-
Mungu Anaweza Kukusaidia Ujitayarishe kwa Ajili ya Siku Yake KuuIzingatie Siku ya Yehova Maishani
-
-
SEHEMU 1
Mungu Anaweza Kukusaidia Ujitayarishe kwa Ajili ya Siku Yake Kuu
Nabii mmoja wa Mungu alisema: “Ile siku kuu ya Yehova iko karibu.” (Sefania 1:14) Siku hiyo inakaribia haraka, nasi tunapaswa kuzingatia hilo akilini nyakati zote. Je, unajua kwamba wale wanaoitwa Manabii Wadogo wana jambo la kukujulisha kuhusu siku hiyo kuu? Sura ya 1 hadi ya 3 ya kitabu hiki itakusaidia kuwajua vizuri manabii hao 12 na ujumbe ulio katika vitabu vyao. Hivyo, unaweza kufaidika kutokana na mambo waliyoandika, na kupata mafundisho muhimu yanayoweza kukusaidia maishani mwako.
-
-
Mjue Yehova na UmtumikieIzingatie Siku ya Yehova Maishani
-
-
SEHEMU 2
Mjue Yehova na Umtumikie
Vile vitabu vya manabii 12 vina ujumbe gani unaotuchochea kutaka kumjua Yehova vizuri zaidi? Kwa nini ujumbe wa Yehova uliotolewa na manabii hao ni muhimu leo? Katika Sura ya 4 hadi ya 7 ya kitabu hiki, utajifunza jinsi unavyopaswa kumwabudu Mungu na kufuata viwango vyake. Kwa mfano, anataka uonyesheje haki unaposhughulika na wengine? Naam, utaona kwamba vitabu hivi 12 vya kinabii vinaweza kuboresha maisha yako leo.
-
-
Mpendeze Mungu Katika Mwenendo na Shughuli ZakoIzingatie Siku ya Yehova Maishani
-
-
SEHEMU 3
Mpendeze Mungu Katika Mwenendo na Shughuli Zako
Ungejibuje ikiwa ungeulizwa, “Yehova anataka nini kutoka kwako?” (Mika 6:8) Mambo yaliyoandikwa na wale manabii 12 yanatusaidia kupata jibu la swali hilo. Kama utakavyoona katika Sura ya 8 hadi ya 10 ya kitabu hiki, vitabu hivyo vinaweza kukusaidia kujua jinsi unavyoweza kuwa msema-kweli nyakati zote na jinsi unavyoweza kuepuka jeuri. Utaona pia kwamba vitabu hivyo vina mashauri mazuri unayoweza kutumia kuhusu maisha ya familia.
-
-
Ingojee Siku ya Yehova kwa ShangweIzingatie Siku ya Yehova Maishani
-
-
SEHEMU YA 4
Ingojee Siku ya Yehova kwa Shangwe
Yehova aliwatumia manabii wake kuonya kuhusu jambo ambalo lingetokea wakati ujao, yaani, kumwagwa kwa hasira yake. Lakini hatupaswi kumwona kuwa Mungu mwenye hasira. Yeye ‘huwashangilia watu wake kwa vilio vya furaha.’ Tunapotazamia siku yake kuu, tuna kila sababu ya ‘kushangilia na kufurahia kwa moyo wote.’ (Sefania 3:14, 17) Utaonyeshaje hivyo kwa matendo na mtazamo wako? Kwa nini ushukuru kwa sababu ya mambo unayojifunza katika vile vitabu 12 vya kinabii?
-
-
Ujumbe wa Yehova wa Wakati Uliopita na LeoIzingatie Siku ya Yehova Maishani
-
-
SURA YA KWANZA
Ujumbe wa Yehova wa Wakati Uliopita na Leo
1, 2. Watu fulani hutafutaje hazina zilizofichika, lakini ni nini kinachoweza kukusaidia kuwa na furaha maishani?
MIAKA nenda miaka rudi, watu wengi wamekuwa wakitumaini kupata hazina zilizofichika. Je, umewahi kusoma masimulizi ya historia kuhusu wavumbuzi, waakiolojia, na wengine ambao wamekuwa wakitafuta hazina kama hizo? Huenda wewe binafsi huzitafuti, hata hivyo, ingekuwaje kama ungepata hazina fulani? Bila shaka, ungeridhika na kushukuru sana hasa ikiwa hazina hiyo ingeyaboresha maisha yako na kuyafanya yawe yenye furaha na yenye mafanikio zaidi.
2 Kwa kawaida si watu wengi hutafuta hazina halisi, hata hivyo, wengi hujitahidi kupata furaha kwa kutafuta pesa, afya bora, na ndoa yenye furaha, hazina ambazo hazipatikani kwa kuchimba kihalisi. Hakuna ramani halisi inayoonyesha jinsi ya kupata hazina hizo. Kama ujuavyo, jitihada zinahitajiwa ili kupata hazina hizo. Ndiyo sababu wengi huthamini mashauri mazuri kuhusu jinsi ya kufikia miradi yao na kufanya maisha yao yawe yenye furaha na yenye mafanikio zaidi.
3, 4. Ni wapi unapoweza kupata mashauri mazuri kuhusu maisha?
3 Kwa kweli, unaweza kupata mashauri mazuri, yaani mwongozo ambao tayari umewasaidia wengine kuwa na furaha. Biblia inatoa mashauri bora zaidi kuhusu maisha, na watu wengi wametambua hivyo. Mwandishi Mwingereza Charles Dickens alisema hivi kuhusu Biblia: “Ndicho kitabu bora zaidi kilichopata na kitakachopata kujulikana ulimwenguni . . . kwa kuwa kina mafundisho bora zaidi ambayo mwanadamu yeyote yule . . . anaweza kuongozwa nayo.”
4 Maoni hayo hayawashangazi hata kidogo wale wote wanaoiona Biblia kuwa imeongozwa na roho ya Mungu. Huenda unakubaliana na maneno tunayosoma kwenye 2 Timotheo 3:16: “Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu.” Yaani, Biblia ina habari muhimu sana inayoweza kuwaonyesha watu jinsi ya kuishi katika ulimwengu wa leo wenye misukosuko mingi. Wale ambao hutii mashauri ya Biblia wanaweza kuwa na maisha ambayo kwa kweli ni yenye furaha na yenye mafanikio zaidi.
5-7. Ni sehemu gani za Biblia zinazoweza kukufaidi?
5 Hata hivyo, unafikiri ni katika vitabu gani vya Biblia unamoweza kupata mashauri hayo? Huenda watu fulani wakafikiri ni katika yale Mahubiri ya Mlimani, ambapo Yesu alitoa mashauri mazuri kuhusu nyanja mbalimbali za maisha ya kila siku. Huenda wengine wakafikiri ni katika vitabu vilivyoandikwa na mtume Paulo. Isitoshe, mtu anaweza kupata mashauri mazuri katika Zaburi na Methali—vitabu vilivyojaa hekima. Kwa kweli, ikitegemea hali na matatizo unayokabili, kitabu chochote cha Biblia chaweza kukusaidia, hata vitabu vya Biblia ambavyo vina mambo ya kihistoria hasa, vitabu kama vile Yoshua hadi Esta. Historia iliyomo ina maonyo kwa kila mmoja anayejitahidi kumtumikia Mungu kwa furaha. (1 Wakorintho 10:11) Naam, vitabu hivyo vina mashauri unayoweza kutumia kuongoza hatua zako ili kufanikisha maisha yako. Kumbuka kwamba “mambo yote yaliyoandikwa zamani yaliandikwa ili kutufundisha sisi, ili kupitia uvumilivu wetu na kupitia faraja kutokana na Maandiko tuwe na tumaini.”—Waroma 15:4; Yoshua 1:8; 1 Nyakati 28:8, 9.
6 Hata hivyo, kuna sehemu ya Biblia ambayo kwa wengi ni kama eneo lenye hazina ambalo halijavumbuliwa bado. Sehemu hiyo ni vile vitabu 12 ambavyo mara nyingi huitwa Manabii Wadogo. Kwa kawaida vitabu hivyo hufuata vile vitabu vikubwa zaidi vya Biblia kama vile Ezekieli na Danieli lakini vinatangulia Injili ya Mathayo. (Katika Biblia nyingi, vitabu hivyo 12 vinafuatana hivi: Hosea, Yoeli, Amosi, Obadia, Yona, Mika, Nahumu, Habakuki, Sefania, Hagai, Zekaria, na Malaki.) Kama tulivyoona, Biblia imeongozwa na roho ya Mungu, nayo inafaa kwa kufundisha na kuwaonyesha watu jinsi ya kuishi. Je, hilo linatia ndani vitabu hivyo?
7 Bila shaka! Kwa kweli, vile vitabu vinavyoitwa Manabii Wadogo vina hazina zinazoweza kutuonyesha jinsi ya kuishi leo. Ili kuelewa ni kwa nini watu fulani hupuuza vitabu hivyo, hebu fikiria jina la vitabu hivyo 12 katika lugha nyingi: vinaitwa Manabii Wadogo. Je, jina hilo laweza kuathiri maoni ya watu kuhusu vitabu hivyo? Je, huenda maoni yako kuhusu vitabu hivyo yakawa yameathiriwa kwa kiasi fulani?
JE, WALE “MANABII WADOGO” NI WADOGO KWELI?
8. (a) Mungu hutumia njia gani muhimu kutoa mwongozo? (b) Vile vitabu 12 vinavyozungumziwa huitwaje mara nyingi, hata hivyo, jina hilo linamaanisha nini?
8 Katika barua aliyowaandikia Waebrania, mtume Paulo alianza kwa kusema hivi: “Mungu, ambaye zamani za kale alisema katika pindi nyingi na katika njia nyingi na mababu zetu kupitia manabii, mwishoni mwa siku hizi amesema nasi kupitia Mwana.” (Waebrania 1:1, 2) Kwa kuwa Mungu alitumia manabii wa kibinadamu kuwasilisha ujumbe wake, hatupaswi kamwe kumwona yeyote kati yao au ujumbe wao kuwa “mdogo.” Hata hivyo, jina “Manabii Wadogo” limewafanya watu fulani wazione habari zilizo katika vitabu hivyo kuwa zenye maana ndogo. Wengine wamekata kauli kwamba ujumbe ulio katika vitabu hivyo si muhimu sana kama ule ulio katika vitabu vingine vya Biblia. Hata hivyo, ukweli ni kwamba katika lugha nyingi jina “Manabii Wadogo”a humaanisha tu kwamba vitabu hivyo 12 ni vifupi kuliko vitabu vingine.
9. Kwa nini umuhimu wa kitabu fulani cha Biblia hautegemei urefu wake?
9 Kwa kuwa tu kitabu fulani ni kifupi, haimaanishi kwamba hakina umuhimu wowote kwako. Kitabu cha Ruthu ni kifupi kuliko vitabu vinavyotangulia na vinavyofuata, hata hivyo, habari zilizomo ni zenye kuchochea kwelikweli! Kitabu hicho kifupi hukazia jinsi tunavyopaswa kushikamana na ibada ya kweli, huonyesha jinsi Mungu anavyowathamini sana wanawake, nacho huandaa habari muhimu kuhusu ukoo wa Yesu. (Ruthu 4:17-22) Mfano mwingine ni ule wa kitabu cha Yuda kilicho karibu na mwisho wa Biblia. Ni kifupi sana hivi kwamba katika Biblia fulani zilizochapishwa, hakijazi hata ukurasa mmoja. Hata hivyo, habari na mwongozo uliomo ni wenye thamani sana. Kinaonyesha jinsi Mungu alivyoshughulika na malaika waovu, maonyo kuhusu watu wafisadi waliojipenyeza kutanikoni, na mahimizo ya kuipigania vikali imani! Kwa hiyo basi, unaweza kuwa na uhakika kwamba ingawa vitabu vya wale wanaoitwa Manabii Wadogo ni vifupi, habari zilizomo na faida unayoweza kupata si ndogo.
VYA KINABII—JINSI GANI?
10, 11. (a) Watu fulani hufikiri nini wanaposikia neno “manabii”? (b) Kulingana na Biblia, manabii walikuwa nani, nao walifanya nini?
10 Jambo lingine la kuzingatia ni yale maneno “manabii” na “kinabii.” Huenda maneno hayo yakaleta wazo la kutabiri kuhusu wakati ujao. Watu wengi hufikiri kwamba kazi ya nabii ni kutabiri matukio ya wakati ujao, na kwamba huenda yeye hufanya hivyo kwa kutumia maneno ya kifumbo yanayoweza kufasiriwa katika njia mbalimbali. Mawazo hayo huathiri jinsi watu fulani huviona vitabu hivyo 12.
11 Ni kweli kwamba unaposoma vitabu hivyo 12, muda si muda utaona vina matabiri mengi, na mengi ya matabiri hayo yanahusu kuja kwa ile siku kuu ya Yehova. Hilo linapatana na maana ya msingi ya neno “nabii.” Nabii ni mtu aliyekuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu na mara nyingi alitumiwa kufunua mambo ambayo yangetokea. Kuanzia Enoko, manabii wengi wa Biblia walitabiri kuhusu wakati ujao.—1 Samweli 3:1, 11-14; 1 Wafalme 17:1; Yeremia 23:18; Matendo 3:18; Yuda 14, 15.
12. Unaweza kuonyeshaje kwamba neno nabii linatia ndani mengi zaidi ya kutabiri mambo?
12 Hata hivyo, twahitaji kukumbuka kwamba kazi ya manabii wa Yehova haikuwa tu kutabiri ujumbe wa Mungu. Mara nyingi Mungu aliwatumia manabii wakiwa wasemaji ili kuwaambia wengine mapenzi yake. Kwa mfano, huenda tusiwaone Abrahamu, Isaka, na Yakobo kama watu waliotabiri kuhusu wakati ujao, hata hivyo, andiko la Zaburi 105:9-15 huwaita manabii. Nyakati nyingine, Mungu aliwatumia kufunua jambo fulani la wakati ujao, kama wakati ambapo Yakobo aliwabariki wanawe. Lakini wazee hao wa ukoo walikuwa manabii pia kwa kuwa waliziambia familia zao mambo ambayo Yehova alisema kuhusu jukumu lao katika kutimiza kusudi la Mungu. (Mwanzo 20:7; 49:1-28) Jambo lingine linaloweza kutusaidia kuelewa jinsi Biblia hutumia neno “nabii” ni kwamba Haruni alikuwa nabii wa Musa. Haruni alitimiza jukumu la nabii kwa kuwa msemaji wa, au “kinywa” cha Musa.—Kutoka 4:16; 7:1, 2; Luka 1:17, 76.
13, 14. (a) Mbali na kutabiri, manabii walifanya mambo gani mengine? (b) Unaweza kufaidikaje kwa kujua kwamba kazi ya manabii haikuwa tu kutabiri?
13 Pia, wafikirie manabii Samweli na Nathani. (2 Samweli 12:25; Matendo 3:24; 13:20) Yehova aliwatumia kutangaza mambo ambayo yangetokea wakati ujao, hata hivyo, aliwatumia kama manabii katika njia nyinginezo. Akiwa nabii, Samweli aliwahimiza Waisraeli waache ibada ya sanamu na kurudia ibada safi. Naye alitangaza hukumu ya Mungu dhidi ya Mfalme Sauli, jambo linalotufundisha kwamba Yehova huthamini utii kuliko dhabihu za kimwili. Ndiyo, kazi ya unabii ya Samweli ilitia ndani kutangaza maoni ya Mungu kuhusu njia bora ya kuishi. (1 Samweli 7:3, 4; 15:22) Nabii Nathani alitabiri kwamba Sulemani angejenga hekalu na kwamba ufalme wake ungekuwa imara. (2 Samweli 7:2, 11-16) Hata hivyo, Nathani alikuwa pia akifanya kazi ya nabii alipotaja dhambi ya Daudi na Bath-sheba na dhambi ya Daudi dhidi ya Uria. Ni nani anayeweza kusahau jinsi Nathani alivyoufunua uzinzi wa Daudi kwa kutumia mfano wa tajiri mmoja aliyemchukua mwana-kondoo mpendwa na wa pekee wa maskini mmoja? Nathani pia alikuwa na jukumu la kupanga ibada ya kweli katika patakatifu pa Mungu.—2 Samweli 12:1-7; 2 Mambo ya Nyakati 29:25.
14 Jambo kuu ni kwamba hatupaswi kuona ujumbe ulio katika vitabu hivyo vya kinabii kana kwamba ni matabiri tu ya wakati ujao. Vitabu hivyo vina ujumbe wa Mungu kuhusu mambo mengine mengi, kutia ndani habari nyingi kuhusu jinsi watu wa Mungu wa wakati uliopita walivyopaswa kuishi na jinsi sisi leo tunavyopaswa kuishi. Kwa hiyo, tuna hakika kwamba habari zilizo katika Biblia, kutia ndani vitabu hivyo 12, ni muhimu sana na zenye faida, na huwasaidia watu kuona jinsi ya kuishi maisha bora. Vitabu hivyo vilivyoongozwa kwa roho ya Mungu hutupa mwongozo muhimu sana unaoweza kutusaidia “tuishi kwa utimamu wa akili na uadilifu na ujitoaji-kimungu katikati ya mfumo wa mambo wa sasa.”—Tito 2:12.
JINSI UNAVYOWEZA KUFAIDIKA
15, 16. (a) Ni mambo gani ya mfano yanayoweza kupatikana katika vitabu vinavyoitwa “Manabii Wadogo”? (b) Ni mambo gani ya kinabii yaliyo katika vitabu hivyo?
15 Tunaweza kufaidika kwa njia mbalimbali tunaposoma Neno la Mungu lililoongozwa kwa roho. Vitabu fulani vya Biblia hutuambia mambo yaliyotokea wakati fulani, vingine ni vya kishairi, na kila kimoja kina ubora wa pekee. Pia kuna vingine vilivyo na habari za mfano au zinazowakilisha mambo ya baadaye, kama vile vitabu hivyo 12. Kwa mfano, Yesu alikuwa akirejelea kitabu cha Yona aliposema: “Kizazi kiovu na chenye uzinzi kinaendelea kutafuta ishara, lakini hakuna ishara kitakachopewa isipokuwa ishara ya nabii Yona. Kwa maana kama vile Yona alivyokuwa katika tumbo la yule samaki mkubwa siku tatu mchana na usiku, ndivyo Mwana wa binadamu atakavyokuwa katika moyo wa dunia siku tatu mchana na usiku. Watu wa Ninawi watasimama katika hukumu pamoja na kizazi hiki nao watakihukumu kuwa chenye hatia; kwa sababu wao walitubu juu ya lile alilohubiri Yona, lakini, tazama! mtu mkuu kuliko Yona yuko hapa.”—Mathayo 12:39-41.
16 Ni wazi kwamba Yesu hakukiona kitabu cha Yona kuwa historia tu ya jinsi Mungu alivyoshughulika na Yona, ya utendaji wa nabii huyo huko Ninawi, na matokeo ya kazi ya Yona ya kutangaza ujumbe wa kuonya wa Mungu. Yesu alitambua kwamba nabii Yona alimwakilisha Yesu Kristo, na pia kufa na kufufuliwa kwake siku ya tatu. Isitoshe, itikio la Waninawi lilikuwa tofauti kabisa na jinsi Wayahudi wengi walivyoitikia mahubiri ya Yesu na kazi alizofanya. (Mathayo 16:4) Basi, tunaelewa kwamba vitabu hivyo 12 vina mambo ya kinabii, au yanayowakilisha jinsi Mungu anavyoshughulika na watu wake leo. Kujifunza mambo hayo ni jambo lenye kupendeza na lenye faida.b
17. Kitabu hiki kinazungumziaje vile vitabu 12?
17 Hata hivyo, kitabu hiki hakikukusudiwa kuzungumzia mifano na ulinganifu mbalimbali wa kitabu cha Yona wala wa vile vitabu vingine 11. Pia, hakichanganui vitabu hivyo mstari kwa mstari. Badala yake, kinazingatia hasa ujumbe ulio katika vitabu hivyo ambao tunaweza kutumia katika maisha yetu ya kila siku. Jiulize hivi: ‘Katika vitabu hivyo 12, ni mwongozo gani mzuri au ni shauri gani ambalo Yehova ananiandalia? Vitabu hivyo vinaweza kunisaidiaje “niishi kwa utimamu wa akili na uadilifu na ujitoaji-kimungu katikati ya mfumo wa mambo wa sasa”? Vinaniambia nini kuhusu maisha ya Kikristo, maadili, maisha ya familia, na mitazamo ya watu katika siku hizi za hatari, kwa kuwa “siku ya Yehova inakuja,” nayo “iko karibu”?’ (Tito 2:12; Yoeli 2:1; 2 Timotheo 3:1) Unapopata majibu yenye kuridhisha, haikosi utapata mistari kadhaa utakayothamini sana, mistari ambayo hukuwa umeitumia kufikia sasa kuwapa wengine kuhusu shauri la Biblia. Kwa kufanya hivyo, hazina yako ya maandiko ya Biblia itaongezeka.—Luka 24:45.
18. Kitabu hiki kimepangwaje, nawe unaweza kufaidikaje?
18 Sura za kitabu hiki zimepangwa katika sehemu nne. Jaribu kuona mambo makuu ya kila sehemu unapoianza. Katika kila moja ya sura 13 zinazofuata, utaona masanduku mawili ambayo yamekusudiwa kukusaidia kukazia fikira mambo ambayo umejifunza. Maswali yaliyo katika masanduku hayo yatakuwezesha kutafakari mambo ambayo umesoma na kuzingatia faida na matumizi yake. Sanduku la kwanza liko karibu katikati ya sura. Unapofika mahali lilipo, fikiria maswali yaliyomo. Kufanya hivyo kutakusaidia kukaza kabisa moyoni mwako mambo ambayo umejifunza. (Mathayo 13:8, 9, 23; 15:10; Luka 2:19; 8:15) Sanduku la pili litakuwezesha kutafakari mambo ambayo umesoma katika sehemu ya mwisho ya sura hiyo na kuyaongeza katika hazina yako ya mambo unayojua. Kwa hiyo, tenga wakati wa kutafakari mambo yaliyo katika masanduku hayo. Yanaweza kukusaidia sana kuona jinsi unavyoweza kufaidika na habari ambayo unajifunza.
19. Ni habari gani unayohitaji kujua kwanza kuhusu vile vitabu 12?
19 Ili kujitayarisha kwa sura inayofuata, jiulize mwenyewe ni mambo gani unayojua kuhusu habari zilizomo katika vitabu hivyo 12. Mungu alitoa ujumbe huo kupitia nani, nao walikuwa watu wa aina gani? Waliishi pindi gani, na hali zilikuwaje? (Chati iliyo katika ukurasa wa 20 na 21 itakusaidia sana; irejelee mara kwa mara unapojifunza sura zinazofuata.) Ujumbe wenyewe ulikuwa na kusudi gani wakati huo, na kujua hilo kwawezaje kukusaidia kuelewa habari hiyo katika muktadha wake? Sura inayofuata itajibu maswali hayo ya msingi.
a Kichapo Encyclopaedia Judaica chataja kwamba jina hilo “yaonekana latokana na jina la Kilatini lililo katika Vulgate (Prophetae Minores). Kivumishi ‘-dogo’ katika jina ‘Manabii Wadogo’ hakimaanishi kwamba wale manabii 12 hawakuwa muhimu kwa kuwalinganisha na Isaya, Yeremia, na Ezekieli, badala yake charejelea ufupi wa vitabu hivyo.”—Buku la 12, ukurasa wa 49.
b Kwa mfano, ona jinsi vitabu vya Hagai na Zekaria vinavyojadiliwa katika kitabu Paradise Restored to Mankind—By Theocracy! kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova ingawa kwa sasa hakichapishwi tena.
-
-
Manabii Waliotangaza Ujumbe UnaotuhusuIzingatie Siku ya Yehova Maishani
-
-
SURA YA PILI
Manabii Waliotangaza Ujumbe Unaotuhusu
1. Kwa nini unapaswa kupendezwa na wale manabii 12 walioandika vitabu vya mwisho vya Maandiko ya Kiebrania?
JE, UNGEPENDA kuwajua wajumbe 12 wa Mungu? Wajumbe hao 12 waliishi kabla Yesu hajaja duniani, kwa hiyo huwezi kuonana nao uso kwa uso. Hata hivyo, unaweza kuwajua na kuona jinsi walivyoweka karibu akilini “ile siku kuu ya Yehova.” Mambo utakayojifunza ni muhimu sana kwa kila Mkristo ambaye kwa hekima anajitahidi kuiweka akilini siku kuu ya Yehova.—Sefania 1:14; 2 Petro 3:12.
2, 3. Kuna ulinganifu gani kati ya maisha yetu na ya wale manabii 12?
2 Maandiko yanawataja manabii wengi sana, vitabu vingi vya Biblia vinaitwa kwa majina ya manabii. Kama wale manabii wengine, manabii 12 tutakaozungumzia wanatuwekea mfano katika kuwa waaminifu na wenye ujasiri. Baadhi yao walifurahi sana kuona ujumbe wao ukibadili mioyo na akili za watu, na kuwasaidia wamrudie Mungu. Wengine waliumia sana moyoni walipowaona waasi wakivunja viwango vya Yehova na kupinga mapenzi yake. Baadhi ya manabii hao 12 walivunjika moyo sana walipowaona wale waliodai kuwa waabudu wa Yehova wakiponda raha na kupuuza ujumbe wao.
3 Manabii hao 12 waliishi nyakati kama zetu zenye misukosuko ya kisiasa, migogoro ya kijamii, na kuzorota kwa hali ya kidini. Kwa kuwa, walikuwa watu wenye “hisia kama zetu,” hapana shaka kwamba walikuwa na mahangaiko na matatizo yao. (Yakobo 5:17) Hata hivyo, walituwekea mfano mzuri, na ujumbe wao unapaswa kuchukuliwa kwa uzito, kwa kuwa umeandikwa katika “maandiko ya kinabii” ili kutufaidi sisi ambao “tumefikiwa na miisho ya mifumo ya mambo.”—Waroma 15:4; 16:26; 1 Wakorintho 10:11.
MANABII 12 NA NYAKATI WALIZOISHI
4. Wale manabii 12 waliishi wakati gani, na Yehova aliwatumia nani kwanza kati yao ili kuwaonya na kuwahimiza watu wake?
4 Huenda ukafikiri kwamba kwa kuwa katika Biblia yako vitabu vya Hosea hadi Malaki vinafuatana, basi vimepangwa kulingana na wakati ambao manabii hao waliishi. Sivyo ilivyo. Kwa mfano, nabii Yona, Yoeli, Amosi, Hosea, na Mika waliishi katika karne ya tisa na ya nane K.W.K.a Wakati huo, wafalme wengi katika ufalme wa kusini wa Yuda na ufalme wa kaskazini wa Israeli hawakuwa waaminifu. Na raia wao waliiga mfano wao, hivyo wakaadhibiwa na Mungu. Wakati huo, Waashuru na baadaye Wababiloni walikuwa wakipigania kuutawala ulimwengu. Waisraeli hawakutambua kamwe kwamba Yehova angetumia serikali hizo mbili kuu za ulimwengu kutekeleza hukumu yake! Hata hivyo, unajua kwamba Mungu aliwatumia manabii waaminifu kuwaonya tena na tena watu wa Israeli na Yuda.
5. Ni kikundi gani cha manabii kilichotangaza hukumu ya Yehova wakati uharibifu wa Yuda na Yerusalemu ulipokuwa ukikaribia?
5 Wakati wa kuhukumu Yuda na Yerusalemu ulipokuwa ukikaribia, Yehova alitumia kikundi kingine cha wajumbe wenye bidii. Ni nani waliokuwa katika kikundi hicho? Nabii Sefania, Nahumu, Habakuki, na Obadia. Wote walitoa unabii katika karne ya saba K.W.K. Mwaka wa 607 K.W.K., Wababiloni waliharibu Yerusalemu na kuwapeleka Wayahudi uhamishoni. Huo ndio msiba mkubwa zaidi uliotokea wakati huo. Kwa mara nyingine tena, ilitukia tu kama Mungu alivyoonya katika unabii uliotolewa na baadhi ya manabii hao aliowatuma wamwakilishe. Walijitahidi kuwaonya watu waache mazoea mabaya kama vile ulevi na ujeuri, lakini watu hawakubadilika.—Habakuki 1:2, 5-7; 2:15-17; Sefania 1:12, 13.
6. Yehova aliwatiaje moyo mabaki waliorudi kutoka uhamishoni?
6 Watu wa Mungu waliporudi kutoka uhamishoni, walihitaji uongozi mzuri, faraja, na vilevile kitia-moyo ili wakazie fikira ibada ya kweli. Kikundi kingine cha manabii—Hagai, Zekaria, na Malaki—kilifanya kazi hiyo. Walitumika katika karne ya sita na ya tano K.W.K. Unapojifunza mengi kuwahusu manabii hao 12 wenye ujasiri walioitetea enzi kuu ya Yehova na kuhusu kazi yao, utapata mambo muhimu unayoweza kutumia katika huduma yako katika nyakati hizi zetu zenye hatari. Hebu sasa tuzungumzie manabii hao kulingana na wakati waliotumika.
JITIHADA YA KUOKOA MATAIFA YENYE UKAIDI
7, 8. Kisa cha Yona kinaweza kutusaidiaje kupambana na hisia zozote za kuvunjika moyo?
7 Je, umewahi kuhisi umevunjika moyo, labda ulihisi kwamba imani yako inadhoofika? Ikiwa ndivyo, kisa cha Yona kitakufaidi sana. Yona aliishi katika karne ya tisa K.W.K. Yaelekea unajua kwamba Mungu alimpa Yona utume wa kwenda Ninawi, jiji kuu la Milki ya Ashuru ambayo ilikuwa ikipanuka. Yona alipewa mgawo wa kushutumu uovu wa Waninawi. Hata hivyo, badala ya kwenda kwenye mgawo wake, karibu kilometa 900 hivi kaskazini-mashariki mwa Yerusalemu, Yona alipanda meli ambayo labda ilikuwa ikielekea kwenye bandari moja huko Hispania. Alikuwa akienda umbali wa kilometa 3,500 upande tofauti kabisa na mgawo wake! Unaonaje? Je, Yona alikimbia kwa sababu ya kuogopa, kukosa imani, au aliudhika kwa sababu alifikiri kwamba huenda Waninawi wangetubu na baadaye kuwatesa Waisraeli? Biblia haitaji sababu hususa. Lakini tunajifunza kwamba tunahitaji kujilinda ili tusikengeushwe.
8 Unajua jinsi Yona alivyotenda alipokaripiwa na Mungu. Yona alipokuwa ndani ya “samaki mkubwa” aliyemmeza alikiri hivi: “Wokovu ni wa Yehova.” (Yona 1:17; 2:1, 2, 9) Baada ya kuokolewa kimuujiza, Yona alitekeleza utume wake, hata hivyo, alikata tamaa sana Yehova alipokosa kuwaharibu Waninawi kwa sababu walitii ujumbe wa Yona na kutubu. Kwa upendo, Yehova alimsahihisha tena nabii huyo aliyekuwa akifikiria tu masilahi yake mwenyewe. Na ingawa baadhi ya watu huenda wakaona tu udhaifu wa Yona, Mungu alimwona kuwa mtumishi mzuri ambaye ni mtiifu na mwaminifu.—Luka 11:29.
9. Ujumbe wa Yoeli wa kinabii unakufaidi kwa njia zipi?
9 Je, ulifadhaika uliposikia watu wakishutumu ujumbe wako wa Biblia na kudai kwamba unawatisha? Ujumbe wa nabii Yoeli, ambaye jina lake linamaanisha “Yehova Ni Mungu,” ulionwa vivyo hivyo na wananchi wenzake. Inaonekana kwamba aliandikia unabii wake huko Yuda mwaka wa 820 hivi K.W.K., katika siku za Mfalme Uzia. Inaelekea kwamba Yoeli na Yona walitumika pamoja wakiwa manabii kwa muda fulani. Yoeli alitabiri kwamba makundi ya nzige waharibifu yangeivamia nchi na kuiacha ukiwa. Naam, siku ya Mungu itishayo ilikuwa karibu sana. Hata hivyo, utajifunza kwamba ujumbe wa Yoeli haukuwa wa uharibifu peke yake. Inatia moyo kwamba alitabiri wale waaminifu ‘wangeponyoka.’ (Yoeli 2:32) Watu wenye kutubu wanaweza kufurahia baraka na msamaha wa Yehova. Inatia moyo kama nini kukumbuka kwamba ujumbe tunaohubiri unatia ndani mambo hayo! Yoeli alitabiri kwamba nguvu za Mungu za utendaji, yaani, roho yake takatifu, itamiminwa “juu ya kila namna ya mwili.” Je, unaona jinsi unabii huo unavyokuhusu? Yoeli alikazia pia njia pekee ya kupata wokovu: “Kila mtu anayeliitia jina la Yehova ataokoka.”—Yoeli 2:28, 32.
10. Yehova alimtumiaje mtu aliyefanya kazi katika majira fulani-fulani tu?
10 Unaweza kumhurumia Amosi ikiwa nyakati nyingine unathamini uzito wa ujumbe tunaotangaza, hasa kwa watu ambao hawaitikii. Amosi hakuwa mwana wa nabii wala hakuwa katika kikundi fulani cha manabii; alikuwa mchungaji wa kondoo na alifanya kazi katika majira fulani-fulani. Alifanya kazi ya kutoa unabii wakati wa Mfalme Uzia wa Yuda, karibu na mwisho wa karne ya tisa K.W.K. Licha ya hali yake ya chini, Amosi (ambaye jina lake linamaanisha “Kuwa Mzigo; Kubeba Mzigo”) alikuwa na ujumbe mzito sana kwa ajili ya Yuda, Israeli, na mataifa jirani. Je, si jambo lenye kutia moyo kujua kwamba Yehova anaweza kumwezesha mtu wa kawaida kufanya kazi muhimu hivyo?
11. Hosea alikuwa tayari kujidhabihu kwa kadiri gani ili kufanya mapenzi ya Mungu?
11 Je, umewahi kujiuliza, ‘Niko tayari kujidhabihu kwa kadiri gani ili nifanye mapenzi ya Yehova?’ Mfikirie Hosea, ambaye aliishi karibu wakati mmoja na Isaya na Mika. Alitumika akiwa nabii kwa muda wa miaka 60 hivi. Yehova alimwagiza Hosea amwoe Gomeri, “mke wa uasherati.” (Hosea 1:2) Kati ya watoto watatu ambao Gomeri alizaa baadaye, inaonekana ni mmoja tu aliyekuwa wa Hosea. Yehova angewezaje kumwambia mtu avumilie aibu ya kuishi na mwenzi asiye mwaminifu? Yehova alikuwa akiwafundisha kuhusu ushikamanifu na kuwa wenye kusamehe. Taifa la kaskazini lilikuwa limemsaliti Mungu kama mke mzinzi anavyomsaliti mumewe. Hata hivyo, Yehova angewaonyesha watu wake upendo na kujaribu kuwasaidia watubu. Hapana shaka kwamba kuchanganua jambo hilo kutaichangamsha mioyo yetu.
12. Ni faida gani unayopata kutokana na mfano wa Mika na matokeo ya kazi yake ya kutoa unabii?
12 Je, hukubali kwamba si rahisi kusitawisha ujasiri na kumtegemea Yehova kabisa katika nyakati hizi za hatari? Ukionyesha sifa hizo, utakuwa kama Mika. Nabii Mika ambaye aliishi wakati mmoja na Hosea na Isaya, alitangaza ujumbe wa hukumu juu ya mataifa ya Yuda na Israeli wakati wa utawala wa wafalme wa Yudea, Yothamu, Ahazi, na Hezekia katika karne ya nane K.W.K. Ufalme wa kaskazini wa Israeli ulikuwa umezorota kwa sababu ya hali mbaya sana ya maadili na ibada ya sanamu. Ufalme huo uliharibiwa wakati jiji la Samaria lilipotekwa na Waashuru mwaka wa 740 K.W.K. Pindi fulani Yuda lilimtii Yehova na nyakati nyingine lilimwasi. Licha ya matukio yenye kuhuzunisha, Mika alipata faraja alipoona ujumbe aliopewa na Mungu ukikomesha kwa muda hali mbaya ya kiroho ya Yuda ambayo hatimaye ilileta msiba. Tunapata faraja iliyoje tunapoona baadhi ya watu wakikubali ujumbe wetu wa wokovu!
KUTABIRI MSIBA ULIOKUWA UKIJA
13, 14. (a) Unaweza kumwigaje Sefania katika ibada yako? (b) Sefania alileta mabadiliko gani ya kiroho?
13 Umaarufu wa Babiloni ulikuwa ukiongezeka huku serikali kuu za ulimwengu za Misri na Ashuru zikiendelea kudidimia. Muda si muda, ukuu wa Babiloni ungeathiri kabisa taifa la Yuda. Manabii wa Mungu walikuwapo ili kuwaonya na kuwashauri waabudu wa Yehova. Wafikirie baadhi ya manabii hao, huku ukikumbuka kwamba leo pia Wakristo wanahubiri ujumbe wenye kuonya.
14 Ikiwa umelazimika kuacha desturi za familia ili ufanye mapenzi ya Yehova, unaweza kuelewa hali ya Sefania. Inaonekana kwamba alikuwa mjukuu wa Mfalme Hezekia na mtu wa ukoo wa Mfalme Yosia. Hivyo inaonekana alikuwa mshiriki wa familia ya kifalme ya Yuda. Hata hivyo, kwa utii Sefania alitangaza ujumbe wa hukumu dhidi ya viongozi wafisadi wa Yuda. Jina lake linamaanisha “Yehova Ameficha.” Alikazia kwamba mtu anaweza ‘kufichwa katika siku ya hasira ya Yehova’ kwa rehema ya Mungu tu. (Sefania 2:3) Jambo la kufurahisha ni kwamba Sefania alipata matokeo mazuri kwa sababu ya ujasiri wake wa kutangaza ujumbe huo. Mfalme Yosia aliyekuwa kijana aliongoza katika kuleta mabadiliko ya kiroho, aliondoa sanamu, akarekebisha hekalu, na kurudisha ibada safi. (2 Wafalme, sura ya 22-23) Lazima Sefania na manabii wenzake (Nahumu, na Yeremia) walimshauri mfalme na kumsaidia sana. Inahuzunisha kwamba Wayahudi wengi hawakutubu kwa moyo wao wote. Baada ya Yosia kufa vitani, walianza tena kuabudu sanamu. Muda si muda, walipelekwa utekwani huko Babiloni.
15. (a) Kwa nini jiji la Ninawi lilistahili ujumbe wa hukumu uliotangazwa na Nahumu? (b) Unaweza kujifunza nini kutokana na mambo yaliyopata Ninawi?
15 Huenda ukahisi kwamba wewe ni mtu asiyefaa kitu, asiyetambuliwa. Wakristo wana pendeleo kubwa la kuwa “wafanyakazi wenzi” wa Mungu, lakini wengi wao si watu maarufu. (1 Wakorintho 3:9) Vivyo hivyo, hatujui mengi kumhusu nabii Nahumu ila tu kwamba alitoka katika mji mdogo ulioitwa Elkoshi, ambao huenda ulikuwa huko Yuda. Hata hivyo, ujumbe wake ulikuwa mzito na muhimu. Jinsi gani? Nahumu alitabiri hukumu dhidi ya Ninawi, jiji kuu la Milki ya Ashuru. Watu wa jiji hilo waliitikia ujumbe wa Yona, lakini baada ya muda walirudia maisha yao ya zamani. Mawe yaliyochongwa yaliyopatikana katika mahali lilipokuwa jiji la Ninawi la kale yanaonyesha kwamba lilikuwa “jiji la umwagaji wa damu” kama Nahumu alivyosema. (Nahumu 3:1) Mawe hayo yaliyochongwa yanaonyesha mateka wa vita wakiteswa kwa ukatili sana. Nahumu alitabiri waziwazi na kwa lugha ya mfano kuhusu kuharibiwa kabisa kwa Ninawi. Ujumbe wake ulitimia, ndivyo na ujumbe tunaotangaza leo utakavyotimia.
16, 17. Tunaweza kujifunza nini kutokana na Habakuki ikiwa matarajio yetu kuhusu mwisho hayajatimia?
16 Kwa karne nyingi, wasomaji fulani wa Biblia hawajaona matarajio yao kuhusu siku ya Yehova yakitimia. Huenda wengine wakafadhaika kwa sababu wanafikiri kwamba hukumu ya Mungu inakawia-kawia. Wewe unahisije? Habakuki alieleza mahangaiko yake yaliyofaa, alipouliza: “Ee Yehova, nililie msaada mpaka wakati gani, nawe usisikie? . . . Kwa nini kuna uporaji na jeuri mbele yangu?”—Habakuki 1:2, 3.
17 Habakuki alifanya kazi ya kutabiri wakati Yuda lilipokuwa likikabili matatizo, baada ya utawala wa Mfalme mzuri Yosia, lakini kabla ya Yerusalemu kuharibiwa mwaka wa 607 K.W.K. Jeuri na ukosefu wa haki ulikuwa umeenea sana. Habakuki alionya kwamba taifa la Yuda halingewaepuka Wababiloni wenye kiu ya kumwaga damu licha ya kwamba lilikuwa limeungana na Misri. Aliandika ujumbe wake kwa njia iliyo wazi sana na yenye kuchochea, aliwafariji kwa kusema kwamba “mwadilifu, ataendelea kuishi kwa uaminifu wake.” (Habakuki 2:4) Hapana shaka kwamba maneno hayo ni muhimu sana kwetu, kwa kuwa mtume Paulo aliyanukuu katika vitabu vitatu vya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. (Waroma 1:17; Wagalatia 3:11; Waebrania 10:38) Isitoshe, kupitia Habakuki, Yehova anatuhakikishia hivi: “Maono hayo bado ni ya wakati uliowekwa . . . Hayatachelewa.”—Habakuki 2:3.
18. Kwa nini Yehova alimwagiza Obadia atangaze unabii wa hukumu juu ya Edomu?
18 Nabii Obadia ndiye aliyeandika kitabu kifupi zaidi katika Maandiko ya Kiebrania—chenye mistari 21 tu. Tunajua tu kwamba alitangaza unabii wa hukumu juu ya Edomu. Waedomu walikuwa wazao wa ndugu ya Yakobo, basi walikuwa “ndugu” za Waisraeli. (Kumbukumbu la Torati 23:7) Lakini Waedomu waliwatendea watu wa Mungu kwa njia isiyo ya kindugu hata kidogo. Mwaka wa 607 K.W.K., karibu na wakati Obadia alipoandika kitabu chake, waliweka vizuizi njiani, wakawashika Wayahudi waliokuwa wakitoroka na kuwapeleka kwa Wababiloni waliokuwa maadui. Yehova alitabiri kwamba Edomu lingeharibiwa kabisa, na unabii huo ulitimia. Kama Nahumu, hatujui mengi kumhusu Obadia, lakini inatia moyo sana kujua kwamba Mungu anaweza kuwatumia watu wa hali ya chini kuwa wajumbe Wake!—1 Wakorintho 1:26-29.
UJUMBE WENYE KUCHOCHEA, KUFARIJI, NA KUONYA
19. Hagai aliwachocheaje watu wa Mungu?
19 Hagai ndiye nabii wa kwanza kati ya manabii watatu ambao walitumika baada ya mabaki waaminifu kurudi kutoka uhamishoni Babiloni mwaka wa 537 K.W.K. Huenda Hagai alikuwa katika kikundi cha kwanza kilichorudi. Akiwa na Gavana Zerubabeli na Kuhani Mkuu Yoshua, huku akishirikiana na nabii Zekaria, Hagai alijaribu kuwahimiza Wayahudi washinde upinzani kutoka katika mataifa mengine na kubadili mtazamo wao wa kutopendezwa na mambo ya kiroho kwa sababu ya kufuatia mali. Walihitaji kumaliza kazi waliyorudi kufanya: kazi ya kujenga upya hekalu la Yehova. Ujumbe wenye sehemu nne ulio wazi kabisa kutoka kwa Hagai, ulitangazwa mwaka wa 520 K.W.K., na ulikazia jina la Yehova na enzi yake kuu. Unaposoma kitabu hicho, utaona usemi “Yehova wa majeshi” mara 14. Ujumbe wenye nguvu wa Hagai uliwachochea watu waendelee na kazi ya kujenga hekalu. Je, huchochewi vivyo hivyo unapojua kwamba Yehova ana nguvu zisizo na mipaka akiwa Mtawala Mwenye Enzi Kuu na kwamba ana mamlaka juu ya jeshi kubwa sana la viumbe wa roho?—Isaya 1:24; Yeremia 32:17, 18.
20. Zekaria alipambana na hali gani iliyokuwa imeenea?
20 Nyakati nyingine unaweza kuvunjika moyo ukiwaona baadhi ya watumishi wa Mungu wakipunguza bidii yao katika utumishi. Ikiwa unahisi hivyo unaweza kuelewa hisia za nabii Zekaria. Sawa na Hagai aliyeishi wakati uleule, aliwachochea waabudu wenzake waendelee na kazi hadi ujenzi wa hekalu ukamilike. Zekaria alijitahidi sana kuwaimarisha watu ili wafanye kazi hiyo kubwa. Licha ya kwamba watu walipenda raha sana, alijitahidi kuwachochea wawe na imani yenye nguvu na kuonyesha imani hiyo kwa matendo. Jitihada zake zilifanikiwa. Zekaria aliandika unabii mwingi kumhusu Kristo. Sisi pia tunaweza kuimarishwa na ujumbe wa kwamba “Yehova wa majeshi” hatawasahau watu wanaotafuta kibali chake.—Zekaria 1:3.
WAMTARAJIA MASIHI
21. (a) Kwa nini ujumbe wa Malaki ulihitajiwa sana? (b) Kitabu cha Malaki kinamalizia Maandiko ya Kiebrania kwa kutoa jambo gani lenye kutia moyo?
21 Malaki ambaye ni nabii wa mwisho kati ya wale manabii 12 aliishi kulingana na jina lake ambalo linamaanisha “Mjumbe Wangu.” Twajua machache kumhusu nabii huyo, ambaye aliishi katikati ya karne ya tano K.W.K. Hata hivyo, kutokana na unabii wake tunajua kwamba alikuwa msemaji jasiri aliyewakemea watu wa Mungu kwa sababu ya dhambi na unafiki wao. Hali ambazo Malaki alieleza zinalingana kabisa na hali zilizotajwa na Nehemia, ambaye inaelekea aliishi wakati mmoja na Malaki. Kwa nini ujumbe wa Malaki ulihitajiwa sana? Makumi kadhaa ya miaka mapema, nabii Zekaria na Hagai walikuwa wamewachochea watu wawe na bidii na shauku, lakini sasa bidii hiyo ilikuwa imedidimia. Wayahudi walikuwa katika hali mbaya sana ya kiroho. Malaki aliwashutumu kwa ujasiri makuhani wanafiki na wenye kiburi, na aliwashutumu watu kwa ibada yao ya shingo upande na dhabihu ambazo walikuwa wakitoa. Hata hivyo, kama vile Neno la Mungu linavyotuahidi maisha mazuri wakati ujao, Malaki alitabiri kuja kwa Yohana Mbatizaji, mtangulizi wa Masihi, na kuja kwa Kristo mwenyewe. Kitabu cha Malaki ambacho ni cha mwisho katika Maandiko ya Kiebrania, kina ujumbe wenye kutia moyo sana, kinatuahidi kwamba “jua la uadilifu litaangaza” kwa wale wanaoliogopa jina la Mungu.—Malaki 4:2, 5, 6.
22. Umejifunza nini kuhusu sifa na ujumbe wa wale manabii 12?
22 Unaweza kuona kwamba watu walioandika vile vitabu 12 vya mwisho vya Maandiko ya Kiebrania walikuwa na imani na usadikisho. (Waebrania 11:32; 12:1) Kielelezo chao na ujumbe wao unaweza kutufundisha mambo muhimu sana tunapoitazamia kwa hamu “siku ya Yehova.” (2 Petro 3:10) Hebu sasa fikiria jinsi ujumbe wao wa kinabii unavyoweza kuathiri wakati wako ujao wa milele!
a Linganisha na chati iliyo kwenye ukurasa wa 20 na 21. Kwa mfano, utaona kwamba Mika na Hosea walikuwa manabii wakati Isaya alipokuwa nabii wa Mungu huko Yerusalemu.
-
-
Siku ya Yehova—Ujumbe MuhimuIzingatie Siku ya Yehova Maishani
-
-
SURA YA TATU
Siku ya Yehova—Ujumbe Muhimu
1, 2. (a) Manabii wote 12 huzungumzia jambo gani muhimu? (b) Baadhi ya wale manabii 12 walizungumziaje moja kwa moja siku ya Yehova?
“ILE siku kuu ya Yehova iko karibu. Iko karibu, nayo inaharakisha sana.” (Sefania 1:14) Manabii wa Mungu walionya tena na tena kuhusu siku ya Yehova inayokaribia. Kwa kawaida, walionyesha jinsi kuja kwa siku hiyo kunavyopaswa kuathiri maisha ya watu ya kila siku, maadili yao, na mwenendo wao. Sikuzote ujumbe huo ulipaswa kutangazwa haraka. Ikiwa ungeusikia ujumbe huo kwa masikio yako mwenyewe, ungetendaje?
2 Unaposoma vile vitabu vya wale manabii 12, utaona kwamba wote hao walizungumzia siku ya Yehova kwa njia moja au nyingine.a Hivyo, kabla ya kuchunguza sura zinazofuata na kuona habari muhimu ambayo manabii hao walitangaza, fikiria ujumbe huu unaokaziwa tena na tena: ile siku ya Yehova. Manabii sita kati yao walitumia maneno hayohayo au mengine yanayofanana na hayo. Yoeli alifafanua waziwazi “ile siku ya Yehova iliyo kuu na yenye kuogopesha.” (Yoeli 1:15; 2:1, 2, 30-32) Amosi aliwaambia Waisraeli wajitayarishe kukutana na Mungu wao, kwa maana siku ya Yehova ingekuwa giza. (Amosi 4:12; 5:18) Baadaye, Sefania alisema maneno yaliyonukuliwa katika fungu la 1. Karibu na wakati wa kuharibiwa kwa Yerusalemu, Obadia alionya hivi: “Siku ya Yehova juu ya mataifa yote iko karibu.”—Obadia 15.
Kama dhoruba yenye kutisha, “siku ya Yehova iko karibu”
3. Kwa nini tunaweza kusema kwamba manabii walioishi baada ya uhamisho walizungumzia siku ya Yehova?
3 Pia, utaona kwamba manabii wawili waliotumwa kwa Wayahudi baada ya kurudi kutoka uhamishoni walitumia maneno kama hayo. Zekaria alisema juu ya siku ambayo mataifa yote yanayokuja kupigana na Yerusalemu yangeharibiwa. Alieleza kinaganaga mambo ambayo yangetokea “siku moja inayojulikana kuwa ni ya Yehova.” (Zekaria 12:9; 14:7, 12-15) Naye Malaki aliwajulisha watu wa Mungu kuhusu kuja kwa “ile siku ya Yehova iliyo kuu na yenye kuogopesha.”—Malaki 4:1-5.
4. Baadhi ya wale manabii 12 wanazungumziaje siku ya Yehova?
4 Ingawa hawakutumia maneno “siku ya Yehova,” wale manabii wengine kati ya wale 12 walizungumzia siku hiyo. Hosea alisema kwamba Yehova angewatoza hesabu Israeli na baadaye Yuda. (Hosea 8:13, 14; 9:9; 12:2) Mara nyingi ujumbe uliotolewa ulihusu mambo ambayo Yehova alifanya zamani hizo. Kwa mfano, Yona alitangaza hukumu ya Mungu dhidi ya Ninawi, naye Mika alieleza mambo ambayo yangetukia wakati ambapo Mungu angechukua hatua dhidi ya watu walioasi. (Yona 3:4; Mika 1:2-5) Nahumu aliahidi kwamba Yehova angelipiza kisasi dhidi ya adui Zake. (Nahumu 1:2, 3) Habakuki alililia haki na kuzungumza kuhusu “siku ya taabu.” (Habakuki 1:1-4, 7; 3:16) Ujumbe fulani katika vitabu hivyo bila shaka uliwahusu Wakristo wa kweli. Kwa mfano, Hagai, mmoja wa manabii walioishi baada ya uhamisho, alitabiri juu ya kutikiswa kwa mataifa. (Hagai 2:6, 7) Mtume Paulo alinukuu maneno ya Hagai 2:6 alipokuwa akiwahimiza Wakristo wawe katika hali inayostahili wakati ambapo Mungu angeondolea mbali mbingu za mfano zenye uovu.—Waebrania 12:25-29; Ufunuo 21:1.
SIKU YA YEHOVA NI NINI?
5, 6. Kulingana na manabii, siku ya Yehova itakuwaje?
5 Unastahili kujua siku ya Yehova itakuwaje. Huenda ukajiuliza, ‘Je, siku ya Yehova inapaswa kuathiri maisha yangu ya sasa na ya wakati ujao?’ Kama vile manabii hao walivyoonyesha, siku ya Yehova ni wakati ambapo Yehova atachukua hatua dhidi ya adui zake ili kutekeleza hukumu, yaani, siku ya vita. Siku hiyo yenye kuogopesha yaelekea itakuwa siku itakayokuwa na mambo yasiyo ya kawaida mbinguni. “Jua na mwezi vitakuwa giza, na nyota zitaondoa mwangaza wake.” (Yoeli 2:2, 11, 30, 31; 3:15; Amosi 5:18; 8:9) Ni nini kitakachoipata dunia, makao yetu? Mika alisema hivi: “Na milima itayeyuka chini [ya Yehova], na nchi tambarare za chini zitapasuka, kama nta kwa sababu ya moto, kama maji yanayomwagwa kwenye mteremko mkali.” (Mika 1:4) Huenda ufafanuzi huo ukawa wa mfano, hata hivyo, twaweza kukata kauli kwamba hatua ambayo Mungu atachukua itasababisha uharibifu mkubwa juu ya dunia na wakaaji wake. Ingawa hivyo, si wanadamu wote watakaoathirika. Manabii haohao walitaja baraka nyingi watakazopata wale ‘wanaotafuta yaliyo mema,’ na ambao wataendelea kuishi.—Amosi 5:14; Yoeli 3:17, 18; Mika 4:3, 4.
6 Wengine kati ya wale manabii 12 walieleza waziwazi kuhusu siku ya Yehova. Habakuki alieleza kinaganaga jinsi Yehova atakavyovunja “milima ya milele” na kuinamisha “vilima vinavyodumu kwa wakati usio na kipimo.” Hiyo ni mifano mizuri inayowakilisha mashirika ya kibinadamu, ambayo huenda yakaonekana kuwa ni ya kudumu. (Habakuki 3:6-12) Naam, siku ya Yehova “ni siku ya ghadhabu, siku ya taabu na ya maumivu makali, siku ya dhoruba na ya ukiwa, siku ya giza na ya weusi, siku ya mawingu na ya weusi mzito.”—Sefania 1:14-17.
7. Ni tauni gani inayotabiriwa, na huenda ikatimizwaje?
7 Hebu wazia tauni itakayowapata wale wanaopigana na Mungu! “Nyama ya mtu itaoza, huku akiwa amesimama kwa miguu yake; na macho ya mtu yataoza yakiwa katika matundu yake, na ulimi wake utaoza ukiwa kinywani mwake.” (Zekaria 14:12) Iwe maono hayo yatatimizwa kihalisi au la, ni wazi kwamba wengi watakumbwa na hali mbaya. Angalau, ndimi za adui za Mungu zitaoza katika maana ya kwamba maneno yao ya ukaidi yatakomeshwa. Nayo macho yataharibiwa yasiweze kuona uwezekano wowote wa kuungana na kuwachukulia hatua watu wa Mungu.
MUNGU MWENYE UPENDO ANAWEZAJE KUFANYA HIVYO?
8, 9. (a) Ili kuelewa ni kwa nini Yehova huchukua hatua dhidi ya waovu, unapaswa kufikiria nini? (b) Ushikamanifu wako katika maisha yako ya kila siku unahusianaje na Yehova kuchukua hatua?
8 Huenda umewahi kusikia watu wakiuliza: ‘Mungu mwenye upendo anawezaje kuleta msiba kama huo juu ya adui zake? Je, lazima Mungu asababishe uharibifu duniani? Kwani, je, Yesu hakuwahimiza watu waendelee kuwapenda hata adui zao na kwamba wakifanya hivyo watakuwa wakionyesha kwamba wao ni wana wa Baba yao aliye mbinguni?’ (Mathayo 5:44, 45) Ili kujibu maswali hayo, fikiria chanzo cha matatizo ya wanadamu. Mungu aliwaumba wanadamu wawili wa kwanza kwa sura na mfano wake—walikuwa wakamilifu. Hata hivyo, walianzisha dhambi na kifo katika jamii ya wanadamu na hivyo mambo hayo yakaingia maishani mwetu. Walijiunga na Shetani Ibilisi katika suala la ni nani aliye na haki kamili ya kuwatawala wanadamu. (Mwanzo 1:26; 3:1-19) Kwa karne kadhaa, Shetani amejaribu kuthibitisha kwamba wanadamu wakichochewa kufanya vingine, basi hawatamtumikia Yehova. Unajua kwamba Shetani ameshindwa. Yesu Kristo na watumishi wengine wengi wa Yehova wamedumisha utimilifu wao kwa Mungu nao wameonyesha kwamba wanamtumikia kwa sababu wanampenda. (Waebrania 12:1-3) Bila shaka, unajua watu wengi ambao wanamtumikia Mungu kwa ushikamanifu.
9 Isitoshe, unahusika katika suala litakalofikia tamati wakati ambapo Yehova atauondolea mbali uovu. Kwa mfano, unaposoma vitabu hivyo 12, utaona kwamba manabii fulani walikazia fikira maisha ya anasa ya watu waliopuuza ibada ya Yehova. Manabii hao waliwahimiza watu wa Mungu ‘waweke moyo wao juu ya njia zao’ na kubadili maisha yao. (Hagai 1:2-5; 2:15, 18; Amosi 3:14, 15; 5:4-6) Naam, manabii hao walikuwa wakiwaonyesha watu jinsi ya kuishi. Wale waliokubali himizo hilo walionyesha kwamba Yehova ndiye Mwenye Enzi Kuu, na kumthibitisha Shetani kuwa mwongo. Yehova atakuwa mshikamanifu kwao atakapowaangamiza adui zake.—2 Samweli 22:26.
10. Kutokana na mambo aliyojionea Mika, Yehova ana sababu gani nyingine ya kuchukua hatua?
10 Mungu ana sababu nyingine ya kuchukua hatua. Hebu fikiria karne ya nane, K.W.K., wakati Mika alipokuwa nabii katika Yuda. Akizungumza kana kwamba yeye ndiye taifa hilo, analinganisha hali ya taifa la Yuda na shamba la mizabibu au na shamba la matunda baada ya mavuno, lisilo na mabaki yoyote ya zabibu au tini. Hivyo ndivyo hali ilivyokuwa katika jamii ya Wayudea, ilikuwa vigumu sana kumpata yeyote aliyekuwa mnyoofu. Waisraeli walikuwa wakiwawinda wenzao, wakioteana ili kumwaga damu. Viongozi na waamuzi wao walikuwa wameazimia kujifaidi kibinafsi. (Mika 7:1-4) Ikiwa ungeishi katika hali kama hizo, ungehisije? Huenda, ungewahurumia watu waliokuwa wakiteseka bure. Basi, lazima Yehova anawahurumia hata zaidi wale wanaokandamizwa! Leo, Yehova anawatazama wanadamu. Unafikiri anaona nini? Wakandamizaji wanawadhulumu kikatili wengine na kuwashambulia kijeuri jirani zao. Washikamanifu ni wachache kwa kulinganishwa na idadi ya watu ulimwenguni. Hata hivyo, hatupaswi kukata tamaa. Kwa kuwa Yehova anawapenda wanaokandamizwa, atatekeleza haki.—Ezekieli 9:4-7.
11. (a) Siku ya Yehova inamaanisha nini kwa wale wanaomwogopa? (b) Ujumbe wa Yona wenye onyo ulibadili jinsi gani maisha ya Waninawi?
11 Ni wazi kwamba, siku ya Yehova inamaanisha uharibifu kwa adui zake na ukombozi kwa wale wanaomwogopa na kumtumikia.b Mika alitabiri kwamba mataifa yangemiminika kwenye mlima wa nyumba ya Yehova, kisha kuwe na amani na umoja ulimwenguni pote. (Mika 4:1-4) Wakati huo, je, watu walibadili maisha yao kwa kuwa manabii walikuwa wakitangaza siku ya Yehova? Baadhi yao walifanya hivyo. Kumbuka kwamba Yona alipotangaza hukumu dhidi ya Ninawi, wakaaji waovu wa jiji hilo, waliokuwa wajeuri, ‘walianza kumwamini Mungu’ nao ‘wakageuka kutoka katika njia yao mbaya.’ Yehova alijizuia asilete msiba wakati huo. (Yona 3:5, 10) Ujumbe huo kuhusu siku ya Yehova ya hukumu iliyokuwa ikikaribia, ulibadili maisha ya Waninawi!
SIKU HIYO INAATHIRIJE MAISHA YAKO?
12, 13. (a) Wale manabii 12 walitabiri kuhusu nani? (b) Kwa nini tunaweza kusema kwamba maneno ya wale manabii 12 yangetimizwa pia baadaye?
12 Huenda mtu akasema, ‘Manabii hao waliishi karne nyingi zilizopita. Ujumbe wao kuhusu siku ya Yehova unanihusuje?’ Ni kweli kwamba manabii hao waliishi miaka mingi iliyopita, hata kabla ya Yesu kuzaliwa, hata hivyo, twapaswa kuzingatia jinsi maneno yao kuhusu siku ya Yehova yanavyotumika katika karne ya 21. Tunaweza kufaidikaje kutokana na mambo waliyosema kuhusu ile siku kuu ya Yehova? Kuna jambo moja linaloweza kutusaidia kuona umuhimu wa ujumbe huo na jinsi tunavyoweza kufaidika kutokana nao. Jambo hilo ni kutambua kwamba manabii hao walionya kuhusu siku ya Yehova dhidi ya Israeli, Yuda, mataifa jirani, na serikali fulani za ulimwengu zilizokuwako wakati huo.c Jambo kuu ni kwamba unabii huo ulitimizwa! Waashuru walivamia Samaria, Yuda lilifanywa ukiwa mwaka wa 607 K.W.K., na mataifa jirani yaliyokuwa katili yakaangamizwa. Hatimaye, unabii mbalimbali hususa kuhusu kuanguka kwa serikali ya ulimwengu ya Ashuru na ya Babiloni ukatimia.
Katika Pentekoste ya 33 W.K., Petro alizungumzia unabii wa Yoeli. Unabii huo unatimizwa katika siku yetu pia
13 Sasa, hebu fikiria siku ya Pentekoste, mwaka wa 33 W.K., muda mrefu baada ya sehemu kubwa ya unabii huo mbalimbali kutimizwa mara ya kwanza. Siku hiyo, mtume Petro alitumia maneno ya nabii Yoeli kuhusiana na kumiminwa kwa roho takatifu ya Mungu. Kisha Petro akanukuu kitabu cha Yoeli na kusema: “Jua litageuzwa kuwa giza na mwezi kuwa damu kabla ya kufika kwa ile siku ya Yehova iliyo kuu na yenye fahari.” (Matendo 2:20) Hilo laonyesha kwamba unabii mbalimbali kuhusu siku ya Yehova bado ungetimizwa tena. Nao unabii wa Yoeli ulitimizwa mara ya pili katika mwaka wa 70 W.K. jeshi la Roma lilipoharibu Yerusalemu. Huo bila shaka ulikuwa wakati wa giza na damu.
14, 15. (a) Kwa nini tunaweza kusema kwamba unabii kuhusu siku ya Yehova unatuhusu leo? (b) Tunaweza kutazamia siku ya Yehova ije wakati gani?
14 Hata hivyo, unabii wa Yoeli pamoja na unabii mwingine mbalimbali kuhusu siku ya Yehova bado utatimizwa tena kwa mara ya mwisho, katika siku zetu sisi tunaoishi katika karne ya 21. Jinsi gani? Petro aliwahimiza Wakristo waweke “karibu akilini kuwapo kwa siku ya Yehova.” Mtume huyo aliendelea kusema: “Tunangojea mbingu mpya na dunia mpya, na humo uadilifu utakaa.” (2 Petro 3:12, 13) Baada ya Yerusalemu kuharibiwa mwaka wa 70 W.K., hakukuwa na mbingu zozote mpya (serikali mpya ya kitheokrasi) wala dunia mpya (jamii ya watu waadilifu chini ya serikali hiyo). Kwa hiyo, lazima maneno hayo ya kinabii kuhusu siku ya Yehova yangetimia tena. Ndiyo, unabii huo mbalimbali unatuhusu sisi leo, sisi tunaoishi katika “nyakati za hatari”!—2 Timotheo 3:1.
15 Maelezo yote kuhusu siku ya Yehova, yanayotolewa katika vitabu hivyo 12 vya Biblia hutukumbusha maneno haya ya Yesu Kristo: “Ndipo kutakapokuwa na dhiki kuu ya namna ambayo haijapata kutukia tangu mwanzo wa ulimwengu mpaka sasa, hapana, wala haitatukia tena.” Alisema kwamba “mara baada ya ile dhiki ya siku hizo jua litatiwa giza, nao mwezi hautatoa nuru yake, nazo nyota zitaanguka kutoka mbinguni, nazo nguvu za mbingu zitatikiswa.” (Mathayo 24:21, 29) Hilo hutusaidia kuelewa wakati ambapo siku ya Yehova itakuja. Inakaribia. Maandiko yanaonyesha kwamba “Babiloni Mkubwa,” ile milki ya ulimwengu ya dini za uwongo, itaharibiwa katika ile dhiki kuu. Kisha, siku ya Yehova, ambayo ndiyo upeo wa dhiki kuu, itawafutilia mbali adui za Mungu wasiwepo tena kamwe duniani.—Ufunuo 17:5, 12-18; 19:11-21.
16. Unabii kuhusu siku ya Yehova utatimizwa katika njia gani kubwa?
16 Mashahidi wa Yehova wameelewa jinsi unabii mbalimbali kuhusu siku ya Yehova utakavyotimizwa. Mara nyingi na katika njia mbalimbali, taifa la Yerusalemu lililoasi, Samaria lililokosa uaminifu, Waedomu wakatili, Waashuru wajeuri, na Wababiloni waliwakilisha mambo mbalimbali katika dini za uwongo. Dini hizo zote zitaharibiwa mwanzoni mwa dhiki kuu. Kisha, katika “ile siku ya Yehova iliyo kuu na yenye kuogopesha,” waandamani wake wa kisiasa na kibiashara wataangamizwa.—Yoeli 2:31.
IWENI TAYARI
17, 18. (a) Kwa nini Amosi alitangaza ole kwa wale waliokuwa ‘wakiitamani siku ya Yehova?’ (b) Ni nini kingewapata wale ambao hawangekuwa tayari kwa siku ya Yehova?
17 Kwa kuwa ujumbe wa hukumu unahusu hasa dini za uwongo, baadhi ya Wakristo wanaweza kuhisi kwamba utimizo wa unabii huo hautawaathiri. Hata hivyo, mambo ambayo Amosi aliwaambia Waisraeli yana faida kwa wote: “Ole wao wanaoitamani siku ya Yehova!” Baadhi ya Waisraeli wa siku za Amosi walifikiri kwamba siku ya Yehova itamaanisha tu baraka, wakiamini kwamba ni siku ambayo Yehova angetenda kwa niaba ya watu wake. Hata waliitamani siku hiyo! Hata hivyo, Amosi aliendelea kusema kwamba kwa wale wanaohangaikia masilahi yao wenyewe, siku ya Yehova ingekuwa “giza, wala si nuru.” Naam, Waisraeli hao wangepata ghadhabu ya Yehova!—Amosi 5:18.
18 Kisha Amosi akaeleza kile ambacho kingewapata wale waliokuwa wakiitamani siku ya Yehova. Hebu wazia kwamba mtu anamkimbia simba kisha akutana na dubu. Halafu amkimbia dubu huyo na kujificha ndani ya nyumba. Aufunga mlango huku akihema na kuegemea ukutani kisha aumwa na nyoka. Hivyo ndivyo itakavyokuwa kwa wale ambao hawako tayari kabisa kwa siku ya Yehova.—Amosi 5:19.
Kama Mika, uwe na mtazamo wa kumngojea Mungu wa wokovu
19. Tunaweza kujitayarishaje kwa ajili ya siku ya Yehova?
19 Je, unaona jinsi masimulizi hayo yanavyoweza kukufaidi? Kumbuka kwamba maneno ya Amosi yaliwahusu watu waliokuwa wamejiweka wakfu kwa Mungu. Hata hivyo, walihitaji kubadili matendo na mitazamo yao. Je, hupaswi kuchunguza maisha yako ili uone kama uko tayari kwa ajili ya siku hiyo kuu au kama unahitaji kufanya mabadiliko fulani? Unaweza kuthibitishaje kwamba kwa kweli uko tayari? Bila shaka, si kwa kujenga nyumba, kujiwekea akiba ya chakula, kujifunza jinsi ya kusafisha maji au kujiwekea sarafu za dhahabu kama vile watu fulani hufanya ili kujitayarishia majanga fulani. Sefania anasema: “Fedha yao wala dhahabu yao hazitaweza kuwakomboa katika siku ya ghadhabu ya Yehova.” Kwa hiyo, kuwa tayari hakumaanishi kujiwekea hazina ya vitu vya kimwili. (Sefania 1:18; Methali 11:4; Ezekieli 7:19) Badala yake, tunapaswa kuwa macho kiroho na kuishi kila siku tukiwa tayari. Tunahitaji kuwa na mtazamo na mwenendo mzuri. Mika alisema: “Mimi, nitaendelea kumtazamia Yehova. Nitaonyesha mtazamo wa kumngojea Mungu wa wokovu wangu.”—Mika 7:7.
20. Ni mambo gani yasiyoweza kubadili kamwe mtazamo wetu wa kungojea?
20 Ukiwa na mtazamo huo wa kungojea, utathibitisha kwamba uko tayari, ukitazamia siku ya Yehova. Hutahangaikia tarehe ambayo siku hiyo itakuja au muda ambao umengoja. Unabii wote kuhusu siku hiyo utatimizwa katika wakati uliowekwa na Yehova, nayo siku hiyo haitachelewa. Yehova alimwambia Habakuki: “Maono hayo bado ni ya wakati uliowekwa, nayo yanafanya haraka kuelekea mwisho, wala hayatasema uwongo. Hata yakikawia [kwa maoni ya wanadamu], endelea kuyatarajia; kwa maana bila shaka yatatimia. Hayatachelewa [kwa maoni ya Yehova].”—Habakuki 2:3.
21. Mambo utakayojifunza katika kitabu hiki yatakufaidije?
21 Katika kitabu hiki, utajifunza jinsi unavyoweza kuwa na mtazamo wa kumngojea Mungu wa wokovu. Unaweza kutazamia kupata faida gani? Kitabu hiki kitazungumzia hasa sehemu ya Biblia ambayo huenda hufahamiani nayo sana, yaani, vile vitabu 12 vinavyoitwa Manabii Wadogo. Kwa hiyo, utajifunza mambo mengi yenye kusisimua sana. Kwa mfano, katika Sehemu ya 2, utaona jinsi unavyoweza ‘kumtafuta Yehova’ na kuendelea kuishi. (Amosi 5:4, 6) Vitabu hivyo 12 vinaweza kukusaidia kuona jinsi unavyoweza kumjua Yehova vizuri zaidi na kuwa na maoni bora kuhusu kumtumikia, hata kikamili zaidi. Bila shaka, manabii hao watakusaidia kuelewa zaidi utu wa Yehova. Katika Sehemu ya 3, utaelewa vizuri zaidi jinsi Yehova anavyotaka uwatendee washiriki wa familia yenu na wengineo. Kutimiza matakwa hayo kutakusaidia kuwa tayari kwa ajili ya siku hiyo kuu. Hatimaye, katika Sehemu ya 4, utaona mashauri ya manabii kuhusu mtazamo unaopaswa kuwa nao kadiri siku ya Yehova inavyozidi kukaribia, utajifunza pia jinsi huduma yako ya Kikristo inavyohusika. Bila shaka, utafurahi sana unaposoma ujumbe wa manabii hao kuhusu wakati wako ujao.
22. Ungependa kufanya nini kuhusiana na shauri linalopatikana katika vitabu vya wale manabii 12?
22 Je, unakumbuka maneno ya Sefania yaliyonukuliwa mwanzoni mwa sura hii? (Sefania 1:14) Ujumbe wake ulibadili maisha ya Mfalme Yosia aliyekuwa kijana. Yosia alianza kumtafuta Yehova akiwa na umri wa miaka 16 tu. Alipokuwa na umri wa miaka 20, alichukua hatua ya kukomesha ibada ya sanamu kama Sefania alivyokuwa amewatia moyo watu wa Yuda na Yerusalemu. (2 Mambo ya Nyakati 34:1-8; Sefania 1:3-6) Je, onyo kuhusu siku ya Yehova limebadili maisha yako ya kila siku kama ilivyokuwa kwa Yosia? Acheni tuone jinsi manabii hao 12 wanavyoweza kutusaidia.
a Isaya aliyeishi wakati mmoja na kikundi cha kwanza cha wale manabii 12, na pia Ezekieli aliyeishi wakati mmoja na kikundi cha pili, walionya kuhusu siku ya Yehova.—Isaya 13:6, 9; Ezekieli 7:19; 13:5; ona Sura ya 2 ya kitabu hiki, fungu la 4-6.
b Unaweza kupata habari zaidi kuhusu matokeo hayo mazuri kwa kusoma Hosea 6:1; Yoeli 2:32; Obadia 17; Nahumu 1:15; Habakuki 3:18, 19; Sefania 2:2, 3; Hagai 2:7; Zekaria 12:8, 9; na Malaki 4:2.
c Baadhi ya wale manabii 12 walitabiri mambo yaliyohusu, si taifa moja tu, bali mataifa kadhaa.
-
-
Yehova—Mungu Anayetabiri na KutimizaIzingatie Siku ya Yehova Maishani
-
-
SURA YA NNE
Yehova—Mungu Anayetabiri na Kutimiza
1, 2. (a) Kwa nini watu fulani huhisi kwamba maisha hayana mwelekeo? (b) Wale manabii 12 wanaelezaje utu wa Yehova?
WATU wengi wanahisi kwamba maisha yao hayana mwelekeo. Wanaposoma habari, wanakata kauli kwamba jamii yote ya wanadamu haina tumaini lolote. Jitihada za kusuluhisha matatizo ya ulimwengu zinaonekana kuwa za bure tu. Tunapaswa kukumbuka kwamba baadhi ya wale manabii 12 tunaozungumzia walikabili hali kama hizo zenye kuhangaisha, na walitangaza ujumbe wenye tumaini ambao unaweza kutufaidi, nasi tunaweza kuutumia kuwafariji wengine.—Mika 3:1-3; Habakuki 1:1-4.
2 Jambo kuu linalopatikana katika vitabu hivyo vya kinabii ni kwamba Yehova, Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu, ana mamlaka kamili juu ya wanadamu na anapendezwa kabisa na hali yetu. Kwa kweli, kila mmoja wetu anaweza kusema, “Yehova anataka mimi niwe na maisha mazuri.” Manabii hao 12 wanaeleza sifa za “Yehova wa majeshi” kwa njia yenye kuvutia sana. Mungu anaweza ‘kuigusa nchi, iyeyuke,’ hata hivyo, anawahakikishia hivi watu wake: “Yeye anayewagusa ninyi anaigusa mboni ya jicho langu.” (Zekaria 2:8; Amosi 4:13; 9:5) Je, hutiwi moyo unaposoma maandiko yanayoonyesha jinsi Mungu anavyotenda kwa upendo na jinsi anavyorehemu na kusamehe? (Hosea 6:1-3; Yoeli 2:12-14) Kwa kweli, vitabu vya manabii hao havielezi kila jambo kuhusu utu wa Mungu; ili kuujua kabisa utu wa Mungu mtu anahitaji kujifunza vitabu vyote 66 vya Biblia. Hata hivyo, vitabu hivyo 12 vinaweza kutusaidia kuelewa vizuri zaidi utu wa Mungu wenye kuvutia na kazi zake.
3. Wale manabii 12 wanathibitishaje kwamba Yehova ni Mungu wa kusudi?
3 Vitabu hivyo vya wale manabii 12 vinaweza kuimarisha imani yetu katika Yehova akiwa Mtabiri mwenye kutegemeka wa mambo ya wakati ujao na Mtimizaji asiyeshindwa wa kusudi lake. Wanathibitisha kwamba hatimaye ataifanya dunia iwe paradiso chini ya ufalme wake. (Mika 4:1-4) Baadhi ya manabii hao wanaeleza jinsi Yehova alivyotayarisha njia kwa ajili ya kuja kwa Masihi na fidia ambayo ingewaweka wanadamu huru kutoka katika dhambi na kifo. (Malaki 3:1; 4:5) Kwa nini ni muhimu kujua mambo hayo yote?
MWENYE ENZI KUU ALIYE NA UPENDO ANA MAMLAKA KAMILI
4, 5. (a) Wale manabii 12 wanakazia kweli gani ya msingi kumhusu Mungu? (b) Uwezo wa Yehova unakuhusuje?
4 Kumbuka jinsi haki ya Mungu ya kutawala ilivyotiliwa shaka, kama sura iliyotangulia ilivyoonyesha. Baadhi ya malaika mbinguni waliasi mamlaka ya Yehova na kutilia shaka nia yake, hivyo wakakosa kumtii na wakasababisha mvurugo mkubwa na jeuri duniani. Basi, ni wazi kwamba kuheshimu na kujitiisha kwa enzi kuu ya Yehova ni muhimu ili kuwe na uelewano ulimwenguni pote na amani miongoni mwa wanadamu. Kwa hiyo, kwa haki Yehova ameazimia kuitetea enzi yake kuu. Hebu tuone jinsi vile vitabu 12 vya kinabii vinavyoweza kutusaidia kuelewa suala hilo vizuri zaidi.
5 Wakiwa wajumbe wa Yehova, manabii walikazia sana cheo chake cha juu. Kwa mfano, Amosi anatumia usemi “Bwana Mwenye Enzi Kuu” mara 21 ili kulitukuza jina na enzi kuu ya Mweza-Yote. Hilo linaonyesha kwamba ukuu wa Mungu wa kweli hauna kifani na hakuna jambo lolote linaloweza kumshinda. (Amosi 9:2-5; ona sanduku “Yehova Mweza-Yote.”) Yehova peke yake ndiye aliye na haki ya kuwa Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote, naye hawezi kulinganishwa kwa njia yoyote na sanamu ambazo hazina uhai. (Mika 1:7; Habakuki 2:18-20; Sefania 2:11) Kwa kuwa Yehova ndiye Mfanyizaji wa vitu vyote, ana haki ya kuwa mtawala mkuu juu ya wote. (Amosi 4:13; 5:8, 9; 9:6) Kwa nini hilo ni muhimu kwako?
6. Kila mwanadamu anahusikaje katika kutimizwa kwa kusudi la Mungu?
6 Ikiwa umewahi kubaguliwa, kutendewa isivyo haki, au kuonewa, inatia moyo kujua kwamba Mwenye Enzi Kuu ana upendo na anawajali wote. Ingawa Yehova alikuwa na uhusiano wa pekee na taifa moja la kale, alitangaza azimio lake la kuwabariki watu wa mataifa na lugha zote. Yeye ndiye “Bwana wa kweli wa dunia yote.” (Mika 4:13) Mungu aliahidi kwamba jina lake “litakuwa kuu kati ya mataifa.” (Malaki 1:11) Baba yetu wa mbinguni anapojitambulisha kwa watu wote bila ubaguzi, ‘watu kutoka katika lugha zote za mataifa’ wanakubali kwa furaha mwaliko wake wa kuja kumwabudu.—Zekaria 8:23.
7. Kwa nini maana ya jina la Yehova ni muhimu?
7 Jina la Mungu linahusiana sana na sifa zake na makusudi yake. (Zaburi 9:10) Nyakati za Mika, jina la Yehova lililetewa suto kwa sababu watu wengi walioitwa kwa jina hilo hawakumtii kamwe. Nabii huyo aliongozwa na roho takatifu kukazia “ukuu wa jina la Yehova” na kusema kwamba “mtu mwenye hekima inayotumika ataliogopa jina [la Mungu].” (Mika 5:4; 6:9) Kwa nini? Tumaini lolote lenye kutegemeka ulilo nalo kuhusu wakati ujao wa milele linahusiana na maana ya jina hilo: “Yeye Husababisha Kuwa.” Tafadhali soma Yoeli 2:26 na ufikirie furaha unayoweza kupata ukiitwa kwa jina hilo na kuwajulisha wengine kumhusu Mungu huyo ambaye anaweza kuwa chochote anachotaka kuwa ili kuwafaidi viumbe wake wote. Mungu amethibitisha kwamba anaweza kutimiza chochote kwa sababu uwezo wake hauna mipaka. Unabii mwingi sana uliotangazwa na wale manabii 12 ulitimia na hivyo kuthibitisha jambo hilo.
8. Jina la Yehova limekuchocheaje?
8 Mamilioni ya watu wamefaidika sana kwa kujifunza kwamba Yehova anaweza kusababisha au kutimiza chochote anachotaka. Yoeli alionyesha hivyo katika maneno haya yanayojulikana sana yaliyonukuliwa na waandishi Wakristo: “Kila mtu anayeliitia jina la Yehova ataokoka.” (Yoeli 2:32; Matendo 2:21; Waroma 10:13) Je, tunaunga mkono tangazo la Mika, kwamba “sisi tutatembea katika jina la Yehova Mungu wetu mpaka wakati usio na kipimo, naam, milele”? (Mika 4:5) Naam, tunapoteswa au tunapokabili matatizo, tunaweza ‘kupata kimbilio katika jina la Yehova’ tukiwa na uhakika.—Sefania 3:9, 12; Nahumu 1:7.
9. Mungu ana mamlaka kubwa kadiri gani juu ya watawala wanadamu?
9 Unaposoma vitabu hivi vya kinabii, unaweza kuimarisha usadikisho wako kwamba Yehova ana mamlaka hata juu ya wanadamu wanaotawala na wale wanaofanya maamuzi makubwa. Ana uwezo wa kuwaongoza watende kupatana na mapenzi yake. (Methali 21:1) Fikiria kisa cha Dario Mkuu wa Uajemi. Maadui wa ibada ya kweli walimwomba awasaidie kukomesha kazi ya kujenga upya hekalu la Yehova huko Yerusalemu. Jambo lililotukia lilikuwa kinyume kabisa cha matarajio yao! Mwaka wa 520 K.W.K. hivi, Dario alitekeleza amri ya Koreshi na kuunga mkono kazi ya ujenzi iliyofanywa na Wayahudi. Vikwazo zaidi vilipotokea, ujumbe wa Mungu kwa Zerubabeli, Gavana Myahudi, ulikuwa: “‘Si kwa jeshi, wala kwa nguvu, bali kwa roho yangu,’ Yehova wa majeshi amesema. Wewe ni nani, Ee mlima mkubwa? Utakuwa nchi tambarare mbele ya Zerubabeli.” (Zekaria 4:6, 7) Hakuna chochote kitakachomzuia Yehova asiuharibu mfumo huu mwovu wa mambo na kuleta paradiso ambayo itafurahiwa na waabudu wake.—Isaya 65:21-23.
10. Mungu ana uwezo mkubwa kadiri gani, na hilo linamaanisha nini?
10 Kumbuka pia kwamba Yehova hudhibiti nguvu za asili. Anaweza kuzitumia kuwaharibu maadui wake akiamua kufanya hivyo. (Nahumu 1:3-6) Zekaria alitumia lugha ya mfano ili kukazia jinsi Yehova anavyoweza kuwalinda watu wake: “Yehova mwenyewe ataonekana juu yao, na mshale wake utaenda kama umeme. Naye Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova atapiga baragumu, ataenda pamoja na dhoruba za upepo wa kusini.” (Zekaria 9:14) Basi je, itakuwa vigumu kwa Mungu kuonyesha ukuu wake juu ya mataifa yasiyomwogopa leo? La hasha!—Amosi 1:3-5; 2:1-3.
MTIMIZAJI WA AHADI ANAYETEGEMEKA
11, 12. (a) Kwa nini Ninawi lilionwa kuwa jiji lisiloweza kushindwa? (b) Matokeo yalikuwa nini kwa Ninawi kulingana na neno la Mungu la unabii?
11 Jiwazie ukiishi katika karne ya tisa K.W.K. katika eneo ambalo leo linaitwa Mashariki ya Kati. Yaelekea ungekuwa umesikia kuhusu jiji kuu la Ninawi. Lilikuwa jiji maarufu sana la Ashuru ambalo lilikuwa kwenye ukingo wa mashariki wa Mto Tigris, kilometa 900 hivi kaskazini-mashariki mwa Yerusalemu. Yaelekea ungekuwa umesikia kuhusu ukubwa wake wenye kuvutia—mzingo wake ulikuwa kilometa 100 hivi! Watu waliotembea huko Ninawi walisema kwamba lilikuwa jiji la kifahari kama Babiloni kwa sababu lilikuwa na majumba ya kifalme, mahekalu, barabara pana, bustani za umma, na maktaba kubwa sana. Isitoshe, wataalamu wa kijeshi walisema kwamba kuta zake za ndani na za nje zilikuwa kubwa sana na hazingeweza kupenywa.
12 “Haliwezi kushindwa!” Haikosi watu wengi walisema hivyo kuhusu Ninawi. Lakini baadhi ya manabii kutoka taifa dogo la Yuda walisisitiza kwamba Yehova alikuwa ametangaza uharibifu wa ‘jiji hilo la umwagaji wa damu.’ Hukumu ya Mungu juu ya jiji hilo ilisimamishwa kwa muda watu walipokubali ujumbe wa Yona. Hata hivyo, Waninawi walirudia matendo yao maovu. Nahumu alitabiri hivi: “Ninawi . . . , utaliwa na upanga . . . Hakuna kitulizo cha msiba wako.” (Nahumu 3:1, 7, 15, 19; Yona 3:5-10) Wakati huohuo, Mungu alimtumia Sefania kutabiri kwamba Ninawi lingekuwa mahame yenye ukiwa. (Sefania 2:13) Je, jiji hilo kuu la kisiasa lisiloweza kushindwa lingeshindwa kama Yehova alivyotabiri? Swali hilo lilijibiwa mwaka wa 632 K.W.K. wakati Wababiloni, Wasikithe, na Wamedi walipolizingira Ninawi. Mafuriko ya ghafula yaliubomoa ukuta wake, na wavamizi wakaingia jijini. (Nahumu 2:6-8) Muda si muda, jiji hilo ambalo lilikuwa na nguvu sana likawa rundo la magofu. Ninawi lingali ukiwa hadi leo.a Hilo “jiji lenye furaha” halikuweza kulizuia neno la Mungu lisitimie!—Sefania 2:15.
13. Ni uthibitisho gani unaoonyesha kwamba unabii wa wale manabii 12 ulitimia?
13 Unabii kuhusu Ninawi ni mfano mmoja tu wa unabii mwingi uliotimizwa. Hebu tazama ramani ya kisasa ya Mashariki ya Kati. Je, unaweza kupata Amoni, Ashuru, Babiloni, Edomu, au Moabu? Huwezi! Ingawa mataifa hayo yalikuwa maarufu wakati mmoja, wale manabii 12 walitabiri kwamba yangetoweka. (Amosi 2:1-3; Obadia 1, 8; Nahumu 3:18; Sefania 2:8-11; Zekaria 2:7-9) Mataifa hayo yalitoweka kabisa, taifa moja baada ya lingine. Yehova alisema kwamba hayangekuwapo tena, na ndivyo ilivyotukia! Na utabiri wa manabii hao kuhusu kurudi kwa mabaki ya Wayahudi kutoka utekwani Babiloni ulitimia kikamili!
14. Kwa nini unaweza kutegemea ahadi za Yehova na kuzizingatia maishani mwako?
14 Uthibitisho huo wa kwamba Yehova ana uwezo wa kutoa unabii unakupa uhakika gani? Unaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atatimiza ahadi zake; yeye ni Mungu “asiyeweza kusema uwongo.” (Tito 1:2) Isitoshe, Mungu anatujulisha katika Neno lake mambo tunayohitaji kujua. Unaweza kutegemea maneno ya Yehova ya unabii na kuzingatia kufanya mapenzi yake maishani mwako. Vile vitabu 12 havizungumzii tu unabii uliotimizwa zamani. Kuna unabii mwingi unaoendelea kutimizwa sasa na mwingine utatimizwa hivi karibuni. Kwa hiyo, vitabu hivyo 12 vinaweza kukusaidia kuwa na uhakika kwamba unabii unaohusu nyakati zetu na wakati ujao utatimizwa. Zingatia kabisa unabii huo.
Jiji la Ninawi lilionekana haliwezi kushindwa, hata hivyo, unabii wa Yehova ulitimizwaje?
BABA ANAYEJALI
15. Hali ya Mika itakusaidiaje unapokabili matatizo fulani maishani?
15 Mungu hutabiri mambo mengine yenye kutegemeka mbali na kutoa unabii kuhusu mataifa au hali ya ulimwengu. Yehova hutabiri na kutimiza unabii kwa njia ambazo zinakuhusu wewe binafsi. Jinsi gani? Huenda nyakati nyingine ukakabili matatizo fulani maishani mwako. Unajua kwamba huhitaji tu mtu anayeelewa hali yako, bali mtu unayeweza kumtumaini akusaidie. Katika karne ya nane K.W.K., haikosi Mika alikuwa mpweke sana alipokabili watu wa Yuda wenye kiburi. Huenda alidhani kwamba yeye peke yake ndiye aliyekuwa mwaminifu duniani, hivi kwamba hangeweza hata kuwatumaini watu wa familia yake. Kila mahali, alipata watu wenye kiu ya damu, wadanganyifu, na wafisadi. Hata hivyo, Mika alitiwa nguvu na ahadi za Mungu kwamba atawatunza waaminifu Wake bila kujali wanavyotendewa na wengine. Wewe pia unaweza kutiwa moyo, hasa ikiwa wewe ni mwabudu wa Yehova na unajikuta ukiwa peke yako au ukiwa na waabudu wachache wa Yehova, miongoni mwa watu wengi wasiomheshimu Mungu.—Mika 7:2-9.
16. Kwa nini unaweza kuwa na hakika kwamba Mungu anaona ufisadi na ukandamizaji na kwamba atawakomboa waadilifu?
16 Wafalme wasio waaminifu walipokuwa wakitawala Yuda na Israeli, matajiri na wenye mamlaka walikuwa wenye pupa na waliwakandamiza wengine kama ilivyo kawaida leo. Utumwa haramu ulisitawi kwa sababu ya kodi za juu na unyakuzi wa mashamba. Maskini walionewa, hata walitendewa kikatili. (Amosi 2:6; 5:11, 12; Mika 2:1, 2; 3:9-12; Habakuki 1:4) Kupitia wajumbe wake, Mungu alisema wazi kwamba hawezi kuvumilia ufisadi na uonevu na kwamba atawaadhibu wale wanaoendelea kutenda uovu. (Habakuki 2:3, 6-16) Anatabiri kwamba ‘atanyoosha mambo kuhusu mataifa yenye nguvu’ na kwamba watumishi wake waaminifu “wataketi, kila mtu chini ya mzabibu wake na chini ya mtini wake, wala hakutakuwa na mtu yeyote anayewatetemesha.” (Mika 4:3, 4) Hebu wazia jinsi habari hiyo ilivyo yenye kutia moyo! Mungu ametabiri na kutimiza mambo mengine mengi. Unaweza kuwa na hakika kwamba ahadi hiyo itatimia pia, sivyo?
17, 18. (a) Kwa nini Mungu anawapa watu tumaini? (b) Tunapaswa kuionaje nidhamu ya Yehova?
17 Yehova hatimizi ahadi zake ili tu kuthibitisha kwamba ana uwezo wa kutabiri, kana kwamba anataka kuwapendeza wanadamu. Matendo yake yote yanachochewa na upendo unaotegemea kanuni, kwa sababu “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:8) Mkumbuke Hosea, aliyeishi katika karne ya nane K.W.K. Kama vile Gomeri, mke wa Hosea alivyokosa kuwa mwaminifu kwake, ndivyo Waisraeli walivyokosa kuwa waaminifu kwa Yehova. Ibada yao ya sanamu ilikuwa kama uzinzi; walichanganya ibada ya Baali na ibada safi ya Yehova. Pia, kwa njia ya mfano, ‘walifanya uasherati’ na Ashuru na Misri. Yehova angechukua hatua gani? Hosea alipaswa kujitahidi kumtafuta mkewe asiye mwaminifu na kumrudisha. Upendo ulimchochea Yehova kuwatafuta watu wake. “Nilizidi kuwavuta kwa kamba za mtu wa udongo, kwa kamba za upendo, . . . nami kwa upole nikamletea kila mmoja wao chakula.” (Hosea 2:5; 11:4) Ikiwa wangetubu kwa unyoofu, Mungu angewasamehe, na wangekuwa tena na uhusiano mzuri pamoja naye. (Hosea 1:3, 4; 2:16, 23; 6:1-3; 14:4) Je, huchochewi na upendo wa Yehova? Jiulize, ‘Ikiwa Yehova alionyesha upendo wa aina hiyo wakati uliopita, je, sina sababu ya kuwa na hakika katika upendo wake mwororo, mshikamanifu, usiobadilika, na unaodumu?’—Hosea 11:8.
18 Vile vitabu 12 vya kinabii vinaweza pia kukusaidia kutambua kwamba upendo wa Mungu unaweza kuhusisha nidhamu. Yehova aliwahakikishia watu wake walioasi kwamba ‘hangewaangamiza kabisa.’ (Amosi 9:8) Nidhamu ilipohitajika, Mungu hakukosa kuwatia nidhamu, hata hivyo, walipaswa kujua kwamba nidhamu yake ingekuwa ya muda! Andiko la Malaki 1:6 linamfananisha Yehova na baba mwenye upendo. Unajua kwamba baba anaweza kuwatia nidhamu watoto wake wapendwa ili kuwarekebisha. (Nahumu 1:3; Waebrania 12:6) Hata hivyo, upendo wa Baba yetu wa mbinguni humfanya asiwe mwepesi wa hasira, na andiko la Malaki 3:10, 16 hutuhakikishia kwamba atawabariki sana watumishi wake.
19. Unapaswa kujiuliza maswali gani ya kujichunguza?
19 Malaki anaanza kitabu chake kwa kutuhakikishia hivi: “‘Nimewapenda ninyi,’ Yehova amesema.” (Malaki 1:2) Unapofikiria uhakikishio huo wa Mungu kwa Waisraeli, jiulize: ‘Je, kuna lolote ninalofanya ambalo huenda likanizuia nisifaidike na upendo wa Mungu? Je, kuna lolote ambalo ningependa kujua kuhusu upendo wa Mungu linaloweza kunifaidi zaidi?’ Ukielewa upendo wa Mungu vizuri zaidi, unaweza kuwa na hakika kwamba atakupenda milele.
MSAMAHA HULETA WOKOVU
20. Msamaha kutoka kwa Mungu huletaje wokovu?
20 Unaposoma vitabu hivi vya kinabii, utatambua kwamba nyakati nyingine Yehova alitoa unabii wa maangamizi. Kwa nini? Mara nyingi alifanya hivyo ili kuwachochea watu wake watubu. Ili kutimiza hilo, aliwaruhusu wageni waharibu Samaria mwaka wa 740 K.W.K. na Yerusalemu mwaka wa 607 K.W.K. Mambo ambayo Mungu alitabiri yalitimizwa, lakini baadaye aliwaruhusu wale waliotubu warudi katika nchi yao. Naam, vitabu hivyo vinakazia kwamba Mungu husamehe kwa neema na kuwakubali wale wanaoacha dhambi na kumrudia. (Habakuki 3:13; Sefania 2:2, 3) Mika alichochewa kutangaza hivi: “Ni nani aliye Mungu kama wewe, anayesamehe kosa na kuuachilia ukosaji wa mabaki ya urithi wake? Hatashikilia hasira yake milele, kwa maana yeye hupendezwa na fadhili zenye upendo.” (Mika 7:18; Yoeli 2:13; Zekaria 1:4) Utimizo wa unabii unathibitisha hivyo.
21. (a) Wale manabii 12 wanasema nini kumhusu Masihi? (b) Ni unabii gani kumhusu Masihi unaokupendeza?
21 Yehova alitaja msingi halali wa msamaha wa kudumu alipotabiri kwamba Masihi angekuja na kutoa uhai wake wa kibinadamu kuwa “fidia inayolingana” kwa ajili ya wanadamu wenye dhambi. (1 Timotheo 2:6) Amosi alitabiri kuhusu mabadiliko ambayo Masihi, mwana wa Daudi angeleta. (Amosi 9:11, 12; Matendo 15:15-19) Mika hata alitabiri kuhusu mahali hususa ambapo Yesu angezaliwa, yule ambaye angewaletea uzima wote ambao wangekuwa na imani katika dhabihu Yake. (Mika 5:2) Na Zekaria alimtaja “Chipukizi,” Yesu, ambaye “ataketi na kutawala juu ya kiti chake cha ufalme.” (Zekaria 3:8; 6:12, 13; Luka 1:32, 33) Bila shaka, imani yako itaimarishwa ukichunguza unabii mwingine zaidi kama huo.—Ona sanduku “Unabii Kumhusu Masihi.”
22. Mambo ambayo wale manabii 12 wanafunua kumhusu Yehova yatakusaidiaje kuwa na uhakika zaidi kumwelekea?
22 Unaposoma ujumbe wa wale manabii 12, utakuwa na uhakika zaidi katika ushindi wa mwisho wa Mungu. Yehova ndiye Mtetezi wetu, na ataleta haki ya kweli. Neno la Mungu linadumu. Yeye hukumbuka mapatano yake na watu wake, huwajali watumishi wake, naye huwakomboa kutoka kwa wote wanaowakandamiza. (Mika 7:8-10; Sefania 2:6, 7) Yehova hajabadilika. (Malaki 3:6) Inatia moyo kama nini kujua kwamba hakuna matatizo wala vizuizi vyovyote vinavyoweza kumzuia Mungu asitimize kusudi lake! Anaposema kwamba siku yake ya hukumu itakuja, lazima itakuja. Kwa hiyo, endelea kuitazamia siku ya Yehova! “Yehova atakuwa mfalme juu ya dunia yote. Katika siku hiyo Yehova atakuwa mmoja, na jina lake litakuwa moja.” (Zekaria 14:9) Ametabiri hilo; naye atalitimiza.
a Mnamo Novemba 2002, kabla ya vita kuzuka nchini Iraki, Profesa Dan Cruickshank alizuru eneo hilo. Aliripoti hivi kwenye televisheni ya shirika la utangazaji la BBC: ‘Pembeni mwa jiji la Mosul kuna magofu ya jiji kubwa la Ninawi. Kuanzia miaka ya 1840 na kuendelea, waakiolojia wa Uingereza wenye hamu ya uvumbuzi walichimbua magofu ya jiji hilo pamoja na ya jiji la Nimrud. Kutembelea majiji hayo ya Ashuru kuliongoza kwenye uvumbuzi wa ustaarabu wa kale sana. Ustaarabu huo uliokuwa umesahaulika, umetajwa kifupi katika Biblia.’
-
-
“Mtafuteni Yehova” Kupitia Ibada InayompendezaIzingatie Siku ya Yehova Maishani
-
-
SURA YA TANO
“Mtafuteni Yehova” Kupitia Ibada Inayompendeza
1. Ni baraka gani ulizo nazo miongoni mwa watu wa Mungu?
UNA pendeleo kubwa sana la kumjua Mungu ambaye hutimiza unabii! Unaweza kujionea utimizo wa maneno haya ya nabii Hosea: “Nitakuchumbia uwe wangu katika uaminifu; nawe hakika utamjua Yehova.” Hosea alikuwa akizungumzia hali zenye usalama zinazofanana na paradiso, ambazo watu wa Mungu wangefurahia baada ya kurudi kutoka uhamishoni Babiloni. Vivyo hivyo, watu wa Mungu leo wanafurahia ufanisi na usalama wa kiroho; hali yao ni kama paradiso. (Hosea 2:18-20) Sasa, kwa kuwa wewe ni mtumishi wa Mungu aliyejiweka wakfu, unaitwa kwa jina lake, yaani, wewe ni Shahidi wa Yehova. Hapana shaka kwamba ungependa kuendelea kuitwa kwa jina hilo.—Isaya 43:10, 12; Matendo 15:14.
Amosi
2, 3. (a) Kwa nini Yehova alichukia ibada ya watu wake wa zamani? (b) Kwa nini tunapaswa kufikiria kwa uzito ujumbe wa wale manabii?
2 Taifa la Israeli la kale lilikuwa wakfu kwa Yehova, aliyewapa sheria ambazo hakuna taifa lingine lolote lilipata. (Kumbukumbu la Torati 4:33-35) Hata hivyo, kufikia mwishoni mwa karne ya tisa K.W.K., hali ya Waisraeli ilikuwa imebadilika sana hivi kwamba Mungu alimtumia nabii Amosi awaambie: “Nimechukia, nimezikataa sherehe zenu . . . Mkinitolea matoleo mazima ya kuteketezwa, hata katika matoleo yenu ya zawadi sitapata furaha.” (Amosi 5:21, 22) Ingawa Mungu hasemi hivyo kuhusu kutaniko lake la ulimwenguni pote leo, ungehisije ikiwa ungemsikia akisema hivyo kuhusu ibada yako binafsi? Je, kuna lolote ambalo kila mmoja wetu anaweza kujifunza?
3 Zamani hizo, watu wa Mungu walidai kwamba walikuwa wakimwabudu Yehova katika njia inayompendeza. Hata hivyo, wengi wao walikuwa wakiitumikia miungu ya kipagani, kama vile Baali wa Wakanaani na sanamu za ndama, au walikuwa wakitoa dhabihu katika mahali pa juu. Walikuwa wakiliinamia jeshi la mbinguni huku wakitoa viapo kwa Yehova. Kwa hiyo, Mungu wa kweli aliwatuma manabii wawahimize watu wamrudie katika ibada ya kweli. (2 Wafalme 17:7-17; 21:3; Amosi 5:26) Basi, ni wazi kwamba hata watumishi waliojiweka wakfu kwa Mungu wanapaswa kuzingatia matendo na mitazamo yao ili kuhakikisha kwamba inapatana na ibada ambayo inampendeza Yehova.
“KUMJUA MUNGU”
4. Ni hali gani zilizokuwako wakati wa utawala wa Mfalme Yeroboamu wa Pili?
4 Hebu wazia wakati ambapo nabii wa kwanza kati ya wale manabii 12 alipotangaza ujumbe wa Mungu. Ilitabiriwa kwamba siku ya Yehova dhidi ya ufalme wa Israeli wenye makabila kumi ingekuja. Hata hivyo, ilionekana kwamba taifa hilo lilikuwa na ufanisi. Kama vile Yona alivyotabiri, Mfalme Yeroboamu wa Pili alirudisha mpaka wa Israeli kutoka kaskazini kuelekea Damasko hadi Bahari ya Chumvi. (2 Wafalme 14:24-27) Ingawa Yeroboamu alifanya yaliyokuwa mabaya, Yehova alivumilia, wala hakutaka kulifagilia mbali taifa la Israeli. Mungu aliwapa Waisraeli wakati wa kutosha ili watubu, ‘wamtafute Yehova na kuendelea kuishi.’—Amosi 5:6.
5. Yehova aliwakataa Waisraeli kwa sababu gani?
5 Waisraeli waliokuwa na ufanisi wangeweza kuutumia wakati huo kumrudia Yehova kwa kujifunza juu yake na kufanya mambo yanayompendeza. Badala yake, walijitegemea na kuhisi kwamba ‘taabu hiyo haitakuja karibu wala kuwafikia.’ (Amosi 9:10) Tunaweza kusema kwamba walimsahau Yehova kwa kuwa “walishiba, kisha moyo wao ukaanza kujiinua.” (Hosea 13:6) Hatupaswi kuhisi kwamba hiyo ni historia ya kale tu ambayo haituhusu. Ona ni kwa nini Yehova alikuwa na kesi dhidi ya Waisraeli: “Kwa kuwa wewe mwenyewe umeukataa ujuzi, mimi pia nitakukataa wewe usiwe kuhani kwangu.” Walikuwa wakfu kwa Yehova nao walizungukwa na washiriki wa familia waliokuwa wakfu. Hata hivyo, wao binafsi walikosa “kumjua Mungu.”—Hosea 4:1, 6.
6. Waisraeli walikosa kumjua Mungu katika maana gani?
6 Si kwamba hawakuwa wamesikia maneno ya Mungu, ambayo wazazi Waisraeli walipaswa kuwafundisha watoto wao. Haikosi wengi wao walikuwa wamesikia masimulizi fulani ya Biblia kutoka kwa wazazi wao, katika mazungumzo, au kwenye makusanyiko. (Kutoka 20:4, 5; Kumbukumbu la Torati 6:6-9; 31:11-13) Kwa mfano, walikuwa wamesikia yaliyompata Haruni alipomfanyiza yule ndama wa dhahabu wakati ambapo Musa alikuwa amepanda Mlima Sinai kupokea zile Amri Kumi. (Kutoka 31:18–32:9) Kwa hiyo, Waisraeli walioishi siku za manabii hao walikuwa na ujuzi fulani kuhusu Sheria nao walikuwa wamesikia masimulizi ya kihistoria. Hata hivyo, ujuzi wao ulikuwa bure kwa kuwa haukuwachochea kumwabudu Mungu katika njia ambayo yeye alitaka.
Mtu anaweza kuanzaje kumsahau Yehova?
7. (a) Waisraeli waliachaje kwa urahisi kumtii Mungu? (b) Mkristo anaweza ‘kuanzaje kumsahau Mtengenezaji wake’?
7 Huenda ukauliza, ‘Waisraeli wangewezaje kunaswa kwa urahisi hivyo hata waache kumtii Mungu?’ Hosea anaeleza ilivyokuwa: “Israeli akaanza kumsahau Mtengenezaji wake.” (Hosea 8:14) Neno la Kiebrania linatafsiriwa vizuri hapa kwa maneno “wakaanza kumsahau.” Waisraeli hawakumsahau Yehova ghafula. Badala yake, kadiri muda ulivyopita walianza kusahau umuhimu wa kumwabudu katika njia inayompendeza. Je, unafikiri kwamba Mkristo anaweza kutumbukia katika mtego kama huo? Kwa mfano, mfikirie mtu ambaye anachukua kwa uzito jukumu lake la kuandalia familia yake. (1 Timotheo 5:8) Ili afanye hivyo, lazima aione kazi yake kuwa muhimu. Huenda hali fulani ikazuka, naye ahisi kwamba hana budi kukosa mikutano fulani ya Kikristo ili afanye kazi. Baada ya muda, huenda ikawa rahisi zaidi kwake kukosa mikutano, na muda si muda liwe zoea lake. Uhusiano wake na Mungu unadhoofika polepole—tayari ‘ameanza kumsahau Mtengenezaji wake.’ Mkristo ambaye wazazi wake au watu wake wa ukoo si waamini, anaweza pia kukumbwa na hali kama hiyo. Anahitaji kuamua kiasi cha wakati atakachotumia pamoja nao, naye atafanya hivyo wakati gani. (Kutoka 20:12; Mathayo 10:37) Atahitaji pia kuamua kiasi cha wakati kinachoweza kutumiwa kwa ajili ya safari mbalimbali, mapendezi ya kibinafsi, au burudani.
8. Katika siku za Amosi, “usafi wa meno” ulimaanisha nini?
8 Sisi tumejifunza Neno la Mungu na kuutumia ujuzi wetu. Hata hivyo, kila mmoja wetu anapaswa kufikiria kwa uzito maneno fulani yanayotumiwa katika kitabu cha Amosi: “usafi wa meno.” Kupitia Amosi, Mungu aliwaonya watu Wake hivi: “Mimi pia, niliwapa ninyi usafi wa meno katika majiji yenu yote na upungufu wa mkate katika mahali penu pote.” (Amosi 4:6) Usafi huo haukutokana na kupiga mswaki. Ulitokana na kutokula chochote, kutokana na njaa. Isitoshe, hilo lilikuwa onyo kuhusu ‘njaa wala si njaa ya mkate, na kiu, wala si kiu ya maji, bali ya kuyasikia maneno ya Yehova.’—Amosi 8:11.
Mkristo anawezaje kufa njaa kiroho ajapokuwa na chakula kingi cha kiroho?
9, 10. (a) Mkristo anawezaje kufa njaa kiroho? (b) Kwa nini tunapaswa kuwa macho kuona hatari za kufa njaa kiroho?
9 Kwa njia ya kiroho, mambo ambayo Amosi alitaja yanatimizwa na hali yenye kusikitisha ya Jumuiya ya Wakristo. Kinyume na hilo, “malango ya mbinguni” yamefunguliwa kwa ajili ya watu wa Mungu ulimwenguni pote. Wamebarikiwa kwa chakula kingi cha kiroho. (Malaki 3:10; Isaya 65:13, 14) Ingawa hivyo, huenda Mkristo akajiuliza, ‘Mimi binafsi ninafurahia kwa kadiri gani chakula hicho cha kiroho?’ Watafiti wamegundua kwamba sehemu ya ubongo wa wanyama inayochochea hamu ya kula inapovurugwa, wanyama hao hupoteza hamu ya kula hivi kwamba wanaweza kufa njaa ingawa kuna chakula kingi! Je, Mkristo anaweza kuwa na njaa kiasi cha kufa kiroho ajapokuwa na chakula kingi cha kiroho?
10 Unapozingatia hali yako mwenyewe, fikiria hili: Yehova aliwaandalia Waisraeli chakula kingi cha kiroho. Walikuwa na Sheria ambayo ingeweza kuimarisha uhusiano wao pamoja na yeye; walikuwa na programu ya elimu ya kukazia ujuzi wa Mungu katika akili za watoto wao; nao walikuwa na manabii ambao wangewasaidia kuelewa mapenzi ya Mungu. Hata hivyo, walianza kumsahau Yehova. Biblia inasema kwamba katika siku za Hosea, “walishiba [kimwili], kisha moyo wao ukaanza kujiinua.” (Hosea 13:6; Kumbukumbu la Torati 8:11; 31:20) Ikiwa hatutaki hali yetu ya kimwili iwe muhimu kuliko uhusiano wetu na Mungu, tunapaswa kukumbuka kila siku hatari hiyo inayotukabili.—Sefania 2:3.
ZINGATIA MAMBO MAZITO ZAIDI
11, 12. (a) Wakati wa utawala wa Mfalme Uzia, kwa nini manabii walihitaji kuwatia moyo watu wamrudie Yehova? (b) Yoeli alikazia uhitaji gani?
11 Yeroboamu wa Pili alipokuwa akitawala Israeli, Uzia (aliyeitwa pia Azaria) alikuwa akitawala Yuda. Alipanua eneo lake na kupanua Yerusalemu. Uzia “alionyesha nguvu kwa kiwango kisicho cha kawaida” kwa sababu “Mungu wa kweli a[li]endelea kumsaidia.” Pia, “akaendelea kufanya yaliyokuwa sawa machoni pa Yehova,” naye “akaendelea kuwa na mwelekeo wa kumtafuta Mungu.” Hata hivyo, watu wengi katika Yuda waliendelea kufukiza moshi wa dhabihu katika sehemu za juu.—2 Mambo ya Nyakati 26:4-9.
12 Unaweza kuona kwamba ingawa watu wa Yuda na Israeli waliitwa kwa jina la Mungu, mara nyingi ibada yao ilitia ndani mambo ambayo hayakumpendeza. Manabii walijaribu kuwasaidia watofautishe ibada ya kweli na ibada ya uwongo. Mungu aliwasihi hivi kupitia Yoeli: “Rudini kwangu kwa mioyo yenu yote, kwa kufunga, kwa kulia, na kwa kuomboleza.” (Yoeli 2:12) Kumbuka: Mungu alitaka watu wake wamrudie ‘kwa mioyo yao yote.’ Naam, tatizo lilikuwa mioyoni mwao. (Kumbukumbu la Torati 6:5) Kwa njia fulani, walikuwa wakimwabudu Yehova kidesturi tu, kwa mioyo nusu-nusu. Alikazia tena na tena kupitia manabii umuhimu wa fadhili zenye upendo, haki, na unyenyekevu—sifa ambazo hutoka moyoni.—Mathayo 23:23.
13. Wayahudi waliorudi kutoka uhamishoni Babiloni walihitaji kuzingatia nini?
13 Halafu, fikiria yaliyotokea baada ya Wayahudi kurudi nyumbani. Ingawa ibada ya kweli inayopatana na Sheria ilirudishwa, mambo hayakuwa shwari. Wayahudi walifunga siku zilezile ambazo matukio yaliyohusianishwa na uharibifu wa Yerusalemu yalikuwa yakiadhimishwa. Yehova aliwauliza: “Je, kweli mlifunga kwa ajili yangu mimi?” Jiji hilo lilifanywa ukiwa kwa sababu Yehova alitekeleza haki, jambo ambalo hawakupaswa kuombolezea. Badala ya kutazama nyuma na kufunga kwa kuomboleza, Wayahudi hao walipaswa kushangilia, wakifurahi katika majira ya sherehe kwa sababu ya baraka za ibada ya kweli. (Zekaria 7:3-7; 8:16, 19) Isitoshe, walipaswa kuzingatia mambo mengine. Mambo gani? “Fanyeni hukumu kwa haki ya kweli; na mtendeane kwa fadhili zenye upendo na rehema . . . wala msipangiane jambo lolote baya mioyoni mwenu.” (Zekaria 7:9, 10) Sisi sote tunaweza kufaidika kutokana na mambo ambayo manabii hao waliwafundisha watu wa Mungu kuhusu kumwabudu Mungu kwa moyo wote.
14. (a) Waliorudi kutoka uhamishoni walipaswa kutia ndani nini katika ibada yao? (b) Manabii walikaziaje mambo mazito zaidi kuhusiana na ibada?
14 Ibada ya moyo wote inatia ndani nini? Watu wa Mungu walipaswa kufanya nini kabla na baada ya uhamisho? Viwango vya Mungu kuhusu maadili vilipaswa kufuatwa. Pia kulikuwa na mambo au matendo hususa ambayo Sheria iliwataka wafanye, kutia ndani kukusanyika ili kusikiliza na kujifunza mapenzi ya Mungu. Isitoshe, Mungu aliwatumia manabii wake kukazia uhitaji wa kusitawisha na kuonyesha fadhili zenye upendo, haki, upole, rehema, na kiasi. Ona jinsi Yehova alivyokazia mambo hayo: “Mimi ninapendezwa na fadhili zenye upendo, na si dhabihu; ninapendezwa na kumjua Mungu kuliko matoleo mazima ya kuteketezwa.” “Mjipandie mbegu kwa uadilifu; mvune kulingana na fadhili zenye upendo.” (Hosea 6:6; 10:12; 12:6) Mika alitangaza hivi: “Yehova anataka nini kutoka kwako ila kutenda haki na kupenda fadhili na kuwa na kiasi katika kutembea na Mungu wako?” (Mika 6:6-8) Naye nabii Sefania aliwahimiza hivi watu wa Mungu: “Mtafuteni Yehova, ninyi nyote mlio wapole wa dunia . . . Utafuteni uadilifu, utafuteni upole.” (Sefania 2:3) Sifa hizo ni muhimu ili kumwabudu Mungu kwa njia inayompendeza.
Je, unajitahidi kuwahubiria watu wa namna zote habari njema?
15. Kupatana na himizo la manabii, Wakristo wanapaswa kufanya nini katika ibada yao?
15 Sifa hizo zinatimiza nini katika ibada yetu? Unajua kwamba kuhubiri habari njema ya Ufalme ni muhimu. (Mathayo 24:14; Matendo 1:8) Lakini huenda ukauliza: ‘Je, mimi huona kazi ya kuhubiri katika eneo letu kuwa ngumu, au hata mzigo wenye kulemea? Au mimi huiona kazi hiyo kuwa nafasi ya kuwasaidia watu wanaohitaji kuusikia ujumbe wa Biblia wenye kuokoa uhai? Je, mimi huwaonyesha rehema?’ Ndiyo, rehema na fadhili zenye upendo zapaswa kutuchochea kuwaonya wengine kuhusu siku ya Yehova. Haki na uadilifu pia ni muhimu tunapojitahidi kuwafikia watu wa namna zote tukiwa na ujumbe huo.—1 Timotheo 2:4.
16, 17. Kwa nini upole na kiasi ni muhimu katika ibada yetu?
16 Pia, hebu fikiria wajibu wetu wa kuhudhuria mikutano ya Kikristo, ambayo unajua ni muhimu. (Waebrania 10:24, 25) Je, umefikiria jinsi kufanya hivyo huhusisha upole na kiasi? Wapole ni wanyenyekevu vya kutosha kukubali maagizo na kisha kuyatumia mambo wanayojifunza. Kwa kufanya hivyo wanatekeleza maamuzi ya hukumu ya Yehova. Mtu mwenye kiasi anajua kwamba amepungukiwa katika mambo fulani na anahitaji kutiwa moyo na kujifunza mengi zaidi kupitia mikutano.
17 Mifano hiyo inatusaidia kuona kwamba tunaweza kufaidika kutokana na mambo ambayo manabii hao walifundisha. Hata hivyo, vipi ikiwa unahisi kwamba unahitaji kufanya mabadiliko fulani kuhusu mambo hayo ambayo yametajwa? Au vipi ikiwa umefanya makosa mazito, na kila unapoyakumbuka dhamiri yako hukusumbua? Wale manabii 12 wanaweza kukupa faraja na msaada.
MRUDIE YEHOVA
18. (a) Wale manabii 12 wanaweza kumfariji nani hasa? (b) Unahisije kumhusu Yehova ambaye huwasihi watu wake wamrudie?
18 Kama vile tumeona, kazi ya manabii tunaochunguza haikuwa kushutumu na kulaumu tu. Walimwakilisha Yehova kwa kuwahimiza watu wamrudie. Hebu wazia hisia za Hosea alipokuwa akiwahimiza hivi: “Njooni, turudi kwa Yehova, kwa maana yeye mwenyewe amerarua vipande-vipande, lakini atatuponya. Alizidi kupiga, lakini atatufunga kitambaa. . . . Nasi tutajua, tutafanya bidii kumjua Yehova.” (Hosea 6:1-3) Ni kweli kwamba Yehova Mungu alitekeleza kwa haki hukumu dhidi ya Israeli, kisha Yuda. Hata hivyo, watu wake walipaswa kuyaona mapigo hayo kuwa hatua za kuwarudisha katika hali njema ya kiroho. (Waebrania 12:7-13) Ikiwa watu wa Yehova waliokuwa wameasi wangerudi, ‘angewaponya’ na ‘kuwafunga kitambaa.’ Hebu wazia akilini mwako mtu ambaye amepiga magoti ili kufunga jeraha la mwenzake kwa kitambaa. Sasa, wazia kwamba mtu huyo ni Yehova. Yehova ni Mungu mwenye rehema kama nini, Mungu ambaye huwafunga kwa kitambaa wale wanaotaka kumrudia! Je, hilo halituchochei kutaka kumrudia tukimtendea dhambi?—Yoeli 2:13.
19. Kumjua Yehova humaanisha nini?
19 Kumrudia Mungu humaanisha nini? Hosea anatukumbusha kwamba hatupaswi “kumjua” tu Mungu, bali tunapaswa ‘kufanya bidii kumjua Yehova.’ Kitabu kimoja cha kisasa cha marejeo kinasema hivi kuhusu andiko la Hosea 6:3: “Kuna tofauti kubwa kati ya kujua kumhusu Mungu na kumjua Mungu. Kama vile kusoma hadithi ya watu wawili wanaopendana ni tofauti kabisa na wewe mwenyewe kumpenda mtu.” Tunachohitaji si tu kuwa na ujuzi wa kijuu-juu kumhusu Yehova. Lazima awe halisi kwetu, Rafiki tunayeweza kumtumaini na kuzungumza naye kwa uhuru. (Yeremia 3:4) Tukiwa na uhusiano huo, tunaweza kujua jinsi anavyohisi tunapotenda kwa njia fulani, na hilo hutusaidia sana kumwabudu kwa njia inayompendeza.
20, 21. Mfalme Yosia aliutumiaje ujuzi wa Mungu maishani mwake?
20 Mfalme Yosia alituwekea mfano mzuri wa kufuata ibada ya kweli. Hebu fikiria mambo mengine aliyofanya. Kufikia wakati ambapo Yosia alianza kutawala, taifa hilo lilikuwa limeharibiwa na ibada ya sanamu, jeuri, na udanganyifu ambao ulikuwa umeenea sana wakati wa utawala wa Manase na Amoni. (2 Wafalme 21:1-6, 19-21) Lazima Yosia awe alichochewa sana na himizo la Sefania la ‘kumtafuta Yehova,’ kwa kuwa ‘alianza kumtafuta Mungu wa Daudi.’ Yosia alianzisha mradi wa kuondolea mbali ibada ya sanamu katika Yuda na hata katika eneo ambalo wakati mmoja lilikuwa ufalme wa kaskazini.—Sefania 1:1, 14-18; 2:1-3; 3:1-4; 2 Mambo ya Nyakati 34:3-7.
Yosia hakujitetea wakati ambapo kazi ya kusafisha ilipaswa kufanywa
21 Baada ya kazi hiyo ya kusafisha, Yosia aliendelea kumtafuta Yehova. Aliagiza hekalu lifanyiwe marekebisho. Kazi hiyo ilipokuwa ikiendelea, “kile kitabu cha sheria ya Yehova kupitia mkono wa Musa” kilipatikana. Huenda kilikuwa ile nakala ya awali ya Sheria. Yosia alitendaje aliposikia kitabu hicho kikisomwa? “Mara tu mfalme alipoyasikia maneno ya ile sheria, akayararua mavazi yake mara moja.” Pia, ‘aliurarua moyo wake’ na kutenda kulingana na yaliyosomwa. Hakujaribu kujitetea na kusema kwamba tayari alikuwa amefanya mengi. Je, unakumbuka matokeo ya marekebisho aliyofanya? “Siku zake zote [wana wa Israeli] hawakugeuka kando wasimfuate Yehova Mungu wa mababu zao.”—2 Mambo ya Nyakati 34:8, 14, 19, 21, 30-33; Yoeli 2:13.
Je, utafanya mabadiliko yoyote yanayohitajiwa ili ujipatanishe na viwango vya Biblia?
22. Unaweza kufaidikaje kutokana na mfano wa Yosia?
22 Huenda ukajiuliza, ‘Mimi mwenyewe ningetendaje?’ Je, kama Yosia, ungesikiliza maneno ya manabii hao na kubadili maoni na matendo yako kama ilivyohitajika? Ingawa hatuishi katika siku za Sefania na Yosia, ni wazi kwamba tunapaswa kuitikia ujumbe na shauri la Mungu leo. Kwa hiyo, ikiwa Mkristo anahisi moyoni mwake kwamba anahitaji kubadili maisha yake au ibada yake, ujumbe wa manabii hao 12 unaweza kumchochea kuchukua hatua.—Waebrania 2:1.
23. Ukiona kwamba unahitaji kufanya marekebisho fulani, unaweza kufanya nini?
23 Nyakati nyingine, huenda ukahisi kama Yona alivyohisi alipokuwa ndani ya tumbo la yule samaki mkubwa: “Nimefukuzwa kutoka mbele za macho yako! Nitapataje kuliona tena hekalu lako takatifu?” (Yona 2:4) Hata hivyo, maneno haya ya Yehova yanaweza kututia moyo kwelikweli, hasa sisi wanadamu ambao si wakamilifu na ambao hufanya makosa! “Rudini kwangu, nami nitarudi kwenu.” (Malaki 3:7) Ukiona kwamba unahitaji kuimarisha uhusiano wako na Yehova, wazee katika kutaniko lenu watafurahi kukusaidia. Mtu anapoendesha gari, huanza kwa mwendo wa polepole. Akiisha kuondoka, huwa rahisi kwake kuongeza mwendo. Wewe pia unaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atakukaribisha na kukusaidia, kwa kuwa yeye “ana neema na rehema, si mwepesi wa hasira naye ni mwingi wa fadhili zenye upendo.” (Yoeli 2:12-14) Bila shaka, ujumbe wa manabii hao huwatia moyo wote wanaomwabudu Mungu kwa njia inayompendeza.
Wengine wanahitaji ‘kumtafuta Yehova’ kwa kumrudia
-
-
“Haki Itiririke”—Siri ya Kumjua MunguIzingatie Siku ya Yehova Maishani
-
-
SURA YA SITA
“Haki Itiririke”—Siri ya Kumjua Mungu
1. Kwa nini wewe hupendezwa na haki?
KATIKA historia, kuna watu ambao wamepata umaarufu kwa kupigania haki. Hata hivyo, hebu fikiria hili: Watu hupendezwa na haki kwa kuwa wanadamu wameumbwa kwa mfano wa Mungu. Wewe binafsi hupendezwa na haki na hutaka wengine wakutendee kwa haki kwa sababu umeumbwa kwa mfano wa Yehova, ambaye “hupendezwa” na haki.—Yeremia 9:24; Mwanzo 1:27; Isaya 40:14.
2, 3. Kwa nini tuchunguze vitabu vya wale manabii 12 ili kujifunza kuhusu haki ya Yehova?
2 Unaposoma vitabu mbalimbali vya Biblia, unaweza kuielewa vizuri zaidi haki ya Mungu. Hata hivyo, utafaidika hasa kwa kuchunguza vitabu vya wale manabii 12. Haki inazungumziwa sana katika vitabu hivyo hivi kwamba tafsiri fulani yenye kitabu cha Hosea, Amosi, na Mika iliyochapishwa na shirika fulani la Biblia, inaitwa Justice Now! (Haki Sasa!). Kwa mfano, hebu fikiria jinsi Amosi alivyohimiza: “Haki itiririke kama maji, na uadilifu kama mto unaotiririka daima.” Ona jambo ambalo Mika alitanguliza katika mambo unayopaswa kufanya: “Yehova anataka nini kutoka kwako ila kutenda haki na kupenda fadhili na kuwa na kiasi katika kutembea na Mungu wako?”—Amosi 5:24; Mika 6:8.
3 Kwa hiyo, ili kumjua Yehova vizuri zaidi kiasi cha kuweza kumwiga, bila shaka tunahitaji kuelewa haki yake. Haki ya Yehova ni sehemu ya utu wake, kwa hiyo hatuwezi kusema kwamba tunamjua ikiwa hatuelewi haki yake. Hata watumishi wake wa kweli walijua kwamba “Yehova ni mpenda-haki.”—Zaburi 33:5; 37:28.
Habakuki
4. Eleza ni kwa nini maandishi ya wale manabii 12 yanaweza kuzidisha uhakika wako katika haki ya Mungu.
4 Muda fulani kabla Yehova hajatekeleza hukumu dhidi ya Yerusalemu, nabii Habakuki aliuliza hivi: “Ee Yehova, nililie msaada mpaka wakati gani? . . . Sheria hufa ganzi, na haki haitendeki kamwe. Kwa kuwa mwovu anamzingira mwadilifu, kwa sababu hiyo haki hupotoshwa.” (Habakuki 1:2, 4) Habakuki mwaminifu alikuwa amemjua Yehova kupitia Maandiko yaliyokuwako wakati huo na kupitia mambo ambayo yeye mwenyewe alijionea. Kwa hiyo, alikuwa na hakika kwamba Mungu hutegemeza haki na kuwatia moyo watu waionyeshe. Hata hivyo, nabii huyo alitaka kujua ni kwa nini Yehova anaruhusu uovu. Mungu alimhakikishia Habakuki kwamba Yeye angewatendea waaminifu kwa haki. (Habakuki 2:4) Ikiwa Habakuki na wengine wangeweza kuwa na uhakika kiasi hicho, wewe una sababu nzuri hata zaidi ya kuwa na uhakika. Kwa nini? Leo, tuna Biblia nzima, kwa hiyo sasa kuna habari nyingi kuhusu jinsi Yehova alivyoshughulika na watu na jinsi alivyoonyesha utu wake, kutia ndani haki. Kwa hiyo, wewe unaweza kumjua Yehova vizuri zaidi na kuwa na hakika kwamba haki yake ni kamilifu.
5. Ni jambo gani kuhusu haki linalotupendeza hasa?
5 Alipokuwa akiwatuma wajumbe kwa Israeli, Yehova alikazia kwamba ni muhimu kutenda kwa haki. (Isaya 1:17; 10:1, 2; Yeremia 7:5-7; Ezekieli 45:9) Ni wazi kwamba alikazia jambo hilo kupitia wale manabii 12. (Amosi 5:7, 12; Mika 3:9; Zekaria 8:16, 17) Yeyote anayesoma mambo waliyoandika anaweza kuona kwamba wanawahimiza watu watende haki katika shughuli zao za kila siku. Kuna njia nyingi tunazoweza kutumia mambo tunayojifunza kutoka katika vitabu hivyo 12. Hata hivyo, acheni tuchunguze maeneo mawili ambayo manabii hao walikazia haki kisha tuone jinsi tunavyoweza kutumia maishani mambo tunayojifunza.
HAKI KATIKA BIASHARA NA MAMBO YANAYOHUSU PESA
6, 7. Kwa nini haki katika biashara na katika mambo yanayohusu pesa ni jambo ambalo sisi sote tunapaswa kuhangaikia?
6 Yesu alisema: “Mwanadamu hataishi kwa mkate tu.” (Luka 4:4; Kumbukumbu la Torati 8:3) Hakudai kwamba hatuhitaji mkate, kwa kuwa lazima tule. Kwa walio wengi, hilo humaanisha kufanya kazi au kuwa na mtu fulani katika familia anayefanya kazi ili kuiruzuku. Hivyo ndivyo ilivyokuwa pia kwa watumishi wa kale wa Mungu. Baadhi yao walikuwa na kazi zao za kukuza mazao au kutengeneza vitu kama vile nguo, vyombo vya kupikia, au walikuwa maseremala. Wengine walikuwa waajiri, walioajiri watu wa kuvuna mashamba yao au kutengeneza unga, mafuta ya mizeituni au divai. Wengine walikuwa wafanyabiashara, walionunua na kuuza vitu. Au, huenda wengine walikuwa mafundi, waliorekebisha paa au ala za muziki.—Kutoka 35:35; Kumbukumbu la Torati 24:14, 15; 2 Wafalme 3:15; 22:6; Mathayo 20:1-8; Luka 15:25.
7 Je, unaweza kuona hali zinazolingana na hizo katika maisha yako mwenyewe au katika maisha ya rafiki zako na watu wako wa ukoo? Ni kweli kwamba, huenda njia zinazotumiwa kufanya kazi leo zikawa tofauti, hata hivyo, je hukubali kwamba Mungu angekuwa na maoni yaleyale kuhusu haki katika mambo hayo? Katika ujumbe aliotoa kupitia wale manabii 12, Yehova alionyesha kwamba anatarajia watu wake watende haki katika mambo yote maishani. Tunapochunguza mifano kadhaa, fikiria jinsi wewe binafsi unavyopaswa kuonyesha haki ya Mungu.—Zaburi 25:4, 5.
8, 9. (a) Kwa nini shutuma zilizo katika Malaki 3:5 zapasa kuchukuliwa kwa uzito? (b) Maandiko hupendekeza maoni gani yenye usawaziko kuhusu ajira na kazi?
8 Mungu alitangaza hivi kupitia nabii Malaki: “Nitawakaribia ninyi ili kuhukumu, nami nitakuwa shahidi wa haraka juu ya walozi, na juu ya wazinzi, na juu ya wale wanaoapa kwa uwongo, na juu ya wale wanaoupunja mshahara wa mfanyakazi, . . . wala hawakuniogopa mimi.” (Malaki 3:5) Naam, Yehova aliwashutumu wale waliowatendea wafanyakazi au vibarua wao isivyo haki. Hilo lilikuwa jambo zito kadiri gani? Aliliona tendo la kuwanyanyasa wafanyakazi sawa na kuwasiliana na pepo, uzinzi, na uwongo. Wakristo wanajua jinsi Mungu atakavyowahukumu ‘waasherati, wanaowasiliana na pepo, na waongo wote.’—Ufunuo 21:8.
9 Mambo yaliyokuwa yakitendeka kazini hayakuwa tu mambo yasiyofaa machoni pa wanadamu; haki ya Yehova ilihusika. Alisema kwamba kwa sababu ya hila za wale “wanaoupunja mshahara wa mfanyakazi,” ‘angewakaribia watu hao ili kuwahukumu.’ Ni kweli kwamba Mungu hakusema kwamba mwajiri anapaswa kukubali kila dai la mfanyakazi au kikundi cha wafanyakazi. Kutokana na mfano wa Yesu wa watu walioajiriwa kufanya kazi katika shamba la mizabibu unaweza kuona kwamba mwajiri ana haki ya kuamua mshahara na jinsi kazi itakavyofanywa. (Mathayo 20:1-7, 13-15) Kumbuka kwamba katika mfano wa Yesu, iwe walifanya kazi siku nzima au la, wafanyakazi wote walilipwa dinari moja, ‘mshahara wa siku moja’ waliokubaliana. Pia, tunaweza kuona kwamba mwajiri hakutumia udanganyifu ili kupata faida zaidi huku akiwanyanyasa walioajiriwa.—Yeremia 22:13.
10. Kwa nini tunapaswa kuzingatia jinsi tunavyowatendea wafanyakazi wetu?
10 Ikiwa una biashara yako na umewaajiri wafanyakazi au umempa mtu fulani kibarua, je, mshahara unaowalipa, mambo unayodai wafanye, na unyoofu na uharaka wa kuwalipa unapatana na kanuni ya Malaki 3:5? Ni vizuri kufikiria hilo kwa kuwa suala hilohilo la kutowatendea wafanyakazi kwa haki linazungumziwa katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo pia. Kuhusu wale wanaotenda isivyo haki katika mambo hayo, mwanafunzi Yakobo anauliza hivi: “Je, [Yehova] hawapingi ninyi?” (Yakobo 5:1, 4, 6) Basi, hatukosei tunapokata kauli hii: Wale wasiotenda kwa haki kuhusiana na “mshahara wa mfanyakazi” kwa kweli hawamjui Yehova, kwa kuwa hawaigi haki yake.
11, 12. (a) Andiko la Hosea 5:10 linakazia jambo gani lisilo la haki? (b) Unaweza kutumiaje kanuni ya Hosea 5:10?
11 Sasa soma uone jinsi Yehova alivyowapinga baadhi ya watu maarufu walioishi katika siku za Hosea: “Wakuu wa Yuda wamekuwa kama watu wanaosogeza nyuma mpaka. Nitamwaga ghadhabu yangu kama maji juu yao.” (Hosea 5:10) Hosea alikuwa akishutumu uovu gani? Mkulima Myudea alitegemea shamba lake ambalo mipaka yake ilitiwa alama kwa mawe au miti. ‘Kuusogeza nyuma mpaka’ kungelifanya shamba la mkulima liwe dogo na hivyo kumnyang’anya au kumwibia sehemu ya riziki yake. Hosea aliwalinganisha wakuu wa Yudea, ambao walipaswa kutetea haki za wengine, na watu wanaosogeza nyuma mipaka.—Kumbukumbu la Torati 19:14; 27:17; Ayubu 24:2; Methali 22:28.
Je, wewe hutumia kanuni ya haki katika shughuli zako za kibiashara?
12 Huenda watu fulani leo ambao hufanya kazi ya kuuza mashamba wakashawishiwa ‘kusogeza nyuma mipaka’ ili kuwadanganya wanunuzi. Hata hivyo, kanuni hiyo inawahusu pia wafanyabiashara, waajiri, wafanyakazi, na wateja, yaani, yeyote yule anayehusika katika mikataba au mapatano. Kama ujuavyo, wafanyabiashara fulani hawapendi kuandika mapatano yao, wakijua kwamba baadaye itakuwa rahisi zaidi wao kutotimiza mapatano yao au kudai mambo mengine. Wengine huandika mapatano yao lakini wanatia ndani mambo yasiyoeleweka vizuri ili wapotoshe maana yake kwa faida yao, hata ikiwa kutamwumiza yule mwingine isivyo haki. Je, unafikiri kwamba mtu anayetenda hivyo, awe ni mfanyabiashara au mteja, mwajiri au mfanyakazi, kwa kweli anamjua Mungu wa haki? Yehova alisema hivi katika Neno lake: “Usiusogeze nyuma mpaka [wa wavulana wasio na baba]. Kwa maana Mkombozi wao ana nguvu; yeye mwenyewe atatetea kesi yao dhidi yako wewe.”—Methali 23:10, 11; Habakuki 2:9.
13. Kulingana na Mika 6:10-12, watu wa kale wa Mungu walikuwa wakifanya mambo gani yasiyo ya haki?
13 Andiko la Mika 6:10-12 latusaidia kuielewa haki vizuri zaidi: “Je, bado kuna hazina za uovu katika nyumba ya mwovu, na kipimo cha efa kilichobanwa ambacho kimeshutumiwa? Je, naweza kuwa safi kiadili nikiwa na mizani ya uovu pamoja na mfuko wa mawe ya mizani ya udanganyifu? Kwa maana . . . wakaaji wake mwenyewe wamesema uwongo, na ulimi wao una udanganyifu.” Leo tunapima chakula kwa lita badala ya efa na kilo badala ya mawe ya mizani. Hata hivyo, wazo la Mika linaeleweka wazi. Wafanyabiashara wa siku zake walikuwa wadanganyifu; hawakutumia vipimo halali bali waliwatendea watu isivyo haki. Mungu aliwaita ‘waovu’ ambao “ulimi wao una udanganyifu kinywani mwao” na katika biashara zao.—Kumbukumbu la Torati 25:13-16; Methali 20:10; Amosi 8:5.
14. Onyo la Mika linaweza kutusaidia kuepuka mambo gani yasiyo ya haki yanayofanywa leo?
14 Je, maneno ya Mika kuhusu mawe ya mizani na vipimo vya udanganyifu yanahusu jinsi unavyofanya biashara yako au jinsi unavyojiendesha ukiwa mfanyakazi? Hilo ni jambo la kufikiria kwa kuwa kuna njia chungu nzima ambazo wateja hupunjwa. Kwa mfano, wajenzi wadanganyifu hutumia kiasi kidogo cha simiti kuliko kile kinachohitajiwa wanapokoroga saruji. Au, katika sehemu ambazo hazitaonekana, huenda fundi akatumia vifaa hafifu kuliko vile vilivyolipiwa. Wafanyabiashara fulani huuza vitu wakidai kwamba ni vipya kabisa na kumbe vimetumiwa. Na huenda wewe pia umesikia kuhusu mbinu nyinginezo za biashara ambazo hutumiwa ili kuongeza faida. Je, ungeshawishiwa kuzitumia? Kitabu cha karibuni kuhusu mambo yanayofanywa faraghani kilisema kwamba Mashahidi wa Yehova “wanaamini kwamba Muumba wao anawatazama, na hivyo afadhali wafe kuliko kuiba.” Pia, kilisema: “Watu wengi hutaka kuwaajiri hasa pesa nyingi zinapohusika.” Kwa nini? Kwa sababu Wakristo wa kweli wanajua kwamba Yehova ‘anataka watende haki,’ hata katika biashara zao na mambo yanayohusisha pesa.—Mika 6:8.
“WAKUU KWA AJILI YA HAKI”
15, 16. Viongozi wa siku za Mika waliwatendeaje watu?
15 Kutokana na vitabu vya manabii hao 12, ni wazi kwamba nyakati nyingine, kulikuwa na ukosefu mkubwa wa haki. Wale waliokuwa na mamlaka, ambao walipaswa kuwa kielelezo katika kutenda haki, hawakuwa wakifanya hivyo. (Kutoka 18:21; 23:6-8; Kumbukumbu la Torati 1:17; 16:18) Mika aliwasihi hivi: “Tafadhali sikieni, ninyi vichwa vya Yakobo na ninyi viongozi wa nyumba ya Israeli. Je, si wajibu wenu kujua haki? Ninyi mnaochukia yaliyo mema na mnaopenda ubaya, mnaochuna ngozi kutoka kwa watu na nyama kutoka kwa mifupa yao.”—Mika 3:1-3; Isaya 1:17.
16 Lazima maneno hayo yaliwashtua watu waliozoea maisha ya mashambani. Nyakati nyingine mchungaji angeweza kumkata manyoya mnyama aliyempenda na kumtunza. (Mwanzo 38:12, 13; 1 Samweli 25:4) Lakini “viongozi wa nyumba ya Israeli,” ambao walipaswa “kujua haki,” waliwahujumu watu wa malisho ya Mungu, kana kwamba walikuwa wakichuna ngozi na kurarua nyama ya kondoo na kuivunja mifupa yao vipande-vipande. (Zaburi 95:7) Akitumia mfano mwingine unaohusu maisha ya mashambani, Mika alisema kwamba wakuu ‘waliokuwa wakihukumu ili kupata thawabu’ walikuwa kama ukuta wa miiba. (Mika 7:3, 4) Hebu jiwazie ukipitia eneo lenye miiba mingi. Bila shaka utakwaruzwa, na mavazi yako yatararuka. Hilo laonyesha jinsi viongozi wa watu wa Mungu walivyokuwa. Badala ya kuwatendea ndugu zao kwa haki, walitumia hila na ufisadi.—Mika 3:9, 11.
17. Kulingana na Sefania 3:3, viongozi walikuwa na mtazamo gani?
17 Sefania alisema jambo kama hilo: “Wakuu wake katikati yake walikuwa simba wanaonguruma. Waamuzi wake walikuwa mbwa-mwitu wa jioni ambao hawakutafuna mifupa mpaka asubuhi.” (Sefania 3:3) Hebu wazia jinsi viongozi wa watu wa Mungu walivyokuwa! Walipuuza haki, na kujiendesha kama simba wanaonguruma. Na waamuzi waliokuwa kama mbwa-mwitu wenye pupa, wasiotosheka, walitafuna kila kitu hivi kwamba kufikia asubuhi mifupa tu ndiyo iliyopatikana. Haki ingeweza kutekelezwaje katika hali kama hizo? Haki ilipasuliwa vipande-vipande na viongozi waliowavizia watu badala ya kuwajali.
Wakuu katika siku za Mika na Sefania hawakumjua Yehova
18. Waamuzi katika Israeli walipaswa kuwatendeaje watu wa Mungu?
18 Ni wazi kwamba viongozi wa taifa lililokuwa wakfu kwa Mungu hawakumjua. Ikiwa wangalimjua, wangalitii maneno ya andiko la Zekaria 8:16: “Haya ndiyo mambo ambayo mnapaswa kufanya: Semeni ukweli kila mtu na mwenzake. Hukumuni kwa hukumu ya kweli na ya amani malangoni mwenu.” Wanaume wazee katika Israeli walikutana katika malango ya jiji ambapo walisikiliza kesi, si kwa kuchunguza mambo kijuu-juu tu wala kulingana na maoni yao wenyewe, bali kulingana na maoni ya Mungu. (Kumbukumbu la Torati 22:15) Yehova alikuwa amewaonya wasionyeshe upendeleo kuelekea watu waliokuwa na mali au waliokuwa maarufu. (Mambo ya Walawi 19:15; Kumbukumbu la Torati 1:16, 17) Waamuzi walipaswa kujaribu kurudisha amani kati ya pande mbili zilizokuwa zikizozana, wakitoa ‘hukumu ya amani.’
19, 20. (a) Kwa nini wazee Wakristo wanaweza kujifunza mengi kutokana na wale manabii 12? (b) Wazee wanaweza kuonyeshaje kwamba wanamjua Yehova na haki yake?
19 Mtume Paulo alinukuu sehemu ya andiko la Zekaria 8:16 alipokuwa akiwaandikia Wakristo. (Waefeso 4:15, 25) Kwa hiyo, tunaweza kuwa na hakika kwamba maonyo na mashauri yaliyotolewa na wale manabii 12 kuhusu haki yanatumika katika kutaniko leo. Wanaume wazee, au waangalizi, wanapaswa kuwa kielelezo katika kumjua Yehova na kuonyesha haki yake. Inapendeza kwamba andiko la Isaya 32:1 linawataja kuwa “wakuu kwa ajili ya haki.” Ni mambo gani muhimu tunayoweza kujifunza kuhusu wazee hao kutokana na maonyo na mashauri yaliyotolewa na wale manabii 12?
20 Wazee Wakristo wanapaswa kukumbuka kweli ya Kimaandiko na maoni ya Yehova. Wanapaswa kutegemea mambo hayo wanapofanya maamuzi badala ya kutegemea maoni yao wenyewe au hisia zao. Biblia inaonyesha kwamba huenda kukawa na kesi ngumu, ambazo zinahitaji wakati zaidi ili kujitayarisha, kufanya utafiti wa kibinafsi katika Biblia na vichapo vyenye shauri la hekima kutoka kwa jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara. (Kutoka 18:26; Mathayo 24:45) Wazee wanapojitahidi hivyo, bila shaka watachukia yaliyo mabaya na kupenda yaliyo mema kwa maoni ya Mungu. Kufanya hivyo kutawasaidia ‘kuipatia haki nafasi langoni’ ili ‘wafanye hukumu kwa haki ya kweli.’—Amosi 5:15; Zekaria 7:9.
21. Kwa nini wazee wanapaswa kuepuka kuonyesha ubaguzi, hata hivyo ni nini ambacho huenda kikawachochea kutenda kinyume?
21 Hata ikiwa yule aliye na jukumu la kuhukumu ana ujuzi wa Biblia, huenda akaonyesha ubaguzi. Malaki alisikitika kwa kuwa makuhani, waliopaswa kuwa na ujuzi, ‘walikuwa wakionyesha ubaguzi katika sheria.’ (Malaki 2:7-9) Hilo lingewezekanaje? Mika alisema kwamba baadhi ya waliokuwa vichwa ‘walikuwa wakitoa hukumu ili wale rushwa tu, na makuhani walikuwa wakifundisha ili tu wapate malipo.’ (Mika 3:11) Mzee anawezaje kuwa na maoni kama hayo? Vipi ikiwa mtu anayeshughulika naye amemwonyesha ukarimu wakati uliopita, au vipi ikiwa mzee huyo anaona kwamba huenda akafaidika kwa njia fulani wakati ujao? Au tuseme kwamba anashughulika na mtu wa jamaa yake. Je, maamuzi yake yatategemea vifungo vya familia au kanuni za kiroho? Huenda mzee akaonyesha ubaguzi anaposhughulikia visa vya ukosaji au anapokadiria iwapo mtu anastahili Kimaandiko kupata mapendeleo zaidi ya utumishi katika kutaniko.—1 Samweli 2:22-25, 33; Matendo 8:18-20; 1 Petro 5:2.
Katika shughuli zao zote, wazee ‘huipatia haki nafasi langoni’
22. (a) Wazee wana jukumu gani kuhusiana na haki? (b) Ni sifa gani nyingine za kiroho ambazo wazee wanapaswa kuonyesha wanaposhughulika na wakosaji?
22 Mtu anapofanya kosa zito, wachungaji wa kiroho katika kutaniko wanapaswa kuchukua hatua ya kulilinda dhidi ya uvutano hatari wenye kufisidi. (Matendo 20:28-30; Tito 3:10, 11) Hata hivyo, ikiwa mkosaji ametubu kikweli, wazee ‘watamrekebisha upya mtu huyo katika roho ya upole.’ (Wagalatia 6:1) Badala ya kuwa wakali, wanatii maagizo haya: “Fanyeni hukumu kwa haki ya kweli; na mtendeane kwa fadhili zenye upendo na rehema.” (Zekaria 7:9) Kanuni za Yehova kuhusu jinsi ya kushughulikia kesi mbalimbali katika Israeli la kale hukazia haki yake na rehema. Waamuzi waliowekwa rasmi walikuwa na uhuru wa kufanya maamuzi fulani; wangeweza kuonyesha rehema, ikitegemea hali na mtazamo wa mkosaji. Vivyo hivyo, waangalizi Wakristo wanapaswa kujitahidi kuhukumu “kwa haki ya kweli” na kuonyesha “fadhili zenye upendo na rehema,” na hivyo kuonyesha kwamba wamemjua Yehova.
23, 24. (a) Wazee wanaweza kutegemeaje ‘hukumu ya amani’? (b) Wale manabii 12 wamekusaidia kuelewa nini kuhusu haki?
23 Kumbuka maneno ya andiko la Zekaria 8:16: “Hukumuni kwa hukumu ya kweli na ya amani malangoni mwenu.” Lengo ni nini? ‘Hukumu ya amani.’ Hata wakati ambapo mitume walikuwa hai, kutoelewana na mizozo ilikuwapo kati ya Wakristo. Kama vile Paulo alivyofanya kuhusiana na Euodia na Sintike, huenda wazee leo wakahitaji kutoa msaada. (Wafilipi 4:2, 3) Bila shaka, wazee wanapaswa kujitahidi kutoa ‘hukumu ya amani,’ wakijaribu kurudisha amani kati ya pande mbili zinazozozana. Wanapaswa kutegemeza amani katika kutaniko na amani pamoja na Mungu kupitia mashauri ya Kimaandiko wanayotoa na mtazamo wao wanapofanya hivyo. Hivyo, itaonekana wazi kwamba kwa kweli wanamjua Yehova na haki yake.
24 Maeneo mawili ambayo yamezungumziwa, yanaonyesha kwamba katika maisha yetu ya kila siku ni muhimu kutumia mashauri ya wale manabii 12 kuhusu haki. Itakuwa baraka iliyoje ikiwa sisi na wale wanaotuzunguka tutaacha “haki itiririke”!
-
-
Mtumikie Yehova Kulingana na Viwango Vyake vya JuuIzingatie Siku ya Yehova Maishani
-
-
SURA YA SABA
Mtumikie Yehova Kulingana na Viwango Vyake vya Juu
1. Watu wa Yerusalemu walioishi siku za Sefania, walivionaje viwango vya Yehova?
“YEHOVA hatatenda mema, wala hatatenda mabaya.” Hayo ndiyo yaliyokuwa maoni ya watu wa Yerusalemu walioishi katika siku za Sefania. Walifikiri kwamba Yehova hakuwatazamia waishi kulingana na viwango vyovyote hususa. Sefania alisema kwamba walikuwa ‘wakiganda juu ya machicha yao,’ takataka ambazo hupatikana chini ya divai iliyohifadhiwa. Alimaanisha kwamba watu hao walitaka kutulia katika maisha yao ya starehe, wasisumbuliwe na tangazo lolote la kwamba Mungu ataingilia mambo yao. Hata hivyo, Mungu aliwaambia Wayahudi hao kwamba ‘angepekua Yerusalemu kwa uangalifu kwa kutumia taa’ na ‘kukazia fikira’ wale waliopuuza viwango vyake. Naam, Yehova ana viwango, naye huzingatia jinsi watu wanavyoviona.—Sefania 1:12.
2. Katika eneo lenu, watu kwa ujumla wana maoni gani kuhusu viwango?
2 Leo pia, watu wengi hawapendi kuishi kulingana na viwango. Huenda ukawasikia wakisema, “Fanya upendavyo!” Wengine huwaza hivi: ‘Ikiwa sina pesa za kutosha au siwezi kufanya mambo ninayotaka kufanya, hakuna ubaya kufanya lolote ninalohitaji kufanya ili kubadili hali hiyo.’ Hawazingatii hisia za Mungu wala mapenzi yake. Namna gani wewe? Je, kujua kwamba Mungu ameweka viwango ni jambo linalokupendeza?
3, 4. Viwango vina umuhimu gani?
3 Wengi ambao hupinga wazo la kuishi kulingana na viwango vya Mungu huwa tayari kukubali viwango vya mwanadamu katika mambo mbalimbali maishani. Kwa mfano, hebu fikiria viwango vya mwanadamu kuhusu maji. Serikali nyingi huweka viwango vya ubora wa maji wanayotaka raia watumie. Namna gani ikiwa viwango hivyo vinapuuzwa? Huenda hilo likasababisha kuharisha au magonjwa mengine yanayoenezwa na maji yasiyo safi, magonjwa ambayo huwaathiri watoto hasa. Basi, inaelekea kwamba wewe unafaidika na viwango vilivyowekwa vya maji ya kunywa. “Ikiwa hakungekuwa na viwango vyovyote, muda si muda tungejionea matokeo,” lasema Shirika la Kimataifa la Kuweka Viwango. “Mara nyingi hatuelewi umuhimu wa viwango katika kuongeza ubora, usalama, kutegemeka, na kuwapo kwa bidhaa mbalimbali, na pia katika kuandaa huduma kama hizo kwa gharama ya chini.”
4 Ikiwa unakubali kwamba kuna faida ya kuwa na viwango katika mambo mbalimbali maishani, basi je, si jambo linalopatana na akili kutazamia Mungu awe na viwango kwa ajili ya watu wanaoitwa kwa jina lake?—Matendo 15:14.
JE, VIWANGO VYA MUNGU NI VYENYE KUDAI MNO?
5. Yehova alionyeshaje kupitia Amosi umuhimu wa kuishi kulingana na viwango Vyake?
5 Unapojenga nyumba, viwango ni muhimu. Ikiwa ukuta mmoja hausimami wima, jengo lote linaweza kuporomoka. Au nyufa kati ya kuta zaweza kuifanya nyumba hiyo isikalike. Hivyo ndivyo Amosi alivyoiona hali ya taifa la Israeli la makabila kumi alipokuwa akitoa unabii katika karne ya tisa K.W.K. Alimwona Yehova juu ya ukuta huku ‘timazi ikiwa mkononi mwake.’ Mungu alisema: “Tazama, naweka timazi katikati ya watu wangu Israeli. Nami sitawasamehe zaidi tena.” (Amosi 7:7, 8) Timazi ni kidude fulani kizito ambacho huning’inizwa kwa kamba; hutumiwa kuhakikisha ikiwa ukuta uko wima kabisa. Ukuta wa mfano ambao Amosi alimwona Yehova akiwa amesimama juu yake ‘ulitengenezwa kwa timazi.’ Ukuta huo ulikuwa wima kabisa. Hata hivyo, katika siku za Amosi Waisraeli hawakuwa wima kiroho. Walikuwa sawa na ukuta uliokuwa umeinama, ambao ulihitaji kubomolewa kabla haujaporomoka.
6. (a) Ni jambo gani kuu linalopatikana katika vitabu vya wale manabii 12? (b) Kwa nini tunaweza kusema kwamba viwango vya Mungu si vyenye kudai mno?
6 Unapojifunza vitabu vya wale manabii 12, utaona jambo hili linalorudiwa-rudiwa: Ni muhimu kujipatanisha na viwango vya Mungu. Ujumbe ulio katika vitabu hivyo si shutuma tupu kuelekea watu ambao hawakuishi kulingana na viwango vya juu vya Mungu. Nyakati nyingine, Yehova alipowachunguza watu wake aliona kwamba waliishi kulingana na viwango vyake. Kwa kuwa wangeweza kufanya hivyo, basi ni wazi kwamba Yehova hadai mambo tusiyoweza kutimiza; wanadamu wasio wakamilifu wanaweza kuishi kulingana na viwango hivyo. Fikiria mfano mmoja.
7. Zekaria anatusaidiaje kuona kwamba wanadamu wasio wakamilifu wanaweza kufikia viwango vya Yehova?
7 Baada ya Wayahudi waliorudi kutoka Babiloni kuweka msingi wa hekalu, kazi yao ya kujenga upya ilisimama. Kwa hiyo Mungu aliwatuma manabii wake Hagai na Zekaria wawatie watu moyo waendelee na kazi. Kupitia maono aliyopata Zekaria, Yehova alimtaja Zerubabeli, gavana wa Yuda, akiwa na “timazi mkononi [mwake]” alipokuwa akiweka jiwe la juu kabisa la kumalizia ujenzi wa hekalu. Hekalu hilo lilijengwa kulingana na viwango vya Mungu. (Zekaria 4:10) Fikiria jambo hili lenye kupendeza kuhusu hekalu lililokuwa limekamilika: “Haya saba ndiyo macho ya Yehova. Yanaenda huku na huku duniani kote.” Mungu alimwona Zerubabeli akiweka jiwe la juu kabisa. Na kwa sababu macho yake huona kila kitu, aliona kwamba hekalu hilo lililokuwa limejengwa upya lilifaa machoni Pake. Naam, lililingana na viwango Vyake! Jambo kuu ni kwamba ingawa viwango vya Yehova ni vya juu, wanadamu wanaweza kuvifikia. Baada ya kutiwa moyo na Hagai na Zekaria, Zerubabeli na watu wake walifikia viwango hivyo. Kama Zerubabeli, wewe pia unaweza kuishi kulingana na viwango vya Mungu. Hilo ni jambo lenye kutia moyo sana!
KWA NINI TUKUBALI VIWANGO VYA YEHOVA?
8, 9. (a) Kwa nini Yehova ana haki ya kuwawekea wanadamu viwango? (b) Kwa nini Mungu alikuwa na haki ya kuwataka Waisraeli watii maagizo yake?
8 Akiwa Muumba, Mungu ana haki ya kuwawekea wanadamu viwango na kutazamia tuishi kulingana navyo. (Ufunuo 4:11) Si lazima Yehova atoe orodha ndefu ya kila kitu ambacho anataka wanadamu wafanye kwa kuwa aliwapa dhamiri ya kuwaongoza. (Waroma 2:14, 15) Mungu aliwaambia wanadamu wa kwanza wasile “matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya.” Mti huo uliwakilisha haki ya Mungu ya kuweka viwango kuhusu yaliyo mema na yaliyo mabaya. Unajua vizuri yaliyotokea. (Mwanzo 2:17; 3:1-19) Akizungumzia uamuzi mbaya aliofanya Adamu, Hosea aliandika hivi: “[Waisraeli] wenyewe, kama mtu wa udongo, wamevunja lile agano.” (Hosea 6:7) Hivyo, Hosea anaonyesha kwamba Waisraeli walitenda dhambi kimakusudi.
9 Ni dhambi gani hiyo waliyofanya? “Wamevunja lile agano [la Sheria].” Kwa kuwa Mungu aliwakomboa watu wake kutoka Misri, walikuwa mali yake na hivyo alikuwa na haki ya kuwawekea viwango. Waisraeli walilikubali agano la Yehova, na hivyo walikubali kuishi kulingana na viwango hivyo. (Kutoka 24:3; Isaya 54:5) Hata hivyo, wengi wao walishindwa kuifuata Sheria. Wakawa na hatia ya kumwaga damu, kuua, na kufanya uasherati.—Hosea 6:8-10.
10. Mungu alijaribu kuwasaidiaje wale walioshindwa kufikia viwango vyake?
10 Yehova aliwaweka manabii kama vile Hosea ili kuwasaidia watu wake waliokuwa wakfu. Mwishoni mwa kitabu chake cha kinabii, Hosea alitangaza hivi: “Ni nani aliye na hekima, apate kuelewa mambo haya? Mwenye busara, apate kuyajua? Kwa maana njia za Yehova zimenyooka, na waadilifu ndio watakaotembea katika hizo; bali wakosaji ndio watakaojikwaa katika hizo.” (Hosea 14:9) Mwanzoni mwa sura ya 14 ya kitabu cha Hosea, nabii huyo alikazia uhitaji wa kumrudia Yehova. Wenye hekima wangeelewa kwamba Yehova alionyesha njia zilizonyooka ambazo watu wake walipaswa kufuata. Ukiwa mtumishi aliye wakfu kwa Mungu, bila shaka ungependa kuendelea kutembea katika njia hizo zilizonyooka za Yehova.
Kwa nini wewe hutii viwango ambavyo Muumba aliweka na anavyopendekeza?
11. Kwa nini unapaswa kutii amri za Mungu?
11 Andiko la Hosea 14:9 latusaidia kuona faida za kufuata njia zilizonyooka. Kufuata matakwa ya Mungu hutokeza baraka na faida. Kwa kuwa ndiye Muumba, anajua umbo letu. Mambo anayotaka tufanye ni kwa faida yetu. Kwa mfano, uhusiano wetu na Mungu unaweza kulinganishwa na gari na fundi. Fundi huyo anajua jinsi gari hubuniwa na kutengenezwa. Anajua kwamba kila baada ya kilometa kadhaa gari huhitaji kubadilishwa mafuta ya injini. Ingekuwaje iwapo wewe ungepuuza kiwango hicho, labda kwa kusema kwamba gari halina shida? Muda si muda injini yake ingeacha kufanya kazi. Ndivyo ilivyo pia na wanadamu. Muumba wetu ametupa amri. Twaweza kufaidika kwa kuzitii. (Isaya 48:17, 18) Kujua kwamba kwa kweli tunafaidika hutuchochea hata zaidi kuishi kulingana na viwango vyake na kutii amri zake.—Zaburi 112:1.
12. Kutembea katika jina la Mungu kutaimarishaje uhusiano wetu naye?
12 Zawadi kubwa zaidi ambayo mtu anaweza kupata kwa sababu ya kutii amri za Mungu ni kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu. Tunapofuata viwango vyake na kuona kwamba si vyenye kudai mno navyo hutufaidi, upendo wetu kwa Mwanzilishi wa viwango hivyo huongezeka. Nabii Mika alifafanua uhusiano huo wa karibu kwa njia yenye kupendeza: “Vikundi vyote vya watu vitatembea kila kimoja katika jina la mungu wake; bali sisi tutatembea katika jina la Yehova Mungu wetu mpaka wakati usio na kipimo, naam, milele.” (Mika 4:5) Ni pendeleo lililoje kutembea katika jina la Yehova, kumletea sifa, na kutambua kwamba ana mamlaka maishani mwetu! Hivyo, tungependa kutafakari sifa zake. Kila mmoja wetu na ajitahidi kuimarisha uhusiano wake na Mungu.—Zaburi 9:10.
13. Kwa nini kuliogopa jina la Mungu si jambo baya?
13 Wale wanaoishi kulingana na viwango vya Mungu na kutembea katika jina lake huliogopa jina la Mungu. Hilo si jambo baya. Yehova anawahakikishia hivi: “Kwenu ninyi mnaoliogopa jina langu, jua la uadilifu litaangaza, likiwa na kiponyaji katika mabawa yake; nanyi mtatoka nje na kuukanyaga udongo kama ndama waliononeshwa.” (Malaki 4:2) Katika utimizo wa unabii huo, “jua la uadilifu” ni Yesu Kristo. (Ufunuo 1:16) Leo, anaangaza kwa ponyo la kiroho, na baadaye, ataangaza kwa kuwaponya kimwili wanadamu. Shangwe ya walioponywa inalinganishwa na ndama waliononeshwa ambao ‘hutoka nje na kuukanyaga udongo,’ wakiwa na msisimuko na furaha kwa kuwa huru. Bila shaka wewe mwenyewe umefurahia kiasi kikubwa cha uhuru huo, sivyo?—Yohana 8:32.
14, 15. Ni faida gani unazopata kwa kuishi kulingana na viwango vya Yehova?
14 Faida nyingine ya kufuata viwango vya Mungu ni kwamba unakuwa na uhusiano bora zaidi na wanadamu wenzako. Habakuki alitangaza ole tano—dhidi ya wenye tamaa, wenye kutafuta mapato yasiyo halali, wenye kumwaga damu, wenye kupanga njama ya kufanya upotovu wa kingono, na wenye kuabudu sanamu. (Habakuki 2:6-19) Kwa kuwa Yehova alitangaza ole hizo, basi ni wazi kwamba ana viwango anavyotaka tuishi kulingana navyo. Hata hivyo kumbuka jambo hili: Manne kati ya maovu yanayotajwa yanahusu jinsi tunavyowatendea wanadamu wenzetu. Tukiwa na maoni kama ya Mungu, hatutawadhuru jirani zetu. Hivyo, uhusiano wetu na wengi wao utakuwa bora.
15 Faida ya tatu inahusu furaha ya familia. Watu leo huona talaka kuwa njia bora ya kutatua matatizo ya ndoa. Hata hivyo, kupitia kinywa cha nabii Malaki, Yehova alisema hivi: “Amechukia talaka.” (Malaki 2:16) Tutachunguza kindani andiko la Malaki 2:16 baadaye, lakini kwa sasa, ona kwamba Mungu kwa hekima yake ameweka viwango vya kufuatwa katika familia; na kwa kadiri familia inavyofuata viwango hivyo, ndivyo inavyokuwa na amani. (Waefeso 5:28, 33; 6:1-4) Ni kweli kwamba hakuna yeyote kati yetu aliye mkamilifu na kwa hiyo matatizo yatazuka. Hata hivyo, katika kitabu cha Hosea, Yule “ambaye kila familia mbinguni na duniani hupata jina kutokana naye,” alitoa mfano unaoonyesha jinsi ya kutatua hata matatizo mazito zaidi ya ndoa. Hilo pia tutachunguza baadaye katika kitabu hiki. (Waefeso 3:15) Sasa, acheni tuone ni nini kingine kinachohusika katika kutii viwango vya Mungu.
“CHUKIENI YALIYO MABAYA, PENDENI YALIYO MEMA”
16. Andiko la Amosi 5:15 linahusianaje na viwango vya Mungu?
16 Mwanadamu wa kwanza, Adamu, alifanya uamuzi mbaya kuhusu ni nani aliyekuwa na viwango bora vya yaliyo mema na yaliyo mabaya. Je, sisi tutaamua kwa hekima? Amosi anatuhimiza tuchukue jambo hilo kwa uzito, akitusihi hivi: “Chukieni yaliyo mabaya, pendeni yaliyo mema.” (Amosi 5:15) William Rainey Harper, aliyekuwa profesa wa lugha na fasihi za Kiyahudi katika Chuo Kikuu cha Chicago, alisema hivi kuhusu mstari huo: “Kwa maoni [ya Amosi], kiwango cha yaliyo mema na yaliyo mabaya, ni kuishi kulingana na mapenzi ya Yahweh.” Hilo ni jambo kuu tunaloweza kujifunza kutokana na wale manabii 12. Je, tuko tayari kukubali viwango vya Yehova vya yaliyo mema na yaliyo mabaya? Viwango hivyo vinapatikana katika Biblia na hufundishwa na Wakristo wakomavu wenye ujuzi ambao ni “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.”—Mathayo 24:45-47.
Kufuata mashauri ya wale manabii 12 kunaweza kumsaidiaje mtu kushinda kishawishi cha kutazama picha chafu?
17, 18. (a) Kwa nini tunapaswa kuchukia yaliyo mabaya? (b) Tumia mfano kuonyesha jinsi tunavyoweza kukuza uwezo wa kuchukia kabisa yaliyo mabaya.
17 Kuchukia yaliyo mabaya hutusaidia kuepuka mambo yanayomchukiza Mungu. Kwa mfano, huenda mtu akajua hatari za picha chafu kwenye Intaneti na kujaribu kuziepuka. Hata hivyo, ‘mtu aliye kwa ndani’ anahisije kuhusu vituo vyenye picha chafu? (Waefeso 3:16) Kwa kutii himizo la Mungu lililo katika Amosi 5:15, itakuwa rahisi kukuza uwezo wa kuchukia yaliyo mabaya. Hivyo, anaweza kufaulu kushinda pambano hilo la kiroho.
18 Fikiria mfano mwingine. Je, unaweza kujiwazia ukiwa umeinamia sanamu ya ibada ya ngono? Wazo lenyewe ni lenye kuchukiza, sivyo? Ingawa hivyo, Hosea alisema kwamba mababu za Waisraeli walifanya uasherati mbele za Baali wa Peori. (Hesabu 25:1-3; Hosea 9:10) Inaonekana kwamba Hosea alitaja tukio hilo kwa kuwa ibada ya Baali ilikuwa dhambi kubwa iliyofanywa na ule ufalme wa makabila kumi wa Israeli. (2 Wafalme 17:16-18; Hosea 2:8, 13) Tunaweza tu kuwazia jambo hilo lenye kuchukiza kwelikweli: Waisraeli walikuwa wakiinamia sanamu huku wakifanya uasherati. Kujua jinsi Mungu alivyoshutumu mambo hayo kwaweza kumsaidia kila mmoja wetu kupambana dhidi ya mitego ya Shetani katika Intaneti. Leo, wengi wanaabudu wanawake warembo na wanaume wenye sura za kuvutia wanaoonyeshwa katika burudani zinazopendwa na wengi. Hata hivyo, sisi ambao tumejifunza kutokana na maonyo ya manabii hao kuhusu ibada ya sanamu, tuko tofauti kabisa!
ZINGATIA NENO LA MUNGU
19. Tunaweza kujifunza nini kutokana na jinsi Yona alivyotenda alipokuwa katika tumbo la samaki mkubwa?
19 Unapojitahidi kuishi kulingana na viwango vya juu vya Mungu ujapokabili vishawishi na matatizo, huenda nyakati nyingine ukahisi kwamba umelemewa au hujui la kufanya. Nguvu zako za kiakili na kihisia zinapoonekana kuwa chache, unaweza kukabilije hali ngumu kwa mafanikio? (Methali 24:10) Kuna jambo tunaloweza kujifunza kutoka kwa Yona, ambaye tunajua kwamba hakuwa mkamilifu na alikosea. Kumbuka alilofanya alipokuwa katika tumbo la yule samaki mkubwa. Alisali kwa Yehova. Ona mambo aliyotaja katika sala yake.
20. Unaweza kujitayarishaje kama alivyofanya Yona?
20 Yona aliposali kwa Mungu akiwa “katika tumbo la Kaburi,” alitumia maneno mengi aliyoyajua, maneno ya zaburi. (Yona 2:2) Alikuwa na dhiki nyingi naye alimwomba Yehova amwonyeshe rehema, hata hivyo Yona alikumbuka na kutumia maneno ya Daudi. Kwa mfano, linganisha maneno ya Yona 2:3, 5 na yale yaliyo katika Zaburi 69:1, 2.a Je, huoni kwamba Yona alikuwa amefahamu vizuri maneno ya zaburi za Daudi zilizokuwapo wakati huo? Yona alikumbuka maneno ya zaburi zilizoongozwa kwa roho. Neno la Mungu lililoongozwa kwa roho lilikuwa ‘ndani yake.’ (Zaburi 40:8) Unapokumbwa na hali ngumu inayokudhoofisha kihisia, je, unaweza kukumbuka maneno fulani ya Mungu yanayofaa? Kulifahamu vizuri zaidi Neno la Mungu sasa huenda kukakusaidia sana wakati ujao unapohitaji kufanya maamuzi fulani au kutatua matatizo kupatana na viwango vya Mungu.
UWE NA WOGA UNAOFAA KUMWELEKEA MUNGU
21. Unahitaji kukuza nini ili ushikamane na viwango vya Mungu?
21 Bila shaka, kuwa tu na Neno la Mungu katika hazina yako hakutoshi kukufanya ushikamane na viwango vya Yehova. Nabii Mika anakusaidia kuelewa vizuri zaidi jambo unalohitaji ili ulitii Neno la Mungu: “Mtu mwenye hekima inayotumika ataliogopa jina lako.” (Mika 6:9) Ili uwe mtu mwenye hekima inayotumika, unapaswa kutumia maishani mwako mambo unayojua, na kukuza woga kwa ajili ya jina la Mungu.
22, 23. (a) Kwa nini Yehova alimtuma Hagai kwa Wayahudi waliokuwa wamerudi nyumbani? (b) Ni nini kinachokuhakikishia kwamba unaweza kufuata viwango vya Mungu?
22 Unawezaje kujifunza kuliogopa jina la Mungu? Mfikirie nabii Hagai, aliyeishi baada ya uhamisho. Katika kitabu chake kifupi sana, chenye mistari 38 tu, alilitumia jina la Yehova mara 35! Yehova alipompa Hagai utume katika mwaka wa 520 K.W.K., miaka 16 ilikuwa imepita na kazi ya kujenga upya hekalu la Yerusalemu ilikuwa imefanywa kwa kiwango kidogo tu. Watu wa Mungu walikuwa wamevunjika moyo kwa sababu ya upinzani kutoka kwa adui zao. (Ezra 4:4, 5) Watu hao walidai kwamba wakati wa kulijenga upya hekalu haukuwa umefika. Yehova aliwahimiza hivi: “Wekeni moyo wenu juu ya njia zenu. . . . Jengeni nyumba hii, nipate kuifurahia na nipate kutukuzwa.”—Hagai 1:2-8.
23 Gavana Zerubabeli, Kuhani Mkuu Yoshua, na “mabaki yote ya watu wakaanza kuisikiliza sauti ya Yehova Mungu wao, . . . nao watu wakaanza kuogopa kwa sababu ya Yehova.” Ndipo, Mungu akasema: “Mimi nipo pamoja nanyi.” Hayo ni maneno yenye kutia moyo kama nini! Kwa msaada wa roho ya Mungu, watu “wakaanza kuingia na kufanya kazi katika nyumba ya Yehova.” (Hagai 1:12-14) Woga unaofaa wa kutotaka kumchukiza Mungu uliwachochea watu waliokuwa wamevunjika moyo wachukue hatua licha ya upinzani.
24, 25. Tumia mifano hususa kuonyesha jinsi unavyoweza kutumia kanuni zilizo katika sura hii.
24 Namna gani wewe? Baada ya kujua viwango vya Mungu vinavyohusiana na mambo unayokabili, je, utakuwa na ujasiri unaohitajiwa ili kumwogopa Yehova badala ya wanadamu? Huenda wewe ni mwanamke kijana, na kazini kwenu kuna mwanamume ambaye hafuati kanuni za Mungu kama wewe. Lakini ni mwenye fadhili na anapendezwa nawe. Je, kuna andiko lolote unaloweza kukumbuka, litakalokukumbusha viwango vya Yehova na hatari za kupuuza viwango hivyo? Namna gani andiko la Hosea 4:11? “Uasherati na divai na divai tamu ndivyo vinavyoondoa kusudi jema.” Pamoja na hilo, je, woga wako kwa Mungu utakuchochea ushikamane na viwango vyake na kukataa wakati mwanamume huyo anapokualika katika tafrija fulani? Akianza kukuchezea kimahaba, woga wa kutotaka kumchukiza Mungu wako mwenye upendo waweza kukusaidia ‘kukimbia.’—Mwanzo 39:12; Yeremia 17:9.
25 Sasa, turudie ule mfano wa mtu anayejaribu kushindana na kishawishi cha kutazama picha chafu kwenye Intaneti. Je, atakumbuka maneno ya Zaburi 119:37, ambayo ni sehemu ya sala? “Uyafanye macho yangu yapite ili yasione jambo lisilofaa.” Je, atajikumbusha maneno ya Yesu katika yale Mahubiri ya Mlimani? “Kila mtu ambaye anaendelea kumtazama mwanamke na kumtamani tayari amefanya uzinzi pamoja naye moyoni mwake.” (Mathayo 5:28) Kumwogopa Yehova na kutaka kuishi kulingana na viwango vyake kwapaswa kumchochea Mkristo aepuke mambo yanayoweza kumpotosha. Wakati wowote unaposhawishiwa kutenda kinyume na viwango vya Mungu, jitahidi kumwogopa Mungu hata zaidi. Kumbuka kwamba Yehova anakuambia hivi kupitia Hagai: ‘Nipo pamoja nawe.’
26. Ni mambo gani ambayo tutachunguza?
26 Naam, unaweza kumtumikia Yehova kulingana na viwango vyake na ufaidike kwa kufanya hivyo. Unapoendelea kuchunguza vile vitabu 12 vya kinabii, utaelewa vizuri zaidi viwango vya Mungu, au mapenzi yake. Katika sehemu inayofuata ya kitabu hiki, tutachunguza viwango bora vya Yehova kuhusu mambo haya matatu: mwenendo wetu, shughuli zetu na wengine, na maisha yetu ya familia.
-
-
“Yehova Anataka Nini Kutoka Kwako?”Izingatie Siku ya Yehova Maishani
-
-
SURA YA NANE
“Yehova Anataka Nini Kutoka Kwako?”
1, 2. Kwa nini inatia moyo kuona jinsi Yehova alivyoshughulika na hali mbaya ya maadili ya watu wake wa kale?
HEBU wazia tukio hili: Msichana anashtuliwa na mtu anayebisha mlango kwa nguvu sana. Anaogopa kwamba ni mfanyabiashara mfisadi ambaye amekuja kudai pesa. Amewaibia wengi kwa kutumia mizani ya udanganyifu na kutoza faida haramu. Ili aepuke adhabu, anawahonga wakuu wa mji, na hivyo wanapuuza malalamiko ya wale walioibiwa. Msichana huyo yuko hoi kabisa; baba yake ameiacha familia yao na kumchukua mwanamke mwingine mwenye umri mdogo. Huenda msichana huyo pamoja na mama yake wakauzwa kama watumwa.
2 Tukio hilo lenye kusikitisha ni mojawapo ya mazoea mengi ambayo wale manabii 12 walishutumu. (Amosi 5:12; 8:4-6; Mika 6:10-12; Sefania 3:3; Malaki 2:13-16; 3:5) Kama ungekuwa ukiishi wakati huo, ungetendaje? Hali hiyo inahuzunisha sana, hata hivyo, unaweza kutiwa moyo kuona jinsi Yehova alivyoshughulika kwa njia nzuri na watu wake katika siku za manabii hao. Naam, unaweza kuona katika vitabu hivyo 12 kwamba Mungu alikazia mitazamo na sifa bora kabisa. Mambo yenye kutia moyo aliyosema yanaweza kuimarisha maadili yako, kukuchochea kufanya mema, na kumsifu. Kwa kuwa siku ya Yehova ya hukumu inakaribia haraka, kuzingatia ujumbe wenye kutia moyo ulio katika vitabu hivyo kunaweza kukusaidia kuelewa yale ambayo Mungu anataka tufanye. Anza kwa kuchunguza matukio ya siku za Mika, katika karne ya nane K.W.K.
Yehova anaona ufisadi na ukosefu wa haki
YEHOVA ANATAKA NINI KUTOKA KWAKO?
3, 4. (a) Kitabu cha Mika kinatusihi kwa upendo tufanye nini? (b) Unahisije kuhusu swali lililo katika Mika 6:8?
3 Ukisoma kitabu cha Mika, unaweza kufikiri mwanzoni kwamba ni orodha ndefu ya mashtaka dhidi ya Waisraeli walioasi. Bila shaka, Yehova aliona kuzorota kwa maadili ya watu wake waliokuwa wamejiweka wakfu, kutia ndani watu aliowaita: ‘Wanaochukia yaliyo mema na wanaopenda ubaya.’ (Mika 3:2; 6:12) Hata hivyo, mbali na kuwashutumu waziwazi, alitoa mojawapo ya mahimizo yenye kugusa moyo na yenye kuchochea zaidi katika Biblia. Mika anakazia uangalifu Chanzo cha viwango vya uadilifu, kisha anauliza swali hili lenye kuchochea fikira: “Yehova anataka nini kutoka kwako ila kutenda haki na kupenda fadhili na kuwa na kiasi katika kutembea na Mungu wako?”—Mika 6:8.
4 Je, unaona jinsi Muumba wetu anavyotusihi katika andiko hilo? Anatukumbusha kwa upendo mambo yanayofaa tunayoweza kufanya badala ya kujiruhusu tukengeushwe na uovu uliopo. Yehova anajua kwamba ushikamanifu wetu hutuchochea kusitawisha sifa kama zake, naye ana hakika kwamba tunaweza kufanya hivyo. Ungejibuje kama ungeulizwa hivi: ‘Yehova anataka nini kutoka kwako?’ Je, unaweza kutaja mambo fulani maishani mwako yanayoongozwa au yanayopasa kuongozwa na viwango vya Mungu vya maadili? Uhusiano wako na Mungu na maisha yako yatakuwa bora zaidi ukiendelea kufuata viwango hivyo. Unapoendelea kutazamia paradiso duniani, himizo hili na likutie moyo: “Mjipandie mbegu kwa uadilifu; mvune kulingana na fadhili zenye upendo. Mjilimie udongo unaofaa kwa kilimo, kukiwa kungali na wakati wa kumtafuta Yehova mpaka atakapokuja na kuwatolea ninyi mafundisho kwa uadilifu.” (Hosea 10:12) Hebu sasa tuchunguze mambo fulani makuu kutokana na shauri zuri la Mika 6:8.
‘UWE NA KIASI’
5. Kwa nini ni muhimu “kuwa na kiasi” katika kutembea na Mungu?
5 Mika anasema waziwazi kwamba Yehova anataka ‘tuwe na kiasi tunapotembea’ Naye. Tunaweza kupata faida tukiwa na kiasi kwa sababu “wenye kiasi wana hekima.” (Methali 11:2) Kuwa na kiasi kunatia ndani kutambua mipaka tuliyo nayo kwa sababu ya dhambi ya Adamu. Kutambua kwamba tulizaliwa katika dhambi ni hatua ya kwanza muhimu katika jitihada zetu za kuepuka kutenda dhambi kimakusudi.—Waroma 7:24, 25.
6. Tunaweza kufaidikaje tukiwa wenye kiasi na kutambua matokeo ya dhambi?
6 Kwa nini sifa ya kiasi, pamoja na unyenyekevu wa akili, inaweza kutusaidia kuepuka kutenda dhambi kimakusudi? Kwanza, mtu mwenye kiasi anatambua kwamba dhambi ina nguvu sana. (Zaburi 51:3) Hosea anatusaidia kuelewa kwamba dhambi inaweza kumshawishi mtu sana na sikuzote husababisha madhara mwishowe. Kwa mfano, Yehova aliahidi ‘kuwatoza hesabu’ watu wake wa kale kwa sababu ya kutotii kwao. Je, hilo linaonyesha kwa njia yoyote kwamba watenda-dhambi hao wasio na kiasi wangeweza kuepuka matokeo ya matendo yao? Huenda walidhani hivyo, kwa kuwa mara nyingi dhambi humdanganya mtu na kumfanya mtumwa. Jambo baya zaidi ni kwamba dhambi huwatenga watenda-dhambi na Mungu, na yaelekea inawatumbukiza katika hali mbaya zaidi ya kufikiri kwamba: “Matendo yao hayawezi kuwaruhusu wamrudie Mungu wao.” Kutenda dhambi kimakusudi huharibu msimamo thabiti na sifa za kiadili za mkosaji, na humfanya awe ‘mtu anayetenda madhara.’ Isitoshe, dhambi hufanya maisha ya mtenda-dhambi yawe ya ubatili. Ni kweli kwamba kwa muda fulani, huenda akaonekana anafanikiwa, lakini mtenda-dhambi asiyetubu hawezi kutarajia kuwa na kibali cha Mungu.—Hosea 1:4; 4:11-13; 5:4; 6:8.
7. Watu wenye kiasi huonaje mwongozo wa Yehova?
7 Watu wenye kiasi hutambua pia kwamba wanahitaji mwongozo wa Mungu ili kuepuka matokeo yenye kuhuzunisha ya dhambi. Mika alitabiri kuhusu siku zetu, wakati ambapo watu wengi wangekuja kwa bidii ‘kufundishwa njia za Yehova’ na ‘kutembea katika mapito yake.’ Watu hao wanyenyekevu hutafuta “sheria” na “neno la Yehova.” Inaelekea unafurahi kuwa miongoni mwa wale wanaotamani ‘kutembea katika jina la Yehova’ kwa kutii matakwa yake. Hata hivyo, kama Mika, huenda ukataka kujua mambo mengine yatakayokusaidia kuwa “safi kiadili.” (Mika 4:1-5; 6:11) Kuwa na kiasi na kujitahidi kufanya yale ambayo Yehova anataka ufanye kutakusaidia sana.
DUMISHA VIWANGO VYA JUU VYA MAADILI
8. Umejionea mambo gani kuhusiana na maadili ya ulimwengu leo?
8 Yehova anatuagiza tuwe safi kiadili licha ya uovu ulio katika ulimwengu kwa sababu anataka tuwe na hali nzuri ya kiroho na kimwili. (Malaki 2:15) Ulimwengu umejaa habari nyingi sana za ngono. Watu wengi wana maoni ya kwamba kutazama picha na sinema za ngono, kusoma vichapo vyenye mambo machafu ya ngono, na kusikiliza muziki unaoamsha ashiki ni mambo ya kawaida ya maisha. Isitoshe, kuna watu wasiowaheshimu wanawake, wanawaona kuwa vyombo vya ngono tu. Au huenda vijana shuleni wakafanya mizaha michafu na kusema mambo machafu kuhusu ngono. Utashindaje mikazo hiyo yenye kuchafua?
9. Wengi walikosaje kudumisha viwango vya Yehova wakati wa wale manabii 12?
9 Wale manabii 12 tunaozungumzia wanatoa mashauri mazuri sana. Waliishi kabla ya kubuniwa kwa majumba ya sinema na maduka ya video. Hata hivyo, wakati huo kulikuwa na ishara za viungo vya uzazi, kulikuwa na ule ulioitwa ukahaba mtakatifu, na matendo mapotovu sana ya ngono. (1 Wafalme 14:24; Isaya 57:3, 4; Habakuki 2:15) Mambo ambayo manabii waliandika yanathibitisha hivyo: “Kwa habari ya wanaume, hujiendea zao wenyewe pamoja na makahaba, nao hutoa dhabihu pamoja na wanawake makahaba wa hekaluni.” “Mwanamume na baba yake wamemwendea msichana yuleyule, kwa kusudi la kulitia unajisi jina langu takatifu.” Baadhi yao walitoa kwa ukawaida “malipo ya kahaba” katika sherehe za uzazi.a Uzinzi ulienea kotekote, huku wake na waume wasio waaminifu ‘wakiwafuata wale wanaowapenda kwa tamaa nyingi.’—Hosea 2:13; 4:2, 13, 14; Amosi 2:7; Mika 1:7.
10. (a) Mwenendo mpotovu husababishwa na nini hasa? (b) Watu wa kale wa Mungu walitumbukiaje katika uasherati wa kiroho?
10 Huenda unajua kwamba upotovu wa maadili unahusiana na mtazamo na nia ya mtu. (Marko 7:20-22) Kuhusu watu wake wenye maadili mapotovu, Yehova alisema kwamba “roho ya uasherati [“tamaa ya ngono,” Contemporary English Version] imewafanya watange-tange” na kwamba “wameendeleza mwenendo mpotovu.” (Hosea 4:12; 6:9)b Zekaria alitaja “roho ya uchafu.” (Zekaria 13:2) Watu walikuwa na mtazamo wa kutojali, walipuuza au hata kudharau viwango vya Yehova na mamlaka yake. Kwa hiyo, mtu yeyote mwenye mwelekeo huo anapaswa kubadili kabisa fikira zake na hali yake ya moyoni ili arekebishe nia yake. Wakristo wanapojua hivyo wanapaswa kuthamini hata zaidi jitihada zinazofanywa ili kuwasaidia waepuke ukosefu wa maadili na madhara yake.
JITAHIDI KUWA SAFI
11. Taja baadhi ya matokeo ya ukosefu wa adili.
11 Yaelekea umeona kwamba mara nyingi ukosefu wa adili huvunja familia, huwanyima watoto mwongozo wa wazazi, husababisha magonjwa mabaya sana, na huwafanya watu waue kwa kutoa mimba. Wale wanaopuuza maagizo ya Muumba kuhusiana na ngono kwa kawaida hupata madhara ya kimwili na ya kihisia. Mika aliandika hivi: “Kwa sababu ya uhakika wa kwamba [mtu] amekuwa asiye safi, kuna kuvunja-vunja; na kazi hiyo ya kuvunja-vunja ina maumivu.” (Mika 2:10) Kujua hivyo huimarisha azimio la watu wanaotaka kikweli kumtolea Mungu ibada safi. Wao huepuka kuchafua mioyo na akili zao kwa kufikiria daima mambo maovu.—Mathayo 12:34; 15:18.
12. Tunafaidikaje kwa kukubali maoni ya Yehova kuhusu ngono?
12 Wakristo hawaepuki ukosefu wa adili eti kwa sababu wanaogopa magonjwa au kupata mimba haramu. Wanaona umuhimu wa kuzipenda sheria za Mungu na kuwa na maoni kama yake kuhusiana na maadili. Yehova aliwaumba wanadamu wakiwa na tamaa ya asili ya kufanya ngono ili wenzi wa ndoa waonyeshane upendo. Hilo lilikuwa sehemu ya kusudi la Mungu alipowaumba Adamu na Hawa. Ngono huwa na manufaa inapofanywa na wale wanaostahili, yaani, wenzi wa ndoa tu. Inamfanya mume na mke wawe na uhusiano wa karibu na nyakati nyingine inawawezesha kuzaa. Hata hivyo, watu wanapofanya ngono nje ya ndoa, inasababisha madhara makubwa sana, kama wale manabii 12 walivyosema. Ngono haramu ziliwafanya watu wapoteze kibali cha Mungu. Walipata hasara kubwa sana, na itakuwa vivyo hivyo kwa mtu yeyote anayeshiriki ngono haramu leo.
13. Tunaweza ‘kuondoleaje mbali uasherati’ na kuepuka vishawishi?
13 Hosea aliwasihi watu walioishi nyakati zake ‘waondolee mbali, uasherati kutoka mbele yao,’ akimaanisha kwamba walipaswa kuchukua hatua madhubuti ya kulinda maadili yao. (Hosea 2:2) Ni jambo la hekima kwetu leo kuepuka kabisa hali yoyote inayoweza kutushawishi. Kwa mfano, waweza kushawishiwa daima shuleni au katika ujirani wenu. Huenda usiweze kuhamia shule nyingine au makao mengine, hata hivyo, huenda kukawa na njia nyingine unazoweza kuepuka kishawishi hicho na hivyo ‘kuondolea mbali uasherati kutoka mbele yako.’ Wajulishe wengine kwamba wewe ni Mkristo wa kweli, mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Waeleze viwango na imani yako kwa njia ya heshima na iliyo wazi. Hakikisha kwamba wengine wanajua kwamba umeazimia kufuata viwango vya juu vya Yehova. (Amosi 5:15) Njia nyingine ya ‘kuondolea mbali uasherati’ ni kuepuka ponografia na burudani zisizofaa. Hilo laweza kutia ndani kutupa gazeti fulani au kutafuta marafiki wapya—wale wanaompenda Yehova na wanaokutia moyo ufanye yale anayotaka ufanye. (Mika 7:5) Naam, kwa msaada wa Yehova unaweza kuepuka kuchafuliwa na ukosefu wa adili wa ulimwengu!
Kuwajulisha wengine waziwazi imani yako ya Kikristo ni ulinzi
‘PENDA FADHILI’
14, 15. (a) ‘Kupenda fadhili’ kunamaanisha nini? (b) Kupenda fadhili kunatusaidiaje kutokuwa na lawama?
14 Mika alikazia kwamba Yehova anataka ‘tupende fadhili.’ Mtu mwenye fadhili hufanya mambo mema wala si yale yenye kudhuru. Fadhili inahusiana sana na wema na ubora wa kiadili. Inamaanisha kwamba tunapaswa kuwa wanyoofu na wasiopendelea katika mambo yetu ya kibinafsi na tunaposhughulika na wengine. Katika Sura ya 6 ya kitabu hiki, tulichunguza umuhimu wa kutenda kwa haki na unyoofu katika shughuli mbalimbali muhimu maishani, kama vile biashara na mambo ya kifedha. Lakini hatupaswi tu kuwa wenye haki, wanyoofu, na wenye fadhili katika mambo hayo peke yake.
15 Watu wanaopenda fadhili na wanaotaka kuwafanyia wengine mema hujitahidi kutokuwa na lawama. Yehova aliwaambia hivi Waisraeli ambao hawakuwa wakitimiza wajibu wao wa kutegemeza ibada safi kwa vitu vyao vya kimwili: “Ninyi mnaninyang’anya mimi.” (Malaki 3:8) Je, unajua jinsi ambavyo mtu anaweza ‘kumnyang’anya’ Mungu leo? Namna gani ikiwa Mkristo hushughulikia michango inayotolewa kwa ajili ya kuendeleza kazi ya Ufalme kutanikoni au katika sehemu nyingine? Ni pesa za nani? Michango hiyo ni mali ya Yehova, kwa kuwa imetolewa ili kuendeleza ibada yake. (2 Wakorintho 9:7) Je, mtu yeyote anapaswa kufikiri kwamba anaweza “kuazima” pesa hizo ili kushughulikia hali ya dharura inayomkabili au kutumia michango iliyotolewa kwa ajili ya ibada bila idhini inayofaa? La hasha. Kufanya hivyo ni sawa na kumwibia Mungu! Bila shaka, hilo si tendo la fadhili au wema kuelekea wale waliotoa michango hiyo kwa ajili ya kazi ya Mungu.—Methali 6:30, 31; Zekaria 5:3.
16, 17. (a) Watu fulani walionyeshaje pupa katika siku za Amosi na Mika? (b) Mungu ana maoni gani kuhusu tamaa?
16 Fadhili na wema huwachochea pia Wakristo kuepuka tamaa. Watu wengi katika siku za Amosi walikuwa wenye pupa sana. Watu wakatili wenye pupa walikuwa tayari ‘kumuuza mtu mwadilifu’—mwabudu mwenzao—“kwa sababu tu ya fedha”! (Amosi 2:6) Hali ilikuwa vivyo hivyo katika siku za Mika. Matajiri wa Yuda walinyakua mali ya watu waliokuwa dhaifu wasiweze kujilinda, na hata waliichukua kwa nguvu. (Mika 2:2; 3:10) Watu hao wenye pupa walikuwa wakivunja Sheria ya Yehova kwa kunyakua mashamba ya wenzao. Walivunja Amri ya Kumi na pia maagizo yaliyowakataza kuuza kabisa nchi waliyorithi.—Kutoka 20:13, 15, 17; Mambo ya Walawi 25:23-28.
17 Huenda si kawaida leo kwa wanadamu kuuzwa au kufanywa watumwa kama ilivyokuwa katika siku za manabii. Hata hivyo, namna gani kuhusu kuwakandamiza kifedha au kuwatumia wengine vibaya ili kujipatia faida? Mkristo ambaye anapenda fadhili bila shaka hatawakandamiza waabudu wenzake. Kwa mfano, anatambua kwamba si jambo linalofaa wala lenye fadhili kuanzisha biashara au miradi fulani kwa kusudi la kuwatumia waamini wenzake kama wateja wakuu. Kujipatia faida ya haraka kwa kuwatumia vibaya Wakristo wengine kungeonyesha kwamba mtu ana pupa, sifa ambayo Wakristo wanaonywa waepuke. (Waefeso 5:3; Wakolosai 3:5; Yakobo 4:1-5) Mtu anaweza kuonyesha pupa katika mambo kama vile kupenda pesa, tamaa ya kupata mamlaka au faida, hata ulafi na unywaji wa kupita kiasi, ngono, au mambo mengine. Mika alisema kwamba watu wenye pupa na wanaojifikiria tu ‘hawatashiba.’ Ndivyo ilivyo leo.—Mika 6:14.
Kwa upendo, Wakristo wengi huwasaidia wakaaji wageni kujifunza kumhusu Yehova
18, 19. (a) Baadhi ya wale manabii 12 walisema nini kuhusu upendo wa Yehova kuelekea “mkaaji mgeni”? (b) Kuwajali wengine kwa upendo kutaboreshaje mahusiano katika ujirani wenu?
18 Yehova aliwaagiza watu wake ‘wasimpunje mkaaji yeyote mgeni.’ Mungu alitangaza hivi kupitia Malaki: ‘Nitawakaribia ninyi ili kuhukumu, juu ya wale wanaomfukuza mkaaji mgeni.’ (Zekaria 7:10; Malaki 3:5) Je, eneo lenu limekuwa likibadilika kwa sababu ya kumiminika kwa wakaaji wageni au watu kutoka katika mataifa, malezi au makabila mengine? Huenda wamehamia eneo hilo kwa sababu ya usalama, kutafuta kazi, au maisha bora. Una maoni gani kuelekea watu wenye lugha na maisha tofauti na yako? Je, una mwelekeo wa kubagua, ambao ni kinyume kabisa na sifa ya fadhili?
19 Hebu wazia jinsi baadhi yao watakavyoitikia ukionyesha kwamba watu wa nchi au malezi tofauti wanastahili kufundishwa kweli ya Kikristo sawa na watu wengine. Fadhili itamzuia mtu kuhisi kwamba wageni hao wamekuja kuwanyang’anya mapendeleo yao na haki ya kutumia Jumba la Ufalme au mali nyingine. Mtume Paulo aliwakumbusha baadhi ya Wakristo Wayahudi katika karne ya kwanza, ambao waliwabagua watu wasio Wayahudi, kwamba hakuna mtu hata mmoja aliyestahili wokovu; mtu yeyote angeweza tu kupata wokovu kwa sababu ya fadhili zisizostahiliwa za Mungu. (Waroma 3:9-12, 23, 24) Kuwatendea wengine kwa fadhili kutatufanya tushangilie tukiona kwamba upendo wa Mungu sasa unawafikia watu wengi ambao hapo awali hawakupata fursa ya kuhubiriwa habari njema. (1 Timotheo 2:4) Watu kutoka katika nchi au malezi mengine mara nyingi hukabili matatizo, kwa hiyo tunapaswa kuwatendea kwa fadhili na kuwaonyesha kwamba tunawajali, kwa kuwakaribisha, na kumtendea kila mmoja wao “kama mwenyeji” miongoni mwetu.—Mambo ya Walawi 19:34.
TEMBEA NA MUNGU WA KWELI
20. Baadhi ya Waisraeli walitafuta mwongozo kutoka kwa nani?
20 Mika alikazia pia kutembea na Mungu, kumtumaini akiwa Mungu wa kweli, na kutafuta mwongozo wake. (Methali 3:5, 6; Hosea 7:10) Baada ya Wayahudi kurudi kutoka uhamishoni, baadhi yao walitafuta mwongozo kutoka kwa wabashiri, waaguzi, na miungu ya uwongo, labda ili wapate msaada wakati wa ukame. Ukweli ni kwamba waliwaomba roho waovu wawasaidie, hata ingawa Yehova alikuwa ameshutumu waziwazi mazoea hayo yote. (Kumbukumbu la Torati 18:9-14; Mika 3:6, 11; 5:12; Hagai 1:10, 11; Zekaria 10:1, 2) Wayahudi hao walikuwa wakishirikiana na viumbe wa roho ambao ni maadui wa Mungu wa kweli!
21, 22. (a) Ni mazoea gani ya kuwasiliana na pepo yaliyo ya kawaida katika eneo lenu? (b) Kwa nini watumishi waaminifu wa Yehova hawajihusishi na mazoea ya kuwasiliana na pepo?
21 Leo watu fulani hufikiri kwamba roho waovu wanaotajwa katika Maandiko si halisi bali wanawakilisha tu hali ya uovu. Hata hivyo, Biblia inafunua kwamba roho waovu ni halisi na ndio wanaoongoza unajimu, uchawi, na mambo fulani ya mizungu. (Matendo 16:16-18; 2 Petro 2:4; Yuda 6) Hatari za kuwasiliana na pepo ni halisi pia. Watu wa tamaduni mbalimbali huwategemea waganga wanaodai kwamba wana nguvu zisizo za kawaida, na pia wachawi. Wengine hutafuta mwongozo wa nyota za bahati, kadi za ubashiri, fito za uaguzi, bao za kutabiri, au matufe maalumu ya kubashiri. Ni kawaida kuwaona wengi wakijaribu kuwasiliana na roho za wafu. Inasemekana kwamba watawala fulani hufanya maamuzi wakitegemea wanajimu na wale wanaowasiliana na pepo. Ni wazi kwamba mazoea hayo yote hayapatani kamwe na shauri la Mika kwamba tutembee na Mungu wa kweli, tukifuata mwongozo wake.
22 Bila shaka, ni lazima wewe ukiwa mtumishi mwaminifu wa Yehova uepuke kabisa mazoea hayo. Unaweza kuwa na uhakika kwamba Mungu hawasiliani kamwe kupitia pepo au kutumia uchawi ili kufunua mapenzi yake au kuonyesha nguvu zake. Badala yake, kama andiko la Amosi 3:7 linavyotuhakikishia, Yehova ‘huwafunulia watumishi wake manabii jambo lake la siri.’ Isitoshe, kuwasiliana na pepo kunaweza kumfanya mtu anaswe na kuongozwa na Shetani, kiongozi wa roho waovu, ambaye ni mwongo na ameazimia kuwadanganya watu. Shetani na wafuasi wake wameazimia kutudhuru. Wao ni wakatili daima, na hata wamekuwa wakiwaua watu. (Ayubu 1:7-19; 2:7; Marko 5:5) Ndiyo sababu Mika alishutumu uaguzi na uchawi alipotuhimiza tutembee na Mungu wa kweli.
Ni lazima watumishi wa Mungu waepuke kabisa mazoea ya kuwasiliana na pepo
23. Ni nani pekee anayeweza kujibu maombi yetu yanayofaa?
23 Mwongozo unaofaa wa kiroho hutokana tu na Yehova na ibada yake safi. (Yohana 4:24) Nabii Zekaria aliandika hivi: “Mwombeni Yehova.” (Zekaria 10:1) Hata ukishambuliwa au kushawishiwa na roho waovu, kumbuka kwamba “kila mtu anayeliitia jina la Yehova ataokoka.” (Yoeli 2:32) Uhakikisho huo ni muhimu sana tunapoizingatia siku yake kuu maishani mwetu.
24. Umejifunza mambo gani kutokana na Mika 6:8?
24 Ni wazi kwamba tunastahili kufikiria kwa uzito maneno ya Mika 6:8. Ili kuwa imara kiadili, tunahitaji kuwa na nia inayofaa na sifa kama za Mungu. Hosea alitutia moyo sisi tunaoishi “katika siku za mwisho.” Alisema kwamba katika siku zetu, watu wanaomwogopa Mungu wangeutafuta wema wa Yehova. (Hosea 3:5) Amosi alikazia kwamba Mungu anatuomba tufanye vivyo hivyo: “Tafuteni yaliyo mema, . . . kusudi mwendelee kuishi.” Vilevile anatuhimiza hivi: “Pendeni yaliyo mema.” (Amosi 5:14, 15) Tukifanya hivyo, tutapata burudisho kwa kufanya yale ambayo Yehova anataka tufanye.
a Mtafsiri wa Biblia Joseph Rotherham anasema hivi kuhusu mataifa ya Kanaani ambayo Waisraeli waliiga matendo yao: “Ibada yao ilijaa mambo ya ngono na ilikuwa yenye ukatili sana. Wanawake walijitolea kupoteza staha yao ili kuheshimu miungu yao. Nyumba za makahaba zilikuwa takatifu kwao. Viungo vyao vya uzazi vilionyeshwa waziwazi huku vikiwakilishwa na ishara zenye kuchukiza. Walikuwa na makahaba watakatifu (!), waume kwa wake.”
b Watu wa Mungu walitumbukia pia katika uasherati wa kiroho. Walianzisha urafiki usiofaa na mataifa ya kipagani na kuchanganya ibada ya Baali na ibada ya kweli.
-
-
Kuwatendea Wengine Kama Mungu AnavyotakaIzingatie Siku ya Yehova Maishani
-
-
SURA YA TISA
Kuwatendea Wengine Kama Mungu Anavyotaka
1-3. (a) Huenda Wakristo wengi wakafikiria nini kuhusu jiji la kale la Tiro? (b) Eleza baadhi ya shughuli zilizokuwapo kati ya Mfalme Hiramu na Israeli. (c) Tungependa kujifunza nini kuhusu Tiro?
WEWE hufikiria nini unaposikia jiji la kale la Tiro likitajwa? Wakristo wengi hufikiria jinsi unabii ulivyotimizwa wakati Aleksanda Mkuu alipoondoa vifusi kutoka katika magofu ya jiji la Tiro lililokuwa barani na kutengeneza njia hadi kwenye jiji jipya la Tiro lililokuwa kisiwani na kuliharibu. (Ezekieli 26:4, 12; Zekaria 9:3, 4) Hata hivyo, je, jina Tiro linaweza kukufanya ufikirie jinsi unavyopaswa au usivyopaswa kuwatendea ndugu zako wa kiroho au watu wengine?
2 Tiro liliharibiwa kwa sababu gani? “Kwa sababu ya maasi matatu ya Tiro, . . . kwa sababu ya kulitia mkononi mwa Edomu kundi zima la wahamishwa, na kwa sababu hawakukumbuka agano la ndugu. Nami nitapeleka moto kwenye ukuta wa Tiro.” (Amosi 1:9, 10) Katika nyakati zilizopita, Mfalme Hiramu wa Tiro alimtendea wema Daudi na kuleta vifaa vya ujenzi wa hekalu la Sulemani. Sulemani alifanya agano na Hiramu na kumpa majiji katika Galilaya. Hiramu alimwita Sulemani “ndugu yangu.” (1 Wafalme 5:1-18; 9:10-13, 26-28; 2 Samweli 5:11) Wakati Tiro ‘halikukumbuka agano la ndugu’ na kuwauza baadhi ya watu wa Mungu utumwani, Yehova aliona matendo ya Tiro.
3 Tunajifunza nini kutokana na hatua ya Mungu ya kuwahukumu Wakanaani wa Tiro kwa sababu ya kuwatendea kikatili watu wake? Jambo kuu tunalojifunza linahusu jinsi tunavyowatendea ndugu zetu wa kiroho. Katika sura zilizotangulia za kitabu hiki, tulijifunza mashauri fulani yaliyotolewa na wale manabii 12 kuhusiana na jinsi tunavyopaswa kuwatendea wengine, kama vile kufuata haki katika mambo ya kibiashara na kuwa na mwenendo safi. Hata hivyo, vitabu hivi 12 vinasema mengi kuhusu jinsi Mungu anavyotaka tuwatendee wengine.
USISHANGILIE WENGINE WANAPOPATA MATATIZO
4. Waedomu walikuwa “ndugu” za Waisraeli jinsi gani, lakini waliwatendeaje “ndugu” zao?
4 Unaweza kujifunza jambo fulani kutokana na hatua ya Mungu ya kushutumu Edomu, nchi jirani ya Israeli: “Hupaswi kutazama tukio katika siku ya ndugu yako, katika siku ya maafa yake; wala kushangilia juu ya wana wa Yuda katika siku ya kuangamia kwao.” (Obadia 12) Huenda watu wa Tiro walikuwa “ndugu” zao kibiashara, lakini Waedomu walikuwa “ndugu” za Waisraeli kihalisi, kwa kuwa walikuwa wazao wa Esau, ndugu pacha wa Yakobo. Hata Yehova aliwaita Waedomu “ndugu” za Waisraeli. (Kumbukumbu la Torati 2:1-4) Kwa hiyo, Waedomu walionyesha chuki kikweli kwa kushangilia msiba wa Wayahudi mikononi mwa Wababiloni.—Ezekieli 25:12-14.
5. Huenda tukaonyesha roho kama ya Waedomu katika hali gani?
5 Ni wazi kwamba Mungu hakufurahia jinsi Waedomu walivyowatendea ndugu zao Wayahudi. Hata hivyo, twaweza kujiuliza hivi: ‘Mungu anaonaje matendo yangu kuelekea ndugu zangu?’ Jambo moja la kufikiria ni jinsi tunavyomwona na kumtendea ndugu tunapokosana naye. Kwa mfano, tuseme kwamba Mkristo amekuudhi au amekosana na mtu wako wa ukoo. Ikiwa una “sababu ya kulalamika,” je, utamwekea kinyongo, na kukataa kumsamehe au kutojaribu kutatua tatizo hilo? (Wakolosai 3:13; Yoshua 22:9-30; Mathayo 5:23, 24) Kufanya hivyo kunaweza kuathiri jinsi unavyomtendea ndugu yako; unaweza kumwonyesha ubaridi, kumwepuka au kuongea vibaya kumhusu. Au tuseme kwamba baadaye ndugu huyo anakosea, labda hata anahitaji kushauriwa au kurekebishwa na wazee wa kutaniko. (Wagalatia 6:1) Je, ungeonyesha roho kama ya Waedomu kwa kushangilia kwa sababu ya tatizo linalomkabili ndugu huyo? Mungu anataka utendeje?
6. Tofauti na Zekaria 7:10, andiko la Mika 7:18 linapendekeza tufanye nini?
6 Yehova alimwongoza Zekaria kusema kwamba hataki ‘tupangiane jambo lolote baya mioyoni mwetu.’ (Zekaria 7:9, 10; 8:17) Shauri hilo linafaa hasa tunapohisi kwamba ndugu ametuumiza au amemkosea mtu fulani katika familia yetu. Katika hali kama hizo, ni rahisi ‘kupangiana jambo baya mioyoni mwetu’ na kuonyesha hivyo kwa matendo. Kwa upande mwingine, Mungu anataka tuige mfano wake mzuri. Kumbuka, Mika aliandika kwamba Yehova ‘anasamehe kosa na kuuachilia ukosaji.’a (Mika 7:18) Tutafanyaje hivyo katika shughuli zetu?
7. Kwa nini tunaweza kuamua kuacha tu makosa tuliyotendewa?
7 Huenda tukaumia moyoni kwa sababu ya jinsi tulivyotendewa au jinsi mtu wetu wa ukoo alivyotendewa, lakini kwa kweli, ni jambo zito kadiri gani? Biblia hutaja hatua za kuchukua tunapokosana, au hata tunapomkosea ndugu. Hata hivyo, mara nyingi ni vizuri kutotilia maanani makosa hayo, au ‘kuuachilia ukosaji.’ Jiulize: ‘Je, hii yaweza kuwa moja kati ya zile mara 77 ambazo ninapaswa kumsamehe? Mbona nisiliache tu kosa hilo?’ (Mathayo 18:15-17, 21, 22) Hata ikiwa kosa linaonekana kuwa kubwa sasa, je, litabaki kubwa miaka 1,000 ijayo? Jifunze jambo muhimu kutokana na maelezo ya Mhubiri 5:20 kuhusu mfanyakazi anayefurahia chakula na kinywaji: “Si mara nyingi atakumbuka siku za maisha yake, kwa maana Mungu wa kweli anamshughulisha kwa shangwe ya moyo wake.” Mtu huyo anapofurahia raha yake ya sasa, husahau matatizo anayokabili katika maisha yake ya kila siku. Je, tunaweza kuiga mtazamo huo? Tukikazia fikira shangwe za undugu wetu wa Kikristo, tunaweza kusahau mambo ambayo ni ya muda tu, yale ambayo hatutakumbuka katika ulimwengu mpya. Kufanya hivyo ni tofauti kabisa na kushangilia wengine wanapokabili matatizo au kukumbuka makosa tuliyotendewa.
Mtu anapokukosea, unapaswa kuepuka kufanya nini?
WAAMBIE WENGINE UKWELI
8. Ni wakati gani inapokuwa vigumu kusema ukweli?
8 Vile vitabu 12 vya kinabii huonyesha pia jinsi Mungu anavyotaka sana tuseme ukweli tunaposhughulika na wengine. Bila shaka, tunajitahidi sana kuwaambia wengine “ile kweli ya habari njema.” (Wakolosai 1:5; 2 Wakorintho 4:2; 1 Timotheo 2:4, 7) Hata hivyo, ni vigumu zaidi kusema ukweli katika mazungumzo yetu ya kila siku pamoja na watu wa familia zetu na ndugu zetu wa kiroho kuhusu hali na mambo mbalimbali. Kwa nini?
9. Ni lini tunapoweza kushawishika kutosema ukweli kamili, lakini tunapaswa kujiuliza nini?
9 Ni nani kati yetu hajawahi kusema au kufanya jambo fulani lisilo la fadhili kisha akajulishwa kosa lake? Inaelekea kwamba tuliaibika au kuhisi hatia. Hisia kama hizo zinaweza kumfanya mtu akatae kosa lake au atoe “sababu” ambayo si ya kweli akijaribu kutetea kosa lake au kuonyesha kwamba mashtaka hayo si ya kweli. Au tunapoona aibu, huenda tukashawishiwa kutaja mambo fulani tu na kuacha yale ambayo yanaonekana kuwa mabaya. Hivyo, mambo tunayosema yanaweza kuwa kweli, hata hivyo huenda yakaeleweka kwa njia tofauti kabisa. Ingawa huenda tusiwe tunasema uwongo waziwazi, kama ilivyo kawaida katika ulimwengu leo, je, kweli tutakuwa ‘tukisema kweli kila mmoja na jirani yake,’ au na ndugu yake? (Waefeso 4:15, 25; 1 Timotheo 4:1, 2) Unafikiri Mungu anahisije Mkristo anaposema mambo kwa njia fulani ya werevu akiwa na nia ya kuwapotosha ndugu zake waamini jambo ambalo si la kweli, au si sahihi?
10. Manabii wanaelezaje hali ambayo ilikuwa imeenea katika Yuda na Israeli la kale?
10 Manabii walitambua kwamba hata wanaume na wanawake walio wakfu kwa Yehova nyakati nyingine hupuuza matakwa yake. Hosea alieleza hisia za Mungu kuelekea watu fulani walioishi siku zake: “Na waporwe, kwa maana wamenikosea! Nami mwenyewe nikachukua hatua ya kuwakomboa, bali wao wenyewe wamesema uwongo juu yangu.” Mbali na kusema uwongo ulio wazi na usioweza kukanushwa kumhusu Yehova, baadhi yao walianza “kutangaza laana na kuzoea kufanya udanganyifu,” labda ili wafiche ukweli na kuwapotosha wengine. (Hosea 4:1, 2; 7:1-3, 13; 10:4; 12:1) Hosea aliandika maneno hayo akiwa katika ufalme wa kaskazini wa Samaria. Je, hali ilikuwa tofauti huko Yuda? Mika ajibu: “Watu wake mwenyewe walio matajiri wamejaa jeuri, na wakaaji wake mwenyewe wamesema uwongo, na ulimi wao una udanganyifu kinywani mwao.” (Mika 6:12) Ni vizuri tuzingatie jinsi manabii hao walivyoshutumu “kuzoea kufanya udanganyifu” na wale ambao “ulimi wao una udanganyifu kinywani mwao.” Kwa hiyo, hata Wakristo, ambao bila shaka hawawezi kusema uwongo kimakusudi, wanapaswa kujiuliza hivi: ‘Je, nyakati nyingine mimi huzoea udanganyifu au huwa na ulimi wenye udanganyifu kinywani mwangu? Mungu anataka nijiendesheje kuhusiana na mambo hayo?’
11. Manabii wanaonyeshaje mapenzi ya Mungu kuhusiana na usemi wetu?
11 Inapendeza kwamba Mungu aliwatumia manabii hao pia kueleza waziwazi mambo mema anayotaka tufanye. Andiko la Zekaria 8:16 linasema: “Haya ndiyo mambo ambayo mnapaswa kufanya: Semeni ukweli kila mtu na mwenzake. Hukumuni kwa hukumu ya kweli na ya amani malangoni mwenu.” Katika siku za Zekaria eneo la malango lilikuwa sehemu za umma na wanaume wazee walisikiliza kesi katika sehemu hizo. (Ruthu 4:1; Nehemia 8:1) Hata hivyo, Zekaria hakusema kwamba huo ndio uliokuwa wakati pekee wa kusema ukweli. Ni lazima tuwe wanyoofu hadharani, lakini pia tunahimizwa hivi: “Semeni ukweli kila mtu na mwenzake.” Hiyo inatia ndani kusema ukweli nyumbani mwetu tunapozungumza na mwenzi wetu wa ndoa au watu wetu wa ukoo. Inatia ndani pia mazungumzo yetu ya kila siku pamoja na ndugu na dada zetu wa kiroho, iwe tunazungumza nao uso kwa uso, kupitia simu, au tunawasiliana nao kwa njia nyingineyo. Wana kila sababu ya kuamini kwamba yale tunayosema ni ya kweli. Wazazi Wakristo wanapaswa kukazia akilini mwa watoto wao umuhimu wa kutosema uwongo. Kwa njia hiyo watoto wanapokua wataelewa kwamba Mungu anataka waepuke ulimi ulio na udanganyifu na kuwa wanyoofu kabisa katika yale wanayosema.—Sefania 3:13.
12. Tunaweza kujifunza jambo gani muhimu kutokana na vitabu vya manabii?
12 Kijana au mtu mzima anayeshikamana na njia ya kweli anakubaliana na himizo hili la Zekaria: “Pendeni kweli na amani.” (Zekaria 8:19) Zingatia pia maelezo ya Malaki kuhusu sifa ambazo Yehova aliona katika Mwana Wake: “Sheria ya kweli ilikuwa katika kinywa chake, wala ukosefu wa uadilifu haukupatikana midomoni mwake. Kwa amani na kwa unyoofu alitembea nami.” (Malaki 2:6) Bila shaka Yehova anataka tuonyeshe sifa hizo, sivyo? Kumbuka kwamba tuna Neno lake kamili, kutia ndani vitabu vya wale manabii 12 na mambo yote tunayoweza kujifunza kutokana nao.
EPUKA JEURI
13. Andiko la Mika 6:12 linataja tatizo gani lingine lililokuwapo?
13 Andiko la Mika 6:12 linatuambia kwamba njia moja ambayo watu wa kale wa Mungu waliwatendea wengine vibaya ni kwa ‘kusema uwongo, na ulimi wao ulikuwa na udanganyifu kinywani mwao.’ Hata hivyo, andiko hilo linataja tatizo lingine kubwa sana. Linataja kwamba ‘watu walio matajiri walikuwa wamejaa jeuri.’ Jinsi gani, nasi tunaweza kujifunza nini?
14, 15. Rekodi zinaonyesha nini kuhusu jeuri katika mataifa yaliyokuwa karibu na watu wa Mungu?
14 Fikiria jinsi mataifa fulani ambayo yalikuwa karibu na watu wa Mungu yalivyokuwa. Taifa la Ashuru, na jiji lake kuu la Ninawi, lilikuwa upande wa kaskazini-mashariki. Nahumu aliandika hivi kuhusu taifa hilo: “Ole wake jiji la umwagaji wa damu. Limejaa udanganyifu na unyang’anyi. Mawindo hayaondoki!” (Nahumu 3:1) Waashuru walijulikana kwa sababu ya kupigana kwa ukali na kuwatesa kikatili wafungwa wa vita—baadhi ya wafungwa waliteketezwa au kutolewa ngozi wakiwa hai, na wengine walipofushwa au kukatwa pua, masikio, au vidole. Kitabu kimoja (Gods, Graves, and Scholars) kinasema: “Waninawi walijulikana sana kwa sababu ya kuua, kupora, kuwakandamiza watu, na kuwatesa walio dhaifu; kupitia vita na jeuri ya kila namna.” Tuna maneno yaliyosemwa na mtu aliyeshuhudia (na labda hata kushiriki) jeuri hiyo. Baada ya kusikia ujumbe wa Yona, mfalme wa Ninawi alisema hivi kuhusu watu wake: “Nao wajifunike nguo za magunia, mwanadamu na mnyama wa kufugwa; na wamwite Mungu kwa nguvu na warudi, kila mmoja kutoka katika njia yake mbaya na kutoka katika jeuri iliyokuwa mikononi mwao.”—Yona 3:6-8.b
15 Jeuri ilienea katika mataifa mengine mbali na Ashuru. Edomu, lililokuwa kusini-mashariki mwa Yuda lingeadhibiwa pia. Kwa nini? “Nayo Edomu itakuwa nyika ya mahame yenye ukiwa, kwa sababu ya jeuri kwa wana wa Yuda, ambao walimwaga damu isiyo na hatia katika nchi yao.” (Yoeli 3:19) Je, Waedomu walitii onyo hilo na kuacha matendo yao ya jeuri? Karne mbili hivi baadaye, Obadia aliandika hivi: “Wanaume wako wenye nguvu wataingiwa na woga, Ee Temani [jiji la Edomu], . . . Kwa sababu ya jeuri uliyomtendea ndugu yako Yakobo, . . . utakatiliwa mbali mpaka wakati usio na kipimo.” (Obadia 9, 10) Lakini namna gani watu wa Mungu?
16. Amosi na Habakuki wanatufunulia tatizo gani lililokuwapo siku zao?
16 Amosi alieleza jinsi hali ilivyokuwa katika Samaria, jiji kuu la ufalme wa kaskazini: “‘Mwone machafuko mengi yaliyo katikati yake na visa vya upunjaji vilivyo ndani yake. Nao hawajajua jinsi ya kufanya yaliyo manyoofu,’ asema Yehova, ‘wale wanaoweka jeuri akiba na uporaji.’” (Amosi 3:9, 10) Huenda ukadhani kwamba hali ilikuwa tofauti huko Yuda, ambako kulikuwa na hekalu la Yehova. Lakini Habakuki, aliyeishi Yuda, alimuuliza Mungu hivi: “Nitakuomba msaada kutokana na jeuri mpaka wakati gani, nawe usiokoe? Kwa nini unanionyesha jambo lenye kudhuru, nawe unaendelea kutazama taabu tupu? Na kwa nini kuna uporaji na jeuri mbele yangu?”—Habakuki 1:2, 3; 2:12.
17. Kwa nini huenda jeuri ilisitawi miongoni mwa watu wa Mungu?
17 Je, huenda jeuri ilisitawi miongoni mwa watu wa Mungu kwa sababu walijiruhusu waathiriwe na mtazamo wa Ashuru, Edomu, au mataifa mengine kuelekea jeuri? Sulemani alikuwa amewaonya kuhusu jambo hilo: “Usimwonee wivu mtu mwenye jeuri, wala kuchagua yoyote kati ya njia zake.” (Methali 3:31; 24:1) Baadaye, Yeremia alitaja mambo waziwazi: “Yehova amesema hivi: ‘Msijifunze njia ya mataifa hata kidogo.’”—Yeremia 10:2; Kumbukumbu la Torati 18:9.
Katuni na michezo mingi ya video huwapumbaza vijana na kuwafanya wafikiri kwamba jeuri inakubalika
18, 19. (a) Kama Habakuki angekuwa hai leo, angehisije kuhusu jeuri iliyopo leo? (b) Unahisije kuhusu jeuri katika nyakati zetu?
18 Kama Habakuki angekuwa hai leo, je, hangeshtuliwa na jeuri iliyopo leo? Watu wengi huzoea jeuri tangu ujanani. Katuni zinazowafurahisha wavulana na wasichana huonyesha jeuri. Katuni moja hujaribu kuiponda, kuilipua, au kuiangamiza katuni nyingine. Punde si punde, vijana wengi hupiga hatua na kuanza kucheza michezo ya video inayohusisha kuwashinda maadui kwa kuwapiga risasi, kuwalipua, au kuwaangamiza. Baadhi yao huenda wakadai, ‘Hiyo ni michezo tu.’ Hata hivyo, michezo yenye jeuri inayochezwa kwenye kompyuta nyumbani au katika ukumbi wa michezo hiyo huwazoeza wachezaji kutenda jeuri, na huathiri mitazamo na matendo yao. Shauri hili lililoandikwa kwa mwongozo wa roho takatifu ni la kweli kabisa: “Mtu wa jeuri atamshawishi mwenzake, naye hakika humfanya aende katika njia isiyo njema”!—Methali 16:29.
19 Ingawa Habakuki alilazimika kuendelea kutazama taabu tupu na ‘jeuri iliyokuwa mbele yake,’ mambo hayo yalimhuzunisha sana. Unaweza kujiuliza hivi: ‘Je, angefurahia kuketi pamoja nami na kutazama vipindi vya televisheni ambavyo mimi hutazama kwa ukawaida?’ Pia jiulize, ‘Je, angetenga wakati wa kutazama michezo yenye jeuri, ambayo hata wachezaji huvalia mavazi ya kujikinga kama yale yaliyovaliwa na wale walioshiriki mapigano ya kale ya kufa na kupona?’ Katika michezo fulani, watu wengi husisimuka wanapoona watu wakipigana kijeuri viwanjani au mashabiki wenye fujo wakitwangana. Katika baadhi ya tamaduni, wengi hutazama sinema na video zenye jeuri zinazokazia hasa kupigana vita au karate. Huenda wakadai ni sawa kwa sababu ni mambo ya kihistoria au ni utamaduni wa kale wa taifa, lakini je, sababu hizo zinafanya jeuri ikubalike?—Methali 4:17.
20. Malaki alizungumzia maoni ya Yehova kuhusu jeuri ya aina gani?
20 Malaki anataja zoea lingine la kijeuri anapoeleza maoni ya Yehova kuhusu hila ambayo Wayahudi fulani waliwatendea wake zao. “‘Amechukia talaka,’ Yehova, Mungu wa Israeli, amesema; ‘na yule ambaye amefunika vazi lake kwa jeuri.’” (Malaki 2:16) Maneno ya Kiebrania yaliyotafsiriwa “ambaye amefunika vazi lake kwa jeuri” yameeleweka kwa njia mbalimbali. Wasomi fulani husema kwamba maneno hayo yanamaanisha vazi la mtu kumwagikiwa na damu anapomshambulia mwingine kwa jeuri. Vyovyote vile, kwa wazi Malaki alikuwa akishutumu kumtendea vibaya mwenzi wa ndoa. Naam, Malaki alikuwa akizungumzia jeuri kuelekea washiriki wa familia naye alionyesha kwamba Mungu hakupendezwa na zoea hilo.
21. Wakristo wanapaswa kuepuka jeuri katika hali gani?
21 Jeuri inayofanywa faraghani ndani ya nyumba ya Mkristo, iwe ni kwa maneno au kupitia matendo haikubaliki kama vile jeuri inayofanywa hadharani isivyokubalika. Mungu anaona aina hizo zote za jeuri. (Mhubiri 5:8) Ingawa Malaki alikuwa akizungumza kuhusu mume kumtendea mke jeuri, hakuna andiko lolote la Biblia linalosema kwamba ni sawa kwake kuwatendea jeuri watoto au wazazi wake waliozeeka. Mke pia haruhusiwi kumtendea jeuri mume, watoto, au wazazi wake. Ni kweli kwamba katika familia yenye wanadamu wasiokamilika, wanaweza kukosana, kuchokozana, na nyakati nyingine kuwaka hasira. Hata hivyo, Biblia inatushauri hivi: “Iweni na ghadhabu, lakini msitende dhambi; jua lisitue mkiwa katika hali ya kuchokozeka.”—Waefeso 4:26; 6:4; Zaburi 4:4; Wakolosai 3:19.
22. Tunajuaje kwamba tunaweza kuepuka jeuri tujapozungukwa na watu wengi wajeuri?
22 Huenda watu fulani wakajitetea wanapotenda jeuri, kwa kusema, ‘Nilizaliwa katika familia yenye jeuri kwa hiyo siwezi kuiepuka,’ au ‘Watu wa jamii yetu au utamaduni wetu ni wakali sana, wanakasirika haraka sana.’ Hata hivyo, Mika alipowashutumu ‘matajiri waliojaa jeuri,’ hakuzungumza nao kana kwamba hawangeweza kuepuka jeuri kwa sababu walilelewa katika mazingira ya jeuri. (Mika 6:12) Noa aliishi wakati ambapo dunia ‘ilikuwa imejaa jeuri,’ na wanawe walilelewa katika mazingira hayo. Je, waliiga matendo hayo ya jeuri? La hasha! ‘Noa alipata kibali machoni pa Yehova,’ na wanawe walimfuata wakaokolewa wakati wa Furiko.—Mwanzo 6:8, 11-13; Zaburi 11:5.
23, 24. (a) Ni nini kinachotusaidia kuepuka kujulikana kuwa watu wajeuri? (b) Yehova anahisije kuhusu wale wanaowatendea wengine kama anavyotaka?
23 Mashahidi wa Yehova wanajulikana duniani pote kuwa watu wanaofanya amani wala si wenye jeuri. Wanaheshimu na kutii sheria za Kaisari zinazopinga matendo ya jeuri. (Waroma 13:1-4) Wamejitahidi ‘kufua panga zao ziwe majembe na mikuki yao kuwa miundu’ nao hujitahidi sana kufuatia amani. (Isaya 2:4) Wanajitahidi kuvaa “utu mpya,” ambao unawasaidia kuepuka jeuri. (Waefeso 4:22-26) Wao huiga mfano mzuri wa wazee Wakristo, ambao hawawezi ‘kuwapiga watu’ kwa maneno au kihalisi.—1 Timotheo 3:3; Tito 1:7.
24 Tunaweza na tunapaswa kuwatendea wengine kama Mungu anavyotaka tuwatendee. Hosea anasema: “Ni nani aliye na hekima, apate kuelewa mambo haya? Mwenye busara, apate kuyajua? Kwa maana njia za Yehova zimenyooka, na waadilifu ndio watakaotembea katika hizo.”—Hosea 14:9.
a Neno la Kiebrania linalotafsiriwa “kuuachilia ukosaji” kihalisi linamaanisha “kupita kosa.” Kuhusu maneno “kupita kosa,” msomi mmoja anasema kwamba “yanatokana na wazo la msafiri anayepita bila kuona kitu fulani ambacho hataki kukikazia fikira. Haimaanishi [kwamba Mungu haoni dhambi] bali kwamba hakazii uangalifu visa fulani vya dhambi akiwa na nia ya kuadhibu; yeye husamehe badala ya kuadhibu.”
b Jiji la Kala (Nimrud) lililojengwa upya na Ashurnasirpal lilikuwa umbali wa kilometa 35 hivi kusini-mashariki ya Ninawi. Jumba la Makumbusho la Uingereza lina mabamba ya kuta kutoka Kala, na maelezo yake yanasema hivi: “Ashurnasirpal alieleza kinaganaga ukatili na unyama wake katika vita. Wafungwa walinyongwa au kutundikwa mitini kwenye kuta za majiji yaliyoshindwa . . . ; vijana wanaume na wanawake walitolewa ngozi wakiwa hai.”—Archaeology of the Bible.
-
-
Unaloweza Kufanya Ili Maisha ya Familia Yampendeze MunguIzingatie Siku ya Yehova Maishani
-
-
SURA YA KUMI
Unaloweza Kufanya Ili Maisha ya Familia Yampendeze Mungu
1. Kwa nini Mashahidi wa Yehova kwa ujumla wanakuwa na familia zenye furaha?
MASHAHIDI WA YEHOVA wanajulikana sana kwa sababu ya kuwa na familia zenye furaha. Profesa Bryan Wilson wa Chuo Kikuu cha Oxford aliandika hivi: “Mashahidi hutoa mashauri mengi sana yanayofaa . . . kuhusiana na ndoa, maadili, kuwalea watoto, na masuala mengine muhimu. Wanaweza kuwasaidia sana watu kupitia mashauri thabiti yanayotegemea Biblia Takatifu ambayo ni sehemu ya viwango na miongozo inayotegemeka ya maisha.” Bila shaka, umejifunza mengi kutokana na Neno la Mungu kuhusu kuwa na maisha mazuri ya familia.
2. (a) Umeona familia zikoje katika ulimwengu wa leo? (b) Tutapata mwongozo kuhusu maisha ya familia katika vitabu gani vya Biblia?
2 Kadiri siku ya Yehova inavyokaribia, Shetani anazidi kushambulia familia. Kwa hiyo, kama ilivyokuwa katika siku za Mika, watu wengi leo hawawaamini washiriki wa familia zao wenyewe. Mika aliandika hivi: “Msimwamini mwenzi. . . . Linda milango ya kinywa chako kutokana na yeye anayelala kifuani pako. Kwa maana mwana anamdharau baba, binti anasimama kumpinga mama yake; binti-mkwe kumpinga mama-mkwe wake; adui za mtu ni watu wa nyumba yake.” (Mika 7:5, 6) Unaishi katika ulimwengu ambamo mpango wa familia umezorota, hata hivyo umejitahidi sana kutoathiriwa. Basi, maisha ya familia yenu yatakuwa mazuri zaidi, na yenye kumpendeza Mungu. Ni wazi kwamba umetumia maandiko kama vile Kumbukumbu la Torati 6:5-9; Waefeso 5:22–6:4; na Wakolosai 3:18-21. Hata hivyo, je, unajua kwamba vitabu vya wale manabii 12 vina mashauri mengi kuhusu maisha ya familia yenye furaha? Katika sura hii, tutachunguza mifano michache ya mashauri yanayohusu familia yaliyo katika vitabu hivyo. Lakini usitosheke tu na mashauri hayo hususa. Jitahidi kuona kupitia mifano hiyo mbinu ambazo unaweza kutumia kujifunza mambo mengine katika vitabu hivyo. Kuna maandiko kadhaa mwishoni mwa sura hii yatakayokusaidia kuona jinsi unavyoweza kujifunza mengi kutokana na vitabu hivyo 12.
“AMECHUKIA TALAKA”
3, 4. (a) Watu wengi leo hujaribu kusuluhisha matatizo yao ya ndoa kwa njia gani? (b) Watu wa siku za Malaki walikuwa na mtazamo gani usiofaa kuhusu ndoa?
3 Jambo la kwanza muhimu ni uhusiano kati ya mume na mke. Kwa muda mrefu, watu wengi hawakuona talaka kuwa njia ya kusuluhisha matatizo ya ndoa. Kwa kawaida ilikuwa vigumu kupata talaka; katika karne ya 19 nchini Uingereza, Bunge tu ndilo lingeweza kuidhinisha talaka. Maoni hayo yalizuia familia kuvunjika. Lakini mambo yamebadilika sana leo. Kitabu Encyclopædia Britannica kinasema: “Viwango vya talaka vimeongezeka sana katika nchi nyingi tangu Vita vya Pili vya Ulimwengu . . . Maoni ya watu kuhusu talaka yamebadilika kabisa . . . wengi wao wanakubali talaka.” Talaka imekuwa jambo la kawaida hata katika nchi kama vile Korea, ambako miaka kumi iliyopita, watu walichukia sana zoea hilo. Leo, watu katika nchi nyingi wanahisi kwamba mume na mke ambao wana matatizo ya ndoa watalikiane.
4 Siku za Malaki, karne ya tano K.W.K., Wayahudi wengi walikuwa wakitalikiana. Malaki aliwaambia: “Yehova ametoa ushahidi kati yako na mke wa ujana wako, ambaye wewe umemtendea kwa hila.” Kwa sababu ya waume kuwatendea wake zao kwa hila, madhabahu ya Yehova yalifunikwa kwa machozi ya wanawake waliotendewa hila, “kwa kulia na kuugua.” Inashangaza kwamba makuhani hao wafisadi walipuuza ukatili huo!—Malaki 2:13, 14.
5. (a) Yehova anaonaje talaka? (b) Kwa nini kumtendea mwenzi wa ndoa kwa hila ni jambo zito sana?
5 Yehova alikuwa na maoni gani kuhusu mtazamo mbaya uliokuwapo kuelekea ndoa katika siku za Malaki? Malaki aliandika hivi: “‘Amechukia talaka,’ Yehova, Mungu wa Israeli, amesema.” Pia alikazia kwamba Yehova ‘hajabadilika.’ (Malaki 2:16; 3:6) Je, unaelewa maana ya Maandiko hayo? Tangu zamani, Mungu alichukua msimamo dhidi ya talaka. (Mwanzo 2:18, 24) Alichukia talaka katika siku za Malaki na bado anaichukia leo. Huenda watu fulani wakaamua kumwacha mwenzi wao wa ndoa kwa sababu tu hawaridhiki naye. Hata hivyo, Yehova anauchunguza moyo wao wenye hila. (Yeremia 17:9, 10) Anaona udanganyifu au hila yoyote ambayo mtu anatunga ili kumtaliki mwenzi wake, hata akitoa sababu zipi za kufanya hivyo. Ndiyo, “vitu vyote viko uchi navyo vimefunuliwa wazi machoni pake yeye ambaye tunatoa hesabu kwake.”—Waebrania 4:13.
6. (a) Kuwa na maoni ya Yehova kuhusu talaka kutakusaidiaje? (b) Shauri la Yesu kuhusu talaka lilikazia nini?
6 Huenda ndoa yako haikabili hatari ya talaka, hata hivyo, unapaswa kukumbuka maoni ya Yehova. Hakuna mwanadamu aliye mkamilifu, kwa hiyo tunaweza kutarajia matatizo na kutoelewana katika ndoa. Hata hivyo, je, utachagua talaka na kuiona kuwa njia rahisi ya kusuluhisha matatizo? Wakati wa mabishano makali, je, utataja uwezekano wa kutalikiana? Wengi wamefanya hivyo, lakini maoni ya Mungu kuhusu ndoa yanapendekeza kwamba watu wajitahidi sana kufanikisha ndoa yao. Yesu Kristo alisema kwamba kuna msingi mmoja halali wa talaka—uasherati, yaani, uhusiano wowote wa ngono nje ya ndoa. Hata hivyo, shauri la Yesu lilikazia nini? Aliwaambia hivi wale waliomsikiliza: “Kile ambacho Mungu ameunganisha mtu yeyote asikitenganishe.” Naam, Yesu alikazia kiwango cha Yehova kisichobadilika, ambacho Malaki alikuwa ametaja miaka 450 hivi awali.—Mathayo 19:3-9.
Je, ungefikiria kumtaliki mwenzi wako wa ndoa mnapokosana?
7. Kulingana na shauri lililo katika kitabu cha Malaki, unaweza kudumishaje kifungo cha ndoa chenye nguvu?
7 Basi, wenzi wa ndoa Wakristo wanaweza kudumishaje kifungo chenye nguvu? Malaki anataja siri hii: “Nanyi mjilinde roho yenu, nanyi msitende kwa hila.” (Malaki 2:16) Hiyo inamaanisha kuchanganua mwelekeo wenye nguvu ulio moyoni mwetu. ‘Tukiilinda roho yetu,’ tutaepuka majaribu ya kumtamani mtu ambaye si mwenzi wetu wa ndoa. (Mathayo 5:28) Kwa mfano, vipi ikiwa tunafurahia moyoni mwetu kuonyeshwa mahaba au kuchezewa kimapenzi na mtu mwingine wa jinsia tofauti? Hilo lingemaanisha kwamba hatuilindi roho yetu. Kwa hiyo, jambo kuu ambalo tunajifunza kutokana na wale manabii 12 ambalo litatusaidia kuwa na kifungo cha ndoa chenye nguvu ni kuilinda ‘roho yetu.’
Tunajifunza nini kumhusu Yehova kupitia kisa cha Hosea kumchukua tena Gomeri?
8, 9. Kwa nini kisa cha Hosea na Gomeri kiliandikwa katika Biblia?
8 Hapana shaka kwamba umeazimia kuhakikisha kwamba ndoa yako inafanikiwa. Hata hivyo, huwezi kuepuka matatizo ya ndoa. Ni njia gani nzuri unayoweza kutumia kushughulikia matatizo yoyote yanayotokea, hasa ikiwa unahisi kwamba mara nyingi mwenzi wako ndiye anayeyasababisha? Kumbuka mambo yaliyosemwa kumhusu Hosea katika Sura ya 2 na ya 4 ya kitabu hiki. Mke wake, Gomeri, alikuwa “mke wa uasherati” na ‘aliwafuata wale waliompenda kwa tamaa nyingi.’ Baadaye, aliachwa, akawa maskini na mtumwa. Hosea alimnunua Gomeri kutoka kwa mwanamume aliyekuwa akiishi naye, na alihimizwa ampende. Kwa nini? Ili kuonyesha waziwazi uhusiano wa Yehova na Waisraeli. Yehova alikuwa “mume,” na watu wake walikuwa kama mke wake.—Hosea 1:2-9; 2:5-7; 3:1-5; Yeremia 3:14; Isaya 62:4, 5.
9 Tangu zamani, Waisraeli walimtia Yehova uchungu walipofuata miungu mingine. (Kutoka 32:7-10; Waamuzi 8:33; 10:6; Zaburi 78:40, 41; Isaya 63:10) Ufalme wa kaskazini wenye makabila kumi ulikuwa hasa na hatia ya kuabudu ndama. (1 Wafalme 12:28-30) Isitoshe, Waisraeli hawakumtegemea Mume wao, Yehova, badala yake waliwategemea wapenzi wao wa kisiasa. Pindi moja, walifuata Ashuru kama punda-milia mwenye tamaa ya kupandwa. (Hosea 8:9) Utahisije mwenzi wako wa ndoa akitenda hivyo?
10, 11. Unaweza kumwigaje Yehova inapoonekana kwamba mwenzi wako wa ndoa amekukosea?
10 Kufikia wakati wa Hosea, miaka zaidi ya 700 ilikuwa imepita tangu Waisraeli walipofanya agano na Yehova. Hata hivyo, Mungu alikuwa tayari kuwasamehe, ikiwa tu wangemrudia. Inakisiwa kwamba Hosea alianza kutabiri kabla ya mwaka wa 803 K.W.K., kwa hiyo, Yehova aliendelea kuvumilia Israeli kwa miaka mingine 60 na Yuda kwa miaka karibu 200! Akitumia familia ya Hosea kama mfano, Yehova aliendelea kuwaomba watu wake wa agano watubu. Alikuwa na sababu nzuri za kuvunja ndoa yake na Waisraeli, hata hivyo, aliwatuma manabii tena na tena ili wamsaidie mke wake wa mfano kumrudia, hata ingawa ilimgharimu Yehova.—Hosea 14:1, 2; Amosi 2:11.
11 Namna gani ikiwa inaonekana kwamba mwenzi wako wa ndoa amekukosea, je, utatenda kama Yehova alivyotenda? Je, utajitahidi kuiboresha ndoa yako ili iwe nzuri kama mwanzoni? (Wakolosai 3:12, 13) Ili kufanya hivyo unahitaji unyenyekevu. Yehova alituwekea kielelezo bora sana katika kushughulika na Waisraeli! (Zaburi 18:35; 113:5-8) Mungu ‘alisema kwa kufikia moyo wa Waisraeli,’ hata aliwasihi. Basi, tukiwa wanadamu wasio wakamilifu, tuna sababu nzuri hata zaidi ya kusema kwa kufikia moyo wa mwenzi wetu wa ndoa, kujitahidi kusuluhisha matatizo, na kusamehe makosa. Kwa kweli, jitihada za Yehova zilifaulu. Mabaki ya Waisraeli waliguswa moyo walipokuwa nyikani, yaani, uhamishoni huko Babiloni, na baadaye walirudi katika nchi yao, wakimwita Yehova, “Mume wangu.”—Hosea 2:14-16.a
Mwige Yehova kwa kuanzisha mazungumzo ya kusuluhisha tatizo lolote
12. Kutafakari jinsi Yehova alivyoshughulika na mke wake wa mfano kunaweza kuisaidia ndoa yako jinsi gani?
12 Tatizo kubwa linapotokea, unaweza kufaulu kwa kujitahidi kwa unyoofu kupatana na mwenzi wako. Mungu alikuwa tayari kusamehe hata dhambi nzito ya uasherati wa kiroho iliyofanywa na mke wake wa mfano. Matatizo mengi ya ndoa miongoni mwa Wakristo wa kweli hayajafikia kiwango hicho. Matatizo mengi husababishwa na maneno makali au yenye kuumiza. Kwa hiyo, ikiwa mwenzi wako amekuumiza kwa maneno yenye kuchoma, fikiria hisia za Hosea na za Yehova mwenyewe. (Methali 12:18) Mfano wao unaweza kukusaidia kusamehe, sivyo?
13. Tunajifunza nini tunapozingatia hali ya Yehova ya kuwataka watu wake walioasi watubu?
13 Bado kuna jambo lingine tunalojifunza katika simulizi hilo la kale. Je, Mungu alikuwa tayari kuwa na uhusiano tena na watu wake huku wakiendelea kufanya uasherati? Mungu alimwambia hivi Hosea kuhusu taifa hilo lililokuwa likifanya uzinzi: “Anapaswa kuondolea mbali uasherati wake kutoka mbele yake na matendo yake ya uzinzi kutoka katikati ya maziwa yake.” (Hosea 2:2) Watu hao walihitaji kutubu na ‘kuzaa matunda yanayofaa toba.’ (Mathayo 3:8) Kwa hiyo, kazia fikira makosa yako badala ya makosa ya mwenzi wako. Ikiwa umemkosea mwenzi wako, mbona usijitahidi kupatana naye kwa kumwomba msamaha kutoka moyoni na kutorudia kosa hilo? Unaweza kusamehewa.
“KAMBA ZA UPENDO” —MSINGI WA KUTIA NIDHAMU
14, 15. (a) Kulingana na Malaki 4:1, kwa nini unapaswa kuchukua kwa uzito jukumu la kuwafundisha watoto wako? (b) Unaweza kuwasaidiaje watoto wenu wamjue Yehova?
14 Tunaweza kujifunza mengi zaidi kuhusu maisha ya familia kutokana na jinsi Yehova alivyoshughulika na Waisraeli kama inavyoelezwa katika vitabu vya wale manabii 12. Vitabu hivyo vinaonyesha jinsi ya kuwafundisha watoto wako. Kwa kweli, kuwalea watoto leo si rahisi. Ni lazima wazazi wachukue jukumu lao kwa uzito. Tunasoma hivi: “‘Siku hiyo inayokuja itawateketeza [watu],’ Yehova wa majeshi amesema, ‘hivi kwamba haitawaachia wao mzizi wala tawi.’” (Malaki 4:1) Katika siku hiyo ya kutozwa hesabu, watoto wachanga (matawi) watahukumiwa kwa haki wakati Yehova anapowachunguza wazazi wao (mizizi), ambao wanawajibika kwa ajili ya watoto wachanga. (Isaya 37:31) Wakati ujao wa watoto utakuwa mzuri au mbaya ikitegemea maisha ya wazazi wao. (Hosea 13:16) Ikiwa ninyi (mizizi) hamdumishi msimamo mzuri mbele za Yehova, ni nini kitakachowapata watoto wenu (matawi) katika siku yake ya ghadhabu? (Sefania 1:14-18; Waefeso 6:4; Wafilipi 2:12) Kwa upande mwingine, jitihada zenu za uaminifu za kumpendeza Yehova zinaweza kuwafaidi watoto wenu wachanga.—1 Wakorintho 7:14.
15 Baada ya kunukuu unabii wa Yoeli kuhusu uhitaji wa kuliitia jina la Yehova, mtume Paulo aliandika hivi: “Watawezaje kumwitia yeye ambaye hawajamwamini? Nao watamwaminije yeye ambaye hawajamsikia?” (Waroma 10:14-17; Yoeli 2:32) Paulo alikuwa akizungumza kuhusu huduma yetu ya hadharani, lakini mnaweza kutumia kanuni hiyo katika kuwafundisha watoto wenu. Watamwaminije Yehova ikiwa hawajasikia kumhusu? Je, mnatumia wakati wa kutosha kila siku kuwafundisha watoto wenu jinsi Yehova alivyo mwema, na kuwasaidia wampende kwa moyo wote na kupenda mwongozo wake? Inaelekea kwamba watoto watafanya maendeleo ya kiroho wakisikia daima kumhusu Yehova katika familia.—Kumbukumbu la Torati 6:7-9.
16. Kulingana na Mika 6:3-5, unaweza kumwigaje Yehova unapowatia nidhamu watoto wako?
16 Watoto wanapokuwa wadogo, huenda ikawa rahisi zaidi kuhudhuria mikutano ya Kikristo pamoja nao. Lakini wanapokuwa na umri mkubwa zaidi, wanaanza kuwa na maoni yao wenyewe. Utawasaidiaje watoto wako ikiwa wanakuwa na mwelekeo wa kuasi mara kwa mara? Unaweza kujifunza kutokana na vitabu vya wale manabii 12, na kuona jinsi Yehova alivyoshughulika na Israeli na Yuda. (Zekaria 7:11, 12) Kwa mfano, unaposoma Mika 6:3-5, fikiria hisia zinazoonyeshwa. Waisraeli walikuwa wametenda dhambi; lakini Mungu bado aliwaita “watu wangu.” Aliwasihi hivi: “Tafadhali, enyi watu wangu, kumbukeni.” Badala ya kuwashutumu kwa ukali, alijaribu kufikia mioyo yao. Je, unaweza kumwiga Yehova hata unapowatia nidhamu watoto wako? Hata wakitenda kosa gani, watendee kama sehemu ya familia yako, usiwaaibishe. Badala ya kuwashutumu, wasihi kwa upendo. Waulize maswali ili kujua yaliyo moyoni mwao. Jitahidi kuufikia moyo wao ili waeleze hisia zao kwa uhuru.—Methali 20:5.
17, 18. (a) Ni nini kinachopaswa kukuchochea kuwatia nidhamu watoto wako? (b) Utadumishaje “kamba za upendo” kati yako na watoto wako?
17 Kwa nini unawatia nidhamu watoto wako? Wazazi fulani huwatia nidhamu kwa sababu hawataki familia yao iwe na sifa mbaya. Yehova alionyesha kile kilichomchochea kutoa nidhamu, alipotangaza hivi: “Nilimfundisha Efraimu kutembea, nikawachukua mikononi mwangu . . . Nilizidi kuwavuta kwa kamba za mtu wa udongo, kwa kamba za upendo.” (Hosea 11:3, 4) Katika andiko hilo, Hosea analinganisha uhusiano wa Yehova na Waisraeli na ule wa baba na mwana. Hebu wazia mzazi mwenye upendo, akimwongoza mtoto kwa kamba, akijaribu kumsaidia kutembea mtoto huyo anayeyumbayumba. Anapojikwaa anajitegemeza kwa kamba hizo ili asianguke, na zinamwongoza asipotee njia.—Yeremia 31:1-3.
Ukiwa mzazi, je, unamwiga Yehova kwa kuwaonyesha watoto wako upendo?
18 Je, utaiga upendo wa Yehova kwa Waisraeli? Walimwasi tena na tena, lakini hakuachilia kamba hizo za upendo. Nyakati nyingine huenda watoto wakapotea njia na kukwazwa na mambo madogo, lakini jaribu kudumisha kifungo cha upendo pamoja nao. Kumbuka kwamba Yehova hakuwaonyesha watu wake upendeleo na kupuuza makosa yao. Alishughulikia makosa yao ifaavyo, akawatia nidhamu kwa upendo, na kuwapa msaada waliohitaji. Ukiona kwamba mwana au binti yako anaacha njia ya kweli pole kwa pole, usipuuze jambo hilo. Jitahidi kumsaidia arudi kwenye njia ya kweli, kana kwamba unamwongoza kwa kamba, na kumsaidia kwa upendo wakati huo mgumu. Usikate tamaa kuwasaidia watoto wako wakiwa na matatizo. Ni muhimu sana kutumia wakati pamoja na watoto wako!
19. Kwa nini hupaswi kukata tamaa kuwasaidia watoto wako?
19 Hosea alitabiri kwamba mabaki ya Waisraeli wangekubali nidhamu: “Wana wa Israeli watarudi na hakika watamtafuta Yehova Mungu wao, na Daudi mfalme wao; nao watakuja kwa Yehova na kwa wema wake wakitetemeka katika siku za mwisho.” (Hosea 3:5) Naam, nidhamu ya Yehova iliwarekebisha mabaki ya watu wake. Uwe na mtazamo unaofaa kwamba nidhamu yako itawasaidia watoto wako. Jitahidi kuona sifa zao nzuri. Zungumza nao kwa fadhili huku ukishikamana na kanuni za Biblia kwa uthabiti. Hata ikiwa mtoto aliyeasi hatabadilika sasa, huenda akabadilika wakati ujao.
JIHADHARI NA MASHIRIKA MABAYA!
20. Ni swali gani kuhusu mashirika ambalo watoto wanaweza kupata jibu lake katika vitabu vya wale manabii 12?
20 Ninyi watoto mnaweza kujifunza nini kutokana na vitabu vya wale manabii 12? Mojawapo ya maandiko ambayo huenda yananukuliwa mara nyingi mnapozungumza na wazazi wenu ni 1 Wakorintho 15:33 kuhusu kuepuka mashirika mabaya. Huenda baadhi yenu mkauliza, ‘Lakini je, kuwa na marafiki ambao hawamwabudu Yehova ni vibaya kweli?’ Mnaweza kupata jibu la swali hilo katika vitabu vya wale manabii 12.
21-23. (a) Vijana wanaweza kujifunza nini kutokana na mwenendo wa Waedomu? (b) Ni nani walio rafiki zako kikweli?
21 Ijapokuwa ujumbe ulio katika vitabu vya wale manabii 12 uliwahusu hasa watu wa Mungu, ujumbe ulio katika kitabu cha Obadia uliwahusu Waedomu ambao waliitwa ndugu za Waisraeli.b (Kumbukumbu la Torati 2:4) Tofauti na vitabu vile vingine vya manabii hao 12, Obadia hutumia neno “wewe” anapozungumza na Waedomu. Hebu sasa wafikirie Waedomu. Ni karibu mwaka wa 607 K.W.K., wakati ambapo Yerusalemu linazingirwa. Ingawa Waedomu ni watu wa ukoo wa Yakobo, wanashirikiana na Wababiloni! Waedomu wanadhihaki hivi: “Lifanye ukiwa! Lifanye ukiwa!” (Zaburi 137:7; Obadia 10, 12) Wanapanga kuiteka nchi ya Yuda. Hata wanakula pamoja na Wababiloni, jambo ambalo katika nchi za kale za Mashariki ya Kati linaweza kumaanisha kwamba watu hao wamefanya agano.
22 Angalia jinsi Obadia anavyotabiri kuhusu Waedomu: “Watu walewale [Wababiloni] walio katika agano pamoja nawe wamekudanganya wote. Watu walio na amani pamoja nawe wamekushinda. Wale wanaokula chakula pamoja nawe wataweka wavu chini yako kama mtu asiye na utambuzi.” (Obadia 7) Ni nini kilichowapata Waedomu, ambao walimtoroka ndugu yao, Yakobo, na kuamua kushirikiana na Wababiloni? Hatimaye, Wababiloni wakiongozwa na Nabonido waliwaangamiza Waedomu. Kufikia siku za Malaki, Mungu alikuwa amefanya milima ya Edomu kuwa ukiwa na urithi wa Edomu kuwa wa mbwa-mwitu.—Malaki 1:3.
23 Hebu sasa wafikirie wale unaowaita rafiki zako ambao hawamwabudu Yehova. Je, hujaona kwamba ‘wavulana [au wasichana] walewale walio katika agano,’ au wenye urafiki, mara nyingi wanadanganyana na ‘kuweka wavu chini’ ya wale wanaodai kwamba ni rafiki zao? Udanganyifu wao unapogunduliwa, wao husema nini? Huenda wakasema kwamba rafiki hao waliodanganyika ni washamba, wasioweza kutambua kwamba wanadanganywa. Wanatenda tu jinsi Wababiloni walivyowatendea rafiki zao, Waedomu! Je, unafikiri kwamba “rafiki” kama hao wanaweza kukusaidia unapokumbwa na matatizo? (Obadia 13-16) Kwa upande mwingine, hebu mfikirie Yehova Mungu na watu wake leo. Sikuzote, Yehova huwa tayari kukusaidia. Atakutegemeza wakati wa taabu. Watu wake pia ni ‘rafiki wa kweli wanaopenda nyakati zote,’ ni kama waaminifu ‘waliozaliwa kwa ajili ya wakati wa taabu.’—Methali 17:17.
Je, wale wanaodai kuwa rafiki zako ‘wanaweka wavu chini yako’?
THAMINI UHUSIANO ULIO MUHIMU KUPITA YOTE
24, 25. Jambo muhimu zaidi maishani mwetu lapaswa kuwa nini?
24 Mahusiano ya familia ni muhimu na yanastahili kuimarishwa. Tunaweza kujifunza mambo mengi kuhusu mahusiano ya familia kutoka katika vile vitabu 12 vya kinabii. Tafadhali soma na uchunguze vitabu hivyo kwa kutumia njia tuliyotumia. Ukifanya hivyo utajifunza mambo mengi hata zaidi ambayo yataboresha maisha ya familia yako. Hata hivyo, je, kuwa na maisha ya familia yenye furaha ndilo jambo muhimu zaidi kwa waabudu wa Mungu leo?
25 Yoeli alitabiri jambo linalotupendeza kuhusu kuja kwa siku ya Yehova: “Kusanyeni watu pamoja. Takaseni kutaniko. . . . Bwana-arusi na atoke katika chumba chake cha ndani, bibi-arusi naye atoke katika chumba chake cha ndoa.” (Yoeli 2:15, 16) Kila mtu nyumbani alipaswa kukusanyika pamoja kumwabudu Yehova. Hata wale waliofunga ndoa karibuni, ambao kwa kawaida huwa wamekengeuka fikira wakati huo, hawakupaswa kukosa! Hakuna jambo linalopaswa kuwa muhimu kuliko kukusanyika kwetu mbele za Mungu. Siku ya Yehova inapokaribia kwa haraka, kuwa na msimamo mzuri mbele zake kwapaswa kuwa jambo muhimu zaidi maishani mwetu. Katika sehemu ya mwisho ya kitabu hiki, tutazungumzia kazi ambayo tunapaswa kufanya leo kwa shangwe.
a Ikiwa mume au mke Mkristo ana hatia ya kufanya uzinzi, mwenzi asiye na hatia anapaswa kuamua ikiwa atamsamehe au la.—Mathayo 19:9.
b Kitabu kingine ambacho ujumbe wake haukuwahusu Waisraeli ni kile cha Nahumu. Ujumbe wake uliwahusu Waninawi.
-
-
Yehova Anataka Watu Wapate Uzima—Je, Ndivyo Unavyotaka Pia?Izingatie Siku ya Yehova Maishani
-
-
SURA YA KUMI NA MOJA
Yehova Anataka Watu Wapate Uzima—Je, Ndivyo Unavyotaka Pia?
1, 2. (a) Tunaweza kujifunza nini kutokana na jinsi Yona alivyoitikia uamuzi wa Yehova kuhusu Ninawi? (b) Kwa nini tunapaswa kuchunguza rehema ya Mungu na maoni yake kuhusu uhai?
YEHOVA alifurahi. Lakini nabii Yona alikasirika. Kwa rehema, Mungu hakuangamiza maelfu ya watu. Yona angewaacha waangamie! Yehova aliamua kuwasamehe na kuwaacha watu hao waliokuwa adui za watu wake waishi.
Nyakati nyingine huenda hata watumishi wa Mungu wakakosa kuelewa rehema yake kikamili
2 Kisa cha Yona kinatuonyesha kwamba nyakati nyingine wanadamu hushindwa kuelewa uvumilivu wenye subira wa Mungu nao hushindwa kuonyesha tamaa Yake kwamba wanadamu wapate uzima. Uamuzi wa Yehova wa kutowaangamiza Waninawi ‘haukumpendeza Yona hata kidogo, naye akawaka hasira.’ Je, yawezekana kwamba Yona alijifikiria tu mwenyewe badala ya kutanguliza rehema na kuokoa uhai? Huenda alidhani kwamba kama Waninawi hawangeangamizwa, angeonwa kuwa nabii asiyetegemeka. (Yona 4:1, 10, 11) Namna gani leo, siku ya Yehova ya hukumu inapokaribia haraka? Huenda ukauliza: ‘Ninaweza kuthaminije zaidi msamaha wa Mungu, na kuwasaidia watenda-dhambi wenye kutubu ili wafaidike kikamili zaidi na upendo wake? Ninaweza kuigaje tamaa ya Mungu ya kutaka watu wapate uzima?’
KUONYESHA HAKI NA REHEMA ILI KUOKOA UHAI
3. Je, haki ya Mungu inapingana na rehema yake? Eleza.
3 Watu fulani wanasema kwamba vitabu hivyo 12 vya manabii, vinakazia sana ghadhabu ya Mungu na jinsi anavyowaadhibu watu, na kutekeleza haki. Huenda wakauliza: ‘Mbona havizungumzii rehema ya Yehova? Je, kuokoa uhai ni jambo muhimu kwake?’ Haki ya Mungu na rehema yake hazipingani, badala yake zinakamilishana na husaidia kuokoa uhai. Haki na rehema ni sifa mbili za utu wake wenye usawaziko kamili. (Zaburi 103:6; 112:4; 116:5) Mungu anawaonyesha rehema wale walio na mwelekeo unaofaa kwa kuondoa madhara ya waovu. Kwa njia hiyo anathibitisha haki yake kamilifu. Kwa upande mwingine, kwa sababu ya haki yake kamilifu, Yehova huzingatia kwa rehema udhaifu wa wanadamu wasio wakamilifu. Tunaweza kusema hivi: Yehova hutoa adhabu inapohitajika, na kuonyesha rehema inapowezekana. Katika ujumbe wa manabii, unaweza kupata taarifa nyingi zinazoonyesha usawaziko huo mkamilifu, na zinathibitisha kwamba Mungu anataka watu wapate uzima. Na tuchunguze habari hiyo na kujifunza mambo tunayoweza kutumia maishani leo.
4. Kuna uthibitisho gani kwamba Mungu anataka watu wapate uzima?
4 Nabii Yoeli alitangaza ujumbe wa shutuma, hata hivyo, alikazia pia kwamba Mungu “ana neema na rehema, si mwepesi wa hasira naye ni mwingi wa fadhili zenye upendo.” (Yoeli 2:13) Baada ya miaka 100 hivi kupita, katika karne ya nane K.W.K., Mika alikazia jinsi ambavyo tunahitaji sana msamaha wa Yehova. Baada ya kuuliza “Ni nani aliye Mungu kama wewe?” Mika alisema hivi kumhusu Yehova: “Hatashikilia hasira yake milele, kwa maana yeye hupendezwa na fadhili zenye upendo. Atatuonyesha rehema tena.” (Mika 7:18, 19) Kutokana na simulizi la Yona kuhusu Waninawi, tunaweza kuona kwamba Mungu yuko tayari kubadili uamuzi wa kuwahukumu watu wanaomkasirisha ikiwa wataonyesha toba yao kwa matendo yanayofaa.
5. Ni mambo gani kuhusu rehema ya Mungu na tamaa yake ya kuokoa uhai yanayokuvutia zaidi? (Ona pia sanduku lenye kichwa “Walijitolea.”)
5 Sisi hatuishi katika siku za wale manabii 12. Hata hivyo, je, hatuthamini mambo hayo yanayothibitisha rehema ya Yehova na tamaa yake ya kuwaokoa watu? Hisia hiyo inaweza kuimarisha uhusiano wako pamoja na Mungu na kukuchochea uwasaidie wengine kupata uzima. Ijapokuwa watu wengi leo huishi maisha mapotovu, tuna hakika kwamba Mungu “hataki yeyote aangamizwe bali hutaka wote wafikie toba.” (2 Petro 3:9) Tamaa hiyo ya Yehova inaonyeshwa na maneno yenye kuvutia yaliyosemwa na Hosea alipomchukua tena mke wake mzinzi. Yehova ‘alisema kwa kufikia moyo’ wa watu wake. Haikuwa lazima kwa Mungu kuwasamehe, lakini alikuwa tayari kufanya hivyo ‘kwa kupenda kwake mwenyewe.’ (Hosea 1:2; 2:13, 14; 3:1-5; 14:4) Je, unajua ni kwa nini mtazamo na matendo ya Mungu ni muhimu sana katika kuonyesha rehema? Kwa sababu uhai wa watu unahusika. Unaweza kuona uthibitisho zaidi wa rehema ya Mungu na tamaa yake ya kutaka watu wapate uzima ukichunguza kutaniko la Kikristo, ambalo linafanya kazi unayofanya.
KUWASAIDIA WATU WAPATE UZIMA
6. Mungu anaonyesha kwa njia gani kuu kwamba anataka watu wapate uzima?
6 Kwa nini unashiriki katika kazi ya kuhubiri? Sababu moja kuu ni kwamba unataka kuwasaidia wengine wapate kumjua Mungu wa kweli. Unahitaji kujua jambo hili muhimu kumhusu Yehova: Yeye hutoa maonyo yaliyo wazi kabla ya kutoa adhabu. Hilo linaonyesha rehema yake kwa watu. Hataki watu wafe, anataka wapate uzima. Wale manabii 12 waliwajulisha watenda-dhambi kwamba Mungu alikuwa akiwapa nafasi ya kubadili njia zao ili waepuke hasira yake yenye uadilifu. Tunafanya kazi kama hiyo leo. Ukiwa Mkristo, una pendeleo la kutangaza onyo kuhusu siku inayokuja ya Mungu kulipiza kisasi. Unapotoa onyo hilo, epuka hisia za kutaka kulipiza kisasi na kutaka watu wasiotii wapate adhabu wanayostahili. Jikumbushe kwamba unahubiri ili wengine waipate barabara ya uzima.—Yoeli 3:9-12; Sefania 2:3; Mathayo 7:13, 14.
7. (a) Kwa nini ni muhimu kushiriki katika kazi ya kuhubiri? (b) Kutafakari kuhusu mtazamo wa Yehova kutatusaidiaje watu wanapopuuza ujumbe wetu?
7 Kila mara unapohubiri kweli za Biblia nyumba kwa nyumba, shuleni, kazini, au kwingineko, unamsaidia mtu fulani ambaye anahitaji sana rehema na msamaha wa Mungu. (Hosea 11:3, 4) Huenda ukapingwa au ujumbe wako ukapuuzwa. Hata hivyo, ukiendelea kuhubiri licha ya hali hizo, unamwiga Mungu wetu mwenye rehema, ambaye aliwaambia hivi watu Wake waasi kupitia Zekaria: “Tafadhali, rudini mwache njia zenu mbaya na mwache matendo yenu mabaya.” (Zekaria 1:4) Hatujui ni watu wangapi watakaoitikia unapowaambia kuhusu rehema ya Mungu na kuwaonyesha njia ya uzima. Tena, usisahau kwamba unahubiri kwa sababu Yehova anataka watu wapate uzima, nawe pia unataka.
8. Kwa nini inatia moyo kukumbuka jinsi wengine walivyoitikia rehema ya Mungu?
8 Unaweza kutiwa moyo ukikumbuka jambo hili: Sikuzote kumekuwa na watu fulani wanaokubali ujumbe wa Mungu. Ndiyo sababu Hosea aliwataja wale ambao walitambua kwamba “njia za Yehova zimenyooka.” Nabii huyo aliongeza hivi: “Waadilifu ndio watakaotembea katika hizo.” (Hosea 14:9) Miaka nenda miaka rudi, watu wengi wameitikia mwaliko huu wa Mungu: “Rudini kwangu kwa mioyo yenu yote.” (Yoeli 2:12) Mwaliko huo ulitolewa kwa watu waliomjua Yehova, lakini pia unaonyesha jinsi Mungu anavyowajali wale wanaojifunza kumhusu. Naam, Mungu hajakata tamaa kwa sababu anajua kwamba wanadamu wanaweza kujuta kwa sababu ya mwenendo wao mbaya wa zamani, kutubu, na kuanza kutenda mambo yanayofaa. Wanapofanya hivyo wanapata taraja la kuokoka.—1 Timotheo 4:16.
9. Itikio la Waninawi linaonyesha ni nini kinachohitajiwa?
9 Kuna jambo lingine lililomfanya Yehova awasamehe Waninawi. Tunasoma kwamba watu walichukua kwa uzito ujumbe wa hukumu ya Mungu iliyokuwa ikija, nao “wakaanza kumwamini Mungu.” (Yona 3:5) Wangeokolewa kwa sababu ya imani yao wala si kwa sababu ya kuogopa tu hukumu. Yehova anataka sana watu watubu na kutenda kwa imani, ndiyo sababu ameturuhusu kuwa wahubiri na kuwasaidia watu wafanye uamuzi. Matokeo ni nini? Tunasoma hivi kuwahusu Waninawi: “Mungu wa kweli akaona matendo yao, kwamba walikuwa wamegeuka kutoka katika njia yao mbaya; naye Mungu wa kweli akajuta juu ya msiba ambao alikuwa amesema ataleta juu yao; naye hakuuleta.” (Yona 3:10) Yehova hawezi kudanganywa kwa maneno tu au matendo yasiyo manyoofu. Lazima Waninawi wawe walitubu kikweli na kuonyesha hivyo kwa matendo yao. Mungu aliona kwamba walibadilika kikweli; walionyesha toba ya kweli inayoambatana na imani.
10. Taja baadhi ya pindi ambazo Yehova aliwaokoa watu.
10 Hatupaswi kamwe kukata kauli kwamba Waninawi peke yao ndio waliofaidika kutokana na nia ya Yehova ya kuokoa watu. Wakati wa uharibifu wa Yerusalemu mwaka wa 607 K.W.K.—baada ya huduma ya Obadia, Nahumu, na Habakuki—Yehova alimwokoa Yeremia aliyekuwa mtiifu pamoja na wenzake waliokuwa waaminifu. (Yeremia 39:16-18) Isitoshe, manabii wa Mungu walitabiri kwamba mabaki wenye kutubu wangerudi kutoka Babiloni na kurudisha ibada safi. (Mika 7:8-10; Sefania 3:10-20) Unabii huo umetimizwa kwa njia kubwa sana leo. Baada ya Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, Wakristo watiwa-mafuta walirudia utendaji wenye bidii na kupata kibali cha Yehova wakiwa na tumaini la kupata uzima. Wengi wao walikuwa wameacha kutenda katika ibada ya kweli. Leo pia, watu kutoka katika ‘mataifa mengi wanajiunga na Yehova.’ (Zekaria 2:11) Watu hao wanatumaini kuokoka mwisho unaokuja wa mfumo huu wa mambo. Kwa hiyo, unaposhiriki katika kazi ya kuhubiri hufanyi hivyo ili kuonyesha tu kwamba unatii amri ambayo Wakristo walipewa. Zaidi ya hayo, hatushiriki katika huduma hiyo ili kutimiza tu unabii. (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Unashiriki kazi ya kuhubiri ukiwa na lengo la kuwasaidia watu wajifunze kumhusu Yehova, waonyeshe imani, na kupata uzima.
WALE WANAOMRUDIA YEHOVA WATAPATA UZIMA
11, 12. Wale walioacha kumwabudu Mungu wanaweza kufaidikaje na rehema yake?
11 Yehova anapendezwa na wapya na anataka wapate uzima, hata hivyo, hawasahau wale ambao wamekuwa wakimtumikia. Sisi pia tunapaswa kupendezwa na watu hao na kuwasaidia waendelee kutembea katika barabara ya uzima. Tutawasaidiaje?
12 Labda unawajua watu fulani ambao walijifunza kumhusu Yehova, wakamwamini, na kuwa na bidii katika ibada ya kweli lakini sasa wameacha. Ujumbe ambao Yehova alitoa kupitia wale manabii 12 unaonyesha kwamba alikuwa tayari kuwarehemu wale ambao zamani walikuwa watu wake lakini wakaacha ibada ya kweli. Yuko tayari kufanya vivyo hivyo leo, iwe watu hao wamepeperuka, wamejiondoa, au wametenda dhambi na wanahitaji kutubu. (Waebrania 2:1; 3:12) Ijapokuwa huenda hawafurahii kuwa mbali na Yehova, huenda wanaona ugumu wa kurudi. Mungu anawasihi kama nabii wake anavyosema: “Yehova wa majeshi amesema hivi: ‘Rudini kwangu,’ asema Yehova wa majeshi, ‘nami nitarudi kwenu.’” (Zekaria 1:3) Maneno ya Hosea ni yenye kutia moyo sana! Anasema: “Ee Israeli, rudi kwa Yehova Mungu wako, kwa maana umejikwaa katika kosa lako. Chukueni maneno pamoja nanyi mrudi kwa Yehova. Mwambieni hivi, enyi nyote, ‘Samehe kosa letu; na ukubali lililo jema.’” Naam, hata wale waliotenda dhambi nzito wangeweza kusamehewa na kuponywa kabisa ikiwa wangemrudia Mungu na kutubu kikweli. (Hosea 6:1; 14:1, 2; Zaburi 103:8-10) Hivyo ndivyo ilivyokuwa katika siku za manabii, na ndivyo ilivyo leo.
Utawasaidiaje Wakristo waliokuwa na bidii zamani wamrudie Yehova?
13. Kwa nini tunapaswa kuwaonyesha rehema wale ambao wamesamehewa na Mungu?
13 Hata hivyo, hilo linamaanisha nini kwa Wakristo ambao wameendelea kutembea katika barabara ya uzima? Tutaonyeshaje kwamba tunawaona wengine kama Yehova anavyowaona? Yehova anatutazamia tuwaonyeshe rehema wapya na wale ambao huenda wameacha kumtumikia. Kupitia Hosea, Mungu alisema yale anayotaka kutoka kwetu: “Ninapendezwa na fadhili zenye upendo, na si dhabihu.” Yesu Kristo alieleza hivi wazo hilo: “Nendeni, basi, mkajifunze maana ya jambo hili, ‘Ninataka rehema, wala si dhabihu.’” (Hosea 6:6; Mathayo 9:13) Hatuwezi kuendelea kuwa na uhusiano pamoja na Mungu tusipoonyesha rehema. Ona jinsi mtume Paulo alivyohusianisha kusamehe na kumwiga Mungu: “Iweni wenye fadhili ninyi kwa ninyi, wenye huruma nyororo, mkisameheana kwa hiari kama vile Mungu pia kupitia Kristo alivyowasamehe ninyi kwa hiari. Kwa hiyo, iweni waigaji wa Mungu, kama watoto wapendwa, na endeleeni kutembea katika upendo.” (Waefeso 4:32–5:2) Unamwiga Mungu kwa kadiri gani katika kuonyesha sifa hiyo?
14, 15. Mtazamo wetu kuhusu msamaha wa Yehova unaweza kujaribiwa katika hali gani?
14 Namna gani ikiwa ndugu aliyetenda dhambi nzito alikosa kutubu na ikabidi atengwe na ushirika wa kutaniko? Ndivyo ilivyotukia katika karne ya kwanza. Wakristo ambao walitenda dhambi na kukosa kutubu walitengwa na ushirika. Ikiwa jambo hilo lilitukia mitume wa Yesu wakiwapo, haishangazi kwamba linatukia mara kwa mara leo. Katika visa hivyo, washiriki washikamanifu kutanikoni hukubali mwongozo wa Biblia wa kutoshirikiana na mtu aliyetengwa na ushirika. Ushikamanifu wao kwa Yehova unaweza kumsaidia mkosaji huyo kuona ubaya wa mwenendo wake usiofaa, na hilo laweza kumsukuma atubu. Tunasoma katika Biblia kwamba mtu fulani huko Korintho aliyetengwa na ushirika, alirudishwa kutanikoni baada ya kutubu na kugeuka. (1 Wakorintho 5:11-13; 2 Wakorintho 2:5-8) Mtu anaporudishwa leo, wewe huhisije, na utaonyeshaje kwamba ungependa wengine pia wapate uzima?
15 Mkosaji mwenye kutubu anaweza kuaibika na kuhitaji sana kuhakikishiwa kwamba Mungu na ndugu zake wanampenda na wanataka apate uzima. Ona jinsi Mungu alivyowahakikishia kwa upendo watu wake wa kale ambao walikuwa na nia ya kutubu: “Nitakuchumbia uwe wangu katika uaminifu; nawe hakika utamjua Yehova.” (Hosea 2:20) Kwa kuwa Mungu anahisi hivyo, tunapaswa kuonyesha kwamba tunahisi kama Mungu ambaye anatajwa na Zekaria kuwa Mungu ‘anayeonyesha rehema.’—Zekaria 10:6.
16. Tunapaswa kuhisije mtu anaporudishwa?
16 Mungu anataka watu wapate uzima, kwa hiyo anafurahi wakati mtenda-dhambi anapotubu au mtumishi wake aliyekuwa ameacha kuwa mtendaji anaporudia bidii yake.a (Luka 5:32) Kuhusu yule Mkorintho aliyerudishwa ambaye ametajwa awali, Paulo aliwahimiza washiriki wa kutaniko wamsamehe na kumtia moyo, na kumhakikishia kwamba walimpenda kikweli: “Kemeo hili linalotolewa na walio wengi linamtosha mtu wa namna hiyo, . . . mnapaswa kumsamehe kwa fadhili na kumfariji, ili kwa njia fulani mtu huyo asimezwe na huzuni yake ya kupita kiasi. Kwa hiyo nawahimiza ninyi kumthibitishia upendo wenu.” (2 Wakorintho 2:6-8) Kumbuka kwamba Hosea alimnukuu Yehova akisema hivi kuhusu wale waliokuwa wakitenda dhambi awali: “Nitaponya ukosefu wao wa uaminifu. Nitawapenda kwa kupenda kwangu mwenyewe.” (Hosea 14:4) Je, tutamwiga Yehova, na kufurahi kuwasaidia watu hao kupona ili wapate uzima wa milele?
17, 18. Tunaweza kuwasaidiaje kwa upendo wale ambao wamemrudia Yehova au washiriki wa familia ya mtu aliyetengwa na ushirika?
17 Yehova anaeleza wazi kwamba yeye huwatendea kwa heshima wale wanaorudi, huwakubali na kuwaonyesha upendo wake wote, kama tu Hosea alivyomkaribisha kwa moyo wote mke wake aliyekuwa amekosa uaminifu. Yehova anasema jinsi alivyowatendea watumishi wake: “Nikawa kwao kama wale wanaoondoa nira kwenye mfupa wa mataya yao, nami kwa upole nikamletea kila mmoja wao chakula.” (Hosea 11:4) Yehova huwavuta watu hao wanaomrudia kwa upendo mwingi wenye kuchangamsha moyo! Tunaweza kumwiga kwa kutomwepuka au kutomwonyesha ubaridi mtu ambaye ameonyesha huzuni ya kimungu na kutubu kikweli. Mara tu anaporudishwa kutanikoni, tunapaswa kumfariji ipasavyo badala ya kumfungia kinyongo au kumkasirikia kwa sababu ya makosa aliyotenda zamani.—1 Wathesalonike 5:14.
18 Je, unaweza kufikiria njia nyingine unazoweza kumwiga Yehova wakati mtu anapotengwa na ushirika wa kutaniko? Ikiwa mtu fulani ametengwa na ushirika, je, tunaweza kuwasaidia washiriki wa familia yake ambao ni washikamanifu, labda mwenzi wake ambaye ni mwaminifu kwa Yehova pamoja na watoto wake? Labda wanajitahidi sana kuendelea kuhudhuria mikutano na kushiriki katika huduma. Je, tutawapa utegemezo wa pekee ambao huenda wanahitaji? Njia nyingine ya kuonyesha rehema nyororo ni kutumia “maneno mema, maneno yenye kufariji,” na kuwatia moyo waaminifu hao. (Zekaria 1:13) Kuna nafasi nyingi za kufanya hivyo kabla na baada ya mikutano, katika huduma, au nyakati nyingine. Wao ni wafanyakazi wenzetu, washiriki wapendwa wa kutaniko letu ambao hawapaswi kuepukwa wala kuachwa peke yao. Nyakati nyingine, watoto wa mzazi aliyetengwa na ushirika hujitahidi peke yao kumtumikia Yehova. Kwa kweli tunataka wapate uzima. Tutaonyeshaje hivyo?
“MVULANA ASIYE NA BABA HUONYESHWA REHEMA”
19. Sefania alimsaidiaje kiroho yule aliyekuwa kama “mvulana asiye na baba”?
19 Huduma ya Sefania aliyetumika katikati ya karne ya saba K.W.K., hutuwekea kielelezo katika kuwasaidia wengine. Inaelekea kwamba alikuwa mzao wa familia ya kifalme ya Yuda, labda binamu wa mbali wa Mfalme Yosia. Baba ya mfalme huyo alikuwa ameuawa, na hivyo Yosia akalazimika kuwa mfalme akiwa na umri wa miaka minane. Alikabili tatizo gumu sana: Taifa hilo lilikuwa limetumbukia katika ibada ya sanamu na mazoea yenye kuchukiza. (Sefania 3:1-7) Kijana mchanga Yosia, ambaye hakuwa na baba alihitaji mwongozo stadi na mashauri yenye kutegemeka ili atawale taifa hilo lenye kuasi. Yehova aliandaa mwongozo wa hekima kupitia Yeremia na Sefania, kama ilivyotajwa katika Sura ya 3 na ya 5 ya kitabu hiki. Ingawa Yehova alimtumia nabii wake kuwashutumu “wana wa mfalme” wa Yuda, Hakumshutumu mfalme mwenyewe. (Sefania 1:8; 3:3) Huenda hilo linaonyesha kwamba Mfalme Yosia aliyekuwa kijana alikuwa tayari ameonyesha nia ya kufuata ibada safi. Bila shaka, himizo la nabii huyo lilimsaidia Yosia kuimarisha azimio lake la kuondoa kabisa ibada isiyo safi katika Yuda.
20. Kuwaongoza kiroho wale “wasio na baba” kutanikoni kunaweza kuwasaidiaje?
20 Kama vile Sefania alivyopendezwa na Yosia, ndivyo Yehova anavyopendezwa na wachanga wanaohitaji kutunzwa kama vile watoto ambao wazazi wao wametengwa na ushirika. Hosea alitangaza hivi: “Ni kupitia [Mungu] kwamba mvulana asiye na baba huonyeshwa rehema.” (Hosea 14:3) Je, unamjua mvulana na msichana mwingine yeyote “asiye na baba” ambaye anahitaji mtu wa kumwongoza katika mambo ya kiroho na maishani? Huenda wakawa mayatima wa kiroho, watoto wa familia zenye mzazi mmoja, au watoto ambao wanamtumikia Yehova bila kuungwa mkono na familia zao. Mara nyingi, watoto hao wanapokuwa na mtu wa kuwaongoza kiroho wanashirikiana kwa ukaribu na kutaniko na kukomaa kiroho. Lakini wanapokosa mtu wa kuwaongoza, hali yao inaathiriwa. ‘Wavulana wengi wasio na baba’ wamefanya maendeleo na kuwa watu wakomavu kiroho na wenye usawaziko baada ya kuonyeshwa upendo na Wakristo wakomavu kutanikoni.—Zaburi 82:3.
Je, unaweza kuwaongoza kwa upendo wale ‘wasio na baba’ katika mambo ya kiroho?
21. Wakristo wakomavu wanaweza kuwasaidiaje watoto?
21 Kwa mfano, Wakristo wakomavu wanaweza kumsaidia mama asiye na mume kwa kupendezwa na watoto wake. (Yakobo 1:27) Wazee na wengine wanaweza kuwategemeza kiroho washiriki wa familia zenye uhitaji huku wakiheshimu ukichwa na kujiendesha ifaavyo. Wewe na mwenzi wako wa ndoa au na familia yako mnaweza kumwalika mvulana au msichana asiye na baba. Je, unaweza kuwatendea kwa fadhili watoto ambao huenda ni wapweke? Huenda wakahitaji mtu awahurumie na kuzungumza nao faraghani, na unaweza kufanya hivyo unaposhiriki nao katika huduma. Bila shaka wewe ni mtu mwenye shughuli nyingi, kwa hiyo kumsaidia mtoto fulani kwa ukawaida na kwa muda mrefu kwaweza ‘kuujaribu uhalisi wa upendo wako.’ (2 Wakorintho 8:8) Jitihada zako zitaonyesha kwamba unataka wengine wapate uzima.
22. Unahisije unapoona jinsi Yehova anavyotaka wengine wapate uzima?
22 Inatia moyo kama nini kuona jinsi Mungu anavyopendezwa na watu, na jinsi anavyotaka wapate uzima wa milele! Kwa maoni yake, ni afadhali awaonyeshe upendo watu waadilifu wanaompenda na kuwapa uzima badala ya kuonyesha chuki yake kuelekea wale wanaoamua kutobadilika na wasiostahili uzima wa milele. Tunapongoja kwa hamu siku ya Yehova, na tumwige kwa kuwasaidia wengine watembee katika barabara ya uzima.
a Mifano mitatu yenye kugusa moyo inaonyesha jinsi Mungu anavyowahangaikia sana watu wake waliopotea—mfano wa kondoo aliyepotea, sarafu iliyopotea, na mwana mpotevu.—Luka 15:2-32.
-
-
‘Endeleeni Kuitarajia’ Siku ya YehovaIzingatie Siku ya Yehova Maishani
-
-
SURA YA KUMI NA MBILI
‘Endeleeni Kuitarajia’ Siku ya Yehova
1, 2. (a) Ni maswali gani unayoweza kujiuliza? (b) Baadhi ya wale manabii 12 waliishi katika hali gani, naye Mika alikuwa na mtazamo gani?
UMEKUWA ukingoja kwa muda gani siku ya Yehova iondolee mbali uovu ulio duniani? Utaingoja hadi wakati gani? Ni mtazamo gani utakaokuwa nao, na utaathirije maisha yako? Ni wazi kwamba, majibu yako ni tofauti na maoni ya wafuasi wa dini ambao huishi wapendavyo, wakisubiri kwenda mbinguni.
2 Unapoingojea ile siku kuu, vitabu vilivyoandikwa na wale manabii 12 vyaweza kukusaidia sana. Wengi kati ya manabii hao waliishi wakati ambapo hukumu ya Mungu ilikuwa ikikaribia. Kwa mfano, Mika aliishi wakati ambapo Samaria lilikuwa likikaribia kuharibiwa na Waashuru mwaka wa 740 K.W.K. (Ona chati iliyo katika ukurasa wa 20 na 21.) Baadaye, siku ya Yehova dhidi ya Yuda pia haikuwa na budi kufika. Kwa kuwa Mika hakujua siku hususa ambayo Mungu angechukua hatua, je, aliamua kukaa kitako na kusubiri, akitumaini kwamba muda si muda Mungu atachukua hatua? Mika alisema hivi: “Mimi, nitaendelea kumtazamia Yehova. Nitaonyesha mtazamo wa kumngojea Mungu wa wokovu wangu. Mungu wangu atanisikia.” (Mika 7:7) Naam, akiwa na uhakika wa mambo ambayo yangetokea, Mika alikuwa kama mlinzi aliye chonjo kwenye mnara.—2 Samweli 18:24-27; Mika 1:3, 4.
Sefania
3. Uharibifu wa Yerusalemu ulipokuwa ukikaribia, Habakuki na Sefania walikuwa na mtazamo gani?
3 Kisha, itazame chati tena, uone wakati ambapo Sefania na Habakuki waliishi. Ona kwamba manabii hao wawili waliishi karibu sana na uharibifu wa Yerusalemu uliotokea mwaka wa 607 K.W.K. Hata hivyo, hawangeweza kujua ikiwa hukumu ya Mungu ilikuwa karibu sana au ingetekelezwa makumi ya miaka wakati ujao. (Habakuki 1:2; Sefania 1:7, 14-18) Sefania aliandika hivi: “‘Kwa hiyo endeleeni kunitarajia,’ asema Yehova, ‘mpaka siku nitakaposimama kwenda kuteka nyara, kwa maana uamuzi wangu wa hukumu ni . . . kuzimwagia [falme] shutuma yangu, hasira yangu yote yenye kuwaka.’” (Sefania 3:8) Namna gani Habakuki, aliyeishi muda mfupi baada ya Sefania? Habakuki aliandika: “Maono hayo bado ni ya wakati uliowekwa, nayo yanafanya haraka kuelekea mwisho, wala hayatasema uwongo. Hata yakikawia, endelea kuyatarajia; kwa maana bila shaka yatatimia. Hayatachelewa.”—Habakuki 2:3.
4. Sefania na Habakuki walitoa unabii chini ya hali gani, nao walikuwa na mtazamo gani?
4 Muktadha wa ujumbe ulio katika Sefania 3:8 na Habakuki 2:3 unaweza kutusaidia kuelewa mengi zaidi. Wakati ambapo Wayahudi fulani walikuwa wakisema, “Yehova hatatenda mema, wala hatatenda mabaya,” Sefania alitangaza “siku ya hasira ya Yehova.” Siku hiyo, mataifa adui pamoja na Wayahudi wapotovu wangekabili hasira ya Yehova. (Sefania 1:4, 12; 2:2, 4, 13; 3:3, 4) Je, unafikiri kwamba Sefania aliogopa shutuma na hasira ya Mungu? Hapana, badala yake alipaswa ‘kuendelea kuitarajia’ siku ya Yehova. Huenda ukajiuliza: ‘Namna gani Habakuki?’ Yeye pia alipaswa ‘kuendelea kuitarajia’ siku hiyo. Sefania na Habakuki hawakuchukua mambo vivi hivi tu, wala hawakuendelea na shughuli zao kana kwamba walifikiri kuwa mambo hayangebadilika. (Habakuki 3:16; 2 Petro 3:4) Hata hivyo, kama tulivyojifunza, kuna jambo kuu ambalo manabii hao wawili walipaswa kufanya: Wote wawili walipaswa ‘kuendelea kutarajia.’ Nasi leo twajua hili: Jambo ambalo manabii hao wawili walikuwa wakitarajia lilitimia hakika mwaka wa 607 K.W.K. Kwa hiyo, walitenda kwa hekima kwa kuendelea ‘kutarajia.’
“‘Endeleeni kunitarajia,’ asema Yehova.”—Sefania 3:8
5, 6. Tunapozingatia makusudi ya Mungu yanayotimizwa leo, tunapaswa kuwa na mtazamo gani?
5 Wewe pia unaweza kuwa na hakika kwamba “siku ya hasira ya Yehova” dhidi ya ulimwengu huu itakuja; itatimia hakika. Bila shaka, huna shaka yoyote kuhusu hilo. Kama Sefania na Habakuki, hujui wakati hususa ambayo siku hiyo itafika. (Marko 13:32) Hata hivyo, haitakosa kuja, na unabii wa Biblia unaotimizwa leo unathibitisha kwamba itakuja hivi karibuni. Kwa hiyo, jambo ambalo Yehova alikazia akilini mwa manabii hao linakuhusu wewe pia—‘Endelea kuitarajia.’ Kumbuka jambo hili hakika: Mungu wetu ndiye Mungu pekee ‘anayetenda kwa ajili ya mtu anayeendelea kumtarajia.’—Isaya 64:4.
6 Unaweza kuonyesha mtazamo unaofaa wa kuitarajia siku hiyo na kuthibitisha kupitia matendo yako kwamba una hakika “siku ya hasira ya Yehova” itakuja wakati barabara uliowekwa. Ukiwa na usadikisho huo na kuonyesha hivyo kwa matendo, utakuwa ukitii jambo fulani ambalo Yesu alisema. Aliwahimiza hivi mitume wake na Wakristo wote watiwa-mafuta: “Viuno vyenu na vifungwe mishipi na taa zenu ziwe zikiwaka, nanyi mtakuwa kama watu wanaomngoja bwana wao . . . Wenye furaha ni watumwa ambao bwana anapofika anawakuta wakikesha! Kwa kweli ninawaambia ninyi, Yeye atajifunga na kuwaketisha mezani naye atakuja kando na kuwahudumia.” (Luka 12:35-37) Naam, mtazamo unaofaa wa kungoja huonyesha tuna hakika kwamba siku kuu ya Yehova haitachelewa hata kidogo.
‘KUTARAJIA’ NA ‘KUWA TAYARI’
7, 8. (a) Subira ya Mungu imekuwa na matokeo gani? (b) Petro anatuhimiza tuwe na mtazamo gani?
7 Watumishi wa Mungu wa nyakati zetu walikuwa wakiitarajia siku ya Yehova kabla ya Ufalme wa Mungu kusimamishwa mbinguni mwaka wa 1914 nao wameendelea kuitarajia tangu wakati huo. Bila shaka hawaitarajii siku hiyo kwa kuketi kitako tu. Badala yake, wamekuwa wakifanya kwa bidii kazi ya kuhubiri waliyopewa na Mungu. (Matendo 1:8) Hebu fikiria hili: Ikiwa siku kuu ya Yehova ingekuja mwaka wa 1914, hali yako ingekuwaje? Hata ikiwa ingekuja miaka 40 iliyopita, je, wakati huo ulikuwa mtu mwenye “matendo matakatifu ya mwenendo na vitendo vya ujitoaji-kimungu”? (2 Petro 3:11) Namna gani washiriki wa familia yenu ambao sasa ni Mashahidi au rafiki zako wa karibu sana kutanikoni? Bila shaka, kipindi hiki cha kuitarajia siku hiyo kimekuwezesha wewe na wengine wengi kama wewe kuipata njia ya wokovu, kama andiko la 2 Petro 3:9 linavyoonyesha. Kwa kuwa Yehova hakuharibu ulimwengu wote mwovu mara tu Ufalme uliposimamishwa, watu wengi wamepata nafasi ya kutubu, kama vile Waninawi walivyotubu na kuhifadhiwa. Sisi sote tuna sababu za kukubaliana na maneno haya ya mtume Petro: “Ioneni subira ya Bwana wetu kuwa wokovu.” (2 Petro 3:15) Wakati uliopo unaendelea kuwapa watu nafasi ya kutubu na kurekebisha maisha na maoni yao.
8 Ni kweli kwamba huenda Mkristo akadhani kwamba matukio ya siku za Mika, Sefania, na Habakuki hayamhusu. Huenda akasema: “Huo ni muda mrefu uliopita!” Hata hivyo, tunaweza kujifunza nini kutokana na habari hiyo? Tayari tumetaja shauri la Petro kwamba Wakristo wanapaswa kuwa watu wenye “matendo matakatifu ya mwenendo na vitendo vya ujitoaji-kimungu.” Mara tu baada ya kutaja maneno hayo, Petro anakazia jambo lingine tunalohitaji kufanya—kwamba tunapaswa ‘kungojea na kuweka karibu akilini kuwapo kwa siku ya Yehova.’ (2 Petro 3:11, 12) Kwa hiyo, tunapaswa “kuweka karibu akilini” siku hiyo, na kuendelea ‘kuitarajia.’
9. Kwa nini tunapaswa ‘kuendelea kuitazamia’ siku ya Yehova?
9 Iwe tumekuwa tukimtumikia Yehova kwa miaka michache au makumi ya miaka, je, ‘tunaendelea kutazamia na kuonyesha mtazamo wa kungojea’ kama Mika alivyofanya? (Waroma 13:11) Kwa kuwa sisi ni wanadamu, huenda tukatamani kujua siku hususa ambayo mwisho utakuja na muda unaobaki. Hata hivyo, hatuwezi kujua. Kumbuka maneno ya Yesu: “Ikiwa mwenye nyumba angalijua mwizi anakuja katika kesha gani, angaliendelea kukaa macho na hangaliruhusu nyumba yake ivunjwe. Kwa hiyo ninyi pia iweni tayari, kwa sababu Mwana wa binadamu atakuja katika saa msiyofikiria.”—Mathayo 24:43, 44.
10. Unajifunza nini kutokana na maisha na mtazamo wa mtume Yohana?
10 Maneno ambayo Yesu alisema yanalingana sana na mambo ambayo yaliandikwa na Mika, Sefania, na Habakuki. Hata hivyo, Yesu hakuwa akiwashauri watu wa nyakati za kale, bali alikuwa akiwashauri wafuasi wake, yaani, sisi. Wakristo wengi waaminifu wametii kabisa shauri la Yesu; ‘wako tayari,’ huku wakiendelea kuitarajia siku hiyo. Mtume Yohana alikuwa mfano mzuri. Alikuwa mmoja kati ya wale wanne waliokuwa katika Mlima wa Mizeituni ambao walimuuliza Yesu kuhusu umalizio wa mfumo wa mambo. (Mathayo 24:3; Marko 13:3, 4) Huo ulikuwa mwaka wa 33 W.K., lakini Yohana hangeweza kutazama chati yoyote na kuona mambo yangetokea upesi kadiri gani. Sasa, akilini mwako, songa mbele miaka 60. Yohana tayari amezeeka, hata hivyo, hajachoka wala kuacha kuitarajia siku ya Yehova. Badala yake, alipomsikia Yesu akisema: “Ndiyo; mimi ninakuja upesi,” Yohana aliitikia: “Amina! Njoo, Bwana Yesu.” Yohana hakujuta jinsi alivyokuwa ametumia maisha yake. Alikuwa na hakika kwamba Yehova atakapotekeleza hukumu, Angempa thawabu kila mmoja kulingana na matendo yake. (Ufunuo 22:12, 20) Hata iwe hukumu hiyo ingekuja wakati gani, Yohana alitaka kuwa “tayari,” kama vile Bwana Yesu alivyokuwa ameagiza. Je, hivyo ndivyo unavyohisi?
JE, ‘UNAITARAJIA’ SIKU YA YEHOVA AU ‘UMESHIBA’?
11. Watu wa siku za Mika na Hosea walikuwaje tofauti na manabii hao?
11 Fikiria jambo lingine tunaloweza kujifunza kutokana na manabii walioishi wakati ambapo hukumu za Yehova zilikuwa karibu kutekelezwa, kwanza dhidi ya Israeli, kisha dhidi ya Yuda. Ingawa Mika ‘aliendelea kutazamia na kuonyesha mtazamo wa kungoja,’ wengi walioishi wakati huo hawakufanya hivyo. ‘Walichukia mema na kupenda mabaya.’ Mika alionya kwamba ikiwa hawangebadilika, ‘wangemwomba Yehova msaada, lakini hangewajibu.’ (Mika 3:2, 4; 7:7) Hosea aliyeishi wakati mmoja na Mika alitumia maneno yaliyohusiana na ukulima alipokuwa akiwahimiza watu wa ufalme wa kaskazini wa Israeli: “Mjipandie mbegu kwa uadilifu; mvune kulingana na fadhili zenye upendo. Mjilimie udongo unaofaa kwa kilimo, kukiwa kungali na wakati wa kumtafuta Yehova.” Licha ya hayo, wengine hawakusikiliza. Walilima “uovu,” nao wakavuna ukosefu wa uadilifu. (Hosea 10:12, 13) Walivumilia au kushiriki katika matendo ya ufisadi, ‘wakitumainia njia zao wenyewe’ badala ya njia za Yehova. Huenda wengine leo wakajiuliza, ‘Hilo lingewezaje kuwapata waabudu wa kweli waliokuwa wakiishi katika Nchi Iliyoahidiwa?’ Hosea alionyesha kwamba tatizo lao hasa lilikuwa mtazamo wao ambao ulikuwa kama mtazamo tunaohitaji kujihadhari nao ili kuendelea kuitarajia siku kuu ya Yehova. Yaani, mtazamo wa kuridhika na ‘kushiba.’
12. (a) Hosea alitaja jambo gani lisilopendeza kuhusu Waisraeli kabla ya mwaka wa 740 K.W.K.? (b) Ni mambo gani yanayoonyesha kwamba watu hao ‘walishiba’?
12 Baada ya watu wa Mungu kuingia katika Nchi Iliyoahidiwa, nchi inayotiririka maziwa na asali, walipata ufanisi mkubwa. Waliitikiaje? Hosea alitangaza maneno haya ya Yehova: “Pia wakashiba kulingana na malisho yao. Walishiba, kisha moyo wao ukaanza kujiinua. Ndiyo sababu walinisahau mimi.” (Hosea 13:6) Karne kadhaa mapema, Mungu aliwaonya watu wake kuhusu hatari hiyo. (Kumbukumbu la Torati 8:11-14; 32:15) Hata hivyo, kufikia siku za Hosea na Amosi, Waisraeli walimsahau Yehova na amri zake—“walishiba.” Amosi anatueleza mambo hususa. Anasema kwamba wengi walikuwa na mali za starehe katika nyumba zao, na familia fulani hata zilikuwa na nyumba zaidi ya moja. Walikuwa na chakula bora, walikunywa divai kwa vyombo bora, na kujipaka ‘mafuta yaliyo bora kabisa,’ huenda hata yenye manukato. (Amosi 3:12, 15; 6:4-6) Labda umeona kwamba hakuna lolote kati ya mambo hayo ambalo ni baya, hata hivyo, ni wazi kwamba si vizuri kuyaona kuwa muhimu kupita kiasi.
13. Waisraeli, matajiri kwa maskini, walikuwa na tatizo gani?
13 Ni kweli kwamba si wote katika ufalme wa kaskazini walipata ufanisi na ‘kushiba.’ Baadhi yao walikuwa maskini na walilazimika kutafuta riziki ili walishe familia zao. (Amosi 2:6; 4:1; 8:4-6) Ndivyo ilivyo leo pia katika sehemu nyingi za dunia. Je, shauri la Mungu lililo katika Hosea 13:6 liliwahusu pia maskini waliokuwa katika Israeli la kale, na je, linatuhusu leo? Bila shaka, ndiyo. Yehova alikuwa akionyesha kwamba hata iwe mwabudu wa kweli ni tajiri au la, anahitaji kujihadhari asije akakazia fikira zake zote mambo ya kimwili hivi kwamba ‘amsahau Mungu.’—Luka 12:22-30.
14. Kwa nini inafaa kwetu kuchanganua iwapo bado tunaitarajia siku ya Yehova?
14 Leo, kwa kuwa tunaweza kuona yaliyotukia huko nyuma, na kuna unabii mwingi sana wa Biblia uliotimizwa, tuna kila sababu ya kuwa macho, kuwa tayari, na kuendelea kuitarajia siku ya Yehova. Hata hivyo, namna gani ikiwa tumekuwa tukiitarajia siku ya Yehova kwa muda fulani sasa, labda hata kwa makumi ya miaka? Wakati uliopita tulijikakamua katika huduma na kufanya maamuzi ya kibinafsi yaliyoonyesha tunasadiki kwamba siku ya Yehova haiko mbali. Lakini bado haijaja. Je, bado tunaitarajia? Unaweza kujiuliza, ‘Je, bado mimi ninaitarajia sana siku hiyo, au nimeanza kuona kwamba haitakuja karibuni?’—Ufunuo 2:4.
15. Ni dalili gani zinazoweza kuonyesha ikiwa tumeanza kuacha kuitarajia siku ya Yehova?
15 Kuna mambo mbalimbali yanayoweza kuonyesha ikiwa tunaitarajia siku ya Yehova. Acheni tuchanganue mambo yanayotajwa na Amosi anapowafafanua watu wa siku yake waliokuwa ‘wameshiba.’ Tunapofanya hivyo, tunaweza kujichunguza tuone iwapo kuna dalili zozote zinazoonyesha kwamba ‘tumeshiba.’ Mkristo ambaye awali alionyesha kupitia maoni na matendo yake kwamba anaitarajia siku ya Yehova huenda akaanza kutafuta nyumba au gari la kifahari zaidi, mitindo ya karibuni zaidi ya mavazi, mapambo na vito ghali, au divai bora na vyakula vya bei. Biblia haisemi popote kwamba tujitese wenyewe, au kujinyima raha za kiasi maishani. Mtu ambaye hufanya kazi kwa bidii anapaswa “ale, naam, anywe na kuona mema kwa ajili ya kazi yake yote iliyo ngumu.” (Mhubiri 3:13) Hata hivyo, kuna hatari iwapo Mkristo atakazia fikira zake zote chakula, vinywaji, na sura yake mwenyewe. (1 Petro 3:3) Yesu alitaja kwamba watiwa-mafuta fulani huko Asia Ndogo walipoteza usawaziko wao. Hilo linaonyesha hatari inayowakabili Wakristo wote. (Ufunuo 3:14-17) Je, ndivyo ilivyo leo? Je, tumeanza ‘kushiba,’ labda kwa kuwa na shughuli nyingi za kutafuta vitu vya kimwili? Je, tumeanza kuacha kuitarajia siku ya Yehova?—Waroma 8:5-8.
16. Kwa nini haingefaa kuwahimiza watoto watafute maisha ‘yenye kushibisha’?
16 Mashauri tunayowapa watoto wetu na wengine yanaweza kuonyesha iwapo bidii yetu ya kuitarajia siku kuu ya Yehova imeanza kufifia. Mkristo anaweza kufikiri hivi: ‘Niliamua kutofuatia elimu au kazi fulani kwa kuwa nilidhani kwamba mwisho ulikuwa karibu sana. Sasa nataka kuhakikisha kwamba watoto wangu wamepata elimu itakayowawezesha kuwa na maisha mazuri wakati ujao.’ Huenda watu fulani walioishi siku za Hosea walikuwa na maoni kama hayo. Ikiwa ndivyo, je, kuwashauri watoto wao wawe na maisha ‘yenye kushibisha’ kungewafaidi watoto hao? Isitoshe, ikiwa watoto wa siku hizo walifanya kila wawezalo ili kuwa na maisha hayo ‘yenye kushibisha,’ au yenye kustarehesha, hali yao ingekuwaje mwaka wa 740 K.W.K., wakati ambapo Samaria liliharibiwa na Waashuru?—Hosea 13:16; Sefania 1:12, 13.
Unawatia moyo watoto wako wafuatie maisha ya aina gani wakati ujao?
UWE NA HAKIKA KWAMBA SIKU YA YEHOVA ITAKUJA
17. Tunapaswa kumwiga Mika katika njia gani?
17 Kama waabudu wa kweli wa kale, sisi pia tunaweza kuwa na hakika kwamba ahadi za Mungu zitatimia wakati wake barabara uliowekwa. (Yoshua 23:14) Nabii Mika alitenda kwa hekima kwa kumngojea Mungu wa wokovu wake. Leo, tunapochunguza historia, tunaona kwamba Mika aliishi karibu sana na wakati ambapo Samaria liliharibiwa. Namna gani sisi leo na wakati tunaoishi? Tutakapotafakari maisha yetu, je, tutaona wazi kwamba tulifanya maamuzi yanayofaa, kama vile maamuzi yanayohusu kazi ya kimwili, maisha, na huduma ya wakati wote? Kwa kweli hatujui “siku wala saa.” (Mathayo 24:36-42) Hata hivyo, hakuna shaka yoyote kwamba tutakuwa tukitenda kwa hekima iwapo tutasitawisha mtazamo kama ule wa Mika na kutenda kupatana nao. Mika atakapopata thawabu ya uzima katika paradiso duniani, atakuwa na furaha iliyoje kujua kwamba sisi tumefaidika kutokana na ujumbe wake wa kinabii pamoja na kielelezo chake cha uaminifu! Kuwapo kwetu wakati huo kutakuwa uthibitisho wa kwamba Yehova ndiye Mungu wa wokovu!
18, 19. (a) Obadia alitabiri msiba gani? (b) Obadia aliwapa Waisraeli tumaini jinsi gani?
18 Uhakika wetu una msingi thabiti. Kwa mfano, hebu fikiria kile kitabu kifupi cha kinabii cha Obadia. Kilizungumzia hasa mambo yaliyotokea Edomu la kale, kikitaja hukumu za Yehova dhidi ya watu hao waliomtendea vibaya “ndugu” yao, Israeli. (Obadia 12) Uharibifu uliotabiriwa ulitimia, kama tulivyozungumzia katika Sura ya 10 ya kitabu hiki. Wababiloni wakiongozwa na Nabonido walishinda Edomu katikati ya karne ya sita K.W.K., na taifa la Edomu likakoma kuwako. Hata hivyo, kuna wazo lingine muhimu katika ujumbe wa Obadia, wazo linalohusiana na kuendelea kwetu kuitarajia siku kuu ya Yehova.
19 Babiloni, taifa adui lililoharibu Edomu lilitekeleza pia adhabu ya Mungu dhidi ya watu wasio waaminifu. Mwaka wa 607 K.W.K., Wababiloni waliharibu Yerusalemu na kuwapeleka Wayahudi uhamishoni. Nchi ikawa ukiwa. Je, mambo yalikomea hapo? Hapana. Kupitia Obadia, Yehova alitabiri kwamba Waisraeli wangeimiliki tena nchi yao. Ahadi hii yenye kutia moyo inapatikana katika Obadia 17: “Katika Mlima Sayuni ndipo watakapokuwa wale wanaoponyoka, nao utakuwa kitu kitakatifu; na nyumba ya Yakobo itamiliki mali yao.”
20, 21. Kwa nini andiko la Obadia 17 lapaswa kutufariji?
20 Historia inathibitisha kwamba mambo ambayo Yehova alisema kupitia Obadia yalitokea. Mungu alitabiri, nayo yakatimia. Maelfu ya watu waliohamishwa kutoka Yuda na Israeli walirudi mwaka wa 537 K.W.K. Kwa msaada wa Yehova, waliorudi nyumbani kwao walibadili nchi hiyo iliyokuwa ukiwa ikawa paradiso yenye kusitawi. Unabii kuhusu badiliko hilo la ajabu unapatikana katika Isaya 11:6-9 na 35:1-7. Jambo muhimu ni kwamba ibada ya kweli ilianzishwa tena, kituo chake kikiwa hekalu la Yehova lililojengwa upya. Kwa hiyo, andiko la Obadia 17 linathibitisha pia kwamba ahadi za Yehova zinategemeka. Sikuzote hutimia.
21 Obadia alimalizia unabii wake kwa maneno haya yenye mkazo: “Lazima ufalme utakuwa wa Yehova.” (Obadia 21) Kwa kuwa tunaiamini ahadi hiyo, tunaungojea wakati mtukufu ambapo Yehova, kupitia Yesu Kristo atatawala pasipo upinzani wowote katika ulimwengu mzima, kutia ndani na dunia yetu. Iwe tumekuwa tukiitarajia siku kuu ya Yehova pamoja na baraka zitakazoletwa na siku hiyo kwa muda mfupi au kwa makumi ya miaka, tunaweza kuwa na hakika kabisa kwamba matarajio hayo yanayotegemea Biblia bila shaka yatatimia.
Tunamtumikia Yehova kwa shangwe tukitazamia uzima wa milele
22. Kwa nini ungependa maoni yako yapatane na yale ya Habakuki 2:3 na Mika 4:5?
22 Basi, inafaa kujikumbusha tena uhakikisho wa Habakuki, ambao bila shaka unahusu siku zetu pia: “Maono hayo bado ni ya wakati uliowekwa, nayo yanafanya haraka kuelekea mwisho, wala hayatasema uwongo. Hata yakikawia, endelea kuyatarajia; kwa maana bila shaka yatatimia. Hayatachelewa.” (Habakuki 2:3) Hata ikiwa kwa maoni ya mwanadamu huenda ikaonekana kwamba siku kuu ya Yehova inakawia, siku yake itakuja wakati barabara uliopangiwa. Yehova ametuahidi hilo. Basi, wale ambao wamemtumikia Mungu kwa muda mrefu na wale ambao wamejiunga na ibada yake karibuni wanaweza kusonga mbele pamoja wakiwa na uhakika kama ule unaotajwa katika Mika 4:5: “Sisi tutatembea katika jina la Yehova Mungu wetu mpaka wakati usio na kipimo, naam, milele.”
-
-
“Tangazeni Mambo Haya Kati ya Mataifa”Izingatie Siku ya Yehova Maishani
-
-
SURA YA KUMI NA TATU
“Tangazeni Mambo Haya Kati ya Mataifa”
Ungetendaje ikiwa ungemsikia simba akinguruma?
1. Kwa nini twaweza kusema kwamba Yehova anaposema na nabii wake ni kama simba anaponguruma?
JE, UMEWAHI kumsikia simba akinguruma? Simba hunguruma kwa sauti yenye kuogopesha sana. Mngurumo wake unaweza kusikika umbali wa kilometa nane hivi. Ungefanya nini ikiwa usiku fulani mtulivu ungemsikia simba akinguruma karibu nawe? Huenda ungechukua hatua mara moja. Amosi, mmoja wa wale manabii 12 ambao tunachunguza maandishi yao, alitumia mfano huu: “Kuna simba ambaye amenguruma! Ni nani hataogopa? Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova mwenyewe amesema! Ni nani ambaye hatatoa unabii?” (Amosi 3:3-8) Ikiwa ungemsikia Yehova mwenyewe akizungumza, je, hungechukua hatua kama alivyofanya Amosi? Amosi alichukua hatua mara moja ya kutoa unabii dhidi ya taifa la Israeli la makabila kumi.
2. (a) Unaweza kumwigaje Amosi katika kutimiza utume wa kutoa unabii? (b) Tutazungumzia nini katika sura hii?
2 Huenda ukasema, ‘Lakini mimi si nabii!’ Huenda ukahisi kwamba hustahili kwa sababu hujazoezwa rasmi kuwa nabii. Hata hivyo, mkumbuke Amosi. Alipomkabili Amazia, yule kuhani mwabudu wa ndama, Amosi alisema hivi: “Mimi sikuwa nabii, wala sikuwa mwana wa nabii, bali nilikuwa mchungaji na mminyaji wa tini za mikuyu.” (Amosi 7:14) Ingawa hakuwa mtu mashuhuri, Amosi alikuwa tayari kutimiza utume wake akiwa nabii wa Yehova. Namna gani wewe? Je, unatambua kwamba umepewa mgawo unaolingana kwa njia fulani na mgawo wa wale manabii 12? Unapaswa kutangaza ujumbe wa Mungu leo. Pia, unapaswa kufundisha na kufanya wanafunzi. Unauonaje mgawo huo mzito? Unatangaza ujumbe gani kati ya mataifa? Unatimiza mgawo wako kikamili kadiri gani? Ni nini kinachoonyesha iwapo unafanikiwa katika kazi yako? Acheni tuzungumzie majibu ya maswali hayo.
‘NG’OMBE-DUME WACHANGA WA MIDOMO YAKO’
3. Unaweza kushirikije katika kazi kama ile iliyofanywa na wale manabii ambao tunajifunza vitabu vyao?
3 Je, kweli unashiriki katika kazi kama ile iliyofanywa na manabii? Huenda hujapata kumsikia simba akinguruma katika maana ya kwamba hujapuliziwa moja kwa moja na Yehova. Hata hivyo, katika Neno lake Biblia, umesikia ujumbe muhimu kuhusu siku ya Yehova inayokaribia. Kama tulivyoona katika Sura ya 1 ya kitabu hiki, maneno “nabii” na “-a kinabii” yana maana mbalimbali. Ingawa huenda usiwe nabii kama Amosi na wale manabii wengine wa kale walivyokuwa, bado unaweza kusema kuhusu wakati ujao. Jinsi gani? Unaweza kutangaza ujumbe wa kinabii ambao umejifunza katika Maandiko Matakatifu, kutia ndani vitabu vya wale manabii 12. Huu ndio wakati wa kufanya hivyo.
Tangu mwanzoni mwa karne ya 20 hadi leo, watu wa Mungu wamekuwa ‘wakitoa unabii’
4. Unabii wa Yoeli 2:28-32 unatimizwaje leo?
4 Hebu fikiria jambo hilo kwa njia nyingine. Yehova Mungu alimwambia nabii Yoeli kuhusu wakati ambapo watu wa kila namna watatoa unabii kwa njia ya mfano. “Kisha itakuwa kwamba nitaimimina roho yangu juu ya kila namna ya mwili, na wana wenu na binti zenu watatoa unabii. Nao wazee wenu wataota ndoto. Nao wanaume wenu vijana wataona maono.” (Yoeli 2:28-32) Siku ya Pentekoste, mwaka wa 33 W.K., mtume Petro alitumia maneno hayo kuhusiana na kumiminwa kwa roho takatifu juu ya wale waliokuwa wamekusanyika katika chumba cha juu huko Yerusalemu na kuhusu kazi yao ya kuhubiri “mambo makuu ya Mungu.” (Matendo 1:12-14; 2:1-4, 11, 14-21) Sasa, hebu fikiria wakati wetu. Unabii wa Yoeli umekuwa ukitimizwa kwa njia kubwa tangu mwanzoni mwa karne ya 20. Wakristo watiwa-mafuta—waume kwa wake, wazee kwa vijana—walianza ‘kutoa unabii,’ yaani, kutangaza “mambo makuu ya Mungu,” kutia ndani habari njema ya Ufalme, ambao tayari umesimamishwa mbinguni.
5. (a) Sisi sote tuna pendeleo gani? (b) Unaweza kutoaje “ng’ombe-dume wachanga wa midomo [yako],” na kwa nini ni pendeleo kufanya hivyo?
5 Ingawa hawajazaliwa kwa roho takatifu wawe wana wa Mungu, “mkutano mkubwa” wa “kondoo wengine” wanawaambia hivi wafuasi watiwa-mafuta wa Yesu Kristo: “Tutakwenda pamoja nanyi, kwa maana tumesikia ya kuwa Mungu yupo pamoja nanyi.” (Ufunuo 7:9; Yohana 10:16; Zekaria 8:23) Iwe una tumaini la kuishi milele mbinguni au duniani, una pendeleo la kutoa “ng’ombe-dume wachanga wa midomo [yako].” (Hosea 14:2) Maneno hayo ya unabii wa Hosea yanamaanisha nini? Msomi wa Biblia C. F. Keil asema hivi: “Ng’ombe-dume wachanga . . . ndio waliokuwa wanyama bora wa kutolewa dhabihu za shukrani.” Mtume Paulo alirejelea andiko la Hosea 14:2, alipoandika hivi: “Na tumtolee Mungu dhabihu ya sifa, yaani, tunda la midomo ambayo hulifanyia jina lake tangazo la hadharani.” (Waebrania 13:15) Ndiyo, maneno “ng’ombe-dume wachanga wa midomo yetu” humaanisha kutumia midomo yetu kutoa kilicho bora zaidi, yaani, maneno tunayosema ili kumsifu Yehova.
6. Kwa nini tunapaswa kuchunguza ubora wa dhabihu zetu za sifa?
6 Sisi humtolea Yehova dhabihu za sifa tunaposali kwake kutoka moyoni, tunaposhiriki katika mikutano ya Kikristo kwa kutoa maelezo yanayoonyesha kwamba tunamthamini, na tunapozungumza na wengine kwa shauku katika huduma ya shambani. Hata hivyo, kila mmoja wetu anaweza kujiuliza, ‘Ninaposhiriki katika utendaji huo, dhabihu yangu ni bora kadiri gani?’ Kutokana na mambo ambayo tayari umejifunza, hapana shaka kwamba umechukizwa na makuhani wa siku za Malaki ambao walitoa dhabihu za wanyama wenye kasoro kwenye madhabahu ya Mungu. Yehova alimtumia Malaki kukazia jinsi dhabihu zao zilivyokuwa duni, kwa kuwa hawakuona kwamba walikuwa wakiidharau meza ya Yehova. (Malaki 1:8) Kwa hiyo, tunapaswa kuchunguza ubora wa dhabihu zetu ili kuhakikisha kwamba tunatoa dhabihu bora kabisa zisizo na kasoro yoyote.
UJUMBE UNAOPASWA KUTANGAZWA
7. Tunahitaji ujasiri ili kutimiza lengo gani la ujumbe wetu?
7 Ili tutoe “ng’ombe-dume wachanga wa midomo yetu” katika huduma lazima tuwe na ujasiri, sivyo? Tunahitaji ujasiri kwa sababu ujumbe tunaowatangazia watu unatimiza malengo mawili, na mojawapo ya malengo hayo halipendwi na wengi. Nabii Yoeli aliwaambia watu wa Mungu hivi: “Tangazeni mambo haya kati ya mataifa, ‘Takaseni vita! Amsheni wanaume wenye nguvu! Waacheni wakaribie! Na waje, wanaume wote wa vita!’” (Yoeli 3:9) Huo ni mwito mkubwa kama nini kwa mataifa! Ni tangazo rasmi la vita vya uadilifu vya Yehova dhidi ya watu wanaomkaidi Mungu. Ingawa Yehova anawaagiza watu wake ‘wafue panga zao ziwe majembe na mikuki yao iwe miundu,’ anawaambia mataifa adui ‘wafue majembe yao yawe panga na miundu yao iwe mikuki.’ (Mika 4:3; Yoeli 3:10) Naam, lazima adui za Mungu wajitayarishe kukutana na Muumba wa ulimwengu huu katika vita. Ujumbe huo ambao tunatangaza si wenye kufariji hata kidogo.
8. Kwa nini “mabaki ya Yakobo” wanalinganishwa na simba?
8 Katika ujumbe wa nabii Mika, wale wanaotoa ‘ng’ombe-dume wachanga wa midomo yao’ wanalinganishwa na simba. Aliandika hivi: “Mabaki ya Yakobo watakuwa kati ya mataifa . . . kama simba katikati ya wanyama wa msituni, kama mwana-simba mwenye manyoya shingoni katikati ya makundi ya kondoo, ambaye, anapopita kati, hukanyaga-kanyaga na pia hurarua vipande-vipande; wala hakuna mkombozi.” (Mika 5:8) Kwa nini anawalinganisha na simba? Leo, watu wa Mungu, wakiongozwa na mabaki watiwa-mafuta, lazima waonyeshe ujasiri kama wa simba wanapoyatangazia mataifa ujumbe wenye kuonya.a
Je, unaitangaza siku ya Yehova kwa ujasiri?
9. (a) Ni wakati gani unapohitaji kuwa na ujasiri kama simba? (b) Unaweza kupataje ujasiri unapokabili upinzani au kutopendezwa?
9 Je, una ujasiri kama wa simba unapotangaza ujumbe huo wenye onyo? Huenda ukahitaji ujasiri huo unaposimama mbele ya watu wenye mamlaka, hali kadhalika unapozungumza na marika zako shuleni, kazini au unapozungumza na watu wako wa ukoo ambao si waamini. (Mika 7:5-7; Mathayo 10:17-21) Unaweza kupataje ujasiri unapokabili upinzani au kutopendezwa? Hebu sikiliza jinsi Mika alivyoweza kutimiza kazi ngumu ya kuonya kuhusu uharibifu wa Samaria na Yerusalemu: “Nimejaa nguvu, kwa roho ya Yehova, na ya haki na uwezo, ili nimwambie Yakobo maasi yake na Israeli dhambi yake.” (Mika 1:1, 6; 3:8) Wewe pia unaweza ‘kujaa nguvu’ kwa sababu wewe pia unaweza kupokea kiasi kikubwa cha roho ya Mungu yenye kutia nguvu. (Zekaria 4:6) Kwa kumtegemea Mungu katika sala, utaweza kutangaza maneno yake yanayoweza kufanya masikio yawashe.—2 Wafalme 21:10-15.
10. Tunaweza kumwigaje Sefania tunapotangaza ujumbe kuhusu “siku ya Yehova”?
10 Ingawa unahitaji ujasiri, unapaswa pia kuwa na busara unapowafikia watu ukiwa na ujumbe huo wenye onyo. Tunahitaji kuwa ‘wapole [au, wenye busara] kwa wote,’ hata wakati ambapo ujumbe huo unahusu “siku ya Yehova” inayokaribia. (2 Timotheo 2:24; Yoeli 2:1, 11; Sefania 1:14) Tena, tunaweza kujifunza kutoka kwa wale manabii 12. Ingawa walitangaza kwa ujasiri ujumbe mbalimbali wa hukumu kutoka kwa Yehova, waliwajali wale waliosikiliza. Kwa mfano, nabii Sefania hakusita kusema kwa ujasiri alipokuwa akizungumza na wakuu wenye vichwa vigumu walioishi siku zake, hata hivyo, hakumshutumu Mfalme Yosia aliyekuwa mwaminifu. (Sefania 1:8) Tunapotangaza ujumbe wenye onyo, je, tunaweza kuwasaidia watu tukiwa na maoni ya kwamba wanaweza kuwa kondoo, badala ya kuwa na maoni yasiyofaa kuwaelekea?—Mathayo 25:32-34.
11. (a) Lengo la pili la ujumbe wetu ni nini? (b) Unaweza kuwaigaje wale manabii 12 unapotangaza siku ya Yehova?
11 Lengo la pili la ujumbe wetu ni nini? Linatajwa katika Mika sura ya 5. “Mabaki ya Yakobo watakuwa katikati ya makabila mengi ya watu kama umande kutoka kwa Yehova, kama manyunyu mengi ya mvua juu ya mimea, ambayo hayamtumaini mwanadamu wala kuwangojea wana wa mtu wa udongo.” (Mika 4:1; 5:7) Kwa sababu ya habari njema wanazowatangazia “makabila mengi ya watu” leo, wale “mabaki” wa Yakobo, au Israeli la kiroho, pamoja na waandamani wao ni kama “umande [wenye kuburudisha] kutoka kwa Yehova” na “manyunyu mengi ya mvua juu ya mimea.” Kuna mengi tunayoweza kujifunza katika vitabu 12 vya mwisho vya Maandiko ya Kiebrania kuhusu lengo hilo la pili la ujumbe wetu, kwa kuwa manabii hao hawakutangaza uharibifu tu bali walitangaza kurudishwa pia. Katika huduma yako, je, wewe hukazia mambo yenye kupendeza katika ujumbe huo kuhusu siku ya Yehova?
WEWE HUTANGAZAJE UJUMBE HUO?
12, 13. (a) Kwa nini watu wa Mungu wanalinganishwa na makundi ya wadudu? (b) Unahisije kuhusu mambo yanayotajwa katika Yoeli 2:7, 8?
12 Basi, wewe hutangazaje ujumbe huo wenye malengo mawili? Nabii Yoeli alilinganisha kazi ya watu wa Mungu na mfululizo wa mashambulizi ya wadudu, kutia ndani nzige. (Yoeli 1:4) Hata hivyo, kwa nini tunawalinganisha watu wa Yehova na makundi ya wadudu? Kwa sababu, kama andiko la Yoeli 2:11 linavyoonyesha, Mungu anawaita wadudu hao “jeshi lake.” (Watu wa Mungu wanafananishwa na nzige katika kitabu cha Ufunuo pia. Ona Ufunuo 9:3, 4.) Wadudu ambao Yoeli aliwataja walivamia kama moto wenye kuteketeza, na popote walipovamia palionekana mwanzoni kama “bustani ya Edeni” lakini palibaki pakiwa “nyika iliyo ukiwa.” (Yoeli 2:2, 3) Unaweza kuonyeshaje kwamba unaelewa maana ya unabii wa Yoeli?
13 Hebu fikiria jinsi viumbe hao wadogo walivyo. Yoeli alisema hivi: “Wanakimbia kama wanaume wenye nguvu. Wanapanda ukuta kama wanaume wa vita. Nao huenda kila mmoja katika njia zake, nao hawabadili mapito yao. Wala hawasukumani. Wanasonga mbele kama mwanamume katika mwendo wake; na baadhi yao wakianguka katikati ya silaha, wale wengine hawageuzi mwendo wao.” (Yoeli 2:7, 8) Hakuna “ukuta” wowote wa upinzani unaoweza kuwazuia wao wala mashambulizi yao. “Baadhi yao wakianguka katikati ya silaha,” kama vile ambavyo Wakristo washikamanifu wameuawa na adui wenye kuonea, wengine huendeleza kazi hiyo, wakitimiza utume ambao Yehova amewapa. Je, umeazimia kushikamana na mgawo wa kutangaza siku ya Yehova hadi Mungu aone kwamba umetimizwa? Huenda hata ukawa unaendeleza kazi iliyokuwa ikifanywa na Wakristo fulani waaminifu ambao wamekufa.
Unaweza kupata mafanikio katika huduma yako haidhuru watu wanaitikiaje
14. Unaweza kufanya nini ili kuhakikisha kwamba kazi ya kuhubiri inatimizwa kikamili?
14 Jambo kuu ni kufanya mambo kikamili. Wewe binafsi unaweza kufanya nini ili kuhakikisha kwamba kazi ya kuhubiri inayofafanuliwa katika unabii wa Yoeli inatimizwa kikamili? Kwa kushiriki katika huduma ya nyumba kwa nyumba na kurudi ili kuwafundisha wale wanaopendezwa. Pia, kwa kuwatembelea wale ambao hukuwakuta nyumbani. Unapofanya hivyo unaonyesha kwamba unaelewa vizuri unabii huo. Kuwahubiria watu barabarani hukuwezesha kuwasiliana na watu ambao hungeweza kukutana nao vinginevyo. Isitoshe, kuna njia nyingine: Unaweza kuwasaidia watu walio katika eneo lenu ambao wamehamia kutoka nchi nyingine.b Je, uko macho kutumia nafasi hizo ili kuhakikisha kwamba kazi ya kuhubiri inafanywa kikamili leo?
MAFANIKIO YA HUDUMA YAKO HUTEGEMEA NINI?
15. Watu waliitikiaje ujumbe wa wale manabii 12?
15 Watu huitikiaje ujumbe kuhusu siku ya Yehova yenye kuogopesha? Usishangae unapokabili upinzani au kutopendezwa. Ndivyo ilivyokuwa kwa manabii wengi wa Mungu. Wengi wao walipaswa kutangaza ujumbe mkali wenye onyo. (Yeremia 1:17-19; 7:27; 29:19) Licha ya hayo, manabii kadhaa walipata matokeo mazuri! Angalau watano kati yao, yaani, Yona, Mika, Sefania, Hagai, na Zekaria, walifanikiwa kuchochea mioyo ya watu fulani kutubu dhambi zao za wakati uliopita na kubadili mwenendo wao.
16. Jitihada za nabii Mika zilikuwa na matokeo gani?
16 Inaonekana kwamba kazi ya nabii Sefania ilimchochea Mfalme Yosia aanzishe tena ibada safi. Mika alitangaza kwa ujasiri ujumbe wa hukumu dhidi ya wakuu wa Yuda, nayo matendo ya Mfalme Hezekia yalipatana na maneno ya Mika. (Mika 3:1-3) Baadhi ya wanaume wazee walioishi siku za Yeremia walitaja itikio zuri la Hezekia waliposema kwamba mfalme ‘alimwogopa Yehova na kuanza kuutuliza uso wa Yehova.’ (Yeremia 26:18, 19; 2 Wafalme 18:1-4) Chini ya uongozi wa Hezekia, watu wa Yuda pamoja na wengine kutoka ufalme wa kaskazini waliokubali kwa hiari waliadhimisha Pasaka na Sherehe ya Keki Zisizo na Chachu. Waliendelea na sherehe hizo kwa juma moja zaidi. Matokeo ya kurudia kwao ibada ya kweli yalikuwa nini? “Kukawa na shangwe kubwa Yerusalemu.” (2 Mambo ya Nyakati 30:23-26) Mika alikuwa ameanza kutangaza ujumbe wa Mungu kuhusu uharibifu wa taifa lililoasi ambalo lilitawaliwa na Mfalme Ahazi. Hata hivyo, nabii huyo aliona matokeo ya jitihada zake wakati Hezekia, mwana wa Ahazi, alipoitikia vizuri.
17. Hagai na Zekaria walitimiza nini?
17 Wafikirie pia manabii Hagai na Zekaria. Walikuwa manabii miongoni mwa Wayahudi waliorudi nyumbani, ambao hawakupendezwa na ujumbe wao na ambao walihangaikia masilahi yao tu. (Hagai 1:1, 2; Zekaria 1:1-3) Kufikia wakati ambapo manabii hao wawili walianza migawo yao, miaka 16 ilikuwa imepita tangu msingi wa hekalu uwekwe. Watu walikuwa “mbioni, kila mmoja kwa ajili ya nyumba yake mwenyewe” hali nyumba ya Yehova ilikuwa “imeharibika.” Hagai aliwahimiza hivi Wayahudi hao: “‘Iweni na nguvu, ninyi nyote watu wa nchi,’ asema Yehova, ‘na mfanye kazi.’” Matokeo yakawaje? Yehova “akaiamsha roho” ya Gavana Zerubabeli, ya Kuhani Mkuu Yoshua, na “ya mabaki yote ya watu.” Kwa hiyo, wakaweza kumaliza kazi ya kujenga hekalu.—Hagai 1:9, 12, 14; 2:4.
18, 19. (a) Watu katika nchi fulani wanaitikiaje kutangazwa kwa siku ya Yehova? (b) Utaitikiaje uhitaji wa kuwatangazia watu wote ujumbe wenye onyo?
18 Wengi kati ya wale manabii 12 walitangaza ujumbe kwa mataifa ambayo mwanzoni yalikuwa wakfu kwa Yehova. Huenda ikawa tunawahubiria watu ambao hawajapata kumjua Mungu wa kweli, hata hivyo, bado tunaweza kujifunza kutokana na matokeo ya utendaji wao. Leo pia, katika maeneo mengi, watu wanakubali ujumbe muhimu kuhusu siku ya Yehova. Tunaona matokeo kama yale yaliyotabiriwa na Zekaria: “Mataifa mengi yatajiunga na Yehova siku hiyo, nao watakuwa watu wangu; nami nitakaa katikati yako.” (Zekaria 2:11) Leo, watu wa “mataifa mengi” wanakubali kihalisi ujumbe unaotangazwa na watu wa Mungu. (Ufunuo 7:9) Zekaria alitabiri hivi: “Vikundi vingi vya watu na mataifa yenye nguvu watakuja kumtafuta Yehova wa majeshi katika Yerusalemu na kuutuliza uso wa Yehova.” Wanaitwa “watu kumi kutoka katika lugha zote za mataifa” ambao watashika upindo wa nguo ya Mwisraeli wa kiroho wakisema: “Tutakwenda pamoja nanyi, kwa maana tumesikia ya kuwa Mungu yupo pamoja nanyi.”—Zekaria 8:20-23.
19 Ona kwamba andiko hilo limetaja “lugha zote za mataifa.” Biblia na vichapo vya Biblia vinatafsiriwa katika lugha nyingi, na Mashahidi wa Yehova wanawazoeza wahudumu kuwafundisha watu kutoka katika “lugha zote za mataifa.” (Mathayo 28:19, 20; Matendo 1:8) Huenda umejifunza lugha nyingine ili kuwasaidia watu ambao wanazungumza lugha hiyo katika eneo lenu. Isitoshe watu kadha wa kadha wamejifunza lugha moja au mbili na kuhamia nchi nyingine ambako wengi huitikia kwa hamu habari njema. Je, unaweza kuhamia katika maeneo kama hayo yenye matokeo na ‘kutangaza habari njema katika mataifa’? Fikiria hilo kwa uzito na usali juu yake. Ikiwa una familia, zungumzieni mara kwa mara uwezekano wa kuhamia nchi nyingine, na kuwawekea watoto wenu mradi huo.
20. Yehova alikazia mtazamo gani kuhusu watu wa Ninawi?
20 Nabii mwingine, aliyesikilizwa na watu ambao haikudhaniwa wangemsikiliza, ni nabii Yona. Watu wa Ninawi, kutia ndani mfalme mwenyewe, waliitikia vizuri ujumbe wa Yona, na kumwamini Yehova. Mungu mwenyewe aliuliza: “Je, sipaswi kusikitikia Ninawi lile jiji kubwa, ambalo lina wanadamu zaidi ya 120,000 wasiojua hata kidogo tofauti kati ya mkono wao wa kuume na wa kushoto?” (Yona 4:11) Hebu zingatia maneno hayo unapofikiria lile ambalo hukuchochea kuwatangazia wengine ile siku ya Yehova yenye kuogopesha. Je, unahisi kwamba una deni kwa Yehova kwa kuwa amekuokoa kupitia fidia? Je, unahisi kwamba una wajibu kwa kuwa wewe ni mtumishi aliyejiweka wakfu kwa Yehova? (1 Wakorintho 9:16, 17) Hizo ni sababu muhimu za kutangaza siku ya Yehova. Ingawa hivyo, je, wewe ‘huwasikitikia’ watu unaowatangazia siku ya Yehova? Unaweza kuwa na furaha iliyoje unapoiga rehema ya Mungu na kuchochewa kuzungumza na watu kuhusu siku hiyo!
21. Unaweza kujifunza nini kutokana na jinsi Amosi alivyokabiliana na tisho la Amazia?
21 Hatujui mengi kuhusu jinsi ujumbe wa Yoeli, Obadia, Nahumu, Habakuki, na Malaki ulivyoitikiwa. Hata hivyo, tunajua angalau jinsi ujumbe wa Amosi ulivyopokewa. Amazia alimpinga vikali Amosi, akidai kwamba nabii huyo alikuwa amepanga njama dhidi ya mfalme. Pia alijaribu kumzuia Amosi asihubiri Betheli. (Amosi 7:10-13) Amosi alikabili upinzani huo kwa ujasiri. Leo pia, huenda wafuasi wa dini wakajaribu kuwachochea viongozi fulani wa kisiasa wawatese watu wa Yehova au hata kupiga marufuku kazi yao ya kuhubiri ambayo huwafaidi watu. Je, utamwiga Amosi kwa kuendelea kutangaza habari njema licha ya upinzani?
22. Kwa nini unaweza kusema kwamba huduma inapata mafanikio katika eneo lenu?
22 Ingawa ujumbe wa manabii hao 12 ulipokewa kwa njia tofauti-tofauti, wote hao walitimiza utume wao. Jambo muhimu si kwamba watu wanaitikia ujumbe wetu wenye malengo mawili, bali kwamba tumtolee Yehova “ng’ombe-dume wachanga wa midomo yetu,” yaani, “dhabihu ya sifa” iliyo bora. (Hosea 14:2; Waebrania 13:15) Kisha tuache mambo mikononi mwa Mungu. Atawavuta wale ambao kwa kweli ni kondoo. (Yohana 6:44) Isitoshe, unaweza kupata mafanikio ukiwa mtangazaji wa ujumbe wa Mungu haidhuru watu wanaitikiaje. Unaweza kuwa na hakika kwamba “miguu ya mtu anayeleta habari njema, anayetangaza amani,” ni yenye kupendeza machoni pa wale wanaothamini na kukubali habari njema. Zaidi ya yote, ni yenye kupendeza machoni pa Yehova. (Nahumu 1:15; Isaya 52:7) Kwa kuwa siku ya Yehova iko karibu sana, azimia kuendelea kufanya jambo ambalo Yoeli alitabiri lingefanywa siku zetu: “Tangazeni mambo haya kati ya mataifa, ‘Takaseni vita! Amsheni wanaume wenye nguvu!’” Hilo ni tangazo la vita vya Mungu dhidi ya mataifa.—Yoeli 3:9.
a Huenda unabii huo ulitimizwa mara ya kwanza katika enzi ya Wamakabayo wakati ambapo Wayahudi waliokuwa chini ya uongozi wa Wamakabayo walipowafukuza adui zao kutoka Yuda na kuliweka hekalu wakfu tena. Hilo liliwawezesha mabaki ya Wayahudi kumkaribisha Masihi alipotokea.—Danieli 9:25; Luka 3:15-22.
b Kijitabu Good News for People of All Nations, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova, kimetumiwa kwa mafanikio kuwasaidia watu ambao hawazungumzi lugha kuu ya eneo lenu.
-
-
“Baraka Hata Kusiwe na Uhitaji Tena”Izingatie Siku ya Yehova Maishani
-
-
SURA YA KUMI NA NNE
“Baraka Hata Kusiwe na Uhitaji Tena”
1, 2. (a) Kila mmoja wetu anaweza kufanya maamuzi gani muhimu? (b) Tunaweza kupata baraka kutokana na utimizo wa unabii gani?
HUU ni wakati wa hukumu na wa baraka. Ni wakati wa kuzorota kwa dini na kurudishwa kwa ibada ya kweli. Kwa kweli ungependa kupata baraka pamoja na matokeo mazuri ya sasa na ya wakati ujao yanayotokana na kurudishwa kwa ibada ya kweli! Unaweza kuwaje na hakika kuhusu mambo hayo? Jibu lapatikana katika unabii uliotimizwa kwa njia kubwa mara tu baada ya “siku za mwisho” kuanza katika mwaka wa 1914. (2 Timotheo 3:1) Malaki alitabiri hivi: “‘Bwana wa kweli [Yehova] atakuja kwenye hekalu Lake, ambaye ninyi mnamtafuta, na mjumbe wa agano mnayependezwa naye. Tazama! Atakuja hakika,’ asema Yehova wa majeshi.”—Malaki 3:1.
2 Unabii huo ambao ni muhimu sana maishani mwako unapatikana katika kitabu cha mwisho cha wale manabii 12. Tunapomalizia kuzungumza juu ya vitabu hivyo, mambo ambayo Malaki aliandika yanatupendeza sana. Kitabu chake kinatia ndani maagizo yanayokuwezesha wewe pamoja na watumishi wengine wa Yehova kupokea “baraka hata kusiwe na uhitaji tena.” (Malaki 3:10) Hebu tuchunguze vizuri zaidi sura ya 3 ya kitabu cha Malaki.
WAKATI WA USAFISHAJI WA KIROHO
3. Ni nini kilichotokea miongoni mwa watu wa kale wa Mungu kilichofanya “Israeli wa Mungu” kuchaguliwa?
3 Karne tano baada ya siku za Malaki, Yehova, akiwakilishwa na Kristo (“mjumbe [wa Mungu] wa agano” la Abrahamu), aliingia katika hekalu halisi huko Yerusalemu ili awahukumu watu Wake wa agano. Kwa ujumla, taifa hilo halikustahili kuendelea kuwa na kibali chake, na hivyo Yehova akalikataa. (Mathayo 23:37, 38) Mambo yaliyotokea mwaka wa 70 W.K. yanathibitisha hilo. Bila shaka, Mungu alichagua “Israeli wa Mungu,” taifa la kiroho la watu 144,000 kutoka katika mataifa yote. (Wagalatia 6:16; Waroma 3:25, 26) Hata hivyo, huo haukuwa mwisho wa utimizo wa unabii wa Malaki. Unabii huo unatimizwa leo pia. Isitoshe, unabii huo unahusu tumaini lako la wakati ujao la kupata “baraka hata kusiwe na uhitaji tena.”
4. Ni swali gani lililohitaji kujibiwa baada ya Yesu kuwekwa kuwa Mfalme katika mwaka wa 1914?
4 Kutimizwa kwa unabii wa Biblia huthibitisha kwamba mwaka wa 1914, Yesu Kristo aliwekwa kuwa Mfalme wa Ufalme wa mbinguni wa Yehova. Kisha ukafika wakati wa Yesu kuchagua kikundi cha Wakristo waliostahili kupata kibali cha Mungu. Ni nani ambao wangethibitika kuwa safi kiroho? Jibu linapatikana katika maneno haya ya Malaki: “Ni nani atakayeistahimili siku ya kuja kwake, naye ni nani atakayesimama wakati atakapoonekana? Kwa maana atakuwa kama moto wa msafishaji.” (Malaki 3:2) Yehova alikuja wakati gani na jinsi gani katika “hekalu” lake ili kuhukumu?
5, 6. (a) Yehova alipoingia katika hekalu lake la kiroho ili alikague, alipata hali gani miongoni mwa wengi waliodai kumwabudu? (b) Watumishi watiwa-mafuta wa Mungu walihitaji nini?
5 Ni wazi kwamba, Mungu hakuingia katika hekalu halisi lililojengwa kwa mawe. Hekalu halisi la mwisho lililotumiwa kwa ajili ya ibada ya kweli liliharibiwa mwaka wa 70 W.K. Badala yake, Yehova aliingia katika hekalu la kiroho, mpango unaowawezesha wanadamu kumfikia na kumwabudu kwa msingi wa dhabihu ya fidia ya Yesu. (Waebrania 9:2-10, 23-28) Bila shaka, makanisa ya dini za Kikristo hayakuwa hekalu hilo la kiroho, kwa kuwa makanisa hayo yalikuwa sehemu ya mfumo wa kidini ulio na hatia ya kumwaga damu, kufanya ukahaba wa kiroho, na kuunga mkono mafundisho ya uwongo badala ya ibada safi. Yehova alikuwa “shahidi wa haraka juu” yao, na bila shaka walistahili hukumu kali waliyopata. (Malaki 3:5) Hata hivyo, baada ya Ufalme wa Mungu kusimamishwa, kulikuwa na kikundi cha Wakristo wa kweli katika nyua za hekalu la kiroho la Mungu. Kikundi hicho kilionyesha ushikamanifu kwa Mungu licha ya majaribu makali. Hata hivyo, watiwa-mafuta hao walihitaji pia kusafishwa. Mambo ambayo manabii wale 12 waliandika yalitaja usafishaji huo, kwa maana yalitaja ahadi zenye kutia moyo za kuwarudisha watumishi wa Mungu kiroho na kimwili. Malaki alitabiri kwamba kungekuwa na watu ambao Yehova ‘angewasafisha kama dhahabu na kama fedha.’ Watu hao ‘wangekuwa kwa Yehova watu wanaotoa toleo la zawadi katika uadilifu.’—Malaki 3:3.
6 Kuna mambo mengi leo yanayoonyesha kwamba tangu 1918 na kuendelea, Yehova aliwasafisha Wakristo watiwa-mafuta, na kutakasa ibada, mazoea, na mafundisho yao.a Wakristo hao pamoja na “umati mkubwa” ambao ulijiunga nao baadaye, wamefaidika sana. (Ufunuo 7:9) Wakiwa kikundi chenye muungano, wanaendelea kumtolea “toleo la zawadi katika uadilifu” yaani, “lenye kumpendeza Yehova.”—Malaki 3:3, 4.
Yehova amekuwa akiwasafisha watu wake wakiwa kikundi. Je, sisi binafsi bado tunahitaji kusafishwa?
7. Tunapaswa kujiuliza nini kuhusu msimamo wetu mbele za Mungu?
7 Kwa ujumla, hivyo ndivyo watu wa Mungu walivyo. Hata hivyo, je, twaweza kusema vivyo hivyo kuhusu kila mmoja wetu binafsi? Huenda ukajiuliza, ‘Je, bado kuna mambo ninayohitaji kusafisha katika mtazamo na matendo yangu? Je, bado nahitaji kusafisha mwenendo wangu, kama vile Yehova alivyowasafisha watiwa-mafuta wake?’ Tuliona mwanzoni kwamba manabii hao 12 walikazia maoni na mwenendo usiofaa hali kadhalika tabia na matendo mazuri. Mambo hayo yamekusaidia kujua vizuri zaidi mambo ambayo Yehova ‘anataka kutoka kwako.’ (Mika 6:8) Ona kwamba andiko hilo linasema “kutoka kwako.” Hilo linakazia kwa nini kila mmoja wetu anapaswa kujichunguza aone ikiwa bado anahitaji kutakaswa au kusafishwa.
“TAFADHALI, MNIJARIBU”
8. Yehova amewatolea watu wake mwito gani?
8 Hebu fikiria jinsi Yehova anavyosema kupitia Malaki katika sura ya 3, mstari wa 10. Andiko hilo lina mwito huu mchangamfu: “‘Leteni ghalani sehemu zote za kumi, ili kuwe na chakula nyumbani mwangu; nanyi, tafadhali, mnijaribu kwa njia hii,’ Yehova wa majeshi amesema, ‘kama sitawafungulia ninyi malango ya mbinguni na kuwamwagia baraka hata kusiwe na uhitaji tena.’” Mwito huo unatolewa kwa watu wote wa Mungu. Je, unahisi kwamba mwito huo unakuhusu wewe binafsi pia?
9. Unaweza kumtoleaje Yehova matoleo na sehemu ya kumi?
9 Unaweza kumtoleaje Yehova ‘sehemu ya kumi’? Bila shaka, huwajibiki kutoa matoleo halisi na sehemu za kumi, kama ilivyokuwa chini ya Sheria. Leo, Mungu hutaka tumtolee matoleo ya kiroho. Kama tulivyozungumzia katika sura iliyotangulia, Paulo alilinganisha kazi yetu ya kuhubiri na toleo. (Hosea 14:2) Kisha mtume huyo akataja dhabihu ya aina nyingine, alipoandika hivi: “Msisahau kutenda mema na kushiriki vitu [vya kimwili] pamoja na wengine, kwa maana Mungu hupendezwa vema na dhabihu za namna hiyo.” (Waebrania 13:15, 16) Basi, ni wazi kwamba “sehemu ya kumi” iliyotajwa katika Malaki 3:10 inawakilisha matoleo ya kiroho na ya kimwili. Tukiwa Wakristo waliobatizwa, tumejiweka wakfu kwa Yehova, hata hivyo sehemu ya kumi tunayotoa inawakilisha kile tunachoweza kumtolea Yehova, au kutumia katika utumishi wake. Inatia ndani wakati, nguvu, mali, na michango ya fedha tunayotoa kwa ajili ya utumishi wa Yehova.
10. Unaweza ‘kumjaribuje’ Yehova kwa njia inayofaa?
10 Inafaa kama nini umtolee Yehova sehemu ya kumi ukichochewa na wakfu na ushikamanifu wako pamoja na upendo wa kweli. Tunapaswa kuwa macho sikuzote! Siku ya Yehova inakaribia haraka nayo itakuwa siku “yenye kuogopesha sana.” (Yoeli 2:1, 2, 11) Uhai wa watu umo hatarini. Mungu anawatolea watu mwito ambao wewe mwenyewe unaweza kuitikia. Yehova anakwambia ‘umjaribu.’ Bila shaka, hakuna mwanadamu yeyote duni anayeweza kumjaribu Mungu kana kwamba hategemeki. (Waebrania 3:8-10) Hata hivyo, unaweza kumjaribu kwa unyenyekevu kwa njia inayofaa. Jinsi gani? Ameahidi kwamba atatubariki. Ukimtii, ni kana kwamba unamjaribu, kana kwamba unamuuliza ‘Je, utanibariki?’ Naye hukujibu kwa kujipa wajibu wa kufanya hivyo, na kutimiza ahadi yake. Hivyo, hatua hiyo ya Mungu ya kukuruhusu ‘umjaribu’ hukuhakikishia kwamba atakubariki sana.
11, 12. Ni baraka gani za Yehova kwa watu wake ambazo umejionea wewe binafsi?
11 Ni wazi kwamba watu wa Yehova wametoa matoleo mengi ya kimwili na dhabihu za kiroho naye Yehova amewamwagia “baraka hata kusiwe na uhitaji tena.” Huenda umeona jinsi watu wa Mungu wamebarikiwa, labda kupitia maongezeko makubwa ambayo Mashahidi wa Yehova wamepata tangu mwanzoni mwa karne ya 20 hadi leo. Pia umeona ufahamu wa “mambo mazito ya Mungu” ukiongezeka. (1 Wakorintho 2:10; Methali 4:18) Hata hivyo, fikiria jambo hilo kwa njia nyingine: Wewe binafsi umefaidikaje?
12 Huenda wakati fulani ulikuwa mfuasi wa kanisa fulani, au huenda ulianza tu kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova. Wakati huo, ulifahamu kadiri gani kweli za msingi za Biblia? Sasa linganisha na mambo ambayo umejifunza tangu wakati huo ambayo unaweza kuthibitisha moja kwa moja kwa kutumia Maandiko. Au fikiria mambo mazito ambayo umeelewa, kutia ndani unabii mbalimbali unaotimia leo. Pia fikiria maendeleo ambayo umefanya katika kutumia maandiko fulani ya Biblia maishani mwako. Umepiga hatua kubwa kama nini! Unaweza kusema kama alivyosema mtume Petro: “Tuna neno la kinabii likiwa limefanywa hakika zaidi.” (2 Petro 1:19) Jambo kuu ni hili: Wewe binafsi ‘umefundishwa na Yehova’ na uko miongoni mwa Wakristo wa kweli wanaotaka kumtumikia Yehova milele. (Isaya 54:13) Tayari unaweza kusema kwamba amekubariki kwelikweli.
JINA LAKO KATIKA KITABU CHA UZIMA
13. Jina la mtu linaweza kuandikwaje katika kitabu cha kumbukumbu cha Mungu?
13 Andiko la Malaki 3:16 linataja baraka nyingine kutoka kwa Yehova: “Wakati huo wale wenye kumwogopa Yehova wakasemezana, kila mmoja na mwenzake, na Yehova akaendelea kutoa uangalifu na kusikiliza. Na kitabu cha kumbukumbu kikaanza kuandikwa mbele zake kwa ajili ya wale wenye kumwogopa Yehova na kwa ajili ya wale wanaolifikiria jina lake.” Watiwa-mafuta pamoja na wale wa umati mkubwa ‘wanamwogopa Yehova.’ Je, hulioni kuwa pendeleo kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, yaani, kuwa miongoni mwa watu wenye furaha wanaolifikiria jina la Yehova na kulitukuza ulimwenguni pote? Kujua kwamba Yehova anakumbuka uaminifu wako ni jambo lenye kuridhisha kwelikweli!—Waebrania 6:10.
14. Wale manabii 12 wamekusaidiaje kutambua mitazamo na mazoea ambayo Yehova anachukia?
14 Hata hivyo, wewe binafsi unaweza kufanya nini ili jina lako listahili kuandikwa katika “kitabu cha kumbukumbu,” ambacho hata sasa hivi kinaendelea kuandikwa mbele za Yehova? Kumbuka baadhi ya mashauri yenye hekima ambayo tumepata katika vitabu vya wale manabii 12. Yalitusaidia kufahamu mwenendo, sifa, na mitazamo inayomchukiza Yehova. Kwa mfano, manabii hao walitutahadharisha kuhusu mazoea ambayo Mungu anasema yanapingana na viwango vyake vya uadilifu na yanaweza kuharibu maisha yetu, kama vile “mwenendo mpotovu” na “roho ya uasherati.” (Hosea 4:12; 6:9) Mungu huchukia watu wanaowatendea kwa hila wenzi wao wa ndoa au hata washiriki wa familia zao. (Malaki 2:15, 16) Yehova aliwaongoza manabii hao wakazie kwamba hapendezwi kamwe na jeuri yoyote ile. (Amosi 3:10) Pia, aliwaongoza wakazie uhitaji wa kuepuka ukosefu wa haki au udanganyifu katika biashara na mambo yanayohusu pesa. (Amosi 5:24; Malaki 3:5) Pia, vitabu hivyo 12 vilikazia kwamba wanaume ambao wamekabidhiwa mamlaka hawapaswi kamwe kufanya maamuzi kwa upendeleo au mapendezi ya ubinafsi.—Mika 7:3, 4.
15. Unaweza kupata faida gani kwa kufuata mahimizo ya wale manabii 12?
15 Hata hivyo, manabii hao hawakuachia hapo. Walituonyesha pia faida tunazoweza kupata kwa kuishi kulingana na viwango vya Mungu. Uhusiano wetu na Yehova utakuwa wa karibu zaidi. (Mika 4:5) Makutaniko yetu yatakuwa imara zaidi na yenye bidii iwapo haki itaenea. Ndoa zetu zitakuwa na nguvu zaidi, nazo familia zetu zitakuwa na muungano mzuri zaidi, na zitazingatia zaidi mambo ya kiroho. (Hosea 2:19; 11:4) Tukitenda kwa haki na kwa unyoofu, tutaheshimiwa na wengine. Tutajitahidi kuiga rehema ya Yehova kwa kuhurumiana na kuonyeshana fadhili zenye upendo na ndugu na dada zetu. (Mika 7:18, 19) Naam, tutazingirwa na watu wa kiroho, ndugu na dada wanaopenda kweli na amani. Isitoshe, tutakuwa rafiki za Yehova. (Zekaria 8:16, 19) Je, hukubali kwamba tayari umebarikiwa kwelikweli?
16. Ni tofauti gani iliyo wazi leo, nayo itamaanisha nini siku ya Yehova itakapofika?
16 Kutokana na mambo ambayo tumejifunza, ni kweli kabisa kwamba “tofauti kati ya mwadilifu na mwovu”—tofauti kati ya Wakristo wa kweli na wa uwongo—iko wazi kuliko wakati mwingine wowote. (Malaki 3:18) Tunajitahidi kuishi kulingana na viwango vya Yehova huku ulimwengu kwa ujumla ukizidi kudidimia kwa sababu ya kutomwogopa Mungu. Na ni wazi kwamba “siku kuu ya Yehova” itakapofika, tofauti hiyo itamaanisha uzima au kifo.—Sefania 1:14; Mathayo 25:46.
17. Unaweza kutumiaje habari zilizo katika kitabu hiki wakati ujao?
17 Basi, bila shaka wale manabii 12 wanatoa mashauri yenye faida ya kudumu. Unapokabili matatizo hususa, au unapohitaji kufanya maamuzi fulani, unaweza kuchunguza habari muhimu zilizo katika kitabu hiki. Hivyo, unaweza kuendelea kuonyesha kwamba unatamani kufundishwa njia za Yehova na ‘kutembea katika mapito yake.’ (Mika 4:2) Hata hivyo, kutembea katika mapito hayo si jambo la kufanywa kwa muda tu. Unatamani sana jina lako liandikwe daima katika kitabu cha kumbukumbu cha Yehova, sivyo? Vile vitabu vya wale manabii 12 vinaweza kukusaidia kufaulu.
IMANI HUONGOZA KWENYE WOKOVU
18. Ni takwa gani muhimu linalotajwa katika Yoeli 2:32, na mtume Paulo aliongeza jambo gani katika takwa hilo?
18 Akikazia jambo kuu linaloweza kumfanya mtu apate kibali cha kudumu cha Mungu, Yoeli alisema hivi: “Kila mtu anayeliitia jina la Yehova ataokoka.” (Yoeli 2:32) Mitume wawili, Petro na Paulo walinukuu takwa hilo muhimu. (Matendo 2:21; Waroma 10:13) Paulo aliongeza jambo lingine katika himizo hilo alipouliza hivi: “Watawezaje kumwitia yeye ambaye hawajamwamini?” (Waroma 10:14) Bila shaka wewe ungependa kuliitia jina la Yehova na kumwamini sasa na milele!
Yoeli
19. Kuliitia jina la Yehova kwatia ndani nini?
19 Kuliitia jina la Yehova hutia ndani mengi zaidi ya kulijua na kulitumia jina la Mungu. (Isaya 1:15) Muktadha wa Yoeli 2:32 unakazia toba ya kweli na kuutumainia msamaha wa Yehova. (Yoeli 2:12, 13) Kuliitia jina la Mungu humaanisha kumjua kikweli, kumtumaini, kumtii, na kumtanguliza maishani mwetu. Ndiyo, kumtumikia Yehova kwapaswa kuwa jambo kuu maishani. Kufanya hivyo kutatuwezesha kupata baraka za Yehova. Tutakuwa na maisha yenye kuridhisha na yenye kudumu.—Mathayo 6:33.
20. Unapojenga imani yako, ni zawadi gani nzuri unayoweza kupata?
20 Yehova alisema hivi kupitia Habakuki: “Mwadilifu, ataendelea kuishi kwa uaminifu wake.” (Habakuki 2:4) Usisahau hilo kamwe, likazie kikiki moyoni na akilini mwako. Ni mojawapo ya mafundisho makuu ya Biblia. Paulo alitaja andiko hilo mara tatu katika maandishi yake yaliyoongozwa na roho.b (Waroma 1:16, 17; Wagalatia 3:11, 14; Waebrania 10:38) Kulingana na kweli hiyo, unapaswa kuwa na imani katika dhabihu ambayo Yesu Kristo alitoa kwa ajili ya dhambi zetu. Yesu alieleza hivi: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini . . . awe na uzima wa milele.” Tunasoma hivi pia: “Yule anayemwamini Mwana ana uzima wa milele.” (Yohana 3:16, 36) Ni Mkombozi wetu tu anayeweza kutuponya kupitia dhabihu yake. Baada ya kuandika maneno ya Yehova kuhusu jinsi siku Yake kuu itakavyoufanya ulimwengu mwovu wa Shetani, Malaki alisema hivi: “Kwenu ninyi mnaoliogopa jina langu, jua la uadilifu litaangaza, likiwa na kiponyaji katika mabawa yake.” Naam, Yesu ataangaza akiwa na kiponyaji. Hilo latia ndani maponyo ya kiroho tunayopata leo. Hata hivyo, inasisimua kama nini kujua kwamba hilo litamaanisha afya kamili ya kimwili katika ulimwengu mpya!—Malaki 4:2.
21. Kwa nini unaweza kuwa na imani kwamba Yehova anaweza kutimiza mapenzi yake?
21 Ni muhimu pia kuwa na imani katika uwezo wa Mungu wa kutimiza mapenzi yake. Katika siku za Mika, haikuwa rahisi kuwategemea wanadamu. Nabii huyo alisema hivi: “Msimwamini mwenzi. Msimtegemee rafiki msiri.” Hata hivyo, Mika hakuona ugumu wowote kumtegemea Yehova, nawe pia hupaswi kuona ugumu wowote. Mika alisema hivi: “Nitaendelea kumtazamia Yehova.” (Mika 7:5, 7) Tofauti na wanadamu wasiotegemeka, Yehova ana nia na uwezo wa kutimiza kusudi lake ili kutetea enzi yake kuu na kuwaletea watu wenye imani hali nzuri zenye kudumu.
22. Wale wanaoliitia jina la Yehova kwa imani watapata nini?
22 Unaweza kusema kama alivyosema Habakuki: “Nitafurahi katika Yehova mwenyewe; nitakuwa na shangwe katika Mungu wa wokovu wangu.” (Habakuki 3:18) Nabii Yoeli anataja waziwazi sababu inayowafanya wale wanaoliitia jina la Yehova kwa imani wawe na shangwe: Watu hao “[wa]taokoka” au kama vile Paulo alivyosema “[w]ataokolewa.” (Yoeli 2:32; Waroma 10:13) Wataokoka au kuokolewa jinsi gani? Tayari imani yako imekuokoa kutokana na hila za Shetani na mambo mengine mengi yenye kuumiza yanayowakumba waovu. (1 Petro 1:18) Hata hivyo, mbali na hayo, unaweza kutazamia kwa uhakika kuokolewa wakati mfumo huu mwovu wa mambo utakapoharibiwa. Wokovu huo utakuwezesha kufurahia baraka nyingi zilizotajwa na wale manabii 12.
JINSI PARADISO ITAKAVYOKUWA
23, 24. (a) Wale manabii 12 wanataja mambo gani kuhusu Paradiso ijayo? (b) Mambo ambayo wale manabii 12 waliandika yameathirije mtazamo wako kuhusu wakati ujao?
23 Kuna baraka za kudumu akibani kwa ajili ya “wenye kumwogopa Yehova.” (Malaki 3:16) Baadhi ya wale manabii 12 walitaja jinsi Paradiso ya kidunia iliyo mbele itakavyokuwa. Maelezo yao yanaweza kukupa shangwe na hamu. Kwa mfano, Mika aliandika hivi: “Wataketi, kila mtu chini ya mzabibu wake na chini ya mtini wake, wala hakutakuwa na mtu yeyote anayewatetemesha.” (Mika 4:4) Kwa hakika, chini ya Ufalme wa Mungu, utakuwa salama na kuridhishwa na kazi yako!
24 Kutazamia mwisho wa magonjwa, huzuni, na hata kifo si ndoto tu. Hebu wazia shangwe ya wale watakaofufuliwa wakiwa na tumaini la kuwa wanadamu wakamilifu! Watajionea andiko la Hosea 13:14 likitimizwa kikamili hapa duniani: “Nitawakomboa wao kutoka katika mkono wa Kaburi; nitawaokoa wao kutoka kwenye kifo. Ee Kifo, iko wapi michomo yako? Ee Kaburi, yako wapi maangamizi yako?” Paulo alitumia andiko hilo kuhusu ufufuo wa kimbingu.—1 Wakorintho 15:55-57.
25. Utahisije katika ulimwengu mpya?
25 Hupaswi kuwa na shaka yoyote kwamba ufufuo huo wa duniani utatukia. (Zekaria 8:6) Amosi na Mika walipotabiri kwamba watu wa Mungu wangerudi kutoka uhamishoni, huenda lilionekana kuwa jambo lisiloweza kuaminika. Hata hivyo, unajua kwamba lilitimia. (Amosi 9:14, 15; Mika 2:12; 4:1-7) Waliorudi walisema hivi: “Tulikuwa kama wale waliokuwa wanaota ndoto. Wakati huo kinywa chetu kilijaa kicheko, na ulimi wetu vigelegele vya shangwe. . . . Yehova amefanya jambo kuu katika yale ambayo ametufanyia. Tumekuwa na shangwe.” (Zaburi 126:1-3) Hivyo ndivyo utakavyohisi katika ulimwengu mpya utakapopata “baraka hata kusiwe na uhitaji tena.”
Watumishi wa Yehova wamezingirwa na watu wanaopenda kweli na haki
26. Wale wanaoizingatia siku ya Yehova maishani mwao wana tumaini gani?
26 Baada ya “siku ya Yehova” kufagilia mbali uovu kutoka duniani, “lazima ufalme utakuwa wa Yehova” kikamili. (Obadia 15, 21) Je, hizo si baraka za ajabu kwa raia wake wote watakaoishi duniani? Wewe pia unaweza kuwa miongoni mwa wale ambao maneno ya Malaki sura ya 3 yatawahusu: “‘Nao watakuwa wangu,’ Yehova wa majeshi amesema, . . . ‘Nami nitawaonyesha huruma, kama vile mwanamume anavyomwonyesha huruma mwana wake ambaye anamtumikia.’” (Malaki 3:17) Ni wazi kwamba uaminifu wako, utakaokuwezesha kuokoka, utakuwezesha pia kupata “baraka hata kusiwe na uhitaji tena.” Hilo ni tumaini zuri kama nini!
-