“Sikio” la Fira
Kifungu cha Biblia kinachotaja kwa njia ya mashairi “sikio” la fira (nyoka mkubwa) kimepingwa mara nyingi. (Zaburi 58:4, 5) Lakini gazeti la Kijeremani la sayansi ya maumbo ya wanyama linaloitwa Grzimeks Tier, Sielmanns Tierwelt (yaani, Ulimwengu wa Wanyama wa Grzimek na wa Sielmann) limechapisha makala ambayo linakiri ‘inapingana kabisa’ na maoni ‘ya kwamba fira ni bubu,’ kisha linaendelea kuuliza hivi: “Ni nani anayesema kweli—yale maoni yanayofuatwa kisayansi au mwandikaji wetu?”
Mwandikaji anaeleza habari za fira aliyeishi katika uwanja wake katika Sri Lanka akiwa katika kichuguu cha mchwa. Alimwomba mtumbuiza-nyoka amkamate nyoka huyo asiye wa kufugwa kisha amfanye acheze dansi. Mwandikaji anasema hivi: “Nilipokwisha kumhakikishia mgeni wangu huyo kwamba kwa kweli fira aliishi hapo, yeye aliketi mbele ya kichuguu hicho cha mchwa akaanza kupiga filimbi yake. Baada ya muda mrefu—kwa sababu nilikuwa nimechoka na sikuamini lo lote litatukia—fira yule alitokeza kichwa chake sentimeta kadha nje ya shimo moja. Kabla nyoka huyo hajaweza kufungua kinywa chake mtumbuizaji alienda haraka akamshika kichwa kati ya kidole gumba na vidole vingine viwili.” Halafu Mhindi huyo akamfanya nyoka yule acheze dansi. Angalau katika kisa hicho fira kwa kweli ‘aliisikiliza sauti ya mtumbuizaji.’