Sanduku la Swali
◼ Je, ni jambo linalofaa kwa wahudhuriaji kupiga makofi baada ya kila sehemu kwenye Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na Mkutano wa Utumishi?
Wakati Muumba, Yehova, alipoweka msingi wa dunia, ‘nyota za asubuhi zilipiga vigelegele pamoja kwa shangwe, na wana wote wa Mungu wakaanza kupaaza sauti kwa kushangilia.’ (Ayu. 38:7) Wana hao wa Mungu ambao ni malaika walitamani kumsifu Yehova kwa kazi yake kuu ya uumbaji ambayo ilionyesha hekima, wema, na nguvu zake kwa njia mpya.
Ni vizuri tuonyeshe shukrani zinazotoka moyoni kwa ajili ya jitihada za ndugu zetu na kwa habari wanazotoa. Kwa mfano, kwa kawaida tunapiga makofi baada ya hotuba na maonyesho kwenye mikutano ya pekee, kama vile makusanyiko. Wakati na jitihada zaidi zinahitajiwa ili kutayarisha sehemu hizo. Tunapopiga makofi tunatoa shukrani kwa ajili ya bidii nyingi ambayo imefanywa na msemaji na vilevile tunamshukuru Yehova kwa mafundisho anayoandaa kupitia Neno lake na tengenezo lake.—Isa. 48:17; Mt. 24:45-47.
Namna gani kupiga makofi baada ya sehemu zinazotolewa kwenye Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na Mkutano wa Utumishi? Hakuna sheria zinazokataza kupiga makofi ikiwa makofi yanapigwa ili kuonyesha shukrani ya kutoka moyoni, kama vile baada ya mwanafunzi kutoa hotuba yake ya kwanza kwenye shule. Hata hivyo, kupiga makofi kunaweza kugeuka kwa urahisi kuwa zoea la kidesturi na hivyo kupoteza umuhimu wake. Hivyo, kwa kawaida hatupigi makofi baada ya kila sehemu inayotolewa.
Hata ingawa kwa kawaida hatupigi makofi baada ya kila sehemu inayotolewa kwenye Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na Mkutano wa Utumishi, kuna njia nyingine za kuonyesha shukrani zetu kwa ajili ya mafundisho na jitihada za wale wanaotoa sehemu hizo. Tunaweza kufanya hivyo kwa kuendelea kuwa makini na kuwasikiliza wasemaji kwa uangalifu sana. Na baada ya mikutano, kwa kawaida tunaweza kumwona kibinafsi yule aliyetoa sehemu hiyo na kumshukuru kwa jitihada zake.—Efe. 1:15, 16.