Maswali kutoka kwa Wasomaji
● Je! Yesu ni “mpatanishi” wa Wakristo watiwa mafuta peke yao?
Neno “mpatanishi” linapatikana mara sita peke yake katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo na kuhusiana na Maandiko sikuzote linatumiwa juu ya agano rasmi.
Musa ndiye aliyekuwa “mpatanishi” wa agano la Torati lililofanywa kati ya Mungu na taifa la Israeli. (Gal. 3:19, 20) Hata hivyo, Kristo ndiye “mpatanishi wa agano jipya” kati ya Yehova na Israeli wa kiroho, “Israeli wa Mungu” watakaotumikia pamoja na Yesu mbinguni wakiwa wafalme na makuhani. (Ebr. 8:6; 9:15; 12:24; Gal. 6:16) Mungu alipokuwa akiwachagua wale ambao wangeingizwa katika agano hilo jipya, mtume Paulo aliandika kwamba Kristo alikuwa ndiye ‘mpatanishi mmoja kati ya Mungu na wanadamu.’ (1 Tim. 2:5) Kupatana na akili, hapa, Paulo alikuwa akitumia neno “mpatanishi” katika njia ile ile aliyokuwa akilitumia katika zile safari nyingine tano, ambazo katika hizo neno lilitumiwa kuhusiana na wale waliokuwa wakati huo wakiingizwa katika agano jipya ambalo Kristo ni “mpatanishi” kabla ya kuandikwa 1 Timotheo 2:5. Kwa hiyo katika maana hii halisi ya Biblia Yesu ni “mpatanishi” wa Wakristo watiwa mafuta peke yao.
Agano hilo jipya litakoma wakati wa kutukuzwa kwa mabaki ambao leo wamo katika hilo agano ambalo Kristo ni mpatanishi wake. “Mkutano mkubwa” wa “kondoo wengine” unaoundwa sasa hawamo katika agano hilo jipya. Walakini, kwa kushirikiana na hilo “kundi dogo” la wale ambao bado wangalimo katika agano hilo wanakuja chini ya faida zinazotiririka kutoka kwa hilo agano jipya. Katika wakati wa ule utawala wa miaka elfu, Yesu Kristo atakuwa mfalme wao, kuhani mkuu na hakimu. Kwa habari yenye maelezo zaidi, angalia kitabu Aid to Bible Understanding, kur. 1129 na 1130 chini ya “Mpatanishi”; vilevile God’s “Eternal Purpose” Now Triumphing for Man’s Good, uku. 160, fungu 10; vilevile toleo la Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) la Februari 15, 1966, kur. 105 mpaka 123; toleo la Mnara wa Mlinzi la Mei 15, 1973, kur. 224, 225, chini ya kichwa kidogo “Kuonyesha Njia ya Agano Jipya”; na toleo la Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) la Aprili 1, 1973, kur. 198, 199, chini ya kichwa kidogo “Agano Jipya.”
● Ukoo wa fundi mwenye ujuzi aliyetumwa na Hiramu asaidie kazi ya kujenga hekalu wakati wa utawala wa Sulemani unasimuliwa tofauti katika 1 Wafalme na 2 Mambo ya Nyakati. Kwa sababu gani?
1 Wafalme 7:14 lasomwa hivi: “Naye alikuwa mwana wa mwanamke mjane wa ‘kabila ya Naftali, na babaye alikuwa mtu wa Tiro.” Katika 2 Mambo ya Nyakati 2:14, fundi huyu anasimuliwa kuwa “mwana wa mwanamke wa binti za Dani, na babaye alikuwa mtu wa Tiro.” Mitajo hii inapofahamika kuwa inakamilishana, tofauti inayoelekea kuwapo inaondolewa mara moja. Mamaye alikuwa “mwanamke mjane wa kabila ya Naftali” kwa maana ya kwamba alikuwa ameolewa na mwanamume kutoka kabila hilo. Hata hivyo, kabila lake mwenyewe lilikuwa, la Dani. Baada ya kifo cha mume wake, aliolewa na Mtiro mmoja, na kutokana na ndoa hii akazaliwa yule mwana aliyepata kuwa fundi mwenye ujuzi.