Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w90 7/1 kur. 29-31
  • Heshimu Yehova kwa Mali Zako

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Heshimu Yehova kwa Mali Zako
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Fahari ya
  • Mfunzi Wetu Mkuu Hutuelimisha
  • Tajiri Katika Imani na Kazi Nzuri
  • Mtu Yeyote Aweza ‘Kujaza Mkono Wake’
  • Kutembea kwa Nafsi Yote katika Njia ya Uzima
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Je! Waweza Kufanya Zaidi Umheshimu Yehova?
    Huduma Yetu ya Ufalme—1993
  • Yehova Ategemeza Jeshi Lake la Watumishi wa Wakati Wote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Baraka za Huduma ya Painia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
w90 7/1 kur. 29-31

Heshimu Yehova kwa Mali Zako

‘MIMI si tajiri; mimi ni kijana tu na nina mali chache sana.’ ‘Sikupata kamwe elimu nyingi; mimi ningeweza kumpa Yehova nini?’ ‘Mimi nina mdhoofiko mkubwa; Yehova atalazimika kunipitilia mimi.’ ‘Umri wangu ni mkubwa sana; nimechelewa mno kupata mali.’

Je! mawazo kama haya hupita-pita katika akili yako ufikiriapo kichwa cha makala hii? Hata hivyo, huenda ikawa wewe ni tajiri kuliko ufikirivyo. Kumbuka maneno ya Bwana Yesu kwa kundi katika Smirna: “Mimi najua dhiki na umaskini wako—lakini wewe u tajiri.” (Ufunuo 2:9, NW) Mapema kidogo Yesu alikuwa amesema hivi katika Mahubiri ya Mlimani: “Msijiwekee hazina duniani . . . bali jiwekeeni hazina mbinguni . . . kwa kuwa hazina yako ilipo, ndipo utakapokuwapo na moyo wako.” (Mathayo 6:19-21) Je! maneno hayo ya Bwana-mkubwa wetu yakuchangamsha wewe? Ndiyo, huenda ukawa una kitu fulani ndani yako ambacho Baba yetu wa kimbingu, Yehova, na Mwana wake hukiona kuwa cha thamani kubwa sana. Acheni tuchunguze!

Fahari ya

Ujana—Imara na Bidii

Kijana aweza kumtoleaje Yehova utumishi wenye kuthaminika? Mithali 20:29 hutuhakikishia kwamba vijana wana mali yenye fahari—sulubu (nguvu) ya kimwili. Inaburudisha kama nini kuona kijana akitoa nishati na ubichibichi wake kwenye utumishi wa Mungu wetu.

Acheni tufungue kurasa za historia kule nyuma kwenye mwanzo wa miaka ya 1930 ambapo vijana kadhaa walisikia juu ya ukweli ulio katika Biblia. Mmoja mwenye miaka 16 aliazima kutoka kwa rafiki yake msaada wa kujifunza Biblia Creation, uliochapishwa na Watch Tower Society. Kufikia wakati alipofika ile sura “Uumbaji Mpya” na kusoma juu ya kuwa wakfu, alijua alilotaka kufanya na maisha yake. Mara ile ile, alijiweka wakfu kwa Muumba mweza yote. Mwaka uliofuata alisoma kichapo kingine, Vindication (Kitabu cha Kwanza), akapata habari juu ya tazamio la kushiriki katika kutetewa kwa jina na enzi kuu ya Mungu. Habari hizi ziliamsha tamaa yenye kuwaka ndani yake ya utumishi wa wakati wote. Mwaka uo huo alijaza ombi la mapendeleo ya upainia, na mpaka leo yeye huendelea katika utumishi wa wakati wote. Ingawa sasa hesabu fulani ya marika wake wamemaliza mwendo wao wa kidunia, wengi wa wale ambao wangali hai huonyesha roho ya ujitoaji wa nafsi nzima kwa Baba yetu wa kimbingu.

Je! vijana Wakristo leo huonyesha sifa hii hii yenye kuthaminika? Hakika wao hufanya hivyo! Ripoti za Kitabu-Mwaka huonyesha kwamba sasa umayamaya ulio kama matone-umande wanajiunga kuwa mapainia. (Zaburi 110:3) Ufilipino iliripoti kwamba asilimia 13 ya mapainia wa kawaida wote ni wa chini ya umri wa miaka 20. Je! ndivyo ilivyo mahali penginepo? Naam. Kwa kielelezo, uchunguzi uliofanywa katika visiwa vidogo vya Trinidad na Tobago hufunua kwamba mapainia wapya 282 waliandikishwa kati ya Septemba 1, 1986, na Septemba 30, 1988. Kati ya hesabu hiyo, 48 walikuwa na umri wa chini ya miaka 20. Je! ungependa kusikia kutoka kwa mmoja wao?

Huyu ni Charmaine Francis. Msichana huyu asema: “Tangu nilipokuwa kitoto kichanga, wazazi wangu waliongea nami juu ya kumtumikia Yehova na kuendelea kuwa mwaminifu kwake. Wazazi wangu walipokuwa wakiuliza ningefanya nini kama wao wangetiwa jela kwa kuzihubiri habari njema, mimi nilikuwa nikisema, ‘Nitamtumikia Yehova.’ Nilifanya wakfu wangu nilipokuwa na miaka 13, na nilibatizwa nikiwa na miaka 14. Mara baada ya hapo, wakati wa kila likizo la shule, nilijitia katika upainia msaidizi. Katika 1983 niliingia utumishi wa painia wa kawaida. Katika mwaka wangu wa kwanza wa kupainia, niliiona shangwe ya kusaidia mke wa kinyumbani awe mtumishi wa Yehova. Sasa mimi naongoza mafunzo tisa ya Biblia. Mmoja ana-jitayarisha kwa ajili ya ubatizo, na watatu wengine wanahudhuria mikutano.”

Sasa, je! nyinyi vijana hamwafiki kwamba nyinyi pia mna kitu fulani chenye thamani kubwa cha kumheshimu Yehova nacho? Bila shaka mnacho! Hata ingawa huenda sasa msiwe katika utumishi wa wakati wote, mwaweza kumheshimu Yehova kulingana na hali zenu. Huenda bado mkawa mna miaka mingi iliyobaki ya kwenda shule. Hata hivyo, mna fursa yenye kuthaminika ya kumsifu Yehova kwa walimu na wanadarasa wenzenu. Christian Kalloo, aliye na umri wa miaka kumi, alileta shuleni nakala yake ya kitabu Life—How Did It Get Here—By Evolution or by Creation? Tokeo likawa nini? Aliangusha nakala saba kwa wale wenye kupendezwa na habari hiyo. Pia aliangusha moja katika huduma ya nyumba kwa nyumba. Wewe waweza kufanya hivyo hivyo.—Linganisha Mathayo 21:15, 16.

Mfunzi Wetu Mkuu Hutuelimisha

Nabii Isaya alisema hivi: “Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova mwenyewe amenipa mimi ulimi wa waliofundishwa.” Yeye alimpa Yehova sifa kwa uwezo wake wa kusema. Pia aliandika ahadi ya Yehova: “Roho yangu iliyo juu yako na maneno yangu ambayo mimi nimetia katika kinywa chako—hayataondolewa katika kinywa chako wala kutoka kinywa cha wazao wako wala kutoka kinywa cha wazao wa wazao wako.” (Isaya 50:4; 59:21, NW) Kama vile wanaume wasio na kisomo na wa kikawaida walivyokuja kuwa mitume wa Yesu na Mungu akawahekimisha katika mambo ya kiroho, ndivyo Yehova amehekimisha watu wa kikawaida leo.

Kitabu-Mwaka cha 1986 kina habari za kutia moyo kwa wale ambao wamepata kiasi kidogo tu au wasiopata kiasi chochote cha elimu rasmi. Katika nchi nyingi Mashahidi wa Yehova hupanga kuwe na madarasa ya wasiojua kusoma ili kufundisha watu wazima kusoma. Yehova amewabariki kama nini! Kati ya 1962 na 1984 katika Naijeria, watu 19,238 walifanya maendeleo mazuri kabisa katika kujifunza kusoma na kuandika na sasa kwa kweli wanaweza kujisomea Biblia wenyewe na pia wale ambao wao huwatolea ushahidi. Wamekuwa na baraka nyingi kama nini! Ndugu mmoja alifanya vizuri sana hata akawa mfunzi wa somo la usomaji katika kundi lake.

Pia fikiria ono la Ezekiel Ovbiagele. Yeye hakuweza kusoma alipobatizwa katika 1940. Baada ya kujifunza kusoma, alifanya maendeleo kufikia hatua ya kuandikishwa akiwa painia, na baadaye zaidi, katika 1953, akawekwa kuwa mwangalizi anayesafiri.

Hakuna vizuizi vya umri katika utaratibu wa kujifunza. Huenda watu fulani wakanukuu ile mithali ya zamani: “Huwezi kumfunza mbwa mzee mbinu mpya!” Huenda hiyo ikawa kweli kuhusu mbwa, lakini watu si wanyama. Hata walio wazee-wazee waweza na huweza kujifunza ikiwa kweli wanataka kumjua na kumtumikia Yehova. Huenda ukawa unajua watu fulani ambao wamefanya hivyo. Kwa kielelezo, Alice Okon katika Naijeria alitiwa moyo asome Biblia na kujua juu ya tumaini inalotoa; aliitikia na akashangilia katika tumaini lililo mbele. Akiwa na umri wa miaka 80, mama huyo hakuwa mzee mno kujifunza. Je! wewe hufikiri aliteremesha moyo wa Yehova? Yeye ni tajiri katika imani. Mithali 3:14, NW, hutuhakikishia kwamba kuwa na hekima “ni bora kuliko kuwa na fedha kama pato na kuwa nayo ikiwa zao ni bora kuliko dhahabu yenyewe.” Mtu awezapo kusema ukweli kwa usahihi, maneno yake huwa kama “matofaa ya dhahabu katika vyano vya fedha.”—Mithali 25:11, NW; Wakolosai 3:16.

Tajiri Katika Imani na Kazi Nzuri

Hata Ingawa Hawajiwezi

Mtu aliyezaliwa na hali ya kutojiweza kimwili huenda akahisi amevunjika moyo sana umri wake uongezekapo naye akaja kuijua hali yake. Na ni jambo la kuvuruga sana hisia mtu apatwapo na hali ya kutojiweza akiwa mtu mzima. Je! watu wenye hali hiyo hawana tumaini lolote? La, huenda hata ikawafungulia njia ya kupata uhai wa milele.

Wakati wa Vita ya Ulimwengu 1, Edward Stead aliendesha banda la farasi na magari ya kukodisha katika mji mdogo wa Arvada, Wyoming, U.S.A., na mke wake aliendesha hoteli ndogo. Kukaa mahali penye homa kali ya Kihispania yenye kuhofiwa sana kulipunguza kinga ya mwili wake, naye akapatwa na rheumatoid arthritis (mchochota wa yabisi kavu), iliyofungamanisha viungo vyake hata mwili wake ukakunjamana kuwa umbo la kiti-magurudumu chake. Ingawa alikuwa hoi kwa njia nyinginezo, bado aliweza kusema, na alijongeza mikono yake kidogo. Kwa muda fulani alifikiria kujiua. Halafu akakuta ukweli, naye akaukubali kwa moyo sana.

Kwanza aliketi kwenye mwingilio wa ile hoteli na kuongea na wageni juu ya imani yake mpya aliyoipata karibuni. Aliweza kujongeza mikono yake kutosha kufungua kichapo cha Biblia kuwaonyesha wale waliosimama hapo kusikiliza. Baadhi ya waliothamini jitihada zake walimwita yeye rubani kiwete wa angani. Halafu, yeye akaamua angeweza kutoa ushahidi katika miji mingine ikiwa angejengewa funiko maalumu katika gari la pikapu. Ilifanywa hivyo, na kwa miaka mingi yeye akapainia kwa njia hii isiyo ya kawaida, akisafiri maelfu ya kilometa kati ya Wyoming na Texas, kwa kuandamana na mapainia wachanga wawili au watatu waliomtunza. Kwa muda alioishi, alikuwa kitia-moyo kikubwa kwa wote waliomjua.

Ukihisi umevunjika moyo kwa sababu ya hali fulani ya kutojiweza kimwili, tafadhali soma usimulizi ulio katika kurasa 22-5 za The Watchtower la Novemba 15, 1986. Wanaume wote waliotajwa humo ni wazee, washauri wa kiroho, wenye kustahili kufariji ndugu zao ambao huenda wakawa wana miili mizuri lakini wenye kuhitaji kujengwa kiroho. Wao ni matajiri kama nini machoni pa Mungu!—1 Timotheo 6:18.

Esterleta Dick, mwenye umri wa miaka 63, amekuwa Shahidi aliyebatizwa kwa miaka 16. Katika 1978 mama huyo alipoteza uwezo wake wa kuona, lakini amekuwa akitumikia akiwa painia wa kawaida kwa miaka miwili iliyopita. Hilo lawezekanaje? Haya basi, acha yeye ajibu.

Yeye asema, “Siku moja dada painia mchanga aliniuliza hivi: ‘Dada Dick, sikuzote wewe hufikia miradi yako ukiwa painia msaidizi. Kwa nini usijaribu kuwa painia wa kawaida?’”

Esterleta alihofu angekuwa kizuizi kwa akina ndugu, lakini akakumbuka kwamba mwangalizi wa mzunguko alikuwa ametia moyo kufanya utumishi wa painia. Asema hivi: “Nilijiondokea nikaanza, na sasa nimetumia miaka miwili katika utumishi wa painia. Mimi hufanya ushahidi wa barabarani nami nina ziara za kurudia nyingi. Zaidi ya hilo, mimi huongoza mafunzo ya nyumbani ya Biblia sita. Jinsi gani? Kabla ya kumzuru mwenye nyumba, mimi husomewa nyumbani habari za funzo pamoja na maandiko yaliyoonyeshwa bila manukuu, hivi kwamba naweza kutoa maelezo kwenye funzo. Watatu kati ya wanafunzi wangu wa Biblia huhudhuria mikutano pamoja nami, na mmoja amebatizwa.”

Mtu Yeyote Aweza ‘Kujaza Mkono Wake’

Zawadi

Je! upaji wahusu eneo la kiroho tu? Sivyo. Mfalme Daudi wa zamani alipokuwa akifanya matayarisho kujenga hekalu, aliuliza hivi: “Kuna nani anayejitolea kujaza mkono wake leo zawadi kwa ajili ya Yehova?” (1 Nyakati 29:5, NW) Mtu yeyote angeweza kufanya hivyo. Vivyo hivyo leo, wengi walio wachanga kwa wazee, wenye afya njema kwa wasio nayo, hutaka kutoa mchango wa kujitolea kwa hiari ili kuendeleza masilahi ya Ufalme. Hilo laweza kufanywa kupitia ofisi ya tawi ya nchi ya mtu au kupitia kundi la mahali. Kwa njia hiyo mtu yeyote aweza, kulingana na uwezo wake, kusaidia kuchukua gharama ya kuhakikisha kwamba habari njema zinahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa. Hilo ni pendeleo.—2 Wakorintho 9:8-12.

La maana zaidi, wewe una mali za kiroho za kumheshimia Yehova. Walio wachanga wana nguvu nyingi na ubichibichi wa ujana. Wasio na kisomo waweza kujifunza kutolea Yehova tunda la midomo yao. Wasiojiweza waweza na wameweza kufanya maendeleo katika kupata maarifa, hekima, na uelewevu, hivi kwamba wengi si wasifaji wa wakati wote tu wa Yehova bali pia ni washauri na wachungaji katika kundi la Kikristo. Je! wewe si tajiri kuliko ulivyofikiri? Basi, heshimu Yehova kwa mali zako.—Waebrania 13:15, 16.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki