Kujitoa kwa Hiari
1 Mtunga-zaburi Daudi alitabiri kwamba watu wa Yehova “wanajitoa kwa hiari”; yaani, “wajitoleaji wa mara moja.” (Zab. 110:3; NW, kielezi-chini) Hilo kwa hakika latimizwa miongoni mwa ushirika wetu wa ulimwenguni pote wa akina ndugu. Wakati wa miaka minne ya utumishi iliyopita, watu wa Yehova wametoa saa zaidi ya bilioni moja katika kueneza habari njema ya Ufalme kila mwaka. Na kuongezea kuhubiri na kazi ya kufanya wanafunzi, kuna njia nyingi tunazoweza kujitolea wenyewe kwa hiari ili kusaidia wengine.
2 Njia Tunazoweza Kuonyesha Hiari Yetu: Wengine katika kutaniko huenda wakahitaji msaada wafike kwenye mikutano. Kwa nini usijitolee kwenda nao? Wengine huenda wakawa wagonjwa, wenye kupungukiwa kiafya, au wamelazwa hospitalini. Je, unaweza kujitolea uwatembelee au uwasaidie kwa njia fulani? Huenda kukawa na familia au mtu anayehitaji kitia-moyo. Je, umefikiria kutoa mwaliko wahudhurie funzo lako la familia pindi kwa pindi? Huenda painia au mtangazaji akahitaji mwandamani katika huduma. Kwa nini usijitolee kuhubiri pamoja katika utumishi? Hizi ni baadhi ya njia ambazo twaweza kujitolea tufanye yaliyo mema kuelekea wale tulio na uhusiano nao katika imani.—Gal. 6:10.
3 Akina ndugu wanaweza kuonyesha kwamba wako tayari kutumiwa katika tengenezo la Yehova kwa kujitahidi kufikia sifa za ustahili kuwa wazee na watumishi wa huduma. (1 Tim. 3:2-10, 12, 13; Tito 1:5-9) Tunapoendelea kukua katika idadi, kuna uhitaji wa ndugu wenye sifa za kustahili ambao wako tayari kuchukua uongozi katika kuhubiri na kufundisha na katika kuchunga makutaniko.—1 Tim. 3:1.
4 Labda baadhi yetu twaweza kujiweka tayari kwa ajili ya utumishi wa Yehova kwa kadiri kubwa kwa kujiandikisha kuwa mapainia-wasaidizi mara kwa mara. Pia, tukifanya marekebisho machache yafaayo katika ratiba yetu, huenda tukaweza kuwa mapainia-wasaidizi kwa kuendelea au hata tuchukue utumishi wa painia wa kawaida. Je, hali zaturuhusu tuweze kuhamia eneo lililo na uhitaji mkubwa zaidi ili tusaidie? Je, tungeweza kujiweka tayari ili kutumikia katika Betheli na hivyo tuchangie moja kwa moja maendeleo ya kazi ya ulimwenguni pote? Mengi zaidi pia yanafanywa katika ujenzi wa Majumba ya Ufalme, Majumba ya Kusanyiko, na majengo ya tawi ulimwenguni pote, ambapo hiari ya kufanya kazi yahitajiwa sana. Wale ambao wamejitolea kwa kazi hizi nzuri wanathaminiwa sana, nao wamebarikiwa kwelikweli!—Luka 6:38.
5 Hizi ni siku zenye kusisimua. Kupitia roho yake, Yehova anatimiza kazi ya ajabu duniani akiwa na watu wake wenye hiari! Kupitia tengenezo lake, wakati wowote Yehova atoapo mwaliko wa kushiriki katika utendaji ulioongezeka wa Ufalme, twafanya vema kujiuliza, ‘Je, mimi najitolea kwa hiari?’ Kisha twapaswa kuchunguza kwa njia ya sala mioyo na hali zetu. Ujitoaji kimungu wetu utatusukuma tufanye yote tuwezayo katika utumishi mtakatifu, hivyo tukifanya moyo wa Yehova utereme zaidi!—Sef. 3:17.