Namna Imani Ishindayo Inavyoweza Kukuhusu Wewe
ZAIDI ya Makusanyiko ya Mataifa Yote 100 ya “Imani Ishindayo’’ ya Mashahidi wa Yehova yalipangwa yafanywe 1978 na 1979 katika miji mikubwa kuzunguka ulimwenguni pote. Zaidi ya watu 1,700,000 walikuwa wamekwisha hudhuria makusanyiko hayo kufikia Septemba 1, 1978 na mfuatano wa makusanyiko uliendelea baada ya hapo.
Kusudi la makusanyiko hayo ni nini? Yalifanywa ili kujenga imani. Si imani tu bali imani ishindayo—inayotajwa na mtume Mkristo Yohana aliyeandika hivi: “Huu ndio ushindi ambao umeshinda ulimwengu, imani yetu.”—1 Yohana 5:4, The Bible in Living English.
Imani hii ishindayo imegeuza maisha ya maelfu ya watu. Inaweza kukugeuza wewe pia, hata kama vile ilivyogeuza wengine. Angalia namna hii ilivyo kweli tuchunguzapo kwa ufupi sehemu fulani za “Imani Ishindayo” Makusanyiko ya Mataifa Yote katika nchi za Ulaya.
IMANI YASHINDA VIZUIZI NA MAGUMU
Kwa wengine, kuwapo kwao kwenye makusanyiko haya kulihitaji waonyeshe imani na kushinda vizuizi. Bila shaka umbali haukuwa kizuizi kisichoshindika. Ili kuja kusanyikoni katika Lille, Ufaransa, mhudhuriaji kijana kutoka Poland alisafiri maili 750 (kilometres 1,200) kwa baisikeli katika siku sita.
Mashahidi kutoka Poland walihudhuria kusanyiko katika Copenhagen, Denmark. Hii ilikuwa rahisi zaidi kwa sababu ya kuanzishwa karibuni kwa safari ya meli ya abiria ya moja kwa moja kutoka Svinoucie mpaka mji mkuu wa Denmark. Hata hivyo, safari hiyo iliwagharimu kila mmoja wao malipo (Mshahara) ya mwezi mzima. Walipata vyeti vya kusafiria ingawa walitoa sababu ya safari yao kuwa “kuhudhuria kusanyiko la Mashahidi wa Yehova katika Denmark.” Hata hivyo, ili wapate kutoka Poland walihitaji kuwa na mwaliko pamoja na cheti kilicholipiwa malipo yake katika nchi ya ng’ambo, nao ndugu wa Denmark walitoa vitu hivyo. Licha ya kufurahia kusanyiko kubwa lenye waamini wenzao wengi, wahudhuriaji hawa walifaidika na programu ya siku mbili na nusu katika lugha yao, kutia na michezo mitatu ya kuigiza ya Biblia iliyotolewa kwa kutumia utepe na picha. Pamoja na wahudhuriaji Wazungu, Waspania na Wayugoslavia, ndugu hao wa Poland waliongezea hali ya pekee na kulifanya kusanyiko la Copenhagen kuwa la mataifa yote. Siku mbili za programu ya kusanyiko zilifanywa katika lugha za Kigiriki, Kispania na Kikroati. Kwa hiyo, hata vizuizi vya lugha vilishindwa.
Mume na mke wenye watoto 11 walitaka kuandamana na Mashahidi wengine kutoka visiwa vya Azores na kuhudhuria kusanyiko katika Lisbon, Ureno. Lakini wangepata wapi fedha? Wengine wa watoto walio wakubwa zaidi walisaidia kukusanya fedha kwa muda wa miezi kadha kabla ya kusanyiko hilo. Malipo ya tiketi za ndege, chakula na mambo mengine kama hayo yalikuwa zaidi ya shilingi 8,305.00 (Z2,491.50), hizo ni fedha nyingi sana kwa watu hawa maskini wa visiwani. Walakini walishinda vizuizi hivyo vya kiuchumi kwa kuonyesha imani katika Yehova, na jamaa yote ya watu 13 ilikuwapo kwenye kusanyiko la Lisbon.
Vilevile waokokaji wa kambi za mateso za Nazi walikuwako kwenye “Imani Ishindayo” Makusanyiko ya Mataifa Yote. Mashahidi wawili waliohudhuria kusanyiko katika Burussels, Ubelgiji, walikuwa wangali na mavazi yao yenye mistari. Waliyavaa kwa ajili ya wahudhuriaji wa kipindi cha lugha ya Kiingereza. Mwanamume mmoja ambaye sasa ni mwangalizi wa Kikristo alikuwa na umri wa miaka mitano baba yake alipokamatwa katika mwaka 1941, na angali anakumbuka kwamba alimwuliza mama yake angekaa muda mrefu namna gani wakati alipokamatwa, kwa sababu yeye alifikiri kwamba alikuwa anaenda kwa shughuli (kazi) za kawaida. Yeye hakumwona tena mpaka ilipo-pita miaka minne. Walakini imani ishindayo iliyashinda magumu na mateso yao.
Mume na mke wazee waliletea wahudhuriaji waliokusanyika Helsinki, Finland salamu kutoka Berlin Magharibi. Wote wawili walikuwa wahubiri wa Ufalme wa wakati wote na walikuwa wametumikia katika cheo hicho kwa zaidi ya jumla ya miaka 100 wote wawili! Wasikilizaji walinyamaa wakati mume na mke hawa wachangamfu walipokuwa wakieleza mambo waliyoyaona. Mume huyo alikuwa mshiriki wa Betheli (wafanya kazi katika afisi ya tawi ya Sosaiti) katika wakati wa utawala wa Hitler, naye alikuwa amekamatwa na askari wa Gestapo, na mwishowe akafungwa kwenye kambi ya mateso ya Sachsenhausen pamoja na ndugu wengine 600. Alipofunguliwa mwishoni mwa Vita ya Pili ya Ulimwengu, alitumikia tena katika Betheli. Mke wake alikuwa amefungwa vilevile. Baada ya ndoa yao, wote wawili walijipata katika kambi ya kifungo ya Kikomunisti. Pamoja wamefungwa gerezani miaka 41! Je! walionekana wameshuka moyo au kuvunjika moyo? Hata kidogo! Ndugu huyo alisema hivi: “Kwa pendeleo hili la pekee tunamshukuru Yehova.” Ndiyo, walikuwa wameteseka kwa kutokuwamo kwa Kikristo lakini imani yao ilishinda.
Kweli kweli, walio na imani ishindayo wanashinda vizuizi vikubwa sana, wanavumilia magumu na hawashindwi na watesi wao. Hawasiti, bali, ‘wana imani inayookoa nafsi.’ (Ebr. 10:38, 39) Imani ishindayo yaweza kuwa na matokeo ayo hayo maishani mwako.
IMANI INA NGUVU ZINAZOBADILI MAISHA
Lakini Je! imani inageuza tabia au mwenendo wa mtu mmoja mmoja? Gazeti la Kifaransa Le Soir lilitofautisha utaratibu wa kusanyiko la Kikristo lililofanyiwa mjini Marseilles na mchafuko wa kawaida unaoonekana katika uwanja wa michezo walioutumia. Lilisema: “Watu hao ni wenye amani na urafiki, tayari kuzungumza. . . . Hamna mchafuko wo wote ambao ni kawaida ya kundi la watu. Wote wanakaa kimya vitini vinavyoletwa kwa ajili ya tukio hilo. Hakuna mtu ye yote anayetembea-tembea au kukanyaga-kanyaga nyasi. Hawa si wenda wazimu wa kidini wenye kupiga mayowe, bali ni watu wanaozungumza kwa upole. Wamepata lengo lao maishani, kweli yao pamoja na Mashahidi wa Yehova.”
Likitoa maelezo juu ya “Imani Ishindayo’’ Kusanyiko la Mataifa Yote katika Rumi, gazeti la ltalia Paese Sera liliwataja Mashahidi kama watu wenye “adabu nzuri” na “mwenendo mwema.” Vilevile, juu ya mahali pa kusanyiko, gazeti II Messaggero la Rumi lilieleza hivi: “Hakukuwako na vipande vya karatasi na takataka ambayo, inahuzunisha kusema, inaonekana katika mikutano ya watu wengi inayofanyiwa nchini mwetu.” Hii ilisemekana kuwa “dalili ya utaratibu wa utumishi wa uchukuaji wa takataka, na vilevile kulelewa vizuri kwa wale waliohudhuria.”
Kwa kweli, sifa yote ya mwenendo unaotamanika au wa kumwogopa Mungu lazima imwendee Yehova Mungu. Imani katika yeye pamoja na utumiaji wa Maandiko maishani ndizo zimebadili wale ambao wamekuwa Wakristo wa kweli. (Rum. 12:2; 1 Kor. 6:9-11) Gazeti la Kifaransa Le Dauphiné libéré lilisema hivi: “Na tuondoe wazo lo lote la mfanya kiinimacho anayekugeuza kwa maneno machache ya ulozi na ufito. Hapana, Mashahidi wa Yehova hawapendezwi na kubadilisha ‘ubora’ wa imani yenye msingi imara na ‘wingi’ wa watu wanaowazia kwamba wamepata kusadikishwa kwa imani ya kupokezana.”
Basi, mtu anawezaje kupata imani ya kweli? Gazeti ilo hilo linaendelea kusema hivi: “Inapasa kufahamika kwamba imani kama hiyo inasitawishwa kwa msaada wa Maandiko Matakatifu. Hakuna mtu anayezaliwa akiwa Sha-hidi wa Yehova. Lazima mtu achukue msimamo wakati fulani maishani mwake katika uhuru wote wa ‘kiroho,’ awe alilelewa kati ya Mashahidi wa Yehova au alipata kufahamiana nao kwa kuonana tu.” “Basi imani, chanzo chake ni kusikia; na kusikia huja kwa neno la Kristo.”—Rum. 10:17.
Ndiyo, imani ishindayo inafuata ‘neno linalosikiwa.’ Nazo nguvu zinazobadili maisha za imani msingi wake ni Neno la Mungu. Gazeti Helsingin Sanomat lilisema hivyo, likiripoti juu ya kusanyiko katika Helsinki:
“Makusanyiko makubwa yamekuwa nyakati za maana kwa Mashahidi wa Yehova kwa sababu ya jamaa za sasa na za wakati ujao: Jamaa nzima zinakuja mikutanoni na vijana wanakutana na vijana wengine. Atakayekuwa mwenzi wa ndoa lazima awe ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova.” (Kum. 7:3, 4; 1 Kor. 7:39) Gazeti hilo linaongezea hivi: “Kanuni za Mashahidi wa Yehova zenye kuongoza sehemu nyingine za maisha ya jamaa vilevile ziko wazi: unyumba haukubaliwi na ngono kabla ya ndoa hairuhusiwi. Ndoa inaonwa kuwa ya kudumu. Talaka inakatazwa ‘isipokuwa kwa sababu ya uasherati.’ Mashahidi wa Yehova wanaishi namna hiyo kwa sababu ndivyo inavyosihi Biblia.”
Jamaa nzima zinaweza kufaidika na zinafaidika kutokana na imani. Nao watazamaji wanaweza kuona kwamba Mashahidi wa Yehova kwa ujumla wamegeuzwa na imani yao katika Mungu na Neno lake. Bila shaka, kama mtu mmoja mmoja, imani imewageuza.
IMANI HAIKUBALI VIZUIZI VYA KIKABILA
Sehemu ya maana sana ya kila “Imani Ishindayo” Kusanyiko la Mataifa Yote ilikuwa “Azimio la Imani Yetu.” Kwa itikio lao la uhodari na nguvu, maelfu waliokusanyika wameonyesha kwa njia hiyo nia yao ya kusonga mbele katika utumishi wa Yehova. Na, kati ya mambo mengine, wanauthibitisha ukweli wa maneno haya yaliyomo katika Azimio hilo: “Tumeona yale ambayo imani inaweza kutokeza duniani pote; namna roho ya Mungu imetokeza jambo linaloendelea kuwa la pekee: ‘ushirika wa ndugu’ duniani pote. (1 Pet. 2:17, NW) ‘Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu,’ akasema Kristo Yesu, ‘mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi.’ (Yohana 13:35, NW) Tunafurahia kuwa sehemu ya udugu wa pekee ulio halisi kati ya mataifa yote duniani, udugu unaofungamanishwa pamoja katika upendo usiovunjika—kwa Mungu na Mwanawe, kwa kweli, kwa yaliyo haki, na kwa mmoja na mwenzake.”
Je! haya ni maneno ya bure tu? Bila shaka hapana! Watu mmoja mmoja wa kabila zote na mataifa yote wameshinda chuki ya kitaifa na upendeleo wa kikabila. Wamefungamanishwa katika vifungo visivyovunjika vya upendo wa Kikristo. Kuna uthibitisho wa kutosha kwamba imani ishindayo haitambui (haikubali) vizuizi vya kikabila.
Kwa kweli makusanyiko hayo yaliyopita yalikuwa ya mataifa yote kweli kweli. Kwa mfano, wamisionari waliopata mazoezi katika Shule ya Sosaiti ya Gileadi na wanaotumikia sasa katika mataifa mbalimbali 35 walikuwapo kwenye kusanyiko katika Munich, Jamhuri ya Ujeremani. Vipindi vyao vya kusanyiko vilifanywa katika lugha mbalimbali. Katika programu ya Kiingereza wasemaji walikuwa wametoka katika nchi 11.
Ukweli wa kwamba Mashahidi wa Yehova wanafanyiza udugu wa mataifa yote umeonwa na watazamaji walioko nje. Kwa mfano, katika kuripoti juu ya “Imani Ishindayo” Kusanyiko la Mataifa Yote katika Vienna, Austria, gazeti Wiener Morgen Kurier lilisema hivi: “‘Mashahidi wa Yehova’ wametoka katika hali tofauti tofauti za kijamii, walakini, kifungo kinachowaunganisha ni maoni yao ya ndani yenye nguvu sana ya kidini, ambayo chanzo chake ni Biblia peke yake.”
Shahidi mmoja aliyehudhuria kusanyiko la mataifa yote katika Copenhagen, Denmark, alieleza juu ya kukutana na mfanya kazi wa kijamii ambaye alivutiwa sana na kazi ambayo imefanywa na Mashahidi wa Yehova. Mwanamke huyu anashughulika na watu wazee na wakati wote ameona matokeo yenye faida ambayo yanaletwa na ujumbe wa Ufalme juu ya hawa mmoja mmoja. Mfanya kazi huyu wa kijamii alieleza hivi: “Navutiwa na kazi yenu . . . Pindi nyingine ninaposhughulika na viongozi wa kidini mimi nakatizwa tumaini sana. Ninyi mnao udugu ulio wa mataifa yote peke yake ulimwenguni. Navutiwa na uhodari wenu wa kuhubiri. Endeleeni na kazi hiyo njema!”
IMANI INALETA UJARISI (UHODARI)
Hivyo ndivyo wanavyofanya Mashahidi wa Yehova. ‘Wanaendelea na kazi hiyo njema!’ Imani Ishindayo inaleta ujasiri wa kufuata Ukristo kama njia ya maisha na kutangaza ‘‘habari njema” kwa ujasiri. (Marko 13:10) Kwa habari hiyo, “Azimo la Imani Yetu” lililokubaliwa kwa shauku kwenye “Imani Ishindayo” Makusanyiko ya Mataifa Yote, linasema wazi-wazi hivi:
“Sisi hatutaacha wala hatuwezi kuacha kuyanena mambo ambayo tumeona na kusikia na kupatwa nayo. (Matendo 4:20) Tunalazimika kutaja kwa midomo yetu imani yetu yenye nguvu katika ufalme wa Yehova ushindao, nasi twataka kwa moyo mweupe tuzishiriki baraka za “habari njema” hizi pamoja na watu wote. Kama yule mtume mwaminifu, ombi letu ni kwamba: ‘Mpatanishwe na Mungu.’ (2 Kor. 5:20) Huko ndiko kujikaza kwetu, kutangaza waziwazi habari njema hizi za ufalme wa Yehova Mungu tangu hapa na kuendelea mpaka mwisho wa taratibu hii ya mambo.”—Mt. 24:14; 28:19, 20.
Walipoulizwa, “Je! mnakubali?” wajumbe wa kusanyiko walikuwa wakijibu kwa sauti kuu “Ndiyo!” Walakini walifanya zaidi ya hilo. Walilifanyiza kazi itikio lao.
Kwa kweli, wajumbe waliitoa asubuhi ya siku ya tatu ya kusanyiko kwa ajili ya utendaji wenye shauku wa kutoa ushuhuda shambani. Kwa mfano, iliripotiwa kwamba jitihada hii ”ilitokeza ushuhuda mkubwa usiopata kutolewa tena” katika Dublin, Ireland. Inaripotiwa kwamba, watu wazima 2,650 walikwenda katika Idara ya Utumishi wa Shambani na kupokea vifaa vya kubebea vilivyochapwa vilivyotumiwa katika jitihada hii ya pekee. Mmoja wa wazee Wakristo wa Dublin alisikika akisema hivi: “Kwa mara ya kwanza kuna Mashahidi wengi wanaohubiri katika barabara ya O’Connell zaidi kuliko mapdre wanaotembea hapo.” Mmojawapo wa vitu vilivyotolewa kusanyikoni katika Dublin ambacho bila shaka kitaendeleza kazi ya kuhubiri Ufalme katika Ireland ni trakiti ya lugha ya Gael yenye kichwa “Tu-maini la Pekee la Amani kwa Wanadamu.”
Ndiyo, kazi hiyo ya Kiinjilisti ni wonyesho wa imani ishindayo. Walakini je! inawageuza wale wanaotangaziwa ujumbe wa Ufalme na Mashahidi we Yehova? Ndiyo, katika Paris, Ufaransa, wakati wa asubuhi hii ya utendaji wa pekee, mwanamke mwenye umri wa miaka 30 aliwakaribisha Mashahidi, akisema: “Ziara yenu imeongozwa na Mungu. Nilitaka sana kuzungumza na mtu. Mara tatu mishipa yangu ya fahamu imekataa kufanya kazi na hata nikataka kujiua.” Halafu aliwaeleza siri Mashahidi hao wenye kuzuru, kwamba alikuwa akiona moyoni uhitaji wa kumkaribia Mungu zaidi. Mwanamke huyo alikuwa amefanya uchunguzi juu ya dini fulani za nchi za Mashariki (Asia), lakini hakupata amani ya akili. Kwa hiyo alionyesha nia ya kutaka kujifunza Biblia. Mipango ilifanywa ili aambatane na rafiki kwenye hotuba ya watu wote. Mwanamke huyu alikubali vitabu vilivyotolewa na Mashahidi na alifurahi kupata majibu ya Maandiko kwa maulizo yake.
Mshiriki mmoja wa Baraza Inayoongoza ya Mashahidi wa Yehova na mkewe walikuwa miongoni mwa wale walioshiriki katika utendaji huu wenye kutia imani nguvu katika Lisbon, Ureno. Bila shaka, ndivyo inavyopaswa kuwa, waweza kudhani! Kwa sababu ya msiba uliompata karibuni, alikuwa amevunjika mbavu tatu. Hata hivyo, ilimletea furaha kushiriki pamoja na waamini wenzake katika jitihada hii ya pekee ya utumishi wa shambani.
Ushuhuda mkubwa ulitolewa Rumi, Italia, ambako kusanyiko jingine la mataifa yote lilifanyiwa. Ni kweli kwamba, mji ulikuwa na watu wachache kwa sababu wakaaji wake wengi walikuwa likizoni, na fikira zilikuwa zi-mekazwa sana juu ya kifo cha Papa Paulo wa Sita. Mzee Mkristo kutoka sehemu ya kati ya Italia alisema hivi: “Kila Shahidi katika barabara za Rumi alikuwa akitafuta watu wa kutolea ushuhuda. Nilipomfikia mwanamume mmoja, aliniambia hivi: ‘Tafadhali! Wewe ndiwe Shahidi wa 25 kunisimamisha asubuhi hii!’” Mwanamke mmoja alisema hivi: “Nimekuwa sokoni, nao walikuwa huko. Nilienda kwa mwuza nyama, nao walikuwako, vilevile. Kwenye duka la mboga niliwapata. Hapa nawapata. Nawapata Mashahidi wa Yehova kila mahali.” Ndugu moja aliwaona mapadre wengi wakisoma vitabu walivyoangushiwa asubuhi hiyo.
Likizungumza juu ya utendaji huu wa utumishi wa shambani wa asubuhi ya Ijumaa uliofanywa na wahudhuriaji wa kusanyiko katika Milan, Italia, gazeti la kila siku II Giorno lilieleza kwamba Mashahidi “walipiga milango nyumba kwa nyumba” na “kueleza sababu za imani yao.” Liliongeza kusema hivi: “Mambo yote yalifanywa katika njia ya kupendeza sana, bila waamiriifu hawa kuudhika walipotendwa kama wasumbuaji wanaokuja wakati usiofaa, na kukataliwa kikatili.”
Hata hivyo imani ishindayo inafanya mengi zaidi ya kutoa ujasiri kwa ajili ya jitihada ya muda katika kuzitangaza “habari njema.” Inaendelea kuwapo muda mrefu, ikitegemeza jitihada hizo hata kwa wakati wa miaka mingi. Juu ya hili, kuna ripoti ya kupendeza juu ya Mashahidi wa Yehova katika Italia, kama ilivyochapwa katika gazeti Philadelphia lnquirer. Katika ripoti iliyotoka Rumi, Italia, lilisema katika sehemu moja hivi:
“Wakati Wakatoliki walipokuwa wakingoja katika safu ndefu mwishoni mwa juma iliyopita ili wazuru kaburi la Papa Paulo wa Sita, Waitalia 65,000 hivi walikusanyika chini ya miavuli yenye rangi mbalimbali katika uwanja wa mchezo wa mpira wa Flamingo ili kumtolea Mungu wao ibada.
“Walakini alikuwa Mungu tofauti na yule anayewakilishwa na papa aliyezikwa mapangoni chini ya St. Peter’s Basilica. Huku, katika nchi yenye Wakatoliki wengi zaidi ulimwenguni Mashahidi wa Yehova wamepata msimamo wenye nguvu na unaokua . . .
“Mashahidi wa Yehova, ambao walikuwa na wafuasi 95 katika Italia wakati wa Vita ya Pili ya Ulimwengu, sasa ndio kundi la pili la kidini kwa ukubwa. Bila shaka, wao ndio wanaokua haraka zaidi. . . .
“Idadi yao imekua kutoka 25,810 katika [mwaka] 1972 mpaka 66,315 katika [mwaka] 1977. Na leo wana washiriki 71,796 . . .
“Idadi yao ingali ni ndogo ikilinganishwa na idadi ya watu wa Italia, ambao wengi wao ni Wakatoliki angaa [ni] kwa jina. Walakini wamekufanya kuwapo kwao kujulikane huku. Watu wa kanisa wanasema kwamba Mashahidi wa Yehova wamepiga kila mlango katika Italia kufikia sasa. Kila mshiriki anatazamiwa kufanya kazi ya kiinjilisti.”
Jitihada na uhodari unahitajiwa ili kuendelea kutangaza ujumbe wa ufalme na kukabiliana na vipingamizi vikubwa. Likitaja juu ya “Imani Ishindayo” Kusanyiko la Mataifa Yote la Mashahidi wa Yehova katika Barcelona, Spania, gazeti Diario de Barcelona lilisema hivi: “Mkuu wa [idara ya] utumishi wa uenezaji wa habari za magazeti na radio alisema kwamba wao ‘si sehemu ya ulimwengu.’ Yaweza kuwa hivyo, walakini bila shaka wanaufahamu ulimwengu vizuri nao wana uhodari wa kuueleza wanayoamini.” Ndiyo, imani yenye msingi wa Maandiko ndiyo ambayo sikuzote imekuwa ikitoa “[uhodari wa] kulinena neno la Mungu pasipo hofu.”—Flp. 1:14.
IMANI ISHINDAYO INATOA TUMAINI KWA WAKATI UJAO
“Imani Ishindayo” Makusanyiko ya Mashahidi wa Yehova yalitoa mashauri kamili ya Maandiko. Yalijenga imani.
Nazo faida zake zikiwa zenye kuendelea kwa muda mrefu, kwa kuwa imani ishindayo inatoa tumaini hakika kwa wakati ujao.
Sehemu yenye maana sana ya makusanyiko hayo ya mataifa yote ilikuwa michezo ya Biblia. Ijapokuwako jitihada yenye kuongozwa na dhamiri ya Wakristo hawa waliojiweka wakf ya kutayarisha maonyesho hayo, matatizo yasiyotazamiwa yaweza kutokea. Kwa mfano, mvua kubwa ilinyesha wakati michezo ya kuigiza mitatu kati ya ile mi-nne iliyofanywa, ilipokuwa ikiendelea katika uwanja ulio wazi wa mpira kwenye kusanyiko la Copenhagen, Denmark. Walakini wachezaji waliovikwa mavazi mepesi ya nchi za Mashariki (Asia) walizicheza sehemu zao kwa shauku kama vile wangalifanya chini ya jua lenye joto la kadiri la Mashariki ya Kati. Kwa hiyo, walipata makofi zaidi ya shangwe kutoka kwa wasikilizaji waliokuwa chini ya kinga.
Mbona jitihada nyingi hivyo? Yaelekea sababu yenyewe ilielezwa wazi na gazeti El Noticiero Universal la Barcelona, Spania, lililosema hivi: ‘Lazima mtu akubali sifa ya watu hawa, kwani, hii si kazi ya wakati wote ya wachezaji hawa; wao ni washiriki waliojitolea kucheza. Hivyo wanawasaidia waamini wenzao.’
Hata hivyo, je! michezo hiyo ya kuigiza ilikuwa na matokeo juu ya watazamaji? Bila shaka ndivyo! Mmojawapo ya michezo hiyo ya kuigiza uliokuwa na kichwa “Usitazame Nyuma Wala Usisimame,” ulikuwa juu ya hadithi ya Biblia ya Lutu. (Mwa. sura ya 19) Akizungumza juu ya mchezo huu wa kuigiza, mzee Mkristo alieleza hivi: “Kupenda mali kunadanganya. Twaona namna vitu vya anasa vya jana vimekuwa vitu vya lazima maishani leo, na watu wanajiwekelea mizigo mizito wakijaribu kufuata mitindo ya leo. . . Lo! namna ulivyo ujumbe katika wakati uliofaa!”
Kati ya mambo mengineyo, programu ya makusanyiko ya mataifa yote ilitoa mashauri yanayofaa juu ya ndoa. Je! yana matokeo juu ya watu mmoja mmoja? Ndiyo. Mume na mke mmoja vijana walipotoka kusanyikoni katika Marseilles, Ufaransa walisema hivi: “Lo! namna tulivyothamini kusanyiko hili, sana sana zile hotuba juu ya ndoa, pamoja na inashauri yanayofaa juu ya namna ya kutatua matatizo ya ndoa! Kusanyiko hili lilikuwa la lazima ili kutukumbusha anayosema Yehova katika Neno lake, ili kutusaidia kuimarisha mwungano wetu na kumaliza magumu yetu. Tulitoka kusanyikoni tukiwa tumetiwa nguvu na tukiwa wenye furaha.”
Imani ishindayo yenye msingi wa Neno hakika la Mungu, inageuza watu mmoja mmoja. Inawafaidi. Lo! namna hili lilivyoonyeshwa vizuri kwa habari ya mwanamke mmoja mwenye umri wa miaka 62 aliyebatizwa katika moja-wapo la makusanyiko ya mataifa yote huko Sheffield Uingereza! Akiwa mleta habari za magezeti, yeye alikuwa ameandika na kuwa mhariri wa gazeti la kanisa la mahali hapo. Walakini miaka 20 iliyopita alipatwa na ugonjwa wa ghafula wa ubongo uliomlemaza na tangu wakati huo kanisa hilo likaacha kupendezwa naye. Katika mwaka 1977 mwanamke Mkristo alianza kujifunza Biblia na mwanamke huyu aliyelemazwa na ugonjwa naye anaripoti hivi: “Kila juma alikuwa na karatasi yenye maulizo. Yeye mwenyewe alijitafutia maandiko yote. Kwa kweli tulikuwa tukiiona roho ya Yehova ikitenda kazi mara tulipomwona. Maendeleo yake yalikuwa ya ajabu. Kama vile funzo lilivyoendelea, alifanya maendeleo hata kufikia kusoma mafungu na kushiriki katika mazungumzo.”
“Akawa na maendeleo katika afya yake ya kimwili kadiri hali yake ya kiroho iliyyoendelea,” akaeleza mume wake. Mwanamke huyu aliacha kuvuta tumbako alipojifunza kwamba jambo hilo halimpendezi Yehova, na kubatizwa katika kusanyiko hilo. Walakini huu ulikuwa ushindi kwa imani wenye kuhuzunisha, kwa sababu mwanamke huyu alilazimika kuzamishwa katika maji pamoja na kiti chake cha kubebea wagonjwa. Bila shaka, kweli ya Biblia imempa tumaini hakika kwa wakati ujao. Wakati wa kubatizwa alisema hivi: “Nina furaha sana sana kuwa kati ya wengi hapa!” Sasa, akiwa na tumaini la kweli maishani, maoni yake ni nini? Imani imempa tumaini, naye anasema: ‘Mimi nataka tu kuwaambia wengine juu ya wakati ujao wenye amani ambao Yehova ameuahidi.’
Mashahidi wa Yehova wanaungojea wakati ujao kwa uhakika. Wanaweza kufanya hivyo kwa sababu wana imani ishindayo ambayo hushinda vizuizi na magumu. Ni imani ambayo imekuwa na nguvu zenye kugeuza maisha zao. Wakristo hawa ni wenye furaha kwa sababu wao ni sehemu ya udugu peke yake ulio na umoja ulimwenguni pote. Imani yao haikubali vizuizi vya kikabila. Ni imani iletayo uhodari. Na zaidi ya hayo, hii imani ishindayo inawapa tumaini kwa wakati ujao.
Imani yenye msingi imara wa Biblia yaweza kukugeuza katika njia izo hizo. Pasipo shaka, unaweza kufaidika kutokana na imani ishindayo.
[Picha katika ukurasa wa 18]
Imani inajenga jamaa zenye furaha
[Picha katika ukurasa wa 20]
Wakusanyikaji washiriki “habari njema”
[Picha katika ukurasa wa 22]
Mchezo wa kuigiza juu ya jamaa ya Lutu wafunza somo la maana