Waangalizi Wanaoongoza—Viongozi wa Funzo la Kitabu la Kutaniko
1 Ni pendeleo kubwa kwa mzee mwenye sifa ya ustahili au mtumishi wa huduma kutumikia akiwa kiongozi wa Funzo la Kitabu la Kutaniko. Kutunza mahitaji ya kiroho ya wale walio katika kikundi chake ni daraka zito. Wajibu wake mbalimbali una sehemu tatu.
2 Ufundishaji Stadi: Kiongozi wa Funzo la Kitabu la Kutaniko ahitaji kujitayarisha vizuri ili aweze kukielewesha kikundi kila juma. Yeye hujaribu kuzidisha uthamini wa habari inayochunguzwa. Badala ya kutoa maelezo mengi yeye mwenyewe wakati wa funzo, inapokuwa lazima, atatokeza maswali ya ziada yanayohusu habari hiyo ili kutokeza mambo makuu ya somo hilo. Ugumu alio nao ni kufanya funzo liwe lenye kupendeza na lenye kufundisha na kuhusisha kila mtu katika mazungumzo. Lengo lake ni kujenga kiroho, kukazia thamani yenye kutumika ya funzo hilo, na kufanya habari hiyo ifikie akili na moyo.—1 The. 2:13.
3 Uchungaji Wenye Kusaidia: Kiongozi wa Funzo la Kitabu la Kutaniko ni “kama mahali pa kujificha na upepo, na mahali pa kujisitiri na dhoruba.” (Isa. 32:2) Kwa kweli yeye hujali wote katika kikundi chake na kuona kwamba msaada wa kiroho waandaliwa wakati mmoja kati ya wale anaotunza amevunjika moyo.—Eze. 34:15, 16; 1 The. 2:7, 8.
4 Kueneza Evanjeli kwa Bidii: Kiongozi wa Funzo la Kitabu huwa mwangalifu kufanya mipango inayotumika ili wote katika kikundi chake washiriki kikamili katika huduma ya shambani. Yeye huongoza katika kazi ya kueneza evanjeli, akijua kwamba ukawaida, bidii, na shauku anayoonyesha kwa ajili ya utumishi zitaonyeshwa na kikundi chote. (Kol. 4:17; 2 The. 3:9) Baada ya muda, yeye hujitahidi kuhubiri na kila mshiriki wa kikundi chake. Tukitaka kuboresha stadi zetu za kuhubiri na kufundisha katika huduma, Kiongozi wa Funzo la Kitabu la Kutaniko anaweza kutusaidia tufikie mradi wetu.—1 Tim. 4:16; 2 Tim. 4:5.
5 Kwa kweli tumebarikiwa na zawadi hizi zikiwa wanadamu walio tayari kutusaidia kiroho na kututegemeza kwa upendo. (1 The. 5:14) Na tuonyeshe uthamini wetu kwa uandalizi huu mzuri ajabu kutoka kwa Yehova kwa kushiriki kwa ukawaida katika funzo la kitabu na kutegemeza kwetu kazi ya kueneza evanjeli.—Ebr. 10:25.