Ulimwengu Usio na Uvunjaji wa Sheria—Wewe Unautaka Kiasi Gani?
JE! WEWE umepata kuja nyumbani ukakuta nyingine za mali zako zenye thamani haziko? Ikiwa ndivyo, na kwa kuwa watu zaidi na zaidi wanapatwa na hayo leo, wewe ulionaje?
Watu wengi wanakasirika sana. Wanaona uchungu juu ya pupa na ukosefu wa upendo unaoonyeshwa na wizi, na vilevile wanadharau njia ya kunyemelea ambayo mwizi anatumia.
Lakini wengi wanaona hawana la kufanya. Inaelekea ni vigumu sana kuzuia uvunjaji wa sheria nyakati za kisasa. Kutotumaini njia ya kufikiliza sheria ndiyo sababu nusu ya jumla ya uvunjaji wa sheria hauripotiwi mahali pengi. Duniani pote, habari zinaonyesha kwamba mapolisi wanajaribu kufanya uchunguzi bila mafanikio.
Je! hali ya ulimwengu haikumbushi mtu juu ya maneno aliyosema Yesu kwa kujibu ulizo la wanafunzi wake juu ya “mwisho wa taratibu ya mambo”? Alisema kwamba sehemu ya “ishara” ambayo ingeutangulia mwisho ingekuwa “kuongezeka kwa kutokutii sheria.” (Mt. 24:3, 12, NW) Kwa kweli leo watu kila mahali wanazungumza juu ya uvunjaji wa sheria kupita wakati mwingine wo wote, wakihuzunika kwa sababu yake.
Ni nini ambacho kingehitajiwa ili kuwe na ulimwengu usio na uvunjaji wa sheria wo wote?
MAHALI AMBAPO HASA UVUNJAJI WA SHERIA UNATOKA
Unapofikiria uvunjaji wa sheria na wenye kuivunja, unafikiria nini? Watu wengi wanafikiria wahuni, wavunja nyumba nyakati za usiku, wenye kunajisi wanawake, majambazi na watu wa namna hiyo.
Lakini namna gani juu ya mtengeneza magari au televisheni ambaye kwa kawaida anatoza pesa za kazi asiyoifanya, daktari anayeongeza pesa zaidi kuliko za matibabu aliyokupa, au mwuza nyama anayepima nyama vibaya katika mizani? Au namna gani juu ya mama wa nyumbani anayeficha vitu mfukoni bila kuvilipia anapokuwa dukani, au mfanya kazi anayechukua vifaa vya kampuni yake? Kwa kweli, watu hao wanatofautianaje katika kusudi au njia zao na mwizi anayenyemelea? Na bado wengi wa watu ao hao wanalalamika juu ya ‘kuongezeka kwa uvunjaji wa sheria,’ wakiwa na maana ya uvunjaji wa sheria barabarani.
Na je! hayo yote hayakumbushi mtu juu ya maneno mengine yanayopatikana katika Biblia, yale ya mtume aliyeongozwa na Mungu kusema hivi: “Lakini ufahamu neno hili, ya kuwa siku za mwisho kutakuwako nyakati za hatari. Maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda fedha, . . . wasio safi, wasiowapenda wa kwao, . . . wasiojizuia, wakali, wasiopenda mema”?—2 Tim. 3:1-3.
NJIA YA PEKEE YA KUPATA ULIMWENGU USIO NA UVUNJAJI WA SHERIA
Tukifikiri kwa utimamu tutaona kwamba yako mambo mawili ya msingi ambayo lazima yabadilishwe ndiyo ulimwengu usio na uvunjaji wa sheria upatikane. Ni mambo gani hayo?
Moja ni taratibu ya mambo iliyopo ulimwenguni pote. Kwa sababu gani? Kwa sababu nia ya kuvunja sheria imesitawishwa katika taratibu hiyo tangu zamani za kale. Nia hiyo ni choyo. Pupa ya kibinadamu ndiyo imesitawisha hali zenye kuhuzunisha mamilioni ya wanadamu na kuleta uvunjaji mwingi sana wa sheria barabarani, muda wa karne hizo. Kwa sababu ya wafanya biashara na wanasiasa kutumia watu kwa faida yao wenyewe au kuwaonea na kuwahangaisha watu wengi wanakata tamaa ya kuweza kuwa na maisha bora kwa kutumia njia za uaminifu. Vita vikali sana vya kutimizia malengo ya kitaifa vinaharibu adili za watu na kuwafanya wakatili, vikiwaelekeza kutenda jeuri wakati ujao. Wanasiasa wenye vyeo vikubwa na mahakimu wanazoea upotovu na kufanya watu wasiwe na matumaini katika haki ya sheria. Naam, inaelekea uvunjaji wa sheria umekolea kabisa kati ya jamii ya kibinadamu.
Biblia inaonyesha kwamba tuko karibu sana sana na wakati ambapo Mungu ataleta ulimwengu usio na uvunjaji wa sheria kwa kufutilia mbali taratibu nzima hii ya utawala wa kibinadamu na mahali pake alete taratibu mpya yenye haki yenye kuongozwa na kusimamiwa na Mwana wake mwenyewe, yeye ambaye alihakikisha anapenda wanadamu bila choyo kwa kutoa uhai wake mwenyewe kwa ajili yao. (Dan. 2:44; Mt. 20:28) Ilisemwa hivi kwa unabii juu yake: “Na furaha yake itakuwa katika kumcha [Yehova]; wala hatahukumu kwa kuyafuata ayaonayo kwa macho yake; bali kwa haki atawahukumu maskini, naye atawaonya wanyenyekevu wa dunia kwa adili.” (Isa. 11:3, 4) Chini ya, utawala wake watu watafurahia usalama wa kweli. Lakini ili kuwe na ulimwengu usio na uvunjaji wa sheria, badiliko jingine linahitajiwa. Ni nini hilo?
Ni badiliko katika watu wenyewe. Ndiyo sababu Biblia inasema hivi kwa wale wanaotaka kupata uzima katika taratibu hiyo inayokuja isiyo ya uvunjaji wa sheria: “Msiambiane uongo, kwa kuwa mmevua kabisa utu wa kale, pamoja na matendo yake; mkivaa utu mpya, unaofanywa upya upate ufahamu sawasawa na mfano wake yeye aliyeuumba.”—Kol. 3:9, 10.
Leo watu wengi wanaoonwa mtaani kuwa “raia wenye kuheshimika,” kutia na wanakanisa wengi, wanafanya udanganyifu mdogo mdogo kwa kawaida. Wanajipa udhuru kwa kusema, ‘Aaah, kila mtu anafanya hivyo,’ na, ‘Kwa kuwa watu wanadanganya wapate vyeo vikubwa, hata mimi lazima nifanye hivyo nisipoteze kazi.’ Ufupi wa maisha na ukosefu wa tumaini la kweli la wakati ujao unafanya wengi wafuatie mali za kimwili tu, hata kuwafanya wajitahidi kwa ukali ‘watajirike upesi.’
Kwa hiyo uvunjaji mwingi wa sheria unafanywa na vijana. Kwa sababu gani? Msimamizi wa Association of Chief Police Officers in Great Britain anasema hivi juu ya uvunjaji wa sheria unaofanywa na watoto: “Kama wangalikuwa na tumaini juu ya wakati ujao, uvunjaji mwingi wa sheria usingekuwapo.” Wachunguzi wa uvunjaji wa sheria Franco Ferracuti na Graeme R. Newman wanasema hivi: “Uchunguzi wa Kiamerika umeonyesha kwamba kutotia adabu [katika jamaa] kwa njia nzuri huenda kukawa ndiyo sababu ya kuwa na persenti 70 ya wanaume wenye kuvunja sheria.”
Hayo yote yanahakikisha ukweli wa unabii wa Yesu, kwa maana alisema kwamba “kwa sababu ya kuongezeka kwa kutokutii sheria upendo wa wengi zaidi utapoa.” (Mt. 24:12, NW) Naam, uvunjaji wa sheria wa namna mbalimbali ukiwa unaenea sana, kupenda haki, uaminifu na adabu zinapungua kwa watu zaidi na zaidi.
Kwa kweli, je! kutokutii sheria kwa namna zote hakutokani na ukosefu wa upendo? Yesu Kristo alisema kwamba sheria zote zilizopewa kwa taifa la kale la Israeli zilitegemea amri mbili tu: “Mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa [nafsi] yako yote, na kwa akili zako zote. . . . Mpende jirani yako kama nafsi yako.” (Mt. 22:37-40) Na baada ya kuzungumza juu ya vile imewapasa Wakristo wa kweli waheshimu wenye mamlaka na sheria zao, mtume Paulo aliyeongozwa na Mungu aliendelea kusema hivi: “Pendo halimfanyii jirani neno baya; basi pendo ndilo utimilifu wa sheria.” (Rum. 13:10) Lakini taratibu za kibinadamu haziwezi kamwe kukuza hali ya upendo itakayokomesha uvunjaji wa sheria duniani. Muumba wa mwanadamu peke yake ndiye anayeweza kufanya hivyo na atafanya hivyo kupitia kwa taratibu mpya inayokuja na kupitia kwa elimu juu ya haki itakayokuwako.
Ulimwengu usio na uvunjaji wa sheria unakaribia. Lakini ili ye yote kati yetu aufurahie lazima ajifunze mapenzi, makusudi na kanuni za Yehova Mungu sasa. Yeye ametoa kwa upendo Neno lake Biblia aliloliongoza liandikwe kwa roho yake ili atuwezeshe kujua namna ya kuonyesha upendo wa kweli kwake na kwa jirani yetu. Katika Biblia anatupa tumaini na hakika itakayotuwezesha kuacha kufadhaika na kukata tamaa na kuzuia kishawishi cha “kufanya maendeleo” kwa kutumia udanganyifu.
Je! kweli wewe unataka kuona ulimwengu usio na uvunjaji wa sheria? Basi imekupasa uchukue hatua zilizo za lazima ili kuokoka uharibifu unaokaribia wa taratibu iliyopo ya mambo. Ni katika Taratibu Mpya itakayofuata, ambamo mtakuwa na upendo kwa Mungu na upendo kwa jirani duniani pote, watu wanamoweza kufurahia kuishi bila uvunjaji wa sheria wa namna zote. Ili uweze kuishi wakati huo, tumia nafasi uliyo nayo sasa upate ujuzi wenye kupa nuru na uzima ambao umo katika Neno la Mungu. Kwa sababu wanampenda Mungu na jirani yao, mashahidi wa Yehova wanasaidia bila malipo.
[Blurb katika ukurasa wa 77]
BIBLIA ILITABIRI: “Kwa sababu ya kuongezeka kwa kutokutii sheria upendo wa wengi zaidi utapoa.”—Mt. 24:12, NW.