‘Wamwachao Yehova Wataangamia’
Katika siku za nabii Isaya, wengi wa wakaaji wa Yerusalemu na nchi ya Yuda hawakuwa waaminifu kwa Yehova Mungu wao. Walizoea sana ibada ya sanamu. Kwa hiyo, maneno haya ya Yehova yalielekezwa kwao kupitia kwa Isaya: “Nao wamwachao [Yehova] watateketezwa. Kwa maana watatahayarika kwa sababu ya mialoni [“miti enye nguvu,” NW]— mliyoitamani, nanyi mtaaibishwa kwa sababu ya bustani mlizozichagua.”—Isa. 1:28, 29.
Watu walikuwa wakitoa sadaka na kuwafukizia uvumba miungu wa uongo bustani au vichaka vitakatifu. (Isa. 65:3; 66:17) Vilevile “miti yenye nguvu’ ilikuwa na sehemu katika ibada hiyo ya sanamu. Wakati wa Yehova wa kufikiliza hukumu yake, hiyo miti mitakatifu ingekuwa kitu cha kuwaaibisha waabudu hao wa sanamu. Miungu waliotumikia hawangeweza kuwakinga au kuwalinda kutokana na siku ya hasira.
Unabii wa Isaya unaendelea kusema hivi: “Maana mtakuwa kama mwaloni [“mti mkubwa,” NW]— ambao majani yake yakauka, na kama bustani isiyo na maji.” (Isa. 1:30) Kwa kutumia hivyo usemi huo juu ya “mti mkubwa” na “bustani” uhusu mwabudu sanamu, unabii huo ulionyesha namna watu hao wasio waaminifu ‘wangenyauka’ kutokana na hasira ya Mungu, na kukauka kama bustani katika wakati wa majira ya kiangazi. “Na,” unabii huo waendelea kusema, “mtu hodari [mwabudu sanamu] atakuwa kama makumbi [kama visehemu ovyo, vilivyokatikakatika, vyenye kuteketea upesi vya kitani], na kazi yake [sanamu] kama cheche ya moto; nao [wote wawili mwabudu sanamu na sanamu] watawaka pamoja, wala hapana atakayewazima.” (Isa. 1:31) Jinsi hilo lilivyo onyo lenye nguvu juu ya ibada ya sanamu! Bila shaka, ‘wamwachao Yehova wataangamia.’