“Kweli ya Ufalme” Makusanyiko ya Wilaya
YEHOVA ni “Mungu wa kweli.” (Zaburi 31:5) Mwanawe, Yesu Kristo, alisema hivi juu yake mwenyewe: “Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima.” (Yohana 14:6) Kuhusu Neno la Babaye, yeye alisema, “Neno lako ndiyo kweli.” (Yohana 17:17) Na kundi la Kikristo ni “nguza na msingi wa kweli.”—1 Timotheo 3:15.
Walakini kweli ya Ufalme ni nini? Ndicho kichwa cha mazungumzo katika Biblia yote tangu Mwanzo mpaka Ufunuo. Yehova Mungu aliisema kweli ya Ufalme ya kwanza alipomwambia Nyoka hivi katika bustani ya Edeni: “Nami nitaweka uadui kati yako na huyo mwanamke, na kati ya uzao wako na uzao wake; huo utakuponda kichwa, na wewe utamponda kisigino.” (Mwanzo 3:15) Kati ya kweli za Ufalme za mwisho zilizoandikwa katika Neno la Mungu ni ile ya Ufunuo 21:4: “[Mungu] atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.”
Tukiwa mashahidi Wakristo wa Yehova tuna pendeleo kama nini kuwajulisha wengine kweli ya Ufalme! Ni jambo la maana kama nini tufanye hivyo! Watu wenye njaa ya kutaka kweli wanapiga kite na kuugua kwa sababu ya machukizo wanayoyaona yakitokea. (Ezekieli 9:4) Wengi wanasema hawana tumaini. Kwa kushiriki katika kutimiza unabii wa Yesu katika Mathayo 24:14 tunaweza kuwapa faraja na tumaini wale wote wanaoitamani kweli kabisa.
Ili tuthamini vizuri zaidi kweli ya Ufalme ni nini na ni nini yaliyo madaraka yetu kuhusiana nazo, na ili tuchochewe tufanye yote tuwezayo kutangaza kweli ya Ufalme, kichwa cha makusanyiko ya wilaya ya 1982 ya Mashahidi wa Yehova duniani pote kimefanywa kiwe “Kweli ya Ufalme.” Programu itaanza Alhamisi alasiri na kuendelea mpaka Jumapili jioni. Fanya mipango sasa ya kuhudhuria angaa moja kati ya “Kweli ya Ufalme” makusanyiko ya wilaya tangu mwanzo mpaka mwisho.