“Ongezeko la Ufalme” Makusanyiko ya Wilaya
YEHOVA MUNGU amebariki kweli kweli kazi ya ulimwenguni pote ya kuhubiri Ufalme. Hilo liko wazi katika ripoti yenye kusisimua ndani ya Kitabu cha Mwaka cha 1984 (Kiingereza)! Basi, kinafaa kama nini kichwa cha makusanyiko ya wilaya ya 1984—“Ongezeko la Ufalme”!
Mwaka wa utumishi uliopita ulikuwa na ongezeko la asilimia 6.8 katika hesabu ya wastani ya wahubiri wa habari njema. Kulikuwako maongezeko katika jumla ya saa zilizotumiwa katika kuhubiri, jumla ya ziara za kurudia zilizofanywa na hesabu ya wastani ya mafunzo ya Biblia ya nyumbani, na pia ongezeko lenye kutokeza katika hesabu ya mapainia wasaidizi na wa kawaida. Hudhurio la Ukumbusho lilipanda juu likafika 6,767,707. Hiyo ni asilimia 8.2 zaidi ya mwaka uliotangulia! Hakika, utendaji wa watu wa Mungu umesonga mbele katika sehemu zote, na jambo hilo linatukumbusha maneno ya kiunabii juu ya Mfalme wa Yehova: “Kwa ongezeko la serikali na amani yake hakutakuwa mwisho.”—Isaya 9:7, New International Version.
Hiyo ni tofauti kubwa kama nini na yanayopata makanisa ya Jumuiya ya Wakristo! Si kwamba tu hudhurio la kanisa linapunguka katika sehemu nyingi bali pia kuna ukosefu wenye kuua wa chakula cha kiroho chenye kutoa uhai na ongezeko la kupuuza kushikamana na amri za mwenendo za kimungu.
Lakini je, sisi tukiwa Mashahidi wa Yehova tutategemea sifa tuliyo nayo tayari tuache kujikaza? Hata kidogo! Badala yake, tumeazimia kufanya yote tuwezayo tuongeze faida za Ufalme. Kwa kusudi hilo, karamu ya kiroho yenye kujenga sana inatayarishwa kwa ajili yetu kwenye makusanyiko ya wilaya yajayo. Programu hiyo nzuri itaanza Alhamisi alasiri na itaendelea mpaka Jumapili alasiri. Makusanyiko hayo yatafanywa katika Kenya, Uganda na Zaire. Fanya mipango sasa uwepo tangu mwanzo wenyewe mpaka mwisho wenyewe.