Kujifunza Kitabu Mwabudu Mungu
Kitabu Mwabudu Mungu wa Pekee wa Kweli kimetayarishwa ili kitumiwe tunapojifunza na wapya baada ya kumaliza kitabu Ujuzi. Kujifunza kitabu hicho kwenye Funzo la Kitabu la Kutaniko kutatusaidia tukitumie katika huduma na kuzidisha upendo na uthamini wetu kwa Yehova na tengenezo lake. Tunawezaje kufaidika kabisa tunapojifunza kitabu Mwabudu Mungu?
Kuongoza Funzo: Kwa kuwa tutakuwa tukijifunza sura moja kila juma, waangalizi wa funzo la kitabu watahitaji kutumia wakati vizuri. Itafaa waepuke kutumia wakati mwingi katika mafungu ya kwanza ili kuwe na wakati wa kutosha kuzungumzia mambo mazito ambayo kwa kawaida huwa katika mafungu ya baadaye. Kuzungumzia kifupi sanduku la kurudia mwishoni mwa kila funzo kutawasaidia waliohudhuria wakumbuke mambo makuu.
Nusu ya sura za kitabu Mwabudu Mungu zina mafungu fulani yenye maswali ya kutafakari na ya mazungumzo. Mfano mmoja ni ukurasa wa 48-49. Si lazima maswali hayo yasomwe pamoja na mafungu. Mwangalizi anapoyazungumzia pamoja na kikundi, anapaswa kuhakikisha maandiko yaliyotajwa yanasomwa na kuzungumziwa kadiri wakati unavyoruhusu.
Kutayarisha Mapema: Kutayarisha vizuri kwa ajili ya funzo si kupiga mistari majibu tu. Kutafakari maandiko yaliyotajwa kutatusaidia kutayarisha maelezo na, la muhimu zaidi, mioyo yetu. (Ezra 7:10) Sote tunaweza kutiana moyo kwa kutoa maelezo kwa kiasi.—Rom. 1:11, 12.
Kujifunza kitabu Mwabudu Mungu kutatusaidia kumkaribia Yehova na kuwa tayari kuwasaidia watu wanyoofu wajiunge nasi kumwabudu. (Zab. 95.6; Yak. 4:8) Sote na tufaidike kabisa kutokana na mpango huo mzuri wa kiroho.