Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w79 1/1 kur. 3-6
  • “Onjeni Mwone ya Kuwa (Yehova) yu Mwema”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Onjeni Mwone ya Kuwa (Yehova) yu Mwema”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • YALIYOMPATA DAUDI
  • SAWA NA WATUMISHI WOTE WA MUNGU
  • JE! KUISHI “MAISHA MEMA” KUNATOSHA?
  • SABABU INAYOFAA YA KUJISIFU
  • KUTIA WENGINE MOYO
  • UPAINIA UNAWEZA KUTUSAIDIA TUONJE
  • FAIDA ZENYE KUENDELEA
  • JE! UNAKUFAA WEWE?
  • Yehova Ategemeza Jeshi Lake la Watumishi wa Wakati Wote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Utumishi wa Painia—Je, Wakufaa Wewe?
    Huduma Yetu ya Ufalme—1998
  • Kutembea kwa Nafsi Yote katika Njia ya Uzima
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Baraka za Huduma ya Painia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
w79 1/1 kur. 3-6

“Onjeni Mwone ya Kuwa (Yehova) yu Mwema”

MWALIKO huu​—“onjeni mwone ya kuwa [Yehova] yu mwema,”—​ulitolewa na mwandikaji wa zaburi za Biblia Daudi. (Zab. 34:8) Je! wewe umekubali mwaliko huo? Unawezaje kufanya hivyo?

Kwanza, ni lazima tujue linalosemwa katika Neno la Mungu. Sababu ni kwamba katika Biblia ndimo Yehova anamotuambia juu ya mambo mema atakayowatolea watumishi wake. “Karama ya Mungu ni uzima wa milele,” yasema Biblia. (Rum. 6:23) Walakini Mungu anawatolea watumishi wake zaidi ya hayo. Vilevile yeye anawaahidia amani ya akili na uradhi wa kweli katika maisha, hata katika wakati huu.

Basi, ‘tunaonjaje’ na kuona kwamba kwa kweli Yehova atatupa vitu vizuri namna hiyo? Tunahitaji kumtii katika unyenyekevu, kama anavyotukaribisha: “Mwanangu, usiisahau sheria yangu, bali moyo wako uzishike amri zangu.” (Mit. 3:1) Kwa kuishi maisha zetu kulingana na sheria na amri za Yehova, ni kama kwamba, tunaonja na kuona kama hiyo itakuwa na matokeo mema kwetu.

YALIYOMPATA DAUDI

Mtunga zaburi Daudi alifanya hivyo. Ni kweli kwamba yeye alifanya makosa. Lakini Daudi alikuwa na moyo wa kupenda kumtumikia Yehova, naye kwa kutii aliweka mapenzi ya Mungu mbele maishani mwake. Hili halikuwa jambo jepesi kulifanya sikuzote. Kwa kweli, lilimhatirisha sana Daudi nyakati nyingine.

Kuna wakati ambapo Mfalme Mwisraeli Sauli, alitaka kumwua Daudi, kwa sababu ya wivu. Kwa hiyo Daudi alilazimika kukimbilia nchi ya adui zake Wafilisti. Humo alijifanya mwenda wazimu, akaweza kuponya maisha yake. Daudi alitunga zaburi hii ya 34 wakati huo, maisha yake yalipokuwa katika hatari kubwa. Angalia namna kufahamu hali hizi kunavyoongeza maana katika maneno hayo:

“Nalimtafuta [Yehova] akanijibu, akaniponya na hofu zangu zote. Malaika wa [Yehova] hufanya kituo, akiwazungukia wamchao na kuwaokoa. Onjeni mwone ya kuwa [Yehova] yu mwema; mateso ya mwenye haki ni mengi, lakini [Yehova] huwaponya nayo yote.”​—Zab. 34:4, 7, 8, 19.

Mara nyingi kumtumikia Yehova kunamletea mtu lawama na mateso, kama mambo yaliyompata Daudi yanavyoonyesha. Kwa kuwa hivyo ndivyo ilivyo, huenda watu wengine wakasita kujitoa kabisa katika utumishi wa Mungu. Lakini Daudi, akisema kutokana na yale yaliyompata, anatusihi “[tuonje tuone] ya kuwa [Yehova] yu mwema.” Ndiyo, Daudi alijua kwamba, ijapokuwa magumu yanayopatikana, watumishi wa Mungu wangeweza kuona mkono wa ulinzi wa Yehova wenye nguvu pamoja na “amani ya Mungu ipitayo akili zote.”​—Flp. 4:7.

SAWA NA WATUMISHI WOTE WA MUNGU

Haya yamewapata watumishi wa Mungu katika wakati wote wa historia. Ebu angalia habari katika Waebrania sura ya 11 juu ya watu wa imani katika nyakati zilizotangulia Ukristo; soma habari katika zile Injili nne juu ya maisha ya mtumishi wa Yehova aliye mkuu zaidi, Yesu Kristo; fikiria yaliyowapata mitume Wakristo kama yalivyoandikwa katika kitabu cha Biblia cha Matendo. Tunaona nini?

Tunaona hili: Kwamba kumtumikia Yehova mara nyingi kunatokeza kila namna ya taabu dhihaka za kila namna, mateso na magumu, nyakati nyingine hata kifo chenye maumivu mengi, kama ilivyokuwa kwa habari ya Yesu. Hata hivyo watumishi hawa wa Mungu walikuwa na furaha. Walifurahia amani ya ndani na uradhi kwa kuwa walijua kwamba walikuwa wakimpendeza Baba yao wa kimbinguni, na kwa kujua kwamba wangepokea zawadi yake ya uzima wa milele. Soma, kwa mfano, Matendo 5:40-42.

Tua ujiulize hivi: Mimi nataka nini maishani? Je! mradi wangu ni kuwa mtumishi mwaminifu wa Yehova? Au je! mwendo wangu wa maisha unaonyesha kwamba faida nyingine ni za maana zaidi kwangu? Katika maneno yanayotangulia katika Zaburi 34, Daudi alionyesha nia ambayo sisi sote tunapaswa kuwa nayo: “Nitamhimidi [Yehova] kila wakati, sifa zake zi kinywani mwangu daima.” (Zab. 34:1) Je! sisi, pia, ndiyo tamaa ya moyo wetu? Je! sisi tunasukumwa tutumie afya yetu, uwezo na nguvu tumpe Yehova sifa? Tunaweza kufanya nini ili tumhimidi na kumsifu Yehova?

JE! KUISHI “MAISHA MEMA” KUNATOSHA?

Watu wengine wanaamini kwamba kuishi “maisha mema” tu​—kuwafadhili jirani zao, kuwapenda ndugu na dada zao, kuweka nyumba safi, kusitawisha utu mwema—​ndiyo tu yanayohitajiwa katika kumhimidi na kumsifu Yehova. Lakini, kwa kweli, mengi yanahusika. Sifa lazima zitoke kinywani, kama alivyosema Daudi. Kumsifu Yehova katika njia hii ni takwa la pekee la Wakristo wa kweli. Yesu Kristo alionyesha hili kwa kufanya shughuli (kazi) iliyolitukuza jina na ufalme wa Baba yake.​—Luka 4:43.

Ndipo, karibu na mwisho wa maisha yake ya kidunia, Yesu alisema hivi: “Habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote.” (Mt. 24:14, NW) Kuhubiri huku kungefanywa na nani? Mtume Petro alimwambia Kornelio, mkuu wa jeshi na nyumba yake hivi: “[Kristo] akatuagiza tuwahubiri watu na kushuhudia [kabisa].”​—Matendo 10:42.

Je! amri hii iliwapasa mitume tu pamoja na wazee wengine Wakristo? Hapana, Wakristo wote walipaswa kumwiga Kristo, wakifanya kazi ya kuhubiri kama alivyofanya yeye. Ili kutimiza kazi ya kuhubiri katika dunia yote kama alivyosema Yesu jitihada za Wakristo wote​—wanaume, wanawake na watoto zinahitajiwa. Nayo jitihada hii ya wote inaonyeshwa kati ya Mashahidi wa Yehova​—wote wanashiriki pamoja katika kazi hii kubwa ya kuutangaza Ufalme.

Wale ambao hali zao zinawaruhusu kushiriki zaidi katika kazi hii ya kuhubiri, kuna mpango wa utumishi wa “painia.” Painia ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova ambaye anaweza kutumia saa 90 kila mwezi, au saa 1,000 au zaidi kwa mwaka, katika kazi ya kuhubiri. Katika mwaka uliopita zaidi ya Mashahidi 119,000 kwa wastani kila juma, waliweza kufanya upainia. Lo! utumishi wa maana namna gani walioufanya! Nayo maoni ya mapainia hawa pamoja na watumishi wengine wa Mungu yanapaswa kuwa nini?

SABABU INAYOFAA YA KUJISIFU

Daudi anatusaidia tujue hili, anapoendelea katika Zaburi ya 34 hivi: “Katika [Yehova] nafsi yangu itajisifu.” (Zab. 34:2) Kumjua Yehova na kuwa mmoja wa watumishi wake bila shaka ni jambo linalofaa mtu ajisifie. Bila shaka, kujisifu huku lazima kuwe bila ya mtu kujionyesha haki yake mwenyewe, kwa kuwa hatujisifu katika sisi wenyewe, bali kama alivyosema Daudi, “katika [Yehova].”​—Tazama pia Wagalatia 6:14.

Tunaweza kujisifia mambo ambayo Yehova ametufanyia, jinsi ametuhifadhi, akatuongoza na kuturuzuku. Kwa upande mwingine, isingefaa kujisifu kwa sababu huenda, hali zikaturuhusu tushiriki zaidi katika kazi ya kuhubiri. Mtume Paulo alisema hivi: “Maana, ijapokuwa naihubiri injili, sina la kujisifia; maana nimewekewa sharti.”​—1 Kor. 9:16.

KUTIA WENGINE MOYO

Tena, kwa kumthamini sana Yehova katika moyo wake, Daudi alisema: “Mtukuzeni [Yehova] pamoja nami, [enyi watu,] na tuliadhimishe jina lake pamoja.” (Zab. 34:3) Je! wewe, kama Daudi, unawatia wengine moyo washiriki katika kumsifu Yehova? Mara nyingi, wanalohitaji watumishi wa Mungu ili waanze utumishi wa painia ni kutiwa moyo tu. Ebu angalia mifano hii ya watu wanaofurahi sana kwa sababu waliweza kuanza.

Don na Earlene Steele waliandika hivi: “Tulikuwa na mashaka juu ya kuingia katika [utumishi] wa wakati wote wa painia kwa sababu tuliwaza kwamba tulihitaji kujiwekea akiba ya fedha. . . . tuliondoa wazo hilo tukaiandikia Sosaiti tukaiambia kwamba tulikuwa na akiba ya kutusaidia tuendelee kwa miezi miwili hivi! . . . kwa msaada wa Yehova, tumeweza kuendelea, si kwa miezi miwili tu, bali kwa miaka 27.”​—The Watchtower, 1971, kur. 186-190.

Paul Wrobel alisema hivi: “Walakini sasa [katika mwaka 1946] ugonjwa fulani ulikuwa ukitokea na ulielekea kunizuia nisiingie katika [Utumishi] wa wakati wote. Dakt. wangu alitabiri kwamba baada ya miaka miwili nigetazamia kupooza katika upande wa kuume wa kiweo changu. . . . Niliamua kutumia hiyo miaka miwili katika [utumishi] wa wakati wote nifanye yote niwezayo. Kwa wakati huu, miaka 27 imepita!”​—The Watchtower, 1973, kur. 376-379.

Baada ya kutumia makumi fulani, ya miaka katika utumishi wa wakati wote, Heinrich Dickmann, alikazia kwamba “magumu yote, yawe ya mwilini, yameondolewa na fadhili zisizostahilika za Yehova . . . kulitumaini jina la Yehova kunatoa usalama kweli kweli.”​—The Watchtower, 1972, kur. 395-39

Maelfu, ndiyo, makumi ya maelfu ya mapainia, ambao wameonja na kuona kwamba Yehova ni mwema, wanaweza kujiunga na Daudi katika kutoa mwaliko huu: “Mtukuzeni [Yehova] pamoja nami, [enyi watu,] na tuliadhimishe jina lake pamoja.” (Zab. 34:3) Si kwamba tu mapainia hawa wanawatia watu moyo wanaojifunza nao Biblia wafanye hivyo, bali pia, baada ya kuonja wema wa utumishi wa painia wanapendekeza utumishi wa painia kwa watumishi wengine wa Mungu.

UPAINIA UNAWEZA KUTUSAIDIA TUONJE

Utumishi wa painia unaweza kutusaidia tuuonje zaidi wema wa Yehova. Kwa kuzungumza juu ya mambo ya kiroho kila siku, tunaongeza maarifa. Kisha, hiyo nayo, inaongeza imani yetu. Tunawezeshwa zaidi kutumia shauri la Biblia katika kuyashinda magumu. Tunajifunza kumtegemea Yehova kwa ukamilifu zaidi, tukifanya mambo kwa uwezo wake, si kwa uwezo wetu.

Vilevile, kwa kuwa tumechagua kujinyima mambo fulani ya kimwili ili tuuchukue utumishi wa painia, tunakuja kutegemea zaidi msaada wa Yehova kwa habari ya mambo ya kimwili. Daudi alitaja juu ya namna tunavyomtegemea Yehova aliposema kwamba “wanasimba hutindikiwa, huona njaa; bali wamtafutao [Yehova] hawatahitaji kitu cho chote kilicho chema.”​—Zab. 34:10.

Yesu Kristo aliunga mkono zaburi hii ya Daudi kwa kuwaambia wanafunzi wake hivi: “Msisumbukie maisha yenu, mle nini au mnywe nini; wala miili yenu, mvae nini. . . . Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa.” (Mt. 6:25-33) Kwa hiyo, wale wote wanaotafuta kwanza Ufalme, wawe wako katika utumishi wa painia au hapana, wana ahadi ya Mwana wa Mungu mwenyewe kwamba Yehova atawatimizia mahitaji yao ya mambo ya kimwili. Je! sisi tungetazamia kupata ahadi kutoka chanzo kinachotegemeka zaidi kuliko hicho?

Hata kwa habari ya mwili, utumishi wa painia unaweza kutusaidia tuonje kwa ukamilifu zaidi wema wa Yehova. Hewa safi, mazoezi ya maungo, kujisikia kutimiza jambo fulani pamoja na ushirika mzuri yote hayo yanaweza kusaidia kuleta afya njema.

Mithali ya Kijeremani inasema hivi: “Anayepumzika atachakaa.” Watu wengi ‘wanaopumzika’ baada ya kuacha kazi wamejilinda ‘wasichakae’ kwa kuingia katika utumishi wa painia. Ebu fikiria, kwa mfano, painia mmoja katika Berlin ya Magharibi, Ujeremani, ambaye akiwa na umri wa miaka 86 alimwuliza daktari wake kama lingekuwa jambo la hekima kuacha utumishi wa painia. “Usiache,” akajibu daktari. “Ukiacha, utakufa.” Kwa hiyo leo, akiwa na umri wa miaka 92 ndugu yetu Mkristo bado anaendelea katika utumishi wa painia. Anaeleza hivi: “Nimeamriwa na daktari nisiache upainia.”

FAIDA ZENYE KUENDELEA

Watu wengi wamefanya upainia uwe kazi yao ya maisha baada ya kuuanza. Hili ni jambo lenye kusifika. Wengine wameweza kuufurahia kwa kitambo tu. Hata hivyo hawana la kusikitikia. Uamuzi wao wa kuacha utumishi wa painia kwa sababu ya hali kubadilika, unaweza kuwa si wenye kufahamika tu na watu, bali pia uwe unapatana na Maandiko. Je! waliupoteza wakati waliotumia katika upainia? Hata kidogo.

Ikiwa walifanya utumishi wa painia wakiwa na makusudi yanayofaa na wakiwa na tamaa ya kupata maendeleo ya kiroho, utakuwa umewasaidia kusitawisha hali ya kuwa na maoni ya kiroho zaidi katika maisha. Utakuwa umewasaidia wawe na usawa. Huenda wakawa wamejifunza masomo ambayo yatawasaidia katika maisha yao ya baadaye, mambo kama kujua namna ya kutumia wakati vizuri, namna ya kutumia fedha na namna ya kuridhika na mambo ya lazima ya maisha. Unaweza kusaidia vijana sana wawe wenzi bora wa ndoa na wazazi bora kuliko vile wangeweza kuwa. Ndiyo, utumishi wa painia unaweza kuwa na faida zenye kuendelea.

JE! UNAKUFAA WEWE?

Yehova anaonyesha wema wake kwa watu wake wote; si wa wale tu walio katika utumishi wa painia. Kwa hiyo, wale wanaouchukua wakiwa na sababu nzuri hawapaswi kupatwa na woga kwamba watapoteza kibali ya Yehova. Lakini kila mmoja wetu apaswa kujichunguza kwa unyofu. Je! wewe unasema, “Roho inapenda, bali mwili ni dhaifu”? Lakini je! kweli roho inapenda? Na tuepuke kutumia udhaifu wa mwili kama sababu ya kutopenda kwa roho.

Ikiwa baada ya kufikiria kwa sala bado unasita, basi kumbuka maneno ya Malaki 3:10: “Mkanijaribu kwa njia hiyo, [Onjeni mwone!] . . . mjue kama sitawafungulia madirisha ya mbinguni, na kuwamwagieni baraka, hata isiwepo nafasi ya kutosha.” Ni nani angetaka kukataa mwaliko kama huo, bila kuwa na sababu nzuri?

Na kwa habari ya wale wasioweza kuchukua utumishi wa painia sasa, kumbukeni hili: Kila mmoja wetu anaweza kumwabudu Yehova katika njia iliyo kamili zaidi kwa kujitoa na kumtumikia kwa nafsi yote. Kwa hiyo, endeleeni kuonyesha roho hiyo nzuri ya painia! Endeleeni kumtumikia Yehova kwa nafsi yote nanyi mtaendelea ‘kuonja na kuona kwamba Yehova ni mwema.’

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki