Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w91 7/1 kur. 28-30
  • Kujishughulisha Sana na Habari Njema

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kujishughulisha Sana na Habari Njema
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kiolezo Kwetu Sisi Leo
  • Je! Unafanya Sehemu Yako?
  • Thawabu za Utumishi Uliosawazika
  • Fanya Upatikane!
  • ‘Shughulika kwa Juhudi Nyingi’ na Huduma Yako
    Huduma Yetu ya Ufalme—2001
  • ‘Kufanya Kazi Usiku na Mchana’ Kufanya Wanafunzi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • “Endelea Kusema na Usinyamaze”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
  • “Kutafuta Kwanza Ufalme”
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
w91 7/1 kur. 28-30

Kujishughulisha Sana na Habari Njema

MTUME Paulo alikuwa katika shida inayojulikana na Mashahidi wa Yehova ambao ni wahudumu wa wakati wote—alikuwa na uchache wa fedha. Kwa hiyo katika Korintho alianza ile kazi ya unyenyekevu ya kutengeneza hema aliyokuwa amejifunza akiwa kijana. Kazi hiyo ilikuwa ngumu, na nyakati nyingine huenda ikawa mikono yake ilitoka damu kutokana na kutumia ile nguo ya hema yenye kukwaruza. Mapato yaliandaa riziki na nguo zake kwa shida, lakini aliridhika, kwa kuwa wakati kazi yake ya kimwili ilipoisha kila siku, aliweka kando vyombo vyake vya kazi na kufanya kile kilichomleta Korintho mwanzoni—alihubiri habari njema!—Wafilipi 4:11, 12.

Siku za Sabato, Paulo alienda kwenye sinagogi. Ni kweli, Paulo mwanzoni aliwafikia wasikilizaji wake Wafilipi “katika hali ya udhaifu na hofu na matetemeko mengi.” (1 Wakorintho 2:1, 3) Lakini kwa kuchochewa na itikio la wengine kwa ujumbe wake, Paulo aliendelea ‘kutoa hoja zake katika sinagogi kila sabato, akajaribu kuwavuta Wayahudi na Wayunani.’—Matendo 18:1-4.

Hata hivyo, kwa muda Paulo hakuweza kufanya zaidi ya kuhubiri kwa nusu-wakati tu. Halafu Sila na Timotheo walikuja kutoka Makedonia wakiwa na mchango wa ukarimu ambao ‘ulimpa kadiri ya mahitaji yake.’ (2 Wakorintho 11:9; Wafilipi 4:15) Yenye kutia moyo, pia, ilikuwa habari ya kwamba ndugu katika Thesalonike walikuwa wakisimama imara ujapokuwa mnyanyaso.—1 Wathesalonike 3:6.

Iliathirije Paulo? “Paulo akasongwa [akaanza kujishughulisha, NW] sana na lile neno [“alitoa wakati wake wote kwa kuhubiri,” The Jerusalem Bible; Today’s English Version], akiwashuhudia Wayahudi ya kwamba Yesu ni Kristo.” (Matendo 18:5) Akiwa amepunguziwa mikazo ya kifedha kwa muda fulani, Paulo hakuweza kupumzika mpaka alipokuwa amerudia kuhubiri kwa wakati wote. Alirudia kazi hiyo kwa bidii nyingi yenye uchangamfu, si kuhubiri Wayahudi tu bali pia kuchukua wakati kuandika waraka wake wa kwanza wenye kupuliziwa roho—barua kwa Wathesalonike!

Kiolezo Kwetu Sisi Leo

Rekodi ya kazi ya Paulo yenye shughuli katika Korintho imehifadhiwa ili kutia moyo Wakristo wote wajishughulishe sana sana na habari njema. Paulo aling’amua kwamba Bwana Yesu mwenyewe alikuwa amewapitishia wanafunzi wake pendeleo kubwa la kuwa “nuru ya ulimwengu.” Hawakupaswa wafiche nuru hiyo. Yesu aliwaambia hivi: “Nuru yenu na iangaze mbele ya watu, wapate kuyaona matendo yenu mema, wamtukuze Baba yenu aliye mbinguni.” (Mathayo 5:14-16) Hiyo ilimaanisha kushiriki kikamili katika kazi ya kuhubiri iliyotabiriwa na Yesu. (Mathayo 24:14; 28:19, 20; Matendo 1:6-8) Kazi ya kuhubiri habari njema hiyo ya Ufalme ilikuwa sababu kuu ya kuwapo kwa kundi la Kikristo.

Wakristo wa mapema, kama Paulo, walichukua kazi hiyo ya kuhubiri kwa uzito. Hivyo, wakati adui za Mungu walipodhani walikuwa wamezima nuru ya kweli kwa kumwua kwa ukatili “Mkuu wa uzima,” wafuasi wake waliendelea wakiwa nuru ya ulimwengu, wakihubiri kwa bidii nyingi. (Matendo 3:15) Hata mnyanyaso haukuzuia juhudi zao. Usimulizi wa Bibia wasema hivi: “Kila siku, ndani ya hekalu na nyumbani mwao [nyumba kwa nyumba, NW] hawakuacha kufundisha na kuhubiri habari njema za Yesu kwamba ni Kristo.” (Matendo 5:42) Hakuna jambo lililoweza kuwazuia!

Katika nyakati za ki-siku-hizi, Wakristo wamekuwa pia wakijishughulisha sana na utendaji wa kutoa ushahidi. Kuelekea mwishoni mwishoni mwa karne ya 19, wanafunzi wa Neno la Mungu wenye kudhamiria wakaanza kuona uhitaji wa kushiriki kweli za Biblia pamoja na wengine. Zion’s Watch Tower Tract Society—tengenezo ambalo limekuwa la kimataifa—ilifanyizwa kuwa shirika halali katika 1884. Wanafunzi wa Biblia hawa, waliojulikana tangu 1931 kuwa Mashahidi wa Yehova, wamejaza dunia kihalisi kwa maarifa ya Neno la Mungu. Kujishughulisha kwao katika utendaji huo kumetokeza jeshi kubwa lenye watu zaidi ya milioni nne! Na bila shaka hesabu yao itaendelea kuongezeka chini ya mwongozo wa Yehova.—Isaya 60:22.

Je! Unafanya Sehemu Yako?

Yesu alisema hivi: “Mavuno ni mengi, lakini watenda kazi ni wachache.” (Mathayo 9:37, 38) Katika 1990 watu karibu milioni kumi walihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Yesu. Kuna uwezekano wa ajabu kama nini wa kuongezeka kwa uvuno wa ulimwenguni pote! Lakini katika kushangilia juu ya ongezeko hilo lenye kuendelea, ni lazima kila mmoja ajiulize, ‘Mimi ninashiriki kadiri gani katika kazi hiyo tukufu? Je! ninafanya hivyo kwa ukawaida—kila juma ikiwezekana?’

Ni lazima wazee waongoze katika kazi hiyo wakiwa ‘vielelezo kwa lile kundi.’ (1 Petro 5:3) Ni kweli, wazee wengi wana kazi za kimwili. Ndivyo na mtume Paulo alipokuwa Korintho. Hata hivyo, aliweka kando wakati kwa ajili ya utendaji wa kuhubiri wa kikawaida. Vivyo hivyo wazee wengi leo wanajishughulisha sana na utendaji wa kiroho wakati wa miisho ya juma. Hiyo yaweza kuwa na matokeo ya nguvu na ya kitia moyo kwa wote kundini. Miezi fulani wakati jitihada ya kipekee inapowekwa, makundi mengi huwa na wahubiri wayo wengi katika utumishi wa painia. Siri ni nini? Wazee huongoza katika kuhubiri na katika kutengeneza mipango ya utumishi wa shambani pia.

Watumishi wa huduma waweza pia kuwa uvutano mzuri kwa kundi wakishiriki kikawaida katika utumishi wa shambani. Kumbuka, Maandiko yanawataka wawe “wazito, . . . wanaohudumu kwa njia nzuri.” (1 Timotheo 3:8, 13, NW) Kuwa mwaminifu katika utumishi wa shambani ni muhimu kwa ndugu ili kustahili kuwa mzee au mtumishi wa huduma.—Tito 1:8, 9.

Kama Paulo, wengine wanaweza kupunguza kazi ya kimwili na hivyo kupainia. Hesabu ya mapainia wa kawaida, wasaidizi, na wa pekee iliongezeka kutoka 137,861 miaka mikumi tu iliyopita hadi 536,508 katika 1990. Kwa hakika, ni baraka na kibali cha Yehova tu ambacho kingeweza kutokeza jambo hilo. Hata hivyo, ni lazima mapainia watumie wakati kwa hekima, si kuhesabu wakati tu. Mapainia, je, mnajitayarisha vizuri na mna matokeo mazuri katika utumishi? Je! mnajaribu kufanya maendeleo daima ili utumishi wenu kwa kweli uwe na matokeo?

Thawabu za Utumishi Uliosawazika

Je! unathamini habari yenye kuhifadhi uhai inayotolewa kila mwezi katika gazeti Mnara wa Mlinzi na andamani lalo, Amkeni!? Bila shaka unaithamini. Je! kuthamini kwako kumekusukuma ushiriki katika kueneza majarida hayo? Dada mmoja katika Botswana alifanya hivyo. Hapo kwanza alikuwa amepinga kweli, lakini mume wake alikuwa akimsomea yaliyo ndani ya magazeti. Baada ya muda aligeuka moyo akawa Shahidi. Ingawa hawezi kusoma, anafanikiwa sana katika kuangusha magazeti, akisema hivi, “Sijui kusoma, lakini mume wangu hunisomea magazeti haya. Mimi nayaonea shangwe, nami nina uhakika kwamba wewe utayaonea shangwe pia.”

Kwa nini usishiriki katika kazi hii ya kuokoa uhai kila juma? Mara upatapo sifa za kiroho, kundi la Kikristo litaterema kukusaidia kuanza. Hata hivyo, kuangusha magazeti ni sehemu moja tu ya utumishi. Yeyote anayejishughulisha na habari njema hujitahidi kuwa na utumishi uliosawazika. Kwa mfano, Watch Tower Society huchapisha mamilioni ya vitabu vilivyojadiliwa, navyo hutolewa kwa watu vikiwa chanzo cha daima zaidi cha chakula kizuri cha kiroho. Je! umekuwa stadi vya kutosha katika utumishi wako wa kuangusha vitabu, kama vile Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani?

Na vipi juu ya watu wanaoonyesha kupendezwa? Je! unaweka rekodi nzuri ili uweze kufanya ziara za kuwarudia? Ziara kama hizo zaweza kuongoza kwenye sehemu ya utumishi inayoleta shangwe iliyo kubwa zaidi—kazi ya mafunzo ya Biblia nyumbani. Kumbuka, Yesu alituamuru kwenye Mathayo 28:19, 20 ‘tukafanye wanafunzi, tukiwabatiza.’ Hiyo inamaanisha kujifunza Biblia pamoja nao. Ni kweli, kuanza funzo la Biblia huhitaji kusisitiza. Shahidi mmoja alikutana na wenzi wa ndoa wazee ambao walikubali funzo la Biblia nyumbani kwa uchangamfu. Lakini waliahirisha funzo hilo majuma matatu mfululizo. Hatimaye funzo likaanzishwa. Halafu, kwa muda fulani, wenzi wa ndoa hao wakafuta funzo karibu kila juma la pili. Hata hivyo, mwishowe, mke alifanya maendeleo hadi hatua ya kubatizwa. “Baada ya kubatizwa,” ndugu akumbuka, “macho yake yalijawa na machozi ya furaha, ambayo yalileta machozi ya furaha kwa mke wangu nami pia.” Naam, kujishughulisha sana na habari njema kunaleta shangwe isiyoelezeka!

Fanya Upatikane!

Yesu Kristo na mtume Paulo wametoa violezo vizuri vya ujitoaji vya kuigwa na sisi. Nasi tuna vielelezo bora vingi miongoni mwa Mashahidi wa Yehova katika nyakati za ki-siku-hizi. Wakati unafaa sasa kwa wote wanaojua habari njema kuwa watendaji kamili katika kuijulisha kwa wengine. Biblia inatuhakikishia kwamba kazi ngumu yote hiyo ‘siyo ya bure.’—1 Wakorintho 15:58.

Kama Paulo, wengi wana wajibu wa kifedha kutimiza. Kwa sababu ya hiyo, huenda wengi wasiweze kupainia. Lakini kwa msaada wa Yehova, wote wanaweza kufuata shauri zuri lililotolewa kwenye Warumi 12:11, HNWW: “Msilegee katika bidii, muwe wachangamfu rohoni katika kumtumikia Bwana.” Na kama hali zinabadilika ili ziruhusu wakati zaidi utumiwe katika utumishi wa Yehova, yeyote ampendaye Yehova kwa kweli, kama Paulo, ataitwaa nafasi. Jishughulishe sana na habari njema! Kufanya hivyo hakutakuletea tu mibaraka sasa bali wakati ujao matokeo yatakuwa uhai wa milele pamoja na shangwe na furaha isiyo na mwisho!—Mathayo 19:28, 29.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki