-
Kukua Katika Ujuzi Sahihi Juu ya KweliMashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
Sura ya 10
Kukua Katika Ujuzi Sahihi Juu ya Kweli
MASHAHIDI WA YEHOVA hawajakusudia kuanzisha mafundisho mapya, njia mpya ya ibada, dini mpya. Badala ya hivyo, historia yao ya kisasa huonyesha jitihada ya kudhamiria ya kufundisha yale yanayopatikana katika Biblia, Neno la Mungu lililopuliziwa. Wao huelekeza kwalo likiwa msingi wa imani zao zote na njia yao ya maisha. Badala ya kusitawisha imani ambazo huonyesha mielekeo yenye kuendekeza ya ulimwengu wa kisasa, wao huendelea kujitahidi kujipatanisha kwa ukaribu zaidi na mafundisho na mazoea ya Kibiblia ya Ukristo wa karne ya kwanza.
Katika miaka ya mapema ya 1870, Charles Taze Russell na washirika wake walianzisha funzo la Biblia la moyo wa bidii. Ikawa wazi kwao kwamba Jumuiya ya Wakristo ilikuwa imeondoka sana katika mafundisho na mazoea ya Ukristo wa mapema. Ndugu Russell hakudai kuwa wa kwanza kutambua jambo hilo, naye alikiri waziwazi jinsi alivyokuwa na deni kwa wengine kwa usaidizi waliotoa wakati wa miaka yake ya mapema ya funzo la Maandiko. Alisema kwa uthamini juu ya kazi njema ambayo harakati tofauti-tofauti za yale Marekebisho Makubwa ya Kidini zilikuwa zimefanya ili kuacha nuru ya kweli iangaze kwa uangavu zaidi. Yeye alitaja kwa jina wanaume waliomzidi umri kama vile Jonas Wendell, George Stetson, George Storrs, na Nelson Barbour, ambao walichangia kibinafsi uelewevu wake wa Neno la Mungu katika njia mbalimbali.a
Pia yeye alitaarifu hivi: “Mafundisho mbalimbali tuaminiyo na ambayo huonekana kuwa mapya na ya asili na tofauti sana yaliaminiwa kwa namna fulani muda mrefu uliopita: mathalani—Kuchaguliwa, Neema ya Bure, Rudisho, Kuhesabiwa Haki, Utakaso, Utukuzo, Ufufuo.” Hata hivyo, mara nyingi ilikuwa kwamba kikundi kimoja cha kidini kilitofautishwa kwa uelewevu wa wazi zaidi wa kweli moja ya Biblia; kikundi kingine, na kweli tofauti. Kuendelea kwao zaidi kulizuiwa mara nyingi kwa sababu walifungwa na mafundisho na imani za kidini zilizokuwa na itikadi ambazo zilikuwa zimesitawi katika Babiloni na Misri ya kale au ambazo ziliazimwa kutoka wanafalsafa Wagiriki.
Lakini ni kikundi kipi, ambacho kikisaidiwa na roho ya Mungu, kingejipatia tena hatua kwa hatua “kiolezo cha maneno yenye afya” ambayo Wakristo wa karne ya kwanza walithamini sana? (2 Tim. 1:13, NW) Ni nani ambao ingefaa kusemwa kuwa kweli kwamba kijia chao kingekuwa “kama nuru nyangavu ambayo inaendelea kunurika na kunurika mpaka mchana upate kuthibitishwa imara”? (Mit. 4:18, NW) Ni nani ambao kwa kweli wangefanya ile kazi ambayo Yesu aliamuru aliposema: “Mtakuwa mashahidi wangu . . . hadi sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia”? Ni nani ambao hawangefanya wanafunzi tu bali pia ‘wangewafundisha kushika mambo yote’ ambayo Yesu aliamuru? (Mdo. 1:8; Mt. 28:19, 20, NW) Kwelikweli, je, wakati ulikuwa umekaribia ambapo Bwana angeonyesha utofautisho wa wazi kati ya wale walio Wakristo wa kweli aliowafananisha na ngano na wale wa mwigo ambao alitaja kuwa kama magugu (hasa, magugu ya aina ambayo hufanana sana na ngano mpaka yafikiapo ukomavu)?b (Mt. 13:24-30, 36-43) Ni nani ambao wangethibitika kuwa ndio yule “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ambaye kwake, Bwana-Mkubwa, Yesu Kristo, wakati wa kuwapo kwake katika mamlaka ya Ufalme, angeaminisha daraka zaidi kuhusiana na kazi iliyotabiriwa kwa ajili ya umalizio wa huu mfumo wa mambo?—Mt. 24:3, 45-47, NW.
Kuacha Nuru Iangaze
Yesu aliwaagiza wanafunzi wake washiriki pamoja na wengine nuru ya kweli ya kimungu waliyokuwa wamepokea kutoka kwake. “Ninyi ni nuru ya ulimwengu,” akasema. “Nuru yenu iangaze mbele ya watu.” (Mt. 5:14-16; Mdo. 13:47) Charles Taze Russell na washirika wake walitambua kwamba walikuwa na wajibu wa kufanya hivyo.
Je, wao waliamini kwamba walikuwa na majibu yote, ile nuru kamili ya kweli? Ndugu Russell alijibu swali hilo waziwazi hivi: “Hakika sivyo; wala hatutakuwa nayo mpaka ule ‘mchana mkamilifu.’” (Mit. 4:18) Mara nyingi walirejezea imani za Kimaandiko walizokuwa nazo kuwa “kweli ya sasa”—si wakiwa na wazo la kwamba kweli yenyewe hubadilika bali kwa wazo la kwamba uelewevu wao juu yayo ulikuwa wenye kuendelea.
Hawa wanafunzi wa Biblia wenye moyo wa bidii hawakuepuka wazo la kwamba kuna jambo kama kweli katika mambo ya dini. Walitambua Yehova kuwa “Mungu wa kweli” na Biblia kuwa Neno lake la kweli. (Zab. 31:5; Yos. 21:45; Yn. 17:17) Walijua kwamba kulikuwa na mengi ambayo hawakujua, lakini hawakujizuia kusema kwa usadikisho yale waliyokuwa wamejifunza katika Biblia. Na wakati mafundisho na mazoea ya kidini ya kimapokeo yalipopingana na yale waliyopata yamesemwa waziwazi katika Neno la Mungu lililopuliziwa, basi, kwa kumwiga Yesu Kristo walifunua uwongo, hata ingawa kufanya hivyo kulileta dhihaka na chuki juu yao kutoka kwa makasisi.—Mt. 15:3-9.
Ili kufikia na kulisha wengine kiroho, C. T. Russell alianza utangazaji, katika Julai 1879, wa gazeti Zions’s Watch Tower and Herald of Christ’s Presence.
Biblia—Neno la Mungu Kwelikweli
Usadikisho wa Charles Taze Russell katika Biblia haukuwa jambo la kukubali tu maoni ya kimapokeo yaliyopendwa na wengi wakati ule. Tofauti na hilo, jambo lililopendwa miongoni mwa wengi wakati ule lilikuwa uhakiki wa Biblia. Wale walioutetea walitilia shaka kutegemeka kwa maandishi ya Biblia.
Akiwa kijana, Russell alikuwa amejiunga na Congregational Church naye alikuwa mtendaji katika kazi yalo, lakini kutopatana na akili kwa mafundisho ya kimapokeo kulimwongoza katika hali ya kutilia shaka mafundisho. Alipata kwamba yale aliyokuwa amefundishwa hayangeweza kutetewa kwa kutumia Biblia kwa njia yenye kuridhisha. Kwa hiyo akatupilia mbali mafundisho hayo ya kanisa, na pia Biblia. Halafu, alichunguza dini kuu za Mashariki, lakini hizo pia zilithibitika kuwa zisizoridhisha. Kisha akaanza kujiuliza kama labda imani za Jumuiya ya Wakristo zilikuwa zikiiwakilisha vibaya Biblia. Kwa kutiwa moyo na jambo alilosikia jioni moja kwenye mkutano wa Waadventisti, alianza kujifunza Maandiko kwa utaratibu. Yale aliyoona yakifunuka mbele yake yalikuwa kwelikweli Neno la Mungu lililopuliziwa.
Alikuja kuvutiwa sana na upatani wa Biblia yenyewe pamoja na utu wa Yeye ambaye hutambuliwa kuwa Mtungaji wa Kimungu wayo. Ili kusaidia wengine wanufaike na jambo hilo, baadaye aliandika kitabu The Divine Plan of the Ages, ambacho alitangaza katika 1886. Katika kitabu hicho alitia ndani mazungumzo makuu juu ya “Biblia Ikiwa Ufunuo wa Kimungu Ikionwa kwa Kutumia Akili.” Kuelekea mwisho wa sura hiyo, yeye alitaarifu waziwazi hivi: “Kina na nguvu na hekima na mweneo wa ushuhuda wa Biblia hutusadikisha kwamba si binadamu, bali Mungu Mweza Yote, ndiye mtungaji wa mipango na mafunuo yayo.”
Usadikisho katika Biblia nzima kuwa Neno la Mungu huendelea kuwa msingi wa imani za Mashahidi wa kisasa wa Yehova. Ulimwenguni pote, wana misaada ya kujifunza ambayo huwasaidia kuchunguza binafsi uthibitisho wa kupuliziwa kwayo. Pande za habari hiyo huzungumzwa mara nyingi katika magazeti yao. Katika 1969 walitangaza kitabu Is the Bible Really the Word of God? Miaka 20 baadaye kitabu Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu? kilizungumzia tena habari ya uasilia wa Biblia, kilivuta fikira kwenye uthibitisho zaidi, na kikafikia mkataa uleule: Kwelikweli, Biblia ni Neno la Mungu lililopuliziwa. Kingine cha vitabu vyao, kilichochapwa kwanza katika 1963 na kupatanishwa na habari za karibuni zaidi katika 1990 (katika Kiingereza), ni “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa.” Habari nyingi zaidi zapatikana katika ensaiklopidia yao ya Biblia, Insight on the Scriptures, kilichotangazwa katika 1988.
Kutokana na funzo lao la kibinafsi na la kutaniko la habari kama hizo, wao wanasadikishwa kwamba ijapokuwa wanadamu kama 40 walitumiwa kuandika yale yaliyo katika vitabu 66 vya Biblia kwa pindi ya karne 16, kwa roho yake Mungu mwenyewe alielekeza kwa bidii uandikaji huo. Mtume Paulo aliandika: “Andiko lote limepuliziwa na Mungu.” (2 Tim. 3:16, NW; 2 Pet. 1:20, 21) Usadikisho huo ni jambo lenye nguvu katika maisha ya Mashahidi wa Yehova. Likitoa maelezo juu ya jambo hilo, gazeti la habari la Uingereza lilitaja hivi: “Kwa kila jambo analofanya Shahidi kuna sababu ya Kimaandiko. Kwa kweli, imani yao ya msingi ni kuitambua Biblia kuwa . . . ya kweli.”
Kupata Kumjua Mungu wa Kweli
Kadiri Ndugu Russell na washirika wake walivyojifunza Maandiko, haikuwachukua muda mrefu kuona kwamba Mungu aliyeonyeshwa katika Biblia siye mungu wa Jumuiya ya Wakristo. Hilo lilikuwa jambo la maana kwa sababu, kama vile Yesu Kristo alivyosema, mataraja ya watu ya uhai wa milele yalitegemea kujua kwao Mungu wa pekee wa kweli na yule aliyemtuma, Wakili Mkuu wake wa wokovu. (Yn. 17:3; Ebr. 2:10) C. T. Russell na kikundi kilichoshiriki pamoja naye katika funzo la Biblia walitambua kwamba haki ya Mungu ina usawaziko mkamilifu na hekima ya kimungu, upendo, na nguvu, na kwamba sifa hizo zinaonyeshwa katika kazi zake zote. Kwa msingi wa ujuzi waliokuwa nao wakati huo wa kusudi la Mungu, walitayarisha mazungumzo kuhusu sababu inayofanya uovu uruhusiwe na kuyatia katika kimojapo vichapo vyao vya mapema zaidi na ambacho kiligawanywa kwa wingi sana, kile kitabu cha kurasa 162 Food for Thinking Christians (Chakula kwa Wakristo Wenye Kufikiri), kilichotolewa kwanza kikiwa chapa ya pekee ya Zion’s Watch Tower katika Septemba 1881.
Funzo lao la Neno la Mungu liliwasaidia kujua kwamba Muumba ana jina la kibinafsi na kwamba yeye hufanya iwezekane kwa wanadamu kumjua na kufurahia uhusiano wa karibu naye. (1 Nya. 28:9; Isa. 55:6; Yak. 4:8) Watch Tower la Oktoba-Novemba 1881 lilitaja wazi hivi: “YEHOVA ndilo jina litumiwalo si kwa mwingine ila kwa Mtu Mkuu Kupita Wote—Baba yetu, na yeye ambaye Yesu alimwita Baba na Mungu.”—Zab. 83:18; Yn. 20:17.
Mwaka uliofuata, katika kujibu swali, “Je, nyinyi mwadai kwamba Biblia haifundishi kwamba kuna watu watatu katika Mungu mmoja?” jibu lililotolewa ni: “Ndiyo: Tofauti na hilo, [Biblia] hutuambia kwamba kuna Mungu mmoja na Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo ambaye vitu vyote vyatoka kwake (au aliyeumba vitu vyote). Basi sisi twaamini katika Mungu na Baba Mmoja, na pia katika Bwana mmoja Yesu Kristo . . . Lakini hao ni wawili wala si mtu mmoja. Wao ni mmoja tu katika maana ya kuwa katika upatani. Sisi twaamini pia katika roho ya Mungu . . . Lakini hiyo si mtu kama vile roho ya maibilisi na roho ya Ulimwengu na roho ya Mpinga-Kristo isivyokuwa mtu.”—Zion’s Watch Tower, Juni 1882; Yn. 17:20-22.
Uthamini Wenye Kukua Kuelekea Jina la Mungu
Hatua kwa hatua hao Wanafunzi wa Biblia walizidi kufahamu umaarufu ambao Maandiko yaliyopuliziwa yalilipa jina la kibinafsi la Mungu. Jina hilo lilikuwa limefichwa katika Kiingereza na tafsiri za Biblia za Douay ya Roma Katoliki na King James ya Protestanti, kama vile baadaye ilivyofanywa na tafsiri kadhaa katika lugha nyingi katika karne ya 20. Lakini tafsiri mbalimbali pamoja na vitabu vya marejezo kwenye Biblia vilishuhudia kwamba jina Yehova lapatikana mara elfu nyingi katika maandishi ya lugha za awali—kwa kweli mara nyingi zaidi ya jina jingine lolote, na mara nyingi zaidi ya jumla iliyounganishwa ya majina ya cheo kama vile Mungu na Bwana. Wakiwa “watu kwa ajili ya jina lake,” uthamini wao wenyewe kuelekea jina hilo la kimungu ulikua. (Mdo. 15:14, NW) Katika The Watch Tower la Januari 1, 1926, walitoa lile walilotambua kuwa suala ambalo lazima kila mtu alikabili, yaani, “Ni Nani Atamheshimu Yehova?”
Mkazo ambao waliweka juu ya jina la Mungu haukuwa jambo la ujuzi tu wa kidini. Kama ilivyoelezwa katika kitabu Prophecy (kilichotangazwa 1929), suala kuu linalokabili uumbaji wote wenye akili lahusu jina na neno la Yehova Mungu. Mashahidi wa Yehova hukazia kwamba Biblia huonyesha kwamba lazima kila mtu ajue jina la Mungu na kulitendea kuwa takatifu. (Mt. 6:9; Eze. 39:7) Lazima liondolewe suto lote ambalo limerundikiwa, si na wale tu ambao wamekuwa wakaidi waziwazi kwa Yehova bali pia na wale ambao wamemwakilisha vibaya kwa mafundisho na matendo yao. (Eze. 38:23; Rum. 2:24) Kwa msingi wa Maandiko, Mashahidi hutambua kwamba hali njema ya ulimwengu wote mzima na wakaaji wao yategemea kutakaswa kwa jina la Yehova.
Wajua kwamba kabla Yehova hajachukua hatua ya kuwaharibu waovu, ni wajibu na pendeleo la mashahidi wake kuwaambia wengine kweli juu yake. Mashahidi wa Yehova wamekuwa wakifanya hivyo duniani kote. Wamekuwa wenye bidii sana katika kutimiza daraka hilo hivi kwamba, kimataifa, yeyote ambaye hutumia sana jina Yehova anatambuliwa haraka kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova.
Kufichua Utatu
Wakiwa mashahidi wa Yehova, C. T. Russell na washirika wake walihisi sana daraka la kufichua mafundisho yaliyomwakilisha Mungu vibaya, ili kusaidia wapendao kweli wajue kwamba hayo hayakuwa na msingi wa Biblia. Wao sio waliokuwa wa kwanza kutambua kwamba Utatu si wa kimaandiko,c lakini walifahamu kwamba ikiwa wangekuwa watumishi waaminifu wa Mungu, walikuwa na daraka la kujulisha kweli juu ya utatu. Kwa ujasiri, walifunua mashina ya fundisho hilo kuu la Jumuiya ya Wakristo, kwa manufaa ya wote wapendao kweli.
Watch Tower la Juni 1882 lilitaarifu hivi: “Wanafalsafa wengi wapagani wakipata kwamba ingekuwa hekima kujiunga na orodha ya waliojiandikisha katika dini yenye kuzuka [namna fulani ya Ukristo ulioasi imani uliokubaliwa na maliki Waroma katika karne ya nne W.K.], walianza kutayarisha njia rahisi ya kuuendea kwa kujaribu kuvumbua milingano kati ya Ukristo na Upagani, na hivyo kuziunganisha zote mbili pamoja. Walifanikiwa vizuri sana. . . . Kwa kuwa ile theolojia ya kale ilikuwa na hesabu fulani ya miungu mikuu, pamoja na nusu-miungu mingi ya jinsia zote mbili, hao Wakristo-wapagani (tukiunda neno) wakaanza kutengeneza upya orodha ya theolojia hiyo mpya. Kwa hiyo, wakati huo, fundisho la Miungu watatu likabuniwa—Mungu Baba, Mungu Mwana, na Mungu Roho Mtakatifu.”
Baadhi ya makasisi walijaribu kulipa fundisho lao ladha ya Kibiblia kwa kunukuu maandiko kama vile 1 Yohana 5:7, lakini Ndugu Russell alitoa uthibitisho wa kuonyesha kwamba ilijulikana sana na wasomi kwamba sehemu ya andiko hilo ilikuwa maneno yaliyoongezwa, maneno bandia yaliyopachikwa na mwandishi kuunga mkono fundisho lisilopatikana katika Maandiko. Wateteaji wengine wa Utatu walitumia Yohana 1:1, lakini Watch Tower lilichanganua andiko hilo kwa msingi wa yaliyomo na habari inayolizunguka kuonyesha kwamba hilo haliungi mkono kwa vyovyote imani katika Utatu. Kupatana na hilo, katika toleo lalo la Julai 1883, Watch Tower lilisema hivi: “Funzo zaidi la Biblia badala ya funzo la maandishi ya kanisa lingalifanya habari hiyo kuwa wazi zaidi kwa wote. Fundisho la utatu linapingana kabisa na Maandiko.”
Ndugu Russell alifichua waziwazi upumbavu wa kudai kuamini Biblia na wakati uleule kufundisha fundisho kama vile Utatu, ambalo hupingana na yale ambayo Biblia husema. Hivyo aliandika hivi: “Wanajikuta wakiwa katika mapingano yenye mvurugo kama nini wale wasemao kwamba Yesu na Baba ni Mungu mmoja! Hilo lingehusisha ndani wazo la kwamba Bwana yetu Yesu alikuwa mnafiki alipokuwa duniani na alijisingizia tu kusema na Mungu katika sala, hali Yeye Mwenyewe alikuwa Mungu yuleyule. . . . Tena, sikuzote Baba amekuwa asiyeweza kufa, kwa hiyo hangeweza kufa. Basi, Yesu angaliwezaje kufa? Mitume ni mashahidi bandia wote kwa kujulisha kifo na ufufuo wa Yesu ikiwa Yeye hakufa. Hata hivyo, Maandiko hujulisha kwamba Yeye alikufa hakika.”d
Hivyo, mapema katika historia yao ya kisasa, Mashahidi wa Yehova walikataa katakata fundisho la Utatu la Jumuiya ya Wakristo kwa kupendelea fundisho lenye kupatana na akili, lenye kuchangamsha moyo la Biblia yenyewe.e Kazi ambayo wamefanya katika kutangaza kweli hizi na kuwapa watu kila mahali fursa ya kuzisikia imekuwa ya kadiri isiyopata kufikiwa kamwe na mtu mwingine au kikundi kingine chochote, wakati uliopita au wa sasa.
Hali ya Wafu Ni Nini?
Tangu alipokuwa kijana, C. T. Russell alihangaikia sana hali ya wakati ujao ya wale wasiokubali uandalizi wa Mungu wa wokovu. Alipokuwa kivulana tu, yeye aliamini yale yaliyofundishwa na makasisi juu ya helo; yeye alifikiri kwamba walikuwa wakihubiri Neno la Mungu. Alikuwa akitoka nje usiku na kuandika kwa chokaa maandiko ya Biblia katika mahali yanapoweza kuonekana waziwazi ili wafanyakazi wapitao hapo waweze kuonywa na kupata kuokolewa na hukumu mbaya sana ya mateso ya milele.
Baadaye, baada ya yeye mwenyewe kuwa amejionea yale ambayo kwa kweli Biblia hufundisha, alinukuliwa na mmoja wa washirika wake kuwa alitaarifu hivi: “Ikiwa Biblia inafundisha kwamba mateso ya milele ndiyo hukumu ya wote isipokuwa watakatifu, yapasa kuhubiriwa—naam, kwa sauti kuu ili wote wasikie, kila juma, kila siku, kila saa; ikiwa haifundishi hivyo, uhakika huo wapasa kujulishwa, na doa baya lenye kuvunjia heshima jina takatifu la Mungu liondolewe.”
Kwenye hatua ya mapema ya funzo lake la Biblia, C. T. Russell aliona waziwazi kwamba helo (kuzimu) si mahali pa mateso ya nafsi baada ya kifo. Yaelekea sana alisaidiwa katika jambo hilo na George Storrs, mhariri wa Bible Examiner, ambaye Ndugu Russell alimtaja kwa uthamini mchangamfu katika maandishi yake na ambaye yeye mwenyewe aliandika mengi juu ya yale aliyotambua katika Biblia kuwa ndiyo hali ya wafu.
Lakini namna gani juu ya nafsi? Je, Wanafunzi wa Biblia waliunga mkono imani ya kwamba hiyo ni sehemu ya mtu ya roho, kitu ambacho huendelea kuishi baada ya kifo cha mwili? Tofauti na hilo, katika 1903 Watch Tower lilitaarifu hivi: “Ni lazima sisi tuone kwa uangalifu kwamba somo si kwamba mtu ana nafsi, bali kwamba mtu ni nafsi, au aliyeko. Acha tutwae kielezi kutokana na asili—hewa tupumuayo: inafanyizwa kwa oksijeni na nitrojeni, hapana yoyote yazo ambayo ndiyo angahewa, au hewa; lakini zote mbili ziunganapo, kama zifanyavyo katika kiasi kifaacho cha kemikali, kitu kitokeacho ni angahewa. Ndivyo na nafsi. Mungu husema nasi kutokana na msimamo huu, wa kuwa sisi sote ni nafsi. Yeye hasemi na miili yetu wala pumzi ya uhai wetu, bali yeye husema na sisi tukiwa watu wenye akili, au nafsi. Akitangaza adhabu ya kuhalifu sheria yake, yeye hakusema na mwili wa Adamu hasa, bali na mtu, nafsi, aliyeko mwenye akili: ‘Wewe!’ ‘Katika siku ambayo wewe utakula kutokana nao wewe utakufa hakika.’ ‘Ile nafsi ambayo hufanya dhambi hiyo itakufa.’—Mwa 2:17; Eze. 18:20.” Hiyo ilipatana na yale ambayo Watch Tower lilikuwa limetaarifu mapema sana kama Aprili 1881.f
Basi, imani katika kutokufa kulikorithiwa kwa nafsi ya kibinadamu ilisitawije? Ni nani aliyekuwa mwanzilishi wayo? Baada ya kuchunguza kwa uangalifu Biblia na pia historia ya kidini, Ndugu Russell aliandika katika Watch Tower la Aprili 15, 1894 hivi: “Kwa wazi haikutoka katika Biblia . . . Biblia hujulisha waziwazi kwamba mtu ni mwenye kufa, kwamba yeye aweza kufa. . . . Tukichunguza historia, twapata kwamba, ingawa fundisho la kutokufa kwa kibinadamu halifundishwi na mashahidi wa Mungu waliopuliziwa, ndilo msingi hasa wa dini zote za kipagani. . . . Kwa hiyo, si kweli kwamba Socrates na Plato walikuwa ndio wa kwanza kulifunza: lilikuwa na mwenye kulifunza mapema zaidi ya yeyote wao, na hata hivyo mwenye uwezo zaidi. . . . Maandishi ya kwanza ya fundisho hilo bandia yapatikana katika historia ya kale zaidi ijulikanayo kwa mwanadamu—Biblia. Mfunzi huyo bandia alikuwa Shetani.”g
Kulielekeza “Bomba la Maji” Kwenye Helo
Kwa kupatana na tamaa yenye nguvu ya Ndugu Russell ya kuondolea jina la Mungu doa baya lililotokana na fundisho la moto wa helo wenye mateso ya milele, yeye aliandika trakti iliyozungumzia habari, “Je, Maandiko Hufundisha Kwamba Mateso ya Milele Ndiyo Mshahara wa Dhambi?” (The Old Theology, 1889) Humo alisema hivi:
“Nadharia ya mateso ya milele ilikuwa na chanzo cha kipagani ingawa kama ilivyoaminiwa na wapagani haikuwa fundisho lisilo la huruma kama vile ilivyopata kuwa baadaye, ilipoanza kujishikamanisha hatua kwa hatua na Ukristo wa jina tu wakati huo ulipochanganyana na falsafa za kipagani katika karne ya pili. Ilibaki juu ya uasi-imani mkubwa kubandika kwenye falsafa ya kipagani yale mambo mengi yenye kuogofya yanayoaminiwa sana sasa kwa ujumla, kuyachora kwenye kuta za makanisa, kama ilivyofanywa katika Ulaya, kuyaandika katika taarifa za imani zao na katika nyimbo zao za kidini, na kulipotoa sana Neno la Mungu ili kulipa kufuru hilo lenye kumvunjia Mungu heshima lile linaloonekana kuwa uungaji mkono wa kimungu. Kwa hiyo, ile imani ya kisasa isiyo na uthibitisho, huipokea ikiwa urithi, si kutoka kwa Bwana, wala mitume, wala manabii, bali kutoka kwa ile roho ya kuridhiana iliyodhabihu kweli na kusababu kuzuri, ikapotoa kwa njia ya aibu mafundisho ya Ukristo kwa kuwa na tamaa ya makuu isiyo takatifu na ugomvi juu ya mamlaka na mali na idadi za watu. Mateso ya milele yakiwa adhabu ya dhambi, mjeledi ambao wale wenye kuamini bila uthibitisho, wale wasiojua kitu na wenye ushirikina wa ulimwengu wamepigwa kwao ili watii ukatili kitumwa—hayakujulikana kwa wazee wa ukoo wa enzi zilizopita; hayakujulikana kwa manabii wa enzi ya Kiyahudi na hayakujulikana kwa Bwana na mitume; bali yamekuwa ndiyo fundisho kuu la Ukristo wa Jina tangu ule uasi-imani mkubwa. Mateso ya milele yalitangazwa kwa wote waliokinza au waliopuuza mamlaka ya Kanisa la Roma, na kupasishwa kwayo katika maisha haya kulianza kwa kadiri Kanisa la Roma lilivyokuwa na nguvu.”
Ndugu Russell alifahamu sana kwamba wengi zaidi kati ya watu wenye akili hawakuamini kikweli fundisho la moto wa helo. Lakini, kama vile alivyotaja, katika 1896, katika kijitabu What Say the Scriptures About Hell?, “kwa kuwa wao hufikiri kwamba Biblia hulifundisha, kila hatua ya maendeleo wafanyayo katika akili ya kweli na fadhili ya kidugu . . . katika visa vingi zaidi ni hatua ya kwenda mbali na Neno la Mungu, ambalo wao hushtakia fundisho hilo kwa uwongo.”
Ili kuwavuta watu kama hao wenye kufikiri warudie Neno la Mungu, yeye alitoa katika kijitabu hicho kila andiko katika King James Version ambamo neno helo lilipatikana, ili wasomaji waweze kujionea wenyewe yale ambayo hayo yalisema, na kisha akataarifu hivi: “Twashukuru Mungu, hatupati mahali kama hapo pa mateso ya milele kama inavyofundishwa kimakosa na taarifa za imani za kidini, na vitabu vya nyimbo za kidini, na mimbari. Hata hivyo tumepata ‘helo,’ sheoli, hadesi, ambamo jamii yetu yote ilihukumiwa kwenda kwa sababu ya dhambi ya Adamu, na ambamo wote watoka kwa kukombolewa na kifo cha Bwana yetu; na ‘helo’ hiyo ni ziara—hali ya kifo. Na sisi twapata ‘helo’ nyingine (gehena—kile kifo cha pili—uharibifu kabisa) iliyoletwa kwenye uangalifu wetu ikiwa adhabu ya mwisho juu ya wote ambao, baada ya kukombolewa na kuletwa kwenye ujuzi kamili wa kweli, na kwenye uwezo kamili wa kuutii, bado watachagua kifo kwa kuchagua mwendo wa kupinga Mungu na uadilifu. Na mioyo yetu yasema, Amina. Ni za haki, na za kweli, njia zako, Ee Mfalme wa mataifa. Ni nani asiyekucha, Ee Bwana na kulitukuza jina lako? Kwa kuwa wewe peke yako u mtakatifu kabisa. Na mataifa yote yatakuja na kuabudu mbele zako, kwa kuwa matendo yako ya haki yamedhihirishwa.”—Ufu. 15:3, 4.
Aliyokuwa akifundisha yalikuwa chanzo cha udhia na aibu kwa makasisi wa Jumuiya ya Wakristo. Katika 1903 alitolewa mwito wa kushindana kwenye mjadala wa hadhara. Hali ya wafu lilikuwa mojapo masuala katika mfululizo uliotokea wa mijadala kati ya C. T. Russell na Dakt. E. L. Eaton aliyetumikia akiwa msemaji wa muungano usio rasmi wa wahudumu Waprotestanti katika sehemu ya magharibi ya Pennsylvania.
Wakati wa mijadala hiyo Ndugu Russell alitegemeza imara hoja ya kwamba “kifo ni kifo, na kwamba wapendwa wetu, wafapo, kwa kweli wamekufa, kwamba hawako hai wala pamoja na malaika wala pamoja na roho waovu katika mahali pasipo na tumaini.” Ili kuunga mkono hilo, yeye alirejezea maandiko kama vile Mhubiri 9:5, 10; Warumi 5:12; 6:23; na Mwanzo 2:17. Yeye alisema hivi pia: “Maandiko yanapatana kabisa na yale ambayo wewe na mimi na mtu mwingine yeyote mwenye akili timamu, mwenye kusababu ifaavyo katika ulimwengu atakubali kuwa ndio utu wenye kupatana na akili na wenye kufaa wa Mungu wetu. Ni nini lijulishwalo kuhusu Baba yetu wa mbinguni? Kwamba yeye ni mwenye haki, kwamba yeye ni mwenye hekima, kwamba yeye ni mwenye upendo, kwamba yeye ni mwenye nguvu. Watu wote Wakristo watakiri sifa hizo za utu wa kimungu. Ikiwa ni hivyo, je, sisi twaweza kupata maana yoyote ya neno ambamo tungeweza kumfikiria Mungu kuwa mwenye haki na bado aadhibu kiumbe [aliyeumbwa kwa] mkono Wake kwa umilele wote, haidhuru dhambi yake ilikuwa nini? Mimi si mteteaji wa dhambi; wala siishi katika dhambi mimi mwenyewe, na mimi sihubiri dhambi kamwe. . . . Lakini nakuambia kwamba watu hawa wote waliopo hapa ambao ndugu yetu [Dakt. Eaton] asema wanasema bila staha kwa makufuru yao kwa Mungu na jina takatifu la Yesu Kristo wote ni watu ambao wamefundishwa fundisho hilo la mateso ya milele. Na wauaji-kimakusudi, wevi na watenda maovu wote waliomo gerezani, wote walifundishwa fundisho hilo. . . . Hayo ni mafundisho mabaya; yamekuwa yakidhuru ulimwengu kwa muda wote huu; hayo si sehemu ya fundisho la Bwana hata kidogo, na uwezo wa kuona wa kiroho wa ndugu yetu mpendwa ungali una giza.”
Inaripotiwa kwamba baada ya mjadala huo, kasisi mmoja aliyehudhuria alimwendea Russell na kusema: “Naterema kuona ukielekeza bomba la maji kwenye helo na kuuzima moto huo.”
Ili kueneza hata zaidi kweli juu ya hali ya wafu, Ndugu Russell alitumikia mfululizo wenye kuenea sana wa mikusanyiko ya siku moja, tokea 1905 kufika 1907, ambako alitoa hotuba ya watu wote, “Kwenda Helo na Kurudi! Nani Walio Humo? Tumaini la Kurudi kwa Wengi.” Kichwa hicho kiliamsha hamu, nacho kilivuta fikira sana. Wasikilizaji walijaa kabisa majumba ya kusanyiko katika majiji makubwa na madogo katika Marekani na Kanada kusikiliza hotuba hiyo.
Miongoni mwa wale waliovutwa sana na yale ambayo Biblia husema juu ya hali ya wafu alikuwa mwanafunzi wa chuo kikuu katika Cincinnati, Ohio, aliyekuwa akijitayarisha kuwa mhudumu Mpresbiteri. Katika 1913 alipokea kutoka kwa ndugu yake kijitabu Where Are the Dead? (Wafu Wako Wapi?), kilichoandikwa na John Edgar, Mwanafunzi wa Biblia ambaye pia alikuwa daktari katika Scotland. Mwanafunzi aliyepokea kijitabu hicho alikuwa Frederick Franz. Baada ya kukisoma kwa uangalifu, alijulisha kwa uthabiti hivi: “Hii ndiyo kweli.” Bila kusita, alibadili miradi yake maishani akaingia katika huduma ya wakati wote akiwa kolpota mweneza-evanjeli. Katika 1920 akawa mshiriki wa wafanyakazi wa makao makuu ya Watch Tower Society. Miaka mingi baadaye akawa mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova na, baadaye, msimamizi wa Watch Tower Society.
Dhabihu ya Fidia ya Yesu Kristo
Katika 1872, kuhusiana na uchunguzi wake wa Maandiko, Ndugu Russell na washirika wake walifikiria upya habari ya kurudishwa, kwa kufikiria fidia iliyotolewa na Yesu Kristo. (Mdo. 3:21, KJ) Alisisimuka alipoona kwenye Waebrania 2:9 kwamba ‘Yesu alionja mauti kwa neema ya Mungu kwa ajili ya kila mtu.’ Hilo halikumwongoza aamini katika wokovu wa kila mtu, kwa kuwa yeye alijua kwamba Maandiko husema pia kwamba lazima mtu adhihirishe imani katika Yesu Kristo ili aokolewe. (Mdo. 4:12; 16:31) Lakini alianza kufahamu—ijapokuwa si mambo yote kwa wakati uleule—fidia ya Yesu Kristo ilifanya wanadamu wapate fursa nzuri kama nini. Iliwafungulia njia wapate kile ambacho Adamu alikuwa amepoteza, taraja la uhai wa milele katika ukamilifu wa kibinadamu. Ndugu Russell hakukaa kimya juu ya jambo hilo; yeye alitambua umaana mkubwa wa fidia naye akaitegemeza kwa juhudi, hata wakati washirika wake wa karibu waliporuhusu kufikiri kwao kupotoshwe na maoni ya kifalsafa.
Kufikia katikati ya 1878, Ndugu Russell alikuwa amekuwa, kwa mwaka mmoja na nusu hivi, mhariri-msaidizi wa gazeti Herald of the Morning, ambalo N. H. Barbour alikuwa mhariri mkuu. Lakini wakati Barbour, katika toleo la Agosti 1878 la gazeti lao, alipodharau fundisho la Kimaandiko la fidia, Russell alijibu kwa kutetea kwa juhudi kweli hiyo muhimu ya Biblia.
Chini ya kichwa “Ule Ufuniko,” Barbour alikuwa ametoa kielezi cha jinsi alivyohisi juu ya fundisho hilo, akisema hivi: “Mimi namwambia boi wangu, au mmoja wa watumishi, James aumapo dada yake, wewe kamata inzi, uchome mwili wake kwa sindano umtundike ukutani, nami nitamsamehe James. Hiyo yatolea kielezi fundisho la kutoa kilicho badala.” Ingawa alidai kuamini katika fidia, Barbour alilirejezea kuwa “si la kimaandiko, na lenye kuchukiza sana kwa mawazo yetu yote ya haki”h lile wazo la kwamba kwa kifo chake Kristo alilipa adhabu ya dhambi kwa ajili ya uzao wa Adamu.
Katika toleo lile hasa lililofuata la Herald of the Morning (Septemba 1878), Ndugu Russell alipinga kwa nguvu sana yale ambayo Barbour alikuwa ameandika. Russell alichanganua yale ambayo Maandiko husema kwelikweli na upatani wayo na “ukamilifu wa haki [ya Mungu], na hatimaye rehema na upendo wake mkuu” kama ulivyoonyeshwa kwa njia ya upaji wa fidia. (1 Kor. 15:3; 2 Kor. 5:18, 19; 1 Pet. 2:24; 3:18; 1 Yoh. 2:2) Kufikia masika yaliyofuata, baada ya jitihada nyingi za kusaidia Barbour aone mambo Kimaandiko, Russell aliacha kutegemeza Herald kifedha; na kuanzia toleo la Juni 1879, jina lake halikuonekana tena akiwa mhariri-msaidizi wa kichapo hicho. Msimamo wake wa ujasiri, usio wa kuridhiana kuhusiana na fundisho hilo kuu la Biblia ulikuwa na matokeo makubwa sana.
Muda wote wa historia yao ya kisasa, Mashahidi wa Yehova wametetea daima fundisho la Kimaandiko la fidia. Toleo lilelile la kwanza la Zion’s Watch Tower (Julai 1879) lilikazia kwamba “ustahili kuelekea Mungu umo . . . katika dhabihu kamilifu ya Kristo.” Katika 1919, kwenye mkusanyiko uliodhaminiwa na International Bible Students Association huko Cedar Point, Ohio, programu iliyochapwa ilionyesha kwa njia yenye kutokeza maneno “Karibuni! Nyinyi Nyote Mwaminio Katika Ile Dhabihu Kuu ya Fidia.” Upande wa ndani wa jalada la mbele la Mnara wa Mlinzi huendelea kuvuta fikira kwenye fidia, ukisema hivi kuhusu kusudi la gazeti hilo: “Hutia moyo kuwa na imani katika Mfalme wa Mungu anayetawala sasa, Yesu Kristo, ambaye damu yake iliyomwagwa yafungulia wanadamu njia ya kupata uhai wa milele.”
Wenye Kuendelea, Si Wenye Kufungwa na Itikadi za Kidini
Uelewevu wa wazi wa Neno la Mungu haukuja mara hiyo. Katika visa vingi Wanafunzi wa Biblia walifahamu jambo moja katika kile kigezo cha kweli lakini hawakuelewa kila jambo. Hata hivyo, wao walikuwa tayari kujifunza. Hawakufungwa na itikadi za kidini; walikuwa wenye kuendelea. Yale waliyojifunza walishiriki na wengine. Wao hawakujisifu kwa mambo waliyofundisha; walitafuta ‘kufundishwa na Yehova.’ (Yn. 6:45, NW) Nao walikuja kuthamini kwamba Yehova huwezesha kuwa na uelewevu wa mambo madogomadogo ya kusudi lake katika wakati wake mwenyewe na katika njia yake mwenyewe.—Dan. 12:9; linganisha Yohana 16:12, 13.
Kujifunza mambo mapya hutaka marekebisho katika maoni. Ikiwa makosa yatakubaliwa na mabadiliko yenye manufaa kufanywa, unyenyekevu wahitajiwa. Sifa hiyo na matunda yayo yatamanika kwa Yehova, na mwendo kama huo huvuta sana wapendao kweli. (Sef. 3:12) Lakini unadhihakiwa na wale ambao hujisifia itikadi za kidini ambazo zimeendelea bila kubadilika kwa karne nyingi, ingawa hizo zilifanyizwa na wanadamu wasiokamilika.
Jinsi ya Kurudi kwa Bwana
Ilikuwa katika miaka ya katikati ya 1870 kwamba Ndugu Russell na wale waliokuwa wakichunguza Maandiko pamoja naye walitambua kwamba Bwana arudipo angekuwa asiyeonekana kwa macho ya kibinadamu.—Yn. 14:3, 19.
Ndugu Russell alisema hivi baadaye: “Tulihisi tumehuzunishwa sana na kosa la Waadventisti wa Pili, ambao walikuwa wakimtarajia Kristo katika mwili, na kufundisha kwamba ulimwengu na vyote vilivyomo isipokuwa Waadventisti wa Pili ungeteketezwa katika 1873 au 1874, ambao nyakati zao zilizowekwa kimbele na kukata tamaa na mawazo hafifu kwa ujumla kwa habari ya lengo na jinsi ya kuja kwake yalileta kwa kadiri fulani suto juu yetu na juu ya wale wote waliotamani sana na kupiga mbiu ya kuja kwa Ufalme wake. Maoni hayo yenye makosa yaliyoshikiliwa kwa ujumla hivyo juu ya lengo na pia jinsi ya kuja kwa Bwana yaliniongoza kuandika kijitabu—‘The Object and Manner of Our Lord’s Return.’” Kijitabu hicho kilitangazwa katika 1877. Ndugu Russell alichapisha na kugawanya nakala 50,000 zacho.
Katika kijitabu hicho, yeye aliandika hivi: “Sisi twaamini maandiko hufundisha, kwamba, wakati wa kuja Kwake na kwa wakati fulani baada ya Yeye kuwa amekuja, Yeye ataendelea kuwa asiyeonekana; baadaye akijidhihirisha au kujionyesha Mwenyewe katika hukumu mbalimbali na namna mbalimbali, hivi kwamba ‘kila jicho litamwona Yeye.’” Katika kuunga mkono hilo, yeye alizungumzia maandiko kama vile Matendo 1:11 (‘yeye atakuja jinsi iyo hiyo mlivyomwona akienda’—yaani, bila kuonekana na ulimwengu) na Yohana 14:19, (“bado muda kidogo zaidi na ulimwengu hautaniona tena,” NW). Ndugu Russell pia alirejezea uhakika wa kwamba The Emphatic Diaglott, ambayo ilikuwa imetangazwa kwanza kwa namna kamili katika 1864 ikiwa na tafsiri ya Kiingereza ya neno kwa neno katikati ya mistari, ilitoa uthitibisho wa kwamba neno la Kigiriki pa·rou·siʹa lilimaanisha “kuwapo.” Katika kuchanganua utumizi wa Biblia wa usemi huo, Russell alieleza katika kijitabu hicho hivi: “Neno la Kigiriki litumiwalo kwa ujumla kurejezea kuja kwa pili—Parousia, litafsiriwalo mara nyingi kuja—sikuzote huonyesha kuwapo kwake mwenyewe, kuwa amekuja, amewasili na halionyeshi kamwe kuwa njiani [akija], kama vile tutumiavyo neno kuja.”
Alipokuwa akizungumzia kusudi la kuwapo kwa Kristo, Russell alieleza wazi kwamba hilo halingekuwa jambo ambalo lingetimizwa katika kitambo kimoja cha kutikisa ulimwengu. “Kuja kwa pili, kama kule kwa kwanza,” yeye akaandika, “ni kwa kipindi cha wakati, na si tukio la kitambo.” Wakati wa pindi hiyo, akaandika, “kundi dogo” lingepewa thawabu yao pamoja na Bwana wakiwa warithi-washirika wa Ufalme wake; wengine, labda mabilioni, wangepewa fursa ya uhai mkamilifu juu ya dunia iliyorudishwa kwenye uzuri wa Edeni.—Luka 12:32.
Katika muda wa miaka michache tu, kwa msingi wa funzo zaidi la Maandiko, Russell alitambua kwamba Kristo hangerudi bila kuonekana tu bali pia angeendelea kuwa asiyeonekana, hata wakati adhihirishapo kuwapo kwake kwa hukumu juu ya waovu.
Katika 1876, Russell alipokuwa amesoma kwa mara ya kwanza nakala ya Herald of the Morning, alikuwa amejifunza kwamba kulikuwa kikundi kingine ambacho wakati huo kiliamini kwamba kurudi kwa Kristo kungekuwa kusikoonekana na ambacho kilishirikisha kurudi huko na baraka kwa ajili ya familia zote za dunia. Kutokana na Bw. Barbour, mhariri wa kichapo hicho, Russell akaja pia kushawishwa kwamba kuwapo kusikoonekana kwa Kristo kulikuwa kumeanza katika 1874.i Fikira zilivutwa baadaye kwenye jambo hilo kwa kichwa kidogo “Mpiga-Mbiu wa Kuwapo kwa Kristo,” kilichoonekana juu ya jalada la Zion’s Watch Tower.
Utambuzi wa kwamba kuwapo kwa Kristo ni kwa kutoonekana ukawa msingi wa maana ambao juu yao uelewevu wa unabii mwingi wa Biblia ungejengwa. Hao Wanafunzi wa Biblia wa mapema walitambua kwamba kuwapo kwa Bwana kwapaswa kuwa hangaikio la kwanza la Wakristo wote wa kweli. (Mk. 13:33-37) Walipendezwa sana na kurudi kwa Bwana-Mkubwa na walikuwa chonjo kuona uhakika wa kwamba walikuwa na daraka la kukutangaza, lakini walikuwa hawajatambua mambo yote madogomadogo. Hata hivyo, yale ambayo roho ya Mungu iliwawezesha kuelewa tangu wakati wa mapema sana yalikuwa yenye kutokeza kwelikweli. Mojapo kweli hizo ilihusu ile tarehe ya maana sana iliyoonyeshwa na unabii wa Biblia.
Mwisho wa Nyakati za Mataifa
Kwa muda mrefu habari ya kronolojia ya Biblia ilikuwa imewavutia sana wanafunzi wa Biblia. Waelezaji walikuwa wameonyesha maoni mbalimbali juu ya unabii wa Yesu kuhusu “nyakati za Mataifa” na maandishi ya Danieli juu ya ndoto ya Nebukadreza kuhusu kile kisiki cha mti kilichofungwa kwa pingu muda wa “nyakati saba.”—Luka 21:24, KJ; Dan. 4:10-17.
Mapema kama 1823, John A. Brown, ambaye kitabu chake kilitangazwa katika London, Uingereza, alihesabu zile “nyakati saba” za Danieli sura ya 4 kuwa zenye urefu wa miaka 2,520. Lakini yeye hakutambua waziwazi tarehe ambayo kipindi hicho cha wakati wa kiunabii kilianza au wakati kingekoma. Hata hivyo, yeye alihusianisha hizo “nyakati saba” na Nyakati za Mataifa za Luka 21:24. Katika 1844, E. B. Elliott, kasisi Mwingereza, alivuta uangalifu kwenye 1914 kuwa tarehe iwezekanayo kuwa ukomo wa “nyakati saba” za Danieli, lakini yeye alionyesha pia maoni tofauti yaliyoelekeza kwenye wakati wa Mapinduzi ya Ufaransa. Robert Seeley, wa Uingereza, katika 1849, alishughulikia habari hiyo kwa njia iyo hiyo. Angalau kufikia 1870, kichapo kilichohaririwa na Joseph Seiss na washiriki wake na kuchapwa katika Philadelphia, Pennsylvania, kilikuwa kikionyesha hesabu ambazo zilielekeza kwenye 1914 kuwa tarehe ya maana, hata ingawa sababu kiliyotoa ilitegemea kronolojia ambayo C. T. Russell alikataa baadaye.
Halafu, katika matoleo ya Agosti, Septemba, na Oktoba 1875 ya Herald of the Morning, N. H. Barbour alisaidia kupatanisha mambo madogomadogo ambayo yalikuwa yameonyeshwa na wengine. Akitumia kronolojia iliyotungwa na Christopher Bowen, ambaye ni kasisi katika Uingereza, na kutangazwa na E. B. Elliott, Barbour alihusianisha mwanzo wa Nyakati za Mataifa na kuondolewa kwa Mfalme Sedekia kutoka kwenye ufalme wake kama ilivyotabiriwa kwenye Ezekieli 21:25, 26, akaelekeza kwenye 1914 kuwa waonyesha mwisho wa Nyakati za Mataifa.
Mapema katika 1876, C. T. Russell alipokea nakala moja ya Herald of the Morning. Mara hiyo yeye aliandikia Barbour kisha akatumia wakati pamoja naye katika Philadelphia wakati wa kiangazi, wakizungumzia, miongoni mwa mambo mengine, vipindi vya wakati wa kiunabii. Muda mfupi baada ya hapo, katika makala moja yenye kichwa “Nyakati za Mataifa: Zakoma Wakati Gani?,” Russell pia alitoa sababu juu ya habari hiyo kwa kutumia Maandiko akataarifu kwamba uthibitisho ulionyesha kwamba “nyakati saba zitakoma katika A.D. 1914.” Makala hiyo ilichapwa katika toleo la Oktoba 1876 la Bible Examiner.j Kile kitabu Three Worlds, and the Harvest of This World, kilichotokezwa katika 1877 na N. H. Barbour kwa kushirikiana na C. T. Russell, kilielekeza kwenye mkataa huohuo. Baada ya hapo, matoleo ya mapema ya Watch Tower, kama yale ya tarehe ya Desemba 1879 na Julai 1880, yalivuta fikira kwenye 1914 W.K. kuwa mwaka wa maana sana kwa maoni ya unabii wa Biblia. Katika 1889 sura nzima ya nne ya Buku 2 la Millennial Dawn (baadaye liliitwa Studies in the Scriptures) ilitumiwa kuzungumzia “Nyakati za Mataifa.” Lakini ukomo wa Nyakati za Mataifa ungemaanisha nini?
Hawa Wanafunzi wa Biblia hawakuwa na uhakika kabisa ni jambo gani lingetukia. Walisadikishwa kwamba tokeo halingekuwa kuteketezwa kwa dunia na kufutiliwa mbali kwa uhai wa kibinadamu. Badala ya hivyo, walijua kwamba ingeonyesha hatua yenye maana katika utawala wa kimungu. Mwanzoni, walifikiri kwamba kufikia tarehe hiyo Ufalme wa Mungu ungekuwa umepata udhibiti kamili, wa ulimwengu wote mzima. Wakati jambo hilo halikutukia, uhakika wao katika unabii mbalimbali wa Biblia ulioonyesha tarehe hiyo haukuyumbayumba. Walifikia mkataa kwamba, badala ya hivyo, tarehe hiyo ilionyesha tu mwanzo kwa habari ya utawala wa Ufalme.
Hali kadhalika, mwanzoni walifikiri pia kwamba taabu za duniani pote zikifikia upeo katika machafuko ya utawala (ambayo walielewa kwamba yangeshirikishwa na vita ya “siku kubwa ya Mungu Mweza-Yote”) yangetangulia tarehe hiyo. (Ufu. 16:14, NW) Lakini, miaka kumi kabla ya 1914, Watch Tower lilidokeza kwamba msukosuko wa ulimwenguni pote ambao ungetokeza kuangamizwa kwa mipango yote ya kibinadamu ungekuja mara tu baada ya mwisho wa Nyakati za Mataifa. Walitarajia mwaka 1914 ulete badiliko kubwa kwa Yerusalemu, kwa kuwa unabii ulikuwa umesema kwamba ‘Yerusalemu ungekanyagwa’ mpaka Nyakati za Mataifa zitimie. Walipoona 1914 ukikaribia na bado hawakuwa wamekufa wakiwa wanadamu na ‘kunyakuliwa katika mawingu’ wamlaki Bwana—kupatana na matarajio ya mapema—walitumaini sana kwamba badiliko lao lingetukia mwishoni mwa Nyakati za Mataifa.—1 The. 4:17.
Kadiri miaka ilivyopita nao wakachunguza na kuchunguza tena Maandiko, imani yao katika unabii mbalimbali iliendelea kuwa yenye nguvu, nao hawakusita kutaarifu yale waliyotarajia yangetukia. Kwa mafanikio ya kiwango mbalimbali, walijaribu kuepuka kushikilia bila uthibitisho mambo madogomadogo ambayo hayakutajwa moja kwa moja katika Maandiko.
Je, “Kengele ya Saa” Ililia Mapema Mno?
Bila shaka msukosuko mkubwa ulikumba ulimwengu katika 1914 kwa kufyatuka kwa Vita ya Ulimwengu 1, ambayo kwa miaka mingi iliitwa tu ile Vita Kuu, lakini haikuongoza mara hiyo kwenye kupinduliwa kwa tawala zote za kibinadamu zilizokuwako. Kadiri matukio kuhusiana na Palestina yalivyositawi kufuatia 1914, Wanafunzi wa Biblia walifikiri kwamba waliona uthibitisho wa mabadiliko ya maana kwa ajili ya Israeli. Lakini kadiri miezi na kisha miaka ilivyopita, Wanafunzi wa Biblia hawakupokea thawabu yao ya kimbingu, kama walivyokuwa wametarajia. Waliitikiaje jambo hilo?
The Watch Tower la Februari 1, 1916, lilivuta fikira hususa kwenye Oktoba 1, 1914, kisha likasema: “Hiyo ilikuwa ndiyo hatua ya mwisho ya wakati ambayo kronolojia ya Biblia ilielekeza kwetu kuwa ilihusiana na mambo ambayo yangelipata Kanisa la Katoliki ya Roma. Je, Bwana alituambia kwamba tungechukuliwa huko [mbinguni]? Hapana. Yeye alisema nini? Neno lake na matimizo ya unabii yalionekana yakielekeza bila kukosea kwamba tarehe hiyo ilionyesha mwisho wa Nyakati za Mataifa. Sisi tuliamua kutokana na hilo kwamba ‘badiliko’ la Kanisa lingetukia katika au kabla ya tarehe hiyo. Lakini Mungu hakutuambia kwamba ingekuwa hivyo. Yeye alituruhusu tufikie uamuzi huo; nasi tunaamini kwamba umethibitika kuwa mtihani uliohitajiwa juu ya watakatifu wapendwa wa Mungu kila mahali.” Lakini je, matukio hayo yalithibitisha kwamba tumaini lao tukufu lilikuwa limekuwa la bure? Hapana. Ilimaanisha tu kwamba si kila kitu kilikuwa kikitukia upesi kama walivyokuwa wametarajia.
Miaka kadhaa kabla ya 1914, Russell alikuwa ameandika hivi: “Kwa wazi kronolojia (unabii wa wakati kwa ujumla) haikukusudiwa kuwapa watu wa Mungu habari sahihi ya kronolojia muda wa karne zote. Kwa wazi ilikusudiwa zaidi itumike kama kengele ya saa iwaamshe na kuwatia nishati watu wa Bwana katika wakati ufaao. . . . Lakini tuseme, mathalani, kwamba Oktoba, 1914, ungepita na kusitukie anguko kubwa la serikali za Mataifa. Hilo lingethibitisha au lisingethibitisha nini? Lisingeondoa uthibitisho wa sehemu yoyote ya Mpango wa Kimungu wa Zile Enzi. Bei ya fidia iliyokamilishwa huko Kalvari bado ingekuwa uthibitisho wa utimizo wa mwisho wa Programu ya Kimungu iliyo kubwa kwa ajili ya rudisho la wanadamu. Ule ‘mwito wa juu’ wa Kanisa lipate kuteseka pamoja na Mkombozi na kutukuzwa pamoja naye likiwa washiriki wake au likiwa Bibi-Arusi wake bado ungekuwa vile vile. . . . Jambo pekee lililoathiriwa na kronolojia lingekuwa wakati wa kutimizwa kwa matumaini hayo matukufu kwa ajili ya Kanisa na kwa ajili ya ulimwengu. . . . Na tarehe hiyo ikipita ingethibitisha tu kwamba kronolojia yetu, ‘kengele ya saa’ yetu, ililia mapema kidogo kabla ya wakati. Je, sisi tungefikiri kwamba ni msiba mkuu ikiwa kengele ya saa yetu ingetuamsha nukta chache mapema zaidi asubuhi ya siku fulani kuu yenye kujawa na shangwe na furaha? Hakika sivyo!”
Lakini hiyo “kengele ya saa” haikuwa imelia mapema mno. Kwa kweli, mambo waliyoona ambayo “saa” ilikuwa imewaamsha ndiyo hayakuwa mambo barabara waliyokuwa wametarajia.
Miaka fulani baadaye, wakati nuru ilipokuwa imekuwa nyangavu zaidi, wao walikiri hivi: “Walio wengi kati ya watakatifu hao wapendwa walifikiri kwamba kazi yote ilikuwa imefanywa. . . . Walishangilia kwa sababu ya uthibitisho ulio wazi kwamba ulimwengu ulikuwa umekwisha, kwamba ufalme wa mbingu ulikuwa umekaribia, na kwamba siku ya ukombozi wao ilikaribia. Lakini walikuwa wamekosa kuona jambo jingine ambalo lazima lifanywe. Habari njema ambazo walikuwa wamepokea lazima wangeambia wengine; kwa sababu Yesu alikuwa ameamuru: ‘Habari njema ya ufalme itahubiriwa katika ulimwengu wote, kuwa ushuhuda kwa mataifa yote; hapo ndipo ule mwisho utakapokuja.’ (Mathayo 24:14)”—The Watch Tower, Mei 1, 1925.
Kadiri matukio yaliyofuata 1914 yalivyoanza kufunuka, nao Wanafunzi wa Biblia wakayalinganisha na yale ambayo Bwana-Mkubwa alikuwa ametabiri, walikuja kuthamini hatua kwa hatua kwamba walikuwa wakiishi katika siku za mwisho za mfumo wa kale na kwamba zilianza 1914. Pia walikuja kuelewa kwamba katika mwaka 1914 ndipo kuwapo kusikoonekana kwa Kristo kulipokuwa kumeanza na kwamba, huko hakukuwa katika maana ya kurudi kwake binafsi (hata kwa kutoonekana) kwenye ujirani wa dunia, bali kwa kuelekeza uangalifu wake kwenye dunia akiwa Mfalme anayetawala. Waliona nao wakakubali daraka muhimu lililokuwa lao la kupiga mbiu ya hii “habari njema ya ufalme” kwa ajili ya ushahidi kwa mataifa yote katika huu wakati wa hatari wa historia ya kibinadamu.—Mt. 24:3-14.
Ujumbe ambao wangehubiri juu ya Ufalme ungekuwa nini hasa? Je, ulikuwa tofauti na ujumbe wa Wakristo wa karne ya kwanza?
Ufalme wa Mungu, Tumaini Pekee la Wanadamu
Kama tokeo la funzo la uangalifu la Neno la Mungu, Wanafunzi wa Biblia walioshirikiana na Ndugu Russell walielewa kwamba Ufalme wa Mungu ni serikali ambayo Yehova aliahidi kusimamisha kwa njia ya Mwanae ili kubariki wanadamu. Yesu Kristo, akiwa mbinguni, angekuwa na washirika pamoja naye wakiwa watawala, “kundi dogo” lililoteuliwa na Mungu kutoka miongoni mwa wanadamu. Walielewa kwamba serikali hiyo ingewakilishwa na wanaume waaminifu wa kale ambao wangetumikia wakiwa wakuu katika dunia yote. Hao walirejezewa kuwa “wakuu wa kale.”—Luka 12:32; Dan. 7:27; Ufu. 20:6; Zab. 45:16.
Kwa muda mrefu Jumuiya ya Wakristo ilikuwa imefundisha nadharia ya kwamba ‘wenye kumiliki hupokea haki ya kuwa wafalme kutoka kwa Mungu,’ kuwa njia ya kufanya watu watii. Lakini hao Wanafunzi wa Biblia waliona kutoka Maandiko kwamba wakati ujao wa serikali za kibinadamu haukufanywa salama na uhakikisho wowote wa kimungu. Kupatana na yale waliyokuwa wakijifunza, Watch Tower la Desemba 1881 lilitaarifu: “Bila shaka kusimamishwa kwa ufalme huu, kutahusisha kupinduliwa kwa falme zote za dunia, kwa kuwa zote—hata zile bora kati yazo—zimetegemezwa juu ya utovu wa haki na haki zisizo sawa na uonevu wa wengi na kupendelea wachache—kama tusomavyo: ‘Utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.’”—Dan. 2:44.
Kwa habari ya njia ambayo falme hizo zenye uonevu zingevunjwavunjwa, hao Wanafunzi wa Biblia bado walikuwa na mengi ya kujifunza. Bado wao hawakuelewa waziwazi jinsi manufaa za Ufalme wa Mungu zingeenea kwa wanadamu wote. Lakini wao hawakuchanganyikiwa juu ya Ufalme wa Mungu wakifikiri kwamba ulikuwa hisi isiyoeleweka iliyo ndani ya moyo wa mtu au kuwa ndio ule utawala wa viongozi wa kidini uliotumia Serikali ya kilimwengu kuwa mkono wayo.
Kufikia 1914, watumishi waaminifu wa Mungu wa nyakati za kabla ya Ukristo hawakuwa wamefufuliwa duniani wakiwa wakuu wenye kuwakilisha Mfalme wa Kimesiya, kama ilivyokuwa imetarajiwa, wala wabakio wa “kundi dogo” hawakuwa wamejiunga na Kristo katika Ufalme wa kimbingu katika mwaka huo. Hata hivyo The Watch Tower la Februari 15, 1915, lilitaarifu kwa uhakika kwamba 1914 ulikuwa ndio wakati uliowekwa “wa Bwana wetu kutwaa uweza Wake mkuu na kuanza kutawala,” hivyo kumaliza zile mileani nyingi za utawala usiokatizwa wa Mataifa. Katika toleo lalo la Julai 1, 1920, The Watch Tower lilithibitisha tena msimamo huo na kuushirikisha na zile habari njema ambazo Yesu alikuwa ametabiri kwamba zingehubiriwa duniani pote kabla ya mwisho. (Mt. 24:14) Kwenye mkusanyiko wa Wanafunzi wa Biblia huko Cedar Point, Ohio, katika 1922, uelewevu huo ulitaarifiwa upya katika azimio la ujumla, na Ndugu Rutherford akahimiza wakusanyikaji hivi: “Mtangazeni, mtangazeni, mtangazeni, Mfalme na ufalme wake.”
Hata hivyo, wakati ule Wanafunzi wa Biblia walihisi kwamba kuanzishwa kwa Ufalme, kusimamishwa kwao kikamili mbinguni, hakungetukia mpaka washiriki wa mwisho wa bibi-arusi wa Kristo watukuzwe. Kwa hiyo, hatua kubwa ya kweli ilifikiwa katika 1925, wakati The Watch Tower la Machi 1, lilipotoa makala “Uzaliwa wa Taifa.” Ilitoa funzo lenye kufungua macho juu ya Ufunuo sura ya 12. Makala hiyo ilionyesha uthibitisho wa kwamba Ufalme wa Kimesiya ulikuwa umezaliwa—ukasimamishwa—katika 1914, kwamba wakati huo Kristo alikuwa ameanza kutawala katika kiti chake cha kifalme mbinguni, na kwamba baada ya hapo Shetani alikuwa amevurumishwa chini kwenye ujirani wa dunia kutoka mbinguni. Hizo ndizo zilizokuwa habari njema ambazo zilipasa kupigiwa mbiu, habari za kwamba Ufalme wa Mungu ulikuwa tayari unatenda. Lo, jinsi uelewevu huo uliotiwa nuru ulivyochochea hao wapiga-mbiu wa Ufalme wahubiri hata kwenye miisho ya dunia!
Kwa kila njia ifaayo, watu wa Yehova walitoa ushahidi kwamba Ufalme wa Mungu pekee ndio ungeleta kitulizo cha kudumu na kutatua matatizo yaliyoimarika sana yenye kutaabisha wanadamu. Katika 1931 ujumbe huo ulitolewa kupitia usambazaji wa redio na J. F. Rutherford katika mfumo wa kimataifa wenye kuenea zaidi uliokuwa umepata kutangazwa hewani. Maandishi ya usambazaji huo yalikuwa pia yametangazwa katika lugha nyingi katika kijitabu The Kingdom, the Hope of the World (Ufalme, Tumaini la Ulimwengu)—mamilioni ya nakala zacho yaligawanywa kwa muda wa miezi michache tu. Kuongezea ugawanyaji kwa umma wenye kuenea pote, jitihada za pekee zilifanywa kutia nakala mikononi mwa wanasiasa, wanabiashara mashuhuri, na makasisi.
Miongoni mwa mambo mengine, kijitabu hicho kilisema hivi: “Serikali za ulimwengu za sasa ambazo si zenye uadilifu haziwezi kutoa tumaini lolote kwa watu. Hukumu ya Mungu dhidi yazo yajulisha kwamba lazima ziharibiwe. Kwa hiyo, tumaini la ulimwengu, na tumaini pekee, ni ufalme wenye uadilifu au serikali ya Mungu, Kristo Yesu akiwa Mtawala wayo asiyeonekana.” Walitambua kwamba, Ufalme huo, ungeleta amani na usalama wa kweli kwa wanadamu. Chini ya utawala wao dunia ingekuwa paradiso halisi, na magonjwa na kifo havingekuwapo tena.—Ufu. 21:4, 5.
Habari njema za Ufalme wa Mungu huendelea kuwa imani kuu ya Mashahidi wa Yehova. Tangu toleo la Machi 1, 1939, gazeti lao kuu, ambalo sasa hutangazwa kwa lugha 112, limekuwa na kichwa Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova.
Lakini kabla utawala wa Ufalme haujageuza sura ya dunia iwe paradiso, ingekuwa sharti huu mfumo mwovu wa mambo utoweke. Hilo lingetimizwaje?
Vita ya Ile Siku Kubwa ya Mungu Mweza Yote
Ile vita ya ulimwengu iliyoanza katika 1914 ilitikisa mfumo wa mambo ulioko hadi kwenye misingi yao. Kwa wakati fulani ilionekana kana kwamba matukio yangesonga mbele kama vile Wanafunzi wa Biblia walivyokuwa wametarajia.
Huko nyuma katika Agosti 1880, Ndugu Russell alikuwa ameandika hivi: “Sisi twaelewa kwamba kabla familia ya kibinadamu haijarudishwa au hata kuanza kubarikiwa, serikali za dunia ambazo sasa hufunga na kuonea wanadamu zitapinduliwa zote na kwamba ufalme wa Mungu utatwaa udhibiti na kwamba baraka na rudisho zitakuja kupitia huo ufalme mpya.” ‘Kupinduliwa kwa falme’ kungetukiaje? Akitegemea hali ambazo angeweza kuona wakati ule zikitukia katika ulimwengu, Russell aliamini kwamba wakati wa vita ya Har–Magedoni, Mungu angetumia vikundi vyenye kuzozana vya wanadamu kupindua mipango iliyoko. Alisema hivi: “Kazi ya kubomoa milki ya kibinadamu inaanza. Mamlaka itakayozipindua inatenda kazi sasa. Tayari watu wanapanga majeshi yao chini ya jina la Wakomunisti, Wasosholisti, na Wanamapinduzi, n.k.”
Kitabu The Day of Vengeance (baadaye kiliitwa The Battle of Armageddon), kilichotangazwa katika 1897, kiliongeza habari zaidi juu ya njia ambayo Wanafunzi wa Biblia wakati ule walielewa jambo hilo, kikisema hivi: “Bwana, kwa maongozi yake ya kimungu yenye kushinda, atatwaa uongozi wa ujumla wa jeshi hili kubwa la wasioridhika—wazalendo, warekebishaji, wasosholisti, wateteaji-maadili, wanamachafuko, wajinga na wasio na tumaini—na kutumia matumaini yao, hofu, upumbavu na ubinafsi, kulingana na hekima yake ya kimungu, kutimiza makusudi yake mwenyewe makuu katika kupindua mipango ya sasa, na katika kutayarisha binadamu kwa ajili ya Ufalme wa Uadilifu.” Hivyo wao walielewa kwamba vita ya Har–Magedoni ingeshirikishwa na mapinduzi ya kijamii yenye jeuri.
Lakini je, Har–Magedoni ingekuwa mng’ang’ano tu kati ya vikundi vyenye kuzozana vya wanadamu, mapinduzi ya kijamii yenye kutumiwa na Mungu kupindua mipango iliyoko? Kadiri uangalifu zaidi ulivyokazwa juu ya maandiko yaliyohusu habari hiyo, The Watch Tower la Julai 15, 1925, lilivuta fikira kwenye Zekaria 14:1-3 na kusema: “Kwa hilo tungeelewa kwamba mataifa yote ya dunia, chini ya mwelekezo wa Shetani, yangekusanywa kwenye vita dhidi ya jamii ya Yerusalemu, yaani, wale ambao huchukua msimamo wao upande wa Bwana . . . Ufunuo 16:14, 16.”
Mwaka uliofuata, katika kitabu Deliverance, uangalifu ulikazwa juu ya kusudi la kweli la vita hiyo, kusema: “Sasa Yehova, kulingana na Neno lake, atafanya wonyesho wa nguvu zake kwa wazi sana na kwa njia isiyo na shaka hivi kwamba watu wataweza kusadikishwa juu ya mwendo wao usio wa kimungu na waweze kuelewa kwamba Yehova ndiye Mungu. Hiyo ndiyo sababu iliyofanya Mungu alete lile furiko kuu, aangushe chini Mnara wa Babeli, aharibu jeshi la Senakeribu yule mfalme wa Ashuru, na kumeza Wamisri; na ndiyo pia sababu sasa ataleta taabu nyingine kuu juu ya ulimwengu. Maafa hayo ya hapo kwanza yalikuwa vivuli tu vya lile linalokuja sasa. Kukusanywa huko ni [kuletwa] kwenye siku ile kuu ya Mungu Mweza Yote. Ndiyo ile ‘siku kuu na itishayo ya Bwana’ (Yoe. 2:31), wakati ambapo Mungu atajifanyia mwenyewe jina. Katika pambano hilo kuu na la mwisho vikundi vya watu wa kila taifa, kabila na lugha vitajifunza kwamba Yehova ndiye mwenye nguvu zote, mwenye hekima yote na Mungu mwenye haki.” Lakini watumishi wa Yehova duniani walitahadharishwa hivi: “Katika vita hiyo kuu hakuna Mkristo atakayerusha ngumi. Sababu inayofanya wasifanye hivyo ni kwamba Yehova amesema: ‘Vita si yenu, bali ya Mungu.’” Vita inayozungumzwa hapa kwa wazi si ile ambayo ilipiganwa miongoni mwa mataifa, kuanzia 1914. Ilikuwa ingali inakuja.
Bado kulikuwa na maswali mengine yaliyohitaji kutatuliwa kwa msingi wa Maandiko. Moja la hayo lilihusu utambulisho wa Yerusalemu ambao ungekanyagwa chini ya miguu mpaka mwisho wa Nyakati za Mataifa, kama ilivyotaarifiwa kwenye Luka 21:24; na uliohusiana na huo ulikuwa utambulisho wa Israeli warejezewao katika unabii mwingi sana juu ya kurudishwa.
Je, Mungu Angerudisha Wayahudi Palestina?
Wanafunzi wa Biblia walifahamu vema ule unabii mwingi wa kurudishwa uliotolewa kwa Israeli wa kale na manabii wa Mungu. (Yer. 30:18; 31:8-10; Amo. 9:14, 15; Rum. 11:25, 26) Kufikia 1932, walielewa huo kuwa ulitumika hususa kwa Wayahudi wa asili. Hivyo, waliamini kwamba Mungu angeonyesha Israeli upendeleo tena, akirudisha Wayahudi hatua kwa hatua katika Palestina, na kufungua macho yao yaone kweli kuhusu Yesu akiwa Mfidi na Mfalme wa Kimesiya, na kuwatumia wakiwa wakili ili kutolea mataifa yote baraka. Wakiwa na uelewevu huo, Ndugu Russell alisema na wasikilizaji wengi Wayahudi katika New York na pia katika Ulaya juu ya kichwa “Uzayoni Katika Unabii,” na Ndugu Rutherford, katika 1925, aliandika kitabu Comfort for the Jews.
Lakini hatua kwa hatua ilipata kuwa wazi kwamba jambo lililokuwa likitukia katika Palestina kuhusiana na Wayahudi halikuwa utimizo wa unabii mtukufu mbalimbali wa Yehova unaohusu kurudishwa. Kuachwa ukiwa kulikuja juu ya Yerusalemu ya karne ya kwanza kwa sababu Wayahudi walikuwa wamemkataa Mwana wa Mungu, Mesiya, yule aliyetumwa katika jina la Yehova. (Dan. 9:25-27; Mt. 23:38, 39) Ilikuwa ikizidi kuwa wazi kwamba wakiwa kikundi cha watu hawakuwa wamebadili nia yao. Hakukuwa na toba juu ya tendo lenye kosa lililotendwa na babu zao. Kurudi kwa baadhi yao Palestina hakukusukumwa na upendo wowote kwa ajili ya Mungu au tamaa ya kuona jina lake likitukuzwa kwa utimizo wa Neno lake. Jambo hilo lilielezwa wazi katika buku la pili Vindication, ambalo lilitangazwa na Watch Tower Bible and Tract Society katika 1932.k Usahihi wa msimamo huo ulithibitishwa katika 1949, wakati Taifa la Israeli, ambalo wakati huo lilikuwa ndipo tu limefanyizwa kuwa taifa na kuwa nchi ya makao kwa ajili ya Wayahudi, lilipopata kuwa mshiriki wa Umoja wa Mataifa, hivyo kuonyesha kwamba lilitumainia si Yehova bali mataifa ya kisiasa ya ulimwengu.
Jambo lililokuwa likitukia katika kutimiza unabii huo mbalimbali wa kurudishwa lilielekeza katika upande mwingine. Watumishi wa Yehova walianza kutambua kwamba Israeli wa kiroho, “Israeli wa Mungu,” waliotia ndani Wakristo watiwa-mafuta kwa roho, ndio ambao, katika utimizo wa kusudi la Mungu, walikuwa wakifurahia amani pamoja na Mungu kupitia Yesu Kristo. (Gal. 6:16) Sasa macho yao yakafunguliwa yatambue katika shughuli za Mungu pamoja na Wakristo hao wa kweli utimizo wa ajabu wa ahadi hizo za kurudishwa. Baada ya wakati, walikuja pia kutambua kwamba Yerusalemu uliokuwa umetukuzwa mwishoni mwa Nyakati za Mataifa haukuwa jiji la kidunia tu, au hata kikundi cha watu duniani kikiwakilishwa na jiji hilo, bali, ni “Yerusalemu la kimbingu,” ambako Yehova alimtawaza Mwana wake, Yesu Kristo, akiwa na mamlaka ya kutawala katika 1914.—Ebr. 12:22, NW.
Mambo hayo yakiwa wazi, Mashahidi wa Yehova walikuwa katika hali nzuri zaidi kutimiza bila kupendelea kikundi chochote mgawo wa kuhubiri habari njema za Ufalme “katika dunia yote inayokaliwa kwa ajili ya kuwa ushahidi kwa mataifa yote.”—Mt. 24:14, NW.
Ni nani wa kupewa sifa kwa mafafanuzi hayo yote ya Biblia ambayo yametokea katika vichapo vya Watch Tower?
Njia Ambayo Watumishi wa Yehova Hufundishwa
Yesu Kristo alitabiri kwamba baada ya kurudi kwake mbinguni, yeye angepelekea wanafunzi wake roho takatifu. Hiyo ingetumikia ikiwa msaidizi, ikiwaongoza “ndani ya kweli yote.” (Yn. 14:26; 16:7, 13, NW) Pia Yesu alisema kwamba akiwa Bwana au Bwana-Mkubwa wa Wakristo wa kweli, yeye angekuwa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” au “msimamizi-nyumba mwaminifu,” ambaye angetoa ‘chakula cha kiroho kwa wakati ufaao’ kwa watu wa nyumbani, wale wafanyakazi katika watu wa nyumba ya imani. (Mt. 24:45-47; Luka 12:42, NW) Huyo mtumwa mwaminifu na mwenye busara ni nani?
Toleo lilelile la kwanza la Watch Tower liligusia Mathayo 24:45-47 lilipotaarifu kwamba lengo la watangazaji wa gazeti hilo lilikuwa kuwaweka chonjo kuona matukio yenye kuhusiana na kuwapo kwa Kristo na kuwapa “nyama [ya kiroho] kwa majira yake” watu wa nyumba ya imani. Lakini mhariri wa gazeti hilo hakuwa mwenyewe akidai kuwa ndiye huyo mtumwa mwaminifu mwenye busara, au “mtumishi mwaminifu na mwenye hekima” (kulingana na tafsiri ya King James Version).
Hivyo, katika toleo la Oktoba-Novemba 1881 la gazeti hilo, C. T. Russell alitaarifu hivi: “Sisi twaamini kwamba kila mshiriki wa mwili huo wa Kristo anashiriki katika kazi hii iliyobarikiwa, ama moja kwa moja ama kwa njia isiyo ya moja kwa moja, ya kuwapa nyama kwa majira yake watu wa nyumba ya imani. ‘Ni nani basi huyo mtumwa mwaminifu mwenye hekima ambaye Bwana wake amemfanya mtawala juu ya watu wa nyumba yake,’ awape nyama kwa majira yake? Je, si hilo ‘kundi dogo’ la watumishi waliojitakasa ambao wanatimiza kwa uaminifu nadhiri zao za kujitakasa—ule mwili wa Kristo—na je, mwili wote ukiwa watu mmoja-mmoja na wote kwa ujumla, hauwapi nyama kwa majira yake watu wa nyumba ya imani—ule ushirika mkubwa wa waamini? Mbarikiwa ni mtumishi huyo (ule mwili mzima wa Kristo) ambaye Bwana wake ajapo (Kigiriki elthon) atamkuta akifanya hivyo. ‘Kweli, nawaambia, kwamba atamfanya kuwa mtawala juu ya mali yake yote.’”
Hata hivyo, zaidi ya mwongo mmoja baadaye, mke wa Ndugu Russell alitoa hadharani wazo la kwamba Russell mwenyewe alikuwa ndiye yule mtumishi mwaminifu na mwenye hekima.l Maoni hayo aliyotoa kuhusu utambulisho wa ‘mtumwa mwaminifu’ yalikuja kushikiliwa kwa ujumla na Wanafunzi wa Biblia kwa miaka 30 hivi. Ndugu Russell hakukataa maoni yao, bali yeye binafsi aliepuka kufanya utumizi kama huo wa andiko hilo, akikazia kupinga kwake wazo la kwamba jamii ya makasisi ilipewa utume wa kufundisha Neno la Mungu ikiwa tofauti na jamii ya watu wa kawaida ambayo haikupewa utume huo. Uelewevu uliotolewa na Ndugu Russell katika 1881 kwamba mtumishi mwaminifu mwenye hekima alikuwa kwa kweli mtumishi wa ujumla, akitia ndani washiriki wote wa mwili wa Kristo waliotiwa mafuta kwa roho walioko duniani, ulithibitishwa tena katika The Watch Tower la Februari 15, 1927.—Linganisha Isaya 43:10.
Ndugu Russell alilionaje fungu lake mwenyewe? Je, yeye alidai kuwa na mafunuo ya pekee kutoka kwa Mungu? Katika Watch Tower la Julai 15, 1906 (ukurasa 229), Russell alijibu hivi kwa unyenyekevu: “La, rafiki wapendwa, mimi sidai ukuu wowote, wala nguvu zipitazo za kibinadamu, adhama wala mamlaka; wala mimi sitaki kujitukuza mwenyewe kwa kukadiriwa na ndugu zangu wa nyumba ya imani, isipokuwa katika ile maana ambayo Bwana-Mkubwa aliihimiza, akisema, ‘Ye yote anayetaka kuwa mkubwa kwenu, na awe mtumishi wenu.’ (Mt. 20:27.) . . . Kweli nitoazo, nikiwa msemaji wa Mungu, hazikufunuliwa katika njozi wala ndoto, wala kwa sauti yenye kusikika ya Mungu, wala zote mara moja, bali hatua kwa hatua . . . Wala kufunguka huku kuliko wazi kwa kweli si kwa sababu ya akili ya kibinadamu wala utambuzi wa akili, bali uhakika tu wa kwamba wakati wa Mungu uliowekwa umefika; na kama mimi nisingesema, na hakukupatikana wakili mwingine, mawe yenyewe yangepiga kelele.”
Ni kwa Yehova akiwa Mfunzi Mtukufu wao kwamba wasomaji wa Watch Tower walitiwa moyo watazame, kama vile Mashahidi wa Yehova wote leo wanavyotiwa moyo. (Isa. 30:20) Jambo hilo lilikaziwa kwa nguvu katika Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) la Novemba 1, 1931, katika makala “Waliofundishwa na Mungu,” ambayo ilitaarifu hivi: “Mnara wa Mlinzi hutambua kweli kuwa ni ya Yehova, na si ya kiumbe yeyote. Mnara wa Mlinzi si chombo cha binadamu yeyote au kikundi cha wanadamu, wala hautangazwi kulingana na mapenzi ya wanadamu. . . . Yehova Mungu ndiye Mfunzi mkuu wa watoto wake. Hakika, kutangazwa kwa kweli hizi kunatolewa na wanadamu wasiokamilika, na kwa sababu hizo si kamilifu kabisa kwa namna yazo; lakini zatolewa katika namna ambayo huonyesha kweli ya Mungu ambayo yeye hufundisha watoto wake.”
Katika karne ya kwanza, wakati maswali yaliyohusu mafundisho au utaratibu yalipozuka, hayo yalipelekwa kwenye baraza kuu lenye kuongoza lililotia ndani wanaume wazee kiroho. Maamuzi yalifanywa baada ya kufikiria yale ambayo Maandiko yaliyopuliziwa yalisema pamoja na uthibitisho wa utendaji uliopatana na Maandiko hayo na uliokuwa ukisitawi kama tokeo la utendaji wa roho takatifu. Maamuzi hayo yalipelekwa kwenye makutaniko kwa barua. (Mdo. 15:1–16:5) Utaratibu uo huo unatenda kazi leo miongoni mwa Mashahidi wa Yehova.
Maagizo ya kiroho huandaliwa kwa njia ya makala za magazeti, vitabu, programu za mkusanyiko, na mihtasari kwa ajili ya hotuba za kutaniko—yote hayo hutayarishwa chini ya mwelekezo wa Baraza Linaloongoza la mtumwa mwaminifu na mwenye busara. Yaliyomo huonyesha wazi kwamba yale aliyotabiri Yesu yanatukia leo—kwamba yeye kwelikweli ana jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara inayofundisha kwa uaminifu-mshikamanifu ‘mambo yote aliyoamuru’; kwamba wakili huyo ‘analinda,’ yuko chonjo kuona matukio katika utimizo wa unabii wa Biblia na hasa kuhusiana na kuwapo kwa Kristo; kwamba anasaidia watu wenye kumhofu Mungu waelewe yanayohusika katika ‘kushika’ mambo aliyoamuru Yesu na hivyo kujithibitisha kwamba kwelikweli wao ni wanafunzi wake.—Mt. 24:42; 28:20; Yn. 8:31, 32, NW.
Kwa njia yenye kuendelea, kwa muda wa miaka iliyopita, mazoea ambayo huenda yakawa na matokeo ya kuvuta fikira isivyofaa kwa wanadamu fulani kuhusiana na utayarishaji wa chakula cha kiroho yameondolewa. Kufikia kifo cha C. T. Russell, jina lake akiwa mhariri liliorodheshwa katika karibu kila toleo la Watch Tower. Majina na herufi za kwanza za majina ya wale waliochanga habari yalionekana mara nyingi mwishoni mwa makala walizotayarisha. Kisha, kuanzia na toleo la Desemba 1, 1916, badala ya kuonyesha jina la mtu mmoja akiwa mhariri, The Watch Tower liliorodhesha majina ya halmashauri ya uhariri. Katika toleo la Oktoba 15, 1931, hata orodha hiyo iliondolewa na Isaya 54:13 likachukua mahali payo. Kama lilivyonukuliwa kutoka American Standard Version, lasomeka hivi: “Na watoto wako wote watafundishwa na Yehova; na amani ya watoto wako itakuwa kubwa.” Tangu 1942 imekuwa kanuni ya ujumla kwamba fasihi iliyotangazwa na Watch Tower Society isivute fikira kwa mtu yeyote mmoja kuwa ndiye mwandikaji.a Chini ya usimamizi wa Baraza Linaloongoza, Wakristo walio wakfu katika Amerika ya Kaskazini na Kusini, Ulaya, Afrika, Asia, na visiwa vya bahari wameshiriki sehemu katika kutayarisha habari kama hiyo kwa matumizi ya makutaniko ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote. Lakini sifa yote hupewa Yehova Mungu.
Nuru Yaangaza Zaidi na Zaidi
Kama ionyeshwavyo katika historia yao ya kisasa, yaliyoonwa na Mashahidi wa Yehova yamekuwa kama ilivyoelezwa kwenye Mithali 4:18 (NW): “Kijia cha waadilifu ni kama nuru nyangavu ambayo inaendelea kunurika zaidi na kunurika zaidi mpaka ile siku ipate kuthibitishwa imara.” Kuangaza kwa nuru kumekuwa kwenye maendeleo, kama vile nuru ya mapambazuko hufuatwa na kucha kwa jua na nuru kamili ya mchana mpya. Wakiona mambo kwa ile nuru iliyokuwa ikipatikana, nyakati nyingine wamekuwa na mawazo yasiyo kamili, hata yenye kosa. Hata wajitahidi kadiri gani, hawangeweza hata kidogo kuelewa unabii fulani mbalimbali mpaka huo uanze kutimizwa. Kadiri Yehova alivyoangaza nuru zaidi juu ya Neno lake kwa njia ya roho yake, watumishi wake wamekuwa na nia ya kufanya kwa unyenyekevu marekebisho yaliyohitajiwa.
Uelewevu huo wenye maendeleo haukuwako tu katika kile kipindi cha mapema cha historia yao ya kisasa. Waendelea hata sasa. Kwa kielelezo, katika 1962 kulikuwa na rekebisho la uelewevu kuhusu “mamlaka zilizo kubwa” ya Warumi 13:1-7, NW.
Kwa miaka mingi, Wanafunzi wa Biblia walikuwa wamefundisha kwamba “mamlaka za juu zaidi” (KJ) zilikuwa Yehova Mungu na Yesu Kristo. Kwa nini? Katika The Watch Tower la Juni 1, na Juni 15, 1929, sheria mbalimbali za kilimwengu zilitajwa, na ikaonyeshwa kwamba mambo yaliyoruhusiwa katika nchi moja yalikatazwa katika nyingine. Uangalifu ulivutwa pia kwenye sheria za kilimwengu zilizowataka watu wafanye mambo ambayo Mungu alikataza au zilizokataza mambo ambayo Mungu aliamuru watumishi wake wafanye. Kwa sababu ya tamaa yao ya moyo ya kuonyesha staha kwa mamlaka kuu zaidi ya zote ya Mungu, ilionekana kwa Wanafunzi wa Biblia kwamba “mamlaka za juu zaidi” lazima ziwe Yehova Mungu na Yesu Kristo. Bado walitii sheria za kilimwengu, lakini mkazo ulikuwa juu ya utii kwa Mungu kwanza. Hilo lilikuwa somo la maana, ambalo liliwaimarisha wakati wa miaka ya msukosuko wa ulimwengu uliofuata. Lakini hawakuelewa waziwazi yaliyokuwa yakisemwa na Warumi 13:1-7.
Miaka mingi baadaye, uchanganuzi mpya wa uangalifu wa andiko hilo ulifanywa, pamoja na habari inayolizunguka na maana yalo kwa kufikiria sehemu nyingine yote ya Biblia. Kama tokeo, katika 1962 ilikiriwa kwamba “mamlaka zilizo kubwa” ni watawala wa kilimwengu, lakini kwa msaada wa New World Translation, kanuni ya utii husianifu ilitambuliwa waziwazi.b Hilo halikuhitaji badiliko kubwa lolote katika maoni ya Mashahidi wa Yehova kuelekea serikali za ulimwengu, lakini lilisahihisha uelewevu wao wa sehemu ya maana ya Maandiko. Kadiri wakati ulivyoendelea, kukawa na fursa kwa Mashahidi wakiwa mtu mmoja-mmoja kufikiria kwa uangalifu kama walikuwa wakitimiza kikweli madaraka yao kuelekea Mungu na mamlaka za kilimwengu pia. Uelewevu huo ulio wazi wa “mamlaka zilizo kubwa” umetumika kuwa himaya kwa Mashahidi wa Yehova, hasa katika zile nchi ambako ongezeko la utukuzo wa taifa na makelele ya kutaka uhuru mkubwa zaidi vimetokeza jeuri na kufanyizwa kwa serikali mpya mbalimbali.
Mwaka uliofuata, 1963, utumizi ulio mkubwa zaidi wa “Babiloni Mkubwa” ulitolewa.c (Ufu. 17:5, NW) Pitio la historia ya kilimwengu na kidini lilielekeza kwenye mkataa wa kwamba uvutano wa Babiloni wa kale ulikuwa umeenea si katika Jumuiya ya Wakristo tu bali pia kila sehemu ya dunia. Hivyo, Babiloni Mkubwa alionwa kuwa ile milki ya ulimwengu mzima ya dini bandia. Kujua hivyo kumewawezesha Mashahidi wa Yehova kuwasaidia watu wengi zaidi wa kutoka malezi mbalimbali waitikie ile amri ya Kibiblia: “Tokeni kwake, watu wangu.”—Ufu. 18:4, NW.
Kwelikweli, kufunguka kwa matukio yaliyotabiriwa katika kitabu chote cha Ufunuo kumeandaa nuru nyingi ya kiroho. Katika 1917 funzo la Ufunuo lilitangazwa katika kitabu The Finished Mystery. Lakini “siku ya Bwana,” iliyorejezewa kwenye Ufunuo 1:10, ilikuwa ndipo tu inaanza wakati ule; mengi ya yale yaliyotabiriwa yalikuwa bado kutukia na hayakueleweka waziwazi. Hata hivyo, matukio ya wakati wa miaka iliyofuata yalitupa nuru kubwa zaidi juu ya maana ya sehemu hiyo ya Biblia, na matukio hayo yalikuwa na matokeo makubwa zaidi juu ya funzo lenye kutoa nuru la Ufunuo lililotangazwa katika 1930 katika yale mabuku mawili yaliyoitwa Light. Wakati wa miaka ya 1960 habari nyingine iliyopatanishwa na matukio ya karibuni zaidi ilitokea katika kitabu “Babylon the Great Has Fallen!” God’s Kingdom Rules! na “Then Is Finished the Mystery of God.” Miongo miwili baadaye funzo jingine lenye kina la sehemu hiyo ya Biblia lilifanywa lipatikane. Lugha ya kitamathali ya Ufunuo ilichanganuliwa kwa uangalifu kwa kufikiria semi zinazofanana katika sehemu nyingine za Biblia. (1 Kor. 2:10-13) Matukio ya karne ya ishirini katika utimizo wa unabii mbalimbali yalipitiwa. Matokeo yalitangazwa katika 1988 katika kile kitabu chenye kusisimua Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!
Wakati wa ile miaka ya mapema ya historia ya kisasa, misingi ilikuwa ikiwekwa. Chakula kingi cha kiroho chenye thamani kiliandaliwa. Katika miaka ya karibuni unamna-namna mwingi zaidi wa habari ya funzo la Biblia umeandaliwa ili kutosheleza mahitaji ya Wakristo wakomavu na wanafunzi wapya wa kutoka malezi mengi. Funzo lenye kuendelea la Maandiko, pamoja na utimizo wa unabii wa kimungu, umefanya katika visa vingi iwezekane kueleza mafundisho ya Biblia kwa uwazi zaidi. Kwa sababu funzo lao la Neno la Mungu ni lenye kuendelea, Mashahidi wa Yehova wana chakula cha kiroho kwa wingi, kama vile Maandiko yalivyotabiri ingekuwa kwa watumishi wa kweli wa Mungu. (Isa. 65:13, 14) Marekebisho katika maoni hayafanywi kamwe kwa kusudi la kuwa wenye kukubalika zaidi kwa ulimwengu kwa kukubali kanuni zao za kiadili zenye kushuka. Tofauti na hivyo, historia ya Mashahidi wa Yehova huonyesha kwamba mabadiliko hufanywa kwa kusudi la kushikamana kwa ukaribu hata zaidi na Biblia, kuwa zaidi kama Wakristo waaminifu wa karne ya kwanza, na hivyo kuwa wenye kukubalika zaidi kwa Mungu.
Hivyo, waliyoona yapatana na sala ya mtume Paulo, aliyeandikia Wakristo wenzake hivi: “Sisi . . . hatujaacha kusali kwa ajili yenu na kuomba ili nyinyi mpate kujazwa ujuzi sahihi wa mapenzi yake katika hekima yote na ufahamivu wa kiroho, kusudi mtembee kwa kumstahili Yehova kwa madhumuni ya kumpendeza yeye kikamili mnapoendelea kuzaa matunda katika kila kazi njema na kuongezeka katika ujuzi sahihi wa Mungu.”—Kol. 1:9, 10, NW.
Ongezeko hilo la ujuzi sahihi juu ya Mungu lilikuwa pia na uhusiano na jina lao—Mashahidi wa Yehova
[Maelezo ya Chini]
a Zion’s Watch Tower and Herald of Christ’s Presence, Julai 15, 1906, kur. 229-231.
b Ona Insight on the Scriptures, kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc., Buku 2, ukurasa 1176.
c Kwa kielelezo: (1) Kufikia karne ya 16, harakati za kupinga fundisho la Utatu zilikuwa zenye nguvu katika Ulaya. Kwa kielelezo, Ferenc Dávid (1510-1579), Mhungaria, alijua na alifundisha kwamba fundisho la Utatu halikuwa la Kimaandiko. Kwa sababu ya imani zake, yeye alifia gerezani. (2) Minor Reformed Church, ambalo lilisitawi katika Poland kwa miaka mia moja hivi wakati wa karne ya 16 na ya 17, pia lilikataa Utatu, na wafuasi wa kanisa hilo walieneza fasihi yalo kotekote katika Ulaya, mpaka Wayesuiti walipofanikiwa kuwafanya wafukuzwe kutoka Poland. (3) Sir Isaac Newton (1642-1727), katika Uingereza, alikataa fundisho la Utatu na akaandika sababu zenye habari nyingi za kihistoria na za Kimaandiko za kufanya hivyo, lakini yeye hakuzitangaza wakati wa maisha yake, kwa wazi, kwa sababu ya kuogopa matokeo. (4) Miongoni mwa wengine katika Marekani, Henry Grew alifichua Utatu kuwa si wa kimaandiko. Katika 1824 aliandika habari nyingi juu ya jambo hilo katika An Examination of the Divine Testimony Concerning the Character of the Son of God.
d Ona pia Studies in the Scriptures, Mfululizo 5, kurasa 41-82.
e Mazungumzo kamili ya uthibitisho wa kihistoria na wa Kimaandiko juu ya habari hiyo yametangazwa na Watchtower Bible and Tract Society katika nyakati mbalimbali. Ona “The Word”—Who Is He? According to John (1962), “Mambo Mawili Yasiyobadilika Asiyoweza Mungu Kusema Uwongo” (1968), Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko (1989), na Je, Uamini Utatu? (1990).
f Yale ambayo Maandiko husema kuhusu nafsi yajulikana na wasomi Wayahudi pamoja na wale wa Jumuiya ya Wakristo, lakini yanafundishwa mara chache sana katika mahali pao pa ibada. Ona New Catholic Encyclopedia (1967), Buku 13, kurasa 449-450; The Eerdmans Bible Dictionary (1987), kurasa 964-965; The Interpreter’s Dictionary of the Bible, iliyohaririwa na G. Buttrick (1962), Buku 1, ukurasa 802; The Jewish Encyclopedia (1910), Buku 6, ukurasa 564.
g Katika mazungumzo yenye habari nyingi zaidi juu ya jambo hili, katika 1955, kijitabu What Do the Scriptures Say About “Survival After Death”? kilionyesha kwamba maandishi ya Biblia huonyesha kwamba kwa kweli Shetani alimtia Hawa moyo aamini kwamba yeye hangekufa katika mwili kama matokeo ya kupuuza katazo la Mungu juu ya kula tunda kutoka kwa “mti wa ujuzi wa mema na mabaya.” (Mwa. 2:16, 17; 3:4) Baada ya wakati, kwa wazi hilo lilithibitika kuwa si kweli, lakini kulikuwa na matukio zaidi yaliyokuwa na shina katika uwongo huo wa kwanza. Watu walikubali maoni ya kwamba sehemu isiyoonekana ya mtu huendelea kuishi. Kufuatia Furiko la siku ya Nuhu, hilo liliimarishwa na mazoea ya kimashetani ya roho waovu yaliyokuwa yakitoka Babiloni.—Isa. 47:1, 12; Kum. 18:10, 11.
h Barbour alidai kuamini katika fidia, kwamba Kristo alikufa kwa ajili yetu. Alilokataa ni wazo la “kutoa kilicho badala”—kwamba Kristo alikufa badala ya sisi, kwamba kwa kifo chake Kristo alilipa adhabu ya dhambi kwa ajili ya uzao wa Adamu.
i Hilo liliongozwa na imani ya kwamba mileani ya saba ya historia ya kibinadamu ilikuwa imeanza katika 1873 na kwamba kipindi cha kutokuwa na upendeleo wa kimungu (cha urefu sawa na kipindi kilichotangulia kilichofikiriwa kuwa cha upendeleo) juu ya Israeli wa asili kingekoma katika 1878. Kronolojia hiyo ilikuwa na kosa kwa sababu ya kutegemea tafsiri isiyo sahihi ya Matendo 13:20 katika King James Version, imani ya kwamba kulikuwa kosa la kunakili kwenye 1 Wafalme 6:1, na kushindwa kufikiria kronolojia ya Kibiblia katika kuweka tarehe za milki za wafalme wa Yuda na wa Israeli. Uelewevu ulio wazi zaidi wa kronolojia ya Biblia ulitangazwa katika 1943, katika kitabu “The Truth Shall Make You Free,” halafu ukafanywa kuwa bora mwaka uliofuata katika kitabu “The Kingdom Is at Hand,” na pia katika vichapo vya baadaye.
j Gazeti lililotangazwa na George Storrs, Brooklyn, New York.
k Katika 1978, wakati lilipoombwa litoe taarifa kwa ajili ya vyombo vya habari kuhusu msimamo wa Mashahidi wa Yehova kuhusu Uzayoni, Baraza Linaloongoza lilisema hivi: “Mashahidi wa Yehova huendelea kuchukua ule msimamo wa Kibiblia wa kutokuwamo kwa habari ya harakati na serikali zote za kisiasa. Wao wamesadikishwa kwamba hakuna harakati yoyote ya kibinadamu ambayo itatimiza kile ambacho ni ufalme wa kimbingu wa Mungu pekee uwezao kutimiza.”
l Kwa kusikitisha, si muda mrefu baada ya hilo mwanamke huyo akajitenga na Ndugu Russell kwa sababu ya tamaa yake mwenyewe ya umashuhuri wa kibinafsi.
a Hata hivyo, katika nchi ambako sheria hutaka hivyo, mwakilishi mwenyeji aweza kutajwa kuwa ndiye mwenye daraka kwa yanayotangazwa.
b Mnara wa Mlinzi, (Kiingereza) Novemba 1, Novemba 15, na Desemba 1, 1962.
c Mnara wa Mlinzi, (Kiingereza) Novemba 15, na Desemba 1, 1963.
[Blabu katika ukurasa wa 120]
C. T. Russell alikiri waziwazi ule msaada uliotoka kwa wengine wakati wa miaka yake ya mapema ya funzo la Biblia
[Blabu katika ukurasa wa 122]
Wamechunguza binafsi uthibitisho wa kwamba Biblia ni Neno la Mungu kwelikweli
[Blabu katika ukurasa wa 123]
Wanafunzi wa Biblia walitambua kwamba haki ya Mungu ina usawaziko mkamilifu na hekima yake, upendo, na nguvu
[Blabu katika ukurasa wa 127]
Russell aliona waziwazi kwamba helo si mahali pa mateso baada ya kifo
[Blabu katika ukurasa wa 129]
Watu wengi zaidi wenye akili hawakuamini fundisho la moto wa helo
[Blabu katika ukurasa wa 132]
Msimamo imara wa Russell juu ya fidia ulikuwa na matokeo makubwa sana
[Blabu katika ukurasa wa 134]
Wangeweza kuona kwamba 1914 ulionyeshwa waziwazi na unabii wa Biblia
[Blabu katika ukurasa wa 136]
Si kila kitu kilichotukia upesi kama walivyotarajia
[Blabu katika ukurasa wa 139]
Habari njema za kupigiwa mbiu: Ufalme wa Mungu tayari unatenda!
[Blabu katika ukurasa wa 140]
Je, Har–Magedoni ingekuwa mapinduzi ya kijamii tu?
[Blabu katika ukurasa wa 141]
Hatimaye, katika 1932, “Israeli wa Mungu” walio wa kweli wakatambulishwa
[Blabu katika ukurasa wa 143]
“Mtumwa mwaminifu na mwenye busara”—ni mtu mmoja au ni jamii?
[Blabu katika ukurasa wa 146]
Kwa njia yenye kuendelea, mazoea ambayo huenda yakavuta fikira isivyofaa kwa wanadamu fulani yameondolewa
[Blabu katika ukurasa wa 148]
Mabadiliko yanayofanywa ni kwa kusudi la kushikamana kwa ukaribu hata zaidi na Neno la Mungu
[Sanduku katika ukurasa wa 124]
Kujulisha Jina la Mungu
◆ Tangu 1931 jina Mashahidi wa Yehova limetumiwa kuonyesha wale ambao huabudu na kumtumikia Yehova akiwa Mungu pekee wa kweli.
◆ Tangu Oktoba 15, 1931, jina la Mungu la kibinafsi, Yehova, limeonekana juu ya jalada la mbele la kila toleo la gazeti “Mnara wa Mlinzi.”
◆ Katika wakati ambao jina la Mungu la kibinafsi lilikuwa likiacha kutiwa katika tafsiri nyingi za kisasa za Biblia, Mashahidi wa Yehova walianza kutangaza, katika 1950, “New World Translation,” ambayo ilirudisha jina la Mungu kwenye mahali palipo haki yalo.
◆ Kuongezea Biblia yenyewe, fasihi nyingine nyingi zimetangazwa na Watch Tower Bible and Tract Society ili kukaza uangalifu wa pekee kwenye jina la Mungu—kwa kielelezo, vitabu “Jehovah” (1934), “Let Your Name Be Sanctified” (1961), na “‘The Nations Shall Know That I Am Jehovah’—How?” (1971), pamoja na broshua “Jina la Mungu Litakaloendelea Milele” (1984).
[Sanduku katika ukurasa wa 126]
‘Je, Sisi Tutampinganisha Kristo Mwenyewe?’
Baada ya kufichua kutopatana na maandiko na kutopatana na kufikiri kiakili kwa fundisho la Utatu, C. T. Russell alionyesha ghadhabu yenye uadilifu alipouliza hivi: “Je, hivyo sisi tutapinganisha Mitume na Manabii na Yesu Mwenyewe, na kupuuza kufikiri kiakili na busara, ili tushike fundisho lililopokezwa kwetu na Kanisa fisadi lililoasi imani kutoka ule wakati wa giza, wa ushirikina uliopita? Hasha! ‘Kwa Sheria na ushuhuda! Wasiposema kulingana na Neno hili, ni kwa sababu hamna nuru ndani yao.’”—“The Watch Tower,” Agosti 15, 1915.
[Sanduku katika ukurasa wa 133]
Kweli Yenye Kuendelea
Katika 1882, C. T. Russell aliandika hivi: “Biblia ndiyo kiwango chetu pekee, na mafundisho yayo ni itikadi yetu pekee ya kidini, na kwa kutambua hali yenye kuendelea ya kufunguka kwa kweli za Kimaandiko, sisi tuko tayari na tumejitayarisha kuongeza au kurekebisha itikadi yetu ya kidini (imani) kadiri tupatavyo ongezeko la nuru kutoka katika Kiwango chetu.” —“Watch Tower,” Aprili 1882, uku. 7.
[Sanduku katika ukurasa wa 144, 145]
Imani za Mashahidi wa Yehova
◆ Biblia ni Neno la Mungu lililopuliziwa. (2 Tim. 3:16, 17)
Yaliyomo si historia tu au maoni ya kibinadamu bali neno la Mungu, lililoandikwa kutunufaisha. (2 Pet. 1:21; Rum. 15:4; 1 Kor. 10:11)
◆ Yehova ndiye Mungu pekee wa kweli. (Zab. 83:18; Kum. 4:39)
Yehova ndiye Muumba wa vitu vyote, na akiwa hivyo, yeye pekee astahili kuabudiwa. (Ufu. 4:11; Luka 4:8)
Yehova ndiye Mwenye Enzi Kuu wa Ulimwengu Wote Mzima, yeye ambaye sisi twawajibika kumtii kikamili. (Mdo. 4:24; Dan. 4:17; Mdo. 5:29)
◆ Yesu Kristo ni Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu, yule pekee aliyeumbwa moja kwa moja na Mungu mwenyewe. (1 Yoh. 4:9; Kol. 1:13-16)
Yesu alikuwa wa kwanza wa viumbe vya Mungu; hivyo, kabla ya mimba yake kutungika na yeye kuzaliwa akiwa binadamu, Yesu aliishi mbinguni. (Ufu. 3:14; Yn. 8:23, 58)
Yesu huabudu Baba yake akiwa Mungu pekee wa kweli; Yesu hakudai kamwe kuwa sawa na Mungu. (Yn. 17:3; 20:17; 14:28)
Yesu alitoa uhai wake mkamilifu wa kibinadamu uwe fidia kwa ajili ya wanadamu. Dhabihu yake huwezesha uhai wa milele kwa ajili ya wote ambao hudhihirisha imani kikweli katika hiyo. (Mk. 10:45; Yn. 3:16, 36)
Yesu aliinuliwa kutoka kwa wafu akiwa mtu wa roho asiyeweza kufa. (1 Pet. 3:18; Rum. 6:9)
Yesu amerudi (akiwa amekwisha elekeza fikira zake kwenye dunia akiwa Mfalme) na sasa yupo akiwa roho mtukufu. (Mt. 24:3, 23-27; Yn. 14:19)
◆ Shetani ndiye “mtawala wa ulimwengu” asiyeonekana. (Yn. 12:31; 1 Yoh. 5:19, “NW”)
Mwanzoni alikuwa mwana mkamilifu wa Mungu, lakini aliruhusu hisi za umashuhuri wa kibinafsi usitawi katika moyo wake, akatamani sana ibada iliyokuwa ya Yehova pekee, akashawishi Adamu na Hawa wamtii yeye badala ya kusikiliza Mungu. Hivyo alijifanya mwenyewe Shetani, linalomaanisha “Mpinzani.” (Yn. 8:44; Mwa. 3:1-5; linganisha Kumbukumbu la Torati 32:4, 5; Yakobo 1:14, 15; Luka 4:5-7.)
Shetani ‘anaiongoza vibaya dunia nzima inayokaliwa’; yeye na roho waovu wake ndio wa kulaumiwa kwa sababu ya dhiki yenye kuongezeka duniani katika huu wakati wa mwisho. (Ufu. 12:7-9, 12)
Katika wakati wa Mungu uliowekwa, Shetani na roho waovu wake wataharibiwa milele. (Ufu. 20:10; 21:8)
◆ Ufalme wa Mungu chini ya Kristo utachukua mahali pa serikali zote za kibinadamu nao utakuwa ndiyo serikali moja tu juu ya jamii yote ya kibinadamu. (Dan. 7:13, 14)
Mfumo mwovu wa mambo uliopo utaharibiwa kabisa. (Dan. 2:44; Ufu. 16:14, 16; Isa. 34:2)
Ufalme wa Mungu utatawala kwa uadilifu na utaletea raia zake amani ya kweli. (Isa. 9:6, 7; 11:1-5; 32:17; Zab. 85:10-12)
Waovu watakatiliwa mbali milele, nao waabudu wa Yehova watafurahia usalama wa kudumu. (Mit. 2:21, 22; Zab. 37:9-11; Mt. 25:41-46; 2 The. 1:6-9; Mika 4:3-5)
◆ Sasa sisi tunaishi, tangu 1914,d katika “wakati wa mwisho” wa ulimwengu huu mwovu. (Mt. 24:3-14; 2 Tim. 3:1-5; Dan. 12:4)
Wakati wa pindi hii, ushahidi unatolewa kwa mataifa yote; baada ya hapo mwisho utakuja, si wa dunia, bali wa mfumo mwovu na watu wasiomwogopa Mungu. (Mt. 24:3, 14; 2 Pet. 3:7; Mhu. 1:4)
◆ Kuna njia moja tu iongozayo kwenye uhai; si dini zote au mazoea ya kidini hukubaliwa na Mungu. (Mt. 7:13, 14; Yn. 4:23, 24; Efe. 4:4, 5)
Ibada ya kweli hukazia si sherehe wala wonyesho wa nje-nje bali upendo wa kweli kwa Mungu, ukionyeshwa kwa kutii amri zake na mtu kupenda wanadamu wenzake. (Mt. 15:8, 9; 1 Yoh. 5:3; 3:10-18; 4:21; Yn. 13:34, 35)
Watu wa kutoka mataifa yote, jamii, na vikundi vya lugha waweza kumtumikia Yehova na kuwa na kibali chake. (Mdo. 10:34, 35; Ufu. 7:9-17)
Sala yapasa kuelekezwa kwa Yehova pekee kupitia Yesu; sanamu hazipasi kutumiwa ama zikiwa vitu vya kuabudiwa ama zikiwa misaada katika ibada. (Mt. 6:9; Yn. 14:6, 13, 14; 1 Yoh. 5:21; 2 Kor. 5:7; 6:16; Isa. 42:8)
Mazoea ya kuwasiliana na roho lazima yaepukwe. (Gal. 5:19-21; Kum. 18:10-12; Ufu. 21:8)
Hakuna tofauti kati ya makasisi na watu wa kawaida miongoni mwa Wakristo wa kweli. (Mt. 20:25-27: 23:8-12)
Ukristo wa kweli hautii ndani kushika sabato ya kila juma au kujipatanisha na matakwa mengine ya Sheria ya Musa ili kupata wokovu; kufanya hivyo kungekuwa kumkataa Kristo, aliyetimiza Sheria. (Gal. 5:4; Rum. 10:4; Kol. 2:13-17)
Wale wazoeao ibada ya kweli hawashiriki katika imani ya mchanganyiko. (2 Kor. 6:14-17; Ufu. 18:4)
Wote ambao ni wanafunzi wa Yesu kikweli hubatizwa kwa uzamisho kamili. (Mt. 28:19, 20; Mk. 1:9, 10; Mdo. 8:36-38)
Wote wafuatao kielelezo cha Yesu na kutii amri zake hutoa ushahidi kwa wengine juu ya Ufalme wa Mungu. (Luka 4:43; 8:1; Mt. 10:7; 24:14)
◆ Kifo ni tokeo la kurithi dhambi kutoka kwa Adamu. (Rum. 5:12; 6:23)
Wakati wa kufa, nafsi ndiyo hufa. (Eze. 18:4, “NW,” “Zaire Swahili Bible”)
Wafu hawafahamu lolote. (Zab. 146:4; Mhu. 9:5, 10)
Helo (Sheoli, Hadesi) ni kaburi la ujumla la wanadamu. (Ayu. 14:13, “Dy”; Ufu. 20:13, 14, “KJ,” pambizoni)
Lile “ziwa la moto’ ambamo waovu wasiorekebika hutupwa hufananisha, kama vile Biblia yenyewe husema, “mauti ya pili,” kifo cha milele. (Ufu. 21:8)
Ufufuo ndio tumaini kwa ajili ya wafu na kwa wale wote ambao wamepoteza wapendwa katika kifo. (1 Kor. 15:20-22; Yn. 5:28, 29; linganisha Yohana 11:25, 26, 38-44; Marko 5:35-42.)
Kifo kwa sababu ya dhambi ya Adamu hakitakuwapo tena. (1 Kor. 15:26; Isa. 25:8; Ufu. 21:4)
◆ “Kundi dogo,” 144,000 tu, huenda mbinguni. (Luka 12:32; Ufu. 14:1, 3)
Hao ndio ambao ‘wamezaliwa tena’ wakiwa wana wa Mungu wa kiroho. (Yn. 3:3; 1 Pet. 1:3, 4)
Mungu huwateua kutoka vikundi vyote vya watu na mataifa wakatawale wakiwa wafalme pamoja na Kristo katika ule Ufalme. (Ufu. 5:9, 10; 20:6)
◆ Wengine walio na upendeleo wa Mungu wataishi milele duniani. (Zab. 37:29; Mt. 5:5; 2 Pet. 3:13)
Dunia haitaharibiwa kamwe au kuondolewa wakaaji. (Zab. 104:5; Isa. 45:18)
Kupatana na kusudi la awali la Mungu, dunia yote itakuwa paradiso. (Mwa. 1:27, 28; 2:8, 9; Luka 23:42, 43, “NW,” “ZSB”)
Kutakuwako makao yenye kufaa na chakula kingi cha kufurahiwa na kila mtu. (Isa. 65:21-23; Zab. 72:16)
Magonjwa, aina zote za kutojiweza, na kifo chenyewe yatakuwa mambo ya wakati uliopita. (Ufu. 21:3, 4; Isa. 35:5, 6)
◆ Mamlaka za kilimwengu zapasa kutendewa kwa staha zinayostahili. (Rum. 13:1-7; Tito 3:1, 2)
Wakristo wa kweli hawashiriki katika uasi dhidi ya mamlaka za kiserikali. (Mit. 24:21, 22; Rum. 13:1)
Wao hutii sheria zote zisizohitilafiana na sheria ya Mungu, lakini utii kwa Mungu ni wa kwanza. (Mdo. 5:29)
Wao humwiga Yesu katika kudumisha kutokuwamo kwa habari ya mambo ya kisiasa ya ulimwengu. (Mt. 22:15-21; Yn. 6:15)
◆ Lazima Wakristo wajipatanishe na viwango vya Biblia kuhusu damu na adili katika ngono. (Mdo. 15:28, 29)
Kuingiza damu ndani ya mwili kupitia kinywa au mishipa huhalifu sheria ya Mungu. (Mwa. 9:3-6; Mdo. 15:19, 20)
Wakristo wapaswa kuwa safi kiadili; uasherati; uzinzi, na ugoni-jinsia-moja lazima yasiwe na mahali katika maisha yao, wala ulevi wala matumizi mabaya ya dawa za kulevya. (1 Kor. 6:9-11; 2 Kor. 7:1)
◆ Ufuatiaji wa haki na uaminifu wa kibinafsi katika kutunza madaraka ya ndoa na familia ni ya maana kwa Wakristo. (1 Tim. 5:8; Kol. 3:18-21; Ebr. 13:4)
Ukosefu wa haki katika usemi au katika biashara, pamoja na kujifanya mnafiki, haupatani na kuwa Mkristo. (Mit. 6:16-19; Efe. 4:25; Mt. 6:5; Zab. 26:4)
◆ Ibada yenye kukubalika kwa Yehova hutaka kwamba sisi tumpende zaidi ya mengine yote. (Luka 10:27; Kum. 5:9)
Kufanya mapenzi ya Yehova, na hivyo kuleta heshima kwa jina lake, ndilo jambo la maana zaidi katika maisha ya Mkristo wa kweli. (Yn. 4:34; Kol. 3:23; 1 Pet. 2:12)
Huku wakifanya mema kwa watu wote kadiri wawezavyo, Wakristo hutambua wajibu wa pekee kuelekea watumishi wenzao wa Mungu; hivyo msaada wao wakati wa ugonjwa na msiba huelekezwa kwa hawa hasa. (Gal. 6:10; 1 Yoh. 3:16-18)
Kumpenda Mungu huwataka Wakristo wa kweli watii, si amri yake ya kupenda jirani yao bali pia wasipende njia ya ulimwengu huu ya ukosefu wa adili na ya kupenda vitu vya kimwili. Wakristo wa kweli si sehemu ya ulimwengu na hivyo hawajiungi katika utendaji ambao ungeonyesha kuwa wanashiriki roho yao. (Rum. 13:8, 9; 1 Yoh. 2:15-17; Yn. 15:19; Yak. 4:4)
[Maelezo ya Chini]
d Kwa habari zaidi, ona kitabu “Ufalme Wako Uje.”
[Picha katika ukurasa wa 121]
C. T. Russell alianza kutangaza “Zion’s Watch Tower” katika 1879, alipokuwa na umri wa miaka 27
[Picha katika ukurasa wa 125]
Sir Isaac Newton na Henry Grew walikuwa miongoni mwa wale ambao mapema walikuwa wamekataa Utatu kuwa si wa kimaandiko
[Picha katika ukurasa wa 128]
Katika mjadala wa hadhara, Russell alitoa hoja kwamba wafu ni wafu kabisa, wala hawako hai pamoja na malaika wala pamoja na roho waovu katika mahali pasipo na tumaini
Jumba la Carnegie, Allegheny, Pennsylvania—mahali mjadala ulipofanyiwa
[Picha katika ukurasa wa 130]
Russell alisafiri kwenda katika majiji makubwa na madogo akaseme kweli juu ya helo
[Picha katika ukurasa wa 131]
Frederick Franz, mwanafunzi wa chuo kikuu, alipopata kujua kweli juu ya hali ya wafu, alibadili kabisa miradi yake maishani
[Picha katika ukurasa wa 135]
1914 ukiwa ndio mwisho wa Nyakati za Mataifa ulipewa utangazaji mpana na Wanafunzi wa Biblia, kama vile katika trakti hii ya I.B.S.A. iliyogawanywa wakati wa 1914
[Picha katika ukurasa wa 137]
Katika 1931, kwa kutumia mfumo wa redio wenye kuenea zaidi uliokuwa umepata kutangazwa hewani, J. F. Rutherford alionyesha kwamba ni Ufalme wa Mungu pekee unaoweza kuleta kitulizo cha kudumu kwa binadamu
Ile hotuba “Ufalme, Tumaini la Ulimwengu,” ilisambazwa na vituo 163 wakati uleule mmoja na ikarudiwa na vituo vingine 340 baadaye
[Picha katika ukurasa wa 142]
A. H. Macmillan alitumwa kwa meli kwenda Palestina katika 1925 kwa sababu ya kupendezwa kipekee na fungu la Wayahudi kuhusiana na unabii wa Biblia
-
-
Jinsi Tulivyokuja Kujulikana Kuwa Mashahidi wa YehovaMashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
Sura ya 11
Jinsi Tulivyokuja Kujulikana Kuwa Mashahidi wa Yehova
KATIKA pindi ya miongo ya mapema ya historia yao ya kisasa, mara nyingi walirejezewa tu kuwa Wanafunzi wa Biblia. Wengine walipouliza juu ya jina la tengenezo, mara nyingi ndugu zetu walikuwa wakijibu, “Sisi ni Wakristo.” Ndugu Russell alijibu swali kama hilo kwa kusema, katika Watch Tower hivi: “Sisi hatujitengi wenyewe na Wakristo wengine kwa kuchukua jina lolote lenye kutofautisha au la pekee. Sisi tunatosheka na jina, Wakristo, ambalo kwalo watakatifu wa mapema walijulikana.”—Toleo la Septemba 1888.
Basi, ilitukiaje kwamba leo tunajulikana kuwa Mashahidi wa Yehova?
Jina Wakristo
Wafuasi wa kweli wa Yesu Kristo, katika karne ya kwanza na katika nyakati za kisasa pia, wamejirejezea wenyewe na waamini wenzao kuwa “ndugu,” “marafiki,” na “kutaniko la Mungu.” (Mdo. 11:29; 3 Yoh. 14; 1 Kor. 1:2, NW) Pia wamesema juu ya Kristo kuwa ni “Bwana-mkubwa” na wakasema juu yao kuwa “watumwa wa Kristo Yesu” na “watumwa wa Mungu.” (Kol. 3:24; Flp. 1:1; 1 Pet. 2:16, NW) Mitajo hiyo imetumiwa sana ndani ya kutaniko, na imeeleweka vizuri humo.
Katika karne ya kwanza, namna ya maisha iliyotegemea imani katika Yesu Kristo (na kwa kupanuliwa, kutaniko lenyewe) ilirejezewa kuwa “Ile Njia.” (Mdo. 9:2; 19:9, NW) Tafsiri kadhaa za Matendo 18:25 (NW) huonyesha kwamba iliitwa pia “njia ya Yehova.”a Kwa upande mwingine, baadhi ya wale waliokuwa nje ya kutaniko waliiita kwa dharau “farakano la Wanazareti.”—Mdo. 24:5, NW.
Kufikia 44 W.K. au muda mfupi baada ya hapo, wafuasi waaminifu wa Yesu Kristo walianza kujulikana kuwa Wakristo. Wengine hudai kwamba ni watu wa nje waliowabandika jina Wakristo, wakifanya hivyo kwa njia ya kuwavunjia heshima. Hata hivyo, idadi fulani ya watungaji wa kamusi za Biblia na waelezaji hutaarifu kwamba kitenzi kilichotumiwa kwenye Matendo 11:26 hudokeza kwamba ulikuwa mwelekezo au ufunuo wa kimungu. Hivyo, katika New World Translation, andiko hilo husomwa hivi: “Ilikuwa kwanza katika Antiokia kwamba wanafunzi kwa uongozi wa kimungu waliitwa Wakristo.” (Mifasirio inayofanana na huo inapatikana katika Literal Translation of the Holy Bible, ya Robert Young, Chapa Iliyosahihishwa, ya 1898; The Simple English Bible, ya 1981; na New Testament, ya Hugo McCord, ya 1988.) Kufikia 58 W.K., jina Wakristo likawa lenye kujulikana sana hata na wakuu wa Kiroma.—Mdo. 26:28.
Mitume wa Kristo walipokuwa wangali hai, jina Wakristo lilikuwa lenye kutofautisha na mahususi. (1 Pet. 4:16) Wote waliodai kuwa Wakristo lakini ambao imani zao au mwenendo vilipinga dai lao walifukuzwa kutoka jumuiya ya Kikristo. Hata hivyo, kama vile Yesu alivyokuwa ametabiri, baada ya kifo cha mitume Shetani alipanda mbegu ambazo zilitokeza Wakristo wa mwigo. Watu hao bandia walidai pia kutumia jina Wakristo. (Mt. 13:24, 25, 37-39) Ukristo wenye kuasi imani ulipotumia njia ya kugeuza watu kwa nguvu, wengine walidai kuwa Wakristo ili tu waepuke mnyanyaso. Baada ya wakati, Mzungu yeyote asiyedai kuwa Myahudi, Mwislamu, au Mwatheisti mara nyingi alionwa kuwa Mkristo, bila kujali imani au mwenendo wake.
Majina ya Dharau ya Kubandikwa
Kuanzia karne ya 16 na kuendelea, hali hiyo ilizusha tatizo kwa Warekebishaji wa dini. Kwa kuwa jina Wakristo lilikuwa linatumiwa vibaya sana, wangewezaje kujitofautisha na wengine waliodai kuwa Wakristo?
Mara nyingi walikubali tu kimyakimya kutumia jina la kubandikwa la dharau walilopewa na maadui wao. Hivyo wanatheolojia wenye kumpinga Martin Luther, katika Ujerumani, ndio waliokuwa wa kwanza kutumia jina lake kwa wafuasi wake, wakiwaita Waluther. Wale walioshirikiana na John Wesley, katika Uingereza, walibandikwa jina Wamethodisti kwa sababu walishika kihususa na kufuata wajibu mbalimbali wa kidini kwa utaratibu kuliko ilivyo kawaida. Kwanza Wabaptisti walipinga jina la kubandikwa Anabaptisti (kumaanisha, “Mbatiza-Upya”) lakini hatua kwa hatua wakakubali jina Baptisti ikiwa namna ya kuridhiana.
Namna gani Wanafunzi wa Biblia? Makasisi waliwabandika jina Warusselli na Warutherford. Lakini kukubali jina kama hilo kungechochea roho ya kimafarakano. Haingepatana na karipio walilopewa Wakristo wa mapema na mtume Paulo, ambaye aliandika hivi: “Mmoja asemapo: ‘Mimi ni wa Paulo,’ lakini mwingine asema: ‘Mimi ni wa Apolo,’ je, nyinyi si wanadamu tu [yaani, wenye maoni ya kimwili badala ya yale ya kiroho]?” (1 Kor. 3:4, NW) Baadhi ya watu waliwabandika jina “Wanamapambazuko wa Mileani”; lakini Utawala wa Mileani wa Kristo lilikuwa mojapo tu mafundisho yao. Wengine waliwaita “Watu wa Watch Tower”; lakini hiyo pia haikufaa, kwa kuwa Watch Tower lilikuwa tu mojapo vichapo walivyotumia kuenezea kweli ya Biblia.
Uhitaji wa Jina Lenye Kutofautisha
Baada ya wakati, ikazidi kuwa wazi sana kwamba kuongezea mtajo Wakristo, kutaniko la watumishi wa Yehova kwa kweli lilihitaji jina lenye kutofautisha. Maana ya jina Wakristo ilikuwa imepotoshwa katika akili za umma kwa sababu watu waliodai kuwa Wakristo mara nyingi walikuwa na wazo kidogo tu au hawakuwa na wazo lolote juu ya Yesu Kristo alikuwa nani, yale aliyofundisha, na yale ambayo wao wapaswa kuwa wakifanya ikiwa kwa kweli walikuwa wafuasi wake. Kwa kuongezea, kadiri ndugu zetu walivyofanya maendeleo katika uelewevu wao wa Neno la Mungu, waliona waziwazi uhitaji wa kujitenga na kuwa tofauti na mifumo ya kidini iliyodai kwa udanganyifu kuwa ya Kikristo.
Ni kweli, ndugu zetu mara nyingi walijirejezea kuwa Wanafunzi wa Biblia, na kuanzia katika 1910, walitumia jina International Bible Students Association, kwa habari ya mahali pa mikutano yao. Katika 1914, ili kuepuka mvurugo juu ya shirika lao la kisheria lililokuwa limefanyizwa karibuni lililoitwa International Bible Students Association, walikubali jina Wanafunzi wa Biblia Wenye Kushirikiana kwa ajili ya vikundi vyao vya mahali pao. Lakini ibada yao ilitia ndani mengi zaidi ya kujifunza Biblia. Zaidi ya hilo, walikuwako wengine waliojifunza Biblia—wengine kwa sababu za kidini; wengine, wakiwa wachambuzi; na wengi, wakiwa watu walioiona tu kuwa fasihi bora. Halafu, baada ya kifo cha Ndugu Russell, baadhi ya wale walioshirikiana hapo kwanza walikataa kushirikiana na Watch Tower Society na International Bible Students Association, hata wakapinga kazi ya mashirika hayo. Vikundi hivyo vilivyojitenga vilitumia majina mbalimbali, baadhi yavyo vikishikamana na mtajo Wanafunzi wa Biblia Wenye Kushirikiana. Jambo hilo lilisababisha mvurugo zaidi.
Halafu, katika 1931, sisi tulikubali kwa moyo jina lenye kutofautisha kikweli Mashahidi wa Yehova. Mtunga-vitabu Chandler W. Sterling huita hilo kuwa “tendo la werevu zaidi ya yote” la J. F. Rutherford, wakati huo akiwa msimamizi wa Watch Tower Society. Kama vile mwandikaji huyo alivyoyaona mambo, hiyo ilikuwa hatua ya werevu si kwa kuandalia tu kikundi jina rasmi, bali pia ilifanya liwe jambo rahisi kufasiri marejezo yote ya Biblia ya maneno “shahidi” na “ushahidi” kuwa yatumika hususa kwa Mashahidi wa Yehova. Kwa kutofautisha, A. H. Macmillan, mshirika wa usimamizi wa wasimamizi watatu wa Watch Tower Society, alisema hivi kuhusu tangazo hilo lililofanywa na Ndugu Rutherford: “Hamna shaka akilini mwangu—wala wakati huo wala sasa—kwamba Bwana alimwongoza katika hilo, na kwamba hilo ndilo jina ambalo Yehova ataka sisi tuitwe, na sisi tunafurahi sana na kuterema sana kuwa nalo.” Mambo ya hakika yanaunga mkono maoni gani? Je, jina hilo lilikuwa ‘tendo la werevu’ la Ndugu Rutherford, au lilikuwa tokeo la mwelekezo wa kimungu?
Matukio Yaliyoelekeza Kwenye Jina Hilo
Ilikuwa katika karne ya nane K.W.K. kwamba Yehova alisababisha Isaya aandike: “Ninyi ni mashahidi wangu, asema BWANA [“Yehova,” NW], na mtumishi wangu niliyemchagua; mpate kujua, na kuniamini, na kufahamu ya kuwa mimi ndiye; kabla yangu hakuumbwa Mungu awaye yote, wala baada yangu mimi hatakuwapo mwingine. . . . Ninyi ni mashahidi wangu, asema BWANA [“Yehova,” NW], nami ni Mungu.” (Isa. 43:10, 12) Kama inavyoonyeshwa katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, unabii mwingi ulioandikwa na ule wa Isaya una utimizo kuhusiana na kutaniko la Kikristo. (Linganisha Isaya 8:18 na Waebrania 2:10-13; Isaya 66:22 na Ufunuo 21:1, 2.) Hata hivyo, Isaya 43:10, 12 halikuzungumzwa kirefu kamwe katika The Watch Tower wakati wa miaka 40 ya kwanza ya kuchapwa kwalo.
Hata hivyo, baada ya hapo, funzo lao la Maandiko lilielekeza uangalifu wa watumishi wa Yehova kwenye matukio mapya yenye maana. Ufalme wa Mungu, Yesu akiwa Mfalme wa Kimesiya ulikuwa umezaliwa mbinguni katika 1914. Katika 1925, mwaka ambao jambo hilo lilielezwa wazi katika The Watch Tower, ile amri ya kiunabii, katika Isaya sura ya 43, ya kuwa mashahidi wa Yehova ilipewa ufikirio katika matoleo 11 tofauti ya gazeti hilo.
Katika The Watch Tower la Januari 1, 1926, makala kuu ilizungumzia swali lenye kutokeza wito: “Ni Nani Atamheshimu Yehova?” Katika pindi ya miaka mitano iliyofuata, The Watch Tower lilizungumzia kisehemu cha Isaya 43:10-12 katika matoleo 46 mbalimbali na kila wakati likalitumia kuwahusu Wakristo wa kweli.b Katika 1929 ilitajwa kwamba suala kuu linalokabili viumbe wenye akili lahusu kuheshimu jina la Yehova. Na kuhusu daraka walilo nalo watumishi wa Yehova kwa habari ya suala hilo, Isaya 43:10-12 lilitokezwa mara kwa mara lipate kufikiriwa.
Hivyo mambo ya hakika huonyesha kwamba kama tokeo la funzo la Biblia, uangalifu ulikuwa ukivutwa kwa kurudiarudia kwenye wajibu wao wa kuwa mashahidi wa Yehova. Si jina la kikundi fulani lililokuwa likifikiriwa, bali kazi ambayo wangefanya.
Lakini mashahidi hao wangejulikana kwa jina gani? Ni jambo gani lingefaa kwa kufikiria kazi waliyokuwa wakifanya? Neno la Mungu mwenyewe lilielekeza kwenye mkataa gani? Jambo hilo lilizungumzwa kwenye mkusanyiko katika Colombus, Ohio, Marekani, Julai 24-30, 1931.
Jina Jipya
Zile herufi kubwa JW zilionekana kwa njia yenye kutokeza katika jalada la mbele la programu ya mkusanyiko. Zilimaanisha nini? Ilikuwa mpaka Jumapili, Julai 26, ndipo maana yazo ilipoelezwa. Katika siku hiyo Ndugu Rutherford alitoa hotuba ya watu wote “Ufalme, Tumaini la Ulimwengu.” Katika hotuba hiyo, alipokuwa akitambulisha wale ambao hupiga mbiu ya Ufalme wa Mungu, msemaji huyo alirejezea kipekee jina “Mashahidi wa Yehova” (Jehovah’s Witnesses).
Baadaye siku hiyo Ndugu Rutherford alifuatia hilo kwa hotuba nyingine, ambapo alipokuwa akiitoa alizungumzia sababu jina lenye kutofautisha lilihitajiwa.c Maandiko yenyewe yalielekeza kwenye jina gani? Msemaji alinukuu Matendo 15:14 (NW), ambalo huelekeza uangalifu kwenye kusudi la Mungu la kutwaa watu kutoka mataifa “watu kwa ajili ya jina lake.” Katika hotuba yake alikazia uhakika wa kwamba kama ilivyotaarifiwa kwenye Ufunuo 3:14 (NW), Yesu Kristo ni “shahidi mwaminifu na wa kweli.” Alirejezea Yohana 18:37 (NW), ambapo Yesu alijulisha hivi: “Kwa ajili ya hili nimekuja kuingia ulimwenguni ili nitoe ushahidi juu ya ile kweli.” Alielekeza uangalifu kwenye 1 Petro 2:9, 10 (NW), ambalo husema kwamba watumishi wa Mungu ‘wangetangaza kotekote sifa bora kabisa za yeye aliyewaita nyinyi kutoka katika giza kuingia katika nuru yake ya ajabu.’ Alitoa sababu kwa kutumia idadi fulani ya maandiko kutoka Isaya, ambayo si yote yalieleweka wazi wakati huo, halafu akafikisha utoaji wake kwenye upeo kwa kutumia Isaya 43:8-12, ambalo hutia ndani utume huu wa kimungu: “‘Ninyi ni mashahidi wangu, asema BWANA [“Yehova,” NW], nami ni Mungu.” Basi, Neno la Yehova mwenyewe lilikuwa likiwaelekeza kwenye mkataa gani? Ni jina gani lingekuwa lenye kupatana na njia ambayo kwa kweli Mungu alikuwa akiwatumia?
Jibu lisilo na shaka lilitiwa katika azimio lililokubaliwa kwa idili katika pindi hiyo.d Azimio hilo lilisema hivi kwa sehemu:
“Ili hali yetu ipate kujulikana, na kwa sababu ya kuamini kwamba hii inapatana na mapenzi ya Mungu, kama yanavyoelezwa katika Neno lake, NA IAZIMIWE kama ifuatavyo:
“KWAMBA, sisi tunampenda sana Ndugu Charles T. Russell kwa ajili ya kazi yake, na kwamba tunatambua kwa furaha kwamba Bwana alimtumia na kubariki sana kazi yake, lakini hatuwezi kupatana na Neno la Mungu kukubali kuitwa kwa jina ‘Warusselli’; kwamba Watch Tower Bible and Tract Society na International Bible Students Association na Peoples Pulpit Association ni majina tu ya mashirika tuliyo nayo kama kampuni ya Wakristo, nasi twayasimamia na kuyatumia kuendesha kazi yetu kwa kutii amri za Mungu, hata hivyo hakuna lolote la majina hayo linaloambatana nasi wala kutuhusu vya kufaa kutumiwa tukiwa jamii ya Wakristo wanaofuata hatua za Bwana na Bwana-Mkubwa wetu, Kristo Yesu; kwamba sisi tu wanafunzi wa Biblia, lakini tukiwa jamii ya Wakristo walio shirika, tunakataa kujitwalia au kuitwa kwa jina ‘Wanafunzi wa Biblia’ au majina mengine kama hayo ili kutambulisha hali yetu halisi mbele za Bwana; twakataa kuchukua au kuitwa kwa jina la binadamu yeyote;
“KWAMBA, kwa kuwa tulinunuliwa kwa damu yenye thamani ya Yesu Kristo Bwana na Mkombozi wetu, aliyehesabiwa kuwa mwadilifu na kuzaliwa na Yehova Mungu na kuitwa kwenye ufalme wake, bila kusitasita twatangaza ushikamano na ujitoaji wetu wote kwa Yehova Mungu na ufalme wake; kwamba sisi tu watumishi wa Yehova Mungu walioagizwa kufanya kazi kwa jina lake, na kwa kutii amri yake, tutoe ushuhuda wa Yesu Kristo, na kujulisha watu kwamba Yehova ndiye Mungu wa kweli na Mweza Yote; kwa hiyo kwa furaha tunalikubali na kulichukua jina ambalo kinywa cha Bwana Mungu kimelitaja, nasi twataka tujulikane na kuitwa kwa jina hili, yaani, mashahidi wa Yehova [Jehovah’s witnesses].—Isa. 43:10-12, NW.”e
Kufuatia kutolewa kwa azimio lote, makofi yenye kuendelea na ya sauti kubwa yalionyesha kwamba wasikilizaji walikubaliana kabisa na yaliyosemwa.
Kukubali Daraka
Ilikuwa heshima kama nini kuitwa jina la Mungu pekee wa kweli, Mwenye Enzi Kuu wa ulimwengu wote mzima! Lakini daraka laambatana na jina hilo. Ni daraka ambalo vikundi vingine vya kidini havitaki. Kama vile Ndugu Rutherford alivyosema katika hotuba yake: “Wenye furaha ni hao ambao waweza kutwaa jina ambalo hakuna mtu yeyote chini ya mbingu alitakaye isipokuwa wale ambao wamejitoa kabisa na bila masharti kwa Yehova.” Hata hivyo, inafaa kama nini kwamba watumishi wa Yehova waitwe jina la kibinafsi la Mungu, kwamba walijulishe, na kwamba lishirikishwe kwa njia yenye kutokeza na kupigiwa mbiu kwa kusudi lake!
Kikundi chochote au mtu mmoja-mmoja yeyote ambaye husema kwa jina la Yehova hujiweka chini ya wajibu wa kuwasilisha neno lake kwa njia ya kweli. (Yer. 23:26-28) Lazima wajulishe si maandalizi tu ya Yehova kwa ajili ya kubariki wapendao uadilifu bali pia hukumu zake juu ya wale watendao mambo yasiyo ya uadilifu. Kama vile Yehova alivyoamuru manabii wake katika nyakati zilizopita, ndivyo na leo, mashahidi wake lazima wasiondoe chochote kutoka neno la Mungu kwa kushindwa kulijulisha. (Yer. 1:17; 26:2; Eze. 3:1-11) Lazima wapige mbiu ya “mwaka wa nia njema kwa upande wa Yehova na siku ya kisasi kwa upande wa Mungu wetu.” (Isa. 61:1, 2, NW) Wale waliokuwa wakikubali azimio hilo lililo juu walitambua daraka hilo, na katika sehemu ya pili ya azimio hilo, walijulisha hivi:
“Tukiwa mashahidi wa Yehova kusudi letu moja tu na la pekee ni kuwa watiifu kabisa kwa amri zake; kujulisha kwamba yeye pekee ndiye Mungu Mweza Yote na wa kweli; kwamba Neno lake ni la kweli na kwamba jina lake lastahili heshima na utukufu wote; kwamba Kristo ni Mfalme wa Mungu, ambaye yeye amemweka juu ya kiti cha ufalme cha mamlaka; kwamba ufalme wake sasa umekuja, na katika kutii amri za Bwana lazima sisi tujulishe sasa habari njema hizi kuwa ushuhuda au ushahidi kwa mataifa na kuarifu watawala na watu juu ya tengenezo katili na lenye uonevu la Shetani, na hasa kwa habari ya ‘Jumuiya ya Wakristo,’ ambayo ndiyo sehemu yenye uovu zaidi ya tengenezo hilo lionekanalo, na juu ya kusudi la Mungu la kuharibu hivi karibuni tengenezo la Shetani, tendo hilo kuu litafuatwa upesi na Kristo Mfalme akiletea vikundi vyote vya watu watiifu wa dunia amani na ufanisi, uhuru na afya, furaha na uhai wa milele; kwamba ufalme wa Mungu ndilo tumaini la ulimwengu, hakuna jingine, na kwamba ujumbe huu lazima utolewe na wale wanaotambulishwa kuwa mashahidi wa Yehova.
“Kwa unyenyekevu twaalika watu wote ambao wamejitoa kabisa kwa Yehova na ufalme wake wajiunge katika kupigia wengine mbiu ya habari hizi njema, ili viwango vyenye uadilifu vya Bwana viinuliwe juu, na kwamba watu wa ulimwengu wapate kujua mahali pa kupata kweli na tumaini kwa ajili ya kitulizo; na zaidi ya yote, kwamba lile jina kuu na takatifu la Yehova Mungu lipate kutetewa na kutukuzwa.”
Si katika Colombus, Ohio, katika Marekani tu, bali kufika mbali sana Australia kwamba wasikilizaji walipiga makofi ghafula waliposikia tangazo la jina hilo jipya. Katika Japani, baada ya saa nyingi za jitihada, ni kisehemu kifupi tu cha programu kilichonaswa katika redio ya masafa mafupi katika usiku wa manane. Mara hiyo kikatafsiriwa. Hivyo kile kikundi kidogo cha huko kilisikia azimio hilo na kishindo cha makofi. Matsue Ishii alikuwapo pamoja nao, na kama alivyoandika baadaye, ‘waliinua kilio cha shangwe kupatana na ndugu zao katika Marekani.’ Kufuatia kusanyiko katika Columbus, makusanyiko na makutaniko ya Mashahidi wa Yehova katika nchi zote ambako walikuwa wakiendeleza huduma yao wajionyesha wenyewe kuwa wakubaliana kabisa na azimio hilo. Kutoka Norway, ikiwa kielelezo kimoja, ilikuja ripoti hii: “Kwenye mkusanyiko wetu wa mwaka . . . katika Oslo sisi sote tuliinuka kwa miguu yetu na kwa idili kubwa tuliinua sauti ‘Ndiyo,’ tulipokuwa tukikubali jina letu jipya ‘mashahidi wa Yehova.’”
Ni Zaidi ya Kibandiko
Je, ulimwengu kwa ujumla ungejua kwamba ndugu zetu walikuwa wamekubali jina hilo jipya? Ndiyo, kwelikweli! Hotuba ambayo tangazo la jina letu lilitolewa kwanza iliwakilishwa katika muunganisho wa redio uliopata kuwa mkubwa zaidi kufikia wakati huo. Kuongezea, azimio lililoonyesha jina hilo jipya lilitiwa ndani ya kijitabu The Kingdom, the Hope of the World. Kufuatia mkusanyiko, Mashahidi wa Yehova waligawanya mamilioni ya nakala za kijitabu hicho katika lugha nyingi katika Amerika Kaskazini na Kusini, Ulaya, Afrika, Asia, na visiwa vya bahari. Zaidi ya kutoa nakala nyumba hadi nyumba, walifanya jitihada ya pekee kuitia mikononi mwa kila mkuu wa serikali, mwanabiashara mashuhuri, na kasisi. Baadhi yao waliokuwa wangali hai katika 1992 walikumbuka vema ushiriki wao katika kampeni hiyo yenye umaana.
Si wote waliokipokea vizuri kijitabu hicho. Eva Abbott akumbuka kwamba alipokuwa akiondoka nyumbani mwa kasisi mmoja katika Marekani, kijitabu hicho kilitupwa hewani na kuanguka chini mbele yake. Yeye hakutaka kukiacha hapo, hivyo akakichukua; lakini mbwa mkubwa alinguruma, akakinyakua mkononi mwake, na kukipeleka kwa bwana-mkubwa wake, yule kasisi. Dada huyo alisema: “Kile ambacho sikuweza kupeleka, mbwa huyo alikipeleka!”
Martin Poetzinger, ambaye baadaye alitumikia akiwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, alikumbuka hivi: “Nyuso zenye kushangaa zilionekana kwenye kila mlango tulipojijulisha wenyewe kwa maneno haya: ‘Nimekujia leo nikiwa mmoja wa mashahidi wa Yehova.’ Watu walikuwa wakitikisa vichwa vyao au kuuliza: ‘Lakini nyinyi mngali wanafunzi wa Biblia, sivyo? Au je, mmejiunga na farakano jingine?’” Hatua kwa hatua hali hiyo ikabadilika. Miongo kadhaa baada ya kuanza kutumia jina lao lenye kutofautisha, Ndugu Poetzinger aliandika: “Ni badiliko kubwa kama nini! Kabla sijasema neno watu hutaja: ‘Lazima uwe mmoja wa mashahidi wa Yehova.’” Ndiyo, sasa wanajua jina hilo.
Jina hilo halikuwa kibandiko tu. Awe kijana au mzee, wa kiume au wa kike, wote kati ya Mashahidi wa Yehova hushiriki katika kazi ya kutoa ushahidi kwa Yehova na kusudi lake tukufu. Kama tokeo, C. S. Braden, profesa wa historia ya kidini, aliandika: “Mashahidi wa Yehova wameieneza dunia kihalisi kwa kutoa kwao ushahidi.”—These Also Believe.
Ijapokuwa kazi ya kutoa ushahidi iliyofanywa na ndugu zetu kabla ya kukubali jina Mashahidi wa Yehova ilikuwa ya duniani pote, kwa kutazama nyuma yaonekana kwamba Yehova alikuwa akiwatayarisha kwa ajili ya kazi kubwa hata zaidi—kukusanywa kwa umati mkubwa ambao ungehifadhiwa ukiwa hai kupitia Har–Magedoni, ukiwa na fursa ya kuishi milele katika dunia iliyo paradiso.
[Maelezo ya Chini]
a New World Translation of the Holy Scriptures; A Literal Translation of the New Testament . . . From the Text of the Vatican Manuscript, ya Herman Heinfetter; na tafsiri sita katika Kiebrania. Ona pia kielezi-chini cha Matendo 19:23 katika New World Translation of the Holy Scriptures.
b Miongoni mwa makala kuu za Watch Tower zilizotangazwa wakati wa kipindi hicho zilikuwa “Yehova na Kazi Zake,” “Heshimu Jina Lake,” “Watu kwa Ajili ya Jina Lake,” “Jina Lake Latukuzwa,” “Shahidi Wa-Kweli na Mwaminifu,” “Msifu Yehova!” “Pendezwa na Yehova,” “Yehova Mkuu Kupita Wote,” “Kutetewa kwa Jina Lake,” “Jina Lake,” na “Mwimbie Yehova.”
c Ona makala “Jina Jipya,” katika The Watch Tower la Oktoba 1, 1931.
d The Watch Tower, Septemba 15, 1931, kur. 278-279.
e Ijapokuwa ushahidi waonyesha kwa njia yenye kusadikisha kwenye mwelekezo wa Yehova katika uteuzi wa jina Mashahidi wa Yehova, Mnara wa Mlinzi la Kiingereza (Februari 1, 1944, kur. 42-43; Oktoba 1, 1957, uku. 607) na kitabu “New Heavens and a New Earth” (kur. 231-237) baadaye vilitaja kwamba jina hilo silo lile “jina jipya” lirejezewalo kwenye Isaya 62:2; 65:15; na Ufunuo 2:17, ingawa jina hilo lapatana na uhusiano mpya unaorejezewa katika maandiko hayo mawili katika Isaya.
[Blabu katika ukurasa wa 149]
“Wanafunzi kwa uongozi wa kimungu waliitwa Wakristo”
[Blabu katika ukurasa wa 150]
Jina Wakristo likawa limepotoshwa katika akili za umma
[Blabu katika ukurasa wa 150]
Hawakuwa Wanafunzi wa Biblia tu
[Blabu katika ukurasa wa 157]
“Ninyi ni mashahidi wangu, asema BWANA [“Yehova,” “NW”], nami ni Mungu”
[Sanduku katika ukurasa wa 151]
Jina Mashahidi wa Yehova Katika Mabara ya Amerika
Kiarabu شهود يهوه
Kiarmenia Եհովայի Վկաներ
Kichina 耶和華見證人
Kiingereza Jehovah’s Witnesses
Kifaransa Témoins de Jéhovah
Kigiriki Μάρτυρες του Ιεχωβά
Kigreenland Jehovap Nalunaajaasui
Kiitalia Testimoni di Geova
Kijapani エホバの証人
Kikorea 여호와의 증인
Kipapiamento Testigonan di Jehova
Kipoland Świadkowie Jehowy
Kireno Testemunhas de Jeová
Kisamoa Molimau a Ieova
Kihispania Testigos de Jehová
Kisranantongo Jehovah Kotoigi
Kitagalogi Mga Saksi ni Jehova
Kivietnam Nhân-chứng Giê-hô-va
[Sanduku katika ukurasa wa 152]
Wengine Waliliona
Si “The Watch Tower” pekee lililoonyesha kutoka Biblia kwamba Yehova angekuwa na mashahidi duniani. Kama kielelezo, H. A. Ironside, katika kitabu “Lectures on Daniel the Prophet” (kilitangazwa kwanza katika 1911), alirejezea kwa wale ambao kwao ahadi zenye thamani kuu za Isaya sura ya 43 zingetimizwa na kusema: “Hao watakuwa mashahidi wa Yehova, wakishuhudia nguvu na utukufu wa Mungu mmoja wa kweli, wakati Jumuiya ya Wakristo iliyoasi imani itakuwa imeachwa kwenye lile danganyo lenye nguvu iamini uwongo wa Mpinga-Kristo.”
[Sanduku katika ukurasa wa 153]
Jina Mashahidi wa Yehova Katika Nchi za Mashariki na Visiwa vya Pasifiki
Kibengali যিহোবাব সাক্ষীদেব
Kibikoli, Kisebuano, Kihiligaynoni,
Kisamar-Leyte, Kitagalogi Mga Saksi ni Jehova
Kibislama Ol Wetnes blong Jeova
Kichina 耶和華見證人
Kiingereza Jehovah’s Witnesses
Kifiji Vakadinadina i Jiova
Kigujarati যিহোবাব সাক্ষীদেব
Kihindi যিহোবাব সাক্ষীদেব
Kihiri Motu Iehova ena Witness Taudia
Kiiloko Dagiti Saksi ni Jehova
Kiindonesia Saksi-Saksi Yehuwa
Kijapani エホバの証人
Kikannada যিহোবাব সাক্ষীদেব
Kikorea 여호와의 증인
Kimalayalami যিহোবাব সাক্ষীদেব
Kimarathi যিহোবাব সাক্ষীদেব
Kimarshall Dri Kennan ro an Jeova
Kimyanmar ယေဟောဝါသက်သေများ
Kinepali যিহোবাব সাক্ষীদেব
Kipidgini cha New Guin ea Ol Witnes Bilong Jehova
Kiniue Tau Fakamoli a Iehova
Kipalau reSioning er a Jehovah
Kipangasinani Saray Tasi nen Jehova
Kiponape Sounkadehde kan en Siohwa
Kirarotonga Au Kite o Iehova
Kirusi Свидетели Иеговы
Kisamoa, Kituvalu Molimau a Ieova
Kisinhali যিহোবাব সাক্ষীদেব
Kipidgini cha Visiwa vya Solomon all’gether Jehovah’s Witness
Kitahiti Ite no Iehova
Kitamili যিহোবাব সাক্ষীদেব
Kitelugu যিহোবাব সাক্ষীদেব
Kithailand พยานพระยะโฮวา
Kitonga Fakamo‘oni ‘a Sihova
Kitruki Ekkewe Chon Pwarata Jiowa
Kiurdu
Kivietnam Nhân-chứng Giê-hô-va
Kiyapu Pi Mich Rok Jehovah
[Sanduku katika ukurasas wa 154]
Jina Mashahidi wa Yehova Katika Afrika
Kiafrikaani Jehovah se Getuies
Kiamhari የይሖዋ ምሥክሮች
Kiarabu شهود يهوه
Chicheŵa Mboni za Yehova
Cibemba Inte sha kwa Yehova
Kiefịki Mme Ntiense Jehovah
Kiingereza Jehovah’s Witnesses
Kiewe Yehowa Ðasefowo
Kifaransa Témoins de Jéhovah
Kiga Yehowa Odasefoi
Kiguni Kunnudetọ Jehovah tọn lẹ
Kihausa Shaidun Jehovah
Kiigbo Ndịàmà Jehova
Kiluba Ba Tumoni twa Yehova
Kinyarwanda Abahamya ba Yehova
Kirundi Ivyabona vya Yehova
Kikisi Seiyaa Jɛhowaa
Kikwanyama Eendombwedi daJehova
Lingala Batemwe ya Jéhovah
Kiganda Abajulirwa ba Yakuwa
Kimalagasi Vavolombelon’i Jehovah
Kimoore A Zeova Kaset rãmba
Kindonga Oonzapo dhaJehova
Kireno Testemunhas de Jeová
Kisango A-Témoin ti Jéhovah
Kisepedi Dihlatse tša Jehofa
Kisesotho Lipaki tsa Jehova
Kishona Zvapupu zvaJehovha
Silozi Lipaki za Jehova
Kiswahili Mashahidi wa Yehova
Kitigirinya ናይ የሆዋ መሰኻኽር
Tshiluba Bantemu ba Yehowa
Kitsonga Timbhoni ta Yehova
Kitswana Basupi ba ga Jehofa
Kitwi Yehowa Adansefo
Kivenda Ṱhanzi dza Yehova
Xhosa amaNgqina kaYehova
Kiyoruba Ẹlẹ́rìí Jehofa
Kizulu oFakazi BakaJehova
[Sanduku katika ukurasas wa 154]
Jina Mashahidi wa Yehova Katika Ulaya na Mashariki ya Kati
Kialbania Dëshmitarët e Jehovait
Kiarabu شهود يهوه
Kiarmenia Եհովայի Վկաներ
Kibulgaria Свидетелите на Йехова
Kikroatia Jehovini svjedoci
Kicheki svĕdkové Jehovovi
Kidenmark Jehovas Vidner
Kiholanzi Jehovah’s Getuigen
Kiingereza Jehovah’s Witnesses
Kiestonia Jehoova tunnistajad
Kifinland Jehovan todistajat
Kifaransa Témoins de Jéhovah
Kijerumani Jehovas Zeugen
Kigiriki Μάρτυρες του Ιεχωβά
Kiebrania עדי־יהוה
Kihungaria Jehova Tanúi
Kiiceland Vottar Jehóva
Kiitalia Testimoni di Geova
Kimakedonia, Kiserbia Јеховини сведоци
Kimalta Xhieda ta’ Jehovah
Kinorway Jehovas vitner
Kipoland Świadkowie Jehowy
Kireno Testemunhas de Jeová
Kirumania Martorii lui Iehova
Kirusi Свидетели Иеговы
Kislovaki Jehovovi svedkovia
Kislovenia Jehovove priče
Kihispania Testigos de Jehová
Kisweden Jehovas vittnen
Kituruki Yehova’nın Şahitleri
Kiukrainia Свідки Єгови
-
-
Ule Umati Mkubwa Kuishi Mbinguni? Au Duniani?Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
Sura ya 12
Ule Umati Mkubwa Kuishi Mbinguni? Au Duniani?
TOFAUTI na washiriki wa dini za Jumuiya ya Wakristo, walio wengi kati ya Mashahidi wa Yehova hutazamia uhai wa milele, si mbinguni, bali duniani. Kwa nini iko hivyo?
Haikuwa hivyo sikuzote. Wakristo wa karne ya kwanza walikuwa na taraja la kwamba baada ya wakati wangetawala pamoja na Yesu Kristo wakiwa wafalme wa kimbingu. (Mt. 11:12; Luka 22:28-30) Hata hivyo, Yesu alikuwa amewaambia kwamba warithi wa Ufalme wangekuwa “kundi dogo” tu. (Luka 12:32) Ni nani wangetiwa ndani? Wangekuwa wangapi? Hawakujifunza mambo yote madogomadogo mpaka baadaye.
Wakati wa Pentekoste 33 W.K., wanafunzi wa kwanza wa Yesu Wayahudi walitiwa mafuta kwa roho takatifu wawe warithi-washirika pamoja na Kristo. Katika mwaka 36 W.K., utendaji wa roho ya Mungu ulionyesha waziwazi kwamba watu Wasio-Wayahudi wasiotahiriwa wangeshiriki pia katika urithi huo. (Mdo. 15:7-9; Efe. 3:5, 6) Miaka mingine 60 ilipita kabla mtume Yohana hajafunuliwa kwamba ni 144,000 tu ambao wangechukuliwa kutoka duniani kushiriki Ufalme wa kimbingu pamoja na Kristo.—Ufu. 7:4-8; 14:1-3.
Charles Taze Russell na washirika wake walishiriki tumaini hilo, kama vile walio wengi kati ya Mashahidi wa Yehova kuteremka hadi miaka ya katikati ya 1930. Walijua pia, kutokana na funzo lao la Maandiko, kwamba kutiwa mafuta kwa roho takatifu hakukuonyesha tu kwamba watu walikuwa katika hali ya kupokea utumishi wa wakati ujao wakiwa wafalme na makuhani pamoja na Kristo mbinguni, bali pia kwamba walikuwa na kazi ya pekee ya kufanya wakati wangali katika mwili. (1 Pet. 1:3, 4; 2:9; Ufu. 20:6) Kazi gani? Walijua vizuri na mara nyingi walinukuu andiko la Isaya 61:1 ambalo hutaarifu hivi: “Roho ya Bwana MUNGU i juu yangu; kwa sababu BWANA amenitia mafuta, niwahubiri wanyenyekevu habari njema.”
Kuhubiri kwa Lengo Gani?
Ingawa walikuwa wachache kwa idadi, walijitahidi kuwasilisha kwa kila mtu kadiri ilivyowezekana kweli juu ya Mungu na kusudi lake. Walichapa na kugawanya kiasi kikubwa mno cha fasihi yenye kusimulia habari njema kuhusu uandalizi wake wa wokovu kupitia Kristo. Lakini lengo lao halikuwa hata kidogo kugeuza wale wote waliowahubiri. Basi, kwa nini waliwahubiri? Watch Tower la Julai 1889 lilifafanua hivi: “Sisi ni wawakilishi wake [Yehova] duniani; heshima ya jina lake lazima itetewe mbele ya adui zake na mbele ya wengi wa watoto wake waliodanganywa; mpango wake mtukufu lazima utangazwe kotekote kwa kupingana na mipango yote ya hekima ya kilimwengu ambayo wanadamu wanajaribu na wamekuwa wakijaribu kuvumbua.”
Fikira za pekee zilielekezwa kwa wale waliodai kuwa watu wa Bwana, ambao wengi wao walikuwa washiriki wa makanisa ya Jumuiya ya Wakristo. Lengo la kuwahubiria lilikuwa nini? Kama vile Ndugu Russell alivyoeleza mara nyingi, tamaa ya Wanafunzi wa Biblia wa mapema haikuwa kuvuta washiriki wa kanisa kwenye tengenezo jingine bali kuwasaidia wakaribie Bwana zaidi wakiwa washiriki wa lile kanisa moja la kweli. Hata hivyo, Wanafunzi wa Biblia walijua kwamba, katika kutii Ufunuo 18:4 (NW) lazima wao watoke katika “Babiloni,” ambaye walielewa kuwa amedhihirishwa katika kanisa la jina, makanisa ya Jumuiya ya Wakristo yakiwa na mafundisho na migawanyiko yao yote ya kimafarakano isiyo ya kimaandiko. Katika toleo lilelile la kwanza la Watch Tower (Julai 1879), Ndugu Russell alitaarifu hivi: “Sisi twaelewa kwamba lengo la kutoa ushahidi kwa sasa ni ‘Kutwaa watu kwa ajili ya jina Lake’—lile Kanisa—ambalo wakati wa kuja kwa Kristo litaunganishwa na Yeye, na kupokea jina Lake. Ufu. [3]. 12.”
Waling’amua kwamba, wakati ule, ni “mwito” mmoja tu uliokuwa ukitolewa kwa Wakristo wote wa kweli. Huo ulikuwa mwaliko wa kuwa washiriki wa bibi-arusi wa Kristo, ambaye hatimaye angekuwa na hesabu ya 144,000 tu. (Efe. 4:4; Ufu. 14:1-5) Walijitahidi kuwachochea wawe watendaji wale wote waliodai kuwa na imani katika dhabihu ya fidia ya Kristo, wawe walikuwa washiriki wa kanisa au la, ili wathamini “ahadi zenye bei na zilizo bora sana” za Mungu. (2 Pet. 1:4; Efe. 1:18, NW) Walijitahidi kuwachochea wawe na bidii katika kujipatanisha na matakwa ya kuwa kundi dogo la warithi wa Ufalme. Kwa ajili ya kuimarisha kiroho wote hao, ambao waliona kuwa washiriki wa “watu wa nyumba ya imani” (kwa sababu walidai kuwa na imani katika fidia), Ndugu Russell na washirika wake walijitahidi kwa bidii kufanya ‘chakula cha kiroho kwa wakati ufaao’ kipatikane kupitia safu za Watch Tower na vichapo vingine vyenye msingi wa Biblia.—Gal. 6:10; Mt. 24:45, 46, KJ.
Hata hivyo, wangeweza kuona kwamba si wote waliodai kuwa “wamejitakasa” (au, ‘kuwa wamejitoa wenyewe kikamili kwa Bwana,’ kama vile walivyolielewa kuwa lamaanisha) waliendelea baada ya hapo kufuatia maisha ya kujidhabihu kwa nia, wakifanya utumishi wa Bwana kuwa hangaiko lao la kwanza maishani. Hata hivyo, kama vile walivyoeleza, Wakristo waliojitakasa walikuwa wamekubali kuacha kwa nia asili yao ya kibinadamu, kwa kutazamia urithi wa kimbingu; hakukuwa cha kurudi nyuma; ikiwa hawakupata uhai katika makao ya kiroho, kifo cha pili kingewangoja. (Ebr. 6:4-6; 10:26-29) Lakini Wakristo wengi walioonekana kuwa wamejitakasa walikuwa wakichukua ile njia rahisi, wakishindwa kuonyesha bidii ya kweli kwa ajili ya kazi ya Bwana na wakiepuka kujidhabihu. Hata hivyo, kwa wazi hawakuwa wameikana fidia na walikuwa wakiishi maisha safi kadiri. Ingekuwaje kwa watu kama hao?
Kwa miaka mingi Wanafunzi wa Biblia walifikiri kwamba hicho ndicho kile kikundi kilichoelezwa kwenye Ufunuo 7:9, 14 (KJ), ambao hurejezea “halaiki kubwa” itokayo katika ile dhiki kubwa na kusimama “mbele ya kiti cha ufalme” cha Mungu na mbele za Mwana-Kondoo, Yesu Kristo. Walitoa sababu kwamba ijapokuwa hao huepuka maisha ya kujidhabihu, wangekabiliwa na majaribu ya imani yakimalizikia kwenye kifo wakati wa dhiki baada ya kutukuzwa kwa wale wa mwisho wa bibi-arusi wa Kristo. Waliamini kwamba ikiwa hao waliosemekana kuwa wa halaiki kubwa walikuwa waaminifu wakati huo, wangefufuliwa kwenye uhai wa kimbingu—si kutawala wakiwa wafalme bali ili kuchukua msimamo wao mbele ya kiti cha ufalme. Sababu ilitolewa kwamba wangepewa vyeo hivyo vya pili kwa sababu upendo wao kwa Bwana haukuwa umewaka vya kutosha, kwa sababu hawakuwa wameonyesha bidii ya kutosha. Ilifikiriwa kwamba wao walikuwa watu ambao walikuwa wamezaliwa kwa roho ya Mungu lakini walikuwa wamepuuza kumtii Mungu, labda wakiendelea kushikamana na makanisa ya Jumuiya ya Wakristo.
Pia walidhani kwamba labda—labda tu—wale “wakuu wa kale” ambao wangetumikia wakiwa wakuu duniani wakati wa enzi ya mileani, mwishoni mwa wakati huo, wangepewa kwa njia fulani uhai wa kimbingu. (Zab. 45:16) Walitoa sababu kwamba mataraja kama hayohayo huenda yangengoja wowote ambao “walijitakasa” baada ya warithi wa Ufalme wote 144,000 kuwa wamechaguliwa hatimaye lakini kabla ya wakati wa urudisho kuanza duniani. Kwa kadiri ndogo, hayo yalikuwa maoni yaliyotolewa katika Jumuiya ya Wakristo ya kwamba wale wote walio wema vya kutosha huenda mbinguni. Lakini kulikuwa imani ambayo Wanafunzi wa Biblia walithamini sana kutoka Maandiko ambayo iliwatenga na Jumuiya ya Wakristo yote. Ni ipi hiyo?
Kuishi Milele Duniani Katika Ukamilifu
Walitambua kwamba ingawa idadi ndogo iliyochukuliwa kutoka miongoni mwa wanadamu ingepewa uhai wa kimbingu, kungekuwa wengi zaidi ambao wangependelewa kwa kupewa uhai wa milele duniani, chini ya hali kama zile zilizokuwa zimekuwako katika Paradiso ya Edeni. Yesu alikuwa amefundisha wafuasi wake kusali hivi: “Mapenzi yako na yatendeke, kama ilivyo katika mbingu, pia juu ya dunia.” Pia alikuwa amesema hivi: “Wenye furaha ni wenye tabia-pole, kwa kuwa wao watairithi dunia.”—Mt. 5:5; 6:10, NW.
Kupatana na jambo hilo, chatia moja iliyotangazwa ikiwa nyongeza ya Watch Tower la Julai-Agosti 1881 ilionyesha kwamba kungekuwa wengi kutoka miongoni mwa wanadamu ambao wangepata upendeleo wa Mungu wakati wa Utawala wa Mileani wa Kristo na kwamba wangekuwa ndio “ulimwengu wa wanadamu walioinuliwa kwenye ukamilifu wa kibinadamu na uhai.” Chati hiyo ilitumiwa kwa miaka mingi ikiwa msingi wa hotuba kwa vikundi vikubwa na vidogo pia.
Watu wangeishi duniani chini ya hali gani wakati wa enzi hiyo ya mileani? The Watch Tower la Julai 1, 1912, lilieleza hivi: “Kabla ya dhambi kuingia ulimwenguni, uandalizi wa Kimungu kwa wazazi wetu wa kwanza ulikuwa Shamba la Edeni. Tufikiriapo hilo, acheni akili zetu zigeukie wakati ujao, zikiongozwa na Neno la Mungu; na kwa maono ya akilini twaona Paradiso iliyorudishwa—si bustani tu, bali dunia nzima imefanywa kuwa nzuri, yenye kuzaa matunda, isiyo na dhambi, yenye furaha. Halafu twakumbuka ile ahadi iliyopuliziwa tunayofahamu sana—‘Naye Mungu atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena,’ kwa kuwa mambo ya kwanza ya dhambi na kifo yatakuwa yamepitilia mbali, na vitu vyote vitakuwa vimefanywa kuwa vipya!—Ufu. 21:4, 5.”
Ni Nani Wangeishi Milele Duniani?
Hakukuwa na wazo upande wa Ndugu Russell kwamba Mungu alikuwa akitolea wanadamu uchaguzi—uhai wa kimbingu kwa wale walioutaka na uhai katika paradiso ya dunia kwa wale waliofikiri wangependelea huo. Watch Tower la Septemba 15, 1905, lilitaja wazi hivi: “Hisia zetu au tamaa zetu zenye nguvu si ndizo mwito. Ama sivyo ingedokeza kwamba twajitolea mwito sisi wenyewe. Akisema juu ya ukuhani wetu, yule Mtume hujulisha, ‘Hapana mtu ajitwaliaye heshima hii, ila yeye aitwaye na Mungu,’ (Ebr. 5:4), na mahali pa kuhakikisha mwito wa Mungu si katika hisia zetu bali katika Neno la Mungu mwenyewe la ufunuo.”
Kwa habari ya fursa ya kuishi katika paradiso ya dunia iliyorudishwa, Wanafunzi wa Biblia waliamini kwamba hiyo ingetolewa kwa watu baada tu ya kundi dogo lote kuwa limepokea thawabu yalo na ile enzi ya mileani kuwa imeletwa kwa ukamili. Huo, walielewa, ungekuwa ndio wakati wa “urudisho wa vitu vyote,” kama ulivyorejezewa kwenye Matendo 3:21. (KJ) Hata wafu wangeinuliwa wakati huo ili wote waweze kushiriki katika uandalizi huo wa upendo. Ndugu walikuwa wakiona jamii yote ya kibinadamu (isipokuwa wale waliokuwa wameitwa kwenye uhai wa kimbingu) ikipewa fursa yao wakati huo ya kuchagua uhai. Kama walivyoelewa, huo ungekuwa ndio wakati ambao Kristo, akiwa katika kiti chake cha ufalme cha kimbingu, angebagua watu, mmoja kutoka kwa mwingine, kama mchungaji abaguavyo kondoo na mbuzi. (Mt. 25:31-46) Wale watiifu, wawe wamezaliwa wakiwa Wayahudi au Wasio-Wayahudi, wangethibitika kuwa “kondoo wengine” wa Bwana.—Yn. 10:16, NW.b
Baada ya Nyakati za Mataifa kukoma, walifikiri kwamba wakati wa urudisho ulikuwa karibu sana; hivyo kutoka 1918 mpaka 1925, walipiga mbiu: “Mamilioni wanaoishi sasa hawatakufa kamwe.” Ndiyo, walielewa kwamba watu walioishi wakati ule—wanadamu kwa ujumla—walikuwa na fursa ya kuokoka na kuingia moja kwa moja katika wakati wa urudisho na kwamba wakati huo wangeelimishwa katika matakwa ya Yehova ya uhai. Wakitii, wangefikia hatua kwa hatua ukamilifu wa kibinadamu. Wakiasi, baada ya wakati, wangeharibiwa milele.
Wakati wa miaka hiyo ya mapema, ndugu hawakuwa na wazo lolote kwamba ujumbe wa Ufalme ungepigiwa mbiu kwa kadiri kubwa sana na kwa miaka mingi kama vile imekuwa. Lakini waliendelea kuchunguza Maandiko na kujitahidi kuitikia yale ambayo hayo yalionyesha kuwa ndiyo kazi ambayo Mungu alitaka wafanye.
“Kondoo” Kwenye Mkono wa Kuume wa Kristo
Hatua ya maana kwelikweli katika kuelewa kusudi la Yehova ilitegemea kielezi cha Yesu cha kondoo na mbuzi, kwenye Mathayo 25:31-46. (NW) Katika kielezi hicho Yesu alisema hivi: “Wakati Mwana wa binadamu awasilipo katika utukufu wake, na malaika wote pamoja naye, ndipo atakapoketi juu ya kiti chake cha ufalme chenye utukufu. Na mataifa yote yatakusanywa mbele yake, naye atatenganisha watu mmoja na mwenzake, kama vile mchungaji atenganishavyo kondoo na mbuzi. Naye atawaweka kondoo kwenye mkono wake wa kuume, lakini mbuzi kwenye mkono wake wa kushoto.” Kama vile kielezi hicho kiendeleavyo kuonyesha, “kondoo” ni wale ambao husaidia “ndugu” za Kristo, hata kutafuta kuwaletea kitulizo wanaponyanyaswa na kuwa gerezani.
Kwa muda mrefu ilikuwa imefikiriwa kwamba kielezi hicho kilihusu wakati wa enzi ya mileani, wakati wa rudisho, na kwamba hukumu ya mwisho irejezewayo katika kielezi hicho ilikuwa ile ambayo ingetukia mwishoni mwa Mileani. Lakini katika 1923, sababu za kuwa na maoni mengine ya mambo zilionyeshwa na J. F. Rutherford, msimamizi wa Watch Tower Society, katika hotuba yenye kuelimisha katika Los Angeles, California. Hiyo ilitangazwa baadaye mwaka huo katika toleo la Oktoba 15 la The Watch Tower.
Ilipokuwa ikizungumzia wakati ambapo kielezi hicho cha kiunabii kingetimizwa, makala hiyo ilionyesha kwamba Yesu alikitia kikiwa sehemu ya jibu lake kwa ombi la ‘ishara ya kuwapo kwake na ya umalizio wa mfumo wa mambo.’ (Mt. 24:3, NW) Makala hiyo ilieleza sababu “ndugu” warejezewao katika kielezi hicho hawangeweza kuwa Wayahudi wa enzi ya Gospeli wala wanadamu ambao huonyesha imani wakati wa pindi ya mileani ya kutahini na kuhukumu bali lazima wawe wale ambao ni warithi pamoja na Kristo wa Ufalme wa kimbingu, ndiyo sababu inayofanya utimizo wa kielezi hicho lazima uwe wakati ambapo baadhi ya warithi-washirika wa Kristo wangali katika mwili wenye nyama.—Linganisha Waebrania 2:10, 11.
Yaliyowapata ndugu hao watiwa-mafuta wa Kristo walipokuwa wakijitahidi kutoa ushahidi kwa makasisi na kwa watu wa kawaida wanaoshirikiana na makanisa ya Jumuiya ya Wakristo yalionyesha pia kwamba unabii uliotiwa katika kielezi cha Yesu ulikuwa tayari ukitimizwa. Jinsi gani hivyo? Itikio la wengi kati ya makasisi na washiriki mashuhuri wa makanisa yao lilikuwa lenye uhasama—hawakuwapa kikombe cha maji yenye kuburudisha, ama kihalisi ama kitamathali; badala ya hivyo, baadhi yao walichochea wafanyaghasia wararue mavazi ya ndugu hao na kuwapiga, au walidai kwamba wakuu wawatie gerezani. (Mt. 25:41-43) Kwa kutofautisha, washiriki wengi wanyenyekevu wa kanisa walipokea ujumbe wa Ufalme kwa nderemo, wakawatolea kiburudisho wale waliouleta, na kufanya yale waliyoweza ili kuwasaidia hata wakati watiwa-mafuta walipotiwa gerezani kwa ajili ya habari njema.—Mt. 25:34-36.
Kwa kadiri Wanafunzi wa Biblia wangeweza kuona, wale ambao Yesu alisema habari yao kuwa kondoo walikuwa wangali katika makanisa ya Jumuiya ya Wakristo. Walitoa sababu kwamba hao walikuwa watu ambao hawakudai kuwa wamejitakasa lakini walikuwa na staha kubwa kwa Yesu Kristo na kwa watu wake. Hata hivyo, je, wangeweza kubaki katika makanisa?
Kuchukua Msimamo Imara kwa Ajili ya Ibada Safi
Funzo la kitabu cha kiunabii cha Biblia cha Ezekieli lilitoa nuru juu ya jambo hilo. La kwanza la mabuku matatu ya maelezo yenye kichwa Vindication lilitangazwa katika 1931. Lilieleza umaana wa yale ambayo Ezekieli aliandika juu ya hasira ya Yehova dhidi ya Yuda na Yerusalemu la kale lenye kuasi imani. Ijapokuwa watu wa Yuda walidai kutumikia Mungu aishiye wa kweli, walikubali sherehe za kidini za mataifa yaliyowazunguka, wakatolea uvumba sanamu zisizo na uhai, na kwa ukosefu wa adili wakaweka tumaini lao katika miungano ya kisiasa, badala ya kuonyesha imani katika Yehova. (Eze. 8:5-18; 16:26, 28, 29; 20:32) Katika yote hayo, walikuwa barabara kama Jumuiya ya Wakristo; hivyo, kwa upatani, Yehova angetekeleza hukumu juu ya Jumuiya ya Wakristo kama vile alivyofanya juu ya Yuda na Yerusalemu lisilo jaminifu. Lakini sura ya 9 ya Ezekieli huonyesha kwamba kabla ya kutekelezwa kwa hukumu ya kimungu, baadhi ya watu wangetiwa alama kwa ajili ya kuhifadhiwa. Ni nani hao?
Unabii huo husema kwamba hao waliotiwa alama wangekuwa ‘wakiugua na kulia kwa sababu ya machukizo yote yanayofanyika’ katikati ya Jumuiya ya Wakristo, au Yerusalemu la ufananisho. (Eze. 9:4) Hakika, basi, hawangekuwa wakishiriki kimakusudi katika machukizo hayo. Kwa hiyo buku la kwanza la Vindication lilitambulisha hao wenye alama kuwa watu ambao hukataa kuwa sehemu ya matengenezo ya makanisa ya Jumuiya ya Wakristo na ambao kwa njia fulani huchukua msimamo wao upande wa Bwana.
Habari hiyo ilifuatiliwa katika 1932 na mazungumzo ya maandishi ya Biblia kuhusu Yehu na Yonadabu na maana yayo ya kiunabii. Yehu alipewa utume na Yehova awe mfalme juu ya ule ufalme wa makabila kumi ya Israeli na kutekeleza hukumu ya Yehova juu ya nyumba ya Ahabu na Yezebeli yenye uovu. Yehu alipokuwa njiani kwenda Samaria kung’oa ibada ya Baali, Yehonadabu (Yonadabu), mwana wa Rekabu, alitoka kumlaki. Yehu alimuuliza Yehonadabu: “Je, moyo wako umenyoka, kama moyo wangu ulivyo?” naye Yehonadabu akajibu: “Ndio.” “Nipe mkono wako,” Yehu akamwalika, akampandisha Yehonadabu juu ya gari lake. Kisha Yehu akahimiza: “Fuatana nami, ukaone wivu wangu kwa BWANA.” (2 Fal. 10:15-28) Yehonadabu, ingawa hakuwa Mwisraeli, alikubaliana na yale ambayo Yehu alikuwa akifanya; yeye alijua kwamba Yehova, Mungu wa kweli, apasa kupewa ujitoaji usiotia ndani wengine. (Kut. 20:4, 5) Karne nyingi baadaye, wazao wa Yehonadabu walikuwa wangali wakionyesha roho ambayo Yehova alikubali, hivyo Yeye akaahidi: “Yonadabu, mwana wa Rekabu, hatakosa kuwa na mtu wa kusimama mbele zangu hata milele.” (Yer. 35:19) Hivyo swali likazuka, Je, kuna watu duniani leo ambao si Waisraeli wa kiroho wenye urithi wa kimbingu lakini ambao ni kama Yehonadabu?
Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) la Agosti 1, 1932, lilieleza hivi: “Yehonadabu aliwakilisha au alifananisha ile jamii ya watu iliyo duniani sasa . . . [ambao] hawapatani na tengenezo la Shetani, ambao huchukua msimamo wao upande wa uadilifu, na ndio ambao Bwana atahifadhi wakati wa Har–Magedoni, awapitishe taabu hiyo, na kuwapa uhai wa milele duniani. Hao ndio walijumuika kuwa jamii ya ‘kondoo’ ambao huwapendelea watu wa Mungu waliotiwa mafuta kwa roho, kwa sababu wao wajua kwamba watiwa-mafuta kwa roho wa Bwana wanafanya kazi ya Bwana.” Wale waonyeshao roho kama hiyo walialikwa wawe na ushiriki katika kupeleka ujumbe wa Ufalme kwa wengine kama vile watiwa-mafuta walivyokuwa wakifanya.—Ufu. 22:17.
Kulikuwa na wengine (ingawa wachache wakati ule) waliokuwa wakishirikiana na Mashahidi wa Yehova waliong’amua kwamba roho ya Mungu haikuwa imetia ndani yao tumaini la uhai wa kimbingu. Wakaja kujulikana kuwa Wayonadabu, kwa kuwa, kama vile Yonadabu (Yehonadabu) wa kale, walilihesabu kuwa pendeleo kutambulishwa pamoja na watumishi wa Yehova watiwa-mafuta, na walifurahia kushiriki katika mapendeleo ambayo Neno la Mungu liliwaelekeza kwayo. Je, watu hao waliokuwa na matarajio ya kutokufa kamwe wangekuwa wengi kabla ya Har–Magedoni? Je, iliwezekana, kama ilivyokuwa imesemwa, kwamba idadi yao ingefika mamilioni?
Ule “Umati Mkubwa”—Wao Ni Nani?
Tangazo lilipotolewa juu ya mipango ya Mashahidi wa Yehova kuwa na mkusanyiko katika Washington, D.C., tokea Mei 30 hadi Juni 3, 1935, Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) lilisema hivi: “Kufikia sasa si Wayonadabu wengi ambao wamekuwa na pendeleo la kuhudhuria mkusanyiko, na mkusanyiko huko Washington huenda ukawa faraja na manufaa halisi kwao.” Hakika ilithibitika kuwa kweli.
Kwenye mkusanyiko huo fikira ya pekee ilitolewa kwenye Ufunuo 7:9, 10 (NW) ambalo husomeka hivi: “Baada ya mambo haya nikaona, na, tazama! umati mkubwa, ambao hakuna mtu aliyeweza kuuhesabu, kutoka katika mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha, wamesimama mbele ya kiti cha ufalme na mbele ya Mwana-Kondoo, wamevaa kanzu nyeupe; na kulikuwa na matawi ya mitende mikononi mwao. Nao wafuliza kulia kwa sauti kubwa, wakisema: ‘Sisi tunawiwa wokovu na Mungu wetu, aketiye juu ya hicho kiti cha ufalme, na kwa Mwana-Kondoo.’” Ni nani wanaojumuika kuwa huo umati mkubwa, au “halaiki kubwa”?—KJ.
Kwa miaka mingi, hata kufikia 1935, hawakueleweka kuwa walewale kondoo katika kielezi cha Yesu cha kondoo na mbuzi. Kama ilivyokwisha kutajwa, ilifikiriwa kwamba walikuwa jamii ya pili ya kimbingu—ya pili kwa sababu walikuwa wamepuuza kutii Mungu.
Hata hivyo, maoni hayo yalizusha maswali yenye kuendelea. Baadhi yayo yalizungumzwa mapema katika 1935 wakati wa chakula cha mchana kwenye makao makuu ya Watch Tower Society. Wengine miongoni mwa wale waliotoa maelezo yao wakati huo walidokeza kwamba halaiki kubwa ilikuwa jamii ya kidunia. Grant Suiter, ambaye baadaye alipata kuwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alikumbuka hivi: “Kwenye funzo moja la Betheli, lililoongozwa na Ndugu T. J. Sullivan, niliuliza hivi: ‘Kwa kuwa halaiki kubwa hupata uhai wa milele, je, hao ambao hujumuika kuwa wa kikundi hicho hushika uaminifu-maadili?’ Kulikuwa na maelezo mengi lakini hakukuwa na jibu lenye kueleza dhahiri.” Basi, Ijumaa, Mei 31, 1935, kwenye mkusanyiko wa Washington, D.C., jibu lenye kuridhisha lilitolewa. Ndugu Suiter alikuwa ameketi kwenye roshani akitazama chini juu ya mkutano huo, na jinsi alivyosisimuka hotuba hiyo ilipokuwa ikifunuka!
Muda mfupi baada ya mkusanyiko huo, Mnara wa Mlinzi, katika matoleo yalo ya Agosti 1 na 15, 1935, lilitangaza yale yaliyosemwa katika hotuba hiyo. Lilitaja kwamba jambo la maana katika kuelewa mambo ifaavyo ni kuthamini uhakika wa kwamba kusudi kuu la Yehova si kuokolewa kwa wanadamu bali kutetewa kwa jina lake mwenyewe (au, kama vile tungesema sasa, kuondolewa lawama kwa enzi kuu yake). Hivyo kibali cha Yehova ki juu ya wale washikao uaminifu-maadili kwake; yeye hathawabishi wale ambao hukubali kufanya mapenzi yake kisha wakaleta suto juu ya jina lake kwa kuridhiana na tengenezo la Ibilisi. Takwa hilo la uaminifu latumika kwa wote ambao wangepata kibali cha Mungu.
Kupatana na jambo hilo, Mnara wa Mlinzi lilisema: “Ufunuo 7:15 ndio kwa kweli ufunguo wa kutambulisha halaiki kubwa. . . . Elezo hilo la Ufunuo juu ya halaiki kubwa ni kwamba ‘wako mbele ya kiti cha ufalme cha Mungu, nao humtumikia yeye waziwazi’ . . . Wao huona na kuelewa na kutii maneno ya Yesu, Mwana-Kondoo wa Mungu, akisema kwao: ‘Msujudie Bwana Mungu wako, umtumikie yeye peke yake’; maneno ambayo huhusu viumbe vyote ambavyo Yehova hukubali.” (Mt. 4:10) Kwa hiyo, yale ambayo Biblia husema juu ya halaiki kubwa, au umati mkubwa, hayangeweza kwa kufaa kueleweka kuwa na maana ya kwamba yanatoa wokovu kwa ajili ya watu ambao hudai kumpenda Mungu lakini ambao hawakujali kufanya mapenzi yake.
Basi, je, umati mkubwa ni jamii ya kimbingu? Mnara wa Mlinzi lilionyesha kwamba lugha ya maandiko haikuelekeza kwenye mkataa kama huo. Kwa habari ya mahali pao “mbele ya kiti cha ufalme,” lilionyesha kwamba Mathayo 25:31, 32 (NW) husimulia juu ya mataifa yote yakikusanywa mbele ya kiti cha ufalme cha Kristo, hata hivyo mataifa hayo yako duniani. Hata hivyo, umati mkubwa ‘umesimama’ mbele ya kiti cha ufalme kwa sababu una kibali cha Yeye aketiye juu ya kiti cha ufalme.—Linganisha Yeremia 35:19.
Lakini kingekuwa wapi kikundi kama hicho—watu “wa mataifa yote,” watu ambao hawakuwa sehemu ya Israeli wa kiroho (walioelezwa mapema kidogo, katika Ufunuo 7:4-8), watu waliokuwa na imani katika fidia (wakiwa wameosha kitamathali mavazi yao katika damu ya Mwana-Kondoo), watu walioshangilia Kristo kuwa Mfalme (wakiwa na matawi ya mitende mikononi mwao, kama ule umati uliolaki Yesu akiwa Mfalme alipoingia Yerusalemu), watu waliokuwa wakijitoa kikweli mbele ya kiti cha ufalme cha Yehova ili kumtumikia? Je, kulikuwa na kikundi kama hicho cha watu duniani?
Katika kutimiza neno lake mwenyewe la kiunabii, Yehova mwenyewe aliandaa jibu. Webster Roe, aliyehudhuria mkusanyiko wa Washington, alikumbuka kwamba kwenye upeo wa hotuba yake, Ndugu Rutherford aliuliza hivi: “Wale wote wenye tumaini la kuishi milele duniani simameni tafadhali.” Kulingana na Ndugu Roe, “zaidi ya nusu ya wasikilizaji walisimama.” Kupatana na hilo, Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) la Agosti 15, 1935, lilitaarifu hivi: “Sasa twaona kikundi ambacho chafaana kabisa na elezo lililotolewa katika Ufunuo saba kuhusu halaiki kubwa. Wakati wa miaka michache iliyopita, na katika wakati ambao ‘injili hii ya ufalme inahubiriwa kuwa ushahidi,’ kumetokea idadi kubwa (na wangali wanakuja) ambayo wakiri Bwana Yesu kuwa Mwokozi wao na Yehova kuwa Mungu wao, ambaye wanaabudu katika roho na katika kweli na kutumikia kwa shangwe. Kwa maneno mengine hao huitwa ‘Wayonadabu.’ Hao wanabatizwa katika ufananisho, wakionyesha kwa njia hiyo kwamba wao . . . wamechukua msimamo wao upande wa Yehova nao wamtumikia yeye na Mfalme wake.”
Wakati huo ilionwa kwamba umati mkubwa wa Ufunuo 7:9, 10 umo miongoni mwa “kondoo wengine” ambao Yesu alirejezea (Yn. 10:16); wao ndio huja kusaidia “ndugu” za Kristo (Mt. 25:33-40); ndio watu waliotiwa alama kwa ajili ya kuokoka kwa sababu ya kuchukizwa na machukizo yanayofanywa katika Jumuiya ya Wakristo nao huyaepuka (Eze. 9:4); wako kama Yehonadabu, ambaye alijitambulisha waziwazi pamoja na mtumishi wa Yehova mtiwa-mafuta katika kutekeleza utume wake aliopewa na Mungu (2 Fal. 10:15, 16). Mashahidi wa Yehova waelewa kwamba hao ni watumishi wenye uaminifu-mshikamanifu wa Mungu ambao wataokoka Har–Magedoni wakiwa na taraja la kuishi milele katika dunia iliyorudishwa kwenye hali za Paradiso.
Kazi Yenye Uharaka ya Kufanywa
Kuelewa kwao maandiko hayo kulikuwa na matokeo makubwa juu ya utendaji wa watumishi wa Yehova. Walitambua kwamba si wao wangeteua na kukusanya washiriki wa umati mkubwa; haikuwa juu yao kuambia watu kama tumaini lao lapaswa kuwa la kimbingu au la kidunia. Bwana angeelekeza mambo kupatana na mapenzi yake. Lakini wakiwa Mashahidi wa Yehova, walikuwa na daraka zito. Walipaswa kutumikia wakiwa wapiga-mbiu wa Neno la Mungu, wakishiriki kweli ambazo Yeye aliwawezesha kuelewa, ili watu waweze kujua juu ya maandalizi ya Yehova na wawe na fursa ya kuyaitikia kwa uthamini.
Zaidi ya hilo, walitambua kwamba kulikuwa na uharaka mkubwa katika kazi yao. Katika mfululizo wa makala zenye kichwa “Kukusanya Ile Halaiki,” zilizotangazwa katika 1936, Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) lilieleza hivi: “Maandiko yanaunga mkono kwa nguvu mkataa wa kwamba kwenye Har–Magedoni Yehova ataharibu watu wa dunia, akiokoa wale tu watiio amri zake za kusimama upande wa tengenezo lake. Katika nyakati zilizopita mamilioni ya mamilioni ya watu wamekwenda kaburini bila kusikia hata kidogo juu ya Mungu na Kristo, na hao kwa wakati uliowekwa lazima waamshwe kutoka kifo na kupewa maarifa ya ukweli, ili wafanye uchaguzi. Hata hivyo, hali ni tofauti, kuhusu watu walioko duniani sasa. . . . Wale wa umati mkubwa lazima wapokee ujumbe wa gospeli kabla ya siku ya vita ya siku ile kuu ya Mungu Mweza Yote ambayo ni Har–Magedoni. Ile halaiki kubwa isipopewa sasa ujumbe kuhusu kweli, itakuwa ni kuchelewa mno wakati kazi ya kuchinja ianzapo.”—Ona 2 Wafalme 10:25; Ezekieli 9:5-10; Sefania 2:1-3; Mathayo 24:21; 25:46.
Kama tokeo la uelewevu huo wa Maandiko, Mashahidi wa Yehova walitiwa bidii mpya kwa ajili ya kazi ya kutoa ushahidi. Leo Kallio, ambaye baadaye alitumikia akiwa mwangalizi asafiriye katika Finland, alisema hivi: “Siwezi kukumbuka wakati uwao wote uliopita nikipata shangwe na bidii kama hiyo, wala siwezi kukumbuka wakati uwao wote nikiendesha baiskeli yangu kwa kasi kama katika siku hizo, nilipoharakisha kuletea wenye kupendezwa habari njema kwamba kwa sababu ya fadhili zisizostahiliwa za Yehova, walipewa toleo la uhai wa milele duniani.”
Wakati wa miaka mitano iliyofuata, idadi ya Mashahidi wa Yehova ilipokuwa ikikua, idadi ya wale walioshiriki mifano kwenye Ukumbusho wa kila mwaka wa kifo cha Kristo ilipungua hatua kwa hatua. Hata hivyo, mmiminiko wa umati mkubwa haukuwa wa haraka kama vile Ndugu Rutherford alivyokuwa ametarajia. Wakati mmoja hata alimwambia Fred Franz, ambaye alikuja kuwa msimamizi wa nne wa Sosaiti: “Inaonekana kama kwamba ‘halaiki kubwa’ haitakuwa kubwa sana hata hivyo.” Lakini tangu hapo, idadi ya Mashahidi wa Yehova imevuvumuka kufikia mamilioni, hali, kwa ujumla, idadi ya wale wanaotarajia urithi wa kimbingu imeendelea kupungua.
Kundi Moja Chini ya Mchungaji Mmoja
Hakuna ushindani kati ya jamii ya watiwa-mafuta na umati mkubwa. Wale walio na tumaini la kimbingu hawadharau wale wanaotarajia kwa hamu kupokea uhai wa milele katika paradiso ya dunia. Kila mmoja wao hupokea kwa shukrani mapendeleo yanayotolewa na Mungu, bila kutoa sababu kwamba kwa njia fulani cheo chake humfanya kuwa mtu bora zaidi au kwa njia fulani mtu wa hali ya chini zaidi ya mwingine. (Mt. 11:11; 1 Kor. 4:7) Kama Yesu alivyotabiri, vikundi vyote viwili vimekuwa kwelikweli “kundi moja,” vikitumikia chini yake akiwa “mchungaji mmoja” wao.—Yn. 10:16.
Hisia walizo nazo ndugu watiwa-mafuta wa Kristo kuelekea waandamani wao wa umati mkubwa zinaonyeshwa vizuri katika kitabu Usalama Ulimwenguni Pote Chini ya “Mwana-Mfalme wa Amani”: “Tangu Vita ya Ulimwengu ya Pili, utimizo wa unabii wa Yesu kwa ‘umalizio wa mfumo wa mambo’ kwa sehemu kubwa ni kwa sababu ya daraka linalotimizwa na ule ‘umati mkubwa’ wa ‘kondoo wengine.’ Ule mwangaza kutoka taa zilizowashwa za mabaki umeangaza macho ya mioyo yao, nao wamesaidiwa kuonyesha nuru kwa wengine ambao wangali wamo katika giza la ulimwengu huu. . . . Wamekuja kuwa wenzi wasioweza kutenganishwa wa mabaki ya ile jamii ya bibi-arusi. . . . Kwa hiyo, shukrani nyingi sana, kwa ule ‘umati mkubwa’ wa kimataifa, wenye kusema lugha nyingi kwa sababu ya sehemu kubwa ambayo umeshiriki katika kutimiza unabii wa yule Bwana-arusi kwenye Mathayo 24:14!”
Hata hivyo, kadiri Mashahidi wa Yehova, kutia na ule umati mkubwa, wameshiriki kwa umoja katika kupiga mbiu ya zile habari njema tukufu za Ufalme wa Mungu, ndivyo umma umekuja kuwatambua kwa sababu ya jambo jingine zaidi ya kazi yao ya kutoa ushahidi kwa bidii.
[Maelezo ya Chini]
a Hiyo “Chati ya Enzi” ilitokezwa tena katika kitabu The Divine Plan of the Ages.
b Zion’s Watch Tower, Machi 15, 1905, kur. 88-91.
[Blabu katika ukurasa wa 159]
Walio wengi kati ya Mashahidi wa Yehova hutazamia uhai wa milele duniani
[Blabu katika ukurasa wa 161]
Imani iliyowatenga na Jumuiya ya Wakristo yote
[Blabu katika ukurasa wa 164]
Wakati wa utimizo wa kielezi cha kondoo na mbuzi
[Blabu katika ukurasa wa 165]
Wakaja kujulikana kuwa Wayonadabu
[Blabu katika ukurasa wa 166]
Mei 31, 1935, ile “halaiki kubwa” ilitambulishwa waziwazi
[Blabu katika ukurasa wa 170]
Tumaini la kimbingu au la kidunia—ni nani aliamuaye?
[Sanduku katika ukurasa wa 160]
Wakati wa Uelewevu
Zaidi ya miaka 250 iliyopita, Sir Isaac Newton aliandika jambo lenye kupendeza juu ya kuelewa unabii, kutia ndani na ule unaohusu “umati mkubwa” wa Ufunuo 7:9, 10. (“NW”) Katika kitabu chake “Observation Upon the Prophecies of Daniel, and the Apocalypse of St. John,” kilichotangazwa katika 1733, yeye alitaarifu hivi: “Unabii huu mbalimbali wa Danieli na Yohana haupaswi kueleweka mpaka wakati wa mwisho: lakini wengine wapaswa kutoa unabii kutokana nao katika hali ya kutaabika na yenye huzuni kwa muda mrefu, na kufanya hivyo kwa gizagiza, ili kugeuza wachache tu. . . . Halafu, asema Danieli, wengi wataenda huko na huko, na maarifa yataongezeka. Kwa kuwa lazima Gospeli ihubiriwe katika mataifa yote kabla ya dhiki kubwa, na mwisho wa ulimwengu. Ule umati wenye kubeba matawi ya mitende, ambao hutoka katika hiyo dhiki kubwa, hauwezi kuwa usiohesabika kutoka mataifa yote, wasipofanywa hivyo kwa kuhubiriwa Gospeli kabla haijaja.”
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 168]
Dunia, Makao ya Milele ya Mwanadamu
Ni nini lililokuwa kusudi la awali la Mungu kwa wanadamu?
“Mungu akawabarikia, Mungu akawaambia, Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi, na kuitiisha; mkatawale samaki wa baharini, na ndege wa angani, na kila kiumbe chenye uhai kiendacho juu ya nchi.”—Mwa. 1:28.
Je, kusudi la Mungu kwa habari ya dunia limebadilika?
“Neno langu . . . halitanirudia bure, bali litatimiza mapenzi yangu, nalo litafanikiwa katika mambo yale niliyolituma.”—Isa. 55:11.
“BWANA, aliyeziumba mbingu, asema hivi; Yeye ni Mungu; ndiye aliyeiumba dunia na kuifanya; ndiye aliyeifanya imara; hakuiumba ukiwa, aliiumba ili ikaliwe na watu; Mimi ni BWANA, wala hapana mwingine.”—Isa. 45:18.
“Basi, nyinyi lazima msali kwa njia hii: ‘Baba yetu uliye katika mbingu, jina lako na litakaswe. Acha Ufalme wako uje. Mapenzi yako na yatendeke, kama ilivyo katika mbingu, pia juu ya dunia.”—Mt. 6:9, 10, “NW.”
“Watenda mabaya wataharibiwa, bali wamngojao BWANA ndio watakaoirithi nchi. Wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele.”—Zab. 37:9, 29.
Ni hali gani zitakazokuwako duniani chini ya Ufalme wa Mungu?
“Lakini ziko mbingu mpya na dunia mpya ambazo tunangojea kulingana na ahadi yake, na katika hizo uadilifu utakaa.”—2 Pet. 3:13, “NW.”
“Taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe. Bali wataketi kila mtu chini ya mzabibu wake, na chini ya mtini wake; wala hapana mtu atakayewatia hofu; kwa kuwa kinywa cha BWANA wa majeshi kimesema hivi.”—Mika 4:3, 4.
“Nao watajenga nyumba, na kukaa ndani yake; watapanda mizabibu, na kula matunda yake. Hawatajenga, akakaa mtu mwingine ndani yake; hawatapanda, akala mtu mwingine; maana kama siku za mti ndivyo zitakavyokuwa siku za watu wangu, na wateule wangu wataifurahia kazi ya mikono yao muda wa siku nyingi.”—Isa. 65:21, 22.
“Hapana mwenyeji atakayesema, Mimi mgonjwa.”—Isa. 33:24.
“Na Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”—Ufu. 21:3, 4, “NW”; ona pia Yohana 3:16.
“Ni nani ambaye kwa kweli hatakuhofu wewe, Yehova, na kulitukuza jina lako, kwa sababu wewe peke yako ni mwaminifu-mshikamanifu? Kwa maana mataifa yote yatakuja na kuabudu mbele yako, kwa sababu maagizo yako ya uadilifu yamefanywa kuwa dhahiri.”—Ufu. 15:4, “NW.”
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 169]
Wale Waendao Mbinguni
Ni wanadamu wangapi ambao wataenda mbinguni?
“Msiwe na hofu, kundi dogo, kwa sababu Baba yenu amekubali kuwapa nyinyi ufalme.”—Luka 12:32, “NW.”
“Nami nikaona, na, tazama! Mwana-Kondoo [Yesu Kristo] amesimama juu ya Mlima Zayoni [wa kimbingu], na pamoja naye mia arobaini na nne elfu wakiwa na jina lake na jina la Baba yake limeandikwa juu ya vipaji vya nyuso zao. Nao wanaimba kama kwamba wimbo mpya mbele ya hicho kiti cha ufalme na mbele ya viumbe hai wanne na wazee; na hakuna yeyote aliyeweza kuwa bingwa wa ule wimbo ila mia arobaini na nne elfu, ambao wamenunuliwa kutoka katika dunia.”—Ufu. 14:1, 3, “NW.”
Je, hao 144,000 wote ni Wayahudi?
“Hakuna Myahudi wala Mgiriki, hakuna mtumwa wala mtu huru, hakuna wa kiume wala wa kike; kwa maana nyinyi nyote ni mtu mmoja katika muungano na Kristo Yesu. Zaidi ya hayo, ikiwa nyinyi ni wa Kristo, kwa kweli nyinyi ni mbegu ya Abrahamu, warithi kuhusiana na ahadi.”—Gal. 3:28, 29, “NW.”
“Yeye si Myahudi aliye hivyo kwa nje, wala tohara si ile ambayo ni ya nje juu ya mwili. Bali yeye ni Myahudi aliye hivyo kwa ndani, na tohara yake ni ile ya moyo kwa roho, wala si kwa mfumo fulani wa sheria iliyoandikwa.”—Rum. 2:28, 29, “NW.”
Kwa nini Mungu achukua wengine kwenda mbinguni?
“Watakuwa makuhani wa Mungu na wa Kristo, na watatawala wakiwa wafalme pamoja naye kwa miaka elfu.”—Ufu. 20:6, “NW.”
[Sanduku/Grafu katika ukurasa wa 171]
Ripoti ya Ukumbusho
Katika muda wa miaka 25, hudhurio la Ukumbusho likawa zaidi ya mara 100 ya idadi ya wenye kushiriki
[Grafu]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
Wenye Kushiriki
Hudhurio
1,500,000
1,250,000
1,000,000
750,000
500,000
250,000
1935 1940 1945 1950 1955 1960
[Picha katika ukurasa wa 167]
Kwenye mkusanyiko wa Washington, D.C., watu 840 walibatizwa
-
-
Twatambuliwa kwa Mwenendo WetuMashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
Sura ya 13
Twatambuliwa kwa Mwenendo Wetu
TWAISHI katika enzi ambayo viwango vya adili vilivyostahiwa kwa muda mrefu vimetupiliwa mbali na sehemu kubwa ya wanadamu. Dini zilizo nyingi za Jumuiya ya Wakristo zimefanya ivyo hivyo, ama kwa sababu ya uvumiliano ama kwa kutoa hoja kwamba nyakati ni tofauti na miiko ya vizazi vya mapema zaidi haitumiki tena. Kama tokeo, Samuel Miller, mkuu wa Masomo ya Kidini katika Chuo Kikuu cha Harvard, alisema hivi: “Kanisa halina makali. Limekubali utamaduni wa wakati wetu na kuufuata.” Athari katika maisha za wale ambao walitegemea makanisa hayo wapate mwongozo imekuwa yenye kuharibu sana.
Kinyume cha hilo, lilipokuwa likizungumza juu ya Mashahidi wa Yehova, L’Eglise de Montréal, gazeti la kila juma la dayosisi kuu ya Katoliki ya Montreal, Kanada, lilisema hivi: “Wana kanuni za adili zenye kutokeza sana.” Hesabu kubwa za walimu wa shule, waajiri-kazi, na wakuu wa serikali hukubaliana na hilo. Ni nini husababisha sifa hiyo?
Kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova huhusisha mengi zaidi ya kushikamana na muundo fulani wa imani za kimafundisho na kutoa ushahidi kwa wengine juu ya imani hizo. Ukristo wa mapema ulijulikana kuwa “Ile Njia,” na Mashahidi wa Yehova hutambua kwamba dini ya kweli leo lazima iwe njia ya maisha. (Mdo. 9:2, NW) Hata hivyo, kama ilivyokuwa katika mambo mengine Mashahidi wa kisasa hawakupata mara moja ufahamu wenye usawaziko wa yale yaliyohusika katika jambo hilo.
“Tabia au Agano—Jipi Kati ya Hayo?”
Ingawa walianza kwa shauri thabiti la Kimaandiko juu ya uhitaji wa kuwa kama Kristo, mkazo ambao baadhi ya Wanafunzi wa Biblia wa mapema walitia katika “kusitawisha tabia,” kama walivyokuita, ulielekea kupunguza pande fulani za Ukristo wa kweli. Baadhi yao walionekana wakiwa na maoni ya kwamba kuwa muungwana—kuonekana sikuzote kuwa mwenye fadhili na mwema, kusema kwa sauti pole, kuepuka wonyesho wowote wa hasira, kusoma Maandiko kila siku—kungewahakikishia kuingia mbinguni. Lakini hao walikosa kuona uhakika wa kwamba Kristo alikuwa amewapa wafuasi wake kazi ya kufanya.
Tatizo hilo lilizungumzwa kwa uthabiti katika makala “Tabia au Agano—Jipi Kati ya Hayo?” katika toleo la Mei 1, 1926, la The Watch Tower.a Ilionyesha kwamba jitihada za kusitawisha “tabia kamilifu” wakati wa kuwa katika mwili zilifanya wengine waache kujitahidi kwa sababu ya kuvunjika moyo, bali wakati uleule, zikitokeza katika wengine mtazamo wa kujitakia uadilifu na zikaelekea kuwafanya wakose kuona thamani ya dhabihu ya Kristo. Baada ya kukazia imani katika damu ya Kristo iliyomwagwa, makala hiyo ilikazia umaana wa ‘kufanya mambo’ katika utumishi wenye utendaji wa Mungu ili kutoa uthibitisho kwamba mtu alikuwa akifuatia mwendo wenye kumpendeza Mungu. (2 Pet. 1:5-10) Wakati huo, ambapo sehemu kubwa ya Jumuiya ya Wakristo ilikuwa ingali ikijisingizia kushikamana na viwango vya adili vya Biblia, mkazo huo juu ya utendaji uliimarisha ile tofauti iliyokuwako kati ya Mashahidi wa Yehova na Jumuiya ya Wakristo. Tofauti hiyo ilipata kuwa wazi hata zaidi kadiri masuala ya kiadili ambayo yalikuwa yakiwa ya kawaida yalikuwa lazima yashughulikiwe na wote waliodai kuwa Wakristo.
“Mjiepushe na Uasherati”
Kiwango cha Kikristo kuhusu adili ya ngono kiliwekwa katika Biblia muda mrefu uliopita kwa lugha iliyo wazi. “Kwa maana haya ndiyo mapenzi ya Mungu, kule kutakaswa kwenu, kwamba mjiepushe na uasherati . . . Kwa maana Mungu alituita sisi, si kwa kuruhusu ukosefu wa usafi, bali kwa kuhusiana na utakaso. Kwa hiyo, basi, mtu aonyeshaye kupuuza anapuuza, si mtu bali Mungu.” (1 The. 4:3-8, NW) “Ndoa iwe yenye kuheshimika miongoni mwa wote, na kitanda cha ndoa kiwe bila kutiwa unajisi, kwa maana Mungu atawahukumu waasherati na wazinzi.” (Ebr. 13:4, NW) “Je, hamjui kwamba watu wasio waadilifu hawatarithi ufalme wa Mungu? Msiongozwe vibaya. Wala waasherati, . . . wala wazinzi, wala wanaume watunzwao kwa makusudi yasiyo ya asili, wala wanaume walalao pamoja na wanaume, . . . hawatarithi ufalme wa Mungu.”—1 Kor. 6:9, 10, NW.
Katika Watch Tower, uangalifu ulivutwa kwenye kiwango hicho cha Wakristo wa kweli mapema kama Novemba 1879. Lakini hakikuzungumzwa kwa kurudiwarudiwa au kwa urefu kana kwamba hilo lilikuwa tatizo kubwa miongoni mwa Wanafunzi wa Biblia wa mapema. Hata hivyo, kadiri mwelekeo wa ulimwengu ulivyopata kuwa wenye kuendekeza zaidi, uangalifu wenye kuongezeka ulielekezwa kwenye takwa hilo, hasa katika miaka ya karibu na Vita ya Ulimwengu 2. Hiyo ilihitajiwa kwa sababu wengine miongoni mwa Mashahidi wa Yehova walikuwa wakichukua maoni ya kwamba maadamu walikuwa wenye bidii katika kutoa ushahidi, ulegevu kidogo katika adili ya ngono ulikuwa jambo la kibinafsi. Ni kweli kwamba Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) la Machi 1, 1935, lilikuwa limetaarifu waziwazi kwamba ushiriki katika huduma ya shambani haukutoa kibali cha mwenendo wa ukosefu wa adili. Lakini si kila mtu aliyezingatia moyoni jambo hilo. Hivyo, katika toleo lalo la Mei 15, 1941, Mnara wa Mlinzi lilizungumzia tena jambo hilo, na kwa kirefu, katika makala yenye kichwa “Siku ya Nuhu.” Lilionyesha kwamba ufasiki wa kingono katika siku ya Nuhu ulikuwa sababu moja iliyofanya Mungu aharibu ulimwengu wa wakati ule, na lilionyesha kwamba jambo ambalo Mungu alifanya wakati huo liliweka kigezo cha jambo ambalo angefanya katika siku yetu. Kwa lugha iliyo wazi lilionya kwamba mtumishi wa Mungu mshika-uaminifu wenye maadili hangeweza kutumia sehemu ya siku yake akifanya mapenzi ya Bwana kisha, saa za baadaye, ajitie katika “kazi za mwili.” (Gal. 5:17-21, NW) Hilo lilifuatiliwa katika Mnara wa Mlinzi la Julai 1, 1942, na makala nyingine ambayo ilishutumu mwenendo usiopatana na viwango vya adili vya Biblia kwa waseja na kwa watu waliofunga ndoa. Hapana mtu aliyepaswa kukata maneno kwamba kushiriki katika kazi ya kuhubiria umma ujumbe wa Ufalme akiwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova kulimpa kibali cha kuwa na maisha ya ulegevu. (1 Kor. 9:27) Baada ya wakati, hatua thabiti hata zaidi zingechukuliwa ili kulinda salama usafi wa kiadili wa tengenezo.
Wengine ambao wakati huo walikuwa wakionyesha tamaa ya kuwa Mashahidi wa Yehova walikuwa wamekulia katika maeneo ambako ndoa za majaribio zilikubaliwa, ambako mahusiano ya kingono kati ya wachumba yalivumiliwa, au ambako mahusiano ya kukubaliana kati ya watu wasiofunga ndoa kisheria yalionwa kuwa jambo la kawaida. Waume na wake wachache walikuwa wakijizuia kufanya ngono. Watu wengine mmoja-mmoja, ingawa hawakuwa wametalikana, walikuwa wametengana na wenzi wao kwa njia isiyo ya hekima. Ili kuandaa mwelekezo uliohitajiwa, Mnara wa Mlinzi, wakati wa miaka ya 1950, lilifikiria hali hizo zote, na likazungumza juu ya madaraka ya ndoa, likakazia katazo la Biblia la uasherati, na likaeleza uasherati ni nini, ili kusiwe na kutoelewa vizuri.b—Mdo. 15:19, 20; 1 Kor. 6:18.
Katika mahali ambako watu waliokuwa wakianza kushirikiana na tengenezo la Yehova walikuwa hawachukui kwa uzito viwango vya adili vya Biblia, jambo hilo lilielekezewa uangalifu wa pekee. Hivyo, katika 1945, wakati N. H. Knorr, msimamizi wa tatu wa Watch Tower Society, alipokuwa Kosta Rika, alitoa hotuba juu ya adili ya Kikristo ambayo alisema hivi: “Nyinyi nyote mlio hapa usiku wa leo ambao mwaishi na mwanamke lakini hamjapanga ndoa yenu kisheria, mimi nawapa shauri. Nenda kwenye Kanisa Katoliki na kuandikisha jina lako kuwa mshiriki, kwa sababu huko waweza kuzoea mambo hayo. Lakini hili ni tengenezo la Mungu, na hamwezi kuzoea mambo hayo hapa.”
Kuanzia na miaka ya 1960, wakati wagoni-jinsia-moja walipokuwa wakizidi kufanya mazoea yao waziwazi, makanisa mengi yalijadili jambo hilo, kisha yakawakubali kuwa washiriki. Baadhi ya makanisa sasa hata huweka rasmi wagoni-jinsia-moja kuwa makasisi. Ili kusaidia watu wenye mioyo myeupe ambao walikuwa na masuala juu ya mambo hayo, vichapo vya Mashahidi wa Yehova vilizungumzia maswali hayo pia. Lakini miongoni mwa Mashahidi hakukupata kamwe kuwa na shaka yoyote juu ya jinsi ugoni-jinsia-moja ungeonwa. Kwa nini? Kwa sababu wao hawatendei matakwa ya Biblia kana kwamba haya ni maoni tu ya wanadamu wa enzi nyingine. (1 The. 2:13) Kwa mteremo wao huongoza mafunzo ya Biblia pamoja na wagoni-jinsia-moja ili hao wajifunze matakwa ya Yehova, na watu kama hao waweze kuhudhuria mikutano ya Mashahidi ili kusikiliza, lakini hapana yeyote ambaye huendelea kuwa mgoni-jinsia-moja anayeweza kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova.—1 Kor. 6:9-11; Yuda 7.
Katika miaka ya majuzi kujitia sana kwa vijana wasiofunga ndoa katika ngono kulipata kuwa jambo la kawaida katika ulimwengu. Vijana katika familia za Mashahidi wa Yehova walihisi msongo, na baadhi yao wakaanza kufuata njia hizo za ulimwengu uliowazunguka. Tengenezo lilishughulikiaje hali hiyo? Makala zilizokusudiwa kusaidia wazazi na vijana waone mambo Kimaandiko zilitangazwa katika Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Drama za hali za maisha halisi zilitolewa katika mikusanyiko ili kusaidia kila mtu apate kujua matunda ya kukataa viwango vya adili vya Biblia na ya manufaa ya kutii amri za Mungu. Mojapo zile za kwanza kati ya hizo, iliyoonyeshwa jukwaani katika 1969, ilikuwa na kichwa “Miiba na Mitego Imo Katika Njia ya Mwenye Kujitegemea.” Vitabu maalumu vilitayarishwa ili kusaidia vijana wathamini hekima ya shauri la Biblia. Hivyo vilitia ndani Kupata Faida Zote za Ujana Wako (kilichotangazwa katika Kiingereza 1976) na Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi (kilichotangazwa katika 1989). Wazee wenyeji walitoa msaada wa kibinafsi wa kiroho kwa watu mmoja-mmoja na familia. Makutaniko ya Mashahidi wa Yehova yalilindwa salama pia kwa kufukuzwa kwa wakosaji wasiotubu.
Kuharibika kwa maadili ya ulimwengu hakukuongoza kwenye maoni ya uendekevu zaidi miongoni mwa Mashahidi wa Yehova. Tofauti na hivyo, Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova limeweka mkazo ulioongezeka juu ya uhitaji wa kuepuka si matendo ya kingono yaliyo haramu tu bali pia mavutano na hali ambazo huharibu kanuni za adili. Wakati wa miongo mitatu iliyopita, limeandaa maagizo ili kuimarisha watu mmoja-mmoja dhidi ya “dhambi za siri” kama vile kupiga punyeto na kuwaweka chonjo kuona hatari za pornografia, vipindi vya televisheni vyenye ukosefu wa adili, na muziki wenye matokeo yenye kupotosha. Hivyo, ingawa mwelekeo wa kiadili wa ulimwengu umekuwa ukishuka, ule wa Mashahidi wa Yehova umekuwa ukipanda juu.
Maisha ya Familia Yenye Kuongozwa na Viwango vya Kimungu
Kushikamana imara na kiwango cha Biblia cha adili ya ngono kumenufaisha sana maisha ya familia ya Mashahidi wa Yehova. Lakini kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova si uhakikisho kwamba mtu hatakuwa na matatizo ya kinyumbani. Hata hivyo, Mashahidi wanasadikishwa kwamba Neno la Mungu hutoa shauri bora kabisa juu ya jinsi ya kuyashinda matatizo kama hayo. Wana upaji mwingi ambao umetolewa na tengenezo ili kuwasaidia kutumia shauri hilo; na wanapolifuata, matokeo ni yenye kunufaisha kwelikweli.
Mapema kama 1904, buku la sita la Studies in the Scriptures liliandaa mazungumzo mengi juu ya madaraka ya ndoa na wajibu mbalimbali wa wazazi. Tangu wakati huo, mamia ya makala zimetangazwa na hotuba nyingi zimetolewa katika kila kutaniko la Mashahidi wa Yehova ili kusaidia kila mshiriki wa familia athamini fungu lake alilopewa na Mungu. Elimu hiyo ya maisha yenye kujenga ya familia si ya wale waliofunga ndoa karibuni tu bali ni programu yenye kuendelea ambayo huhusisha ndani kutaniko zima.—Efe. 5:22–6:4; Kol. 3:18-21.
Je, Ndoa ya Wake Wengi Ingekubalika?
Hata ingawa desturi zinazohusu ndoa na maisha ya familia hutofautiana katika nchi moja hadi nyingine, Mashahidi wa Yehova hutambua kwamba viwango vilivyowekwa katika Biblia hutumika kila mahali. Kazi yao ilipokuwa ikianza barani Afrika katika karne hii ya 20, Mashahidi walifundisha huko, kama wafanyavyo kila mahali, kwamba ndoa ya Kikristo huruhusu mwenzi mmoja tu wa ndoa. (Mt. 19:4, 5; 1 Kor. 7:2; 1 Tim. 3:2) Hata hivyo, walikuwako mamia ambao walikubali tendo la Biblia la kufichua ibada ya sanamu na wakakubali kwa furaha yale ambayo Mashahidi wa Yehova walifundisha kuhusu Ufalme wa Mungu lakini ambao walibatizwa bila kuacha ndoa ya wake wengi. Ili kusahihisha hali hiyo, Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) la Januari 15, 1947, lilikazia kwamba Ukristo hautoi ruhusa kwa ndoa ya wake wengi, hata desturi za mahali ziwe nini. Barua iliyopelekwa kwenye makutaniko ilijulisha wowote waliodai kuwa Mashahidi wa Yehova lakini ambao walikuwa na ndoa ya wake wengi kwamba waliruhusiwa miezi sita ili kurekebisha mambo yao ya ndoa yapatane na kiwango cha Biblia. Jambo hilo lilitiwa nguvu na hotuba iliyotolewa na Ndugu Knorr wakati wa ziara yake barani Afrika mwaka uo huo.
Katika Nigeria, kulikuwa watu wengi wa ulimwengu waliotabiri kwamba jitihada za kukomesha ndoa ya wake wengi miongoni mwa Mashahidi wa Yehova zingemaanisha kwamba idadi ya watu ingepungua. Na ni kweli kwamba si wote waliokuwa na ndoa ya wake wengi na ambao hapo kwanza walikuwa wamebatizwa kuwa Mashahidi walifanya mabadiliko yaliyotakwa hata katika 1947. Kwa kielelezo, Asuquo Akpabio, mwangalizi asafiriye, asimulia kwamba Shahidi mmoja aliyekuwa akikaa kwake katika Ifiayong alimwamsha usiku wa manane na kumwamuru abadili jambo lililokuwa limetangazwa kuhusu takwa la ndoa ya mke mmoja. Kwa sababu alikataa kufanya hivyo, mkaribishi wake alimfukuza aende nje katika mvua iliyokuwa ikinyesha usiku huo.
Lakini kumpenda Yehova kumewapa wengine nguvu inayohitajiwa kutii amri zake. Hapa pana wachache tu kati yao. Katika Zaire mwanamume mmoja aliyekuwa amekuwa Mkatoliki na mwenye ndoa ya wake wengi aliachana na wawili kati ya wake zake ili awe mmoja wa Mashahidi wa Yehova, hata ingawa kumwacha yule aliyependa zaidi aende zake kwa sababu si yeye aliyekuwa ‘mke wa ujana wake’ kulikuwa jaribu kali sana la imani yake. (Mit. 5:18) Katika Dahomey (sasa Benin) aliyekuwa hapo kwanza Mmethodisti ambaye alikuwa angali ana wake watano alishinda vizuizi vigumu sana vya kisheria ili aweze kupata talaka zilizotakwa ndipo astahili ubatizo. Hata hivyo, aliendelea kuandalia riziki hao ambao hapo kwanza walikuwa wake na watoto wake, kama walivyofanya wengine waliowaacha wake zao wa pili. Warigbani Whittington, Mnaijeria, alikuwa mke wa pili kati ya wake wawili wa mume wake. Alipoamua kwamba kumpendeza Yehova, Mungu wa kweli, ndilo lililokuwa jambo la maana zaidi kwake, alikabili ghadhabu ya mume wake halafu ya familia yake mwenyewe. Mume wake alimruhusu kuondoka, pamoja na watoto wake wawili, lakini bila msaada wa kifedha—hata wa nauli. Hata hivyo, yeye alisema hivi: ‘Hapana yoyote ya manufaa za vitu vya kimwili nilizoacha nyuma iwezayo kulingana na kumpendeza Yehova.’
Namna Gani Talaka?
Katika nchi za Magharibi ni vigumu kuona ndoa ya wake wengi, lakini maoni mengine yanayopingana na Maandiko yanazoewa na wengi. Mojawapo ni wazo la kwamba ni afadhali kupata talaka kuliko kuwa na ndoa isiyo na furaha. Katika miaka ya majuzi baadhi ya Mashahidi wa Yehova walianza kuiga roho hiyo, wakitafuta talaka kwa kutegemea misingi kama vile “kutofaana.” Mashahidi wameshughulikiaje jambo hilo? Kampeni yenye juhudi ya elimu kuhusu maoni ya Yehova juu ya talaka huongozwa kwa ukawaida na tengenezo kunufaisha Mashahidi wa muda mrefu pamoja na mamia ya maelfu ya wale wanaoongezwa miongoni mwao kila mwaka.
Mnara wa Mlinzi limeelekeza uangalifu kwenye miongozo gani ya Biblia? Ifuatayo, miongoni mwa mingine: Katika maandishi ya Biblia kuhusu ndoa ya kwanza ya kibinadamu, umoja wa mume na mke unakaziwa; yasema hivi: ‘Lazima mwanamume aambatane na mkewe, nao watakuwa mwili mmoja.’ (Mwa. 2:24) Baadaye, katika Israeli, Sheria ilikataza uzinzi na ikatoa adhabu ya kifo kwa yeyote aliyeufanya. (Kum. 22:22-24) Talaka kwa sababu nyingine zaidi ya uzinzi iliruhusiwa, lakini ‘kwa sababu ya ugumu tu wa mioyo yao,’ kama alivyoeleza Yesu. (Mt. 19:7, 8) Yehova alionaje zoea la mtu kuacha mwenzi wa ndoa ili kuoa mwingine? Malaki 2:16 (NW) hutaarifu: “Amechukia kutaliki.” Hata hivyo, yeye aliruhusu wale ambao walipata talaka waendelee kukaa katika kutaniko la Israeli. Humo, wakikubali nidhamu ya Yehova kwa watu wake, baada ya wakati huenda badala ya moyo wao mgumu kukawa moyo mwororo zaidi, ule ambao ungeweza kuonyesha upendo halisi kwa njia zake.—Linganisha Ezekieli 11:19, 20.
Mara nyingi Mnara wa Mlinzi limetaarifu kwamba wakati Yesu alipokuwa akizungumzia talaka kama ilivyozoewa katika Israeli la kale, alionyesha kwamba kiwango cha juu zaidi kingeanzishwa miongoni mwa wafuasi wake. Alisema kwamba ikiwa yeyote angetaliki mke wake isipokuwa kwa sababu ya uasherati (por·neiʹa, “ngono isiyo halali”) na kufunga ndoa na mwingine, angekuwa akifanya uzinzi; na hata kama hakufunga ndoa tena, angekuwa akimweka mke wake katika hali ya kufanya uzinzi. (Mt. 5:32; 19:9) Hivyo, Mnara wa Mlinzi limeonyesha kwamba kwa Wakristo talaka yoyote ni jambo zito zaidi ya ilivyokuwa katika Israeli. Ingawa Maandiko hayaelekezi kwamba kila mtu apataye talaka apaswa afukuzwe kutoka kutaniko, wale ambao pia hufanya uzinzi na ambao si wenye kutubu hutengwa na ushirika na makutaniko ya Mashahidi wa Yehova.—1 Kor. 6:9, 10.
Mabadiliko makubwa yametukia katika miaka ya majuzi katika maoni ya ulimwengu kuhusu ndoa na maisha ya familia. Ijapokuwa hayo, Mashahidi wa Yehova wameendelea kushikamana na viwango vilivyoandaliwa na Mungu, Mwanzilishi wa ndoa, kama vilivyoandikwa katika Biblia. Kwa kutumia miongozo hiyo, wamejitahidi kusaidia watu wenye mioyo ya haki wazishinde hali ngumu ambazo katika hizo wengi sana hujipata.
Kama tokeo, mabadiliko makubwa yamefanywa katika maisha za wengi ambao wamekubali maagizo ya Biblia kutoka kwa Mashahidi wa Yehova. Wanaume waliokuwa hapo kwanza wapiga-wake, wanaume ambao hawakutimiza madaraka yao, wanaume ambao walitoa uandalizi wa kimwili lakini si wa kihisia-moyo na kiroho—maelfu mengi ya hao wamekuwa waume wenye upendo na akina baba ambao hujali sana watu wa nyumba zao. Wanawake waliokuwa wenye kujitegemea sana, wanawake ambao walipuuza watoto wao na hawakujijali wenyewe au nyumba zao—wengi wao wamekuwa wake ambao hustahi ukichwa na kufuatia mwendo ambao huwafanya wapendwe sana na waume na watoto wao. Vijana ambao kwa ufidhuli walikuwa hawatii wazazi wao na ambao walikuwa waasi dhidi ya jamii kwa ujumla, vijana ambao walikuwa wakiharibu maisha zao wenyewe kwa mambo waliyokuwa wakifanya na hivyo kuletea wazazi wao huzuni ya moyo—wengi wao wamekuja kuwa na kusudi la kimungu maishani, na hilo limesaidia kugeuza utu wao.
Bila shaka, jambo la maana katika kufanikiwa ndani ya familia ni kuwa wafuatiaji wa haki kwa mmoja na mwingine. Ufuatiaji wa haki ni wa muhimu pia katika mahusiano mengineyo.
Takwa la Ufuatiaji wa Haki Hufika Mbali Kadiri Gani?
Mashahidi wa Yehova watambua kwamba ufuatiaji wa haki watakwa katika kila jambo wafanyalo. Ukiwa msingi wa maoni yao, wao huelekeza kwenye maandiko kama haya yafuatayo: Yehova mwenyewe ni “Mungu wa kweli.” (Zab. 31:5) Kwa upande mwingine, kama vile Yesu alivyosema, Ibilisi ndiye “baba ya uwongo.” (Yn. 8:44, NW) Basi, kwa kueleweka, miongoni mwa mambo ambayo Yehova huchukia ni “ulimi wa uongo.” (Mit. 6:16, 17) Neno lake hutuambia: “Sasa kwa kuwa mmeweka mbali ukosefu wa lililo kweli, semeni kweli.” (Efe. 4:25, NW) Na si lazima tu Wakristo waseme kweli, bali kama mtume Paulo, wahitaji pia “kujiendesha wenyewe kwa kufuatia haki katika mambo yote.” (Ebr. 13:18, NW) Hakuna maeneo ya maisha ambapo Mashahidi wa Yehova wanaweza kwa halali kutumia fungu jingine la thamani.
Wakati Yesu alipotembelea nyumba ya Zakayo mtoza ushuru, mwanamume huyo alikiri kwamba mazoea yake ya kikazi yalikuwa yamekuwa yasiyofaa, naye alichukua hatua za kurekebisha matendo ya awali ya unyang’anyi. (Luka 19:8) Katika miaka ya majuzi, ili kuwa na dhamiri safi mbele za Mungu, watu fulani walioanza kushirikiana na Mashahidi wa Yehova wamechukua hatua kama hizo. Kwa kielelezo, katika Hispania mwivi wa kupindukia alianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Upesi dhamiri yake ikaanza kumsumbua; hivyo akarudisha kwa mwajiri-kazi wake wa zamani na majirani wake bidhaa zilizoibwa, kisha akapeleka vitu vingine kwa polisi. Alitakwa alipe faini na kutumikia kifungo kifupi gerezani, lakini sasa ana dhamiri safi. Katika Uingereza, baada ya miezi miwili tu ya funzo la Biblia pamoja na mmoja wa Mashahidi wa Yehova, mtu aliyekuwa hapo kwanza mwivi wa almasi alijitolea kwa polisi, ambao walishangaa; walikuwa wamekuwa wakimtafuta kwa miezi sita. Wakati wa miaka miwili na nusu aliyotumia gerezani, alijifunza Biblia kwa bidii na akajifunza kushiriki kweli za Biblia na wengine. Baada ya kuachiliwa alijitolea abatizwe awe mmoja wa Mashahidi wa Yehova.—Efe. 4:28.
Sifa ya Mashahidi wa Yehova kwa ajili ya ufuatiaji wa haki inajulikana sana. Jambo ambalo waajiri-kazi wamejua si lile tu la kwamba Mashahidi hawatawaibia bali pia la kwamba hawatasema uwongo au kuandika maandishi bandia kwa mwelekezo wa waajiri-kazi—la, hata wajapotishwa kuwa watapoteza kazi yao. Kwa Mashahidi wa Yehova uhusiano mwema pamoja na Mungu ni jambo la maana zaidi ya kibali cha binadamu yeyote. Na wanajua kwamba, hata wawe wapi au wawe wanafanya nini, “vitu vyote viko uchi na vikiwa vimefunuliwa wazi machoni pake ambaye kwake sisi tuna kutoa hesabu.”—Ebr. 4:13, NW; Mit. 15:3.
Katika Italia gazeti la habari La Stampa lilisema hivi kuhusu Mashahidi wa Yehova: “Wanafanya wanayohubiri . . . kanuni bora za adili kupenda jirani, kukataa kuwa na mamlaka, kutofanya jeuri na ufuatiaji wa haki wa kibinafsi (ambazo kwa Wakristo walio wengi ni ‘desturi za Jumapili’ zinazofaa kuhubiriwa tu kutoka mimbari) zaongoza njia yao ya maisha ‘ya kila siku.’” Na katika Marekani, Louis Cassels, mhariri wa habari za dini kwa ajili ya United Press International, Washington, D.C., aliandika hivi: “Mashahidi hushikamana na imani zao kwa uaminifu sana, hata wakati kufanya hivyo kunagharimu sana.”
Kwa Nini Kucheza Kamari Hakujawa Suala Miongoni Mwao
Katika nyakati zilizopita, ufuatiaji wa haki kwa ujumla ulishirikishwa na kuwa tayari kufanya kazi kwa bidii. Kucheza kamari, yaani, kuhatarisha kupoteza kiasi cha fedha kwa kukisia matokeo katika mchezo au tukio jingine, kulidharauliwa na jamii kwa ujumla. Lakini kadiri roho ya ubinafsi ya kutaka kuwa tajiri ilivyoanza kuenea katika karne ya 20, kucheza kamari—halali na kusiko halali—kukaenea. Kunadhaminiwa si na wahalifu tu bali mara nyingi pia na kanisa na serikali za kilimwengu ili kupata fedha. Mashahidi wa Yehova wameshughulikiaje badiliko hilo la maoni katika jamii? Kwa msingi wa kanuni za Biblia.
Kama vile imeonyeshwa katika vichapo vyao, hamna amri hususa katika Biblia isemayo, Ni lazima usicheze kamari. Lakini tunda la kucheza kamari ni baya daima, na tunda hilo bovu limefichuliwa na Mnara wa Mlinzi na Amkeni! kwa nusu karne. Zaidi ya hilo, magazeti hayo yameonyesha kwamba kucheza kamari kwa namna yoyote kwahusu mitazamo ambayo Biblia huonya dhidi yayo. Kwa kielelezo, kupenda fedha: “Kupenda fedha ni mzizi wa mambo mabaya ya namna zote.” (1 Tim. 6:10, NW) Na ubinafsi: “Wala usitamani . . . kitu cho chote alicho nacho jirani yako.” (Kum. 5:21; linganisha 1 Wakorintho 10:24.) Pia pupa: “Mkome kuchangamana katika ushirika pamoja na yeyote aitwaye ndugu ambaye ni . . . mwenye pupa.” (1 Kor. 5:11, NW) Kwa kuongezea, Biblia huonya juu ya kuomba “Bahati [Njema]” kana kwamba ni kani fulani yenye nguvu zipitazo zile za asili ambayo ingeweza kutoa mapendeleo. (Isa. 65:11) Kwa kuwa wanazingatia moyoni maonyo hayo ya Kimaandiko, Mashahidi wa Yehova huepuka kwa imara kucheza kamari. Na tangu 1976 wametia jitihada za pekee kuepuka kuwa na yeyote miongoni mwao ambaye kazi yake ya kimwili ingemtambulisha waziwazi kuwa sehemu ya tengenezo la kucheza kamari.
Kucheza kamari hakujapata wakati wowote kuwa suala kubwa miongoni mwa Mashahidi wa Yehova. Wanajua kwamba badala ya kusitawisha roho ya pato kwa hasara ya wengine, Biblia huwatia moyo kufanya kazi kwa mikono yao, kuwa waaminifu katika kutunza waliyokabidhiwa, kuwa wakarimu, kushiriki vitu na wale wenye uhitaji. (Efe. 4:28; Luka 16:10; Rum. 12:13; 1 Tim. 6:18) Je, jambo hilo hutambuliwa kwa urahisi na wengine wanaokuwa na shughuli pamoja nao? Ndiyo, hasa na wale wanaokuwa na shughuli za kikazi pamoja nao. Ni jambo la kawaida kwa waajiri-kazi kuwatafuta Mashahidi wa Yehova wawafanyie kazi kwa sababu wanajua kudhamiria na kutumainika kwao. Wanajua kwamba dini ya Mashahidi ndiyo huwafanya kuwa watu wa aina walivyo.
Vipi Tumbaku na Matumizi Mabaya ya Dawa za Kulevya?
Biblia haitaji tumbaku, wala haitaji zile dawa nyingine nyingi ambazo hutumiwa vibaya leo. Lakini inaandaa miongozo ambayo imesaidia Mashahidi wa Yehova kuamua ni mwendo gani wa mwenendo ambao ungempendeza Mungu. Hivyo, huko nyuma kama 1895 wakati Watch Tower lilipotoa maelezo juu ya matumizi ya tumbaku, lilielekeza uangalifu kwenye 2 Wakorintho 7:1 (NW), lisemalo hivi: “Kwa hiyo, kwa kuwa tuna ahadi hizi, wapendwa, acheni tujisafishe wenyewe kila unajisi wa mwili na wa roho, tukikamilisha utakatifu katika hofu ya Mungu.”
Kwa miaka mingi shauri hilo lilionekana kuwa latosha. Lakini kadiri kampuni za tumbaku zilivyotumia matangazo kuonyesha uvutaji kuwa wenye kuvutia, halafu matumizi mabaya ya dawa “zisizo halali” yakaenea, shauri zaidi lilihitajiwa. Kanuni nyingine za Biblia zilikaziwa: staha kwa Yehova, Mpaji-Uhai (Mdo. 17:24, 25); kumpenda jirani (Yak. 2:8), na uhakika wa kwamba mtu asiyempenda binadamu mwenzake kwa kweli hampendi Mungu (1 Yoh. 4:20); pia utii kwa watawala wa kilimwengu (Tito 3:1). Ilionyeshwa kwamba neno la Kigiriki phar·ma·kiʹa, ambalo kwa msingi huonyesha “matumizi ya dawa za kulevya,” lilitumiwa na waandikaji wa Biblia kurejezea ‘zoea la kuwasiliana na roho waovu’ kwa sababu ya matumizi ya dawa za kulevya katika mazoea ya kuwasiliana na roho waovu.—Gal. 5:20.
Huko nyuma katika 1946, gazeti Consolation lilifichua hali ya shuhuda zilizotolewa na watu waliolipwa ambazo mara nyingi huwa ni za kudanganya na ambazo hutumiwa katika matangazo ya sigareti. Kadiri uthibitisho wa kisayansi ulivyopatikana, Amkeni!, mwandamizi wa Consolation, pia lilichapisha uthibitisho kwamba matumizi ya tumbaku hutokeza kansa, maradhi ya moyo, dhara kwa mtoto asiyezaliwa wa mwanamke mjamzito, na dhara kwa wasiovuta tumbaku wanaolazimika kuvuta hewa yenye kujaa moshi, pamoja na uthibitisho wa kwamba nikotini hutokeza uzoevu. Uangalifu umevutwa kwenye matokeo yenye kulevya ya bangi na uthibitisho wa kwamba matumizi yayo yaweza kutokeza dhara katika ubongo. Vivyo hivyo hatari kubwa za dawa nyingine za kulevya zimezungumzwa kwa kurudiarudia kwa manufaa ya wasomaji wa vichapo vya Watch Tower.
Muda mrefu kabla mashirika ya serikali kukubali ni kwa kadiri gani yapaswa kuweka watu chonjo kuona madhara ya kutumia tumbaku, Mnara wa Mlinzi, (Kiingereza) katika toleo lalo la Machi 1, 1935, lilieleza wazi kwamba hapana mtu aliyekuwa mtumiaji wa tumbaku ambaye angeweza kuwa mshiriki wa wafanyakazi wa makao makuu ya Watch Tower Bible and Tract Society au awe mmoja wa wawakilishi wake waliowekwa rasmi. Baada ya watumishi wote katika makutaniko ya Mashahidi wa Yehova kuwekwa rasmi na Sosaiti (mpango ambao ulianza katika 1938), Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) la Julai 1, 1942, lilitaarifu kwamba katazo juu ya matumizi ya tumbaku lilihusu pia watumishi hao wote waliowekwa rasmi. Katika maeneo fulani miaka kadhaa ilipita kabla hilo halijatekelezwa kikamili. Hata hivyo, walio wengi wa Mashahidi wa Yehova waliitikia kwa kupendelea shauri hilo la Kimaandiko na kielelezo kizuri cha wale waliochukua uongozi miongoni mwao.
Ikiwa hatua zaidi ya kusonga mbele kupatana na matumizi ya shauri hilo la Biblia, hakuna wowote waliokuwa wangali wanavuta tumbaku waliokubaliwa kwa ajili ya ubatizo kuanzia 1973 na kuendelea. Wakati wa miezi iliyofuata, wale waliokuwa watendaji katika kutokeza tumbaku au kuendeleza uuzaji wa tumbaku walisaidiwa kutambua kwamba hawangeweza kuendelea kufanya hivyo na wakubaliwe kuwa Mashahidi wa Yehova. Shauri la Neno la Mungu lazima litumiwe kwa kupatana katika kila upande wa maisha. Kutumia hivyo kanuni za Biblia kwa habari ya matumizi ya tumbaku, bangi, na ziitwazo eti dawa kali za kulevya kumelinda Mashahidi. Kwa kutumia Maandiko, wameweza pia kusaidia maelfu mengi ya watu ambao maisha zao zilikuwa zikiharibiwa na matumizi mabaya ya dawa za kulevya.
Je, Vinywaji Vyenye Kileo Ni Tofauti?
Vichapo vya Watch Tower havijachukua maoni ya kwamba matumizi ya vinywaji vyenye kileo ni sawa na matumizi mabaya ya dawa za kulevya. Kwa nini sivyo? Vyaeleza hivi: Muumba ajua jinsi tulivyoumbwa, na Neno lake huruhusu matumizi ya kiasi ya vinywaji vyenye kileo. (Zab. 104:15; 1 Tim. 5:23) Lakini Biblia huonya pia dhidi ya ‘kunywa sana,’ na hushutumu vikali ulevi.—Mit. 23:20, 21, 29, 30; 1 Kor. 6:9, 10; Efe. 5:18.
Kwa sababu kunywa vinywaji vyenye kulevya bila kiasi kulikuwa kukiharibu maisha za watu wengi, Charles Taze Russell mwenyewe alipendelea kuviepuka kabisa. Hata hivyo, alikiri kwamba Yesu alitumia divai. Wakati wa karne ya 19 na sehemu ya mapema ya karne ya 20, kulikuwa msukosuko mwingi wa umma ukitaka kuwe katazo la kisheria la kileo katika Marekani. Watch Tower lilielewa maoni ya wale waliokuwa wakijaribu kupigana na dhara kutokana na kileo, lakini halikujiunga na kampeni yao ya kutaka sheria zenye kukataza zipitishwe. Hata hivyo, gazeti hilo lilionyesha kwa uthabiti madhara yatokanayo na kutumia kileo kupita kiasi lilitaarifu mara nyingi kwamba ingekuwa afadhali kujiepusha kabisa na divai na kileo. Wale waliohisi kwamba wangeweza kutumia kileo kwa kiasi walitiwa moyo kufikiria Warumi 14:21 (NW), lisemalo hivi: “Ni vema kutokula nyama au kunywa divai au kufanya jambo lolote ambalo juu yalo ndugu yako akwazika.”
Hata hivyo, katika 1930, wakati msimamizi wa Shirika la Kupinga Nyumba za Kuuzia Kileo katika Marekani alipofikia hatua ya kudai hadharani kwamba tengenezo lake lilikuwa “limezaliwa na Mungu,” J. F. Rutherford, wakati ule akiwa msimamizi wa Watch Tower Society, alitumia pindi hiyo kutoa hotuba za redio kuonyesha kwamba dai kama hilo ni sawa na uchongezi dhidi ya Mungu. Kwa nini? Kwa sababu Neno la Mungu halipigi marufuku matumizi yote ya divai; kwa sababu sheria zenye kukataza hazikuwa zikikomesha ulevi, ambao Mungu hushutumu; na kwa sababu badala ya kufanya hivyo, sheria zenye kukataza matumizi ya kileo zilikuwa zikisababisha kutengenezwa na kugawanywa kwa vileo haramu na kutokeza ufisadi katika serikali.
Matumizi ya vinywaji vyenye kileo au kujiepusha navyo huonwa kuwa jambo la kibinafsi miongoni mwa Mashahidi wa Yehova. Lakini wanashikamana na takwa la Kimaandiko la kwamba waangalizi lazima wawe “wenye kiasi katika mazoea.” Usemi huo unatafsiriwa kutokana na neno la Kigiriki ne·phaʹli·on, ambalo humaanisha, kihalisi, ‘-enye kulevuka, -enye kiasi; kujiepusha na divai, ama kabisa ama angalau kwa matumizi yayo yasiyo ya kiasi.’ Watumishi wa huduma, pia lazima wawe “si wenye kujitoa kwa kunywa divai nyingi.” (1 Tim. 3:2, 3, 8, NW) Hivyo, wanywao kwa wingi sana hawastahili mapendeleo ya pekee ya utumishi. Uhakika wa kwamba wale wachukuao uongozi miongoni mwa Mashahidi wa Yehova huweka kielelezo chema huwapa uhuru wa kusema katika kusaidia wengine ambao huenda wakaelekea kutegemea vinywaji vyenye kileo ili kuuweza mkazo au huenda, kwa kweli, wakahitaji kujiepusha nacho kabisa ili waendelee kukaa wamelevuka. Matokeo ni nini?
Kama kielelezo, ripoti ya habari kutoka kusini-kati mwa Afrika yataarifu hivi: “Kutokana na habari zote, yale maeneo ambamo Mashahidi wa Yehova ni wenye nguvu zaidi miongoni mwa Waafrika sasa ni maeneo yasiyo na matata kwa kadiri kubwa kuliko yale ya wastani. Hakika wamekuwa wenye kutenda dhidi ya wenye kuleta msukosuko, uchawi, ulevi na jeuri ya aina yoyote.”—The Northern News (Zambia).
Njia nyingine ya maana ambayo mwenendo wa Mashahidi wa Yehova hutofautiana na ule wa ulimwengu ni kuhusiana na—
Staha kwa Uhai
Staha hiyo hutokana na kutambua uhakika wa kwamba uhai ni zawadi kutoka kwa Mungu. (Zab. 36:9; Mdo. 17:24, 25) Inatia ndani kutambua kwamba hata uhai wa wasiozaliwa ni wenye thamani machoni pa Mungu. (Kut. 21:22-25; Zab. 139:1, 16) Huzingatia jambo la kwamba “kila mmoja wetu atatoa hesabu kwa Mungu kwa ajili yake mwenyewe.”—Rum. 14:12, NW.
Kupatana na kanuni hizo za Biblia, Mashahidi wa Yehova wamejiepusha daima na zoea la kutoa mimba. Ili kutoa mwelekezo timamu kwa wasomaji walo, gazeti Amkeni! limewasaidia wathamini kwamba usafi wa adili ni takwa la kimungu; limezungumzia kirefu maajabu ya utaratibu wa uzazi pamoja na mambo ya kiakili na ya kimwili yahusuyo uzazi wa mtoto. Katika enzi ya baada ya Vita ya Ulimwengu 2 wakati utoaji-mimba ulipopata kuwa jambo la kawaida zaidi, Mnara wa Mlinzi lilionyesha waziwazi kwamba zoea hilo ni kinyume cha Neno la Mungu. Likisema waziwazi, toleo la Desemba 15, 1969, lilisema hivi: “Utoaji-mimba ili tu kuondolea mbali mtoto asiyetakwa ni sawa na kutwaa uhai wa kibinadamu kimakusudi.”
Kwa Nini Kutiwa Damu Mishipani Kunakataliwa
Staha kwa uhai inayoonyeshwa na Mashahidi wa Yehova imeongoza pia mtazamo wao kuelekea kutiwa damu mishipani. Wakati kutia damu mishipani kulipopata kuwa suala linalowakabili, Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) la Julai 1, 1945, lilifafanua kirefu maoni ya Kikristo kuhusu utakatifu wa damu.c Lilionyesha kwamba damu ya wanyama na pia ya wanadamu ilitiwa ndani ya katazo la kimungu ambalo lilifanywa kuwa wajibu kwa Nuhu na wazao wake wote. (Mwa. 9:3-6) Lilionyesha kwamba takwa hilo lilikaziwa tena katika karne ya kwanza katika amri ya kwamba Wakristo ‘wajiepushe na damu.’ (Mdo. 15:28, 29) Makala iyo hiyo ilionyesha waziwazi kutokana na Maandiko kwamba ni matumizi ya kidhabihu tu ya damu yaliyopata kukubaliwa na Mungu, na kwamba kwa kuwa dhabihu za wanyama zilizotolewa chini ya Sheria ya Musa zilifananisha dhabihu ya Kristo, kutojali takwa la kwamba Wakristo ‘wajiepushe na damu’ kungekuwa uthibitisho wa ukosefu mbaya sana wa staha kwa dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo. (Law. 17:11, 12; Ebr. 9:11-14, 22) Kupatana na uelewevu huo wa mambo, kuanzia 1961 wowote waliopuuza takwa hilo la kimungu, wakakubali kutiwa damu mishipani, na wakadhihirisha mtazamo wa kutotubu walitengwa na ushirika wa makutaniko ya Mashahidi wa Yehova.
Mwanzoni, athari mbaya za kimwili za kutiwa damu mishipani hazikuzungumzwa katika vichapo vya Watch Tower. Baadaye, habari kama hiyo ilipopatikana, hiyo pia ilitangazwa—si ikiwa sababu inayofanya Mashahidi wa Yehova wakatae kutiwa damu mishipani, bali ili kuimarisha uthamini wao wa katazo ambalo Mungu mwenyewe alikuwa ameweka juu ya matumizi ya damu. (Isa. 48:17) Kwa kusudi hilo, katika 1961 kile kijitabu Blood, Medicine and the Law of God kilichofanyiwa uchunguzi mwingi wa uangalifu kilitangazwa. Katika 1977 kijitabu kingine kilichapwa. Hicho, chenye kichwa Mashahidi wa Yehova na Suala la Damu, kwa mara nyingine tena kilikazia uhakika wa kwamba msimamo unaochukuliwa na Mashahidi wa Yehova ni wa kidini, ukitegemea yale yanayosemwa na Biblia, na hautegemei hatari za kiafya au za kitiba. Habari za karibuni zaidi juu ya kichwa hicho ilitolewa katika 1990 katika broshua Damu Yaweza Kuokoaje Uhai Wako? Kwa kutumia vichapo hivyo, Mashahidi wa Yehova wamejitahidi sana kupata ushirikiano wa madaktari na kuwasaidia kuelewa msimamo wa Mashahidi. Hata hivyo, kwa miaka mingi matumizi ya damu mishipani yameonwa na wataalamu wa kitiba kuwa yenye maana sana.
Hata ingawa Mashahidi wa Yehova waliambia madaktari kwamba hawakuwa na katazo la kidini juu ya matibabu yaliyo badala, kukataa kutiwa damu mishipani hakukuwa rahisi. Mara nyingi, msongo mwingi uliletwa juu ya Mashahidi na familia zao wakubali lile lililokuwa wakati huo zoea la kitiba la kidesturi. Katika Puerto Riko katika Novemba 1976, Ana Paz de Rosario mwenye umri wa miaka 45, alikubali upasuaji na utibabu uliohitajiwa lakini akaomba kwamba kwa sababu ya imani zake za kidini, damu isitumiwe. Hata hivyo, wakiwa na amri ya mahakama, polisi watano na wauguzi watatu walikwenda katika chumba chake cha hospitali baada ya usiku kati, wakamfunga kwenye kitanda, na kumtia damu mishipani kwa nguvu, kinyume cha mapenzi yake na yale ya mume na watoto wake. Alipatwa na mshtuko, akafa. Kwa vyovyote hiyo haikuwa kesi ya pekee, wala dhuluma hizo hazikutukia katika Puerto Riko tu.
Katika Denmark, wazazi Mashahidi walifuatwa na polisi katika 1975 kwa sababu walikataa kuruhusu mwana wao mchanga atiwe damu mishipani kwa nguvu lakini, badala ya hivyo, wakatafuta matibabu yaliyo badala. Katika Italia, katika 1982, mume na mke waliokuwa wametafuta kwa upendo msaada wa kitiba katika nchi nne kwa ajili ya binti yao aliyekuwa na ugonjwa usioponyeka walihukumiwa miaka 14 gerezani kwa shtaka la uuaji-kimakusudi baada ya msichana wao kufa alipokuwa akitiwa damu mishipani kwa amri ya mahakama.
Mara nyingi, kuhusiana na majaribio ya kutia damu mishipani kwa nguvu katika watoto wa Mashahidi wa Yehova, uhasama mwingi wa umma umechochewa na vyombo vya habari. Katika visa fulani, hata bila kusikilizwa na mahakama ili wazazi waeleze, mahakimu wameamuru kwamba watoto wao watiwe damu mishipani. Hata hivyo, katika visa zaidi ya 40 katika Kanada, watoto waliotiwa damu mishipani walirudishwa kwa wazazi wao wakiwa wamekufa.
Si madaktari na mahakimu wote hukubaliana na njia hizo za kimabavu. Wachache walianza kuhimiza mtazamo wenye kusaidia. Baadhi ya madaktari walitumia stadi zao kuandaa utibabu bila damu. Kwa kufanya hivyo, walipata ujuzi mwingi katika upasuaji wa kila aina usiotumia damu. Hatua kwa hatua ikaonyeshwa kwamba aina zote za upasuaji zingeweza kufanywa kwa mafanikio, kwa watu wazima na vitoto pia, bila kutia damu mishipani.d
li kuzuia mikabiliano isiyo ya lazima katika hali za dharura, mapema katika miaka ya 1960 Mashahidi wa Yehova walianza kufanya ziara za pekee kwa madaktari wao ili kuzungumzia msimamo wao na kuwaandalia fasihi inayofaa. Baadaye waliomba kwamba taarifa iliyoandikwa iwekwe katika faili za kitiba za watu mmoja-mmoja ikitaarifu kwamba hawapaswi kutiwa damu mishipani. Kufikia miaka ya 1970, walilifanya kuwa zoea la kawaida kubeba wao binafsi kadi ya kutahadharisha wafanyakazi wa kitiba juu ya uhakika wa kwamba hawapaswi kutiwa damu mishipani chini ya hali zozote. Baada ya kushauriana na madaktari na wanasheria, hali ya kadi hiyo ilirekebishwa ili kuifanya kuwa hati ya kisheria.
Ili kutegemeza Mashahidi wa Yehova katika azimio hilo la kuzuia wasitiwe damu mishipani, ili kuondolea mbali kutoelewa vizuri upande wa madaktari na hospitali, na ili kuanzisha roho ya ushirikiano zaidi kati ya mashirika ya kitiba na wagonjwa Mashahidi, Halmashauri za Uhusiano na Hospitali zimeanzishwa kwa mwelekezo wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova. Kutoka halmashauri chache kama hizo katika 1979, idadi yao imeongezeka kufikia zaidi ya 800 katika nchi zaidi ya 70. Wazee walioteuliwa wamezoezwa nao wanaandaa utumishi kama huo katika Amerika Kaskazini, Mashariki ya Mbali, nchi kubwa za Pasifiki Kusini, Ulaya, na Amerika ya Latin. Kuongezea kueleza msimamo wa Mashahidi wa Yehova, wazee hao huwajulisha wafanyakazi wa hospitali juu ya uhakika wa kwamba kuna matibabu mengine halali yaliyo badala ya mitio ya damu. Katika hali za dharura wanasaidia katika kuanzisha mashauriano kati ya madaktari wanaotoa utunzaji wa kwanza na wapasuaji ambao wameshughulikia magonjwa kama hayo kwa ajili ya Mashahidi bila damu. Inapokuwa lazima, halmashauri hizo zimetembelea si wafanyakazi wa hospitali tu bali pia mahakimu ambao wamehusika katika kesi ambazo hospitali zimetafuta amri za mahakama ili kutia damu mishipani.
Wakati staha kwa imani zao za kidini kuhusu utakatifu wa damu haingeweza kuhakikishwa kwa njia nyinginezo, pindi kwa pindi, Mashahidi wa Yehova hata wamewapeleka mahakamani madaktari na hospitali. Kwa kawaida wametafuta tu amri ya kuzuia au hati ya kuwazuia kutenda kimabavu. Ingawa hivyo, katika miaka ya karibuni, hata wameshtaki mahakamani madaktari na hospitali zilizotenda kimabavu ili walipwe ridhaa. Katika 1990 Mahakama ya Rufani ya Ontario, katika Kanada, ilikubaliana na shtaka kama hilo kwa sababu daktari mmoja alikuwa amepuuza kadi iliyokuwa katika kibeti cha mgonjwa iliyokuwa imetaarifu waziwazi kwamba Shahidi huyo hangeweza kukubali kutiwa damu mishipani chini ya hali zozote. Katika Marekani, tangu 1985, angalau mashtaka kumi kama hayo ya kutaka kulipwa ridhaa yamefanywa katika sehemu mbalimbali za nchi, na mara nyingi wale wanaoshtakiwa wameamua kumaliza shtaka hilo nje ya mahakama kwa kulipa kiasi kilichotakwa badala ya kukabili uwezekano wa kwamba kikundi cha mahakimu kingeamuru mshtaki alipe ridhaa kubwa hata zaidi. Mashahidi wa Yehova wameazimia kabisa kutii katazo la kimungu juu ya matumizi ya damu. Wao hawataki kushtaki madaktari mahakamani, lakini watafanya hivyo ikihitajiwa ili kuwazuia wasitumie kwa nguvu juu ya Mashahidi utibabu ambao huwachukiza kiadili.
Umma unazidi kujua hatari zinazoambatana na kutiwa damu mishipani. Kwa kadiri fulani, hiyo ni kwa sababu ya hofu ya kupatwa na UKIMWI. Hata hivyo, Mashahidi wanasukumwa na tamaa yao ya moyo ya kumpendeza Mungu. Katika 1987 gazeti la kila siku la Kifaransa Le Quotidien du Médecin lilitaarifu hivi: “Labda Mashahidi wa Yehova hawakosei kwa kukataa matumizi ya vitu vilivyofanyizwa kwa damu, maana ni kweli kwamba hesabu fulani ya vitu vyenye kuleta maradhi vyaweza kupitishwa kwa damu iliyotiwa mishipani.”
Msimamo uchukuliwao na Mashahidi wa Yehova hautegemei ujuzi wa kitiba wa hali ya juu unaotokana nao. Wana uhakika tu kwamba njia za Yehova zafaa na kwamba ‘yeye hatawanyima chochote kilicho chema’ watumishi wake waaminifu-washikamanifu. (Zab. 19:7, 11; 84:11) Hata ikimpasa Shahidi kufa kama tokeo la kupoteza damu—na hilo limetukia pindi kwa pindi—Mashahidi wa Yehova wana usadikisho kamili kwamba Mungu hasahau waaminifu wake bali atawarudisha kwenye uhai kwa njia ya ufufuo.—Mdo. 24:15.
Wakati Watu Mmoja-Mmoja Wachaguapo Kupuuza Viwango vya Biblia
Mamilioni ya watu wamejifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, lakini si wote wamepata kuwa Mashahidi. Wakati baadhi ya watu hao wanapojifunza vile viwango vya juu vinavyotumika, wanaamua kwamba hiyo siyo namna ya maisha wanayotaka. Wote wanaobatizwa wanapewa kwanza maagizo kamili katika mafundisho ya msingi ya Biblia, na baada ya hapo (hasa tangu 1967) wazee katika kutaniko hupitia mafundisho hayo pamoja na kila mmoja anayetaka kubatizwa. Kila jitihada hufanywa kuhakikisha kwamba wale wanaobatizwa wanaelewa waziwazi si mafundisho tu bali pia yanayotiwa ndani ya mwenendo wa Kikristo. Hata hivyo, namna gani ikiwa baadaye baadhi yao waruhusu kupenda ulimwengu kuwashawishi waingie katika kosa zito?
Mapema kama 1904, katika kitabu The New Creation, uangalifu ulitolewa juu ya uhitaji wa kuchukua hatua ifaayo ili kutaniko lisiharibiwe kiadili. Uelewevu ambao Wanafunzi wa Biblia walikuwa nao wakati huo wa utaratibu wa kushughulika na wakosaji kama inavyoonyeshwa katika Mathayo 18:15-17 ulizungumzwa. Kwa hiyo, kupatana na hilo, katika pindi chache, kulikuwa ‘majaribu ya kihukumu ya kanisa’ ambayo katika hayo uthibitisho wa kosa katika visa vizito ulitolewa kwa kutaniko zima. Miaka mingi baadaye, Mnara wa Mlinzi (Kiingereza), katika toleo lalo la Mei 15, 1944, lilipitia habari hiyo kwa msaada wa Biblia nzima na likaonyesha kwamba mambo kama hayo yaliyohusu kutaniko yapasa kushughulikiwa na ndugu wenye madaraka waliokabidhiwa uangalizi wa kutaniko. (1 Kor. 5:1-13; linganisha Kumbukumbu la Torati 21:18-21.) Hiyo ilifuatwa, katika Mnara wa Mlinzi la Machi 1, 1952, na makala ambazo zilikazia si utaratibu ufaao tu bali pia uhitaji wa kuchukua hatua ili kuweka tengenezo likiwa safi. Kwa kurudiarudia tangu hapo, habari hiyo imepewa ufikirio. Lakini sikuzote malengo yamekuwa yaleyale: (1) kuweka tengenezo likiwa safi na (2) kukazia kwa mkosaji uhitaji wa toba ya moyo mweupe kwa kusudi la kumpata tena.
Katika karne ya kwanza, kulikuwa wengine walioacha imani kwa ajili ya maisha ya ulegevu. Wengine walikengeushwa kutoka katika imani kwa sababu ya mafundisho ya uasi-imani. (1 Yoh. 2:19) Jambo ilo hilo laendelea kutukia miongoni mwa Mashahidi wa Yehova katika karne ya 20. Kwa huzuni, katika miaka ya majuzi imehitajiwa kutenga na ushirika kila mwaka makumi ya maelfu ya wakosaji wasiotubu. Wazee mashuhuri wamekuwa miongoni mwao. Matakwa yaleyale ya Kimaandiko hutumika kwa wote. (Yak. 3:17) Mashahidi wa Yehova wajua kwamba kudumisha tengenezo safi kiadili ni muhimu ili kuendelea kuwa na kibali cha Yehova.
Kuvaa Utu Mpya
Yesu alihimiza watu wawe safi si nje tu bali pia ndani. (Luka 11:38-41) Alionyesha kwamba mambo ambayo sisi husema na kufanya huonyesha yaliyo moyoni mwetu. (Mt. 15:18, 19) Kama vile mtume Paulo alivyoeleza, ikiwa sisi tumefundishwa kwelikweli na Kristo, ‘tutafanywa wapya katika kani inayotendesha akili zetu’ nasi ‘tutavaa utu mpya, ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na uaminifu-mshikamanifu.’ (Efe. 4:17-24, NW) Wale wanaofundishwa na Kristo hutafuta kupata “mtazamo uleule wa akili aliokuwa nao Kristo Yesu” ili wafikiri na kutenda kama alivyofanya. (Rum. 15:5, NW) Mwenendo wa Mashahidi wa Yehova wakiwa watu mmoja-mmoja ni wonyesho wa kadiri ambayo kwa kweli wamefanya hivyo.
Mashahidi wa Yehova hawadai kwamba mwenendo wao hauna waa. Lakini wana moyo wa bidii katika jitihada zao za kuwa waigaji wa Kristo wajipatanishapo na kiwango bora cha mwenendo cha Biblia. Hawakatai kwamba kuna watu mmoja-mmoja wengine ambao hutumia viwango vya juu vya adili katika maisha zao. Lakini kwa habari ya Mashahidi wa Yehova, wanatambuliwa kwa urahisi kwa sababu ya mwenendo wao upatanao na viwango vya Biblia si wakiwa watu mmoja-mmoja tu, bali pia wakiwa tengenezo la kimataifa. Wanasukumwa na shauri lililopuliziwa ambalo limeandikwa kwenye 1 Petro 2:12 (NW): “Dumisheni mwenendo wenu ukiwa bora miongoni mwa mataifa, ili, . . . likiwa tokeo la kazi zenu bora ambazo wamekuwa mashahidi wa kujionea wapate kumtukuza Mungu.”
[Maelezo ya Chini]
a Katika Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) la Oktoba 15, 1941, habari hiyo ilizungumzwa tena, kwa namna iliyofupishwa kidogo, chini ya kichwa “Tabia au Uaminifu-Maadili—Jipi Kati ya Hayo?”
b Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) la Aprili 15, 1951, lilifafanua uasherati kuwa “uhusiano wa kingono wa hiari kwa upande wa mtu asiyefunga ndoa pamoja na mtu wa jinsia tofauti.” Toleo la Januari 1, 1952, liliongeza kwamba Kimaandiko neno hilo lingeweza kuhusu ukosefu wa adili kingono kwa upande wa mtu aliyefunga ndoa.
c Mazungumzo ya mapema zaidi ya utakatifu wa damu yalitokea katika The Watch Tower la Desemba 15, 1927, pamoja na Mnara wa Mlinzi la Desemba 1, 1944 (Kiingereza), ambalo lilitaja kihususa kutia damu mishipani.
d Contemporary Surgery, Machi 1990, kur. 45-49; The American Surgeon, Juni 1987, kur. 350-356; Miami Medicine, Januari 1981, uku. 25; New York State Journal of Medicine, Oktoba 15, 1972, kur. 2524-2527; The Journal of the American Medical Association, Novemba 27, 1981, kur. 2471-2472; Cardiovascular News, Februari 1984, uku. 5; Circulation, Septemba 1984.
[Blabu katika ukurasa wa 172]
“Wana kanuni za adili zenye kutokeza”
[Blabu katika ukurasa wa 174]
Je, kulipata wakati wowote kuwa na shaka juu ya jinsi ugoni-jinsia-moja ungeonwa?
[Blabu katika ukurasa wa 175]
Kuharibika kwa maadili ya ulimwengu hakukuwafanya Mashahidi kuwa wenye kuendekeza zaidi
[Blabu katika ukurasa wa 176]
Wengine walijaribu kuwa Mashahidi bila kuacha ndoa ya wake wengi
[Blabu katika ukurasa wa 177]
Programu yenye juhudi ya kufundisha maoni ya Yehova juu ya talaka
[Blabu katika ukurasa wa 178]
Mabadiliko makubwa katika maisha za watu
[Blabu katika ukurasa wa 181]
Tumbaku—La!
[Blabu katika ukurasa wa 182]
Vinywaji vyenye kileo—kwa kiasi, vikitumiwa
[Blabu katika ukurasa wa 183]
Wameazimia imara kutokubali damu
[Blabu katika ukurasa wa 187]
Kutenga na ushirika—ili kudumisha tengenezo safi kiadili
[Sanduku katika ukurasa wa 173]
‘Kusitawisha Tabia’—Tunda Halikuwa Zuri Sikuzote
Ripoti moja kutoka Denmark: ‘Wengi, hasa miongoni mwa akina ndugu wa umri mkubwa zaidi, katika jitihada zao za moyo mweupe za kuvaa utu wa Kikristo, walijitahidi kuepuka kila kitu kilichofanana kidogo sana na tabia ya ulimwengu ili kwa njia hiyo wajistahilishe Ufalme wa kimbingu. Mara nyingi, lilifikiriwa kuwa jambo lisilofaa kutabasamu wakati wa mikutano, na wengi wa akina ndugu wenye umri mkubwa zaidi walivaa suti nyeusi, viatu vyeusi, tai nyeusi tu. Mara nyingi walitosheka kuishi maisha matulivu na ya amani katika Bwana. Waliamini kwamba ilitosha kufanya mikutano na kuacha makolpota wafanye kazi ya kuhubiri.’
[Sanduku katika ukurasa wa 179]
Yale Ambayo Wengine Huona Katika Mashahidi
◆ “Münchner Merkur,” gazeti moja la habari la Ujerumani, liliripoti kuhusu Mashahidi wa Yehova hivi: “Wao ndio wafuatiaji-haki zaidi na walipaji kodi zaidi wasiochelewa kamwe kuliko wote katika Jamhuri ya Muungano. Utii wao kwa sheria waweza kuonekana katika njia ambayo wanaendesha gari na pia katika takwimu za uhalifu. . . . Wao hutii wale wenye mamlaka (wazazi, walimu, serikali). . . . Biblia, msingi wa matendo yao yote, ndiyo tegemezo lao.”
◆ Meya katika Lens, Ufaransa, aliwaambia Mashahidi hivi baada ya wao kutumia stediamu ya hapo kwa ajili ya mmojapo mikusanyiko yao: “Jambo ninalopenda ni kwamba nyinyi hutimiza ahadi zenu na maafikiano yenu, zaidi ya hilo, nyinyi ni safi, wenye nidhamu, na wenye mpango. Mimi napenda sosaiti yenu. Mimi napinga ukosefu wa utaratibu, nami sipendi watu wazungukao wakichafua na kuvunja vitu.”
◆ Kitabu “Voices From the Holocaust” kina kumbukumbu kutoka kwa mwokokaji mmoja Mpoland wa kambi za mateso za Auschwitz na Ravensbrück aliyeandika hivi: “Mimi niliona watu waliopata kuwa wema sana sana, na watu waliopata kuwa wafidhuli kabisa. Kikundi kilichokuwa chema zaidi ni Mashahidi wa Yehova. Mimi nawapa heko watu hao. . . . Walifanyia watu wengine mambo mazuri ajabu. Walisaidia wagonjwa, walishiriki mkate wao na wengine, na wakampa kila mtu aliye karibu nao faraja ya kiroho. Wajerumani waliwachukia na kuwastahi wakati uleule. Waliwapa kazi iliyo mbaya zaidi ya zote zaidi lakini Mashahidi wa Yehova waliikubali kwa adhama.”
-
-
“Wao Si Sehemu ya Ulimwengu”Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
Sura ya 14
“Wao Si Sehemu ya Ulimwengu”
KWA kadiri kubwa dini ya kisasa ni sehemu ya ulimwengu sana, hivyo inashiriki katika miadhimisho ya kilimwengu na huonyesha sana roho yao ya utukuzo wa taifa. Makasisi wayo mara nyingi hukiri uhakika huo, na wengi wao hupenda mambo yawe hivyo. Tofauti sana na hivyo, Yesu alisema hivi kuhusu wafuasi wake wa kweli: “Wao si sehemu ya ulimwengu, kama vile mimi si sehemu ya ulimwengu.”—Yn. 17:16, NW.
Rekodi huonyesha nini kwa habari ya Mashahidi wa Yehova katika jambo hili? Je, wao wametoa uthibitisho wenye kusadikisha kwamba wao si sehemu ya ulimwengu?
Mtazamo Kuelekea Wanadamu Wenzao
Wanafunzi wa Biblia wa mapema walijua vyema kwamba Wakristo wa kweli hawangekuwa wa ulimwengu. The Watch Tower lilieleza kwamba kwa sababu wafuasi wa Kristo watiwa-mafuta walitakaswa na kuzaliwa kwa roho ili waweze kushiriki katika Ufalme wa kimbingu, walitengwa na ulimwengu kwa tendo hilo la Mungu. Kwa kuongezea, lilitaja kwamba walikuwa chini ya wajibu wa kuepuka roho ya ulimwengu—malengo, kujitakia makuu, na matumaini yao, pamoja na njia zao.—1 Yoh. 2:15-17.
Je, hilo liliathiri mtazamo wa Wanafunzi wa Biblia kuelekea watu ambao hawakushiriki imani zao? Hakika halikuwafanya kuwa wenye kujitenga na watu. Lakini wale waliotumia kikweli yale waliyokuwa wakijifunza kutoka Maandiko hawakutafuta ushirika wa watu wa kilimwengu katika njia ya kwamba wangeshiriki namna yao ya maisha. The Watch Tower lilielekeza watumishi wa Mungu kwenye shauri la Biblia la ‘kufanya lililo jema kuelekea wote.’ Lilishauri pia kwamba wanyanyaswapo wapaswa wajitahidi kuepuka hisi za kulipa kisasi na, badala ya hivyo, kama vile Yesu alivyokuwa amesema, wapaswa ‘kuwapenda adui zao.’ (Gal. 6:10; Mt. 5:44-48, NW) Hasa liliwahimiza wajitahidi kushiriki pamoja na wengine kweli zenye thamani kubwa kuhusu uandalizi wa Mungu kwa ajili ya wokovu.
Yaeleweka, kufanya mambo hayo kungewafanya waonwe na ulimwengu kuwa tofauti. Lakini kutokuwa sehemu ya ulimwengu kwahusu zaidi—mengi zaidi.
Waliojitenga na Walio Tofauti na Babiloni Mkubwa
Ili wawe si sehemu ya ulimwengu, ilikuwa lazima wasiwe sehemu ya mifumo ya kidini iliyokuwa imejihusisha sana katika mambo ya ulimwengu na ambayo ilikuwa imefyonza mafundisho na desturi kutoka Babiloni la kale, adui wa muda mrefu wa ibada ya kweli. (Yer. 50:29) Vita ya ulimwengu ya kwanza ilipolipuka, kwa miongo mingi Wanafunzi wa Biblia walikuwa wamefunua mizizi ya kipagani ya mafundisho ya Jumuiya ya Wakristo kama vile Utatu, kutokufa kwa nafsi ya kibinadamu, na moto wa helo. Walikuwa pia wamefunua rekodi ya makanisa ya kujaribu kutumia serikali kwa ajili ya makusudi yayo wenyewe ya ubinafsi. Kwa sababu ya mafundisho na mazoea ya Jumuiya ya Wakristo, Wanafunzi wa Biblia walikuwa wameihusianisha na “Babiloni Mkubwa.” (Ufu. 18:2, NW) Walitaja kwamba ilichanganya kweli na makosa, Ukristo vuguvugu na mambo halisi ya ulimwengu, na kwamba ule mtajo wa Kibiblia “Babiloni” (unaomaanisha, “Mvurugo”) uliieleza vizuri hali hiyo. Waliwahimiza wapendao Mungu watoke katika “Babiloni.” (Ufu. 18:4, NW) Kwa kusudi hilo, mwishoni mwa Desemba 1917 na mapema katika 1918, waligawanya nakala 10,000,000 za toleo la The Bible Students Monthly lililozungumzia habari kuu “Kuanguka kwa Babiloni,” ambalo lilikuwa ufunuo wenye kupiga sana Jumuiya ya Wakristo. Hilo, nalo, lilitokeza uhasama mkatili kutoka kwa makasisi, ambao walitumia kwa kujifaidi kichaa cha wakati wa vita kujaribu kuponda kazi ya Mashahidi wa Yehova.
Kwa lazima, kutoka katika Babiloni Mkubwa kulihusisha kujiondoa kwa mshiriki wa matengenezo yaliyotetea mafundisho yake bandia. Wanafunzi wa Biblia walifanya hivyo, ijapokuwa kwa miaka mingi waliwaona kuwa ndugu zao Wakristo wale mmoja-mmoja katika makanisa waliodai kuwa wamejitakasa kabisa na kuwa na imani katika fidia. Hata hivyo, Wanafunzi wa Biblia hawakuandika tu barua za kujiondoa katika makanisa ya Jumuiya ya Wakristo bali pia, ilipowezekana, baadhi yao walikuwa wakisoma barua zao wenyewe kwa sauti kubwa kwenye mikutano ya kanisa mahali ambapo ilifaa washiriki kujieleza. Ikiwa hilo halikuwezekana, waliweza kupeleka nakala ya barua yao ya kujiondoa—yenye fadhili ikiwa na ushahidi ufaao—kwa kila mshiriki wa kutaniko.
Je, walikuwa pia wakihakikisha kwamba hawakuchukua pamoja na hilo desturi na mazoea yoyote yasiyo ya kumhofu Mungu ya matengenezo hayo? Hali ilikuwaje katika kipindi kilichoongoza hadi kwenye Vita ya Ulimwengu 1?
Je, Dini Yapasa Ijihusishe na Siasa?
Katika uwanja wa kisiasa, watawala wa mengi ya mataifa makuu, kwa sababu ya mahusiano yao na kanisa la Katoliki au la Protestanti, walikuwa wamedai kwa muda mrefu kuwa wenye kupokea ‘haki ya kutawala kutoka kwa Mungu,’ wakiwa wawakilishi wa Ufalme wa Mungu na kwa upendeleo wa pekee wa Mungu. Kanisa liliipa serikali baraka yalo; nayo serikali ikalipa kanisa utegemezo. Je, Wanafunzi wa Biblia walijiingiza katika jambo hilo pia?
Badala ya kuiga makanisa ya Jumuiya ya Wakristo, walitafuta kujifunza kutokana na mafundisho na kielelezo cha Yesu Kristo na mitume wake. Funzo lao la Biblia liliwaonyesha nini? Vichapo vya mapema vya Watch Tower hufunua ya kuwa walijua kwamba wakati Yesu alipoulizwa maswali na gavana Mroma Pontio Pilato, alitaarifu hivi: “Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu.” Ili kujibu swali kuhusu daraka la Yesu, alimwambia gavana huyo hivi: “Kwa ajili ya hili mimi nimezaliwa, na kwa ajili ya hili nimekuja kuingia ulimwenguni, ili nitoe ushahidi juu ya ile kweli.” (Yn. 18:36, 37, NW) Wanafunzi wa Biblia walijua kwamba Yesu alishikamana na mgawo huo bila kuyumbayumba. Wakati Ibilisi alipomtolea falme zote za ulimwengu na utukufu wazo, yeye alikataa. Wakati watu walipotaka kumfanya mfalme, alijiondoa. (Mt. 4:8-10; Yn. 6:15) Wanafunzi wa Biblia hawakuepuka uhakika wa kwamba Yesu alirejezea Ibilisi kuwa “mtawala wa ulimwengu” na akasema kwamba Ibilisi ‘hakuwa na mshiko juu yake.’ (Yn. 14:30, NW) Wangeweza kuona kwamba Yesu hakutafuta kujihusisha mwenyewe au wafuasi wake katika mfumo wa kisiasa wa Roma bali kwamba yeye alijishughulisha kabisa na kujulisha “habari njema ya ufalme wa Mungu.”—Luka 4:43, NW.
Je, kuamini kwao mambo hayo yaliyoandikwa katika Neno la Mungu kuliwatia moyo wasistahi mamlaka ya serikali? Sivyo kabisa. Badala ya hivyo, kuliwasaidia kuelewa kwa nini matatizo yanayowakabili watawala ni mengi mno, kwa nini kuna uvunjaji-sheria mwingi sana, na kwa nini programu za serikali za kufanya hali ya watu kuwa bora mara nyingi hazifanikiwi. Imani yao iliwafanya kuwa na saburi yajapokuwa magumu, kwa sababu walikuwa na uhakika kwamba kwa wakati wake Mungu angeleta kitulizo cha kudumu kwa njia ya Ufalme wake. Wakati huo walielewa kwamba “mamlaka za juu zaidi,” zirejezewazo kwenye Warumi 13:1-7 (KJ), ilikuwa ni watawala wa kilimwengu. Kupatana na hilo, walihimiza kustahi wakuu wa serikali. Katika kuzungumzia Warumi 13:7, C. T. Russell, katika kitabu The New Creation (kilichotangazwa katika 1904), alitaarifu kwamba Wakristo wa kweli “wangekuwa kiasili ndio wenye moyo mweupe zaidi katika kutambua wakuu wa ulimwengu huu, na wenye kutii zaidi sheria na matakwa ya sheria, isipokuwa mahali ambapo hizo zingepatikana zikihitilafiana na matakwa na amri za kimbingu. Ni watawala wachache wa kidunia ikiwa wako ambao watalaumu utambuzi wa Muumba mkuu zaidi na utii mkuu zaidi kwa amri zake. Kwa hiyo, [Wakristo wa kweli] wapaswa kupatikana miongoni mwa wale wenye kutii sheria zaidi wa wakati huu—si wachochezi, si wagomvi, si walaumuo.”
Wakiwa Wakristo, Wanafunzi wa Biblia walijua kwamba kazi ambayo wapaswa kuwa wakijitoa kwayo ilikuwa kuhubiri Ufalme wa Mungu. Na, kama ilivyotaarifiwa katika buku la kwanza la Studies in the Scriptures, “hilo likifanywa kwa uaminifu, hakutakuwa na wakati wala mwelekeo wa kugaagaa katika siasa za serikali zilizopo.”
Kwa habari hii walikuwa, kwa kadiri kubwa, kama wale Wakristo wa mapema wanaoelezwa na Augustus Neander katika kitabu The History of the Christian Religion and Church, During the Three First Centuries: “Wakristo hawakujihusisha na walikuwa tofauti na serikali, . . . na Ukristo ulionekana ukiweza kuwa na uvutano juu ya maisha za kiraia kwa njia ile tu ambayo, lazima iungamwe, ndiyo safi zaidi, kwa kujitahidi kwa njia yenye kutumika kukaza zaidi na zaidi hisi takatifu ndani ya raia wa taifa.”
Ulimwengu Ulipoenda Vitani
Duniani pote matukio ya Vita ya Ulimwengu 1 yalitahini vikali madai ya wale waliodai kuwa Wakristo. Ilikuwa ndiyo vita yenye kuogofya zaidi iliyopata kupigwa kufikia wakati huo; karibu idadi yote ya watu wa ulimwengu ilihusika kwa njia moja au nyingine.
Papa Benedict 15, ijapokuwa Vatikani iliunga mkono zile Serikali Kuu, alijitahidi kudumisha hali ya kuonekana kutofungamana na upande wowote. Hata hivyo, ndani ya kila taifa makasisi, Wakatoliki na Waprotestanti, hawakudumisha msimamo kama huo wa kutokuwamo. Kuhusu hali katika Marekani, Dakt. Ray Abrams, katika kitabu chake Preachers Present Arms, aliandika hivi: “Makanisa yalichukua umoja wa kusudi usiopata kujulikana kufikia wakati huo katika historia ya kidini. . . . Viongozi hawakupoteza wakati wowote katika kujitayarisha kikamili kwa ajili ya wakati huo wa vita. Katika muda wa saa ishirini na nne baada ya vita kutangazwa, Baraza la Muungano wa Makanisa ya Kristo Katika Amerika lilifanya mipango ya ushirikiano kamili zaidi. . . . Kanisa la Katoliki ya Roma, lilijitayarisha kwa ajili ya utumishi kama huohuo chini ya Baraza la Vita la Katoliki la Kitaifa, likielekezwa na maaskofu wakuu kumi na wanne naye Kardinali Gibbons akiwa msimamizi, lilionyesha ujitoaji huohuo kwa kusudi hilo. . . . Makanisa mengi yalifanya mengi zaidi ya yale yaliyoombwa yafanye. Yakawa vituo vya kuandikisha askari wapya.” Wanafunzi wa Biblia walifanya nini?
Ijapokuwa walijaribu kufanya lile ambalo walihisi kuwa lenye kumpendeza Mungu, sikuzote msimamo wao haukuwa wa kutokuwamo kabisa. Yale waliyofanya yaliongozwa na imani, waliyoshiriki pamoja na wengine waliodai kuwa Wakristo, kwamba “mamlaka za juu zaidi” zilikuwa “zimeagizwa rasmi na Mungu,” kulingana na maneno ya King James Version. (Rum. 13:1) Hivyo, kupatana na mbiu iliyopigwa na rais wa Marekani, The Watch Tower lilihimiza Wanafunzi wa Biblia wajiunge katika kushika Mei 30, 1918, kuwa siku ya sala na dua kuhusiana na matokeo ya vita ya ulimwengu.a
Wakati wa miaka ya vita, hali ambamo Wanafunzi wa Biblia mmoja-mmoja walijikuta zilitofautiana sana. Njia ambayo walizishughulikia ilitofautiana pia. Wakihisi wakiwa na wajibu wa kutii ‘mamlaka zilizopo,’ kama vile walivyowarejezea watawala wa kilimwengu, baadhi yao walikwenda katika mahandaki vitani wakiwa na bunduki na beneti. Lakini wakikumbuka lile andiko, “Usiue,” walikuwa wakipiga silaha zao hewani au kujaribu tu kuangusha silaha kutoka mikononi mwa mpinzani. (Kut. 20:13) Wachache, kama vile Remigio Cuminetti, katika Italia, walikataa kuvaa yunifomu ya jeshi. Serikali ya Italia katika wakati huo haikutoa ruhusa kwa yeyote ambaye kwa sababu ya dhamiri hangetwaa silaha. Alijaribiwa kihukumu mara tano na kufungwa katika magereza na katika hospitali ya wagonjwa wa akili, lakini imani na azimio lake vilidumu bila kutikiswa. Katika Uingereza baadhi ya walioomba wapewe ruhusa walipewa mgawo wa kazi ya maana ya kitaifa au kwenye vikosi vya askari wasiopigana. Wengine, kama vile Pryce Hughes, walichukua msimamo wa kutokuwamo kabisa, bila kujali matokeo kwao binafsi.
Angalau kufikia wakati huo, rekodi ya ujumla ya Wanafunzi wa Biblia haikuwa kabisa kama ile ya Wakristo wa mapema waelezwao katika kitabu The Rise of Christianity, cha E. W. Barnes, aliyeripoti hivi: “Pitio la uangalifu la habari yote ipatikanayo huonyesha kwamba, mpaka wakati wa Marcus Aurelius [maliki Mroma kutoka 161 hadi 180 W.K.], hakuna Mkristo aliyepata kuwa mwanajeshi; na hakuna mwanajeshi, baada ya kuwa Mkristo, aliyeendelea katika utumishi wa kijeshi.”
Lakini, mwishoni mwa Vita ya Ulimwengu 1, hali nyingine ilizuka iliyotaka vikundi vya kidini vionyeshe msimamo wao wa uaminifu-mshikamanifu.
Je, Ni Wonyesho wa Kisiasa wa Ufalme wa Mungu?
Mkataba wa amani, kutia na Agano la Ushirika wa Mataifa, ulitiwa sahihi katika Versailles, Ufaransa, katika Juni 28, 1919. Hata kabla ya mkataba huo wa amani kutiwa sahihi, Baraza la Muungano wa Makanisa ya Kristo Katika Amerika ulionyeshwa kuwa ukipiga mbiu kwamba Ushirika huo ungekuwa “wonyesho wa kisiasa wa Ufalme wa Mungu duniani.” Nayo Seneti ya Marekani ilipokea rundo la barua kutoka kwa vikundi vya kidini vikiihimiza ihalalishe Agano la Ushirika wa Mataifa.
Mashahidi wa Yehova hawakuunga mkono. Hata kabla ya mkataba huo wa amani kuthibitishwa (katika Oktoba), J. F. Rutherford alitoa hotuba katika Cedar Point, Ohio, katika Septemba 7, 1919, ambayo alionyesha kwamba si Ushirika wa Mataifa bali Ufalme uliosimamishwa na Mungu mwenyewe ndio tumaini pekee kwa wanadamu wenye kusononeka. Ingawa walikubali kwamba muungano wa kibinadamu ili kufanya ziwe bora hali ungeweza kutimiza mema mengi, Wanafunzi wa Biblia hao hawakuwa wakiupa visogo Ufalme wa Mungu mwenyewe kwa kuubadilisha na mpango wa kisiasa uliosimamishwa na wanasiasa na kubarikiwa na makasisi. Badala ya hivyo, walianza kazi ya kutoa ushahidi wa duniani pote kuhusu Ufalme ambao Mungu alikuwa ameuweka mikononi mwa Yesu Kristo. (Ufu. 11:15; 12:10) Katika The Watch Tower la Julai 1, 1920, ilielezwa kwamba hiyo ndiyo kazi ambayo Yesu alikuwa ametabiri kwenye Mathayo 24:14.
Kwa mara nyingine tena, kufuatia Vita ya Ulimwengu 2, Wakristo walikabiliwa na suala linalofanana na hilo. Wakati huo, lilihusu Umoja wa Mataifa, mwandamizi wa Ushirika ule. Vita ya Ulimwengu 2, ilipokuwa ingali inaendelea, katika 1942, Mashahidi wa Yehova walikuwa tayari wametambua kutoka Biblia, kwenye Ufunuo 17:8, kwamba tengenezo la amani ya ulimwengu lingesimama tena, pia kwamba lingeshindwa kuleta amani ya kudumu. Jambo hilo lilielezwa na N. H. Knorr, wakati huo akiwa msimamizi wa Watch Tower Society, katika hotuba ya mkusanyiko “Amani—Je, Inaweza Kudumu?” Kwa ujasiri Mashahidi wa Yehova walipiga mbiu ya maoni ya hali hiyo ya ulimwengu iliyokuwa ikisitawi. Kwa upande ule mwingine, viongozi Wakatoliki, Waprotestanti, Wayahudi walishiriki hasa katika mazungumzo katika San Francisco katika 1945 ambayo katika hayo Katiba ya UM iliandikwa. Kwa watazamaji wa matukio hayo, ilikuwa wazi ni nani waliotaka kuwa “rafiki ya ulimwengu” na ni nani waliokuwa wakijaribu kuwa “si sehemu ya ulimwengu,” kama Yesu alivyokuwa amesema ndivyo wanafunzi wake wangekuwa.—Yak. 4:4; Yn. 17:14, NW.
Rekodi ya Kutokuwamo kwa Kikristo
Ingawa Mashahidi wa Yehova walitambua upesi baadhi ya masuala yaliyohusu uhusiano wa Mkristo na ulimwengu, mambo mengine yalitaka wakati zaidi. Hata hivyo, Vita ya Ulimwengu 2 ilipokuwa ikiongeza mwendo katika Ulaya, makala yenye maana katika Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) la Novemba 1, 1939, iliwasaidia kuthamini maana ya kutokuwamo kwa Kikristo. Wafuasi wa Yesu Kristo, ikataarifu makala hiyo, wana wajibu mbele za Mungu kuwa wenye kujitoa kabisa kwake na Ufalme wake, ile Theokrasi. Sala zao zapaswa kuwa kwa ajili ya Ufalme wa Mungu, si kwa ajili ya ulimwengu. (Mt. 6:10, 33) Kwa msaada wa yale ambayo Yesu Kristo alifunua kwa habari ya utambulisho wa mtawala asiyeonekana wa ulimwengu (Yn. 12:31; 14:30), makala hiyo ilitoa sababu hivi, mtu ambaye amejitoa kwa Ufalme wa Mungu angewezaje kupendelea upande mmoja au ule mwingine katika pigano kati ya vikundi vya ulimwengu? Je, Yesu hakuwa amesema kuhusu wafuasi wake: “Wao si sehemu ya ulimwengu, kama vile mimi si sehemu ya ulimwengu”? (Yn. 17:16, NW) Msimamo huu wa kutokuwamo kwa Kikristo si ule ambao ulimwengu kwa ujumla ungeelewa. Lakini je, kweli Mashahidi wa Yehova wangeishi kulingana nao?
Kutokuwamo kwao kulitahiniwa vikali wakati wa Vita ya Ulimwengu 2, kwa kutokeza sana katika Ujerumani. Mwanahistoria Brian Dunn alitaarifu hivi: ‘Mashahidi wa Yehova hawakupatana na Unazi. La maana zaidi ya makatazo ya Nazi kwao lilikuwa kutokuwamo kwao kwa siasa. Hilo lilimaanisha kwamba hakuna mwamini ambaye angechukua silaha, kutumikia katika cheo, kushiriki katika miadhimisho ya umma, au kufanya ishara yoyote ya utii.’ (The Churches’ Response to the Holocaust, 1986) Katika A History of Christianity, Paul Johnson aliongeza hivi: “Wengi walihukumiwa kifo kwa kukataa utumishi wa kijeshi . . . au wakapelekwa Dachau au jela za wenye kichaa.” Ni Mashahidi wangapi katika Ujerumani waliotiwa gerezani? Mashahidi wa Yehova katika Ujerumani waliripoti baadaye kwamba 6,262 kati yao walikuwa wamekamatwa na 2,074 katika hesabu hiyo walikuwa wametiwa katika kambi za mateso. Waandikaji walimwengu kwa kawaida huonyesha tarakimu za juu zaidi.
Katika Uingereza, ambako wote wanaume na wanawake walitiwa katika jeshi, sheria ilikuwa na mpango wa kutoa ruhusa ya kutoingia jeshini; lakini mahakama nyingi ziliwanyima ruhusa hiyo Mashahidi wa Yehova, na mahakimu walipasisha juu yao hukumu za gerezani zilizozidi jumla ya miaka 600. Katika Marekani, mamia ya Mashahidi wa Yehova wakiwa wahudumu Wakristo walipewa ruhusa ya kutoingia katika utumishi wa kijeshi. Wengine zaidi ya 4,000, walionyimwa ruhusa iliyoandaliwa na Sheria ya Utumishi wa Kuteua, walikamatwa na kutiwa gerezani kwa vipindi vya urefu wa kufika miaka mitano. Katika kila nchi duniani, Mashahidi wa Yehova walishikamana na msimamo uleule wa kutokuwamo kwa Kikristo.
Hata hivyo, mtihani wa uhalisi wa kutokuwamo kwao haukukoma vita ilipokwisha. Ijapokuwa hatari ya 1939-1945 ilikuwa imepita, mapigano mengine yalikuja; na hata katika nyakati za amani ya kadiri, mataifa mengi yalichagua kudumisha utumishi wa kijeshi wa lazima. Mashahidi wa Yehova, wakiwa wahudumu Wakristo, waliendelea kukabili vifungo vya gerezani mahali ambapo hawakupewa ruhusa ya kutoingia utumishi wa kijeshi. Katika 1949, wakati John Tsukaris na George Orphanidis walipokataa kuchukua silaha kupigana na wanadamu wenzao, serikali ya Ugiriki iliamuru wauawe. Vitendo (vya aina mbalimbali) vilivyotendwa juu ya Mashahidi wa Yehova katika Ugiriki vilikuwa tena na tena vya kikatili sana hivi kwamba baada ya wakati Baraza la Ulaya (Halmashauri ya Haki za Kibinadamu) lilijaribu kutumia mamlaka yalo kwa niaba yao, lakini kwa sababu ya msongo kutoka Kanisa Orthodoksi la Ugiriki, hata kufikia 1992 mahimizo yao yalikuwa yameepukwa kwa werevu, isipokuwa katika visa chache. Hata hivyo, baadhi ya serikali zililiona kuwa jambo lisilofaa kuendelea kuadhibu Mashahidi wa Yehova kwa sababu ya imani zao za kidini za kidhamiri. Kufikia miaka ya 1990, katika nchi chache, kama vile Sweden, Finland, Poland, Uholanzi, na Argentina, serikali haikuwa ikisonga Mashahidi watendaji washiriki katika utumishi wa kijeshi au utumishi wa lazima wa taifa ulio badala ya wa kijeshi, ingawa kila kisa kilichunguzwa kwa uangalifu.
Katika mahali pamoja baada ya pengine, Mashahidi wa Yehova wamelazimika kukabili hali zilizotatiza kutokuwamo kwao kwa Kikristo. Serikali zilizokuwa zikitawala katika Amerika ya Latin, Afrika, Mashariki ya Kati, Ireland Kaskazini, na kwingineko zimekabili upinzani wa jeuri kutoka kwa majeshi ya kimapinduzi. Likiwa tokeo, serikali na majeshi ya upinzani pia yamesonga Mashahidi wa Yehova waunge mkono kwa tendo. Lakini Mashahidi wa Yehova wamedumisha kutokuwamo kamili. Baadhi yao wamepigwa kikatili, hata kuuawa, kwa sababu ya msimamo waliochukua. Hata hivyo, mara nyingi, kutokuwamo halisi kwa Kikristo kwa Mashahidi wa Yehova kumewapatia staha kutoka kwa maofisa wa pande zote mbili, nao Mashahidi huruhusiwa kuendelea bila kusumbuliwa katika kazi yao ya kuwaambia wengine habari njema juu ya Ufalme wa Yehova.
Katika miaka ya 1960 na ya 1970, kutokuwamo kwa Mashahidi kulipatwa na mitihani ya kinyama kuhusiana na dai la kwamba raia wote wa Malawi wanunue kadi iliyoonyesha uanachama katika chama cha kisiasa chenye kutawala. Mashahidi wa Yehova waliliona jambo hilo kuwa kinyume cha imani zao za Kikristo kushiriki katika hilo. Likiwa tokeo, walipatwa na mnyanyaso usio na kifani katika ukatili wake wenye kuumiza. Makumi ya maelfu walilazimika kutoroka nchi hiyo, na baada ya wakati wengi walirudishwa nchini kwa nguvu wakakabili unyama zaidi.
Wajaponyanyaswa kijeuri, Mashahidi wa Yehova hawajatenda kwa roho ya uasi. Imani zao hazihatarishi serikali yoyote wanayoishi chini yayo. Kwa kutofautisha, Baraza la Makanisa Ulimwenguni limesaidia kifedha mapinduzi, na mapadri Wakatoliki wameunga mkono majeshi ya uviziaji. Lakini ikiwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova angeshiriki katika vitendo vya kimapinduzi, ingekuwa sawa na kukana imani yake.
Ni kweli kwamba Mashahidi wa Yehova huamini kwamba serikali zote za kibinadamu zitaondolewa na Ufalme wa Mungu. Ndivyo inavyotaarifu Biblia kwenye Danieli 2:44. Lakini, kama vile Mashahidi huonyesha, badala ya kusema kwamba wanadamu wangesimamisha Ufalme huo, andiko hilo hujulisha kwamba “Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme.” Vivyo hivyo, wao hueleza kwamba, andiko hilo halisemi kwamba wanadamu wanaruhusiwa na Mungu kutayarishia Ufalme huo njia kwa kuondoa tawala za kibinadamu. Mashahidi wa Yehova hutambua kwamba kazi ya Wakristo wa kweli ni kuhubiri na kufundisha. (Mt. 24:14; 28:19, 20) Kupatana na staha yao kwa Neno la Mungu, rekodi huonyesha kwamba hapana yeyote wao amejaribu kupindua serikali ya aina yoyote popote ulimwenguni, wala hawajapata kamwe kufanya njama ya kumdhuru mkuu yeyote wa umma. Gazeti la habari la Italia La Stampa lilisema kuhusu Mashahidi wa Yehova hivi: “Wao ndio raia walio waaminifu zaidi ambao yeyote angetamani: wao hawaepi kodi wala kutafuta kuchenga sheria zisizowafaa kwa ajili ya faida yao wenyewe.” Hata hivyo, kwa sababu ya kutambua uzito wa jambo hilo machoni pa Mungu, kila mmoja wao ameazimia kwa imara kuendelea kuwa “si sehemu ya ulimwengu.”—Yn. 15:19; Yak. 4:4, NW.
Wakati Mifano ya Kitaifa Ilipopata Kuwa Vitu vya Kuabudiwa
Adolf Hitler alipoingia mamlakani katika Ujerumani, wimbi la kichaa cha kizalendo lilienea ulimwenguni pote. Ili kuwaandikisha watu katika jeshi, ushiriki katika sherehe za kizalendo ulifanywa kuwa wa lazima. Katika Ujerumani kila mtu alitakwa kutoa salamu iliyoamriwa na kupaaza sauti “Heil Hitler!” Huko kulikuwa kusifu Hitler kuwa mwokozi; kulimaanishwa kuwasilishe wazo la kwamba matumaini yote ya watu yalitegemea uongozi wake. Lakini Mashahidi wa Yehova hawangeweza kujiunga katika hisia kama hizo. Wao walijua kwamba ibada yao lazima imwendee Yehova pekee na kwamba Yeye alikuwa amemtokeza Yesu Kristo kuwa Mwokozi wa wanadamu.—Luka 4:8; 1 Yoh. 4:14.
Hata kabla Hitler hajawa dikteta katika Ujerumani, Mashahidi wa Yehova, katika kijitabu The Kingdom, the Hope of the World (kilichotangazwa katika 1931), walikuwa wamepitia kielelezo cha Kimaandiko cha wale waandamani watatu Waebrania wenye ujasiri wa nabii Danieli katika Babiloni. Walipoamriwa na mfalme wainame mbele ya taswira muziki fulani upigwapo, Waebrania hao waaminifu walikuwa wamekataa kuridhiana, naye Yehova alikuwa ameonyesha wazi kibali chake kwa kuwakomboa. (Dan. 3:1-26) Kijitabu hicho kilionyesha kwamba sherehe za kizalendo ziliwakabili Mashahidi wa Yehova katika nyakati za kisasa kukiwa na jaribu kama hilo la uaminifu wao.
Hatua kwa hatua, msukosuko wa sherehe za kizalendo za lazima ulienea kuvuka mipaka ya Ujerumani. Katika Juni 3, 1935, kwenye mkusanyiko katika Washington, D.C., wakati J. F. Rutherford alipoombwa atoe maelezo juu ya kusalimu bendera shuleni, alikazia uaminifu kwa Mungu. Miezi michache baadaye, wakati Carleton B. Nichols, Jr., mwenye miaka minane, wa Lynn, Massachusetts, alipokataa kusalimu bendera ya Marekani na kujiunga katika kuimba wimbo wa kizalendo, jambo hilo liliripotiwa magazetini nchini pote.
Ili aeleze jambo hilo, Ndugu Rutherford alitoa hotuba ya redio katika Oktoba 6 juu ya habari “Kusalimu Bendera,” ambayo alisema hivi: “Kwa watu wengi kusalimu bendera ni sherehe tu na kuna maana kidogo au hakuna maana yoyote. Kwa wale ambao hufikiria jambo hilo kwa maoni ya Kimaandiko, linamaanisha mengi.
“Bendera huwakilisha mamlaka zitawalazo zenye kuonekana. Kujaribu kwa sheria kulazimisha raia au mtoto wa raia asalimu kitu au chochote, au kuimba zile ziitwazo eti ‘nyimbo za kizalendo,’ si haki na ni kosa kabisa. Sheria hutungwa na kufikilizwa ili kuzuia yasitendwe matendo dhahiri ambayo hutokeza dhara kwa mwingine, nazo hazitungwi kwa kusudi la kumlazimisha mtu ahalifu dhamiri yake, na hasa dhamiri hiyo inapoelekezwa kupatana na Neno la Yehova Mungu.
“Kukataa kusalimu bendera, na kusimama kimya, kama vile mvulana huyo alivyofanya, hakungeweza kudhuru yeyote. Ikiwa mtu aamini kwa moyo mweupe kwamba amri ya Mungu hukataza kusalimu bendera, basi kumlazimisha mtu huyo kusalimu bendera kinyume cha Neno la Mungu, na kinyume cha dhamiri yake, humdhuru sana mtu huyo. Serikali haina haki kwa sheria au kwa njia nyingineyo yote kudhuru watu.”
Maelezo zaidi ya sababu za msimamo uliochukuliwa na Mashahidi wa Yehova yaliandaliwa katika kijitabu Loyalty (Uaminifu-Mshikamanifu), kilichotangazwa pia katika 1935. Uangalifu ulielekezwa kwenye maandiko kama yafuatayo: Kutoka 20:3-7, ambalo liliamuru kwamba ibada imwendee Yehova pekee na kwamba watumishi wa Mungu hawakupaswa kufanya au kuinama mbele ya sanamu au mfano wa chochote mbinguni au duniani; Luka 20:25, ambapo Yesu Kristo alielekeza kwamba si vitu vya Kaisari tu vinavyopaswa kurudishiwa Kaisari bali pia vilivyo vya Mungu lazima vitolewe Kwake; na Matendo 5:29 (“NW”), ambapo mitume walitaarifu kwa uthabiti, “Lazima sisi tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.”
Katika Marekani, suala la ufaaji wa kumlazimisha mtu yeyote asalimu bendera lilipelekwa mahakamani. Katika Juni 14, 1943, Mahakama Kuu Zaidi ya Marekani ilibadili uamuzi wayo yenyewe wa hapo mapema na, katika kesi ya West Virginia State Board of Education v. Barnette, ikaamua kwamba kusalimu bendera kwa kulazimishwa hakupatani na hakikisho la uhuru lililoandikwa katika katiba ya taifa lenyewe.b
Suala lihusulo sherehe za utukuzo wa taifa halikuhusu tu Ujerumani na Marekani. Katika Amerika Kaskazini na Kusini, Ulaya, Afrika, na Asia, Mashahidi wa Yehova wamenyanyaswa kikatili kwa sababu ya kutoshiriki kwao, hata ingawa wao husimama kwa heshima wakati wa kusalimu bendera au sherehe kama hizo. Watoto wamepigwa; wengi wamefukuzwa shuleni. Kesi nyingi za mahakama zimeshindaniwa.
Hata hivyo, watazamaji wamehisi kushurutishwa wakiri kwamba, katika hili, kama vile katika mambo mengine, Mashahidi wa Yehova wamethibitika kuwa kama Wakristo wa mapema. Hata hivyo, kama ilivyotaarifiwa katika kitabu The American Character: “Kwa idadi iliyo kubwa sana . . . makatao ya Mashahidi yalikuwa yasiyoeleweka kama yalivyokuwa makatao ya Wakristo [katika Milki ya Kiroma] ya kutotoa dhabihu ya kisherehe kwa Maliki wa Kimungu yalivyokuwa kwa Trajan na Pliny.” Hilo lilipasa kutarajiwa, kwa kuwa Mashahidi wa Yehova, kama vile Wakristo wa mapema, waliona mambo si kama vile ulimwengu uyaonavyo bali kulingana na kanuni za Biblia.
Msimamo Wao Wataarifiwa Waziwazi
Baada ya Mashahidi wa Yehova kuwa wamevumilia mitihani mikali ya kutokuwamo kwao kwa Kikristo kwa miaka mingi Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) la Novemba 1, 1979, lilithibitisha tena msimamo wao. Lilieleza pia sababu ya tendo lililochukuliwa na Mashahidi mmoja-mmoja, liliposema: “Likiwa tokeo la funzo lao la bidii la Neno la Mungu, vijana hao Wakristo waliweza kufanya uamuzi. Hapana mwingine yeyote aliyewafanyia uamuzi huo. Waliweza kuufanya mmoja-mmoja, kwa msingi wa dhamiri ya kila mmoja iliyozoezwa kwa njia ya Biblia. Uamuzi wao ulikuwa kujiepusha na matendo ya chuki na jeuri dhidi ya wanadamu wenzao wa mataifa mengine. Naam, waliamini, na walitaka kushiriki katika utimizo wa unabii wa Isaya ujulikanao sana: ‘Nao watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu; taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe.’ (Isa. 2:4) Vijana hao wa mataifa yote walifanya hivyo hasa.”
Wakati wa miaka ambayo kushikamana kwao na kutokuwamo kwa Kikristo kulipokuwa kukitahiniwa, kuchunguzwa upya kwa yale ambayo Biblia husema, kwenye Warumi 13:1-7 (NW) juu ya “mamlaka zilizo kubwa” kuliongoza kwenye taarifa iliyo wazi zaidi ya uhusiano wa Mashahidi kwa serikali za kilimwengu. Hiyo ilitangazwa katika matoleo ya Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) ya Januari 1, Februari 1, na Machi 1, 1964, na ikathibitishwa tena katika toleo la Novemba 1, 1990. Makala hizo zilikazia cheo cha Yehova Mungu akiwa “Mkuu Kupita Wote,” wakati huohuo zikionyesha kwamba watawala wa kilimwengu ni “mamlaka zilizo kubwa” kwa kuhusiana tu na wanadamu wengine na katika uwanja wao wa utendaji ambao katika huo Mungu huwaruhusu kutenda katika mfumo wa mambo uliopo. Makala hizo zilionyesha uhitaji wa Wakristo wa kweli kuwastahi kwa kudhamiria watawala hao wa kilimwengu na kuwapa utii katika mambo yote ambayo hayapingani na sheria ya Mungu na dhamiri yao iliyozoezwa kwa njia ya Biblia.—Dan. 7:18; Mt. 22:21; Mdo. 5:29; Rum. 13:5, NW.
Kushikamana imara na viwango hivyo vya Biblia kwa Mashahidi wa Yehova kumewapa sifa ya kuwa wenye kujitenga na ulimwengu, sifa inayowakumbusha watu juu ya Wakristo wa mapema.
Ulimwengu Ulipokuwa na Sikukuu Zao
Mashahidi wa Yehova walipoondolea mbali mafundisho ya kidini yaliyokuwa na mianzo ya kipagani, waliacha pia kushiriki katika desturi nyingi ambazo zilikuwa zimechafuliwa vivyo hivyo. Lakini kwa wakati fulani, sikukuu fulani hazikupewa uchunguzi wa uangalifu ziliohitaji. Mojapo hizo ilikuwa ni Krismasi.
Sikukuu hiyo iliadhimishwa kila mwaka hata na washiriki wa wafanyakazi wa makao makuu ya Watch Tower Society kwenye Kao la Betheli katika Brooklyn, New York. Kwa miaka mingi walikuwa wamejua kwamba Desemba 25 haikuwa tarehe sahihi, lakini wakatoa sababu kwamba kwa muda mrefu watu wengi walikuwa wameishirikisha tarehe hiyo na kuzaliwa kwa Mwokozi na kwamba kutendea wengine mema kwafaa siku yoyote. Hata hivyo, baada ya uchunguzi zaidi wa habari hiyo, washiriki wa wafanyakazi wa makao makuu ya Sosaiti, pamoja na wafanyakazi kwenye ofisi za tawi za Sosaiti katika Uingereza na Uswisi, waliamua kuacha kushiriki katika miadhimisho ya Krismasi, hivyo hakuna msherehekeo wa Krismasi uliofanywa huko baada ya 1926.
R. H. Barber, mshiriki wa wafanyakazi wa makao makuu aliyefanya uchunguzi kamili wa chanzo cha desturi za Krismasi na tunda zilizokuwa zikizaa, alitoa matokeo yake katika tangazo la redio. Habari hiyo ilitangazwa pia katika The Golden Age la Desemba 12, 1928. Ulikuwa mfichuo kamili wa mianzo yenye kumvunjia Mungu heshima ya Krismasi. Tangu hapo, mianzo ya kipagani ya desturi za Krismasi imepata kujulikana na umma kwa ujumla, lakini ni watu wachache ambao hufanya mabadiliko katika njia yao ya maisha likiwa tokeo. Kwa upande ule mwingine, Mashahidi wa Yehova wana nia ya kufanya mabadiliko yanayohitajiwa ili wawe wenye kukubalika zaidi wakiwa watumishi wa Yehova.
Walipoonyeshwa kwamba kuzaliwa kwa Yesu kulikuwa kumekuwa kwenye kupendeza zaidi watu wengi kuliko fidia iliyoandaliwa na kifo chake; kwamba kelele za ulevi za sikukuu hiyo na roho ambayo zawadi nyingi zilitolewa hazimheshimu Mungu; kwamba wale wanajimu ambao kutoa zawadi kwao kulikuwa kukiigwa walikuwa kwa kweli wanajimu walioongozwa na mashetani; kwamba wazazi walikuwa wakiwawekea watoto wao kielelezo cha kusema uwongo kwa yale waliyowaambia juu ya Baba Krismasi; kwamba “Mtakatifu Nikolasi” (Baba Krismasi) kwa kweli lilikuwa jina jingine la Ibilisi mwenyewe; na kwamba miadhimisho hiyo ilikuwa, kama vile alivyokiri Kardinali Newman katika kitabu chake Essay on the Development of Christian Doctrine, “vyombo na nyongeza hasa za ibada ya mashetani” ambazo kanisa lilikuwa limekubali—walipojulishwa mambo hayo, Mashahidi wa Yehova waliacha mara hiyo na kwa daima kushiriki sehemu yoyote katika misherehekeo ya Krismasi.
Mashahidi wa Yehova huwa na nyakati za shangwe pamoja na familia na marafiki wao. Lakini hawashiriki katika sikukuu na misherehekeo inayoshirikishwa na miungu ya kipagani (kama ilivyo kwa sikukuu kama vile Ista, Siku ya Mwaka Mpya, Siku ya Mei, na Siku ya Mama). (2 Kor. 6:14-17) Kama vile Wakristo wa mapema,c wao hata hawaadhimishi siku za kuzaliwa. Pia kwa staha wao huepuka kushiriki katika sikukuu za kitaifa ambazo hufanya kumbukumbu ya matukio ya kisiasa au ya kijeshi na huepuka kuwapa heshima ya kiibada mashujaa wa kitaifa. Kwa nini? Kwa sababu Mashahidi wa Yehova si sehemu ya ulimwengu.
Kuwasaidia Wanadamu Wenzao
Kuheshimu mno miungu kulikuwa ndicho kiini cha maisha ya kijamii na ya kitamaduni ya Milki ya Kiroma. Kwa kuwa Wakristo waliepuka kushiriki katika chochote kilichotiwa waa na miungu ya kipagani, watu waliuona Ukristo kuwa dharau kwa njia yao ya maisha; na kulingana na mwanahistoria Tacitus, Wakristo walisemekana kuwa wachukia wanadamu. Akiwasilisha hisia kama hiyo, Minucius Felix, katika maandishi yake, hunukuu Mroma mmoja akisema hivi kwa Mkristo aliyemjua: “Nyinyi hamhudhurii maonyesho; hamshiriki sehemu katika maandamano . . . mwakirihi michezo mitakatifu.” Jamii ya watu wa ulimwengu wa Kiroma ya kale haikuwaelewa sana Wakristo.
Vivyo hivyo leo, wengi katika ulimwengu hawawaelewi Mashahidi wa Yehova. Huenda watu wakasifu viwango vya juu vya kiadili vya Mashahidi lakini wahisi kwamba Mashahidi wapaswa kushiriki pamoja na ulimwengu unaowazunguka katika utendaji wao mbalimbali na kujihusisha katika kusaidia kufanya ulimwengu kuwa mahali bora zaidi. Hata hivyo, wale wapatao kuwajua Mashahidi wa Yehova kwa kushuhudiwa wenyewe hupata kujua kwamba kuna sababu ya Kibiblia kwa kila jambo wafanyalo.
Kuliko kujifungia mbali wenyewe na wengine wa wanadamu, Mashahidi wa Yehova hutumia maisha yao katika kusaidia wanadamu wenzao katika njia ambayo Yesu Kristo aliwekea kielelezo. Wao husaidia watu kujifunza jinsi ya kukabiliana kwa mafanikio na matatizo ya maisha sasa kwa kuwafahamisha kwa Muumba na kwa miongozo ya maisha iliyoonyeshwa katika Neno lake lililopuliziwa. Wao hushiriki pamoja na majirani bila malipo kweli za Biblia ziwezazo kugeuza maoni yote ya mtu juu ya maisha. Kiini cha imani yao ni kujua kwamba “ulimwengu unapilitia mbali,” na kwamba upesi Mungu atajiingiza ili kukomesha mfumo mwovu wa mambo uliopo, na kwamba wakati ujao mtukufu wawangojea wale waendeleao kuwa si wa ulimwengu na kuweka imani yao kamili katika Ufalme wa Mungu.—1 Yoh. 2:17, NW.
[Maelezo ya Chini]
a The Watch Tower, Juni 1, 1918, uku. 17.
b Kwa habari zaidi, ona Sura ya 30, “Kutetea na Kuthibitisha Kisheria Habari Njema.”
c The History of the Christian Religion and Church, During the Three First Centuries, cha Augustus Neander, uku. 190.
[Blabu katika ukurasa wa 188]
Hawajitengi na watu, lakini hawashiriki namna ya maisha ya ulimwengu
[Blabu katika ukurasa wa 189]
Walijiondoa katika makanisa ya Jumuiya ya Wakristo
[Blabu katika ukurasa wa 190]
“Wakristo hawakujihusisha na walikuwa tofauti na serikali”
[Blabu katika ukurasa wa 194]
Kutokuwamo kwa Kikristo kulitahiniwa
[Blabu katika ukurasa wa 198]
‘Hakuna mwingine aliyewafanyia uamuzi’
[Blabu katika ukurasa wa 199]
Sababu iliyofanya waache kuadhimisha Krismasi
[Sanduku katika ukurasa wa 195]
Si Tisho kwa Serikali Yoyote
◆ Ilipokuwa ikiandika juu ya walivyotendewa Mashahidi wa Yehova katika nchi moja ya Amerika ya Latini, tahariri moja katika “World-Herald” la Omaha, Nebraska, Marekani, ilisema: “Yataka uwazio wa ushupavu wa upande mmoja na hofu isiyo na msingi kuamini kwamba Mashahidi wa Yehova hutokeza tisho la aina yoyote kwa serikali yoyote ya kisiasa; wao si wataka-mapinduzi na ni wapenda amani wakiwa kikundi cha kidini kadiri iwezekanavyo, nao huomba tu kwamba waruhusiwe kufuatia imani yao kwa njia yao wenyewe.”
◆ “Il Corriere di Trieste,” gazeti moja la habari la Italia, lilitaarifu hivi: “Mashahidi wa Yehova wapasa kusifiwa kwa ajili ya imara na ushikamano wao. Tofauti na dini nyinginezo, umoja wao wakiwa kikundi cha watu huwazuia kutosali kwa Mungu yuleyule mmoja, katika jina la Kristo yuleyule mmoja, abariki pande mbili zenye kupingana katika pigano, au kutochanganya siasa na dini ili kutumikia masilahi ya Kiongozi wa Serikali au vyama vya kisiasa. La mwisho lakini lenye umaana uleule, wako tayari kukabili kifo kuliko kuvunja . . . ile amri USIUE!”
◆ Baada ya Mashahidi wa Yehova kuwa wamevumilia marufuku ya miaka 40 katika Chekoslovakia, gazeti la habari “Nová Svoboda” lilisema hivi, katika 1990: “Imani ya Mashahidi wa Yehova huwakataza kutumia silaha dhidi ya wanadamu, na wale waliokataa utumishi wa msingi wa kijeshi na hawakufanya kazi katika migodi ya makaa-mawe walikwenda gerezani, hata kwa miaka minne. Kutokana na hilo tu ni wazi kwamba wana imara kubwa ya kiadili. Tungeweza kutumia watu kama hao wasio na ubinafsi hata katika shughuli za kisiasa za juu kabisa—lakini hatutaweza kamwe kuwaingiza humo. . . . Bila shaka, watambua mamlaka za kiserikali lakini waamini kwamba ni Ufalme wa Mungu tu uwezao kutatua matatizo yote ya kibinadamu. Lakini usikosee—wao hawashikilii mambo bila kutumia akili. Ni watu ambao hujishughulisha sana na wanadamu.”
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 200, 201]
Mazoea Ambayo Yameachwa Kabisa
Msherehekeo huu wa Krismasi kwenye Betheli ya Brooklyn katika 1926 ulikuwa ndio wao wa mwisho. Wanafunzi wa Biblia walikuja kufahamu hatua kwa hatua kwamba wala mwanzo wa sikukuu hiyo wala mazoea yaliyoshirikishwa nayo hayakumheshimu Mungu
Kwa miaka mingi, Wanafunzi wa Biblia walivaa msalaba na taji kuwa beji ya utambulisho, na ishara hiyo ilikuwa katika jalada la mbele la “Watch Tower” tokea 1891 hadi 1931. Lakini katika 1928 ilikaziwa kwamba si ishara ya kupamba bali utendaji wa mtu akiwa shahidi ndio ulioonyesha kuwa alikuwa Mkristo. Katika 1936 ilionyeshwa kwamba uthibitisho huonyesha kwamba Kristo alikufa juu ya mti, si juu ya msalaba wenye maboriti mawili
Katika kitabu chao “Daily Manna,” Wanafunzi wa Biblia waliweka orodha ya siku za kuzaliwa. Lakini baada ya wao kuacha kuadhimisha Krismasi na wakati walipopata kujua kwamba misherehekeo ya kuzaliwa ilikuwa ikitoa kwa viumbe heshima isivyostahili (hiyo ikawa sababu moja Wakristo wa mapema hawakusherehekea kamwe siku za kuzaliwa), Wanafunzi wa Biblia waliacha zoea hilo vilevile
Kwa miaka ipatayo 35, Pasta Russell alifikiri kwamba ile Piramidi Kubwa ya Gizeh ilikuwa lile jiwe la ushahidi la Mungu, ikiunga mkono vipindi vya wakati wa Biblia. (Isa. 19:19) Lakini Mashahidi wa Yehova wameacha wazo la kwamba piramidi fulani ya Misri ina uhusiano wowote na ibada ya kweli. (Ona “Mnara wa Mlinzi” matoleo ya Novemba 15 na Desemba 1, 1928, Kiingereza)
[Picha katika ukurasa wa 189]
Nakala milioni kumi ziligawanywa
[Picha katika ukurasa wa 191]
Baadhi yao walikwenda katika mahandaki wakiwa na bunduki, lakini wengine, kutia ndani A. P. Hughes wa Uingereza, na R. Cuminetti wa Italia, walikataa kujihusisha kama huko
[Picha katika ukurasa wa 193]
Mashahidi wa Yehova walikataa kukubali Ushirika wa Mataifa au UM kuwa watoka kwa Mungu bali walitetea tu Ufalme wa Mungu kupitia Kristo
[Picha katika ukurasa wa 197]
Carleton na Flora Nichols. Wakati mwana wao alipoepuka kusalimu bendera, hilo likawa habari za taifa zima
-