‘Kufungwa Viuno’ kwa Ajili ya Kazi Iliyoko Mbele
“Simameni, hali mmejifunga kweli viunoni.”—Efe. 6:14.
1. Kwa sababu gani watumwa wa Bwana wangefurahishwa?
KATIKA Uyahudi, pengine wakati wa vuli ya mwaka 32 W.K., ndipo Yesu alipowaambia wanafunzi wake hivi: “Heri watumwa wale, ambao bwana wao ajapo atawakuta wanakesha, Amin, nawaambieni, atajifunga na kuwakaribisha chakulani, atakuja na kuwahudumia. Na akija zamu ya pili, au akija zamu ya tatu, na kuwakuta hivi, heri watumwa hao.” (Luka 12:37, 38) Hata kama Bwana asingekuja upesi walivyotazamia, wangeendelea kukesha hata zamu ya tatu ya ulinzi—ambayo ndiyo yenye giza nene zaidi kabla ya mapambazuko.—Linganisha Mathayo 25:13.
2. Ni jambo gani linalofanya watumwa wapaswe kukesha?
2 Hata kipindi hiki cha kumngojea Yesu, Mwana wa Adamu, kikiendelea zaidi kuliko ilivyotazamiwa, ni hakika kwamba atafika kama mwivi! Mtu ye yote asilegee akidhani kwamba hatafika milele. Lazima wakati huo ufike! Ni kama vile Yesu mwenyewe anavyotuhakikishia: “Lakini fahamuni neno hili, Kwamba mwenye nyumba angalijua saa atakayokuja mwivi, angalikesha, wala asingaliacha nyumba yake kuvunjwa. Nanyi jiwekeni tayari, kwa kuwa saa msiyodhani ndipo ajapo Mwana wa Adamu.”—Luka 12:39, 40.
3. Ni jambo gani linalotakiwa zaidi ya kukesha? (1 Pet. 1:13)
3 Walakini, watumwa wa Yesu hawakeshi tu. Bwana anawatazamia ‘wajifunge viuno’ kwa ajili ya utumishi, kama vile yeye anavyojifunga’ awatumikie. Awaambia: “Viuno vyenu na viwe vimefungwa, na taa zenu ziwe zinawaka; nanyi iweni kama watu wanaomngojea bwana wao.” (Luka 12:35, 36) Tukiwa na bidii ya kufanya mambo hayo tutahesabiwa kuwa “heri” Bwana ajapo.
KUFUNGA VIUNO KWA AJILI YA UTUMISHI WA MUNGU
4. Twawezaje ‘kujifunga viuno’ kwa ajili ya utumishi wa Mungu? (Zab. 18:31, 39)
4 Maana yake nini kwa mtumwa ‘kufunga viuno’? Zamani za kale mashujaa wa vita walikuwa wakijifunga viuno kwa mshipi wa ngozi. Uliwaimarisha walipoelekea vitani. Vivyo hivyo, yawapasa leo Wakristo ‘wajifunge,’ wajitayarishe kwa ajili ya utendaji. Mtume Paulo atuambia kwamba ili ‘tupate kuweza kuzipinga hila za Shetani,’ yatupasa ‘tuvae silaha zote za Mungu.’ Kwanza, hiyo yatuhitaji ‘tufunge’ kweli katika viuno vyetu. Tutasaidika ‘kumpinga’ yule mwovu tukiendelea kujifunza na kuthamini sana kweli ya Neno la Mungu.—Efe. 6:11-14; angalia Kingdom Interlinear.
5. Ni fundisho gani litakalotusaidia ‘tujifunge viuno ‘ na kwa ajili ya utendaji gani?
5 Vita yetu ya kiroho ni halisi. Kwa hiyo yatupasa ‘tufunge daima viuno vyetu.’ Yatupasa tuendelee kujifunza Neno la Mungu, kusitawisha imani yenye kuzidi kuwa yenye nguvu, ili tuweze kuwa tayari sana kukinga kila silaha ambayo huenda Shetani mjanja akatutupia. ‘Tukifundishwa na Yehova,’ hakuna silaha itakayofanikiwa juu yetu. (Isa. 54:13, 17) ‘Kujifunga’ viuno kunatufanya tuzitangaze “habari njema za ufalme” kwa uchangamfu, na utendaji huo unatuletea wokovu sisi wenyewe na wale wanaotusikiliza.—Matendo 8:12; 1 Tim. 4:16.
6. Yehova alimhakikishia Yeremia kwamba matokeo yangekuwaje ‘akijifunga viuno’? (Linganisha 1 Wafalme 18:46.)
6 ‘Tutajifunga’ viuno kama nabii Yeremia, aliyemtumikia Yehova zaidi ya miaka 40 bila kuacha. Wakati Yehova alipomwagiza kwanza Yeremia, alimwambia hivi:
“Haya basi, wewe jifunge viuno, ukaondoke, ukawaambie maneno yote niliyokuamuru; usifadhaike kwa ajili yao, nisije nikakufadhaisha wewe mbele yao. Maana, tazama, nimekufanya leo kuwa mji wenye boma, na nguzo ya chuma, na kuta za shaba, juu ya nchi yote; juu ya wafalme wa Yuda, na juu ya wakuu wake, na juu ya makuhani wake, na juu ya watu wa nchi hii. Nao watapigana nawe; lakini hawatakushinda; maana mimi nipo pamoja nawe, asema [Yehova], ili nikuokoe.”—Yer. 1:17-19.
7. Twaweza kuonyeshaje kwamba twathamini uhusiano wetu na Yehova?
7 Lo! jinsi maneno hayo yanavyotutia moyo! Yanatupa uthibitisho leo, kwamba hata watumishi wa Mungu wafanyiwe hila na serikali za namna gani au watu wa namna gani, yeye atatupigia vita, nasi tutashinda. Lakini lazima sikuzote tuthamini sana uhusiano wetu wa karibu na Yehova, kama mashahidi wake, walioagizwa kuutangaza ujumbe wake kati ya mataifa yaliyohukumiwa maangamizi. Maadamu wakati upo, sikuzote na ‘tujifunge’ kwa ajili ya utumishi huu, tuwe wenye juhudi kujulisha wengine kweli!
“WEWE JIFUNGE VIUNO”
8. Ni jambo gani linalotulazimisha tuendelee na utumishi wa Mungu kama Yeremia?
8 Kama nabii Yeremia, imetulazimu ‘tujifunge viuno’ kwa muda mrefu, tukiuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi. Huu “wakati wa mwisho” umekwisha endelea zaidi ya miaka 62, na wengi wetu tume kuwa tukieleza wengine “maarifa” ya kweli kwa miaka 20, 30, 40 au zaidi. (Dan. 12:4) Pengine nyakati nyingine tulijisikia kama Yeremia aliposema: “Sitamtaja [Yehova], wala sitasema tena kwa jina lake.” Lakini kujifunga kweli viunoni petu kwatulazimisha tusonge mbele na utumishi wa Mungu. Neno lake linakuwa ‘kama moto uwakao, uliofungwa ndani ya mifupa yetu,’ hata hatuwezi kuepuka kujulisha watu jina na ufalme mtukufu wa Yehova.—Yer, 20:9 Zab. 96:2, 10.
9. Ni jambo gani linaloonyesha Yehova anaendelea kuangalia watu wake? (Zab. 3:8)
9 Ripoti zenye kusisimua zilizopokewa kutoka kwa Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote kuhusu utendaji wao wa mwaka wa utumishi wa 1976 zaonyesha kwamba, Yehova anaendelea kutusaidia ‘tujifunge’ kwa ajili ya utumishi huu wa maana kupita wote. Kwa ujumla, maendeleo ni makubwa sana. Kilele cha watangazaji Ufalme ulimwenguni pote kiliongezeka wakawa 2,243,390. Jumla kubwa ya watu 196,656 waliojiweka wakf karibuni walibatizwa, nayo makundi yaliongezeka yakawa 40,155. Ingawa utendaji wa Mashahidi ulishuka kwa saa 23,000,000 ulimwenguni pote, walifanya jambo la kusifika kwa kutumia saa 359,258,019 katika utumishi wa kueleza hadhara ya watu ‘habari njema za ufalme,’ na waliongoza nyumbani kwa watu wastani ya mafunzo ya Biblia 1,339,466. (Linganisha Matendo 2:46, 47.) Orodha iliyo katika kurasa 254 mpaka 257 inatoa maelezo zaidi.
10. Kupatana na Mithali 10:22, ni mambo gani ambayo watumishi wa Mungu waliona katika zile bara mbili za Amerika mwaka 1976?
10 Ripoti za kufurahisha zilitoka kwa Mashahidi wa Yehova katika nchi nyingi. Kwa mfano, katika zile bara mbili za Amerika, Canada yasema hivi: “Mambo makubwa katika utumishi wetu wa shambani wa 1976 yalikuwa vilele viwili katika wahubiri wa Ufalme, na kile cha karibuni zaidi kilikuwa cha watangazaji 62,880 wa habari njema katika Mei.” Costa Rica waandika hivi: “Karibu kila Jumba la Ufalme linafurika watu wenye kupendezwa. Kwa hiyo makundi kumi mapya yalianzwa wakati wa mwaka.” Honduras watuambia hivi: “Zaidi ya nusu ya wahubiri wetu wote [wa Ufalme] walibatizwa miaka mitatu iliyopita.”
11. (a) Ijapokuwapo marufuku, ndugu zetu katika Argentine walishiriki je kutimiza Warumi 10:18? (b) Kwa kuangalia orodha, ni maongezeko gani mengine yaliyokuwako Katika bara zile mbili za Amerika?
11 Katika Argentine, Mashahidi wa Yehova sasa ni marufuku, na ndugu fulani wamefungwa gerezani. Lakini, “neno la Mungu halifungwi.” (2 Tim. 2:9) Wanaendelea kuzitangaza “habari njema,” na lifuatalo ni kati ya mambo yanayofurahisha waliyoona:
“Watu wa umri wote na wenye vizuizi vya kimwili wanaitikia mwito wa Yehova kumsifu. (Zaburi 148:12, 13) Dada painia alitembea maili sita (kilomita karibu 10) akaongoze funzo kwa kizee-mke, wa miaka 105. Funzo lilipoendelea, mwanamke huyo aliona ana daraka la kuhubiri, kwa hiyo akatumia mkongojo wake kutembelea jirani zake akawaeleza mambo mazuri sana aliyokuwa akijifunza. Kwa kuhubiri kwake mafunzo mawili yalianzwa, na moja lilianzwa kwa mwanamume mmoja aliyekuwa amefukuza dada painia katika nyumba yake.”
Kumekuwa na msukosuko mwingi Chile, lakini kilele cha Mashahidi wenye bidii kiliongezeka kwa kiasi cha 18 kwa mia, wakawa 16,862. Brazil yaripoti hudhurio kubwa la watu 212,441 katika makusanyiko 24 ya wilaya ya “Enzi Kuu ya Kimungu.”
12. (a) Kupatana na Warumi 15:10, 11, 13, orodha yaonyesha nini juu ya furaha na tumaini la Mashahidi wa Ulaya? (b) Ni ripoti gani za kupendeza zilizotoka Spania na Ureno?
12 Namna gani utendaji wa Mashahidi wa Yehova Ulaya? Finland yatueleza kwamba ushuhuda wa Ufalme umetolewa sana hata kila toleo jipya la trakti Kingdom News linaenezwa katika kila nyumba nchini. Makundi ya watu wanaomiminika kwenye mikutano ya Kikristo Austria yanapendeza hata kuliko milima ya huko, na Majumba ya Ufalme mapya kumi na saba yaliwekwa wakf mwaka jana. Spania imekuwa ikiweka wakf Majumba mapya ya Ufalme sita kila mwezi, hivi kwamba makundi yao 614 yanatumia zaidi ya Majumba ya Ufalme 440, na vilevile majumba mawili ya makusanyiko ya mizunguko. Ureno yaandika kwamba, miaka miwili iliyofuata mapinduzi ya Aprili 24, 1974, watangazaji Ufalme wameongezeka kwa kiasi cha 41 kwa mia, nayo hesabu ya makundi ya Mashahidi wa Yehova imetoka 172 ikawa zaidi ya 300.
13. Ripoti kutoka Asia, kutia na zilizomo orodhani, zaonyeshaje Matendo 2:39 imetimizwa?
13 Ziko habari zenye kutia moyo pia kutoka Asia. Wamisionari wenye bidii Pakistan walifurahi kuona kilele kipya cha mashahidi wa Ufalme 192 nchini mwao. Kutoka Lebanon yenye kuvuma vita yaja ripoti hii:
“Makombora yaliangukia majengo yaliyokuwa karibu yetu—moja katika jengo lililokuwa kando yetu na jingine karibu mita 30 (futi 98) kutoka tulipokuwa; hilo lilitukia siku tatu zilizopita. Jana tulifurahi kwenda [kutoa ushuhuda] nyumba kwa nyumba kwa saa mbili na nusu, tukiwa waangalifu tusisumbue watu. Tulifurahia pendeleo hilo.”
India waandika kwamba walitangaza Ufalme katika maeneo mapya katika Punjab na mashariki ya kaskazini ya Assam. Ijapokuwa magumu, kazi ndogo ilifanywa kati ya mamilioni ya watu wa Afghanistan, Nepal na Bangladesh. Katika Korea, watu wengi sana walihudhuria mwadhimisho wa Ukumbusho katika jengo la tawi la Seoul la Watch Tower Society hata ikawa lazima kuwe na mikutano mitano, mingine katika chumba cha kulia cha Betheli na katika chumba cha kupumzikia, na vilevile katika Jumba la Ufalme. Zaidi ya watu 60,000 walihudhuria Ukumbusho katika Korea yote.
14. Ni habari na tarakimu gani zenye kutia moyo zinazoripotiwa kutoka Afrika yenye ugomvi mwingi?
14 Yako mabadiliko makubwa Afrika yote, nayo mateso yanaendelea kuwaka mahali mbalimbali. Kutoka nchi moja yaripotiwa kwamba, Mashahidi wanalazimika kuamka usiku wa manane kusoma andiko la siku bila kusumbuliwa. Katika nchi nyingine ambako kazi ya Yehova ni marufuku, makundi mapya kumi na tisa yalianzwa na watu 195 wakaonyesha wamejiweka wakf kwa Yehova kwa kubatizwa majini. Nchi nyingine yenye marufuku yaripoti hivi:
“Tulistaajabishwa na hudhurio la Ukumbusho, ambalo lilipita wastani ya mwaka jana ya wahubiri wa Ufalme kwa kiasi cha 94 kwa mia.”
Zaire yaandika kwamba nchi hiyo watu zaidi sasa wanajifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova kuliko hapo kwanza. Brazzaville, katika Congo, wasema kwamba mwezi Desemba walikuwa na kilele cha kusifika cha mapainia wasaidizi 580 shambani, na hiyo ni karibu theluthi moja ya jumla yao ya wahubiri wa Ufalme mwezi huo. Sasa Sierra Leone kiasi cha 25 kwa mia cha mashahidi wao wa Ufalme wako katika utumishi wa wakati wote wa “painia.” Katika Zambia, makundi mengi yalianzwa, na kukawa na kilele kipya cha Mashahidi 57,885 wenye bidii katika shamba, kwa hiyo watu wote wa nchi hiyo wanaweza kugawanywa na kuwa 89 kwa kila mhubiri mmoja.
15. Je! visiwa ‘vina furaha,’ kama inavyotajwa katika Zaburi 97:1? Orodha yaonyesha nini?
15 Namna gani visiwa vya bahari? Kutoka kile kisiwa kikubwa cha Australia yaja ripoti kwamba makundi yenye kuzungumza lugha za kigeni yamekua hata waangalizi wa mizunguko wenye kuzungumza Kigiriki na Kiitalia watatumiwa miezi kadha kila mwaka. Ripoti kutoka British Isles (Uingereza) yasema kwamba watu 157,070 walihudhuria Ukumbusho, na kwamba kuanzia mwaka huu, kiasi cha 75 kwa mia cha Mashahidi Waingereza watakuwa wakihudhuria makusanyiko ya mizunguko katika majumba yao wenyewe. Iceland walitiwa moyo kwa kuwa na kilele kikubwa zaidi kupita nyakati zilizotangulia cha kubatiza watu kumi na tisa, wote wakiwa wenyeji. Katika Taiwan (na vile-vile katika Hong Kong) maendeleo mazuri ajabu yalifanywa kati ya Wachina, likaripotiwa ongezeko la kiasi cha 31 kwa mia katika yale makundi mawili ya Taipei. Sri Lanka waeleza hivi: “Watu 43 walibatizwa mwaka huu. Wengi wao walikuwa wamekuwa Wakatoliki.” Kutoka Tahiti, katika French Polynesia, yaja ripoti hii: “Ufalme ulihubiriwa katika visiwa kumi na vitano visivyokuwa vimehubiriwa, vyenye watu 7,700, na yalipatikana maandikisho 610 ya The Watchtower na Awake! ya Kitaiwan.” Jamhuri ya Cape Verde yatuambia hivi: “Linalotendeka katika visiwa hivi ni jambo lisilo la kawaida! Wahubiri shambani wameongezeka kiasi cha 125 kwa mia, kukawa na kilele cha 60.”
16. Mashahidi walio katika nchi zenye marufuku wanaonyeshaje kwamba ‘wanafurahi wakiwa katika mateso’? (Kol. 1:24)
16 Ripoti zilizotolewa juu zinahusu kisehemu tu cha kazi ya ulimwenguni pote ya Mashahidi wa Yehova. Unaweza kuona ripoti kamili katika kurasa zilizomo. Katika nchi zaidi ya 40 Mashahidi wa Yehova wanaendesha kazi yao wakiwa katika marufuku rasmi au vizuizi, kwa hiyo si hekima kutaja baadhi yazo kwa majina na kutoa ripoti zake kwa urefu. Walakini, tarakimu za jumla zatia ndani utendaji wao wa kujinyima pia. Twafurahi pamoja na Mashahidi wote waaminifu kwamba Yehova aliubariki sana utangazaji wa Ufalme wake mwaka jana.
KUTAZAWUA MBELE
17. Yatupasa tukumbuke maneno na mfano gani wa Yesu?
17 Mwisho ukaribiapo, twaweza kutazamia taabu ziongezeke duniani. Huenda imani yetu ikajaribiwa kweli kweli. Lakini yatupasa tukumbuke sana maneno ya Yesu kwamba “sharti Injili ihubiriwe kwanza katika mataifa yote.” (Marko 13:10) Yesu alitangaza pia: “Msujudie [Yehova] Mungu wako, umwabudu yeye peke yake.” (Luka 4:8) Yesu mwenyewe alituwekea mfano bora wa kufanya hivyo. (Luka 8:1; 10:1) Tufuatapo mfano huo, na kujishughulisha tukiutangaza ufalme wa Mungu, wakati unakwenda haraka. Hilo linatufurahisha, tunapokwenda haraka kuelekea mwisho.
18. Twapaswa kutiwa moyo namna gani na nia ya Paulo?
18 Mtume Paulo alitumikia akiwa katika hali mbalimbali zenye magumu, lakini sikuzote alikuwa na maoni haya: “Ole wangu nisipoihubiri Injili!” (1 Kor. 9:16) Ungekuwa “ole” kwetu pia tukipunguza mwendo katika utumishi wa Yehova wakati huu ambapo “siku za mwisho” zimefikia upeo. (2 Tim. 3:1, 14) Baada ya miaka mingi ya kujaribiwa, Paulo alikuwa bado amekaza nia aendelee kutumikia kwa nguvu zake zote. Kama alivyosema katika Wafilipi 3:13, 14: “Ndugu, sijidhanii nafsi yangu kwamba nimekwisha kushika [zawadi]; ila natenda neno moja tu; nikiyasahau yaliyo nyuma, nikiyachuchumilia yaliyo mbele; nakaza mwendo, niifikilie mede ya thawabu.”
19. Saburi ya Yehova imewezeshaje watu kupata wokovu na kuleta ongezeko? (Isaya 42:8-10)
19 Basi na tuwe wenye nguvu tutumikie, tumngojeapo Yehova. Saburi yake imekwisha wezesha umati wa watu wapate wokovu. Kama Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ingetokeza “dhiki kubwa”: Katika Ujeremani, ni maelfu machache tu—kutia na wale waaminifu waliokuwa katika kambi za mateso za Hitler—ambao wangeokoka, na hali leo wako 102,044 wanaotumikia katika njia ya wokovu Ujeremani ya Magharibi, pamoja na wengine wengi Berlin na Ujeremani ya Mashariki. Katika Italia ya Wakatoliki, mwaka 1951 ni watangazaji wa Ufalme 1,741 tu waliokuwa wakiripoti utumishi, hali leo wana kilele cha Mashahidi 60,156 shambani. Katika Japan, walikuwako Mashahidi wachache tu wenye ‘kusimama imara’ kwa ajili ya “habari njema” wakati vizuizi vya wakuu wa jeshi na Washinto vilipoondolewa mwaka 1945, lakini leo nchi nzima imekwisha gawiwa watu wa kuhubiri—na kwa kawaida eneo lote linamalizwa na kilele cha Mashahidi 38,367, tena karibu kiasi cha 25 kwa mia cha idadi hiyo wamo katika utumishi wa wakati wote wa “painia.” Miujiza hii ya wokovu na mpanuko imetokea baada ya Vita ya Ulimwengu ya Pili.
20. Yatupasa tuwe na hakika gani, na yatupasa kuionyeshaje?
20 Ni nani ajuaye Yehova akusudia kutenda mambo gani zaidi ya ajabu kabla ya wakati aliowekea “dhiki kubwa”? (Zab. 86:8-10) Bila kujali mapenzi ya Yehova ni nini kwa siku zinazokaribia, na tuendelee ‘kusimama imara,’ tukiwa tumefungwa viuno kwa ajili ya utumishi wake. Na tuwe na hakika kwamba sikuzote “msingi wa Mungu ulio imara umesimama, wenye muhuri hii, Bwana awajua walio wake.” (2 Tim. 2:19) Tunapojitoa tufanye utumishi wa Ufalme, Yehova na atutumie kutafuta wengi zaidi “walio wake,” ili sote pamoja tupate kufurahia fadhili zake zisizostahilika alizoonyesha kupitia kwa Kristo Yesu, sasa na umilele wote utakaokuja!
—Kutoka The Watchtower, Jan. 1, 1977.