Umewatayarisha Watoto Wako?
1 . Kwa nini ni muhimu kwa watoto wanaoenda shule kuwa tayari?
1 Watoto wetu wanaporudi shuleni baada ya likizo, wanakabili magumu na mikazo mingi. Pia, wanakuwa na fursa za ‘kutoa ushahidi juu ya ile kweli’ (Yoh. 18:37) Wako tayari?
2 . Ili wawe tayari, watoto wako wanapaswa kujua nini?
2 Je, watoto wako wanaelewa kabisa kushiriki katika sherehe za kitaifa na sikukuu za kipagani kunahusisha nini na kwa nini hilo ni kosa? Wako tayari kukabili mikazo ya kufuatilia elimu ya juu, kuanzisha urafiki wa kimapenzi, na kutumia kileo au dawa za kulevya? Je, watasema tu dini yao inawakataza kushiriki utendaji usiofaa, au wanajua jinsi ya kueleza wanayoamini?—1 Pet. 3:15.
3 . Wazazi wanaweza kutumiaje jioni ya Ibada ya Familia kuwatayarisha watoto wao?
3 Tumia Jioni ya Ibada ya Familia: Bila shaka, mtakuwa na mazungumzo mengine kuhusu matatizo mbalimbali ambayo huenda watoto wako wakakabili katika kipindi chote cha mwaka wa shule. Watoto wako watapata ujasiri wa kupambana na matatizo iwapo mtayazungumzia kabla ya wao kurudi shuleni. Kwa nini usitumie jioni moja au zaidi za Ibada ya Familia kufanya hivyo? Unaweza kuwauliza watoto wako ni nini kinachowahangaisha zaidi wanapojiandaa kurudi shuleni. Mambo ambayo mliyashughulikia katika miaka iliyopita yanaweza kurudiwa kwa sababu sasa watoto wana umri mkubwa na wana uelewaji mwingi zaidi. (Zab. 119:95) Unaweza kutia ndani vipindi vya mazoezi ambavyo unaigiza kama mwalimu, mshauri, au mwanafunzi mwingine. Wafundishe watoto wako jinsi ya kujibu wakitumia Biblia na vifaa vingine kama vile kitabu Kutoa Sababu na Vijana Huuliza. Mzazi mmoja alitumia vipindi vya mazoezi kutayarisha watoto wake wawafikie walimu wao wapya kila mwanzo wa mwaka na kuwajulisha kwamba wao ni Mashahidi wa Yehova.—Ona Mnara wa Mlinzi, Desemba 15, 2010, ukurasa wa 3-5.
4 . Wazazi wenye hekima watafanya nini?
4 Matatizo ambayo vijana Wakristo wanakabili katika hizi siku za mwisho yanazidi kuwa ‘magumu kushughulika nayo.’ (2 Tim. 3:1) Wazazi wenye hekima watajaribu kuyafikiria kimbele. (Met. 22:3) Kabla ya shule kufunguliwa kila muhula, fanya yote uwezayo kuwasaidia watoto wako wawe tayari.