Tumia Biblia kwa Ustadi
1. Kwa nini Biblia ni muhimu sana?
1 Kutumia kwa ustadi Neno la Mungu lililoandikwa kwa mwongozo wa roho yake, kunatuwezesha kutangaza na kufundisha kweli kwa njia yenye kueleweka, na kufunua mapokeo na mafundisho ya uwongo ya wanadamu.—2 Tim. 2:15; 1 Pet. 3:15.
2. Ni nini kitakachotusaidia kupata maandiko kwa ustadi zaidi?
2 Ongeza Ustadi Wako wa Kuitumia Biblia: Kadiri unavyoendelea kutumia kifaa fulani, ndivyo ustadi wako wa kukitumia unavyoongezeka. Unaposoma Biblia nzima, unapata kujua habari kuu ya Biblia na pia unaweza kukumbuka maandiko na kuyapata kwa urahisi zaidi. Ustadi wako wa kuitumia Biblia unapoongezeka, utasema kwa shauku na kwa uhakika zaidi katika huduma ya shambani au unapowahubiria watu isivyo rasmi.—1 The. 1:5.
3, 4. (a) Tunaweza kuongeza ustadi wetu wa kuitumia Biblia kwa njia zipi? (b) Je, umetumia njia nyingine kuongeza ustadi wako wa kutumia Maandiko?
3 Wakati wa mikutano ya kutaniko, jitahidi kufungua Biblia yako na kufuatana na msemaji kila anaposoma andiko. Unapojifunza kibinafsi au kutayarisha sehemu zitakazozungumziwa katika mikutano ya kutaniko, soma maandiko yasiyonukuliwa na utafakari kuhusu jinsi yanavyoweza kutumiwa. Wengi wanaona kwamba kusoma maandiko moja kwa moja katika Biblia badala ya kutumia kompyuta au karatasi zilizochapwa, kunawasaidia kuyapata baadaye wanapohitaji kuyatumia katika huduma.—Yoh. 14:26.
4 Familia fulani wametenga wakati wa kukariri maandiko ya Biblia ili kuyakumbuka. Wanaweza kufanya hivyo kwa kutumia kadi ambazo zina andiko fulani kwenye upande mmoja na maneno ya andiko hilo kwenye upande ule mwingine. Wanatumia kadi hizo kuona kama wanaweza kukumbuka maneno yaliyonukuliwa ni ya andiko gani, nalo andiko ambalo limeonyeshwa tu bila kunukuliwa linasema nini. Kufanya mazoezi kuhusu mambo ya kusema shambani, na jinsi ya kuitumia Biblia kujibu swali au kumjibu mtu anayepinga, huboresha ustadi wetu.
5. Kwa nini tunahitaji kuongeza ustadi wetu tunapoitumia Biblia?
5 Biblia haina kifani. Biblia tu ndiyo inayoweza kuwafanya watu ‘wawe wenye hekima kwa ajili ya wokovu.’ (2 Tim. 3:15) Kwa kuwa watu wengi katika eneo letu hawajui kwamba Biblia ina hazina, tuna sababu nzuri ya kuongeza ustadi wetu tunapowaonyesha jinsi Biblia inavyoweza kuwanufaisha.—Met. 2:1-5.