Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • jv sura 5 kur. 42-60
  • Kupiga Mbiu ya Kurudi kwa Bwana

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kupiga Mbiu ya Kurudi kwa Bwana
  • Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Jitihada ya Kutafuta Sana Kweli
  • Aimarishwa Tena Katika Imani
  • Uvutano wa Wengine
  • Unabii Mbalimbali Unaohusu Wakati na Kuwapo kwa Bwana
  • ‘Aazimia Kufanya Kampeni Yenye Juhudi kwa Ajili ya Kweli’
  • Russell Aachana na Barbour
  • “Si Kama Ni Mpya, Si Kama Ni Yetu Wenyewe, Bali Kama ya Bwana”
  • “Kujengana Katika Imani Iliyo Takatifu Zaidi”
  • “Je, Wewe Unahubiri?”
  • “Lazima Wewe Uliache”
  • “Kweli Yacho Ilinasa Moyo Wangu Mara Hiyo”
  • Makao Makuu Kwenye Bible House
  • Kuungamanisha Kundi Lenye Kukua
  • Kufungua Mlango wa “Kueneza Gospeli Kupitia Magazeti ya Habari”
  • Kuhamia Brooklyn
  • Kupanua Kazi ya Kupiga Mbiu ya Habari Njema
  • Kukua Katika Ujuzi Sahihi Juu ya Kweli
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Kutahini na Kupepeta Kuanzia Ndani
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Ufalme Unazaliwa Mbinguni
    Ufalme wa Mungu Unatawala!
  • Kutengenezwa Ili Kumsifu Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
Pata Habari Zaidi
Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
jv sura 5 kur. 42-60

Sura ya 5

Kupiga Mbiu ya Kurudi kwa Bwana

“Historia inayofuata imetolewa si kwa sababu tu nimehimizwa nitoe pitio la miongozo ya Mungu katika kijia cha nuru, bali hasa kwa sababu mimi naamini inahitajiwa kabisa kweli isimuliwe kwa unyoofu, ili shaka na taarifa zisizo sahihi zikomeshwe, na kwamba wasomaji wetu waweze kuona jinsi kufikia hapa Bwana amesaidia na kuongoza.”a

KUFUATIA maneno hayo Charles Taze Russell alianza na akaendelea kutoa muhtasari wa matukio yaliyomwongoza hata kufikia kutangaza vitabu Millennial Dawn (vilivyoitwa baadaye Studies in the Scriptures) na Zion’s Watch Tower and Herald of Christ’s Presence (lijulikanalo sasa kama Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova). Historia hii inawapendeza kipekee Mashahidi wa Yehova. Kwa nini? Kwa sababu uelewevu wao wa sasa wa kweli za Biblia na utendaji wao waweza kufuatiliwa kurudi nyuma mpaka miaka ya 1870 na kazi ya C. T. Russell na washirika wake, na kutoka hapo mpaka kwenye Biblia na Ukristo wa mapema.

Charles Taze Russell alikuwa nani? Je, historia ya kazi yake hutoa uthitibisho wa msaada na mwongozo wa Bwana?

Jitihada ya Kutafuta Sana Kweli

C. T. Russell alizaliwa katika Marekani, katika Allegheny (sasa ni sehemu ya Pittsburgh), Pennsylvania, katika Februari 16, 1852. Alikuwa mwana wa pili wa Joseph L. na Ann Eliza (Birney) Russell, ambao walikuwa Wapresbiteri wa nasaba ya watu wa Scotland na Ireland. Mama yake Charles alikufa wakati yeye alipokuwa na umri wa miaka tisa tu, lakini tokea umri wa mapema, Charles alivutwa na wazazi wake wawili wenye akili zenye kufikiria mambo ya kidini. Kama vile mshirika wa baadaye wa C. T. Russell alivyosema, “walizoeza hilo tawi dogo; nalo likakua kuelekea Bwana.” Ingawa alilelewa akiwa Mpresbiteri, hatimaye Charles alijiunga na Congregational Church kwa sababu alipendelea maoni yalo.

Kwa wazi kijana Charles alikuwa mwanabiashara kwelikweli. Akiwa na umri wa miaka 11 tu, alipata kuwa mshirika wa kibiashara wa baba yake katika duka la nguo za wanaume lenye kusitawi. Charles alikuza biashara hiyo, hatimaye yeye mwenyewe akawa akiendesha maduka kadhaa tofauti. Ijapokuwa mambo yalimwendea vizuri kibiashara, kiroho yeye alisumbuka sana. Kwa nini ilikuwa hivyo?

Wazazi wa Charles waliamini kwa moyo mweupe itikadi za kidini za makanisa ya Jumuiya ya Wakristo nao walimlea akazikubali pia. Hivyo kijana Charles alifundishwa kwamba Mungu ni upendo, na hata hivyo kwamba yeye alikuwa ameumba watu wakiwa na hali ya kutokufa iliyorithiwa na alikuwa ameandaa mahali penye moto ambapo angetesa milele wote isipokuwa wale ambao wangekuwa wameandikiwa kimbele kuokolewa. Wazo kama hilo lilichukiza moyo mnyoofu wa tineja Charles. Yeye alifikiri hivi: “Mungu ambaye angetumia uwezo wake kuumba viumbe vya kibinadamu ambavyo alitangulia kujua na kuandikia kimbele kwamba vingepasa kuteswa milele, angekuwa wala si mwenye hekima, mwenye haki wala mwenye upendo. Viwango vyake vingekuwa chini kuliko vya wanadamu wengi.”

Lakini kijana Russell hakuwa mwatheisti (mtu asiyeamini kuwako kwa Mungu); ilikuwa tu kwamba hangeweza kukubali mafundisho ya makanisa yaliyoeleweka kwa ujumla. Yeye alieleza hivi: “Hatua kwa hatua niliongozwa kuona kwamba ingawa moja ya kila itikadi ya kidini ilikuwa na mambo fulani ya kweli, kwa ujumla, zilikuwa zenye kupotosha na zenye kupinga Neno la Mungu.” Kwelikweli, katika itikadi za kidini za makanisa, ‘mambo ya kweli’ yalifunikwa chini ya mvurugo wa mafundisho ya kipagani ambayo yalikuwa yamepenyeza ndani ya Ukristo uliochafuliwa wakati wa uasi-imani wa karne nyingi. Akitupilia mbali itikadi za kidini za makanisa na kutafuta kweli Russell alichunguza dini fulani kuu za Mashariki, akapata tu kwamba hizo hazikuridhisha.

Aimarishwa Tena Katika Imani

Ingawa hivyo, lile tawi lilikuwa limezoezwa na wazazi wenye kumhofu Mungu; lilikuwa na nia ya “kuelekea Bwana.” Alipokuwa angali anatafuta sana kweli, jioni moja katika 1869, jambo fulani lilitukia ambalo liliimarisha tena imani ya Charles iliyokuwa ikiyumbayumba. Alipokuwa akitembea karibu na duka la Russell katika Federal Street, alisikia nyimbo za kidini zikitoka katika jumba la chini ya usawa wa ardhi. Kwa maneno yake, ilitukia hivi:

“Inaonekana ni kwa tukio lisilotazamiwa tu kwamba, jioni moja niliingia ndani ya jumba lililochakaa, lenye vumbi, mahali nilipokuwa nimesikia kwamba ibada za kidini zilikuwa zikiendeshwa, ili nione kama watu hao wachache waliokutana humo walikuwa na jambo la akili la kutoa kuliko zile itikadi za kidini za yale makanisa makuu. Humo, kwa mara ya kwanza, nikasikia jambo fulani juu ya maoni ya Waadventisti wa Pili [Advent Christian Church], mhubiri akiwa ni Bw. Jonas Wendell . . . Hivyo, nakiri kuwa na deni kwa Waadventisti pamoja na madhehebu nyinginezo. Ingawa maelezo yake ya Maandiko hayakuwa wazi kabisa, . . . yalitosha, chini ya Mungu, kuimarisha tena imani yangu yenye kuyumbayumba katika kupuliziwa kimungu kwa Biblia, na kuonyesha kwamba maandishi ya mitume na ya manabii yameunganika yasiweze kutenganika. Niliyosikia yaliniingiza katika Biblia yangu nijifunze kwa bidii na uangalifu zaidi kuliko nilivyopata kufanya, nami nitamshukuru Bwana sikuzote kwa ajili ya mwongozo huo; kwa kuwa ingawa Uadventisti haukuniongoza kwenye kweli yoyote moja, ulinisaidia sana katika kuondolea mbali makosa, na hivyo kunitayarisha kwa ajili ya ile Kweli.”

Mkutano huo ulitia nguvu mpya kwenye azimio la kijana Russell la kutafuta sana kweli ya Kimaandiko. Ulimrudisha kwenye Biblia yake akiwa na hamu zaidi kuliko hapo awali. Upesi Russell akaja kuamini kwamba wakati ulikuwa karibu kwa wale waliomtumikia Bwana kupata ujuzi ulio wazi wa kusudi Lake. Hivyo, katika 1870, wakichochewa na idili, yeye pamoja na watu wachache waliojuana naye katika miji ya Pittsburgh na Allegheny ulio karibu waliungana na kuunda darasa kwa ajili ya funzo la Biblia. Kulingana na mshirika wa baadaye wa Russell, darasa hilo dogo la Biblia liliongozwa kwa njia hii: “Mtu angezusha swali. Wangelizungumza. Wangeangalia maandiko yote yenye kuhusiana nalo, hatimaye wakati walipokuwa wametosheka na upatani wa maandiko hayo, wangeeleza uamuzi wao na kuuandika.” Kama vile Russell alivyokiri baadaye, kipindi cha “tokea 1870 hadi 1875 kilikuwa wakati wa ukuzi wa daima katika neema na ujuzi na kumpenda Mungu na Neno lake.”

Walipoendelea kufanya utafiti juu ya Maandiko, mambo kadhaa yakawa wazi zaidi kwa watafutaji-kweli hao wenye moyo mweupe. Waliona kweli za Kimaandiko zilizohusu kufa kwa nafsi ya kibinadamu na kwamba kutokufa kulikuwa zawadi ambayo ingefikiwa na wale waliopata kuwa warithi-washirika pamoja na Kristo katika Ufalme wake wa kimbingu. (Eze. 18:20; Rum. 2:6, 7) Walianza kufahamu fundisho la dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo na fursa ambayo upaji huo ulifanya iwezekane kwa wanadamu. (Mt. 20:28) Walikuja kutambua kwamba ijapokuwa Yesu alikuja kwanza duniani akiwa mwanadamu katika mwili, wakati wa kurudi kwake angekuwapo bila kuonekana akiwa mtu wa roho. (Yn. 14:19) Walijifunza zaidi kwamba lengo la kurudi kwa Yesu lilikuwa, si kuharibu kila mtu, bali kubariki familia tiifu za dunia. (Gal. 3:8) Russell aliandika: “Tulihisi tumehuzunishwa sana na kosa la Waadventisti wa Pili, ambao walikuwa wakimtarajia Kristo katika mwili, na kufundisha kwamba ulimwengu na vyote vilivyomo isipokuwa Waadventisti wa Pili ungeteketezwa.”

Kweli za Kimaandiko ambazo zilipata kuwa wazi kwa darasa hili dogo la Biblia hakika zilitofautiana sana na mafundisho ya kipagani ambayo yalikuwa yamepenyeza ndani ya Ukristo wakati wa karne nyingi za uasi-imani. Lakini je, Russell na washirika wake wenye akili za kiroho walipata kweli hizi kutoka Biblia bila kusaidiwa na wengine?

Uvutano wa Wengine

Russell alirejezea waziwazi sana usaidizi katika funzo la Biblia ambao alikuwa amepokea kutoka kwa wengine. Yeye hakukubali tu udeni wake kwa Mwadventisti wa Pili Jonas Wendell bali yeye alisema pia kwa shauku juu ya watu wengine wawili waliomsaidia katika funzo la Biblia. Russell alisema hivi juu ya wanaume hao wawili: “Funzo la Neno la Mungu pamoja na ndugu hawa wathaminiwa liliongoza, hatua kwa hatua, ndani ya malisho ya majani mabichi zaidi.” Mmoja, George W. Stetson, alikuwa mwanafunzi mwenye bidii wa Biblia na pasta wa Advent Christian Church katika Edinboro, Pennsylvania.

Yule mwingine, George Storrs alikuwa mtangazaji wa gazeti Bible Examiner, katika Brooklyn, New York. Storrs, ambaye alizaliwa Desemba 13, 1796, alikuwa amechochewa mwanzoni kuchunguza yale ambayo Biblia ilisema juu ya hali ya wafu kama tokeo la kusoma jambo fulani lililokuwa limetangazwa (ingawa wakati huo bila kujitambulisha jina) na mwanafunzi wa Biblia aliye mwangalifu Henry Grew wa Philadelphia, Pennsylvania. Storrs alipata kuwa mteteaji mwenye bidii wa kile kilichoitwa kutokufa kwenye masharti—fundisho la kwamba nafsi ni yenye kufa na kwamba kutokufa ni zawadi ambayo ingefikiwa na Wakristo waaminifu. Yeye alitoa sababu pia kwamba kwa kuwa waovu hawana hali ya kutokufa, hakuna mateso ya milele. Storrs alisafiri sana, akitoa mihadhara juu ya habari ya kwamba waovu hawana hali ya kutokufa. Miongoni mwa vichapo vyake vilivyotangazwa mlikuwamo Six Sermons, ambacho hatimaye kilifikia mwenezo wa nakala 200,000. Bila shaka, maoni yenye nguvu yenye msingi wa Biblia ya Storrs juu ya kufa kwa nafsi pamoja na kulipia na rudisho (kurudishwa kwa kilichopotezwa kwa sababu ya dhambi ya Adamu; Mdo. 3:21) yalikuwa na uvutano mzuri wenye nguvu kwa kijana Charles T. Russell.

Lakini mwanamume mwingine aliyekuwa na uvutano mkubwa sana juu ya maisha ya Russell pia alisababisha uaminifu-mshikamanifu wake kwa kweli ya Kimaandiko utahiniwe.

Unabii Mbalimbali Unaohusu Wakati na Kuwapo kwa Bwana

Asubuhi moja katika Januari 1876, Russell mwenye umri wa miaka 23 alipokea nakala ya jarida la kidini linaloitwa Herald of the Morning. Kutokana na picha katika jalada, yeye angeweza kuona kwamba lilihusiana na Uadventisti. Mhariri, Nelson H. Barbour, wa Rochester, New York, aliamini kwamba lengo la kurudi kwa Kristo si kuharibu familia za dunia bali kuzibariki na kwamba kuja kwake kungekuwa si katika mwili bali akiwa roho. Aa! hilo lilipatana na yale ambayo Russell na washirika wake katika Allegheny walikuwa wameamini kwa muda fulani!b Ingawa hivyo, ajabu ni kwamba Barbour aliamini kutokana na unabii mbalimbali unaohusu wakati wa Kibiblia kwamba Kristo alikuwa tayari yupo (bila kuonekana) na kwamba wakati ulikuwa umefika wa kufanya kazi ya mavuno ya kukusanya “ngano” (Wakristo wa kweli waliojumuika kuwa jamii ya Ufalme).—Mt., sura 13.

Russell alikuwa ameepuka unabii mbalimbali wa Kibiblia unaohusu wakati. Lakini, sasa, yeye alijiuliza: “Je, ingeweza kuwa kwamba unabii mbalimbali unaohusu wakati ambao nilikuwa nimepuuza kwa muda mrefu sana, kwa sababu ya kutumiwa vibaya na Waadventisti, ulikuwa kwa kweli umekusudiwa uonyeshe wakati ambao Bwana angekuwapo bila kuonekana ili kusimamisha Ufalme wake?” Akiwa na kile kiu chake kisichotoshelezeka cha kweli ya Kimaandiko, ilikuwa sharti Russell ajifunze zaidi. Hivyo alipanga kukutana na Barbour katika Philadelphia. Mkutano huo ulithibitisha maafikiano yao juu ya mafundisho kadhaa ya Biblia na kuandaa fursa kwao wajadiliane. “Tulipokutana mara ya kwanza,” Russell akataarifu baadaye, “alikuwa na mengi ya kujifunza kutoka kwangu juu ya ujalivu wa rudisho unaotegemea utoshelevu wa fidia iliyotolewa kwa ajili ya wote, kama vile mimi nilivyokuwa na mengi ya kujifunza kutoka kwake juu ya wakati.” Barbour alifaulu kumsadikisha Russell kwamba kuwapo kusikoonekana kwa Kristo kulikuwa kumeanza katika 1874.c

‘Aazimia Kufanya Kampeni Yenye Juhudi kwa Ajili ya Kweli’

C. T. Russell alikuwa mtu wa masadikisho hakika. Akiwa amesadikishwa kwamba kuwapo kusikoonekana kwa Kristo kulikuwa kumeanza, aliazimia kupiga mbiu ya jambo hilo kwa wengine. Baadaye alisema hivi: “Kujua uhakika wa kwamba tayari tulikuwa katika kipindi cha mavuno kulinipa msukumo wa kueneza Kweli ambao sikuwa nimepata kuwa nao hapo awali. Kwa hiyo niliazimia kufanya kampeni yenye juhudi kwa ajili ya Kweli.” Sasa Russell aliamua kupunguza shughuli zake za kibiashara ili ajitoe mwenyewe afanye kazi ya kuhubiri.

Ili kupinga maoni yoyote yenye kosa kuhusu kurudi kwa Bwana, Russell aliandika kijitabu The Object and Manner of Our Lord’s Return. Kilitangazwa katika 1877. Mwaka huohuo Barbour na Russell walitangaza kwa kushirikiana kitabu Three Worlds, and the Harvest of This World. Kitabu hiki chenye kurasa 196 kilizungumza habari za rudisho na unabii mbalimbaliunaohusu wakati wa Kibiblia. Ingawa kila habari ilikuwa imezungumzwa na wengine awali, katika maoni ya Russell kitabu hiki kilikuwa ndicho “cha kwanza kuunganisha hilo wazo la rudisho na unabii unaohusu wakati.” Kilitoa maoni ya kwamba kuwapo kusikoonekana kwa Yesu Kristo kulianza tarehe ya vuli ya mwaka 1874.

Russell alipokuwa akisafiri na kuhubiri, ikawa wazi kwake kwamba kitu fulani zaidi kilihitajiwa ili kuendeleza mbegu za kweli alizokuwa akipanda zikiwa hai na zimetiliwa maji. Jawabu lilikuwa nini? “Jarida la kila mwezi,” akasema Russell. Hivyo yeye na Barbour waliamua kufufua utangazaji wa jarida Herald, lililokuwa limeacha kuchapwa kwa sababu ya maandikisho kufutwa na fedha kumalizika. Russell alichanga fedha zake mwenyewe ili kulifufua hilo jarida, akiwa mmoja wa wahariri washirika walo.

Yote yalienda sawasawa kwa kitambo—yaani, mpaka 1878.

Russell Aachana na Barbour

Katika toleo la Agosti 1878 la Herald of the Morning, mlitokea makala iliyoandikwa na Barbour ambayo ilikana thamani yenye kubadilishana na kifo cha Kristo. Russell, ambaye alikuwa mchanga kuliko Barbour kwa miaka karibu 30, angeweza kuona kwamba kwa kweli, huko kulikuwa ni kukana sehemu yenye maana ya fundisho la fidia. Hivyo katika toleo lililofuata (Septemba 1878), Russell, katika makala moja yenye kichwa “Kule Kulipia,” alitetea fidia na kupinga taarifa za Barbour. Ubishi huo uliendelea katika kurasa za jarida hilo kwa miezi michache iliyofuata. Hatimaye, Russell aliamua kujiondoa katika ushirika na Bw. Barbour akaacha kuendelea kulitegemeza Herald kifedha.

Ingawa hivyo, C. T. Russell, alihisi kwamba kujiondoa kwenye Herald hakukutosha; fundisho la fidia lazima litetewe na lazima mbiu ipigwe juu ya kuwapo kwa Kristo. Kwa hiyo, katika Julai 1879, Russell alianza kutangaza Zion’s Watch Tower and Herald of Christ’s Presence.d Russell alikuwa ndiye mhariri na mtangazaji, kukiwa na wengine watano ambao hapo kwanza waliorodheshwa kuwa wachangaji wa makala kwenye safu zalo. Toleo la kwanza lilikuwa na nakala 6,000 zilizochapwa. Kufikia 1914 chapa ya kila toleo ilikuwa nakala kama 50,000.

“Si Kama Ni Mpya, Si Kama Ni Yetu Wenyewe, Bali Kama ya Bwana”

C. T. Russell alitumia Watch Tower na vichapo vingine kutegemeza kweli za Biblia na kukanusha mafundisho bandia ya kidini na falsafa za kibinadamu ambazo zilipinga Biblia. Hata hivyo, yeye hakudai kuvumbua kweli mpya.

Kuanzia sehemu ya pili ya karne ya 18, wahudumu na wasomi wengi wa Biblia walikuwa wamekuwa wakifichua mafundisho bandia ya kutokufa kwa nafsi na adhabu ya milele kwa waovu. Ufichuo huo ulikuwa umeripotiwa kikamili katika kitabu Bible Vs. Tradition, cha Aaron Ellis, kilichotangazwa katika 1853 na George Storrs kwanza katika Uingereza na kisha katika Marekani. Lakini hakuna yeyote wakati ule aliyefanya mengi zaidi ya C. T. Russell na washirika wake kufanya kweli hii ijulikane.

Namna gani mafundisho mengine ya Biblia ambayo yalizungumzwa katika Watch Tower na vichapo vingine? Je, Russell alijichukulia sifa kamili kwa kufunua kweli hizi zenye thamani? Russell alieleza hivi: “Tuliona kwamba kwa karne nyingi mafarakano na vyama mbalimbali vilikuwa vimegawanya mafundisho ya Biblia miongoni mwavyo vyenyewe, vikiyachanganya kwa kadiri fulani na makisio na makosa ya kibinadamu . . . Tuliona kwamba lile fundisho la maana la kuhesabiwa haki kwa imani na si kwa kazi lilikuwa limejulishwa waziwazi na Luther na karibuni zaidi na Wakristo wengi; kwamba haki na uweza na hekima ya kimungu zilikuwa zimehifadhiwa kwa uangalifu ingawa hazikuwa zimefahamiwa waziwazi na Wapresbiteri; kwamba Wamethodisti walithamini na kusifu upendo na huruma za Mungu; kwamba Waadventisti waliamini lile fundisho la kurudi kwa Bwana; na Wabaptisti miongoni mwa mambo mengine waliamini kwa usahihi fundisho la ubatizo kwa njia ya ufananisho, hata ingawa walikuwa wamepoteza maana ya ule ubatizo halisi; kwamba kwa muda mrefu baadhi ya Wayunivasali walikuwa wameamini kijuujuu mawazo fulani kuhusu ‘rudisho.’ Na hivyo, karibu madhehebu yote yalitoa uthibitisho kwamba waanzilishi wayo walikuwa wamekuwa wakitafuta kweli: lakini kwa wazi kabisa yule Adui mkuu alikuwa amepiga vita dhidi yao na alikuwa amegawanya kimakosa Neno la Mungu ambalo yeye hangeweza kuangamiza kabisa.”

Kuhusu kronolojia ambayo alitoa mara nyingi, Russell alisema hivi: “Tusemapo kronolojia ‘yetu’ tunamaanisha tu ile tutumiayo, kronolojia ya Biblia, ambayo ni ya watu wote wa Mungu ambao huikubali. Kwa kweli ilitumiwa katika namna ileile tuitoayo leo muda mrefu kabla ya siku zetu, kama vile unabii mbalimbali tutumiao ulivyotumiwa kwa makusudi tofauti na Waadventisti, na kama vile mafundisho mbalimbali tuaminiyo na ambayo huonekana kuwa mapya na ya asili na tofauti sana yaliaminiwa kwa namna fulani muda mrefu uliopita: mathalani—Kuchaguliwa, Neema ya Bure, Rudisho, Kuhesabiwa Haki, Utakaso, Utukuzo, Ufufuo.”

Basi Russell alifahamuje daraka ambalo yeye na washirika wake walitimiza katika kujulisha kweli za Kimaandiko? Yeye alieleza hivi: “Kazi yetu . . . imekuwa kukusanya hivi vipande vya kweli vilivyotawanyika kwa muda mrefu na kuvitoa kwa watu wa Bwana—si kama ni mpya, si kama ni yetu wenyewe, bali kama ya Bwana. . . . Lazima sisi tujiondolee dai lolote la sifa hata kwa ajili ya kupata na kupanga upya vito vya kweli.” Yeye alitaarifu zaidi hivi: “Kazi ambayo Bwana amependezwa kutumia vipawa vyetu duni haikuwa sanasana ya uanzilishi bali ya kujenga upya, kurekebisha, kupatanisha.”

Hivyo Russell alikuwa mwenye kiasi sana kuhusu mambo aliyotimiza. Hata hivyo, “vipande vya kweli vilivyotawanyika” ambavyo alikusanya pamoja na kuvileta kwa watu wa Bwana vilikuwa bila mafundisho ya kipagani yenye kumvunjia Mungu heshima kama vile Utatu na kutokufa kwa nafsi, ambayo yalikuwa yameimarika sana katika makanisa ya Jumuiya ya Wakristo kama tokeo la ule uasi-imani mkubwa. Zaidi ya mtu mwingine yeyote katika wakati huo, Russell na washirika wake walipiga mbiu ulimwenguni pote juu ya maana ya kurudi kwa Bwana na juu ya kusudi la kimungu na mambo ambayo lilihusisha.

“Kujengana Katika Imani Iliyo Takatifu Zaidi”

Watu wenye mioyo minyoofu waliziitikia kwa haraka kweli zenye kuweka huru ambazo C. T. Russell na washirika wake walikuwa wakipigia mbiu kupitia kurasa zilizochapwa na mihadhara pia. Russell, akiwa bado na miaka iliyopungua 30, alitambua upesi kwamba kulikuwa na uhitaji wa wasomaji wa Watch Tower kupata kujuana na waamini wenzao na kutiana moyo. Wanafunzi wa Biblia katika Pittsburgh walikuwa wakifanya hivyo kwa kukutana kwa ukawaida, lakini ni jambo gani ambalo lingeweza kufanywa kusaidia wasomaji wa Watch Tower mahali penginepo?

Jibu lilikuja katika matoleo ya Watch Tower ya Mei na Juni 1880. Humo Russell alitangaza mipango yake ya kutembelea miji na majiji kadhaa katika Pennsylvania, New Jersey, Massachusetts, na New York. Kwa kusudi gani? “Wasomaji wetu,” tangazo hilo likaeleza, “wametawanyika sana, mahali pengine wako 2 na 3, na kuendelea mpaka kufikia 50. Mahali pengi hawajuani kabisa, na hivyo wanakosa huruma na faraja ambazo Baba yetu alikusudia zapaswa kuwajia kwa ‘kukutana wenyewe pamoja kama ilivyo namna ya wengine.’ Ni kusudi Lake kwamba twapaswa ‘Kuimarishana,’ na kujengana katika imani iliyo takatifu zaidi. Mikutano iliyopendekezwa twatumaini, yaweza kusaidia kujuana kibinafsi.”—Ebr. 10:24, 25.

“Mikutano iliyopendekezwa” ilifanywa wakati wa safari ya Russell, nayo ilithibitika kuwa yenye mafanikio sana; wasomaji wa Watch Tower walivutwa pamoja karibu zaidi. Upesi safari hizo na nyinginezo za kutembelea “vikundi vidogo vya wangojeaji” zikatokeza kuundwa kwa madarasa kadhaa, au eklesia (yaliyoitwa baadaye makutaniko), yaliyokuwa katika maeneo yaliyotangulia kutajwa na pia katika Ohio na Michigan. Madarasa hayo yalitiwa moyo yafanye mikutano kwa ukawaida. Lakini mikutano ya aina gani?

Darasa la Pittsburgh lilikuwa limeanzisha desturi ya kukutana pamoja angalau mara mbili kila juma. Mara nyingi mkutano mmoja wa darasa la Pittsburgh ulitia ndani mhadhara uliotolewa kwa eklesia yote na msemaji aliyestahili, labda katika jumba lililokodiwa. Lakini kwenye ule mkutano mwingine ambao kwa kawaida ulifanywa katika makao ya faragha, wale waliohudhuria walialikwa walete Biblia, konkodansi, karatasi na kalamu—na kushiriki.

Ushirika wa kiroho wenye uchangamfu walioupata katika mikutano hiyo ya kawaida ya kila juma ulikuwa badiliko lenye kuburudisha kutoka kwa yale mazingira yenye ubaridi, yasiyojali watu binafsi kwenye ibada za mengi ya makanisa ya Jumuiya ya Wakristo. Lakini Russell na washirika wake sio waliokuwa wa kwanza kutokeza wazo la kukutana pamoja kwa ukawaida. Desturi hiyo ya kukusanyika, hata katika makao ya faragha, ilianzishwa na Wakristo wa karne ya kwanza.—Rum. 16:3, 5; Kol. 4:15.

“Je, Wewe Unahubiri?”

C. T. Russell na washirika wake waliamini kwa nguvu sana kwamba walikuwa katika wakati wa mavuno na kwamba watu walihitaji kusikia kweli zenye kuweka watu huru. Hata hivyo, walikuwa wachache kwa hesabu. Watch Tower lilikuwa likitimiza uhitaji muhimu, lakini je, mengi zaidi yangeweza kufanywa? Russell na wafanyakazi wenzake walifikiri hivyo. Katika pindi ya 1880 walianza kutokeza Bible Students’ Tracts (baadaye ziliitwa pia Old Theology Quarterly), na hizo ziliandaliwa wasomaji wa Watch Tower kwa ajili ya ugawanyaji wa bure kwa umma.

Ndiyo, wasomaji wa Watch Tower walitiwa moyo washiriki pamoja na wengine kweli zenye thamani walizokuwa wakijifunza. “Je, wewe unahubiri?” ndilo swali lililozushwa katika toleo lenye kuunganishwa la Watch Tower la Julai na Agosti 1881. Lilikuwa jambo la maana kadiri gani kwao kuhubiri? Makala hiyo iliendelea kuarifu hivi: “Sisi twaamini kwamba hakuna yeyote ambaye atakuwa wa lile kundi dogo isipokuwa wahubiri. . . . Ndiyo, sisi tuliitwa tuteseke pamoja naye na kupiga mbiu ya hizi habari njema sasa, ili wakati uwadiapo tuweze kutukuzwa na kufanya mambo yanayohubiriwa sasa. Sisi hatukuitwa, wala kutiwa mafuta tupokee heshima na kukusanya mali, bali kutumika na kutumikishwa, na kuhubiri habari njema.”

Inafaa kwamba hao Wanafunzi wa Biblia wa mapema walihisi sana uhitaji wa kuhubiri habari njema. Kwa kweli, utume wa kuhubiri ulikuwa umepewa kwa Wakristo wa karne ya kwanza; ni daraka linalokalia Wakristo wote wa kweli hadi leo hii. (Mt. 24:14; 28:19, 20; Mdo. 1:8) Lakini ni nini lililokuwa lengo la kuhubiri kulikofanywa na Russell na wasomaji wa mapema wa Watch Tower? Je, lilikuwa tu kugawanya fasihi ya Biblia au kuamsha waenda-kanisa waone kweli za Kimaandiko?

“Lazima Wewe Uliache”

“Tokeni kwake, watu wangu,” Biblia ilionya zamani sana. Katika yeye nani? “Babiloni Mkubwa, mama wa makahaba na wa mambo yenye kuchukiza sana ya dunia.” (Ufu. 17:5; 18:4, NW) Kwa nini kuondoka katika Babiloni? “Kwa maana dhambi zake zimetungamana pamoja hadi mbinguni, na Mungu amekumbuka matendo yake yasiyo ya haki.” (Ufu. 18:5, NW) Ni nani huyu mama aliye kahaba ambaye watu wapaswa kujitenga naye?

Martin Luther na viongozi wengine wa Mapinduzi Makubwa ya Kidini walitambulisha Kanisa Katoliki na upapa walo kuwa Babiloni Mkubwa. Namna gani makanisa ya Protestanti yaliyozuka kama tokeo la hayo Mapinduzi Makubwa ya Kidini? Uhakika ni kwamba, isipokuwa kukataa kwayo ukuu wa papa, baadhi yayo hayakuwa tofauti sana na Ukatoliki katika muundo wa kikanisa, na yalidumisha mafundisho yasiyo ya kimaandiko kama vile, Utatu, kutokufa kwa nafsi, na mateso ya milele. Kwa sababu hiyo baadhi ya wahubiri walihimiza watu wajiweke huru si na Kanisa Katoliki tu bali pia na mifumo ya makanisa makuu ya Protestanti.

C. T. Russell na washirika wake walitambua pia kwamba kahaba huyu mwenye sifa mbaya hakuwa Kanisa Katoliki pekee. Hivyo, ingawa Watch Tower la Novemba 1879 lilitambulisha Babiloni Mkubwa na “Upapa ukiwa MFUMO,” makala hiyo iliongeza hivi: “Lazima sisi twende mbele zaidi tuonyeshe kwamba hurejezea (si washiriki mmoja-mmoja, bali mifumo ya makanisa) makanisa mengine yaliyoungana na Milki za dunia. Kila kanisa linalodai kuwa bikira safi aliyeposwa kwa Kristo, lakini kwa kweli limeungana na kutegemezwa na (hayawani) wa ulimwengu lazima sisi tulishutumu kwa lugha ya maandiko kuwa ni kanisa kahaba.”

Basi, wasomaji wa Watch Tower walitiwa moyo wafanye nini? Russell aliandika hivi: “Ikiwa kanisa unalohusiana nalo, huishi katika muungano wa uzinzi pamoja na ulimwengu, lazima wewe uliache, ikiwa utadumisha mavazi yako yakiwa meupe.” Russell na washirika wake hawakuelewa mweneo kamili wa uvutano wa Babiloni Mkubwa. Hata hivyo, wasomaji wa Watch Tower walihimizwa wajitenge na mifumo ya kanisa ambayo ilikuwa yenye ufisadi na ya kilimwengu.—Yn. 18:36.

“Kweli Yacho Ilinasa Moyo Wangu Mara Hiyo”

Kutangazwa kwa kweli za Biblia kulichukua hatua ya maana ya kusonga mbele katika 1886 kwa kutolewa kwa buku la kwanza la mfululizo ulioahidiwa wa vitabu viitwavyo Millennial Dawn, vilivyoandikwa na C. T. Russell. Buku la kwanza liliitwa The Divine Plan of the Ages. Lilikuwa na mafunzo juu ya vichwa 16 vya habari, kama vile “Kuwako kwa Muumba Mkuu Zaidi Mwenye Akili Kwathibitishwa,” “Biblia Ikiwa Ufunuo wa Kimungu Ikionwa kwa Kutumia Akili,” “Kurudi kwa Bwana Wetu—Lengo Lako, Rudisho la Vitu Vyote,” na “Kuruhusiwa kwa Uovu na Uhusiano Wako na Mpango wa Mungu.” Hatimaye, C. T. Russell aliandika mabuku mengine matano ya mfululizo huu wa Millennial Dawn.e

Russell hakuishi aweze kuandika buku la saba lililokusudiwa la mfululizo huo, lakini ugawanyaji wenye kuenea sana wa mabuku sita ambayo alimaliza uliitikiwa vizuri sana na watu wenye mioyo minyoofu. “Kitabu chako MILLENNIAL DAWN kilinijia Vuli iliyopita,” akaandika mwanamke mmoja katika 1889, “[ilikuwa] mara ya kwanza kupata wazo kwamba kulikuwa na vitabu kama hivyo. Nilikipata Jumamosi moja jioni, nikaanza kukisoma mara hiyo nami sikukiweka chini kamwe, isipokuwa wakati nililazimika, mpaka kilipomalizika. Kweli yacho ilinasa moyo wangu mara hiyo; kuanzia hapo nilijiondoa katika Kanisa Presbiteri ambamo kwa muda mrefu sana nilikuwa nikipapasa gizani nipate kweli, nisiipate.”

Ilitaka ujasiri kwelikweli siku hizo ili mtu ajiondoe katika kanisa lake. Mwanamke mmoja katika Manitoba, Kanada, aliyepata Millennial Dawn katika 1897 alionyesha hilo. Mwanzoni, alijaribu kukaa na kanisa lake na kufundisha shule ya Jumapili ya mahali pao. Siku ikafika, katika 1903, alipoamua kujiondoa kanisani. Alisimama na kuwaambia wote waliokuwapo sababu iliyomlazimisha ajitenge na kanisa. Jirani wa karibu zaidi (mwenye kuthaminiwa na watu katika jumuiya ndogo katika siku hizo) alijaribu kumshawishi arudi kanisani. Lakini mwanamke huyo alisimama imara, hata ingawa kulikuwa hakuna kutaniko la Wanafunzi wa Biblia karibu. Kama vile mwana wake alivyoieleza hali yake baadaye: “Hakuna mtumishi wa funzo [mzee] wa kuegemea. Hakuna mikutano. Moyo uliopondeka [tu]. Biblia iliyochakaa. Saa ndefu za kutoa sala.”

Mlikuwa nini katika Millennial Dawn, Watch Tower, na vichapo vingine vya Sosaiti ambacho kilinasa mioyo ya watu na kuwasukuma wachukue hatua hiyo yenye kukata maneno? C. T. Russell alitumia njia ya kueleza mafundisho ya Biblia ambayo ilikuwa tofauti na waandikaji wengi wa siku zake. Yeye aliamini Biblia kuwa Neno la Mungu lisilokosea na ambalo mafundisho yake yapasa kupatana. Kwa hiyo, ikiwa sehemu yoyote ya Biblia ilikuwa ngumu kueleweka, yeye alihisi, yapasa kuelezwa na kufasiriwa na sehemu nyingine ya Neno lililopuliziwa. Yeye hakujaribu kutegemeza maelezo aliyotoa kwa ushuhuda wa wanatheolojia wa siku zake au kwa maoni ya walioitwa eti mababa wa kanisa wa mapema. Kama vile yeye alivyoandika katika Buku 1 la Millennial Dawn: “Sisi twaamini kuwa ni kosa la kawaida la sasa na la nyakati zote kwa watu kuamini mafundisho fulani kwa sababu wengine walifanya hivyo, ambao waliwatumainia. . . . Watafutaji wa kweli wapasa kumwaga maji yenye matope ya mapokeo kutoka vyombo vyao na kuvijaza kwenye ile chemchemi ya kweli—Neno la Mungu.”

Kadiri idadi yenye kuongezeka ya watafutaji hao wa kweli ilivyoitikia yale waliyokuwa wakisoma katika vichapo vya Watch Tower Society, mabadiliko fulani yasiyotazamiwa yakawa yanahitajiwa huko Allegheny.

Makao Makuu Kwenye Bible House

Wanafunzi wa Biblia katika Allegheny, walioshirikishwa na kutangazwa kwa Watch Tower, walionwa kuwa ndio wenye uzoefu zaidi katika kufanya kazi ya Bwana nao walitegemewa na eklesia, au makutaniko yote, kuwa ndio waliokuwa wakichukua uongozi. Mwanzoni walikuwa na ofisi za makao makuu kwenye 101 Fifth Avenue, Pittsburgh, na baadaye kwenye 44 Federal Street, Allegheny. Hata hivyo, katika miaka ya 1880, upanuzi ukawa wahitajiwa. Hivyo Russell alipanga kujenga vifaa vikubwa zaidi. Katika 1889 jengo la matofali la orofa nne kwenye 56-60 Arch Street, Allegheny, lilikamilishwa. Likiwa na thamani ya dola 34,000, lilijulikana kuwa Bible House. Lilitumika likiwa makao makuu ya Sosaiti kwa miaka kama 19.

Kufikia mwaka wa 1890, ile familia ndogo ya Bible House ilikuwa ikitumikia mahitaji ya washiriki mamia kadhaa wenye kutenda wa Watch Tower Society. Lakini kadiri miaka ya 1890 ilivyoendelea, wengi zaidi walionyesha kupendezwa katika yale ambayo hao walikuwa wakifanya. Kwa kweli, kulingana na ripoti moja isiyo kamili iliyochapishwa katika Watch Tower, katika Machi 26, 1899, Ukumbusho wa kifo cha Kristo uliadhimishwa katika mikutano mbalimbali 339 kukiwa na washiriki 2,501. Ingawa hivyo, ni jambo gani lingesaidia kuendeleza kuungamanishwa kwa ile idadi ya Wanafunzi wa Biblia iliyozidi kukua?

Kuungamanisha Kundi Lenye Kukua

C. T. Russell aliwatia moyo wasomaji wote wa Watch Tower waje pamoja popote walipoweza ili kuunda vikundi, vidogo au vikubwa, kusudi wajengane kiroho. Shauri la Kimaandiko lilitolewa kupitia safu za Watch Tower. Wawakilishi wasafirio wa Watch Tower Society walipelekwa pia kutoka makao makuu ili kuwasiliana na vile vikundi mbalimbali na kuvijenga kiroho.

Pindi kwa pindi, kulikuwa pia na makusanyiko ya pekee yaliyohudhuriwa na Wanafunzi wa Biblia kutoka mahali pengi. “Huu ni MWALIKO WA PEKEE kwa kila msomaji awezaye kuja,” likahimiza toleo la Machi 1886 la Watch Tower. Ilikuwa pindi gani? Mwadhimisho wa kila mwaka wa Mlo wa Jioni wa Bwana, ambao ungefanywa Jumapili, Aprili 18, 1886, katika Allegheny. Ingawa hivyo, mengi zaidi yalipangiwa: Mfululizo wa mikutano ya pekee uliratibiwa wakati wa jioni za juma lililofuata. Wanafunzi wa Biblia katika Allegheny walifungua makao yao—na mioyo yao—bila malipo kwa wajumbe wenye kuzuru. Kwa muda wa miaka michache iliyofuata, makusanyiko kama hayo yalifanywa huko Allegheny wakati wa Ukumbusho wa kifo cha Bwana.

Katika pindi ya miaka ya mwishoni-mwishoni ya 1890, mikusanyiko ilianza kupangwa katika mahali pengi. C. T. Russell alitoa hotuba mara nyingi katika pindi hizo. Ilikuwaje kumsikiliza?

Ralph Leffler, ambaye alimsikia C. T. Russell akitoa hotuba, alikumbuka hivi: “Alipokuwa jukwaani mbele ya wasikilizaji, sikuzote yeye alivaa koti refu jeusi na tai nyeupe. Sauti yake haikuwa kubwa, naye hakutumia kamwe maikrofoni au kipaaza sauti, kwa kuwa havikuwa vimebuniwa; hata hivyo, kwa njia fulani sikuzote sauti yake ilipenya kufikia sehemu ya mbali zaidi ya jumba la wasikilizaji. Angeweza kunasa usikivu wa wasikilizaji wengi si kwa muda wa saa moja bali nyakati nyingine kwa muda wa saa mbili au tatu. Sikuzote yeye alianza mhadhara wake kwa kuinama kidogo kwa ungwana mbele ya wasikilizaji. Alipokuwa akihutubu, hakusimama tuli kama sanamu, bali sikuzote alikuwa akitembeatembea, akitoa ishara kwa mikono yake, na kupiga hatua toka upande huu hadi ule mwingine au kwenda mbele na kurudi nyuma. Sikumwona hata mara moja akiwa na muhtasari au hati mikononi mwake—Biblia tu, ambayo alitumia mara nyingi sana. Alisema kutoka moyoni na kwa njia ambayo ilikuwa yenye kusadikisha sana. Kwa kawaida kitu pekee kilichokuwa jukwaani siku hizo ni meza ndogo ikiwa na Biblia juu yayo na mtungi wa maji na bilauri ambayo kutoka kwayo msemaji alikonga maji pindi kwa pindi.”

Mikusanyiko hiyo ya mapema ilikuwa vipindi vya ushirika mchangamfu na kiburudisho cha kiroho. Ilitumika kutia nguvu umoja wa Wanafunzi wa Biblia wote na kutangaza kweli za Biblia. Kwa wakati huohuo, miaka ya 1890 ilipokuwa ikikaribia mwisho, ikawa wazi kwa Wanafunzi wa Biblia kwamba mengi zaidi yalihitaji kufanywa katika kueneza kweli za Biblia. Lakini bado hesabu yao ilikuwa ndogo kwa kadiri fulani. Je, kulikuwa na njia ya kufikia watu mamilioni zaidi ambao wangeweza kufikiwa kwa njia zilizokuwa zikitumiwa wakati huo? Hakika kulikuwa!

Kufungua Mlango wa “Kueneza Gospeli Kupitia Magazeti ya Habari”

Kufikia mwisho wa karne ya 19, ulimwengu ulikuwa umeenezwa nyuzi za simu. Mawasiliano ya simu yalikuwa si ghali na yalikuwa ya kasi; yalikuwa yamebadili sana uchapishaji wa magazeti ya habari. Habari zingeweza kupelekwa kwa haraka katika umbali mrefu na kuchapishwa katika magazeti ya habari. Katika sehemu ya mapema ya karne ya 20, C. T. Russell na washirika wake waliona magazeti ya habari kuwa njia yenye matokeo ya kufikia idadi kubwa za watu. Baadaye Russell alisema hivi: “Magazeti ya habari yamekuwa jambo kubwa katika maisha ya kila siku katika ulimwengu uliostaarabika.”

Toleo la Desemba 1, 1904, la Watch Tower lilitangaza kwamba mahubiri ya C. T. Russell yalikuwa yakitokea katika magazeti ya habari matatu. Toleo lililofuata la Watch Tower, chini ya kichwa “Kueneza Gospeli Kupitia Magazeti ya Habari,” liliripoti hivi: “Mamilioni ya mahubiri yametawanywa hivyo karibu na mbali; na angalau baadhi yayo yametokeza mema. Ikiwa Bwana apenda tutaterema kuona ‘mlango’ huu ukiendelea kufunguka, au hata ufunguke zaidi.” Mlango wa “kueneza gospeli kupitia magazeti ya habari” ulifunguka hata zaidi. Kwa kweli, kufikia 1913 ilikadiriwa kwamba kupitia magazeti ya habari 2,000 mahubiri ya Russell yalikuwa yakifikia wasomaji 15,000,000!

Ingawa hivyo, Russell aliweza kuhakikishaje kwamba mahubiri ya kila juma yalichapishwa hata wakati alipokuwa akisafiri? Kila juma alipelekea shirika la magazeti ya habari, barua ya simu ya mahubiri (yenye urefu upatao safu mbili za gazeti). Nalo shirika hilo, likapelekea upya kwa njia ya simu wachapaji wa magazeti ya habari mahubiri hayo katika Marekani, Kanada, na Ulaya.

Russell alisadikishwa kwamba Bwana alikuwa amesukuma mlango wa kuhubiri kupitia magazeti ya habari ukawa wazi kabisa. Wakati wa mwongo wa kwanza wa karne ya 20, ujumbe wa Biblia ambao Russell na washirika wake walikuwa wakipigia mbiu ulipata kujulikana kwa mapana sana kupitia mahubiri hayo ya magazeti ya habari. Pindi moja kichapo kimoja kiitwacho The Continent kilitaarifu hivi kuhusu Russell: “Maandishi yake yasemekana kuwa na mwenezo mkubwa zaidi kupitia magazeti ya habari kila juma kuliko yale ya mtu mwingine yeyote aliye hai; labda, mkubwa zaidi ya mwenezo uliojumlishwa pamoja wa maandishi ya makasisi na wahubiri wote katika Amerika Kaskazini.”

Kuhamia Brooklyn

Kazi ya kuhubiri kupitia magazeti ya habari ilipokuwa ikiongeza mwendo, Wanafunzi wa Biblia walitafuta mahali pengine ambapo kutoka hapo wangetolea mahubiri. Kwa nini? Ile Bible House katika Allegheny ilikuwa imekuwa ndogo mno. Pia ilifikiriwa kwamba mahubiri ya Russell yakitoka jiji kubwa zaidi, lenye kujulikana vizuri zaidi, tokeo lingekuwa ni kutangazwa kwa mahubiri hayo katika magazeti ya habari mengi zaidi. Lakini jiji gani? Watch Tower la Desemba 15, 1908, lilieleza hivi: “Kwa ujumla tulikata kauli, baada ya kutafuta mwongozo wa Kimungu, kwamba Brooklyn, N.Y., likiwa na idadi kubwa ya watu wa tabaka la katikati, na ambalo lilijulikana kuwa ‘Jiji la Makanisa,’ lingekuwa, kwa sababu hizi, mahali petu pakuu penye kufaa zaidi kwa ajili ya kazi ya mavuno kwa wakati wa miaka michache iliyobaki.”

Kwa hiyo, katika 1908, wawakilishi kadhaa wa Watch Tower Society, kutia ndani mshauri wa kisheria wayo, Joseph F. Rutherford, walitumwa kwenda New York City. Lengo lao lilikuwa nini? Kupata haki ya umiliki wa mali ambayo C. T. Russell alikuwa ameiona wakati wa safari ya mapema zaidi. Walinunua ile “Plymouth Bethel” ya zamani, iliyokuwa kwenye 13-17 Hicks Street, Brooklyn. Ilikuwa imetumika kuwa jengo la kimisheni kwa ajili ya Plymouth Congregational Church lililokuwa karibu, ambapo Henry Ward Beecher alitumikia wakati mmoja akiwa pasta. Wawakilishi wa Sosaiti walinunua pia yale yaliyokuwa hapo kwanza makao ya Beecher, jengo la orofa nne la matofali kwenye 124 Columbia Heights, yaliyokuwa umbali wa majengo machache.

Lile jengo la Hicks Street lilirekebishwa na kupewa umbo jipya na kuitwa Brooklyn Tabernacle. Lilikuwa makao ya ofisi za Sosaiti na jumba la mikutano. Baada ya marekebisho makubwa, yale yaliyokuwa hapo kwanza makao ya Beecher kwenye 124 Columbia Heights yakawa makao mapya ya wafanyakazi wa makao makuu ya Sosaiti. Yangeitwaje? Watch Tower la Machi 1, 1909, lilifafanua hivi: “Makao hayo mapya tutayaita ‘Betheli’ [kumaanisha, “Nyumba ya Mungu”].”f

Kazi ya “kueneza gospeli kupitia magazeti ya habari,” kama ilivyoitwa, iliongeza mwendo baada ya kuhamia Brooklyn. Lakini hiyo haikuwa njia pekee ya kufikia halaiki za watu.

Kupanua Kazi ya Kupiga Mbiu ya Habari Njema

Katika 1912, Russell na washirika wake walijasiria kuanzisha jambo la kielimu lililokuwa la utaalamu ambao haukujulikana wakati huo. Kwa kweli, lingefikia mamilioni ya watu ulimwenguni pote. Ilikuwa ile “Photo-Drama of Creation” (Drama-Picha ya Uumbaji)—muunganisho wa picha ya sinema na utoaji wa slaidipicha, ukiambatanishwa na muziki uliorekodiwa na hotuba zilizorekodiwa katika rekodi za santuri. Ilikuwa yenye urefu wa saa zapata nane na ilitolewa katika sehemu nne. Licha ya “Photo-Drama” ya kawaida, ile “Eureka Drama,” iliyokuwa yenye mihadhara iliyorekodiwa na mirekodi ya muziki au rekodi pamoja na slaidi, ilifanywa ipatikane pia. Ingawa hiyo haikuwa na picha ya sinema, ilitolewa kwa mafanikio katika maeneo yasiyokuwa na idadi kubwa ya watu.

Ebu wazia mandhari hiyo ya kihistoria: Katika Januari 1914, wakati wa enzi ya sinema zisizo na sauti,g wasikilizaji 5,000 walikusanyika katika The Temple, jengo moja kwenye West 63rd Street, katika New York City. Ilikuwa lazima kuzuia wengi zaidi wasiingie kwa kukosa nafasi. Ilikuwa pindi gani? Lo! wonyesho wa kwanza katika New York wa “Photo-Drama of Creation”! Mbele ya wasikilizaji kulikuwapo kiwambo kikubwa cha kuonyeshea picha ya sinema. Walipokuwa wakitazama—na kusikiliza—jambo fulani lenye kustaajabisha kwelikweli likatukia. C. T. Russell, wakati huo akiwa katika miaka yake ya mapema ya 60, akatokea katika kiwambo. Midomo yake ikaanza kusema, na maneno yake yangeweza kusikika! Utoaji ulipoendelea, ulipeleka wahudhuriaji—kwa njia ya maneno, picha za rangi, na muziki—kutoka uumbaji wa dunia mpaka mwisho wa Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo. Katika pindi ya utoaji waliona pia (kwa njia ya upigaji picha wa kuongeza mwendo) mambo mengine ambayo yalistaajabisha—kufunuka kwa ua na kuanguliwa kwa kifaranga. Walivutiwa kwelikweli!

Kufikia mwisho wa 1914, “Photo-Drama” ilikuwa imetolewa kwa mamilioni ya watu katika Amerika Kaskazini, Ulaya, New Zealand, na Australia. Hakika “Photo-Drama” ilithibitika kuwa njia yenye mafanikio sana ya kufikia halaiki za watu katika kipindi kifupi cha wakati.

Kwa wakati huohuo, namna gani juu ya Oktoba 1914? Kwa miongo ya miaka Russell na washirika wake walikuwa wamekuwa wakipiga mbiu kwamba Nyakati za Mataifa zingekoma katika 1914. Matarajio yalikuwa makubwa. C. T. Russell alikuwa amechambua wale waliokuwa wameweka tarehe mbalimbali za kurudi kwa Bwana, kama vile William Miller na baadhi ya vikundi vya Waadventisti wa Pili. Hata hivyo, tangu wakati wa ushirika wake wa mapema na Nelson Barbour, yeye alisadiki kwamba kulikuwa na kronolojia iliyokuwa sahihi, ikitegemea Biblia, na kwamba ilielekeza kwenye mwaka 1914 kuwa mwisho wa Nyakati za Mataifa.

Mwaka huo wenye maana kubwa ulipokuwa ukikaribia, kulikuwa na matarajio makubwa miongoni mwa Wanafunzi wa Biblia, lakini yote waliyokuwa wakitarajia hayakuwa yamesemwa moja kwa moja katika Maandiko. Ni nini lingetukia?

[Maelezo ya Chini]

a Watch Tower, Julai 15, 1906, uku. 229.

b Wala Barbour wala Russell sio waliokuwa wa kwanza kueleza kurudi kwa Bwana kuwa kuwapo kusikoonekana. Mapema zaidi, Sir Isaac Newton (1642-1727) alikuwa ameandika kwamba Kristo angerudi na kutawala “bila kuonekana kwa wanadamu.” Katika 1856, Joseph Seiss, mhudumu Mluther katika Philadelphia, Pennsylvania, alikuwa ameandika juu ya kuja kwa pili kwenye hatua mbili—pa·rou·siʹa, au kuwapo kusikoonekana, kukifuatwa na udhihirisho wenye kuonekana. Kisha, katika 1864, Benjamin Wilson alikuwa ametangaza Emphatic Diaglott yake ikiwa na usomekaji wa katikati ya mistari “kuwapo,” kwa ajili ya neno pa·rou·siʹa, si “kuja,” na B. W. Keith, mshirika wa Barbour, alikuwa ameelekeza uangalifu wa Barbour na washirika wake kwenye jambo hilo.

c Uelewevu ulio wazi zaidi wa kronolojia ya Biblia ulitangazwa katika miaka ya baadaye. Ona Sura ya 10, “Kukua Katika Ujuzi Sahihi juu ya Kweli.”

d Neno “Watch Tower” (Mnara wa Mlinzi) si la maandishi ya Russell au la Mashahidi wa Yehova pekee. George Storrs alitangaza kitabu katika miaka ya 1850 kilichoitwa The Watch Tower: Or, Man in Death; and the Hope for a Future Life. Jina hilo lilitiwa pia katika kichwa cha majarida mbalimbali ya kidini. Linatokana na wazo la kuendelea kukaa macho ili kuona utimizo wa makusudi ya Mungu.—Isa. 21:8, 11, 12; Eze. 3:17; Hab. 2:1.

e Yalikuwa: Buku 2, The Time Is at Hand (1889); Buku 3, Thy Kingdom Come (1891); Buku 4, The Day of Vengeance (1897; baadaye likaitwa The Battle of Armageddon); Buku 5, The At-one-ment Between God and Man (1899); na Buku 6, The New Creation (1904). Wakati mabuku hayo ya Millennial Dawn yalipoanza kuitwa Studies in the Scriptures, Buku 1 liliitwa “Mfululizo 1,” Buku 2 likawa “Mfululizo 2,” na kadhalika. Jina Studies in the Scriptures lilitumiwa katika chapa chache kuanzia kama Oktoba 1904, na jina hilo jipya lilitumiwa kwa kawaida zaidi kuanzia 1906.

f Baadaye, jengo lenye kupakana na Betheli, kwenye 122 Columbia Heights, lilinunuliwa, hivyo kuongezea ukubwa wa Kao la Betheli. Pia, katika 1911 jengo zaidi liliongezwa upande wa nyuma wa Kao la Betheli, na kuandaa makazi mapya.

g Ijapokuwa kulikuwa na majaribio ya mapema ya kuunganisha picha ya sinema na sauti, enzi ya picha zenye maneno ilianza katika Agosti 1926 kwa kutolewa kwa picha ya kilimwengu Don Juan (yenye muziki lakini bila maneno), ikifuatwa na The Jazz Singer (ikiwa na maneno) katika vuli ya 1927.

[Blabu katika ukurasa wa 51]

‘Waitwa kuhubiri habari njema’

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 44]

“Acheni Vyote Viwili Vikue Pamoja Mpaka Mavuno”

Kulitukia nini kwa Ukristo wa kweli baada ya karne ya kwanza? Katika kielezi kimoja, Yesu alikuwa ameonya kwamba Ibilisi angepanda “magugu,” Wakristo wa mwigo, miongoni mwa “ngano,” Wakristo wa kweli, “wana wa ufalme.” Vyote viwili vingekua pamoja mpaka “majira ya mavuno,” ule “umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mt. 13:24-30, 36-43, “NW”) Wakati wa ule uasi-imani mkubwa uliositawi baada ya kifo cha mitume, “magugu” yalikuwa na nguvu sana kwa karne nyingi.

Lakini namna gani ile “ngano”? Ni nani waliokuwa miongoni mwa “wana wa ufalme” wakati wa ule uasi-imani wa karne nyingi? Hatuwezi kusema kwa uhakika. Magugu halisi ya kielezi cha Yesu kwa kawaida huonwa kuwa darneli-ndevu, ambazo hufanana sana na ngano mpaka zikomaapo, wakati inapoweza kutofautishwa kwa urahisi na ngano kwa mbegu zake nyeusi zilizo ndogo kuliko za ngano. Vivyo hivyo, ni wakati wa “mavuno” tu kwamba tofauti iliyo wazi ingeonwa kati ya Wakristo wa mwigo na wale “wana wa ufalme” wa kweli. Hata hivyo, Yesu alisema: “Acheni vyote viwili vikue pamoja mpaka mavuno.” Basi, Ukristo wa kweli, haukupata kamwe kufutiliwa mbali kabisa.

Katika muda wa karne zote sikuzote kumekuwa na wapendao kweli. Kutaja wachache tu: John Wycliffe (karibu 1330-1384) na William Tyndale (karibu 1494-1536) waliendeleza mbele kazi ya kutafsiri Biblia hata kwa kuhatarisha maisha au uhuru wao. Wolfgang Fabricius Capito (1478-1541), Martin Cellarius (1499-1564), Johannes Campanus (karibu 1500-1575), na Thomas Emlyn (1663-karibu 1741) walikubali Biblia kuwa Neno la Mungu na wakakataa Utatu. Henry Grew (1781-1862) na George Storrs (1796-1879) si kwamba tu walikubali Biblia na kukataa Utatu, bali pia walionyesha uthamini kwa ajili ya dhabihu ya fidia ya Kristo.

Ijapokuwa hatuwezi kutambulisha kwa uhakika kabisa wowote wa hao kuwa “ngano” ya kielezi cha Yesu, hakika “Bwana awajua walio wake.”—2 Tim. 2:19.

[Sanduku kaitika ukurasa wa 45]

George W. Stetson—“Mtu Mwenye Uwezo Wenye Kutokeza”

C. T. Russell alikubali kwa shukrani usaidizi ambao alipewa na George W. Stetson, wa Edinboro, Pennsylvania, katika kujifunza Maandiko. Stetson alikufa katika Oktoba 9, 1879, akiwa na umri wa miaka 64. Mwezi uliofuata “Watch Tower” lilikuwa na tangazo la kifo cha Stetson ambalo lilifunua staha yenye kina ambayo Russell mwenye umri wa miaka 27 alikuwa nayo kwake. “Ndugu yetu alikuwa mtu mwenye uwezo wenye kutokeza,” akaandika Russell, “na aliacha matarajio maangavu ya heshima za kilimwengu na za kisiasa ili aruhusiwe kuhubiri Kristo.” Ombi la Stetson wakati wa kufa lilikuwa kwamba C. T. Russell atoe mahubiri ya maziko yake; Russell alikubali ombi hilo. “Watu wapatao elfu moja na mia mbili walihudhuria ibada ya maziko,” akaripoti Russell, “hivyo kutoa uthibitisho wa jinsi ndugu yetu alivyokadiriwa kuwa wa maana sana.”—“Watch Tower,” Novemba 1879.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 46]

George Storrs—“Rafiki na Ndugu”

C. T. Russell alijihisi kuwa na deni kwa George Storrs, ambaye alikuwa na umri mkubwa kuliko wake kwa miaka 56. Russell alikuwa amejifunza mengi kutoka kwa Storrs juu ya kufa kwa nafsi. Kwa hiyo wakati Storrs alipolala akiwa mgonjwa mahututi mwishoni-mwishoni mwa 1879, Russell alijitolea kuchapisha katika “Watch Tower” taarifa juu ya hali ya Storrs. “Ndugu yetu,” akaandika Russell, “ambaye amekuwa mhariri wa ‘The Bible Examiner’ kwa muda mrefu sana ajulikana kwa wengi zaidi kati ya wasomaji wetu; pia kwamba yeye amelazimishwa na ugonjwa mahututi asiendeleze gazeti lake.” Kwa kadirio la Russell, Storrs alikuwa na “sababu nyingi za kumshukuru Mungu kwa kuwa na pendeleo la kutumia maisha marefu sana na ya kujitakasa sana kwa Bwana-Mkubwa.” Storrs alikufa katika Desemba 28, 1879, akiwa na umri wa miaka 83. Tangazo la kifo chake lilitokea katika toleo la Februari 1880 la “Watch Tower,” ambalo lilisema: “Twaomboleza kumpoteza rafiki na ndugu katika Kristo hata hivyo, ‘si kama wale wasio na tumaini.’”

[Picha]

George Storrs

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 48]

“Nakuachia ‘Herald’”

Katika masika ya 1879, C. T. Russell aliacha kabisa kutegemeza gazeti “Herald of the Morning,” ambalo alikuwa ameshiriki kulitangaza pamoja na N. H. Barbour. Katika barua aliyomwandikia Barbour yenye tarehe ya Mei 3, 1879, Russell alifafanua sababu yake: “Kumezuka tofauti ya maoni kati yetu kwa habari ya fundisho la neno la Baba yetu [kuhusu thamani yenye kubadilisha ya fidia] na ingawa nakupa sifa kwa weupe wote wa moyo na unyoofu katika maoni yako, ambayo nadai mwenyewe maoni yaliyo kinyume, hata hivyo lazima niongozwe na uelewevu wangu mwenyewe wa neno la Baba yetu, na kwa sababu hiyo nakufikiria wewe kuwa unakosea. . . . Mambo yenye kuleta tofauti yaonekana kwangu kuwa ya msingi sana na ya maana sana hivi kwamba ushirika kamili na sikitiko kama lile lipaswalo kuwamo miongoni mwa watangazaji na wahariri wa jarida au gazeti, haupo tena kati yangu nawe, na kwa sababu ndivyo ilivyo, mimi nahisi kwamba uhusiano wetu wapaswa kukoma.”

Katika barua ya kufuatia ya tarehe ya Mei 22, 1879, Russell aliandika hivi: “Sasa nakuachia ‘Herald.’ Najiondoa nisihusiane nalo kabisa, nisiulize chochote kutoka kwako . . . Tafadhali toa tangazo katika nambari ifuatayo ya ‘Herald’ juu ya kujiondoa huko na uondoe jina langu.” Kuanzia toleo la Juni 1879, jina la Russell halikutokea tena akiwa mhariri-msaidizi wa “Herald.”

Barbour aliendelea kutangaza “Herald” mpaka 1903, wakati, kulingana na maandishi yapatikanayo ya maktaba, lilipokoma kuchapishwa. Barbour alikufa miaka michache baadaye, katika 1906.

[Picha]

Nelson H. Barbour

[Sanduku katika ukurasa wa 54]

Sababu Akaitwa Pasta

Charles Taze Russell alirejezewa na washirika wake kuwa Pasta Russell. Kwa nini? Kwa sababu ya utendaji wake katika kuchunga kundi la Mungu. Waefeso 4:11 huarifu kwamba, Kristo angewatoa wengine kwenye kutaniko lake wawe “mapasta” (“King James Version”), au “wachungaji.” Hakika Ndugu Russell alitumikia akiwa mchungaji wa kiroho katika kutaniko la Kikristo.

Kwa sababu ya kazi ya upasta ambayo yeye alifanya chini ya Mchungaji Mkuu, Yesu Kristo, makutaniko fulani yalikiri kwa kura kwamba yeye alikuwa pasta wao. Halikuwa jina la cheo alilojichukulia mwenyewe. Kikundi cha kwanza kumpigia kura kuwa pasta wao kilikuwa kutaniko katika Pittsburgh, Pennsylvania, katika 1882. Baada ya hapo, alipigiwa kura kuwa pasta na makutaniko mengine kama 500, katika Marekani na Uingereza.

Huko nyuma, ilikuwa desturi kwa makutaniko kupiga kura kila mwaka kwa ajili ya wale ambao wangewasimamia miongoni mwao. Leo, wazee Wakristo miongoni mwa Mashahidi wa Yehova hawachaguliwi na makutaniko ya mahali pao bali wanawekwa na Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova. Uangalifu unatumiwa pia wa kutotumia maneno kama vile “pasta” au “mzee” yakiwa majina ya cheo.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 56, 57]

Photo-Drama of Creation”

“Photo-Drama of Creation” iliunganisha picha ya sinema na utoaji wa slaidi, ikipatanishwa na sauti. Utoaji huo wenye kutokeza ulipeleka wasikilizaji kutoka wakati wa uumbaji mpaka mwisho wa Mileani.

Angalau seti 20 zenye sehemu nne zilitayarishwa, ikiwezesha sehemu ya “Photo-Drama” ionyeshwe katika majiji 80 tofauti kila siku. Ilikuwa vigumu kwelikweli kutimiza mapatano hayo 80. Ratiba za garimoshi hazikuwa zenye kufaa sikuzote. Makutaniko hayakuweza sikuzote kukodi mahali pa kuonyeshea katika tarehe zilizotakiwa. Hata hivyo, kufikia mwisho wa 1914, “Photo-Drama” ilikuwa imeonyeshwa jumla ya wasikilizaji zaidi ya 9,000,000 katika Amerika Kaskazini, Ulaya, na Australia.

[Picha]

“Hati ya mpangilio wa sinema” ya “Photo-Drama,” yenye mihadhara na vielezi vingi

Majumba ya sinema yaliyotumiwa wakati wote kwa ajili ya maonyesho ya “Photo-Drama”

Chicago

New York

Projekta ya sinema

Projekta ya slaidi

Rekodi za santuri

Slaidi kutoka sinema “Photo-Drama”

Hati ya kutangazia

[Sanduku katika ukurasa wa 60]

“Jihadharini na 1914!”

Wakati Vita ya Ulimwengu 1 ilipofyatuka katika 1914, “The World,” wakati huo likiwa gazeti kuu la habari katika New York City, lilitaarifu hivi katika sehemu ya jarida: “Ule mfyatuko wa vita wenye kuogofya katika Ulaya umetimiza unabii wenye kutokeza. . . . ‘Jihadharini na 1914!’ ndicho kimekuwa kilio cha mamia ya waevanjeli wasafirio, ambao, wakiwakilisha imani hii ya kigeni [iliyoshirikishwa na Russell], wameenda huku na huku nchini wakieleza fundisho kwamba ‘Ufalme wa Mungu umekaribia.’”—“The World Magazine,” Agosti 30, 1914.

[Picha katika ukurasa wa 42]

Charles Taze Russell

[Picha katika ukurasa wa43]

Joseph L. Russell, baba ya Charles, alikuwa mshiriki wa darasa la funzo la Biblia la Allegheny na mshirika wa karibu wa mwana wake katika utendaji wa Watch Tower Society mpaka kifo chake katika 1897

[Picha katika ukurasa wa 50]

Wanafunzi wa Biblia waligawanya makumi ya mamilioni ya nakala za trakti zilizofichua makosa ya kidini, zikaeleza kweli za Kimaandiko na kupiga mbiu ya ule mwaka wa maana wa 1914

[Picha katika ukurasa wa 52]

C. T. Russell aliandika mabuku sita ya “Millennial Dawn” (1886 hadi 1904) na trakti, vijitabu, na makala za “Watch Tower” kwa kipindi cha zaidi ya miaka 37

[Picha katika ukurasa wa 53]

Alipokuwa akitoa mihadhara, Ndugu Russell hakutumia hati zozote, naye sikuzote alikuwa akitembeatembea—akitoa ishara kwa mikono yake na kupiga hatua toka upande huu hadi ule mwingine jukwaani

[Picha katika ukurasa wa 58]

Ilikadiriwa kwamba mwaka mmoja, kupitia magazeti ya habari 2,000, mahubiri ya C. T. Russell yalikuwa yakifikia wasomaji 15,000,000

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki