, Fred Hoyle na Chandra Wickramasinghe, 1981, ukurasa 24.

5, 6. Ni utimizo gani mbalimbali wa unabii ambao hutoa uthibitisho kwamba waandikaji wa Biblia walipuliziwa na Mungu?

5 Unabii, kwa kweli historia iliyoandikwa kabla haijatukia, labda ndio sehemu kuu ya Biblia ambayo hutegemeza dai layo la kupuliziwa kimungu. Kwa mfano, nabii Isaya alitabiri si kwamba tu Yerusalemu lingeangamizwa na Babuloni na kwamba taifa zima la Kiyahudi lingechukuliwa mateka bali pia kwamba baada ya wakati fulani jenerali Mwajemi Koreshi angeshinda Babuloni na kukomboa Wayahudi kutoka utekwa. (Isaya 13:17-19; 44:27–45:1) Je! wewe waweza kufikiria njia yoyote, isipokuwa kupuliziwa kimungu, ambayo kwayo, Isaya angeweza kutabiri kwa mafanikio uzaliwa wa Koreshi, jina lake, na yale ambayo angefanya hasa miaka 200 mbeleni? (Ona kisanduku, Mungu—‘Mfunua Mafumbo’ Kupitia Unabii.”))

MUNGU—‘MFUNUA MAFUMBO’ KUPITIA UNABII

ALIPOKUWA akisema na mfalme wa kale, nabii Danieli alisema hivi: “Fumbo ambalo mfalme ameulizia habari zake—watu wenye hekima, wapungaji pepo, wafanya mizungu, na waaguzi hawawezi kumwambia mfalme. Lakini kuna Mungu katika mbingu afunuaye mafumbo.” (Danieli 2:27, 28) Je! kuna uthibitisho kwamba kwa kweli Mungu ni Mfunua mafumbo kupitia unabii? Ifuatayo ni baadhi ya mifano.

Kuanguka kwa Babuloni: “BWANA akasema hivi kwa Koreshi, mpakwa-mafuta Wake—ambaye ameshika mkono wake wa kulia, akikanyagia chini mataifa mbele yake, akifungua mishipi viunoni mwa wafalme, akifungua milango mbele yake naye asiruhusu lango likae limefungwa.”—Isaya 45:1; unabii uliotolewa wapata 732 K.W.K. Ona pia Yeremia 50:35-38; 51:30-32, unabii uliotolewa kabla ya 625 K.W.K.

Utimizo—539 K.W.K.: Wanahistoria Herodoto na Zenafani husimulia kwamba Koreshi Mwajemi aligeuza maji ya Frati, yaliyopita katikati ya Babuloni, akayatuma majeshi yake kupitia katikati ya mto, wakipata walinzi Wababuloni ambao hawakutarajia chochote na kutwaa jiji hilo katika usiku mmoja. Hata kwa mbinu hiyo, Koreshi hangaliweza kuingia jiji kama malango kwenye kingo za Frati yaliyoingia jijini hayakuwa yameachwa wazi kizembe. ‘Malango hayakukaa yamefungwa,’ kama vile unabii ulivyotabiri.

Mwisho wa Tiro: “Bwana MUNGU akasema hivi: Mimi nitakuchukulia hatua wewe, Ee Tiro! Nitavurumisha mataifa mengi dhidi yako, kama vile bahari huvurumisha mawimbi yake. . . . Nami nitakwangua udongo wake kutoka kwake na kumwacha akiwa mwamba mtupu. . . . Nao watatupa ndani ya maji mawe yako na mbao na udongo.”—Ezekieli 26:3, 4, 12, unabii uliotolewa wapata 613 K.W.K.

Utimizo—332 K.W.K.: Aleksanda Mkuu alijenga daraja la ardhi, au chungu ya udongo, toka bara kwenda kisehemu cha kisiwa cha Tiro (kilometa 0.8 toka ufuoni) ili majeshi yake yaweze kupiga miguu kuvuka na kushambulia jiji la kisiwani. The Encyclopedia Americana huripoti hivi: “Kwa kutumia vifusu vya kisehemu cha bara cha jiji, ambacho alikuwa amebomoa, alijenga chungu kubwa ya udongo katika 332 ili kuunganisha kisiwa na bara.” Baada ya mazingiwa mafupi kwa kulinganisha, jiji la kisiwani liliangamizwa, na unabii wa Ezekieli ukatimizwa katika mambo yao yote hata yale madogomadogo. Hata ‘mawe na mbao na mavumbi’ ya Tiro la kale (sehemu ya bara ya jiji) ‘yaliwekwa katikati hasa ya maji.’

Kuharibiwa kwa Yerusalemu: “Ndipo Isaya akamwambia Hezekia, ‘Sikia neno la BWANA wa Majeshi: Wakati waja ambao kila kitu katika kao lako la kifalme, ambacho babu zako wa kale wamejiwekea hadi leo hii, kitachukuliwa kupelekwa Babuloni; hakuna kitu kitakachoachwa nyuma.’”—Isaya 39:5, 6, unabii uliotolewa wapata 732 K.W.K.; ona pia Isaya 24:1-3; 47:6.

Yule Yeremia nabii alipiga mbiu hivi: “Mimi . . . nitawaleta [Wababuloni] dhidi ya nchi hii na wakazi wayo . . . Nchi hii yote itakuwa magofu yaliyoachwa ukiwa. Na mataifa hayo yatatumikia mfalme wa Babuloni miaka sabini.”—Yeremia 25:9, 11, unabii uliotolewa kabla ya 625 K.W.K.

Utimizo—607 K.W.K. (586 K.W.K. kulingana na kronolojia za kilimwengu zilizo nyingi): Babuloni iliangamiza Yerusalemu baada ya mazingiwa ya mwaka mmoja na nusu. Jiji na hekalu viliteketezwa, na Wayahudi wenyewe wakachukuliwa kupelekwa Babuloni. (2 Mambo ya Nyakati 36:6, 7, 12, 13, 17-21) Taifa zima lilikaa utekwani kwa miaka 70, kama vile Yeremia alivyokuwa ametabiri. Kuachiliwa kwao kimuujiza katika 537 K.W.K. na Koreshi Mkuu, aliyeshinda Babuloni, kulitimiza unabii wa Isaya, uliokuwa umemtaja kwa jina. (Isaya 44:24-28) Nabii Danieli, akiwa utekwani katika Babuloni, alihesabu wakati barabara wa kuachiliwa kwa watu wake, akitegemeza uamuzi wake juu ya unabii wa Yeremia.—Danieli 9:1, 2.

6 Baadhi ya unabii mbalimbali wenye kutokeza sana umerekodiwa na Danieli, nabii aliyeishi katika karne ya sita K.W.K. Si kwamba tu alitabiri kuangushwa kwa Babuloni na Wamedi na Waajemi bali pia alitabiri matukio ambayo yangetukia baada ya wakati wake, katika wakati ujao uliokuwa mbali sana. Kwa mfano, unabii wa Danieli ulitabiri kuinuka kwa Ugiriki ikiwa milki ya ulimwengu chini ya Aleksanda Mkuu (336-323 K.W.K.), kugawanywa kwa milki ya Aleksanda miongoni mwa majenerali wake wanne baada ya kifo chake kisichotazamiwa, na kuinuka kwa Milki ya Roma, pamoja na nguvu zake za kijeshi zenye kutisha (karne ya kwanza K.W.K.). (Danieli 7:6; 8:21, 22) Matukio hayo yote sasa ni mambo ya hakika yasiyokanushika ya historia.

7, 8. (a) Baadhi ya watu wametoa shtaka gani dhidi ya unabii mbalimbali wa Biblia? (b) Ni nini huthibitisha kwamba shtaka la udanganyifu halina msingi mzuri?

7 Kwa sababu unabii mbalimbali wa Biblia umetimizwa kwa usahihi sana, wachambuzi wameuita kwa dharau madanganyo, yaani, historia iliyoandikwa baada ya kutukia na kufanywa kwa ubandia kuwa unabii. Lakini mtu angewezaje kwa njia yenye akili kushikilia kwamba makuhani wa Kiyahudi wangejasiria kubuni unabii? Na kwa nini wabuni unabii mbalimbali wenye kuwachambua vibaya sana iwazikavyo? (Isaya 56:10, 11; Yeremia 8:10; Sefania 3:4) Kwa kuongezea, taifa zima lenye kujua kusoma na kuandika, lililozoezwa na kuelimishwa kwa kutumia Biblia ikiwa maandishi yalo matakatifu, lingewezaje kudanganywa kwa danganyo kama hilo?—Kumbukumbu la Torati 6:4-9.

8 Kungewezaje kuwa na udanganyifu wowote kuhusiana na kutoweka kwa staarabu nzima-nzima, kama vile Edomu na Babuloni, hali matukio hayo yalitukia karne nyingi baada ya kukamilishwa kwa Maandiko ya Kiebrania? (Isaya 13:20-22; Yeremia 49:17, 18) Hata kama mtu ashikilia kwamba unabii huo mbalimbali uliandikwa baada ya pindi ya wakati wa manabii wenyewe, bado ulirekodiwa kabla ya karne ya tatu K.W.K., kwa kuwa kufikia wakati huo ulikuwa tayari ukitafsiriwa katika Kigiriki katika Septuagint. Pia, Hati-kunjo za Bahari ya Chumvi (ambazo hutia ndani sehemu za vitabu vyote vya kiunabii) ni zenye tarehe ya karne ya pili na ya kwanza K.W.K. Kama ilivyoonyeshwa, unabii mwingi mbalimbali ulitimizwa baada tu ya tarehe hizo.

Je! Biblia Imejaa Mambo Yenye Kupingana?

9-12. (a) Kwa nini baadhi ya watu husema kwamba Biblia hujipinga yenyewe? (b) Baadhi ya “mambo yenye kujipinga” hutatuliwaje?

9 Lakini baadhi ya watu hupinga: ‘Biblia imejaa mambo yenye kupingana na yenye kuhitilafiana.’ Mara nyingi sana, wale ambao hushikilia hayo hawajajichunguzia wao wenyewe jambo hilo bali wamesikia tu kutoka kwa wengine mfano mmoja au miwili inayodaiwa kuwamo. Kwa kweli yale yanayodhaniwa mara nyingi kuwa mambo yenye kuhitilafiana yanatatuliwa kwa urahisi ikikumbukwa kwamba waandikaji wa Biblia mara nyingi walisema habari yao kwa maneno machache. Mfano wa jambo hilo unapatikana katika masimulizi ya uumbaji. Katika kulinganisha Mwanzo 1:1, 3 na Mwanzo 1:14-16, wengi wameuliza jinsi inavyoweza kuwa kwamba Mungu ‘alifanya’ vile vimulikaji katika siku ya nne ya uumbaji hali nuru—kwa wazi kutoka kwa vimulikaji vivyo hivyo—ilikuwa ikifikia dunia katika siku ya kwanza ya uumbaji. Katika kisa hiki mwandikaji Mwebrania aliondoa uhitaji wa maelezo marefu kwa uteuzi wa uangalifu wa maneno. Angalia kwamba mistari 14-16 husema juu ya “kufanya” tofauti na “kuumba” katika Mwanzo 1:1, na “mianga [vimulikaji]” tofauti na “nuru” katika Mwanzo 1:3. Hiyo yaonyesha kwamba katika siku ya nne ya uumbaji ndipo jua na mwezi, ambazo tayari zilikuwako, zilipopata kuonekana waziwazi kupitia anga zito la dunia.a

10 Orodha za nasaba pia zimetokeza mvurugo. Kwa mfano, Ezra huorodhesha majina 23 katika nasaba yake ya kikuhani kwenye 1 Mambo ya Nyakati 5:29-40 (6:3-14, UV) lakini yeye huorodhesha majina 16 tu kwa kipindi icho hicho wakati wa kutoa nasaba yake mwenyewe kwenye Ezra 7:1-5. Hiyo, si hitilafu, bali ni kufupiza tu. Kuongezea, kulingana na kusudi la mwandikaji katika kurekodi tukio, yeye alikazia, akapunguza, akaongezea, au akaacha mambo mengi ambayo mwandikaji mwingine wa Biblia aliyasema kwa njia tofauti katika kurekodi tukio lile lile. Hayo si mambo yenye kupingana, bali ni masimulizi tofauti tu yakionyesha njia ya mwandikaji ya kuona mambo na watu waliokusudiwa.b

11 Mara nyingi, kule kunakoonekana kuwa kutopatana kwaweza kutatuliwa kwa kuchunguza habari muktadha. Kwa mfano, “Kaini alipata wapi mke wake?” ni swali ambalo husikiwa mara nyingi, kukazia imani kwamba hiyo hufunua hitilafu katika masimulizi ya Biblia. Dhana ni kwamba Adamu na Hawa walikuwa na wana wawili tu, Kaini na Abeli. Gumu hilo linatatuliwa kwa urahisi ikiwa mtu anaendelea kusoma. Mwanzo 5:4 husema: “Baada ya kuzaliwa kwa Sethi, Adamu aliishi miaka 800 na kuzaa wana na mabinti.” Hivyo Kaini alioa mmoja wa dada zake au labda mpwa wake wa kike, jambo ambalo lingalipatana kabisa na kusudi la Mungu la awali la kuzidisha jamii ya kibinadamu.—Mwanzo 1:28.

12 Kwa wazi kuna mambo mengi ya historia ya kibinadamu yasiyoandikwa kuwa Rekodi ya Kimungu. Lakini kila jambo lililohitajiwa, kwa wale walioisoma kwanza na kwetu sisi leo pia, limetiwa ndani bila kuifanya iwe nyingi mno na isiyoweza kusomeka.

Ieleweke na Wasomi Tu?

13-15. (a) Ni kwa nini baadhi ya watu huamini kwamba Biblia ni ngumu mno kwetu kuweza kuielewa? (b) Sisi twajuaje kwamba Mungu alikusudia Neno lake lieleweke?

13 Je! umepata kuuliza: “Kwa nini kuna fasiri nyingi sana za Biblia zenye kuhitilafiana?” Baada ya kusikiliza wajuzi wa kidini wakipingana, baadhi ya watu wenye mioyo myeupe huvurugika na kuvunjika moyo. Mkataa ambao wengi hufikia ni kwamba Biblia haieleweki nayo hujipinga. Kama tokeo, wengi huikataa Biblia kabisa, wakiamini kwamba ni ngumu sana kuweza kusomeka na kueleweka. Wengine, wakabiliwapo na fasiri hizo nyingi sana tofauti-tofauti za kidini, hawataki kuchunguza Maandiko kwa uzito. Baadhi yao husema: “Watu wenye elimu wamejifunza kwa miaka mingi katika seminari za kidini. Ningewezaje kuwa na msingi wa kutilia shaka yale wanayofundisha?” Lakini je, hivyo ndivyo Mungu huona mambo?

14 Wakati Mungu alipolipa taifa la Israeli Sheria, yeye hakuonyesha kwamba alikuwa akiwapa mfumo wa ibada ambao hawangeweza kuelewa, ambao ingekuwa lazima kuuacha mikononi mwa wajuzi au “wasomi” wa kitheolojia. Kupitia Musa, kwenye Kumbukumbu la Torati 30:11, 14, Mungu alijulisha hivi: “Hakika, Agizo hili ambalo nakuagiza leo hii si lenye kutatiza mno kwako, wala si lisiloweza kufikilika. Sivyo, jambo hilo li karibu sana nawe, katika kinywa chako na katika moyo wako, ili kulishika.” Taifa lote, si viongozi tu, liliambiwa: “Zingatia moyoni maagizo hayo ambayo ninakuamuru leo hii. Yakaze ndani ya watoto wako. Yakariri ukaapo nyumbani na uendapo njiani, ulalapo na uamkapo.” (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7) Amri za Mungu, zote zikiwa zimeandikwa, zilikuwa wazi vya kutosha kwa taifa zima kuweza kufuata, wazazi na watoto pia.c

15 Kurudi huko nyuma sana katika siku za Isaya, viongozi wa kidini walijiletea shutumu la Mungu kwa kujitwalia wenyewe daraka la kuongeza na kufasiri sheria ya Mungu. Nabii Isaya aliandika: “Watu hao wamekaribia Mimi kwa kinywa chao na kuheshimu Mimi kwa midomo yao, bali wameweka mioyo yao mbali na Mimi, na ibada yao kwangu Mimi imekuwa amri ya wanadamu, waliyojifunza kwa kukariri.” (Isaya 29:13) Ibada yao ilikuwa imekuwa amri ya wanadamu, si ya Mungu. (Kumbukumbu la Torati 4:2) ‘Amri hizo za wanadamu,’ fasiri na maelezo yao wenyewe, ndizo zilizokuwa zenye kupingana. Maneno ya Mungu hayakupingana. Ndivyo ilivyo leo.

Je! Kuna Msingi Wowote wa Kibiblia kwa Torati ya Mdomo?

16, 17. (a) Baadhi ya watu huamini nini kuhusu sheria ya mdomo? (b) Biblia huonyesha nini kuhusu sheria ya mdomo?

16 Baadhi ya watu huamini kwamba Musa alipokea “Torati ya Mdomo” kuongezea ile “Torati Iliyoandikwa.” Kulingana na imani hiyo, Mungu aliagiza kwamba amri fulani zisiandikwe bali zipitishwe kwa neno la mdomo toka kizazi hadi kizazi, zikihifadhiwa hivyo kwa pokeo la mdomo. (Ona kisanduku, “Je! Torati Ina “Nyuso Sabini”?”) Hata hivyo, masimulizi ya Biblia huonyesha waziwazi kwamba Musa hakuamriwa kamwe kupitisha sheria ya mdomo. Kutoka 24:3, 4 hutuambia hivi: “Musa akaenda na kuwaambia watu kwa kuzirudia amri zote za BWANA na kanuni zote; nao watu wote wakajibu kwa sauti moja, wakisema, ‘Mambo yote ambayo BWANA ameamuru tutafanya!’” Ndipo Musa “akaandika amri zote za BWANA.” Mbele kidogo, katika Kutoka 34:27 twaambiwa hivi: “Naye BWANA akasema kwa Musa: Andika amri hizi, kwa kuwa kwa kulingana na amri hizi mimi nafanya agano pamoja na wewe na pamoja na Israeli.” Sheria ya mdomo isiyoandikwa haikuwa na fungu lolote katika agano ambalo Mungu alifanya pamoja na Israeli. (Ona kisanduku, “Sheria ya Mdomo Ilikuwa Wapi . . .”.) Biblia haina mtajo wowote katika mahali popote kuhusu kuwako kwa sheria ya mdomo.d La maana zaidi, mafundisho yayo hupingana na Maandiko, yakiongeza lile wazo lenye kosa la kwamba Biblia hujipinga. (Ona kisanduku, “Kifo Na Nafsi—Ni Nini?”) Lakini mwanadamu, wala si Mungu, ndiye wa kulaumiwa kwa mvurugo huo.—Isaya 29:13. (Ona visanduku, “Showing Honor to the Divine Name.”))

JE! TORATI INA “NYUSO SABINI”?

KATIKA Israeli leo ni kawaida kusikia watu wakinukuu usemi wa Kiyahudi ujulikanao sana-​“Kuna nyuso sabini kwenye Torati”​—kuonyesha kwamba wao huamini kwamba Maandiko yaweza kufasiriwa katika njia nyingi tofauti-tofauti, hata zenye kupingana. Hiyo huonwa kuwa kweli kwa habari ya Sheria iliyoandikwa na pia ile inayoitwa eti sheria ya mdomo pia. The Encyclopedia of Judaism hueleza hivi: “Ile Sheria ya Mdomo si fungu la sheria lililo kamili; linatia ndani maoni mengi tofauti-tofauti na hata yenye kuhitilafiana. Kuhusu hayo wataalamu walisema, ‘Yote ni maneno ya Mungu aliye hai.’” (Ukurasa 532) Hata hivyo, je, ni jambo la akili kuamini kwamba Mungu angepulizia maoni yenye kuhitilafiana na yenye kuleta mgawanyiko? Mambo hayo yenye kupingana yalipataje kukubaliwa?

Muda wote wa kipindi wakati Maandiko ya Kiebrania yalikuwa yakiandikwa (wapata 1513–wapata 443 K.W.K.), wawakilishi wa Mungu waliowekwa rasmi walieleza wazi mambo yenye kubishaniwa, mara nyingi sana Mungu mwenyewe akiwaunga mkono kwa wonyesho wa nguvu za kimungu au kwa kutimiza unabii mbalimbali ambao alikuwa amewapa wautamke. (Kutoka 28:30; Hesabu 16:1–17:15 [16:1-50, UV]; 27:18-21; Kumbukumbu la Torati 18:20-22) Wakati huo mtu alipofundisha maelezo au fasiri zenye kupinga, hakuonwa kuwa msomi, bali mwasi-imani. Mungu alionya taifa zima hivi: “Iweni waangalifu kushika yale tu ambayo mimi nawaagiza nyinyi: wala msiyaongezee wala msiondoe kutoka kwayo.”​—Kumbukumbu la Torati 13:1 (12:32, UV).

Hata hivyo, baada ya wakati badiliko la msingi lilitukia katika kufikiri kwa taifa la Israeli. Mafarisayo, waliopata kuwa mashuhuri katika Dini ya Kiyahudi wakati wa karne ya kwanza W.K., walikubali fundisho la “Torati ya mdomo,” ambayo walikuwa wamesitawisha karne mbili mapema. Walifundisha kwamba zaidi ya kulipatia taifa la Israeli Sheria iliyoandikwa kwenye Mlima Sinai, wakati uleule Mungu alipitisha kwao sheria ya mdomo. Kulingana na imani hiyo, sheria hiyo ya mdomo iliyopuliziwa ilifasiri na kueleza wazi mambo ya Sheria iliyoandikwa, mambo ambayo Mungu alikuwa amemwambia kimakusudi Musa asiyaandike. Sheria hiyo ya mdomo haikupasa kuandikwa bali ilipasa kupitishwa kwa neno la mdomo, toka kwa mwalimu hadi kwa mwanafunzi, toka kizazi hadi kizazi. Hivyo iliwapa Mafarisayo mamlaka ya pekee, ambao walijiona wenyewe kuwa watunzi wa pokeo hilo la mdomo.g

Baada ya uharibifu wa hekalu la pili katika 70 W.K., maoni hayo ya Kifarisayo yalishinda, nayo Dini ya Kiyahudi ikapata kuwa namna ya dini yenye kutawalwa na marabi, haikuwa imepata kuwa hivyo wakati uliopita.h Marabi, badala ya makuhani au manabii, wakiisha kupewa umashuhuri mpya, ile sheria ya mdomo ilipata kuwa jambo jipya kuu la Dini ya Kiyahudi. Kama vile The Encyclopedia of Judaism hutaarifu: “Ile Torati ya Mdomo ikaja kuonwa kuwa ya maana zaidi ya ile Torati Iliyoandikwa kwa kuwa ufafanuzi na uelewevu wa ile ya pili ulitegemea ya kwanza.”—1989, ukurasa 710.

Kadiri marabi walivyopata umashuhuri na kadiri mapokeo yakaongezeka, marufuku ya kutoandika sheria hiyo ya mdomo iliondolewa. Katika sehemu ya mwishomwisho ya karne ya pili na mapema katika karne ya tatu W.K., Judah Ha-Nasi (135-219 W.K.) aliandika kwa utaratibu mapokeo hayo ya mdomo ya kirabi katika kitabu kiitwacho Mishna. Nyongeza za baadaye ziliitwa Tosefta. Marabi nao wakaona uhitaji wa kutoa maelezo juu ya Mishna, nazo fasiri hizo za pokeo la mdomo zikawa msingi wa mkusanyo mkubwa wa vitabu viitwavyo Gemara (vilivyokusanywa tokea karne ya tatu hadi ya tano W.K.). Vitabu vyote hivyo pamoja vikaja kujulikana kuwa Talmud. Maelezo juu ya mawazo hayo yote ya kirabi huendelea hadi siku zetu. Kwa kuwa haiwezekani kupatanisha maoni hayo yote yenye kutofautiana sana, je, ishangaze kwamba wengi hupendelea kuona “nyuso sabini kwenye Torati”?

g Fundisho hilo, lililoendelezwa mwanzoni na Mafarisayo, lilikataliwa na wengi kati ya marika yao katika taifa la Kiyahudi. Masadukayo, wengi wao wakiwa makuhani, pamoja na Waesene wa karne ya kwanza, walikataa wazo hilo la Kifarisayo. Leo, Wakaraite (tangu karne ya nane W.K.), pamoja na harakati za Wapendao Mabadiliko na Wasiopenda Mabadiliko ya Dini ya Kiyahudi, hawaoni sheria hiyo ya mdomo kuwa yenye kupuliziwa kimungu. Hata hivyo, Dini ya Kiyahudi ya Orthodoksi leo huyaona mapokeo hayo kuwa yenye kupuliziwa na kuwa lazima yafuatwe pia.

h Encyclopaedia Judaica hutaarifu hivi: “Ule mtajo wa cheo rabi watokana na nomino rav, ambayo katika Kiebrania cha Biblia humaanisha ‘mkuu’ na haionekani katika Biblia [ya Kiebrania].”

SHERIA YA MDOMO ILIKUWA WAPI . . .

. . . Musa aliporudia kuliambia taifa zima la Israeli amri zote za Mungu? Wakati huo taifa lilikubali kutimiza yale aliyokuwa amerudia kuliambia, kisha Musa “akaandika amri zote za BWANA.”—Kutoka 24:3, 4, Italiki ni zetu.

. . . Yoshua alipokusanya taifa la Israeli baada ya kuingia katika Bara Lililoahidiwa na kuwasomea tena maneno yote ambayo walikuwa wamekubali kutimiza? “Hapakuwa na neno kati ya yale yote ambayo Musa alikuwa ameamuru ambalo Yoshua alikosa kusoma mbele ya kusanyiko lote la Israeli.”—Yoshua 8:35, Italiki ni zetu.

. . . katika siku za Mfalme Yosia ‘kitabu cha Sheria ya Musa’ kilichokuwa kimepotea kilipopatikana wakati hekalu lilipokuwa likitengenezwa? Aliposikia akisomewa yaliyokuwamo, Yosia alirarua mavazi yake kwa kihoro, akijua kwamba kwa muda wa vizazi vingi Sheria hiyo haikuwa imetimizwa kulingana na yaliyoandikwa. Ndipo alipofanya mipango ili kuadhimisha Sikukuu ya Kupitwa, ambayo haikuwa sikuzote imeadhimishwa ifaavyo pindi yote ya wafalme na waamuzi kabla yao. Ilikuwa wapi sheria ya mdomo ‘iliyopitishwa kwa uaminifu’ wakati wa mamia hayo ya miaka? Kama ingekuwako, habari hiyo isingalisahauliwa kamwe. Ni rekodi iliyoandikwa tu yenye kuhifadhiwa kwa usahihi ambayo iliwezesha taifa lirudie kufanya mapenzi ya Mungu ifaavyo.—2 Wafalme 22:8–23:25.

. . . nabii Yeremia alipojulisha kwamba: “Tokea yule mdogo zaidi hata yule mkuu zaidi, wote ni wenye pupa ya pato; kuhani na nabii pia, wote hutenda kwa kibandia”? (Yeremia 6:13) Kupitia muda wote wa sehemu iliyo kubwa ya historia ya taifa la Israeli, hiyo ndiyo iliyokuwa hali ya kiroho ya viongozi wa taifa hilo, hasa makuhani, waliokuwa na daraka la kufundisha Sheria. (Malaki 2:7, 8) Rekodi zilizoandikwa hujisemea zenyewe, lakini je, wanaume waliokuwa hawaaminiki sana hivyo wangetegemewa wahifadhi kwa uaminifu pokeo la mdomo?

. . . muda wa miaka zaidi ya elfu moja ya kuandikwa Maandiko ya Kiebrania? Kuanzia Musa hadi Malaki, hakuna mtajo wowote wa kuwako Sheria kama hiyo ya mdomo. Ni baada tu ya mamia ya miaka, wakati wa kipindi cha marabi, mafarakano ya kidini yenye kuhitilafiana yalipong’ang’ania udhibiti na mamlaka juu ya taifa la Kiyahudi, ndipo twapata wazo hilo likitajwa. Je! mamia hayo ya miaka ya kimya juu ya habari hiyo na ushuhuda wa Maandiko yaliyopuliziwa havikanushi dai la kwamba kulipata kuwako wakati wowote sheria kama hiyo ya mdomo iliyopuliziwa?

17 Tofauti na fasiri zenye kupingana za wanadamu, Biblia yenyewe ni wazi na yenye kutumainika. Mungu ametuandalia uthibitisho wa kutosha ndani ya Neno lake kwamba ule ulimwengu wenye amani ulioonwa katika njozi kwenye Isaya 2:2-4 si ndoto tu bali ni uhakika utakaotimizwa karibuni. Si mwingine ila Mungu mwenyewe, Mungu wa unabii, Mungu wa Biblia, ndiye atautimiza.

HATI-KUNJO ZA BAHARI YA CHUMVI

Hati za Bahari ya Chumvi

Zenye tarehe ya kabla ya Wakati wa Kawaida, hizo hufunua usahihi wa kupitishwa kwa maandishi-awali ya Biblia kupitia karne nyingi. Zathibitisha pia kwamba unabii mbalimbali ulirekodiwa kabla ya utimizo wao

a Yapasa iangaliwe kwamba zile “siku” sita za uumbaji hazitii ndani ile taarifa kwenye Mwanzo 1:1, ambayo hurejezea uumbaji wa yale maumbo ya kimbingu. Zaidi ya hilo, neno la Kiebrania litafsiriwalo “siku” huruhusu kuwe na wazo la kwamba matukio yaelezwayo kwenye Mwanzo 1:3-31 yalitukia kwa ‘vipindi vya wakati’ sita ambavyo vingeweza kuwa na urefu wa maelfu mengi ya miaka.—Linganisha Mwanzo 2:4.

b Ili kuona mifano, ona kitabu “Je! Biblia Hujipinga Yenyewe?”

c Maswali magumu ya kesi za hukumu yalishughulikiwa na mpango wa hukumu ulioonyeshwa waziwazi. (Kumbukumbu la Torati 17:8-11) Katika mambo mengine yoyote ya maana yaliyoonekana kutokuwa wazi, ili kupokea jibu la Mungu, taifa lilielekezwa, si kwa sheria ya mdomo, bali kwa Urimu na Thumimu mikononi mwa makuhani.—Kutoka 28:30; Mambo ya Walawi 8:8; Hesabu 27:18-21; Kumbukumbu la Torati 33:8-10.

d Baadhi ya watu wamejaribu kufasiri maneno kwenye Kumbukumbu la Torati 17:8-11 kuwa yakidokezea pokeo la mdomo lililopuliziwa. Hata hivyo, kama ilivyotajwa katika kielezi cha chini kwenye fungu la 14, maneno hayo hushughulikia tu utaratibu wa hukumu katika kesi za hukumu. Angalia kwamba suala halikuwa kama desturi tofauti-tofauti au mapokeo yalipitishwa kupitia karne nyingi au la. Bila shaka kulikuwako mapokeo fulani yaliyopitishwa kwa habari ya jinsi ya kutimiza kihususa sehemu fulani za Sheria. Lakini uhakika wa kwamba pokeo limedumu muda mrefu hauthibitishi kwamba lilipuliziwa. Kwa mfano, angalia pokeo lililositawi kuhusu ile nyoka ya shaba.—Hesabu 21:8, 9; 2 Wafalme 18:4.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki