Kujifunza Kutoka kwa Wahubiri Wenye Uzoefu Zaidi
Tunawathamini sana wahubiri wenye uzoefu walio kutanikoni. Baadhi yao wamekuwa wakimtumikia Yehova kwa miaka mingi. Wengine wameboresha uwezo wao wa kuhubiri hivi karibuni. Wahubiri hao wamejionea jinsi ambavyo Yesu ameongoza kutaniko la Kikristo katika siku hizi za mwisho kwa kupanua kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi. (Mt. 28:19, 20) Kwa kushiriki katika huduma, wamepata “nguvu zinazopita zile za kawaida” wanapokabili hali ngumu na majaribu. (2 Kor. 4:7) Kuna mengi ya kujifunza kutoka kwa wahubiri hao wenye uzoefu. Wanapopata fursa, wao hufurahia sana kufundisha wengine mambo waliyojifunza. (Zab. 71:18) Hivyo basi, tunapaswa kutafuta fursa za kujifunza kutoka kwao. Tunawezaje kufanya hivyo?
Katika Huduma: Ili wahubiri wapya au wasio na uzoefu mwingi wawe na matokeo katika huduma, wanahitaji kuzoezwa. Wanaweza kujifunza mambo mengi sana kwa kuwatazama wahubiri wakomavu wanapokuwa katika huduma. (Ona makala katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Februari 15, 2015 yenye kichwa, “Dumisha Bidii Yako Katika Huduma” fungu la tatu chini ya kichwa kidogo, “Wasaidie Wasio na Uzoefu.”) Umefaidikaje kwa kuhubiri na wahubiri kama hao?
Je, unaweza kumwomba mhubiri mwenye uzoefu ahubiri pamoja nawe? Ikiwa mhubiri huyo ana matatizo ya afya au ya uzee, labda unaweza kuongoza moja kati ya mafunzo yako ya Biblia nyumbani kwake mara kwa mara. Baada ya funzo, mwombe mhubiri huyo akupe mashauri na madokezo.
Tenga Wakati wa Kuwa Pamoja Nao: Wafahamu vizuri wahubiri wenye uzoefu kwa kutenga wakati wa kuwa pamoja nao. Unaweza kumwalika mmoja wao kwenye ibada yenu ya familia. Ikiwa mhubiri ana matatizo ya afya au ya uzee, je, mnaweza kufanya ibada ya familia nyumbani kwake? Muulize jinsi alivyoipata kweli. Amepata baraka gani? Amejionea ukuzi gani wa kiroho katika eneo lenu? Kumtumikia Yehova kumemletea shangwe gani?
Kumbuka kwamba huenda wahubiri hao wasiweze kutimiza mambo mengi. Kama ilivyo kwetu sote, wahubiri ambao wametumikia kwa muda mrefu wana zawadi zinazotofautiana katika huduma. (Rom. 12:6-8) Wengine wana umri mkubwa na hivyo huenda wasiweze kutumia muda mwingi pamoja nasi. Hata hivyo, tunaweza kujifunza mengi kutoka kwa wahubiri hao wenye uzoefu ambao wamemtumikia Yehova kwa uaminifu.