Mwenendo Mwema Unavuta
KAZI ya kuhubiri na kufundisha ya mashahidi wa Kikristo wa Yehova haipiti bila kuonwa na watu wote. Na mwenendo wao mwema wa kila siku unatoa nguvu za kweli kwa maneno yao. Kwa sababu hiyo mara nyingi watu wanakuwa na nia ya kuwasikiliza. Hii inaonyeshwa vema na waliyoona mashahidi wa Yehova katika nchi mbalimbali.
● Katika mji unaochimbwa madini wa Ghana ambapo uhalifu na ugomvi mkali wa wafanya kazi umewapa mapolisi kazi nyingi, kiongozi wa dini alimfikia mmoja wa mashahidi wa Yehova na kutaka funzo la Biblia. Akieleza sababu ya ombi lake, alisema: “Niliitwa kwenye kikao cha polisi siku moja kuwadhamini washiriki wawili wa kanisa langu waliokuwa wamepigana na kukamatwa. Nikamwuliza mkuu wa polisi aifute kesi ili niiamue kanisani. Akaniuliza, ‘Unawajua wale watu wanaoenda nyumba kwa nyumba wakiihubiri Biblia, mashahidi wa Yehova?’ Nikasema, ‘Nawajua,’ naye akaniambia, ‘Hutawaona wakati wo wote wakipigana au kufanya jambo lo lote litakalowafanya polisi kuwaleta kwenye kituo chao. Sababu gani usiwaulize washiriki wako wajifunze Biblia pamoja nao na kufuata Neno la Mungu kama wao wanavyofanya?’”
Kiongozi huyu wa dini anafanya maendeleo mema katika funzo lake la Maandiko pamoja na mashahidi wa Yehova na anahudhuria mikutano yao. Vile vile amefuata shauri la polisi huyo na kuwatia moyo washiriki wa kanisa lake kujifunza na Mashahidi. Wengine kati yao wanaonyesha kupendezwa kwa kweli.
● Mmoja wa mashahidi wa Yehova wa Martinique anayefanya kazi bandarini anaeleza aliyoona: ‘Nyakati za chakula ni kawaida ya wafanya kazi kufanya kila namna ya mzaha. Mara nyingi ni ya matusi. Hili linapotukia mimi naondoka. Mmoja wa wenzi wangu wa kazi aliona hivyo na kuuliza, “Wewe si Mkatoliki, ama sivyo?” Nikamwambia mimi ni mmoja wa mashahidi wa Yehova na kumweleza sababu ya kutoshiriki katika mazungumzo kama hayo. Kisha nikasema naye juu ya taratibu mpya ya Mungu, ambapo uovu, upotovu na mambo kama hayo hautakuwapo. Nikaeleza vile vile namna wale wanaoendelea na mwenendo mwema wa Kikristo watafurahia amani na furaha duniani. Hii ilimpendeza mwenzi wangu wa kazi. Akataka kujua namna nilivyopata ujuzi huo na kuonyesha tamaa ya kutaka funzo la Biblia la nyumbani. Leo yeye na mkewe ni mashahidi wa Yehova.’
● Katika shule moja Swaziland Shahidi wa miaka kumi na mmoja aliokota kifuko cha pesa chenye shilingi 5.00 Akakipeleka kwa waalimu wa mtafute mwenyewe. Jambo hili liliwashangaza waalimu sana. Walimpata mwenyewe na kumrudishia kifuko chake. Wenzi wa shule wa yule Shahidi mchanga walimdhihaki kwa kufanya hivyo, lakini uaminifu wake ulileta matokeo mema. Wazazi wa kijana huyo wa kike aliyekuwa amepoteza kifuko hawakuwa na nia nzuri kuwaelekea mashahidi wa Yehova. Lakini walitaka kujua hali ya kidini ya yule kijana wa kike aliyekuwa ameonyesha uaminifu kama huo. Walipoambiwa kwamba ni mmoja wa mashahidi wa Yehova, wakamwambia binti yao, ‘Hao ndiyo namna ya watoto unaopaswa kuwa nao kama marafiki.’ Wakauliza kwamba yule Shahidi mchanga aongoze funzo la Biblia na binti yao. Tangu wakati huo baba ya yule Shahidi mwenye umri wa miaka kumi na mmoja ameanza funzo la Biblia na wazazi wenyewe vile vile.
● Katika Turkey Shahidi mchanga aliyekuwa akihudhuria masomo ya jioni ilimpasa ajaze ombi la hati ya kumfahamisha mwanafunzi ili apate faida kutokana na nauli zilizopunguzwa za kusafiri. Ulizo moja katika ombi hilo lilikuwa juu ya kazi ya nje. Ingawa karibu wanafunzi wote walifanya kazi fulani ili kuhudhuria shule hiyo, walishauriwa kuandika “Hapana.” Lakini, Shahidi akaandika “Ndiyo.” Hii ilileta mgogoro mwingi kati ya wanafunzi wengine. Walijua kwamba ni Shahidi na waliogopa kufunuliwa wazi kama waongo. Kwa hiyo walimkaza ageuze jibu lake. Na hata Shahidi aliambiwa aende kwa kiongozi wa shule, ambaye vile vile alimwambia ageuze jibu lake ili apatane na wanafunzi wengine wote. Shahidi akakataa kabisa, akifahamisha kwamba udanganyifu ni tofauti na imani yake. Jibu lake mwishowe likakubaliwa. Kama matokeo hakupokea hati ya kumfahamisha mwanafunzi. Lakini, mwanafunzi mwenzake, kwa kuvutwa na uaminifu wake, akakubali kujifunza Biblia pamoja naye. Mwanafunzi huyo tangu hapo amekuwa Shahidi aliyebatizwa.
● Katika United Arab Republic kikundi cha vijana wa kike kiliwafikia dada wawili wa damu shuleni. Mmoja kati ya kikundi hicho akapaza sauti: ‘Tulitaka tu kuwasifuni kwa sababu ya mwenendo wenu mwema. Wakati wa miaka miwili ambayo tumewajua hatujawaona kama wenye magumu au vingine bali wenye fadhili na upendo.’ Kijana mwingine wa kike akasema: ‘Na lisilo la kawaida kabisa ni kwamba ninyi mu dada wawili na hali inaelekea mna upendo wa kweli kati yenu. Hakuna wakati tumewaona mkigombana.’ Dada wakajibu: ‘Mnachotusifia kwa kweli kimeletwa na kujifunza kwetu Biblia. Kanuni tunazojifunza kutokana na funzo letu tunajaribu kuzitumia katika maisha yetu ya kila siku. Biblia ina mashauri mengi juu ya fadhili, upendo na mwenendo mzuri.’ Ndipo mmoja wa dada hawa akatoa Biblia yake, anayobeba kila mara, na kuwasomea wale vijana wa kike juu ya matunda ya roho. (Gal. 5:22, 23) Kijana mmoja wa kike ambaye hakuwapenda wale dada akasema: ‘Hamjui ya kuwa wasichana (vijana wa kike) hawa wawili mnaosifu sana hata hawaendi kanisani?’ Basi mmoja wa hawa dada akajibu kwa wepesi: ‘Wewe unaenda kanisani, sivyo? Sababu gani, basi, si wewe unayesifiwa kwa sababu ya mwenendo mwema?’ Mazungumzo yalipomalizika, dada walikuwa wamemaliza kupanga kuongoza mafunzo ya Biblia na hesabu fulani ya wale wasichana. Sasa kumi kati yao wanafunzwa Biblia.
● Jamaa inayojulikana sana Seoul, Korea, ilikuwa nguzo katika mojawapo ya makanisa yenye nguvu ya Kiprotestanti katika mji. Jamaa hii ilikuwa karibu karibu sana. Ingawa waliishi sehemu mbalimbali za mji, walikuwa wakionana. Kwa miaka mingi wote walikuwa wamewafukuza mashahidi wa Yehova walipowatembelea. Wachungaji wao walikuwa wamewaonya wasisikilize mafundisho ya Mashahidi yasiyopatana na ya Kanisa. Ndipo mmoja wa dada za ile jamaa akamkodisha Shahidi fulani chumba. Mwenendo unaostahili wa Kikristo wa Shahidi haukupita bila kuonwa. Uliyafungua macho ya mwanamke huyu, ukimfanya aazimie kwamba mashahidi wa Yehova si wazushi bali watu wanaozoea kweli Ukristo.
Mwishowe akakubali kuwa na funzo la Biblia. Mara moja akaanza kusema na washiriki wengine wa jamaa yake na kuwauliza watembelewe na Mashahidi. Kulingana na habari ya karibuni zaidi, washiriki watano wa jamaa hiyo sasa wamebatizwa. Tisa wanashiriki pamoja na mashahidi wa Yehova katika kazi yao ya kuhubiri. Wengine wanajifunza Biblia na washiriki wengine zaidi wa jamaa hiyo. Yote haya yaliletwa na ushuhuda wa unyamavu wa mwenendo unaostahili wa mtu mmoja.
Mashahidi wa Yehova kila mahali wanajaribu kuishi kupatana na kanuni za Biblia—si kuwapendeza wengine, lakini kwa sababu wanajua hili tu ndilo jambo la haki kufanya. Ni wonyesho wa upendo wao kwa Yehova Mungu. Kama vile mtume Yohana aliandika: “Huku ndiko kumpenda Mungu, kwamba tuzishike amri zake.”—1 Yohana 5:3.