Mahubiri ya Mlimani—Sikuja Kutangua Bali Kutimiliza
KATIKA Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu alionyesha upendo wake mwingi sana na heshima nyingi kwa Neno la Mungu lililoandikwa. Alisema hivi: “Msidhani ya kuwa nalikuja kuitangua [T]orati au [M]anabii [yaani,Maandiko yote ya Kiebrania]; la, sikuja Kutangua bali kutimiliza.”—Mt. 5:17.
Kwa maneno na kwa matendo pia Yesu alijionyesha kuwa tofauti waalimu wa kidini Wayahudi wa siku zake. Alizungumza juu ya wakati ambao watu wasingemwabudu Mungu tena hekaluni katika Yerusalemu. (Yohana 4:21) Yeye aliyafananisha mafundisho yake na “divai mpya” ambayo huharibu “viriba vikuukuu.” (Luka 5:37) Vilevile Yesu alikula pamoja na “watoza ushuru na wenye dhambi” na kufanya miujiza ya kuponya wakati wa siku ya Sabato kila juma. (Marko 2:13-17; 3:1-5) Hatua hizi hazikuvunja sheria yo yote ya Mungu; lakini zilipingana na mapokeo ya Kiyahudi ambayo yalionwa kuwa ya maana zaidi kuliko Maandiko ya Kiebrania.a Kwa kuwa walimwona Yesu kuwa mvunja sheria ya Mungu, Mafarisayo na wafuasi wa Herode walikuwa wakifanya hila ya kumwua hata kabla hajayatoa Mahubiri yake ya Mlimani yajulikanayo sana.—Marko 3:6.
Hata hivyo, Mwana wa Mungu aliwahakikishia wasikilizaji wake kwamba hakuja “kuitangua” Torati. Yeye hakuziasi amri zayo wala kutangaza sehemu yo yote yayo kuwa haikuwahusu Waisraeli. Badala yake, Yesu alikuja “kutimiliza” sheria hiyo ya Mungu. Akiwa mtu asiye na dhambi, aliifuata kabisa, hata ‘kufikia mauti, naam, mauti ya mti wa mateso.’ (Flp. 2:8, NW; Ebr. 4:15; 1 Pet. 2:22) Vilevile kifo chake cha dhabihu kilitimiza mifano ya unabii iliyotolewa na mpango wa Torati wa dhabihu za wanyama.—Dan. 9:26, 27; Ebr. 10:1-9.
Yesu alitimiliza si mambo ya Torati iliyoandikwa peke yake, bali pia roho iliyoonyeshwa na Torati hiyo. Ijapokuwa Torati ilikataza matendo yenye dhambi, Yesu alikataza maelekeo yanayotokeza matendo ya namna hiyo. Kwa mfano, uuaji na uzinzi ulivunja sheria ya Mungu; walakini Yesu alionyesha kwamba kuendelea kumkasirikia mtu na kumtazama mwanamke kwa tamaa ni maelekeo ya akili yanayoongoza kwenye makosa ya namna hiyo. (Mt. 5:21, 22, 27, 28; Yak. 1:13-15) Na zaidi ya hayo, dhabihu aliyoitoa Yesu kwa kupenda ya uhai wake wa kibinadamu kwa faida ya wanadamu ilikuwa wonyesho wa upendo wa kiasi cha juu zaidi, ambao Biblia inauita “utimilivu wa sheria.”—Rum. 13:8-10; linganisha Yohana 15:13.
Kisha katika mahubiri yake, Yesu alisema: “Amin, nawaambia, Mpaka mbingu na nchi zitakapoondoka [Ni vyepesi zaidi mbingu na dunia kuondolewa, NW]— yodi moja wala nukta moja ya [T]orati haitaondoka, hata yote yatimie.”—Mt 5:18.
Kama inavyoonyeshwa katika tafsiri ya Kingdom Interlinear, hapa Yesu alitumia neno “Amin,” linalomaanisha “hakika,” “na iwe hivyo.” Akiwa Mwana wa Mungu aliyetiwa mafuta, Masihi aliyeahidiwa, bila shaka angaliweza kuhakikisha ukweli wa semi zake.—Linganisha 2 Wakorintho 1:20; Ufunuo 3:14.
Sheria ya Mungu itatimia mpaka ‘herufi iliyo ndogo zaidi au nukta moja ya herufi.’ Katika alfabeti ya Kiebrania iliyokuwako wakati huo, herufi ndogo zaidi ilikuwa yodi. Herufi fulani za Kiebrania zilikuwa na mstari mdogo sana sana uliokwenda upande au ncha. Waandishi na Mafarisayo waliiona kuwa ya maana sana, si maneno na herufi za sheria ya Mungu tu, bali pia hiyo mistari midogo iliyokwenda upande au ‘nukta zilizo ndogo zaidi.’ Mapokeo ya waalimu wa kidini wa Kiyahudi yanamwonyesha Mungu kama kwamba akisema: “Sulemani na maelfu wanaofanana naye watapita, walakini ncha moja yayo (Torati [vitabu vitano vya kwanza vya Musa]) sitairuhusu ifutwe.”
Uwezekano wa kukosa kutimia ulikuwa mdogo sana hata kwa jambo lililo dogo zaidi la sheria ya Mungu hata kwamba ‘ingekuwa vyepesi mbingu na dunia ziondoke.’ Hii ilikuwa sawasawa na kusema kwamba ‘halitakosa kutimia kamwe,’ kwa maana Maandiko yanaonyesha mbingu na dunia halisi zitadumu milele.—Zab. 78:69; 119:90.
Yesu alikazia zaidi heshima yake nyingi kwa sheria ya Mungu, akisema: “Basi mtu ye yote atakayevunja amri moja katika hizi zilizo ndogo, na kuwafundisha watu hivyo, ataitwa mdogo kabisa katika ufalme wa mbinguni; bali mtu atakayezitenda na kuzifundisha, huyo ataitwa, mkubwa katika ufalme wa mbinguni.”—Mt. 5:19.
Mtu aweza ‘akavunja’ mojawapo ya amri hizi kwa kukosa kuzitii kwa makusudi. Au, angeweza kufanya lililoonwa kuwa baya zaidi, yaani, kufundisha Wayahudi wenzake walio chini ya Torati kwamba nyingine za amri zayo hazikuwahusu. Wakati agano la Torati lilipokuwa likitenda kazi, lilikuwa wonyesho wa mapenzi ya Mungu kwa watu wake. Kuvunja au kufundisha mambo yaliyo kinyume cha amri ambazo huenda wengine waliziona kuwa na maana “ndogo” kungekuwa kumwasi Mungu.—Linganisha Yakobo 2:10, 11.
Torati ilitolewa ili kuwaongoza Waisraeli kwa Masihi, ambaye angekuwa mtawala mkuu katika ufalme wa Mungu. (Gal. 3:24; Isa. 11:1-5; Dan. 7:13, 14) Kwa hiyo, kuhusiana na kuingia katika ufalme wa Mungu, watu waliovunja amri za Mungu wangeitwa ‘wadogo.’ Wao wasingeingia katika ufalme huo hata kidogo. —Mt. 21:43; Luka 13:28.
Kwa upande mwingine, wale walioitii torati ya Musa kwa kadiri ya uwezo wao “wangeitwa ‘wakubwa’ katika ufalme wa mbinguni.” Wao wangekuwa namna ya watu waliokubali Yesu kuwa ndiye Masihi na ambao baadaye waliitwa waushiriki utawala wa Ufalme pamoja naye. (Luka 22:28-30; Rum. 8:16, 17) Linalopendeza ni kwamba, Maandiko hutaja wafalme kuwa “watu wakuu.”—Mt. 25:6; Luka 1:32.
Halafu Yesu alitoa usemi ambao huenda ukawa uliwashtua wasikilizaji wake: “Nawaambia ya kwamba, haki yenu isipozidi hiyo haki ya waandishi na Mafarisayo, hamtaingia kamwe katika ufalme wa mbinguni.”—Mt. 5:20.
“Waandishi” wa siku za Yesu walikuwa jamii ya wanaume wenye elimu ya Torati. Ijapokuwa huenda wengine wao walikuwa Masadukayo, waandishi wengi walikuwa wa “madhehebu” ya Mafarisayo, ambao madai yao kuhusiana na usafi wa kisheria, utoaji wa zaka na matakwa mengine ya kidini yalizidi matakwa ya Musa.—Matendo 15:5.
Viongozi hao wa kidini walikuwa na maoni ya kisheria yasiyofaa juu ya kupata haki. Waliamini kwamba ilitokana tu na matendo ambayo kwa halisi yalilingana na yaliyoandikwa katika torati. Kulingana na mapokeo ya Kiyahudi, kila wakati alipotii amri moja, alipata “sifa njema.” Iliaminiwa kwamba kila kosa lilitokeza “deni.” Ilifahamika kwamba wingi wa deni ulimfanya mtu “mwovu.”
Hata hivyo, maoni hayo ya kisheria, hayakupatana na kanuni ya Mungu ya yaliyo haki. (Rum. 10:2, 3) Fikira hazikukaziwa katika kusitawisha sifa kama vile upendo, haki, upole, fadhili na uaminifu. Hali Mungu huziona kuwa za muhimu zaidi kuliko kutii kwa halisi maoni ya kisheria. (Kum. 6:5; Law. 19:18; Mik. 6:8) Akiwa na sababu nzuri Yesu alitamka hivi: “Ole wenu waandishi na Mafarisayo, wanafiki! kwa kuwa mnalipa zaka za mnanaa na bizari na jira, lakini mmeacha mambo makuu ya sheria, yaani, adili, na rehema, na imani.”—Mt. 23:23; linganisha Luka 11:42.
Haki ya Wakristo yapaswa izidi “hiyo haki ya waandishi na Mafarisayo.” Kulingana na aliyosema Yesu, wale wote wanaotaka kuwa waabudu wa kweli wa Mungu lazima wamwabudu “Baba katika roho na kweli.” (Yohana 4:23, 24) Lazima ibada yao iwe, si matendo ya nje-nje tu ya utawa yanayopatana na orodha ya sheria, bali “katika roho,” ikiongozwa na mioyo yenye kujaa imani na upendo.—Mt. 22:37-40; Gal. 2:16.
a Orodha ya kale ya sheria za Kiyahudi iitwayo The Mishnah inasema hivi: “Mkazo mwingi zaidi unahusu [utii wa] maneno ya Waandishi kuliko [kutii] maneno ya Sheria [iliyoandikwa].”—Kijitabu Sanhedrin, 11:3, kilichotafsiriwa na Herbert Danby.