Kurudi Shuleni Tena
1 Katika mwezi wa Januari, vijana wetu wanashughulika na mwaka mpya wa shule. Kuna mambo yenye kufurahisha ya kutazamia, lakini kuna mambo machache pia yawezayo kusababisha fadhaiko. Vijana wengi watagawiwa wafunzi tofauti, waandikishwe kwenye mitaala mipya, na kuwekwa kwenye ushirika wa karibu na wanafunzi wageni. Vijana wetu wanataka kushirikiana na mamlaka za shule na kufaana na wanafunzi wenzao, lakini wanapaswa kukumbuka kwamba wapaswa kulinda dhidi ya chochote kiwezacho kudhuru kiroho.—1 Kor. 15:33.
2 Hangaiko kubwa kwa watoto na vijana Mashahidi ni kuepuka athari ya ulimwengu yenye kuharibu, ambayo huenea kwenye mifumo ya kielimu katika mabara mengi leo. Vijana na wazee Wakristo lazima wawe wenye moyo-mkuu katika kukinza viwango vya kilimwengu na kufikiri kunakochochewa kuhusu masuala ya kiadili, nao lazima ‘walinde’ kwa kuendea na kuongozwa na Neno la Yehova. (Zab. 119:9) Wazazi wenye kujali wanahitaji kujulishwa kuhusu yanayotiwa ndani ya mfumo wa masomo ya shule ili wawapatie watoto wao mwelekezo unaofaa. Ikiwa wanalofunzwa shuleni au mahali penginepo hupingana na utakatifu na usafi unaohitajika kwa watumishi wa Yehova, hilo lapaswa kuepukwa.—1 Pet. 1:15, 16.
3 Pia ni jambo la kawaida kukabili masuala yanayohusu sherehe za kitaifa, misherekeo ya sikukuu, utendaji wa michezo, au mikusanyiko ya kijamii. Broshua Shule na Mashahidi wa Yehova ni yenye msaada kwa vijana Wakristo kuhusu mambo haya. Hali ziwezekanazo kuwa ngumu zaweza kushindwa au kupunguzwa wazazi wa watoto wachanga wanapochukua hatua ya kuwafikia walimu wakiwa na nakala ya kichapo hiki. Wanaweza kueleza kwamba hiki kitasaidia mwalimu aelewe ni kwa nini Mashahidi wa Yehova wanachagua kutoshiriki utendaji fulani. Kujulisha habari hii kwa mwalimu kwaweza kufanya mengi katika kutokeza roho ya ushirikiano.
4 Kwa kuongezea, ingekuwa vizuri kwa wanafunzi Wakristo wawe na nakala ya kibinafsi ya broshua Shule pamoja na vitabu vyao vya kusoma shuleni. Mara nyingi fursa hutokea ya kutoa ushahidi kwa wanafunzi wengine waulizao maswali wakati uangalifu unapokaziwa itikadi zetu. Pia, nyakati zote watoto Mashahidi wanapaswa kubeba wao binafsi kadi zao za Mwelekezo wa Mapema Kuhusu Tiba/Ondoleo la Hatia au Kadi ya Utambulishi iliyo ya sasa, iliyoshuhudiwa vizuri, na kutiwa sahihi. Wale wanaotumia shauri hili kwa hakika watakuwa kama ‘mwenye busara ayaonaye mabaya na kujificha.’—Mit. 22:3.