Je, Wewe Umefunguliwa Mlango wa Upainia Sasa?
1 Andiko letu la mwaka wa 1999 latukumbusha kwamba tungali katika “siku [ya Yehova] ya wokovu.” (2 Kor. 6:2) Lakini siku yake ya wokovu itakwisha upesi. Kisha “siku yake ya hukumu” itaanza. (2 Pet. 2:9) Ingawa Yehova aendelea kuwapa wanadamu fursa ya kupata wokovu, inasisimua kama nini kuona idadi inayoongezeka inayozidi kuitikia!
2 Watu wa Yehova wamejitahidi kukabili mwito wa kufikia watu wenye kupendezwa kabla haijawa kuchelewa mno. Kwa wahubiri wengi wa Ufalme, hilo limemaanisha kufanya utumishi wa painia. Je, wewe umefunguliwa mlango wa kupainia sasa? Kwa nini twauliza?
3 Uthamini Waonyeshwa: Kama ilivyotangazwa katika Huduma ya Ufalme Yetu ya Januari 1999, takwa la saa kwa mapainia wa kawaida na wasaidizi limepunguzwa. Ili kutimiza takwa hilo jipya, mapainia wa kawaida wanahitajiwa kutoa muda wa saa 70 katika huduma kila mwezi, hiyo ikiwa jumla ya muda wa saa 840 kwa kila mwaka wa utumishi. Mapainia-wasaidizi watatumia muda wa saa 50 katika utumishi kila mwezi. Haya ni baadhi ya maelezo mengi ya uthamini ambayo yamepokewa kwa sababu ya marekebisho hayo:
“Hiyo ni zawadi yenye baraka kama nini kutoka kwa Baba yetu wa kimbingu!”
“Hakuna maneno yanayoweza kueleza hisiamoyo za shangwe, upendo, na shukrani kwa uandalizi huu!”
“Itafanya iwe rahisi zaidi kutimiza ratiba zetu!”
“Twasali kwamba wengi zaidi waingie katika utumishi wa wakati wote na kufurahia baraka zinazotokana na kumtumikia Yehova kwa njia kubwa.”
4 Tukaribiapo upeo wa siku ya Mungu ya wokovu, ni dhahiri kwamba Yehova hutaka watu wake wampe sifa kubwa ya mwisho. Ukubwa na mkazo wa ujumbe huu umeongezeka kwa (1) ukuzi wenye kuendelea wa idadi ya wapiga-mbiu wa Ufalme na (2) kila mmoja kutafuta namna ya kuongeza anachoweza katika kuhubiri Ufalme. Yehova yule “aikuzaye,” amefanikisha njia zote mbili kwa kubariki roho ya utayari ya wote waliokubali wokovu.—1 Kor. 3:6, 7; Zab. 110:3.
5 Usikose Kusudi Lake: Paulo alisihi Wakristo wenzake hivi kuhusu siku ya Yehova ya wokovu: “Tukiwa tunafanya kazi pamoja naye [Yehova], twawasihi sana nyinyi pia msiipokee fadhili isiyostahiliwa ya Mungu na kukosa kusudi layo.” ‘Hatutakosa kusudi lake’ tukiiona hii kuwa “wakati wenye kukubalika hasa” kufanyia bidii wokovu wa wengine katika kila fursa. (2 Kor. 6:1, 2) Leo, maneno ya Paulo yana umuhimu hata zaidi. Wakristo wanaoonyesha upendo wa moyoni kwa Yehova huliona kuwa pendeleo kushiriki kikamili kwa kadiri wawezavyo katika huduma aliyowapa. Je, wewe sasa waweza kushiriki kikamili zaidi katika huduma ukiwa painia wa kawaida?
6 Ni Mradi Usiopita Kiasi: Katika Afrika Mashariki, mradi wetu ni kuona mapainia wa kawaida 4,000 wakijiandikisha kufikia Septemba 1. Twaamini kwamba huu ni mradi usiopita kiasi unaoweza kufikiwa. Kwa nini tuna uhakika hivyo? Mnamo Machi 1997 ndugu na dada 3,645 walifanya upainia-msaidizi, na Aprili 1998, karibu 3,900 walifanya upainia-msaidizi. Wengi wao waliripoti muda wa saa 60—upungufu wa saa 10 tu kwa takwa la painia wa kawaida! Hata kama 700 tu kati ya waliofanya upainia-msaidizi wanajiandikisha kuwa mapainia wa kawaida kabla ya mwisho wa mwaka huu wa utumishi, tungeweza kuanza Septemba kwa mapainia wa wakati wote 4,000 au zaidi!
7 Ratiba Yahitajiwa: Je, ungali waona kuwa vigumu kufikia muda wa saa 70 za utumishi wa shambani kwa mwezi? Labda kufikiria kuhusu muda wa saa 17 kwa juma kutasaidia. Ukitumia ratiba za mfano zilizo kwenye ukurasa ufuatao, jaribu kutengeneza ratiba ya painia wa kawaida itakayofaa hali zako binafsi. Unapoipanga, zungumza na mapainia wenye uzoefu upate maoni yao ya jinsi ya kusawazisha utumishi wa painia na madaraka ya kibinafsi na ya familia. Mwulize mwangalizi wenu wa mzunguko jinsi ambavyo mapainia katika mzunguko huo hupanga ratiba ya utumishi kila juma. Kisha mtegemee Yehova abariki mipango yako ya kupainia.—Mit. 16:3.
8 Ufanye Uwe Mradi wa Familia: Je, mmefikiria kufanya upainia kuwe mradi wa familia? Huenda familia yenu ikaketi kuzungumzia jinsi ambavyo—kwa mpango mzuri na ushirikiano mzuri—mshiriki mmoja au wawili wa familia wanaweza kupainia. Ni jambo lenye kueleweka ikiwa wengine wataona kwamba baada ya kuchanganua hali zao kwa unyofu hali zao hazitawaruhusu wafanye upainia wa kawaida wakati huu. Ikiwa ndivyo ilivyo, weka mradi wa kupainia wakati ujao. Lakini anza kufanya mipango ya kujitahidi kuweka tarehe hususa ya kuanza kupainia. Labda unaweza kufanya upainia-msaidizi mara kadhaa wakati wa mwaka huu ili ufikie hatua kwa hatua utumishi wa painia wa kawaida.
9 Zaidi ya mapainia 3,300 wanaotumikia sasa katika Afrika Mashariki wana hali tofauti-tofauti. Si wote walio na afya nzuri, na wengi wao wana madaraka ya familia na wajibu wa kutimiza wa kifedha. Mapainia wengi wamepita umri wa miaka 50, na baadhi yao wana zaidi ya umri wa miaka 65. Wengine ni waseja, na wengi wana umri wa miaka 20 au chini. Robo hivi ya mapainia wote ni akina ndugu, na wengi wao wana madaraka ya familia na ya kutaniko. Wote hao ‘wanajinunulia kabisa wakati unaofaa’ wa kupainia, jambo ambalo katika hali nyingi limemaanisha kuishi maisha sahili lakini yenye uradhi.—Kol. 4:5.
10 Je, Wahitaji Kufanya Mambo Yawe Sahili? Kufanya maisha yako yawe sahili ndio ufunguo unaokufungulia mlango wa kupainia. Je, maisha yako ni kama nyumba kubwa mno iliyo na vyumba na vitu visivyohitajiwa, ikihitaji wakati mwingi, fedha, na kazi kuitunza? Ikiwa ndivyo ilivyo, kujirekebisha ufae hali za kiasi zaidi kwaweza kukuruhusu ufanye upainia. Je, unaweza kupunguza wakati unaotumia katika kazi ya kimwili? Je, unaweza kununua wakati kutoka katika shughuli zisizo za maana au kuonyesha usawaziko mzuri zaidi kuhusu wakati unaotumia katika tafrija?
11 Biblia hutuonya hivi kwa upole kwenye 1 Timotheo 6:8: “Tukiwa na riziki na cha kujifunika, tutakuwa wenye kuridhika na vitu hivi.” Kuridhika na vitu vichache ni jambo la maana ili kufanya yote tuwezayo katika utumishi wa Yehova na kufanya iwe rahisi zaidi kutanguliza masilahi ya kiroho. (Mt. 6:22, 33) Kwenye ukurasa wa 104 wa 1998 Yearbook katika ripoti ya Japani, madokezo kadhaa yametolewa kuhusu sababu inayofanya kuwe na roho nzuri ya upainia katika nchi hiyo. Fikiria hii moja: “Ni kweli kwamba kwa ujumla nyumba za Wajapani ni zenye kiasi, hivyo zikihitaji wakati mchache kutunzwa, na kwa ujumla, maisha huwa sahili kidesturi.” Je, kimsingi, hiyo si maana ya 1 Timotheo 6:8?
12 Tufeni pote, watumishi wa Mungu wanahubiri habari njema kwa mkazo zaidi kabla siku ya Yehova ya wokovu kufikia mwisho wake. Ni jambo la kupongezwa kwamba mwaka jana wastani wa karibu watu 700,000 walishiriki katika namna fulani ya utumishi wa painia kila mwezi. Je, waweza kurekebisha maisha yako ili ujiunge nao? Twakuomba uchunguze hali zako kwa uangalifu na kwa sala unapojibu swali hili: “Je, Wewe Umefunguliwa Mlango wa Upainia Sasa?”
[Blabu katika ukurasa wa 3]
MRADI: MAPAINIA WA KAWAIDA 4,000!
[Sanduku katika ukurasa wa 4]
Ratiba za Mfano za Painia wa Kawaida
Saa 17 zahitajiwa kila juma
Siku Moja ya Katikati ya Juma na Mwisho-Juma
Siku Saa
Ijumaa 8
Jumamosi 6
Jumapili 3
Jumla ya Saa: 17
Siku Mbili za Katikati ya Juma na Jumamosi
Siku Saa
Jumanne 7
Alhamisi 7
Jumamosi 3
Jumla ya Saa: 17
Siku Tatu za Katikati ya Juma na Jumapili
Siku Saa
Jumatatu 5
Jumatano 5
Ijumaa 5
Jumapili 2
Jumla ya Saa: 17
Jioni Mbili na Mwisho-Juma
Siku Saa
Jumatatu 3
Jumatano 3
Jumamosi 8
Jumapili 3
Jumla ya Saa: 17
Tengeneza Ratiba Yako Mwenyewe ya Painia wa Kawaida
Siku Saa
Jumatatu
Jumanne
Jumatano
Alhamisi
Ijumaa
Jumamosi
Jumapili
Jumla ya Saa: 17