Saidia Wengine Watambue Thamani ya Biblia
1 Yesu aliandaa kile wanafunzi wake walichohitaji. Luka 24:45 laripoti hivi: “Akawafunulia akili zao wapate kuelewa na maandiko.” Alijua kwamba ikiwa walitaka kuwa na kibali cha Baba yake, ilikuwa muhimu kwao kujifunza na kuelewa Neno la Mungu, Biblia. (Zab. 1:1, 2) Kazi yetu ya kuhubiri ina lengo lilo hilo. Mradi wetu ni kuanzisha mafunzo ya Biblia, ambapo twaweza ‘kuwafundisha watu wayashike yote ambayo Yesu aliamuru.’ (Mt. 28:20) Ukiwa wakumbuka hilo, yafuatayo ni baadhi ya madokezo ya mambo yawezayo kusaidia unapofanya ziara za kurudia.
2 Ikiwa hapo mwanzo ulizungumza juu ya kitabu “Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu?” waweza kuendelea na mazungumzo yako katika njia hii:
◼ “Ningependa kukuonyesha jambo jingine lionyeshalo thamani itumikayo ya shauri la Biblia. Watu wengi huliona kuwa jambo gumu kupatana vizuri na wengine. Twaweza kufanya nini ili tusitawishe uhusiano bora zaidi na wale wanaotuzunguka? [Baada ya itikio, fungua kwenye ukurasa 168, fungu 15, na usome Mathayo 7:12. Ongeza mawazo yanayoelezwa katika fungu 16.] Hiki ni kielelezo kingine cha hekima inayopatikana katika shauri la Biblia. Wakati ujao nikutembeleapo, ningependa kukuonyesha shauri ambalo Biblia hutoa kusaidia waume na wake wapate furaha kubwa zaidi katika uhusiano wao.” Fanya mipango ya kurudi kuzungumza juu ya kurasa 170-172, ambazo zaonyesha kile ambacho Biblia hupendekeza kwa maisha ya familia yenye furaha.
3 Ikiwa ulisema na mtu aliyeonyesha kupendezwa na Biblia, basi labda mfikio huu waweza kuwa wenye matokeo katika kuanzisha funzo:
◼ “Karibu watu wote unaoongea nao watakuambia wangependa kuishi katika ulimwengu wenye amani na ulio salama. Ikiwa hilo ndilo kila mtu ataka, kwa nini tuna ulimwengu ambao umejawa na msukosuko na ujeuri mwingi sana? [Ruhusu itikio.] Biblia New World Translation hukuonyesha ni mahali gani katika Biblia uwezapo kupata jibu la swali hilo.” Fungua kwenye ukurasa 1659, na uonyeshe “Bible Topics for Discussion” Na. 43a, “Ni nani mwenye daraka la taabu ya ulimwengu.” Soma 2 Wakorintho 4:4. Eleza jinsi Mungu atakavyomharibu Ibilisi na atakavyoleta ulimwengu wenye amani na furaha idumuyo. Soma Ufunuo 21:3, 4. Kisha waweza kusema: “Wakati ujao nikutembeleapo, ningependa kukuonyesha baadhi ya maandiko yanayoeleza ni kwa nini waweza kutazamia ulimwengu bila taabu.”
4 Ikiwa ulitumia mfikio wa moja kwa moja ili kuanzisha funzo na kulikuwa na itikio zuri, waweza kusema hili unaporudi:
◼ “Tulipoongea hapo mbele, tulizungumza juu ya baadhi ya sababu kwa nini kuna manufaa ya kujifunza Biblia. Jitihada ya moyo mweupe ya kujifunza zaidi yaweza kutusaidia tuthamini kile ambacho Mungu ametuwekea. [Soma Yohana 17:3.] Tumesitawisha programu ya funzo la Biblia ambayo imesaidia maelfu wajifunze zaidi juu ya kile ambacho Mungu ameahidi na jinsi tuwezavyo kumpendeza.” Onyesha kitabu Kuishi Milele, pitia vichwa vya sura, na uonyeshe jinsi tunavyoongoza funzo la Biblia.
5 Ikiwa wewe waweza kusaidia watu wenye moyo mweupe watambue thamani ipitayo yote ya Neno la Mungu, umewasaidia katika njia bora iwezekanayo. Hekima ambayo wao waweza kujifunza kupitia funzo la kurasa zayo yaweza kuwa “mti wa uzima,” ambao utawaletea furaha nyingi.—Mit. 3:18.