Elimu ya Kilimwengu na Miradi Yako ya Kiroho
1 Kupata elimu nzuri ya msingi unapokuwa mchanga kwaweza kukupa stadi zinazohitajiwa ili uweze kusoma na kuandika vizuri na kuelewa kwa ujumla jiografia, historia, hesabu, na sayansi. Wakati uo huo, unaweza kujifunza kufikiri waziwazi, kuchanganua mambo, kutatua matatizo, na kutoa mawazo yenye kusaidia. Elimu kama hiyo itakunufaisha maishani mwako. Elimu ya kilimwengu yaweza kuhusianaje na miradi yako ya kiroho maishani na kukusaidia upate “hekima kamili na busara”?—Mit. 3:21, 22.
2 Uwe Mwenye Mafaa Katika Utumishi wa Mungu: Unapokuwa shuleni, uwe makini darasani na ufanye vizuri masomo ya shule unayofanyia nyumbani. Ukiwa na mazoea mazuri ya kusoma na kujifunza, unaweza kuchunguza Neno la Mungu kwa urahisi zaidi na kuendelea kuwa mwenye nguvu kiroho. (Mdo. 17:11) Ujuzi uliosawazika utakusaidia uzungumze na watu wa malezi, mapendezi, na itikadi mbalimbali unapowakuta katika huduma. Elimu unayopata shuleni itakusaidia unapotekeleza madaraka yako ya Kikristo katika tengenezo la Mungu.—Linganisha 2 Timotheo 2:21; 4:11.
3 Jifunze Kujitegemeza: Ukitia bidii, unaweza pia kujifunza stadi zinazohitajiwa ili kujiruzuku baada ya kumaliza shule. (Linganisha 1 Timotheo 5:8.) Chagua masomo yako kwa uangalifu. Badala ya kukazia fikira somo ambalo halina fursa nyingi za kupata kazi, fikiria kujifunza kazi au stadi itakayokuwezesha kupata kazi inayofaa mahali popote. (Mit. 22:29) Mazoezi hayo yatafanya uweze kujitegemeza iwapo unaweza kuamua kutumikia mahali palipo na uhitaji mkubwa.—Linganisha Matendo 18:1-4.
4 Kupata elimu nzuri ya msingi shuleni kwaweza kukusaidia upanue huduma yako. Tia bidii upate stadi zinazohitajiwa kujitegemeza unaposonga mbele katika utumishi wa Yehova. Hivyo, elimu yako itakusaidia kufikia miradi yako ya kiroho.