Ndoa za Kati ya Washiriki wa Jamaa ya Karibu—Inawapasa Wakristo Wazioneje?
MIAKA michache iliyopita mahakma katika mojawapo ya nchi za Scandinavia ilitoa uamuzi wa kwamba hakuna hatua iliyopaswa kuchukuliwa juu ya mwanamume aliyekuwa akiishi pamoja na dada yake katika uhusiano wa ndoa. Mjumbe wa bunge ya nchi hiyo alisema kwamba angependezeka sheria ya nchi hiyo iliyohusu ngono kati ya washiriki wa jamaa ya karibu ibadilishwe ili uhusiano kama huo uwe halali. Visa vya namna hiyo vyaweza kutajwa katika nchi nyinginezo.
Ni ndoa ya namna gani inayoonwa kuwa ndoa kati ya washiriki wa jamaa ya karibu? Biblia inatoa habari gani inayoweza kuwasaidia Wakristo kuamua maoni wanayopaswa kuwa nayo kuhusiana nazo?
Neno la Kiingereza “incest,” (zinaa za maharimu) lamaanisha uhusiano wa ngono kati ya washiriki wa jamaa ya karibu. Neno la Kiingereza linatokana na neno la Kilatini incestus. Walakini katika Kilatini, incestus lamaanisha tu “kutokuwa safi,” (“uchafu”) Kwa hiyo lina maana kubwa zaidi ya neno la Kiingereza linalotokana nalo. Zinaa zote za maharimu, bila shaka, ni uchafu, walakini uchafu wote si zinaa za maharimu. Maana ya pekee ya neno la Kiingereza ilitokana na neno hilo la Kilatini incestus katika hati ya Kilatini ya Vulgate iliyotafsiri Mambo ya Walawi 18:17, ambapo ngono kati ya washiriki fulani fulani wa jamaa zinaelezwa.a Tafsiri za Kikatoliki katika Kiingereza zilitumia neno hilo katika namna ya Kiingereza, na, baada ya muda kupita, likaja kuwa na maana hiyo ya pekee ya uhusiano wa ngono kati ya washiriki wa jamaa ya karibu.
Hata hivyo, jambo ya maana kwa wale wanaoheshimu Neno la Mungu, si neno la Kilatini au Kiingereza linalotumiwa, bali yale yanayosemwa na Maandiko juu ya uhusiano huo wenyewe. Jambo moja ni kwamba, agano la Torati lililopewa kwa taifa la Israeli lilikataza uhusiano wa ndoa kati ya watu wa ukoo. (Law. 18:7-18; 20:14, 19-21; Kum. 27:23) Kwa Wakristo, jambo la maana zaidi ni tamaa ya kudumisha ndoa katika hali ya kuheshimika na kuepuka kuiletea suto, katika kuzifikiria dhamiri za wengine, ndani na nje ya kundi.—Ebr. 13:4; 1 Kor. 10:32, 33; 2 Kor. 4:2.
Katazo la agano la Torati juu ya namna fulani za uhusiano wa ndoa kati ya washiriki wa jamaa ya karibu linatupa kanuni zenye kuongoza. Walakini bado ni jambo la hakika kwamba Wakristo hawako chini ya Torati hiyo iliyopewa kwa Israeli wa asili. Hivyo, kundi la Kikristo halina mamlaka ya kujaribu kulazimisha wafu wafuate Torati hiyo kwa kusisitiza kwamba washikamane na orodha yake kwa kuepuka kila mojawapo ya makatazo ya ndoa yaliyoorodheshwa (yaliyoandikwa) humo.—Matendo 15:10, 11; Rum. 6:14; Gal. 2:21.
Yaweza kuonwa kwamba sehemu fulani za makatazo hayo yaelekea kuwa yalikusudiwa kuhifadhi utaratibu wa haki za urithi kati ya Waisraeli. Ujamaa wenyewe au uhusiano wa karibu kwa sababu ya ndoa peke yake hauelekei kuamua juu ya kufaa kiadili au kutofaa kiadili kwa uhusiano. Kwa hiyo, mwana hangeweza kuoa shangazi yake walakini hakukuwa na katazo lo lote kwamba mjomba asioe mpwawe mwanamke. (Law. 18:12-14) Kwa wazi, uhusiano wa karibu wa damu (au, mashangazi na wajomba kupitia kwa ndoa wakihusika, ujamaa huo) haukuwa mkubwa zaidi au mdogo zaidi katika visa vyote viwili. Hata hivyo ndoa moja iliruhusiwa na nyingine ilikatazwa.
Mwanamume hangeweza kumwoa mjane wa nduguye, jambo ambalo leo, halionwi katika nchi nyingi kuwa ndoa kati ya washiriki wa jamaa ya karibu. Na hata hivyo, inaweza kuonwa kwamba, chini ya agano la Torati, wakati mwanamume alipokufa bila kuwa na mwana wa kumrithi, nduguye alipaswa kulingana na Torati hiyo kumwoa mjane wa nduguye amzalie mrithi katika jina la ndugu yake. Hilo laonyesha kwamba ndoa hiyo haikuonwa kiasili au kihalisi kuwa mbaya au isiyo ya adili.—Law. 18:16; Kum. 25:5, 6.
Ndoa kati ya binamu wa karibu, ambao ni uhusiano wa karibu sana wa damu, haikukatazwa. Kuoa dada ambaye ni mtoto wa mzazi mmoja kulikatazwa, walakini hakukuwa na katazo la kwamba mwana hangeoa binti ya kambo, yaani, binti aliyelelewa na baba yake, wala si binti aliyezaliwa na wazazi wa mwana huyo.—Law. 18:11.b
MAMBO YA MAANA KWA WAKRISTO
Uhakika wa kwamba Wakristo hawako chini ya agano la Torati bila shaka haumaanishi kwamba ndoa yo yote kati ya washiriki wa jamaa moja, hata wawe wa karibu namna gani inakubaliwa na Wakristo. Ni jambo la kuangaliwa kwamba, kikizungumza juu ya zinaa za maharimu (incest), kitabu Encyclopaedia Britannica (Micropaedia, Kitabu cha 5, uku, 323) kinataja ndoa kati ya wazazi na watoto na kati ya ndugu na dada na kusema kwamba “zinaa za maharimu zinalaumiwa ulimwenguni pote na kwa kawaida huonwa kuwa jambo la kuchukiza.” Katika makala nyingine (Macropaedia, Kitabu cha 10, uku, 479) kinasema hivi: “Kanuni inayokaribia sana kuwa ya ulimwenguni pote inayopatikana katika utamaduni wote unaojulikana wa kibinadamu ni ule mwiko wa zinaa za maharimu—katazo la ngono kati ya mwanamume na mamaye, dada, binti, au wengine wa jamaa wanaotajwa waziwazi.” Kinasema (uku. 480) juu ya ‘utatu wa msingi’ mama, dada, binti wanaopatikana katika zinaa za maharimu za namna hiyo zinazokatazwa.
Tukigeukia Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yaliyoongozwa na Mungu, inaelekea kuwa wazi kwamba wakati mtume Paulo alipomwandikia Timotheo kwamba inampasa kushughulika na “wanawake wazee kama mama, wanawake vijana kama ndugu wa kike; katika usafi wote,” agizo lake lilipata nguvu katika uhakika wa kwamba kufanya ngono pamoja na mama au dada ya mtu kulionwa kuwa jambo lisilokubalika kabisa, kwa asili likiwa ni ufisadi. (1 Tim. 5:2) Na, kwa kuwa kama vile ambavyo tumekwisha kuona kwamba ngono za namna hiyo zinaonwa kama chukizo katika karibu kila mahali, ni wazi kwamba uhusiano kama huo hauwezi kutimiza agizo la Biblia, “ndoa na iheshimiwe na watu wote.”—Ebr. 13:4.
Ijapokuwa uwezekano wake wa kutokea ni mdogo sana, hakuwezi kuwa na shaka lo lote kwamba ye yote anayeingia katika uhusiano wa ndoa wa mzazi na mtoto au wa ndugu na dada bila shaka angeonwa kuwa asiyekubalika katika kundi la Kikristo la Mashahidi wa Yehova, na kwa hiyo, hangekubaliwa abatizwe isipokuwa auvunje uhusiano huo kwanza. Ye yote ambaye amekuwa mshiriki aliyebatizwa wa kundi na anayeingia katika uhusiano wa namna hiyo kwa kufaa angetengwa na ushirika wa kundi naye hangekubaliwa tena kundini isipokuwa kwa kuuvunja uhusiano huo.
UHUSIANO ULIO NJE YA WASHIRIKI WA JAMAA YA KARIBU
Namna gani juu ya uhusiano ulio nje ya washiriki wa jamaa ya karibu? Kwa kuwa agano la Torati haliwahusu Wakristo, haielekei kuwa na msingi wa kutosha wa Kimaandiko wa kushikilia sana jambo hilo, hata ingawa kadiri ndoa inavyokaribia uhusiano wa karibu zaidi wa damu, ndivyo inavyolipasa kundi kuonyesha waziwazi zaidi namna linavyoiona ndoa hiyo kuwa isiyofaa. Hapa kanuni ya Kimaandiko ya upendo inahusika sana, kwa kuwa inajulikana kwamba kadiri uhusiano wa damu unavyokaribiana ndivyo uwezekano unavyokuwa mkubwa zaidi wa watoto kuwa na kasoro za kuzaliwa. (Rom. 13:8-10) Tena, ni jambo la hakika kwamba, katika wakaaji wa mtaa fulani kwa kawaida “kuchukizwa na zinaa za maharimu kunapungua kadiri uhusiano wa damu unavyokuwa wa mbali zaidi.” (Encyclopaedia Britannica, Micropaedia, Kitabu cha 5, uku 323) Hivyo, ijapokuwa uhusiano fulani wa ndoa nje ya washiriki wa jamaa ya karibu huenda isihitaji mtu atengwe na ushirika wa kundi, bila shaka wazee wa kundi wapaswa kuangalia kadiri ya kukaribiana kwa jamaa za hao walio katika uhusiano huo wa ndoa, na vilevile maoni ya washiriki wa kundi na watu wa mtaa, na kuacha jambo hilo liwaongoze kuamua kama watu hao walio katika uhusiano huo wa ndoa ni mifano mizuri inayoweza kutumiwa kundini.
Ujamaa huenda usiwe uhusiano wa damu bali kupitia kwa ndoa. Kwa kufaa Mkristo anajaribu kuepuka jambo linaloweza kuchochea maoni mabaya ya watu wa nje kwa sababu ya kuvunja kanuni zilizoimarika sana kuhusiana na sehemu hii ya mambo. Kwa hiyo, ijapokuwa wakati watu wa ujamaa mmoja ambao uhusiano wao si wa damu wanapooana hakuwi na hatari za kuwa na watoto wenye kuzaliwa wakiwa na kasoro, hata hivyo bado kukaribiana kwa ujamaa wao kwaweza kuharibu heshima ya ndoa yao machoni pa watu. Kama vile ilivyokwisha kuonyeshwa, jambo hilo lapaswa kuhangaikiwa sana na Mkristo. (Ebr. 13:4) Kama vile alivyosema mtume, inatupasa tusitake ‘kuwa kikwazo’ kwa jirani zetu.—1 Kor. 10:32, 33, NW.
Kwa habari hii, namna gani juu ya kisa kinachoelezwa katika 1 Wakorintho 5:1? Hapa mtume anaeleza juu ya uasherati kati ya mwanamume na mke wa baba yake, kwa wazi mama wa kambo ya mwanamume huyo. Habari hiyo haielezi kwamba walioana, kwa hakika mtume huyo anaiita “zinaa [“uasherati,” NW],” (porneia). Habari hiyo haisemi kwamba baba ya mwanamume huyo alikuwa bado anaishi, ijapokuwa maneno katika 2 Wakorintho 7:12, yakitumiwa kuhusiana na jambo hilo, yangeonyesha kwamba alikuwa bado anaishi. Kwa hiyo inaonekana kwamba hakikuwa kisa kilichohusu ndoa bali kilihusu mwanamume akiishi katika uasherati pamoja na mamaye wa kambo. Walakini, ijapokuwa huenda ndoa isihusike, kwa kuwa Paulo ataja kisa hiki kuwa uasherati ambao ni “namna isiyokuwako hata katika Mataifa,” inakuwa wazi kwamba uhusiano wa jamaa uliokuwako uliufanya uasherati huo kuwa jambo lenye kuaibisha hata zaidi.1 Kor. 5:1.
KUENDELEZA USAWA UNAOFAA KATIKA MAONI YETU
Bila, shaka, si wajibu wa kundi la Kikristo kusisitiza kwamba kanuni zote zenye kutofautiana za ulimwengu zinazohusu zinaa zifuatwe kabisa kabisa, wala kutenda kama watekelezaji wa sheria za Kaisari zinazokataza ndoa za namna fulani (sheria ambazo nyingine zazo huzidi hata yale yaliyokatazwa na agano la Torati). Sheria za kibinadamu na ufafanuzi wazo wa neno “zinaa za maharimu” hazipatani bali hutofautiana sana. Katika jamii fulani, mwanamume anayeoa katika ukoo au kijiji au, katika visa fulani, hata katika kabila lake huenda akaonwa kama amefanya ndoa ya zinaa. Katika jamii nyingine, inakuwa kinyume cha hiyo naye mtu analaumiwa asipooa katika kabila au ukoo wake. (Encyclopaedia of Religion and Ethics ya Hastings, Kitabu cha 4, uku. 253) Katika jamii fulani za Mashariki, linaonekana kuwa jambo lisilofaa ikiwa watu wenye jina moja la jamaa wanaoana, hata ukoo wao uwe mbali namna gani. (Encydopaedia Britannica, Macropaedia, Kitabu cha 5, uku. 32) Katika nchi fulani au mikoa ndoa kati ya binamu zinakubaliwa, katika nchi na mikoa mingine hazikubaliwi kisheria.
Ijapokuwa mambo haya ya hakika hayatoi kanuni za adili kama zile zinazoongoza kwenye kukubalika au kutokubalika kwa mtu katika kundi la Kikristo au kutengwa nalo, zaweza kuwa na matokeo juu ya kama mtu aweza kutumiwa kama mfano mzuri kundini au hapana. Mengi yanategemea namna watu wanavyoona ndoa ya washiriki fulani wa ukoo mmoja, kama ni jambo lanaloonwa kuwa lenye kuaibisha sana au ni jambo linatojawa tu mara kwa mara.—1 Tim, 3:7, 10.
Inapokuwa kwamba watu waliingia katika ndoa hiyo kabla ya kubatizwa, nayo ndoa hiyo haihusu washiriki wa jamaa ya karibu na pengine ndoa hiyo imetokeza watoto, basi ingeelekea kwamba kanuni ya 1 Wakorintho 7:24 yaweza kutumiwa katika hali ya namna hiyo. Katika visa fulani huenda ndoa hiyo ikawa ya namna isiyoweza kukubaliwa kisheria katika sehemu hiyo. Ikiwa wanaohusika waweza kwenda katika mahali pengine ambako ndoa ya namna hiyo yaweza kukubaliwa kisheria, hilo laweza kuwa jambo lenye faida kwa vile laweza kusaidia kufanya ndoa hiyo iheshimiwe kwa kadiri fulani machoni pa wengine. Ikiwa hilo haliwezekani, nao wanaohusika wanatamani kubatizwa na kustahili katika mambo mengine, nafasi yaweza kutolewa kwao waweke sahihi kwenye hati ya kuonyesha azimio lao la kuendelea kuwa waaminifu katika ndoa yao hiyo. Huo ungeonwa kuwa wonyesho wao wa kuikubali ndoa yao na kuiona kuwa yenye kudumu mahali pa kuonyesha kwamba kundi linaikubali ndoa hiyo.
Bila shaka wale wanaohangaikia sana kuwa na kibali ya Yehova na baraka yake watajilinda wasifanye lo lote linaloweza kuleta suto juu ya Jina na Neno lake. Wajapowekwa huru na agano la Torati lililopewa kwa Waisraeli, Wakristo wa kweli watatii kwa bidii maneno ya mtume yaliyoongozwa na Mungu: “Uhuru wenu usiwe sababu ya kuufuata mwili, bali tumikianeni kwa upendo.”—Gal. 5:13.
[Maelezo ya Chini]
a Neno la Kiebrania linalotafsiriwa hivyo ni neno zimmah. Strong analieleza kuwa lamaanisha “mpango fulani, hasa mbaya.” Keil-Delitzsh asema hivi: ‘Uvumbuzi, ubuni halisi.’ Tafsiri ya Septuagint ilitumia neno la Kigiriki asebyma kwa neno hilo naye Liddell-Scott asema neno hili lamaanisha ‘tendo ovu au najisi, lenye kukufuru.’ Katika tafsiri ya Kiswahili ya Union Version limetafsiriwa “uovu mkuu.” Na katika tafsiri ya Kiingereza ya New World limetafsiriwa “mwenendo mpotovu.”
b Angalia kwamba orodha iliyoonyeshwa katika kitabu Aid to Bible Understanding, ukurasa wa 1041, inaonyeshwa kwa makosa kwamba ndoa za namna hiyo zilikatazwa. Kwa hakika andiko hilo (Mambo ya Walawi 18:11) lataja waziwazi kwamba huyo binti ni “binti ya mkewe baba yako,” hivyo si binti wa kulelewa. Ramani iliyo katika Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) wa Februari 1, 1975, ukurasa 73, kwa usahihi haikutia ndani ndoa ya mtu aliyeoa dada yake wa kambo kuwa ilikatazwa.